Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts

MBUNGE ANNE KILANGO AONGOZA MAPOKEZI YA SHUJAA WA AFCON U -17 SAME MASHARIKI

June 10, 2026 Add Comment



Mamia ya wananchi wa Kata ya Kalemawe, Kijiji cha karamba wilayani Same, wamejitokeza kwa wingi kumpokea nyumbani kwao nyota chipukizi wa soka, Issa Chole, ambaye ni mchezaji wa timu ya taifa ya vijana ya Serengeti Boys chini ya umri wa miaka 17.

Mapokezi hayo yaliongozwa na Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, Anne Kilango, pamoja na viongozi mbalimbali wa eneo hilo na wananchi waliokusanyika kumpongeza kijana huyo kwa kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya AFCON 2026 kwa vijana chini ya miaka 17.



Shangwe na nderemo zilitawala katika kijiji hicho huku wananchi wakionesha fahari yao kwa mafanikio ya Issa Chole, ambaye ameibuka kuwa mmoja wa vijana wanaolipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa kupitia mchezo wa soka.

Akizungumza katika hafla hiyo, Anne Kilango alisema mafanikio ya Issa Chole ni jambo kubwa kwa wakazi wa Same Mashariki na Taifa kwa ujumla kwani yanaonesha kuwa vijana wa eneo hilo wana uwezo wa kufikia ndoto zao wanapopewa fursa sahihi.


Alisema ujio wa mchezaji huyo nyumbani ni heshima kubwa kwa jimbo hilo na ushahidi kwamba uwekezaji katika michezo unaweza kuzaa matokeo chanya kwa vijana na jamii kwa ujumla.

Kilango alibainisha kuwa Issa Chole ni miongoni mwa vijana waliopitia mashindano ya Samia Cup, yanayoandaliwa kila mwaka katika Jimbo la Same Mashariki kwa lengo la kuibua na kukuza vipaji vya michezo.


Kwa mujibu wa mbunge huyo, zaidi ya timu 91 kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo hushiriki mashindano hayo, ambayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwapa vijana nafasi ya kuonesha uwezo wao.


Alisema kupitia mashindano hayo, vijana wengi wameanza kuonekana katika ngazi za juu za soka na wengine wamepata nafasi ya kujiendeleza katika taaluma ya michezo.


“Leo tunashuhudia matunda ya Samia Cup. Issa ametufanya tujivunie kama wananchi wa Same Mashariki na kama Watanzania. Hii ni ishara kwamba tuna vijana wengi wenye vipaji ambao wanahitaji kuungwa mkono,” alisema Kilango.


Aliongeza kuwa ataendelea kuimarisha mashindano hayo ili kuhakikisha vipaji zaidi vinaibuliwa na kupata nafasi ya kuiwakilisha Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.


Mbunge huyo pia aliahidi kuanzisha na kuendeleza michezo mingine ikiwemo mpira wa miguu kwa wasichana na mpira wa pete, kwa lengo la kuwapa vijana na watoto wa kike fursa zaidi za kukuza vipaji na kujenga ajira kupitia michezo.


Kwa upande wake, Issa Chole aliwashukuru wananchi wa Kalemawe pamoja na Anne Kilango kwa mapokezi makubwa aliyoyapata, akisema hakuwahi kutarajia kupokelewa kwa namna hiyo baada ya kurejea kutoka majukumu ya timu ya taifa.


Alisema mafanikio yake yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na mashindano ya Samia Cup yaliyompa nafasi ya kuonekana na kuanza safari yake ya soka la ushindani, huku akiwataka vijana wengine kushiriki mashindano hayo kwa nidhamu, kujituma na kuwa na malengo makubwa maishani.


Baba mzazi wa mchezaji huyo, Mzee Musa Chole, alisema anajivunia maendeleo ya mwanawe katika soka na kusisitiza kuwa nidhamu, mazoezi na kujituma ndiyo msingi wa mafanikio katika mchezo huo.Aidha, alimuomba Mbunge Anne Kilango kuendelea kuunga mkono vijana kupitia Samia Cup ili vipaji zaidi viweze kuibuliwa na kuendelezwa.


Naye mmoja wa wananchi wa Kata ya Kalemawe alisema jitihada za mbunge huyo katika kuendeleza michezo zimekuwa na manufaa makubwa kwa vijana, kwani zimewapa hamasa ya kujituma, kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya, ulevi na vitendo vingine vinavyoweza kuharibu maisha yao, huku akimpongeza kwa kujitokeza kushiriki mapokezi hayo ambayo yameonesha mshikamano mkubwa kati ya viongozi na wananchi.

MUHEZA YAANZA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2026

June 06, 2026 Add Comment

 

DC awapongeza wananchi kwa mwitikio mkubwa wa Jogging

Na Oscar Assenga, Muheza

MAANDALIZI ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026 katika Wilaya ya Muheza yamezidi kushika kasi baada ya wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mazoezi ya Jogging yaliyoandaliwa ikiwa ni sehemu ya kujiandaa na tukio hilo muhimu la Kitaifa.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, Mkuu wa Wilaya ya Muheza Ayoub Sebabili  aliwapongeza wananchi kwa mwitikio wao mkubwa, akisema ushiriki huo unaonyesha utayari wa wakazi wa wilaya hiyo kuupokea Mwenge wa Uhuru unaotarajiwa kuwasili Juni 23 mwaka huu.

Alisema mazoezi hayo yamelenga kuwaweka wananchi katika hali nzuri ya afya, kuimarisha mshikamano na kuwaandaa kimwili na kiakili kuelekea mapokezi ya mwenge huo.

“Tunawashukuru wananchi wote waliojitoa kushiriki mazoezi haya. Hii ni ishara nzuri ya ushirikiano katika maandalizi ya tukio muhimu la kitaifa ambalo Wilaya ya Muheza itakuwa mwenyeji wake,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alibainisha kuwa jogging nyingine itafanyika Juni 13 mwaka huu na kutoa wito kwa wananchi ambao hawakupata nafasi ya kushiriki safari hii kujitokeza kwa wingi ili kuwa sehemu ya maandalizi hayo.

Alisisitiza kuwa mazoezi hayo ya kilomita tano yanafanyika kwa mwendo wa kawaida ili kuwezesha kila mwananchi kushiriki bila kujali umri au hali yake ya kiafya.

“Tunawakaribisha vijana, wanawake, wazee pamoja na watu wenye ulemavu kushiriki mazoezi haya. Lengo letu ni kuona wananchi wote wanakuwa sehemu ya maandalizi ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026,” alisema.

Muheza inatarajia kuupokea rasmi Mwenge wa Uhuru Juni 23, huku maandalizi mbalimbali yakiendelea kufanyika kuhakikisha tukio hilo linafanyika kwa mafanikio na kuacha alama chanya kwa wananchi wa wilaya hiyo.

MBUNGE MWAKIOJA ATANGAZA NEEMA YA SOKA WILAYA MKINGA,AGAWA VIFAA VYA MICHEZO KWA TIMU ZINAZOSHIRIKI LIGI YA WILAYA

May 04, 2026 Add Comment


>Agawa vifaa vya michezo kwa timu zote zinazoshiriki Ligi ya wilaya ya Mkinga

Na Oscar Assenga, MKINGA

Mbunge wa Jimbo la Mkinga mkoani Tanga (CCM), Twaha Mwakioja, ameahidi kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo kuinua kiwango cha soka wilayani humo kwa kuwekeza katika elimu na maendeleo ya waamuzi pamoja na makocha.

Akizungumza wakati wa mchezo wa Ngao ya Jamii uliokwenda sambamba na uzinduzi wa Ligi ya Wilaya ya Mkinga, uliofanyika katika Uwanja wa Chamazi, Kata ya Matamba, Mwakioja alisema lengo lao ni kuwekeza katika michezo kwa vijana ili kuwapatia ajira, kuboresha afya zao, pamoja na kuimarisha amani, mahusiano mema na ushirikiano miongoni mwao.

Alieleza kuwa dhamira yao ni kuwashika mkono vijana ili waweze kupiga hatua kutoka ngazi ya wilaya, kwenda mkoa, kanda na hatimaye ligi za juu, huku yeye akiwa bega kwa bega nao kuhakikisha wanafikia malengo yao.

Mbunge huyo alibainisha kuwa wamepata taarifa ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali, ikiwemo uhaba wa makocha na waamuzi wenye sifa. Hivyo, wamejipanga kuwekeza katika mafunzo ya makocha ili kila kata iwe na angalau kocha mmoja mwenye ujuzi na mafunzo rasmi, pamoja na kuandaa waamuzi wenye vyeti ili kuboresha usimamizi wa michezo.

Alisisitiza kuwa uwekezaji huo utaenda sambamba na ushirikiano na Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga katika kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.

Aidha, alisema mpango wao ni kuhakikisha kila kata na kijiji kinakuwa na timu ya mpira wa miguu inayoshiriki ligi ya wilaya. Aliongeza kuwa watawekeza zaidi ili kuibua timu imara zitakazoweza kushiriki ligi za ngazi ya mkoa, kanda na hatimaye Ligi Kuu, hatua itakayosaidia kuitangaza Mkinga katika ramani ya soka nchini.

Katika kuonyesha dhamira hiyo, Mwakioja alikabidhi jezi na mipira kwa timu zinazoshiriki ligi hiyo, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha na kusaidia maendeleo ya michezo wilayani humo.

Kwa upande wake, Katibu wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Fadhili Habibu, alisema ratiba ya ligi hiyo imeanza Mei 4 katika kituo cha Mkinga, huku kituo cha Maramba kikitarajiwa kuanza Mei 6 (Jumatano), ambapo kutakuwa na vituo vinne vitakavyochezwa katika Kijiji cha Maramba, ikiwa ni pamoja na mechi kati ya Viva Dynamo na Maramba FC.

Habibu alisema lengo la ligi hiyo ni kusimamia na kuibua vipaji vya vijana, pamoja na kuwapa mwelekeo wa maendeleo yao kisoka. Alimshukuru mbunge kwa kujitoa na kushirikiana nao katika kufanikisha malengo hayo.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Soka Wilaya ya Mkinga, Hassan Zumo, alimpongeza mbunge kwa juhudi zake za kuendeleza michezo wilayani humo, akieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa na matarajio ya ushindani mkubwa katika ligi hiyo, hasa baada ya timu kukabidhiwa vifaa.

Zumo aliongeza kuwa tangu kuanzishwa kwa chama hicho mwaka 2008, wamekuwa wakipeleka vilabu katika mashindano ya ngazi ya mkoa lakini wamekuwa wakikwama kutokana na changamoto za kifedha. Hata hivyo, alisema kupitia uongozi wa Mbunge Mwakioja, wana matumaini ya kupata timu itakayoweza kufika hadi Ligi Kuu.

Aidha, timu zinazoshiriki mashindano hayo zimeahidi kujituma na kupambana kwa juhudi zote ili kuhakikisha ligi hiyo inaleta mafanikio na tija kwa vijana wa Wilaya ya Mkinga.




TCDC YAICHALAZA KILIMO KWA BAO 2 – 1

TCDC YAICHALAZA KILIMO KWA BAO 2 – 1

April 17, 2026 Add Comment

Timu ya Mpira wa miguu ya TCDC Sports Club imechukua alama tatu (3) baada cha kuifunga Timu ya Mpira wa miguu ya Wizara ya Kilimo goli mbili (2) kwa moja (1) katika mechi iliyochezwa leo Aprili 17, 2026 saa 2:30 3:45 katika viwanja vya Venite mkoani Njombe.

Timu hizo zimekutana katika mashindano ya Michezo ya Wafanyakazi (Meimosi) yanayoyafanyika kitaifa mkoani Njombe.

Hapo Kesho Aprili 18, 2026 Timu ya Mpira wa miguu TCDC Sport Club inatarajia kukutana na Timu ya Mpira wa miguu ya TAMISEMI saa10:15 jioni katika viwanja vya Kibena mkoani humo.

TCDC YAKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA WACHEZAJI

TCDC YAKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA WACHEZAJI

April 14, 2026 Add Comment

Mrajis na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Tanzania (TCDC) Dkt. Benson Ndiege kushirikiana na Uongozi wa TCDC Sports Club wanunua vifaa vya michezo kwa wachezaji 42 kuelekea mashindano ya Michezo ya Meimosi mjini Njombe.

Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Aprili 14, 2026 jijini Dodoma wakati wa kuwaaga wanamichezo wakielekea mjini Njombe.

Vifaa vilivyonunuliwa ni jezi za mprira wa miguu, viatu, mipira na vifaa vingine vya michezo.

MWENYEKITI WA CCM MKOA TANGA AINGILIA KATI KUINUSURU KLABU YA AFRICAN SPORTS ISISHUKE DARAJA

April 12, 2026 Add Comment

 

Na Oscar Assenga,Tanga

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga, Rajab Abdurhaman  ameanza jitihada za kuinusuru Klabu ya African Sports ambayo ipo hatarini kushuka daraja kufuatia matokeo mabaya katika Ligi ya Championship.

Rajab aliyasema hayo baada ya kukutana na wachezaji pamoja na viongozi wa klabu hiyo, ambapo alieleza kuwa hali ya timu si ya kuridhisha, akifananisha na mgonjwa aliye katika chumba cha mahututi.

Alibainisha kuwa kwa sasa African Sports inashika nafasi ya 15 kati ya timu 16, hali inayoiweka katika hatari kubwa ya kushuka daraja endapo haitafanya vizuri katika mechi zilizobaki.

Akizungumzia historia ya klabu hiyo, alisema ni moja ya timu zenye heshima kubwa nchini na mshindani wa jadi wa Coastal Union, hivyo ni muhimu kurejesha ushindani wa soka la Tanga.

Katika hatua ya kuokoa timu hiyo, Mwenyekiti huyo  alitangaza kuchangia Shilingi milioni 20 ambazo tayari alikwisha kuziweka kwenye akauti, huku Mbunge wa Jimbo la Tanga akiahidi kutoa milioni tano na mdau mwingine kuahidi milioni 20, ikiwa ni sehemu ya kufikia lengo la kukusanya milioni 45 zinazohitajika kuiwezesha timu kumaliza msimu salama.

Alisema atahakikisha fedha hizo zinapatikana ili kutatua changamoto zinazoikabili klabu hiyo na kuwawezesha wachezaji kucheza kwa utulivu.

Aidha, aliwataka wachezaji kujituma katika mechi zilizobaki ili kuinusuru timu, akisisitiza kuwa wana dhamana ya kulinda heshima ya klabu hiyo.

Kwa upande mwingine, aliwashauri viongozi wa klabu kuweka mikakati ya muda mfupi na mrefu, ikiwemo kutovunja kambi mara baada ya msimu kumalizika ili kuboresha maandalizi ya msimu ujao.

Aliongeza kuwa mabadiliko ya mara kwa mara ya kikosi na maandalizi hafifu yamekuwa yakichangia kushuka kwa kiwango cha timu, na kusisitiza kuwa kwa mipango madhubuti wanaweza kurejea Ligi Kuu katika msimu ujao.






DC SUMAYE - NMB KIJIJI DAY NI HATUA MUHIMU YA KUWAFIKIA WANANCHI WA VIJIJINI KUWAPATIA ELIMU YA FEDHA

April 12, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, Lushoto

Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Zephania Sumaye, ameishukuru Benki ya NMB Bank Plc kwa kuandaa tukio la kipekee la Kijiji Day, akisema ni hatua muhimu katika kuwafikia wananchi vijijini na kuwapatia elimu ya kifedha.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto (CCM), alisema kuwa wizara ina malengo mahsusi ya miaka mitano, likiwemo kuhakikisha wananchi wanapata uhuru wa kiuchumi.

Alisisitiza kuwa uhuru huo hauwezi kupatikana bila wananchi kujihusisha na taasisi za kifedha, ikiwemo benki kama NMB.

Alieleza kuwa tukio la Kijiji Day ni sehemu ya utekelezaji wa malengo hayo, kwani linawawezesha wananchi kupata elimu ya kifedha pamoja na huduma mbalimbali za kibenki moja kwa moja walipo.

Tukio hilo lilifanyika katika Kata ya Magamba, ambapo wananchi walipata fursa ya kujifunza na kunufaika na huduma zinazotolewa na benki hiyo.

Aidha, alisema moja ya malengo ya serikali ni kuhakikisha jamii ya Lushoto inaunganishwa na kuwa kitu kimoja.

Alibainisha kuwa njia mojawapo ya kuimarisha mshikamano huo ni kupitia michezo na mabonanza, kama ilivyofanyika katika tukio hilo ambapo NMB ilitumia siku nzima kushirikiana na wananchi wa Kijiji cha Magamba.

Alisisitiza umuhimu wa elimu kwa maendeleo ya mwanadamu, akieleza kuwa hata katika mafundisho ya dini mbalimbali, elimu imepewa kipaumbele kikubwa.

Alifananisha juhudi za NMB na msemo usemao: “Usimpe mtu samaki, mfundishe kuvua.” Akasema benki hiyo inafanya kazi kubwa kwa kuwafundisha wananchi namna ya kutumia huduma za kifedha kwa ufanisi, badala ya kuwapatia msaada wa moja kwa moja bila uelewa.

Aliongeza kuwa kama benki zingetoa mikopo bila elimu ya matumizi sahihi, matokeo yasingekuwa endelevu,Hivyo, matukio kama Kijiji Day yanafungua njia ya kuwafikia wananchi, kuwapa elimu na kuwasogezea huduma za kifedha karibu zaidi.

Aliwahimiza NMB kuendelea na juhudi hizo pamoja na kuandaa mabonanza yatakayoongeza furaha, mshikamano na uelewa wa wananchi kuhusu huduma zao, jambo litakalosaidia kujenga imani na umiliki wa wananchi kwa benki hiyo.

Katika tukio hilo la Kijiji Day lililofanyika Magamba, shughuli mbalimbali zilifanyika ikiwemo mbio za marathon, huduma ya chakula, pamoja na mabonanza mengine. Lengo kuu lilikuwa ni kuwafikia wananchi, kuwapa elimu ya kifedha na kuwajengea uelewa mpana kuhusu huduma za benki.

Awali akizungumza Meneja wa Kanda ya Kaskazini wa NMB Bank Plc, Baraka Ladislaus, amesema benki hiyo inaendelea kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi kupitia matamasha ya Kijiji Day yanayofanyika vijijini.

Alisema lengo la mpango huo ni kuwafikia wananchi walipo, kuwapatia elimu ya kifedha na kuwaunganisha na huduma mbalimbali za kibenki ili kuwawezesha kiuchumi.

Alieleza kuwa pamoja na elimu ya kifedha, tukio hilo linaambatana na shughuli za kijamii ikiwemo upandaji miti kwa kushirikiana na Taifa Gas, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuhifadhi mazingira na kuifanya Tanzania kuwa ya kijani.

Aidha, alisema NMB ina mtandao mpana wa mawakala zaidi ya 80,000 nchi nzima wanaotoa huduma karibu asilimia 60 ya mahitaji ya kifedha ya wananchi, sambamba na matumizi ya magari maalum ya kibenki yanayowafikia wananchi vijijini.

Aliongeza kuwa benki hiyo imeboresha huduma zake za kidijitali ikiwemo programu ya NMB Mkononi, inayorahisisha upatikanaji wa huduma kwa wateja popote walipo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto Whitney Mwinzagi aliwataka wananchi kutumia vyema elimu wanayoipata na kuelekeza mikopo wanayoipata kuitumia shughuli za uzalishaji mali badala ya matumizi yasiyo na tija.