CLIMATE CHANGE MARATHON KUTIMUA VUMBI WILAYANI PANGANI SEPTEMBA 28 MWAKA HUU

August 02, 2024

Na Oscar Assenga,PANGANI

MBIO za Mabadiliko ya Tabia ya nchi "Climate Change Marathon 2024 " zinatarajiwa kufanyika Septemba 28 mwaka huu katika wilaya ya Pangani Mkoani Tanga  itakuwa kwa mara ya kwanza zikihusish washiriki kutoka ndani na nje 

Akizungumza kuhusu mbio hizo pamoja na maandalizi yake Mkurugenzi wa Taasisi ya Tree of Hope Fortunata Manyeresa alisema kwamba msimu huu mbio hizo zitakuwa zikilenga kukusanya fedha zitakazotumika kugawa majiko ya gesi ya kupikia kwa wanawake ikiwa ni agenda ya kitaifa kuondokana na matumizi ya Kuni na mkaa.

Alisema kwamba wanufaika katika mbio hizo ambao ni wanawake kutoka katika wilaya za Pangani na Handen Mkoani Tanga hususani waliopo katika Kijiji cha Msomera ambao walihama kutoka hifadhi ya Taifa Ngorongoro zikiandaliwa na Taasisi ya Tree of Hope kwa kushirikiana na Asasi ya Muungano wa Jinsia na Mabadiliko ya tabianchi.

Manyeresa alisema mbio hizo zitatanguliwa na bonanza la michezo mbalimbali ambapo pia washiriki watapata fursa ya kutembelea Hifadhi ya Taifa ya  Saadani ikiwemo kaya zaidi ya 50  zikitarajiwa kunufaika mpango huo.

"Mbio za mabadiliko ya tabianchi kwa mwaka 2024 zinalenga kukusanya fedha kwa ajili ya kuhamasisha jamii kutumia nishati mbadala ili kuwasaidia wanawake katika wilaya za Pangani na Handeni waliopo Kijiji cha Msomera na tunategemea zaidi ya kaya 50 zitanufaika, mpango huu unalenga pia kupunguza uchafuzi wa mazingira tunatarajia kwamba tukio hili litaongeza uelewa kwa jamii juu ya athari za mabadiliko ya tabia nchi" alisema Manyeresa.

Awali akizungumza Mkurugenzi kutoka mtandao wa FEMAPO Mathias Lyamunda alisema mbio hizo zitajumuisha Kilomita 21 mshindi akiondoka na kitita cha shilingi 500,000, Kilomita 10 atakayezawadiwa shilingi 300,000 ,Kilomita 5 (250,000) pamoja na Kilomita 2.5 ambapo kila mshiriki atanakiwa kuthibitisha ushiriki wake kwa gharama ya shilingi elfu 35000,na kwa watoto ni elfu 10,000.

Naye kwa upande wake Katibu wa chama cha riadha Mkoa wa Tanga Hassan Mwagomba aliishukuru  taasisi  ya Tree of Hope kwa kuona umuhimu wa kuanzisha mbio hizo huku akiwataka  wadau wengine kushirikiana nao katika kuunga mkono jitihada mbalimbali za Serikali katika kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa jamii pamoja na utunzaji wa mazingira.