Showing posts with label michezo. Show all posts
Showing posts with label michezo. Show all posts

MWANA FA AZINDUA RASMI AWESO CUP ,TIMU 80 KUCHUKUANA KUMPATA BINGWA

September 13, 2026 Add Comment






Na Oscar Assenga, PANGANI

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma ‘Mwana FA’, amezindua rasmi Mashindano ya Aweso Cup katika Kijiji cha Sakura wilayani Pangani huku akizitaka klabu kubwa nchini pamoja na wadau wa soka, kufuatilia mashindano hayo kwa lengo la kuibua vipaji vipya.

Mwinjuma amesema  hayo katika Kijiji cha Sakura, Wilaya ya Pangani, mkoani Tanga, wakati akizindua rasmi Mashindano ya Kombe la Aweso, yanayoshirikisha jumla ya timu 80 kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.

Ambapo alisema Pangani ina vijana wengi wenye vipaji ambao wanahitaji kupewa nafasi ya kuonekana na watu wanaoweza kuwasaidia kufikia viwango vya juu.

Amesema uwekezaji unaofanyika leo katika michezo unaweza kuleta matokeo makubwa kwa vijana na Taifa kwa ujumla hapo baadaye.

“Ukiwekeza leo, kuna faida kubwa kesho. Tunawekeza kwenye michezo, maendeleo na utalii. Tunataka kuitoa Pangani pangoni na kuipandisha hadi kupaa angani,” amesema Mwinjuma.

Amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya michezo, huku ikiweka mkazo pia katika ugunduzi, malezi na utunzaji wa vipaji vya vijana.

TIMU YA U17 MFANO

Mwinjuma ametumia mafanikio ya timu ya Taifa ya vijana chini ya miaka 17 (U17) kama mfano wa matokeo ya uwekezaji katika vipaji.

Amesema timu hiyo imeonyesha uwezo mkubwa kwa kufika fainali ya michuano ya Afrika, kabla ya kupoteza mchezo huo, na baadaye kufuzu kwa mara ya kwanza kushiriki Kombe la Dunia.

Kwa mujibu wa Mwinjuma, Serikali imeendelea kusambaza mawakala na wataalamu katika maeneo mbalimbali ambako kuna mashindano ili kuhakikisha vipaji vinagunduliwa na kuendelezwa.

“Wadau wa michezo, Aweso Cup ina vipaji vingi. Kuna zaidi ya timu 80 zinazoshiriki. Tunawaomba wadau wa timu za Taifa, Simba, Yanga na klabu nyingine waje kuwaona vijana hawa kwa sababu wanaweza kufanya mambo makubwa,” amesema.

Amesema ni wakati sasa kwa wadau wa michezo kuanza “kuwathamini vyao” kwa kuwapa vijana wa Pangani na maeneo mengine nafasi ya kuonyesha uwezo wao.

Mashindano ya Aweso Cup yanatarajiwa kuwa jukwaa muhimu kwa vijana wa Pangani kuonyesha vipaji vyao, huku wadau wa michezo wakitarajiwa kutumia mashindano hayo kama sehemu ya kutafuta wachezaji wenye uwezo wa kuendelezwa zaidi.

Awali akizungumza  Waziri wa Maji na Mbunge wa Pangani kwa tiketi ya CCM, Jumaa Aweso, amewataka wadau wa michezo nchini kujitokeza katika mashindano mbalimbali ili kubaini na kuendeleza vipaji vya vijana.

Amesema mashindano hayo yameandaliwa kwa lengo la kuwapa vijana nafasi ya kuonyesha uwezo wao katika michezo, huku akisisitiza kuwa uwepo wa viongozi, makocha na wadau wengine ni muhimu katika kuwasaidia vijana wenye vipaji kufikia hatua kubwa zaidi.

“Wadau wa michezo tunapaswa kujitokeza katika mashindano kama haya kwa sababu hapa ndipo vipaji vinapopatikana. Vijana wanahitaji kuonekana, kutambuliwa na kupewa nafasi ya kuendeleza vipaji vyao,” alisema Aweso.

Amesema uwekezaji katika michezo unaweza kuwa sehemu muhimu ya kuwainua vijana kiuchumi, ikiwamo kuwapatia ajira na fursa nyingine kupitia michezo pamoja na sekta ya utalii.

Naye kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Michezo ambaye pia ni Katibu Tawala wa Wilaya hiyo (DAS), Esther Gama, alisema mashindano hayo yatachezwa kwa mfumo wa mtoano (Knock-out) na kutaja zawadi nono zinazowasubiri washindi ambapo Mshindi wa Kwanza (Bingwa):Tsh Milioni 10, Mshindi wa Pili: Tsh Milioni 5,Mshindi wa Tatu: Tsh Milioni 3 huku Kikundi Bora cha Ushangiliaji: Pikipiki aina ya Boxer.

MANARA: AWESO CUP INA DOUMBIA WENGI

September 13, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga, PANGANI

MSEMAJI wa Timu za Taifa za Tanzania, Haji Manara, amesema mashindano ya Aweso Cup 2026 yameibua vipaji vingi vya soka ambavyo kwa uwezo wake vinaweza kuizidi hata thamani ya mshambuliaji wa Simba, Ibrahim Doumbia.

Manara alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika uzinduzi rasmi wa michuano hiyo uliofanyika katika Uwanja wa Sakura, Pangani, Mkoa wa Tanga, akisisitiza kuwa Tanzania ina hazina kubwa ya vipaji vinavyohitaji kuibuliwa na kuendelezwa.

Kwa utani ulioibua shangwe na vicheko kutoka kwa mashabiki waliohudhuria uzinduzi huo, Manara alisema kiwango cha baadhi ya wachezaji alichokiona katika michuano hiyo kinaonyesha kuwa Pangani inaweza kuwa chanzo cha wachezaji wengi wenye uwezo wa kucheza soka la juu.

“Huyu Doumbia wa Simba anaweza kupatikana mara tano ndani ya michuano hii. Tumeshuhudia vipaji vikubwa sana hapa Pangani,” alisema Manara.

Kauli hiyo aliitoa huku akitumia fursa hiyo kuwataka wadau wa soka nchini kuendelea kuwekeza katika vipaji vya ndani badala ya kutegemea zaidi usajili wa wachezaji kutoka nje ya nchi.

Alisema Tanzania ina vijana wengi wenye uwezo mkubwa ambao wakipewa nafasi, mafunzo na mazingira mazuri wanaweza kufikia viwango vya juu na kuwa sehemu ya mafanikio ya soka la Taifa.

“Wakati mwingine badala ya kuwekeza kutafuta vipaji nje, tuna vipaji bora zaidi ndani ya Tanzania. Tusiishie tu kutafuta wachezaji nje, hata nyumbani hapa Pangani tumeona mechi zimechangamka,” alisema.

Manara, ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kariakoo, alisema idadi kubwa ya timu zinazoshiriki Aweso Cup ni ishara kwamba eneo hilo lina msingi mzuri wa kukuza vipaji vya soka.

Alisema kuwepo kwa takribani timu 80 katika jimbo moja la uchaguzi kunapaswa kuwa chachu kwa viongozi na wadau wa michezo kuangalia namna ya kuviendeleza vipaji hivyo kwa ajili ya soka la baadaye.

Katika hotuba yake, Manara pia alikumbusha historia ya Pangani katika kuzalisha wachezaji wenye majina makubwa, akimtaja nyota wa zamani wa Yanga, Fadili Bwanga, ambaye aliwahi kucheza soka la kulipwa nje ya nchi.

Michuano ya Aweso Cup 2026 imeandaliwa chini ya usimamizi wa Mbunge wa Pangani ambaye pia ni Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, ikiwa na lengo la kuibua na kukuza vipaji vya soka katika jimbo hilo.

Mashindano hayo yalizinduliwa rasmi na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma ‘MwanaFA’, katika hafla iliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali pamoja na mashabiki wa soka.

Manara alimpongeza Aweso kwa kuandaa mashindano hayo na kusema hatua hiyo ni muhimu katika kuwapa vijana nafasi ya kuonyesha vipaji vyao.

Aidha, aliahidi kuendelea kufuatilia michuano hiyo hadi hatua ya fainali.

TANZANITE ROYAL GIN YASOGEZA MBELE MANYARA TANZANITE MARATHON 2026, WASANII KUTUMBUIZA

August 19, 2026 Add Comment

 

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.
Na Mwandishi Wetu, Manyara

Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa na burudani ya aina yake baada ya wasanii maarufu nchini, Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue, kuthibitisha kushiriki na kutumbuiza katika tukio hilo litakalofanyika Agosti 22, 2026 mjini Babati, mkoani Manyara.

Ushiriki wa wasanii hao umewezeshwa na kampuni ya Mati Super Brands Ltd kupitia kinywaji chake cha Tanzanite Royal Gin, hatua inayoongeza ushiriki wa sekta binafsi katika kufanikisha mbio hizo zinazolenga kuunganisha michezo, burudani na shughuli za kijamii.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amekabidhi wasanii hao T-shirt rasmi za Manyara Tanzanite Marathon, ikiwa ni sehemu ya maandalizi kuelekea tukio hilo ambalo limeendelea kupata mwitikio kutoka kwa wadau mbalimbali.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 imebeba kaulimbiu “Hatua Moja Okoa Maisha”, ikiwa na lengo la kukusanya Shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa wodi maalumu ya kuwahudumia watoto njiti wanaozaliwa kabla ya wakati.
Ujio wa Dully Sykes, Banana Zoro na Mr Blue unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wanariadha, vikundi vya jogging na wananchi watakaoshiriki au kujitokeza kushuhudia mbio hizo. Burudani hiyo pia inalenga kuwapa washiriki na watazamaji uzoefu wa kipekee huku ikihamasisha jamii kuunga mkono kampeni ya kuokoa maisha ya watoto njiti..
Mchango wa Mati Super Brands Ltd kupitia Tanzanite Royal Gin unaendelea kuonesha nafasi ya sekta binafsi katika kusaidia shughuli zenye manufaa kwa jamii. Ushiriki huo unatarajiwa kuongeza mvuto wa marathon na kuwafikia watu wengi zaidi kupitia michezo na burudani.

Kwa ujumla, Manyara Tanzanite Marathon 2026 inatarajiwa kuwa jukwaa linalounganisha michezo, burudani, utalii na uwajibikaji kwa jamii, huku kila hatua ya washiriki ikilenga kuchangia upatikanaji wa huduma bora kwa watoto njiti mkoani Manyara.

WMA YASHIRIKI CRDB BANK MARATHON 2026

August 16, 2026 Add Comment

  

 Na WMA – Dar es Salaam

16 Agosti 2026

Wafanyakazi wa Wakala wa Vipimo (WMA) wameshiriki katika CRDB Bank Marathon 2026, iliyofanyika jijini Dar es Salaam, ambapo watumishi kutoka Makao Makuu Dodoma na WMA Mkoa wa Dar es Salaam waliungana na washiriki wengine katika mbio hizo.

DKT.DOTO BiTEKO ANOGESHA MASHINDANO YA NGALAWA TAMASHA KIZIMKAZI

August 13, 2026 Add Comment




Naibu Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko amesema kuwa mashindano ya ngalawa race ni miongoni mwa matukio makubwa ya kiburudani yanayoipamba Kizimkazi Festival 2026.


Mashindano hayo yamefanyika Kizimkazi, Kusini Unguja Agosti 12, 2026 yaliyokuwa na ushindani mkubwa ambapo Nassor Pandu wa Mkunguni ameibuka mshindi wa mashindano ya ngalawa ikiwa ni sehemu ya shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Tamasha la Kizimkazi.

“ Ni dhahiri kwamba mashindano haya yamekuwa muhimu kwa vijana na jamii kwa ujumla. Tukio hili limewaleta pamoja wadau mbalimbali na kuchangia kwa kiasi kikubwa juhudi za kuboresha mazingira ya michezo na burudani,” amesema Dkt. Biteko.

Dkt. Biteko ameongeza kuwa mashindano ya Ngalawa race Kizimkazi Festival yameendelea kutoa fursa za kiuchumi kwa vijana mbalimbali katika kushindana hadi kupata timu mbili bora za Mchangamle na Mkunguni ambapo kila timu imehusisha manahodha 10.



Mwisho.

STANBIC BANK PUMPS TZS 30 MILLION INTO 13TH CHINA ENTERPRISES BASKETBALL TOURNAMENT

August 01, 2026 Add Comment


#Msigwa, Amb. Chen lead opening ceremony in Dar


By Prosper Makene 

Dar es Salaam, Tanzania – Saturday, August 1, 2026: Stanbic Bank Tanzania_ has reaffirmed its commitment to community engagement and bilateral trade with a TZS 30 million sponsorship of the 13th Annual Chinese Enterprise Association (Tanzania)'s Basketball Tournament, which officially kicked off on Saturday at Don Bosco Grounds, Oysterbay.

MUHEZA YAJIZATITI KUANDIKA HISTORIA KWENYE MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2026

June 14, 2026 Add Comment

 




Na Mwandishi Wetu, Muheza

Mkuu wa Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, Ayoub Sebabili, amewahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi katika shughuli za mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026, akisema ushiriki mkubwa wa wananchi utasaidia wilaya hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Kitaifa ya Mwenge wa Uhuru.

Sebabili ametoa wito huo wakati wa zoezi la Jogging lililoandaliwa kama sehemu ya maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, ambapo aliwashukuru wananchi kwa kujitokeza kwa wingi na kushiriki shughuli hiyo.

Alisema Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kuwasili wilayani Muheza Juni 23, 2026 ukitokea Wilaya ya Mkinga na kupokewa katika eneo la Kilapura, huku ukitarajiwa kulala katika Uwanja wa Jitegemee.

"Niwashukuru kwa namna mlivyojitokeza leo. Ushiriki wenu unaonyesha dhamira ya kuhakikisha Muheza inafanya vizuri katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru. Kila mmoja wetu awe balozi wa kuhamasisha wananchi wengine kujitokeza kwa wingi," alisema Sebabili..

Kwa upande wake, Mratibu wa Mwenge wa Uhuru Wilaya ya Muheza Amiri Msuya alisema maandalizi yanaendelea vizuri na kuwa viongozi katika ngazi zote wamepewa jukumu la kuhamasisha wananchi wa makundi mbalimbali, wakiwemo vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika shughuli hizo.

Alisema Mwenge wa Uhuru utapitia maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo kwa ajili ya kuzindua na kukagua miradi ya maendeleo pamoja na kutoa ujumbe wa umoja, uzalendo na mshikamano wa kitaifa.

Kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa, Mwenge wa Uhuru utaanzia Kata ya Mlingano kabla ya kuelekea Machemba kwa uzinduzi wa mradi na ukaguzi wa banda la lishe litakaloonyesha juhudi za Halmashauri ya Muheza katika kupambana na utapiamlo, malaria na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.

Baadaye utaelekea katika Shule ya Venance Mabeyo na Kata ya Mpapayu kwa ajili ya uzinduzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo.

Katika Kata ya Genge, Mwenge wa Uhuru utazindua maabara katika Shule ya Sekondari Chief Mang'enya iliyojengwa kwa nguvu za wananchi na kuweka jiwe la msingi katika mradi wa madarasa mapya kwa ajili ya maandalizi ya wanafunzi wa Kidato cha Kwanza mwaka 2027.

Mratibu huyo alisema pia kutakuwa na shughuli za Klabu ya Wapinga Rushwa pamoja na programu mbalimbali za elimu kwa jamii.

Katika Kata za Magila na Majengo, Mwenge wa Uhuru utatembelea kikundi kilichonufaika na mkopo wa asilimia 10 wa Halmashauri unaotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, ambapo kikundi hicho kimepata Sh25 milioni kwa ajili ya shughuli za maendeleo ya kiuchumi.

Aidha, katika eneo la Mikwamba kutakuwa na maonesho ya fursa za zabuni kupitia PPRA, yakilenga kuhamasisha vikundi maalumu kushiriki katika zabuni zinazotengwa kwa makundi hayo.

Ratiba hiyo itahitimishwa kwa shughuli mbalimbali katika Kata ya Tongwe na eneo la Mpaa, ikiwemo uzinduzi wa daraja la karavati, uzinduzi wa Jengo la Havest Inn na mkesha wa Mwenge wa Uhuru katika Uwanja wa Jitegemee.

Viongozi hao wamewataka wananchi kuzingatia amani, utulivu na usalama katika kipindi chote cha shughuli hizo, huku wakisisitiza kuwa vitendo vya uhalifu na uvunjifu wa amani havitavumiliwa.

Akizungumza katika hafla hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) wa Muheza, Mohamed Mfaki, aliwashukuru wananchi kwa ushirikiano wao katika maandalizi ya mapokezi ya Mwenge wa Uhuru na kuwataka kuendelea kushiriki kikamilifu.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk Juma Mhina, alisema wilaya hiyo imejipanga kufanya vizuri zaidi mwaka huu na inalenga kushika nafasi ya kwanza kitaifa katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru


Alisema maandalizi yaliyoanza mapema chini ya usimamizi wa Mkuu wa Wilaya yanalenga kuongeza ushiriki wa wananchi na kuhakikisha shughuli zote zinafanyika kwa mafanikio makubwa.

"Malengo yetu ni kuona wananchi wanajitokeza kwa wingi katika shughuli zote za Mwenge wa Uhuru. Tunataka Muheza iwe mfano wa mafanikio na ushirikiano katika mapokezi ya Mwenge wa Uhuru 2026," alisema Dk Mhina.

mwisho

MBUNGE ANNE KILANGO AONGOZA MAPOKEZI YA SHUJAA WA AFCON U -17 SAME MASHARIKI

June 10, 2026 Add Comment



Mamia ya wananchi wa Kata ya Kalemawe, Kijiji cha karamba wilayani Same, wamejitokeza kwa wingi kumpokea nyumbani kwao nyota chipukizi wa soka, Issa Chole, ambaye ni mchezaji wa timu ya taifa ya vijana ya Serengeti Boys chini ya umri wa miaka 17.

Mapokezi hayo yaliongozwa na Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, Anne Kilango, pamoja na viongozi mbalimbali wa eneo hilo na wananchi waliokusanyika kumpongeza kijana huyo kwa kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya AFCON 2026 kwa vijana chini ya miaka 17.



Shangwe na nderemo zilitawala katika kijiji hicho huku wananchi wakionesha fahari yao kwa mafanikio ya Issa Chole, ambaye ameibuka kuwa mmoja wa vijana wanaolipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa kupitia mchezo wa soka.

Akizungumza katika hafla hiyo, Anne Kilango alisema mafanikio ya Issa Chole ni jambo kubwa kwa wakazi wa Same Mashariki na Taifa kwa ujumla kwani yanaonesha kuwa vijana wa eneo hilo wana uwezo wa kufikia ndoto zao wanapopewa fursa sahihi.


Alisema ujio wa mchezaji huyo nyumbani ni heshima kubwa kwa jimbo hilo na ushahidi kwamba uwekezaji katika michezo unaweza kuzaa matokeo chanya kwa vijana na jamii kwa ujumla.

Kilango alibainisha kuwa Issa Chole ni miongoni mwa vijana waliopitia mashindano ya Samia Cup, yanayoandaliwa kila mwaka katika Jimbo la Same Mashariki kwa lengo la kuibua na kukuza vipaji vya michezo.


Kwa mujibu wa mbunge huyo, zaidi ya timu 91 kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo hushiriki mashindano hayo, ambayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwapa vijana nafasi ya kuonesha uwezo wao.


Alisema kupitia mashindano hayo, vijana wengi wameanza kuonekana katika ngazi za juu za soka na wengine wamepata nafasi ya kujiendeleza katika taaluma ya michezo.


“Leo tunashuhudia matunda ya Samia Cup. Issa ametufanya tujivunie kama wananchi wa Same Mashariki na kama Watanzania. Hii ni ishara kwamba tuna vijana wengi wenye vipaji ambao wanahitaji kuungwa mkono,” alisema Kilango.


Aliongeza kuwa ataendelea kuimarisha mashindano hayo ili kuhakikisha vipaji zaidi vinaibuliwa na kupata nafasi ya kuiwakilisha Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.


Mbunge huyo pia aliahidi kuanzisha na kuendeleza michezo mingine ikiwemo mpira wa miguu kwa wasichana na mpira wa pete, kwa lengo la kuwapa vijana na watoto wa kike fursa zaidi za kukuza vipaji na kujenga ajira kupitia michezo.


Kwa upande wake, Issa Chole aliwashukuru wananchi wa Kalemawe pamoja na Anne Kilango kwa mapokezi makubwa aliyoyapata, akisema hakuwahi kutarajia kupokelewa kwa namna hiyo baada ya kurejea kutoka majukumu ya timu ya taifa.


Alisema mafanikio yake yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na mashindano ya Samia Cup yaliyompa nafasi ya kuonekana na kuanza safari yake ya soka la ushindani, huku akiwataka vijana wengine kushiriki mashindano hayo kwa nidhamu, kujituma na kuwa na malengo makubwa maishani.


Baba mzazi wa mchezaji huyo, Mzee Musa Chole, alisema anajivunia maendeleo ya mwanawe katika soka na kusisitiza kuwa nidhamu, mazoezi na kujituma ndiyo msingi wa mafanikio katika mchezo huo.Aidha, alimuomba Mbunge Anne Kilango kuendelea kuunga mkono vijana kupitia Samia Cup ili vipaji zaidi viweze kuibuliwa na kuendelezwa.


Naye mmoja wa wananchi wa Kata ya Kalemawe alisema jitihada za mbunge huyo katika kuendeleza michezo zimekuwa na manufaa makubwa kwa vijana, kwani zimewapa hamasa ya kujituma, kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya, ulevi na vitendo vingine vinavyoweza kuharibu maisha yao, huku akimpongeza kwa kujitokeza kushiriki mapokezi hayo ambayo yameonesha mshikamano mkubwa kati ya viongozi na wananchi.

MUHEZA YAANZA MBIO ZA MWENGE WA UHURU 2026

June 06, 2026 Add Comment

 

DC awapongeza wananchi kwa mwitikio mkubwa wa Jogging

Na Oscar Assenga, Muheza

MAANDALIZI ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026 katika Wilaya ya Muheza yamezidi kushika kasi baada ya wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mazoezi ya Jogging yaliyoandaliwa ikiwa ni sehemu ya kujiandaa na tukio hilo muhimu la Kitaifa.

Akizungumza baada ya mazoezi hayo, Mkuu wa Wilaya ya Muheza Ayoub Sebabili  aliwapongeza wananchi kwa mwitikio wao mkubwa, akisema ushiriki huo unaonyesha utayari wa wakazi wa wilaya hiyo kuupokea Mwenge wa Uhuru unaotarajiwa kuwasili Juni 23 mwaka huu.

Alisema mazoezi hayo yamelenga kuwaweka wananchi katika hali nzuri ya afya, kuimarisha mshikamano na kuwaandaa kimwili na kiakili kuelekea mapokezi ya mwenge huo.

“Tunawashukuru wananchi wote waliojitoa kushiriki mazoezi haya. Hii ni ishara nzuri ya ushirikiano katika maandalizi ya tukio muhimu la kitaifa ambalo Wilaya ya Muheza itakuwa mwenyeji wake,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alibainisha kuwa jogging nyingine itafanyika Juni 13 mwaka huu na kutoa wito kwa wananchi ambao hawakupata nafasi ya kushiriki safari hii kujitokeza kwa wingi ili kuwa sehemu ya maandalizi hayo.

Alisisitiza kuwa mazoezi hayo ya kilomita tano yanafanyika kwa mwendo wa kawaida ili kuwezesha kila mwananchi kushiriki bila kujali umri au hali yake ya kiafya.

“Tunawakaribisha vijana, wanawake, wazee pamoja na watu wenye ulemavu kushiriki mazoezi haya. Lengo letu ni kuona wananchi wote wanakuwa sehemu ya maandalizi ya kuupokea Mwenge wa Uhuru 2026,” alisema.

Muheza inatarajia kuupokea rasmi Mwenge wa Uhuru Juni 23, huku maandalizi mbalimbali yakiendelea kufanyika kuhakikisha tukio hilo linafanyika kwa mafanikio na kuacha alama chanya kwa wananchi wa wilaya hiyo.