JAMII IELIMISHWE KUHUSU USULUHISHI NJE YA MAHAKAMA-JAJI MKUU

June 21, 2024

 Na Mwandishi Wetu -WKS


Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema kuwa ni vyema Wizara ya Katiba na Sheria kupitia Kampeni ya Msaada wa Kisheria ya Mama Samia ikaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu faida za kufanya usuluhishi wa migogoro nje ya Mahakama ili kuepuka kutumia muda mrefu kusikiliza Mashauri, kuepuka gharama kwa wanaohusika katika migogoro (Wadaawa) na kuepuka msongamano wa Mashauri Mahakamani.


Profesa Ibrahim alisema hayo katika mazungumzo na Naibu Waziri wa Wizara ya Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini wakati alipomtembelea Jaji Mkuu katika Ofisi za Mahakama ya Rufani Kivukoni Jijini Dar es Salaam Juni 20,2024 kwa lengo la kufahamu majukumu na muundo wa Muhimili wa Mahakama, Kuimarisha mashirikiano baina ya Wizara na Muhimili na kujifunza namna walivyoweza kufanikiwa kwenye masuala ya miradi ya maendeleo na matumizi ya TEHAMA.


“Katiba ya Tanzania katika kipengele cha utoaji haki, inasisitiza katika kukuza na kuendeleza usuluhishi baina ya wanaohusika katika migogoro. Suala la kusuluhishwa kwa dakika thelathini linaweza kuchukua miaka zaidi ya kumi. Zipo baadhi ya Nchi ambazo zaidi ya asilimia tisini na tano (95%) ya Mashauri yanaisha kwa njia ya Usuluhishi. Ni vyema Sheria ielekeze kuwa, kabla ya suala kwenda Mahakamani lianze kwenye Usuluhishi kwani najenga ukaribi na sio uadui.” Alisema Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof Ibrahim Hamis Juma.


Kwa upande wake Naibu Waziri wa Katiba na Sheria Mhe. Jumanne Sagini ameupongeza Muhimili wa Mahakama kwa kazi kubwa wanazofanya katika kusimamia utoaji haki kwa Wananchi, kusimamia ujenzi wa Mahakama katika maeneo mbalimbali Nchini na pia kufanya mageuzi katika utendaji wa Mahakama ikienda sambamba na matumizi ya TEHAMA.


Katika mazungumzo hayo, Naibu Waziri Sagini amesema katika kipindi cha nyuma cha utendaji kazi kama Katibu Tawala, kumekuwa na changamoto ya Kamati ya Maadili ya Mahakimu katika ngazi za Wilaya na Mikoa kutokutana na kufanya vikao na limekuwa likisahaulika ambapo Jaji Mkuu amesema kuwa kwa sasa Kamati hiyo ikiwa na Katibu wa Tume ya Utumishi wa Mahakama imekuwa ikizunguka katika Mikoa mbalimbali Nchini kwa lengo la kuzijulisha Kamati za Wilaya na Mikoa namna ambavyo zinatakiwa kufanya kazi na kuzijengea uwezo zaidi.


Kikao hicho kilihudhuriwa na Msajili Mkuu wa Mahakama Mhe. Eva Kiaki Nkya, Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe. George Hillary Herbet, Naibu Msajili Mahakama Kuu Mhe. Venance Mlingi ambaye pia ni Katibu wa Jaji Mkuu wa Tanzania na Mhe. Hakimu Mkazi Jovine Constatine ambaye pia ni Katibu wa Msajili Mkuu wa Mahakama.





SERIKALI KUJA NA MKAKATI WA ULINZI KWA WATU WENYE UALBINO

June 21, 2024

 -Serikali kuja na mkakati wa ulinzi wa watu wenye Ualibino


Na Janeth Raphael MichuziTv- Bungeni Dodoma

Serikali kuja na Mpango wa Kuzuia Ukatili dhidi ya Watu wenye Ualbino (NAP) kwa kushirikiana na Chama cha Watu wenye Ualbino (TAS) na Wakuu wa Mikoa wote Tanzania Bara kwa lengo la kuweka mikakati ya pamoja ya ulinzi wa watu wenye ualbino.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa wakati wa kipindi cha maswali ya papo kwa papo kuhusu kupinga ukatili dhidi ya watu wenye ualbino.

Ameongeza kusema Serikali itaendelea Kutoa elimu ya ukatili dhidi ya Watu wenye Ulemavu wakiwemo Watu wenye Ualbino kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii, Maafisa Maendeleo ya Jamii na Maafisa Elimu Maalum wa Mikoa yote nchini.

“Tufanya mapitio ya Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2004 ikiwa ni pamoja na kuandaliwa kwa Mkakati wake wa Utekelezaji wa Miaka Mitano (National Five Year Implementation Strategy 2024/2025- 2029/2030) na Mkakati wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Miaka Mitano ambayo itazinduliwa mwaka ujao wa fedha 2024/2025,” alisema Waziri Mkuu.

Aidha serikali itakamilisha na kuzindua Mkakati wa miaka mitatu 2024-2027 wa Upatikanaji wa Teknolojia saidizi kwa Watu wenye Ulemavu wakiwemo watu wenye Ualbino, mkakati huu umepangwa kuzinduliwa mwezi Julai, 2024.

Ambapo ubainishaji na usajili wa watu wenye ulemavu ngazi za kijiji na mtaa kwa kutumia Mfumo wa Kielektroniki na Kazidata ya Watu wenye Ulemavu litaendelea ikiwa ni pamoja na kusimamia utekelezaji wa Mwongozo wa Ujumuishwaji wa Watu wenye Ulemavu.
Katika hatua Nyingine Waziri Mkuu, Mhe. Majaliwa amesema serikali itaboresha mifumo ya kisheria ili kuimarisha ulinzi na usalama wa mtoto kwa kufuata Sheria ya Mtoto Sura ya 13, Kanuni za ulinzi wa Mtoto za Mwaka 2015 na Mfumo wa Taifa Jumuishi wa Usimamizi wa Mashauri ya Watoto, Katika kuwahudumia watoto wanaohitaji ulinzi na usalama.

Pia tutanzisha Mfumo wa taarifa Jumuishi wa kitaifa wa kushughulikia Mashauri ya watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi nchini (NICMS 2017). Hadi Aprili, 2024, jumla ya watoto 708,957 (ME 340,661, KE 368,296) wanaoishi katika mazingira hatarishi wametambuliwa katika Halmashauri zote nchini na kupatiwa huduma kulingana na mahitaji yao.

“Tunatarajia kuanzisha Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto kupitia Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA). Halmashauri zote 184 zimepewa jukumu la kutoa elimu, kulinda na kutoa taarifa kuhusiana na ukatili, “alisema Waziri Mkuu.

Ameeleza kuhusu uanzishwaji wa Dawati la Ulinzi na Usalama wa Mtoto Ndani na Nje ya Shule. Sambamba na Kuanzisha Nyumba Salama kwa ajili ya kuhudumia Wahanga wa ukatili. Ambapo jumla ya Nyumba salama 16 katika mikoa 9 ya Tanzania Bara zimeanzishwa hadi kufikia Aprili 2024;