WAMILIKI WA VYOMBO VYA USAFIRI JIJINI TANGA WATISHIA KUSITISHA HUDUMA

November 14, 2013
Na Oscar Assenga, Tanga.
BAADHI ya wamiliki wa vyombo vinavyotoa huduma ya Usafiri jijini Tanga wametishia kusitisha kuendelea kutoa huduma hiyo kutokana na gharama kubwa wanazozipata wakati wa matengenezo yanayotokana na ubovu wa barabara zilizopo jijini Tanga.
Hatua hiyo inatokana na baadhi ya barabara za jijini Tanga kuwa na mashimo hali ambayo inapelekea kuleta usumbufu mkubwa kwa watumiaji wake hasa nyakati zinapokuwa zikinyesha mvua.

Mwenyekiti wa Muungano wa wasafirishaji abiria mkoa wa Tanga,(Muwata) Hatwabi Shabani  alisema barabara ambazo zimekuwa kero kubwa sana ni Sahare, Makorora, Mikanjuni, Raskazone mwisho,Japani,Kivumbitifu na Kasera.

Shabani alisema kutokana na ubovu wa njia hizo wamiliki wa magari zinazofanya safari zake katika maeneo hayo wamekuwa wakipata hasara na hivyo kumuomba mkurugenzi wa Jiji la Tanga kuangalia uwezekano wa kuzifanyia matengezo barabara hizo.

Mwenyekiti huyo alisema wao kupitia muungano wao wanaomba maeneo hayo yafanyiwe matengenezo madogo madogo angalau kufukia yale mashimo ambapo magari mengi yanaharibika kitendo ambacho kinapelekea baadhi ya wamiliki kutaka kuhamisha magari kutokana na gharama kubwa za matengenezo.

Aliongeza kuwa wanaiomba Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha wanazifanyia kazi changamoto hizo ili chama hicho kiweze kutoa huduma bora kwa wakazi wa Jiji la Tanga.

TAARIFA KUTOKA SHIRIKISHO LA SOKA NCHINI TFF LEO

November 14, 2013
Release No. 195
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Novemba 14, 2013

KIM ATEUA 32 KUIKABILI KENYA
Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ameunda kikosi cha wachezaji 32 kwa ajili ya mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Kenya (Harambee Stars) itakayochezwa Jumanne, Novemba 19 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kikosi hicho kinajumuisha wachezaji 16 walioitwa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, na wengine 16 kutoka Future Taifa Stars. Awali kambi ya Future Taifa Stars iliyoanza Novemba 9 mwaka huu na kuvunjwa leo asubuhi ilikuwa na wachezaji 30.

Wachezaji walioitwa ni makipa wanne; Aishi Manula (Azam), Ally Mustafa (Yanga), Deogratias Munishi (Yanga) na Ivo Mapunda (Gor Mahia, Kenya). Mabeki ni Aggrey Morris (Azam), Ismail Gambo (Azam), Kelvin Yondani (Yanga), Michael Pius (Ruvu Shooting), Nadir Haroub (Yanga) na Said Moradi (Azam).

Viungo wakabaji ni Erasto Nyoni (Azam), Himid Mao (Azam), Shomari Kapombe (AC Cannes, Ufaransa) na Vincent Barnabas anayechezea Mtibwa Sugar ya Morogoro. 

Viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruna Chanongo, Hassan Dilunga (Ruvu Shooting), Jonas Mkude (Simba), Ramadhan Singano (Simba), Salum Abubakar (Azam) na William Lucian (Simba).

Viungo washambuliaji ni Faridi Musa (Azam), Joseph Kimwaga (Azam), Mrisho Ngasa (Yanga), Mwingi Kazimoto (Markhiya, Qatar) na Simon Msuva (Yanga).

Washambuliaji ni Elias Maguli (Ruvu Shooting), Juma Liuzio (Mtibwa SugarMbwana Samata (TP Mazembe, DRC) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, DRC).
Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)