Na Stella Kalinga, Simiyu
Serikali mkoani Simiyu imeomba kuwepo kwa kikundi cha ulinzi cha kijeshi katika Wilaya ya Busega ili
kusaidia mapambano dhidi ya vitendo vya uhalifu ikiwemo uvuvi haramu na kuwezesha ufugaji wa samaki
ndani ya Ziwa Victoria kufanyika kwa usalama.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe.Anthony Mtaka wakati wa Hafla ya kumpongeza
Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi hapa nchini, Jenerali Venance Mabeyo iliyoandaliwa na ndugu zake kijijini
kwao Yitimwila ‘A’ katika Kata ya Kiloleri Wilayani Busega.
“Tumepata changamoto nyingi sana kwenye ziwa, matukio mengi ya kihalifu liliwemo la uvuvi haramu ,
sisi kama mkoa tulikuja na wazo kwamba tungehitaji tupate ‘detouch’ moja eneo la Ziwa ili ukanda huu
baada ya kufanya kazi kubwa ya kuchoma makokoro ya wananchi, tuwapeleke kwenye uvuvi wa kisasa
hususani ufugaji wa samaki ziwani, jambo ambalo Mheshimiwa Rais analipa kipaumbele sana; na namna
pekee ya kufanya ufugaji ule wa samaki ziwani, suala la ulinzi na usalama ni muhimu sana; ” alisema Mtaka.
Mkuu
wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Venance Mabeyo (katikati) akionesha silaha
alizokabidhiwa na Wazee wa Busega kama ishara ya ushujaa kwake wakati
wa hafla iliyoandaliwa na ndugu zake kijijini kwao Yitimwila A wilayani
Busega kumpongeza kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe.Dkt.John Magufuli.
Aidha, Mtaka amesema pamoja na kufanya ufugaji wa samaki katika Ziwa Victoria, Serikali ya Mkoa
imefanya makubaliano na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii NSSF kuwawezesha wananchi wa Busega kufanya
kilimo cha Umwagiliaji kwa kutumia maji ya ziwa hilo ambayo ni ya uhakika.
“Tumeongea na NSSF kwa ajili ya kuanzisha mradi ambao hautazidi bilioni moja, tutaleta mbegu za aina ya
nyanya na pilipili zinazotakiwa ili wananchi wa Busega wazalishe kwa wingi. Hatutakuwa tayari kuona
wananchi wanalima nyanya na kuuza ndoo moja shilingi 500, tumepanga kuanzisha mradi wa kuzalisha
‘chill sauce’ na ‘tomato source’ .”alisema Mtaka.
Ameongeza kuwa Wataalam wa Wilaya na Mkoa kwa kushirikiana na Wataalam wa Wizara ya Maji na
Umwagiliaji , Kituo cha Utafiti wa Kilimo Ukiriguru wanafanya upembuzi yakinifu kuona namna
miundombinu ya umwagiliaji itakavyojengwa ili kuwawezesha wananchi wa Busega kulima muda wote
kupitia kilimo cha Umwagiliaji badala ya kutegemea mvua.
Mkuu
wa Mkoa wa Simiyu,Mhe.Anthony Mtaka akizungumza na viongozi na waalikwa
katika hafla ya kumpongeza Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance
Salvatory Mabeyo, kijijini kwao Yitimwila A wilayani Busega, kuteuliwa
na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt.John Magufuli kwa
nafasi hiyo.
Mtaka amesema Serikali mkoani Simiyu imedhamiria kuhakikisha katika kipindi cha miaka mitatu ijayo
Mkoa hauingizi bidhaa kutoka mikoa mingine na badala yake wananchi wake watazalisha na kutumia bidhaa
zao wenyewe, hivyo ameomba Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kuona namna ya kuweka vituo vya kuuza zana
za kilimo katika maeneo ya kanda ya Ziwa ili wananchi wapate zana bora za kisasa zitakazowasaidia kulima
kisasa.
Kwa upande wake Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi hapa nchini, Jenerali Venance Mabeyo amewataka wananchi
wa Busega kubadili mtazamo wao na kutumia maji ya ziwa Victoria kwa manufaa yao kwa ajili ya kilimo
cha umwagiliaji ili wasikumbwe na tatizo la upungufu wa chakula kunapotokea ukame.
Kuhusu suala la ulinzi katika Ziwa Victoria amesema ombi la Serikali ya Mkoa la kuwa na kikundi cha
Ulinzi, viongozi watalitafakari kuona namna ya kulishughulikia na akaeleza kuwa tayari Jeshi limeweka
kikundi kidogo cha kiulinzi kutoka Jeshi la wanamaji, lakini kutokana na ukubwa wa Ziwa Victoria kikundi
hicho hakiwezi kuhimili kufanya doria maeneo yote na akaahidi kukiimarisha zaidi.
Mkuu
wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance Mabeyo, akizungumza na viongozi na
waalikwa mbalimbali kijijini kwao Yitimwila A wilayani Busega , katika
hafla ya kumpongeza kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe.Dkt.John Magufuli kwa nafasi hiyo.