Wanunuzi wa madini wakikagua
madini ya vito kutoka kwa mfanyabiashara wa madini wa Tanzania katika
banda la Tanzania kwenye maonesho kimataifa ya 56 ya Madini ya vito na
usonara yanayofanyika mjini Bankok, Thailand.
Ofisa kutoka Wakala wa Ukaguzi wa
Madini Nchini (TMAA), Bi. Stella akimpatia maelezo mmoja kati ya
wanunuzi wa madini ya vito waliofika katika banda la Tanzania kutaka
maelezo ya jinsi ya kuweza kununua madini hayo ya vito yanayopatikana
Tanzania.
Wanunuzi wa Madini ya vito
waliofika katika banda la Tanzania wakipata maelezo kutoka kwa maofisa
wa Wizara ya Nishati na Madini waliopo kwenye banda la Tanzania.
Wanunuzi mbalimbali wa madini ya
vito waliofika katika banda la Tanzania wakijadiliana namna ya kununua
madini ya vito kutoka kwa Wafanyabiashara wa Tanzania.
Picha ya pamoja kati ya ujumbe
kutoka Wizara ya Nishati na Madini ya Tanzania na maofisa waandamizi
wanaosimamia maonesho ya kimataifa ya Madini ya vito mara baada ya
ufunguzi rasmi kufanyika jijini Bangkok, Thailand.
…………………………………………………………………
Na Mwandishi Wetu, Bangkok
Maonesho ya 56 ya vito na usonara yameanza kwa kishindo jijini
Bangkok, Thailand huku Tanzania ikiwa imeng’ara kutokana na madini ya
tanzanite kuzalishwa katika nchi ya Tanzania pekee duniani.
Maonesho ya kimataifa ya vito na usonara yameanza rasmi tarehe
10 hadi 14 ambapo hufanyika kila mwaka nchini Thailand na kukutanisha
wauzaji na wanunuzi wa madini ya vito na usonara duniani.
Katika maonesho hayo ambapo wachimbaji na wauzaji wa madini
wanashiriki ili kujitangaza pamoja na kutafuta masoko ya madini yao kwa
sasa na katika siku zijazo ambapo wanunuzi wengi wamejitokeza na kutaka
kujua utaratibu wa kuweza kununua madini hususan ya vito mbalimbali
yanayopatikana Tanzania.
Wanunuzi hao wengi wamejitokeza kutoka katika nchi za Brazil,
Canada, India, Thailand, Hongkong na Marekani ambapo pia wameahidi
kushiriki katika maonesho ya kimataifa ya vito ambayo yatafanyika mjini
Arusha.
Lengo la Tanzania kushiriki maonesho hayo nchini Thailand ni
kutangaza madini ya vito mbalimbali yaliyopo nchini ikiwamo tanzanite
ambayo inapatikana Tanzania pekee katika eneo la Mererani wilayani
Simanjiro mkoa wa Manyara.
Aidha, ziara hiyo pia inatoa fursa kubwa kwa taifa la Tanzania
hususan katika sekta ya Madini kuvutia wanunuzi mbalimbali duniani
wanaoshiriki maonesho ya Bangkok kuja pia Tanzania katika maonesho ya
kimataifa ya vito yanayofanyika kila mwaka mkoani Arusha kununua madini
ya vito na kuufanya mji wa Arusha kuwa kituo kikubwa cha madini ya vito
katika bara la Afrika.
Ni dhahiri kwamba maonesho hayo ya vito Bangkok ni jitihada za
serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini hususan Idara ya Madini
kuwatafutia masoko wachimbaji na wafanyabiashara wa madini hasa wale
wadogo.
Katika maonesho hayo wachimbaji na wafanyabiashara wa madini
hasa ya vito wapata mawasiliano kwa wanunuzi mbalimbali wa kimataifa
badala ya kuwatumia madalali ili kuweza kuuza madini yao kwa wanunuzi
walengwa na kuuza madini kwa bei nzuri na hatimaye kupata faida
maradufu.
Maonesho hayo ya vito yanatoa fursa pia kwa sekta nyingine
kujitangaza pamoja na kuitangaza Tanzania duniani mathalan sekta ya
utalii ambapo madini ya vito yanakwenda pia na ujumbe wa vivutio vya
utalii vilivyopo nchini ikiwamo mbuga za wanyama pamoja na mlima wa
Kilimanjaro.