Showing posts with label elimu. Show all posts
Showing posts with label elimu. Show all posts

BI.SAKINA MWINYIMKUU: JENGENI UTAMADUNI WA UTENDAJI UNAOTEGEMEA MATOKEO

July 25, 2025 Add Comment


*Dodoma, Julai 25, 2025*  

Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Bi. Sakina Mwinyimkuu, amewataka watumishi wa umma kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo ya ufuatiliaji na tathmini ili kuongeza uwajibikaji na ufanisi katika kazi zao.

Akifunga rasmi mafunzo hayo ya siku tano yaliyofanyika jijini Dodoma, Bi. Sakina amesisitiza umuhimu wa kujenga utamaduni wa kazi bora unaozingatia matokeo (results-based performance), kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

> “Mafunzo haya si kwa manufaa yenu binafsi pekee, bali yatumike kama nyenzo ya kuleta mabadiliko chanya katika taasisi zenu, sambamba na kuendeleza maadili ya uwajibikaji,” amesema Bi. Sakina.

Ametoa rai kwa washiriki kuwa mabalozi wa kueneza uelewa huo kwa wengine katika maeneo yao ya kazi, ili kuimarisha utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia viwango vya kitaifa vya ufuatiliaji na tathmini ya maendeleo.





KAMPENI YA "TUWAAMBIE KABLA HAWAJAHARIBIWA" YAENDELEA SEKONDARI ROBANDA ,SERENGETI

July 16, 2025 Add Comment

Katika mwendelezo wa kampeni ya kitaifa ya TUWAAMBIE KABLA HAWAJAHARIBIWA, Sajenti Emmanuel kutoka Jeshi la Polisi, kitengo cha Dawati la Jinsia na Watoto, ametembelea Shule ya Sekondari Robanda iliyopo Kijiji cha Robanda, Kata ya Ikoma, Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, na kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na wanafunzi wa kidato cha tano.


Akiwa shuleni hapo, Sajenti Emmanuel amewahimiza wanafunzi hao kujitambua na kuelekeza nguvu zao katika masomo ili kufikia malengo yao ya kitaaluma na maisha kwa ujumla, amesisitiza umuhimu wa kuepuka mahusiano ya kimapenzi wakiwa bado shuleni, akieleza kuwa vitendo hivyo vimekuwa chanzo kikuu cha kukatisha ndoto za wanafunzi wengi nchini.

Aidha, amewataka wanafunzi kuwa mstari wa mbele katika kupambana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa kutoa taarifa mapema kwa mamlaka husika, amebainisha kuwa taarifa zinaweza kutolewa katika ofisi ya Dawati la Jinsia na Watoto iliyo katika kituo cha polisi, kwa Afisa wa Ustawi wa Jamii, au kwa viongozi wa serikali ya kijiji na kata.

Kampeni hiyo inalenga kuwafikia vijana walioko mashuleni na katika jamii kwa ujumla, ikiwa ni jitihada za pamoja kati ya serikali, vyombo vya dola, na wadau wa maendeleo katika kutokomeza matukio ya ukatili wa kijinsia na kusaidia vijana kufikia ndoto zao kwa usalama.

KIKWETE NA MALALA WAONYA: BAJETI ZA ELIMU ZISIPUUZWE WAKATI WA MISUKOSUKO YA KIUCHUMI NA KISIASA DUNIANI

July 15, 2025 Add Comment

 Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai, wameonya juu ya mwenendo hatarishi duniani wa kupunguza au kupuuza bajeti za elimu hasa wakati wa misukosuko ya kiuchumi na kisiasa.


Wakizungumza kwenye mjdala kuhusu elimu uliofanyika Jumapoili usiku katika hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam, viongozi hao wawili waliwataka viongozi wa serikali, wafadhili na washirika wa maendeleo kulinda na kuendeleza uwekezaji kwenye elimu, wakisisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya kudumu.


“Elimu haipaswi kuwa mhanga wa kwanza wakati wa janga. Si anasa—ni uhai wa maendeleo,” alisema Dkt. Kikwete. “Tukiacha kuwekeza katika elimu leo, tunajitengenezea matatizo makubwa kesho.”


Malala aliongeza kuwa madhara ya kupunguzwa kwa bajeti ya elimu huathiri zaidi wasichana. “Kila matatizo yanapotokea, wasichana ndiyo huathirika kwanza—hutolewa shule, ndoto zao hukatizwa. Hili si tu dhuluma, bali ni upumbavu wa kisera,” alisema.


Katika ziara yao katika Shule ya Sekondari Kibasila siku ya Jumatatu, Dkt. Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya GPE, alitangaza kuwa Tanzania itapokea msaada wa dola milioni 88 za Kimarekani kuanzia mwakani. 


Dkt. Kikwete alisema tangu kujiunga na GPE mwaka 2013, Tanzania imepokea zaidi ya dola milioni 344 zilizowezesha ujenzi wa zaidi ya madarasa 3,000, vyoo 7,600, nyumba za walimu 64, shule mpya 18, vituo vya walimu 252, na usambazaji wa vitabu milioni 36.


Kwa upande wake, Malala alitangaza msaada wa dola milioni 3 kutoka kwenye Malala Fund kusaidia wasichana waliokatishwa masomo kutokana na ujauzito au sababu nyingine za kijamii.


Malala pia alipongeza hatua ya serikali ya Tanzania ya mwaka 2021 ya kuruhusu wasichana waliopata ujauzito kurejea shule. 


“Uamuzi huu ulikuwa wa kishujaa na wa kibinadamu,” alisema. “Wasichana sasa wanaweza kurudi shule ndani ya miaka miwili au kujiunga na vituo vya elimu mbadala.”


Hata hivyo, wote walikiri changamoto bado zipo, na kwamba chini ya asilimia 50 ya wasichana wanaokamilisha shule ya msingi, na ni asilimia 16 pekee wanaoendelea hadi sekondari ya juu, sababu kubwa  zikiwa ni umaskini, mila kandamizi, na uhaba wa miundombinu.


Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga, alieleza kuwa kupitia Mpango wa Samia Scholarship ulioanzishwa 2023, wasichana 1,320 tayari wamenufaika kwa kusomea kozi za sayansi vyuo vikuu.


“Mpango huu pamoja na sera ya re-entry ni silaha muhimu kuhakikisha wasichana hawapotei kwenye mfumo wa elimu,” alisema.


Dkt. Neema Mwakalinga, mchambuzi wa elimu, alisema ushirikiano na GPE na Malala Fund umeinua hadhi ya Tanzania kimataifa. “Sio tu fedha—ni pia ushauri wa kitaalamu, uraghibishaji, na dhamira ya kisiasa ya kweli.”

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary  Kipanga, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai akivishwa skafu alipowasili kutembelea  shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika moja ya madarasa walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika moja ya madarasa walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai  akiwa na baadhi ya wanafunzi wanamichezo alipotembelea  shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaamsiku ya Jumatatu. 

  

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakimwagilia mti baada ya Malala Kuupanda, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. Kushoto  ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati yeye na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. 

 Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akipokea zawadi ya kitabu kutoka kwa mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai baada ya mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akimpa zawadi ya kitabu cha  Global Partnership for Education (GPE)  mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai baada ya mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu
 

NISHATI SAFI YA KUPIKIA NI AGENDA YA DUNIA,WIZARA INAITEKEKEZA KWA VITENDO - DKT.KAZUNGU

July 04, 2025 Add Comment


*📌Apokea Magari Mawili kutoka Umoja wa Ulaya kwa ajili ya kuanza kampeni ya kutoa elimu ya uhamasishaji wa nishati safi ya kupikia nchi nzima*


*📌 Amshukuru Dkt Samia kwa kuwa kinara wa nishati safi na kuibeba ajenda hiyo*


*📌 Umoja wa Ulaya waridhishwa na jitihada za Tanzania kwenye kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia*


*📌UNCDF yaahidi kushirikiana na Wizara kuhakikisha watanzania wanafikiwa na elimu ya nishati safi*


Naibu katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia umeme na nishati Jadidifu, Dkt Khatibu Kazungu leo 04 Julai, 2025 amepokea magari mawili yatakayotumika kwa ajili ya kampeni ya kuhamasisha na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia chini ya kampeni ya nishati safi ya kupikia Okoa Maisha na Mazingira itakayoendeshwa nchi nzima na Wizara ya nishati kwa kushirikiana na UNCDF.

‘’ Ajenda ya Nishati safi ya kupikia ni ajenda ya Dunia na sisi Wizara ya Nishati tuko tayari kwa utekelezaji ili kumuunga mkono Mhe. Rais Samia’’ Amesema Dkt. Kazungu

Aidha, ameishukuru Umoja wa Ulaya, na UNCDF kwa kutekeleza mradi wa nishati safi ya kupikia chini ya mfuko wa Cook fund kwa kuwa umesaidia kubadili maisha na mitazamo ya wananchi kuhusu  utekelezaji wa miradi ya Nishati safi.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo,  Balozi wa Umoja wa Ulaya Mhe. Balozi Christine Grau amesema umoja wa Ulaya uko tayari kuendelea kuisaidia Tanzania kwenye utekelezaji wa Nishati safi ya kupikia na tayari EU imetoa kiasi cha Euro Milioni 19.4 sawa na shilingi Bilioni 59 kutekeleza miradi ya nishati safi ya kupikia kwa mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Pwani, Morogoro  na Mwanza. 

Kuhusu magari amesema magari hayo mawili yana thamani ya Euro 130,000 na amewataka wizara ya Nishati kuhakikisha wananchi wa vijijini wanafikiwa na nishati safi ya kupikia

Tanzania inajipanga kutekeleza kwa vitendo mkakati wa Taifa wa Nishati safi ya kupikia chini ya mkakati wa Mawasiliano wa Taifa ili kutoa elimu kwa wananchi na kufikia lengo la Serikali la asilimia 80 ya watanzania kuanza kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.




CRDB Bank Foundation, StartHub Africa zaungana kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu

June 13, 2025 Add Comment

 

Meneja Uendelezaji Biashara Changa wa CRDB Bank Foundation, Sharron Nsule akitoa elimu ya ujasiriamali kwa wanafunzi walioshiriki semina katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Dar es Salaam, Tanzania – June 2025: Katika kuendeleza jitihada za kuinua ujasiriamali na kuwawezesha wanafunzi wabunifu, Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kushirikiana na StartHub Africa imevitembelea vyuo vikuu vitatu nchini na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanafunzi wanaopenda kumiliki biashara baada ya masomo yao.

Ushirikiano huo unaotekelezwa kupitia programu ya “Uni Launch and Scale” tayari umewafikia zaidi ya wanafunzi 1,000 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Chuo Kikuu cha Iringa na Taasisi ya Uhasibu Arusha (AIA) na kuwapa fursa ya kupata walezi wa kibiashara na mitaji wezeshi kutoka CRDB Bank Foundation.

Akizungumzia mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Esther Mwambapa amesema vyuo hivi vitatu ni mwanzo tu kwani lengo lililopo ni kuwafikia wanafunzi wengi zaidi na kuwawezesha ili wanapohitimu au wakai wanaendelea na masomo yao waanze kushiriki shughuli za kuujenga uchumi baada ya kuwapa elimu ya fedha, mafunzo ya ujasiriamali na uhakika wa kupata mtaji wezeshi.

“Lengo letu ni kuamsha ari ya ujasiriamali iliyomo ndani ya wanafunzi wetu wa vyuo vikuu na kutoa mazingia rafiki kwao kuanzisha biashara zitakazoajiri vijana wenzao badala ya wao wenyewe kuwa waombaji wa kazi wakihitimu. Kupitia ushirikiano huu tunajenga kizazi cha vijana waliowezeshwa kushiriki kuujenga uchumi wa taifa letu,” anasema Tully.

Katika vyuo vitatu ambako wataalamu wa CRDB Bank Foundation na StartHub Africa wamepita, jumla ya biashara 30 zinazomilikiwa na kuendeshwa na wanafunzi zitachaguliwa baada ya kukaguliwa ili kuingizwa kwenye mpango maalumu wa mafunzo ya usimamizi na uendeshaji biashara, utayari wa kifedha na utimamu wa bidhaa.

“Kwa kushirikiana na StartHub Africa pamoja na vyuo vikuu hivi, tunaamini tunaendeleza juhudi za kukuza ubunifu hasa wa kidijitali miongoni mwa wanafunzi wetu hivyo kujenga msingi imara wa biashara zinazoweza kukua na kuwanufaisha wananchi wengi,” amesema Tully.

Programu ya Uni Launch and Scale ambayo CRDB Bank Foundation inashirikiana na StartHub Africa kuitekeleza inalenga kuwawezesha wanafunzi wa vyuo vikuu kutekeleza uwekezaji wanaoukusudia kwa kuwapa mafunzo, ulezi wa kibiashara na uwezeshaji wa mitaji kupitia Programu ya Imbeju iliyojielekeza kuwainua vijana, wanawake na makundi maalumu.

Meneja Programu wa StartHub Africa, Zagaro Emanuel anasema katika ushirikiano huu wanakusudia kuwawezesha vijana wengi wabunifu kupitia mafunzo ya ujasiriamali na elimu ya fedha hivyo kuchangia kuujenga uchumi na kusukuma mbele maendeleo ya Tanzania.

“Tunawahamasisha wanafunzi na wahitimu wa vyuo vikuu, tunawandaa waanzilishi wapya wa biashara watakaosaidia kuleta mapinduzi ya kiuchumi na kuimarisha ujasiriamali nchini kwa kushirikiana na vyuo vikuu, wawekezaji na wawezeshaji. Tukiwa pamoja na Taasisi ya CRDB Bank Foundation, tunaamini tutafika mbali na kuwajumuisha wanafunzi wengi zaidi nchini,” anasema Emanuel.

Meneja huyo anaongeza kwamba programu hiyo inawapa wanafunzi jukwaa la kujitangaza katika soko la ndani, kitaifa na kimataifa na wanapowasilisha mawazo ya miradi yao, wanajiweka kwenye nafasi nzuri zaidi ya kuvutia mitaji huku vyombo vya habari vikiwarahisishia kujulikana kwa biashara zao hivyo kujiongezea umanifu kwa wadau ambalo ni jambo jema kwa kila biashara.

DKT.BITEKO AFURAHISHWA NA UTATUZI CHANGAMOTO ZA ARDHI MONDULI

April 24, 2025 Add Comment


📌 Azindua Shule ya Sekondari Migungani, awataka wanafunzi kutunza miundombinu


📌 Asema Serikali yajipanga kujenga mradi mkubwa wa umeme Monduli


Na Ofisi ya Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati


Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ameupongeza uongozi wa Wilaya ya Monduli kwa jitihada zao za kutatua migogoro ya ardhi wilayani humo ikiwa ni utekelezaji wa agizo la  Serikali la  kuwataka viongozi kutatua changamoto za wananchi katika maeneo yao.

Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo Aprili 23, 2025 wilayani Monduli, mkoani Arusha wakati akihutubia wananchi mara baada ya kuzindua Shule Mpya ya Sekondari ya Migungani iliyopo wilayani humo.


“Naomba kuwapongeza tena uongozi wa Wilaya ya Monduli kwa kuendelea kufanya kazi nzuri sana hapa wilayani kwa maslahi mapana ya wananchi wa Monduli. Nimejulishwa kuwa, mmefanya mengi mno ikiwemo utatuzi wa changamoto na migogoro ya ardhi hapa wilayani. Nimejulishwa kuwa sehemu kubwa ya changamoto hizi mmefanikiwa kuzitatua hongereni sana,” amesema Dkt. Biteko.

Ameipongeza pia kamati ya kutatua kero za wananchi inayoongozwa na Mkuu wa Wilaya ikiwa na wataalamu mbalimbali ambayo imejiwekea utaratibu wa kupokea kero kutoka kwa wananchi na kuzipatia ufumbuzi, ambapo ameitaka pia iratibu zoezi la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu masuala ya ardhi.

Akiwa shuleni hapo, Dkt. Biteko amewapongeza wananchi kwa kujenga shule hiyo ya Sekondari Migungani na kufikia asilimia 85 ya ujenzi huku Serikali ikichangia shilingi milioni 500.


“ Sote tunafahamu kuwa, elimu ni msingi mkubwa wa maendeleo. Sisi wana Monduli tayari tunayo shule yetu hii ambayo imeshakamilika. Hii ni miongoni mwa shule zilizopo Wilayani hapa ambazo zitaendelea kutupatia elimu kwa vijana wetu,” amesema Dkt. Biteko.

Ameongeza kuwa Shule hiyo itakuwa na uwezo wa kuwa na wananfunzi 400 na hivyo amewataka wanafunzi kutunza miundombinu sambamba na kujifunza kwa bidi ili wajiandae kuwa wazalendo na raia wema huku wakiwa na uwezo wa kutafuta majibu ya matatizo watakayokumbana nayo.


Kuhusu miradi ya umeme wilayani humo, amesema kuwa mwaka huu Serikali inatarajia kujenga mradi mkubwa wa umeme kwa lengo la kuuongezea nguvu umeme  unaopatikana ili uweze kufika  Loliondo na kusaidia wilaya hiyo kuwa na  umeme wa uhakika.

Aidha, Dkt. Biteko amezungumzia maadhimisho ya miaka 61 ya Muungano kwa kuwataka Watanzania kuenzi muungano huo kwa kujenga Taifa moja kwa kushikamana  na kufanyakazi kwa pamoja kwa kushirikiana.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Festo Kiswaga amesema kuwa Wilaya hiyo ni tegemeo kwa Chama Cha Mapinduzi na wamekuwa wakishirikiana na wananchi katika kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo.

Pia, amesema Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo barabara, hospitali, shule na kuwa Wilaya hiyo ni kati ya wilaya zinazofanya vizuri katika elimu na huku akimshukuru Rais Samia kwa kuwekeza katika elimu nchini.


MWISHO

WAISHUKURU TAASISI YA UMOJA WA WASAIDIZI WA SHERIA UWASHEM KUWAWEZESHA KUTATUA MIGOGORO BAINA YA WAVUVI NA WAKULIMA WA MWANI

April 07, 2025 Add Comment

 


WANANCHI wanaofanya shughuli za  Uvuvi na Wakulima wa Zao la Mwani wanaoishi katika kijiji cha Mwaboza wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga wameishukuru taasisi ya Umoja wa wasaidizi wa Sheria 'UWASHEM' kwa kuwawezesha kutatua mgogoro baina yao kutokana na matumizi ya rasilimali bahari ambapo kupitia elimu waliyoipata imewawezesha kuwaunganisha.


Awali wakizungumza katika mdahalo wa pamoja  ulioandaliwa na taasisi hiyo kwa lengo la kutambua changamoto zilizopo baina yao Kila mmoja ameonekana kumshutumu mwingine kuwa chanzo cha mgogoro kwa kile walichoeleza kuwa wamekuwa wakigombania maeneo hali iliyopelekea kukosa maelewano na hatimaye kuwaingiza kwenye mgogoro.

Wakizungumza baadhi yao wamesema kuwa pamoja na elimu waliyoipata kupitia shirika la UWASHEM' ni vyema Serikali ikatenga maeneo maalum ili kuwasaidia wananchi hao kufanya shughuli zao bila bughuza  na hatimaye kuendelea kujipatia kipato Chao cha Kila siku

Mratibu wa miradi kutoka shirika la UWASHEM' Swalehe Sokolo amesema kuwa  kupitia mradi huo wanaoutekeleza imesaidia kwa kiasi kikubwa kutatua changamoto baina ya Wavuvi na Wakulima wa Zao la Mwani ambapo pia wameweza kuwaunganisha na viongozi wa Serikali.

Kwa upande wake mratibu wa mradi wa KUJENGA AMANI PAMOJA kutoka shirika la shirika la We World  Zacharia Msabila amesema wanafanya kazi na  taasisi zilizopo karibu na jamii ambapo kupitia ufadhili wanaoutoa itasaidia kufikia malengo waliyoyatarajia.

Diwani wa kata ya Moa Staruki Njama amekiri uwepo wa migogoro ya muda mrefu biana ya Wakulima wa Zao la Mwani na Wavuvi katika kijiji cha Mwaboza ambapo shirika la UWASHEM' limekuja kuleta suluhisho kupitia elimu waliyoitoa ambapo amewapongeza kwa jitihada walizozifanya huku akisisitiza  wananchi kuendelea kufuatia na kutekeleza Sheria zilizowekwa.

Shirika la umoja wa usaidizi wa Sheria Mkinga "UWASHEM'' linatekeleza mradi wa KUJENGA AMANI  PAMOJA katika wilaya hiyo kwa kushirikiana na shirika la 4H Tanzania  ukifadhiliwa na shirika la We World kwa lengo la kuleta amani baina ya wananchi kutatua changamoto mbalimbali ambazo zinaweza kupelekea uvunjifu wa amani.

VETA TANGA WAADHIMISHA MIAKA 30 YA KUANZISHA KWAKE KWA KUFANYA UKARABATI SHULE YA MSINGI CHANGA

March 16, 2025 Add Comment


Na Oscar Assenga,TANGA

CHUO cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Jijini Tanga katika kuadhimisha miaka 30 ya kuanzishwa kwake wamefanya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo kufanya ukarabati wa majengo ,Miundombinu ya Umeme ,Tehama pamoja na kwashonea sare wanafunzi wa Shule ya Msingi Changa ya Jijini Tanga.

Akizungumza kuhusu maadhimisho hayo Mkuu wa VETA kituo cha Tanga,Gideon Lairumbe alisema kwamba wameamua kuadhimisha katika shule hiyo kutokana na kwamba ni miongoni mwa wanufaika wa maadhimisho ya VETA ambayo kitaifa kilele chake kitafanyika Jijini Dar es salaam kuanzia Machi 17 hadi 21 mwaka huu mgeni rasmi anatarajiwa kuwa waziri Mkuu Kassim Majaliwa.

Alisema kwa ngazi ya kituo cha Tanga,VETA imefanya ukarabati darasa la awali kujenga sakafu ya nje ya shule,mfumo wa umeme,Tehama na kuziba maeneo hatarishi maeneo hatarishi ya mmomonyoko wa udongo wakati wa mvua .

Eneo jingine ambalo shule hiyo imenufaika na VETAni kuwashonea sare wanaf unzi 150,kupiga rangi na kukarabati mfumo wa jiko la kupikia zikiwamo sufuria.

Shule nyingine iliyonufaika na VETA katika maadhimisho hayo ni ya Msingi Juhudi wa mamambayo wanafunzi wenye mahitaji maalumu wameshonewa sare na kwa upande wa Mama lishe katika mitaa mbalimbali wamepewa kofia na vizibao vya kuwahudumia wateja.

“Tumefanya hivi ikiwa ni jithada za VETA kurejesha imani kwa jamii ambayo imekuwa ikiihudumia kwa kipindi cha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake lakini pia kuwavuta vijana kujiunga katika mafunzo yake ambayo yamesaidia kwa kiasi kikubwa kutoa ajira”amesema Lairumbe.

Yussuph Ilias ambaye ni mzazi wa wanafunzi wawili wanaosoma shule ya Msingi Changa amesema ukarabati uliofanywa na VETA umesaidia kwani imebadilika na kuwa ya kisasa na kuwawezesha awanafunzi kusoma bila wasiwasi.

“Kwa mfano upande wa baharini shule ya Changa inapakana na bahari ya Hindi..kule chini kulikuw na mmompnyoko ambao ulikuwa ukitutia wasiwasi wazazi kuhusu usalama wa watoto,lakini VETA wameweka vifusi na hali imekuwa nzuri”amesema Ilias.

Makamu Mwenyekiti wa wanafunzi wa Chuo cha VETA Tanga,Mariam Hashim amewaomba wazazi kuwapeleka vijana wao waliohitimu shule za Sekondari na vyuo mbalimbali ili kupata mafunzo ya ufundi yatakayowasaidia kujiajiri.

“Mfano ni mimi nimehitimu chuo kikuu lakini nimeamua kuja VETA kupata ujuzi wa ufundi wa umakenika na kabla sijamaliza mwaka wangu wa pili tayari kuna mashirika matatu yamenifuata na yameahidi kunipa kazi”amesema Mariam.