NHC TANGA KUWAONDOA KWENYE NYUMBA ZAO WAPANGAJI WENYE MADENI SUGU

December 09, 2022

 Meneja wa Shirika la Taifa la Nyumba(NHC) Mkoani Tanga  Mhandisi Mussa Kamendu  akizungumza na waandishi wa habari
Meneja wa Shirika la Taifa la Nyumba(NHC) Mkoani Tanga  Mhandisi Mussa Kamendu  akizungumza na waandishi wa habari



 Na Oscar Assenga,Tanga


SHIRIKA la Taifa la Nyumba Mkoani Tanga (NHC) limesema kwamba wapangaji wenye madeni sugu iwapo watashindwa kulipa mpaka mwezi Desemba mwaka huu mapema mwakani watalazimika kuwaondoa kwenye nyumba zao kupitia madalali ambao wameingia nao mkataba wa kukusanyia madeni hayo.

Hatua hiyo inatokana na kampeni ambayo waliianzisha ya kipindi cha miezi mitatu kuanzia Octoba-Desemba kuhakikisha wapangaji wanaodaiwa wanalipa madeni yao huku akieleza baada ya kupita muda huo watalazimika kuchukua hatua hizo.

Hayo yalisemwa na Meneja wa Shirika la Nyumba Mkoani Tanga  Mhandisi Mussa Kamendu wakati akizungumza na Waandishi wa Habari ambapo alisema kwa mkoa wa Tanga wana dalali wanaowasaidia kukusanya madeni kwa niaba ya Shirika hilo

Mhandisi Kamendu  alisema kwamba utaratibu ulipo mtu akiwa anadaiwa kodi shirika huwa linamwandikia notisi ndani ya  siku 30 kumjulisha kwamba shirika litavunja mkataba iwapo deni lake hatalipwa ndani ya kipindi hicho .

Alisema baada ya kupita muda huo shirika huwa linampa kazi dalali ambaye wameinga naye mkataba kwa kumpatia orodha ya watu ambao katika siku 30 ambazo wamewapa hawajalipa madeni yao na dalai wanatoa notisi siku 14.


" Deni lao likishaenda kwa Dalali wao wanakuwa wanamsubiri akusanye hilo yule mpangaji anabaki yeye na dalali waendelea na zoezi la kudai ikishapita siku 14 kama hajalipa kinachofuata anatolewa kwa nguvu kwenye nyumba kwa kukamatiwa mali zake ambazo dalali atakaa nazo kwa kipindi fulani huku akimjulisha aliyekamatiwa vitu  vyake alipe deni ili kuweza kufidia kodi anayodaiwa kama hajalipa dalali atauza hivyo vitu kuweza kupata pesa ya kulipa deni la nyumba "Alisema

Hata hivyo Meneja huyo alisema kwa mkoa huo wana dalali anaitwa Cops Option Mat hao ndio wanawakusanya  madeni kwa wadaiwa sugu waliopo kwenye mkoani humo.

Meneja huyo alisema kwamba kwa mkoa huo malimbikizo ya madeni mpaka mwezi Novemba mwaka huu ni zaidi ya Milioni 105 ambapo kati yao ni watu binafsi,taasisi za Serikali,binafsi na nyengine mbalimbali.

Alisema kulikuwa na wapangaji ambao waliwatoa na baada ya hilo zoezi waliweza kulipa na wengine wanaendelea kulipa hivyo wanategemea mwitikio utaendelea kuwa mzuri wa kulipa kodi wanaodaiwa.

Mwisho.