DC Mwanga aisifu Lushoto Shooting, “Asema fitna zikiwekwa pembeni hakuna timu itakayoifikia  mkoani Tanga”

DC Mwanga aisifu Lushoto Shooting, “Asema fitna zikiwekwa pembeni hakuna timu itakayoifikia mkoani Tanga”

March 06, 2013
Na Oscar Assenga, Lushoto.

MKUU wa wilaya ya Lushoto, Alhaji Majid Mwanga amesema fitna ya michezo zikiwekwa pembeni mpira ukichezwa hakuna timu yoyote mkoani Tanga itakayoweza kuifikia timu ya Lushoto Shooting ya Lushoto.

Mwanga alitoa kauli hiyo juzi wakati wa halfa ya kuipongeza timu ya Lushoto Shooting kwa kufanikiwa kumaliza vema mzunguko wa kwanza wa ligi ya mkoa.

Alisema licha ya timu hiyo kumaliza ligi hiyo wakati katika nafasi nzuri lakini bado haijamfurahisha hivyo kuwataka viongozi kuhakikisha wanaiandaa vema kwa ajili ya duru la pili pamoja na kuchukua ubingwa wa ligi hiyo.

Aidha aliwataka viongozi wa timu hiyo kuwa wabunifu kwa kubuni miradi ambayo inaweza kuwasaidia katika timu yao kuliko kuendelea kuwategemea wafadhili ambao huenda wakati mwengine wasiwasaidie.

Akizungumzia suala la nidhamu,DC Mwanga alisema hategemei kusikia nidhamu kwenye timu za wilaya hiyo hazipo wakati zikiwa zinashiriki katika mashindano mbalimbali ikiwemo kuacha kuingia uwanjani na vitu visivyostahili.

Alisema kazi kubwa ya wilaya hiyo ni kuhakikisha wachezaji hao wanauzwa kwa gharama yoyote ili waweze kuleta mafanikio na watakuwa tayari kuwauza mahali popote duniani kutokana na viwango vyao.

Awali akizungumza ,Katibu wa chama cha soka Mkoa wa Tanga,Beatrice Mgaya aliwataka wachezaji wa timu hiyo kuzingatia nidhamu pamoja na kujiandaa vya kutosha ili kuweza kutimiza azma yao ambayo yamejiwekea na kuhaidi kuisapoti timu hiyo.

Katika halfa hiyo pia wadau wa michezo wilayani humo waliweza kufanya harambee ya kuichangia timu hiyo ambapo jumla ya sh.milioni 3,480,000 zilipatikana ambapo kati ya hizo fedha taslimu zilikuwa ni 150,000 na ahadi zilikuwa ni 3,330,000.

Naye Katibu wa timu ya Lushoto Shooting,Frank Shemptemba  alisema timu hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo kuwa na vifaa za kufanyia mazoezi ambayo havikizi mahitaji ya wachezaji na mara nyingi wachezaji hujitafutia wenyewe hali ambayo inasababisha  kuwa na vifaa ambavyo sio bora.

Shemptemba alisema pamoja na timu hiyo kufanya vizuri kwenye mzunguko wa kwanza lakini pia waliwashukuru wadau mbalimbali akiwemo mkuu wa wilaya Lushoto na Korogwe ,Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini,Steven Ngonyani “Maji Marefu”Shabani Boznia,Julius Kimako kwa jitihada zao kuisapoti timu hiyo.

Mwisho.

“Wizara itenge bajeti za kutosha kwenye Halmashauri”
 

Na Oscar Assenga, Lushoto.

WIZARA ya Habari,Vijana Utamaduni na Michezo imeshauriwa kutenga bajeti ya kutosha katika Mashindano ya Shimisemita ambayo hushirikisha timu kutoka halmashauri mbalimbali hapa nchini ili kuzipa ufanisi na ushindani timu zinazoshiriki.

Ushauri huo ulitolewa jana na Afisa Michezo wa wilaya ya Lushoto,Stephen Shemdoe wakati akizungumza na gazeti hili na kuongoeza kuwa licha ya kufanya hivyo lakini pia alishauri kuwa uwepo utaratibu wa kushirikisha kila idara ili kuleta hamasa zaidi kwa idara kufanya maandalizi.

Shemdoe alisema suala lengine ni kuhakikisha usafiri kwa timu ambazo zinashiriki mashindano hayo zinawafikia walengo kwa wakati ili kurahisisha ushiriki wao kwani zinapochelewa huwaondolea hamasa washiriki hali ambayo huzifanya timu kushindwa kufanya vizuri licha ya kujiandaa.

Aidha alisema tiyari timu za halmashauri hiyo ambazo zitashiriki mashindano hayo mwaka huu zimekwisha kuanza mazoezi tokea jana na wanatarajia kucheza mechi mbalimbali za majaribio.

Shemdoe alisema ili mashindano hayo msimu huu yaweza kuwa na msisimuko na ushindani waamuzi ambao wanachezesha mashindano hayo wawe wale ambao wanatambulika na chama cha waamuzi nchini FRAT na wenye kujua kutafsiri vema sheria kumi na saba za mpira wa miguu.

Afisa Michezo huyo alisema timu ambazo zilianza kujiandaa ni za mchezo wa mpira wa miguu na mpira wa pete ambazo mwishoni mwa wiki zinatarajiwa kucheza mechi za kujipima nguvu na timu za halmashauri ya Korogwe.

Mwisho.

“Lushoto waunga mkono Agiza la RC Gallawa”

“Lushoto waunga mkono Agiza la RC Gallawa”

March 06, 2013
Na Oscar Assenga, Lushoto.
WANANCHI wa wilaya ya Lushoto wameunga mkono Agizo la Mkuu wa Mkoa wa Tanga,Luteni Mstaafu Chiku Gallawa la kufanya usafi katika maeneo yao kila Jumammosi ya kwanza ya mwezi kwa kuchagua maeneo korofi kwa kufanya usafi wa pamoja.

Mwishoni mwa mwezi uliopita Mwandishi wa blog hiii aliweza kupita maeneo mbalimbali wilayani humo nyakati za asubuhi na kujionea maduka yakiwa yamefungwa huku umati mkubwa wa wananchi wakiwa katika maeneo yao kwa ajili ya kushiriki katika zoezi la usafi.

Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa zoezi hilo,Mkazi wa Lushoto mjini,Philipo Katemba alisema zoezi hilo la usafi wamelipokea kwa mikono miwili na kueleza kuwa endapo wananchi watashirikiana kwa pamoja kila wakati basi upo uwezekano mkubwa wilaya yao kushika nafasi ya kwanza katika usafi mkoani hapa kutokana na mwamko wa wananchi kijitokeza kushiriki.

Katemba ambaye pia ni mfanyabishara wilayani humo, aliongeza kuwa zoezi la usafi lilianza muda mrefu lakini wakati huu ndio limetiliwa mkazi zaidi ambapo wananchi wameweza kuhamasika zaidi kwa kujitokeza kwa wingi kuliko ilivyokuwa huku nyuma.

Naye Katibu wa Baraza la Biashara wilayani Lushoto (BBW) David Mkami alisema mchakati huo wa usafi ni mzuri kwa kuwa unaufanya mji wao katika hali ya usafi na kuwa na muonekano mzuri zaidi na kuwataka wafanyabishara kuendelea kuunga mkono agizo hilo katika maeneo yao ya kazi.

Mwisho.
DC Mwanga "awataka Vijana kupenda soka"

Na Oscar Assenga, Lushoto.

MKUU wa wilaya ya Lushoto,Alhaji Majid Mwanga amewataka vijana kupenda michezo na kuithamini kwa kuwa michezo ni ajira ambayo inaweza kuwainua kimaisha endapo wataithamini na kuipa kipaumbele kwa kucheza kwa kujituma pamoja na kuonyesha nidhamu wakati wa michezo.

Alhaji Mwanga alitoa wito huo mwishoni mwa wiki wakati fainali ya Mashindano ya Kombe la Shambalai Cup yaliyofanyika kwenye uwanja wa soka Moa Mwangoi wilayani humo na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa soka wilayani humo akiwemo mdhamini wake Abasi Shambalai.

Alisema michezo mara nyingi huwakinga vijana kujiingiza katika makundi mabaya katika jamii zinazowazunguka pamoja na kuwaepusha kutumia madawa ya kulevya ikiwemo bangi hivyo kuwata vijana kupenda kushiriki katika michezo na kuacha utumiaji wa madawa ya kulevya.

  “Wilaya yetu haipo salama kutokana na kuwepo watu ambao wanaendesha kilimo cha bangi hivyo kupitia mashindano mbalimbali ya mpira miguu wilayani tuwe tunapiga vita matumizi ya madawa ya kulevya “Alisema Mwanga.

Aidha DC Mwanga alisema mashindano hayo yawe chachu kubwa ya wafadhili wengine kujitokeza ili kuweza kuinua kiwango cha soka wilayani humo pamoja na kuhamasisha michezo wilayani humo.

Alieleza endapo suala hilo litatiliwa mkazo mkubwa upo uwezekano wa wilaya hiyo kuwa na timu ambayo itaweza kuja kushiriki ligi daraja la kwanza ikiwemo ligi kuu siku zijazo.

Pamoja na hayo Mkuu huyo wa wilaya alisifu jitihada za waandaaji wa mashindano hayo na kueleza malengo hasa kombe hili yaliyokusudiwa yamefanikiwa kwa asilimia kubwa kutokana na vijana wengi kuhamasika kushiriki.

Katika fainali hiyo,Timu ya Mlalo City waliweza kuibuka kuwa mabingwa wapya wa mashindano hayo na kukabidhiwa Kombe la Mashindano hayo pamoja na kitita cha sh.500,000 jezi na mpira kutoka kwa mdhamini wa mashindano hayo,mshindi wa pili ,alipata kitita cha sh.200,000 na jezi,mshindi wa tatu,Kwemshasha alipewa kitita cha sh.200,000 na mpira na mshindi wa nne,Manyigu Fc alipata 100,000.

Lakini pia washindi wengine waliozawadiwa ni katika awamu ya nane bora ambapo mshindi wa kwanza alipewa kitita cha sh.100, 000 jezi na mpira mmoja, mshindi wa pili alipewa kitita cha sh.50, 000 jezi na mpira na mshindi wa tatu alipewa jezi seti na mpira na kitita cha sh.25,000.

Aidha Mratibu wa Kombe hilo, Fineas Gabriel Mashombela alisema mashindano hayo yalishirikisha timu zaidi ya 50 kutoka maeneo mbalimbali wilayani humo na lengo lake lilikuwa ni kuinua vipaji vya wachezaji wachanga.

                             Mwisho.  
MJUMITA -Wizara ya maliasili inawalinda mabwana Afya wasio waadilifu"

MJUMITA -Wizara ya maliasili inawalinda mabwana Afya wasio waadilifu"

March 06, 2013
Na Oscar Assenga,Korogwe. 

MTANDAO wa jamii usimamizi wa hifadhi ya mazingira ya misitu (MJUMITA) umeishukia wizara ya mali asili na utalii kwa kusema kuwa imekuwa ikiwalinda mabwana miti wasio waadilifu wanaojihusisha na vitendo haramu vya uvunaji wa mazao ya msitu hali inayoweza kusababisha jangwa nchini Tanzania. 

Hivyo kwa kushindwa kuchukua hatua dhidi ya watumishi wanaobainika kuhusika uendeshaji hujuma kwenye misitu ya hifadhi, mwenyekiti wa mtandao huo wa jamii Revocatus Njau alisema ni dhahiri kwamba hivi sasa wizara ya mali asili na utalii imepoteza muelekeo wa kusimamia misitu asilia nchini na kubainisha kuwa kila mwaka takribani hekta 130,000 zinapotea kwa miti kukata ovyo ili kuuzwa. 

Mwenyekiti huyo wa Taifa wa mtandao wa MJUMITA,Revocatus Njau alitoa taarifa hiyo juzi kwenye kikao cha ujirani mwema kilichowashirikisha viongozi wa wilaya za Lushoto na Korogwe kilichofanyika mjini Lushoto ambapo mgeni rasmi alikuwa mkuu wa mkoa wa Tanga Luteni mstaafu Chiku Gallawa.

Akizungumza mbele ya wajumbe wa mkutano huo,Njau alisema kushamiri kwa vitendo haramu vya uvunaji wa mazao ya misitu vinaonekana kupata Baraka ya wizara husika kwa vile mpaka sasa licha ya shughuli ya kuwa na taarifa za uvunaji haramu kuenea kwa kasi hakuna hatu zilizochukuliwa. 

Alisema kuwa MJUMITA kwa upande wake imeshaifahamisha wizara na mamlka nyingine juu ya matukio ya uhalifu yanavyoendelea katika misitu mbalimbali hapa nchini vitendo ambavyo vikiachiwa kuendelea bila hatua za makusudi na moyo wa uzalendo kuwepo basi ni dhahiri kuwa jangwa linaweza kujitokeza. 

Njau alikwenda mbali zaidi akisema hivi sasa inaonekana kuwa kuanzia wizarani umeundwa mtandao wa kuwalinda mabwana miti wanaojihusisha na uvunaji haramu wa misitu vitendo ambavyo alivyovitolea mifano kwenye mkutano huo ambavyo viliwasikitisha na kuwashangaza wajumbe wa mkutano huo. 

Katika kudhibitisha hilo Njau alisema,wakati jitihada mbalimbali zinafanyika kuwadhibiti wahalifu hao viongozi wakuu huchukua hatua ya kuwasaidia kujinanusua na makosa waliyoyafanya ambapo alitolea mfano wa bwana miti mmoja wa wilayani Lushoto aliyefungwa jela na kutolewa akirejeshwa kazini. 

Njau alisema kwamba bwana miti huyo Shabani Kanju mwaka 2008 alifungwa baada ya kubainika kuwa na makosa ya kukata miti asilia lakini cha kushangaza afisa hifadhi wa wilaya ya Lushoto alikwenda kukata rufaa ambapo mfungwa huyo alitolewaa gerezani kwa kuonekana kuwa hakuwa na hatia. 

Aliongeza kusema kuwa hivi sasa bwana miti huyo Shabani Kanju amehamishia makazi yake kwa kujenga nyumba anayoishi na familia yake jirani na msitu wa Kisima Gonja ambako kila uchao magogo,mbao na miti ya aina mbalimbali imekuwa ikivunwa bila huruma bila ya wahusika kukamatwa huku yeye akiwepo.

 “Kwa kweli inasikitisha inavyoonekana mheshimiwa mkuu wa mkoa kuna mtandao ulioanzia wizarani ambao unawalinda mabwana miti wanaokata miti inayohifadhiwa,mazingira mengi yanaeleza hivyo kwa vile wizara tumeipa taarifa kwa maandishi na hata kukaa nao ana kwa ana,hakuna kinachofanyika”alisema Njau akimuomba mkuu wa mkoa wa Tanga kusaidia kunusuru misitu ya Tanga.

 Ili kuweza kuinusuru misitu ya hifadhi hapa nchini Njau alisema iko haja kwa wizara kuona umuhimu wa kuzishirikisha kada nyingine katika dhana nzima ya ulinzi akibainisha kuwa hivi sasa mabwana miti kutoka halmashauri wanaonekana kutoshirikishwa hali inayochangia uhalifu kuongezeka kwa kasi. Mwenyekiti huyo wa MJUMITA alibainisha kuwa mpaka sasa athari kubwa ya mazingira zimeanza kujitokeza katika maeneo mbalimbali nchini akiyataja baadhi yake kuwa ni misitu ya Nguru kusini (Mor),Mamiowa (Kilosa Mor),Oldzungwa (Mor),Ruvu kusini (Pwani) na wilaya za Korogwe na Lushoto. 

Naye meneja mradi wa shirikal la kuhifadhi misitu asilia Simon Lugazo katika mada aliyoitoa kwenye mkutano huo wa ujirani mwema alisema kuwa shirika lake limefanikiwa kusambaza huduma ya maji kwenye maeneo mbalimbali ,usimamizi shirikishi wa misitu na kuandaa mipango ya usimamizi wa upandaji miti lengo likiwa kuhifadhi mazingira na kati ya 1999 hadi 2002 wamepanda miti 2 mil. 

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Tanga Luteni mstaafu Chiku Gallawa aliyekuwa mgeni rasmi kwenye mkutano huo alielezea masikitiko yake juu ya vitendo vya uharibifu wa mazingira vinavyoendelea kufanyika hapa nchini akisema vikiachiwa kuendelea njaa na jangwa litaweza kujitokeza hivyo amani na utulivu inaweza kujitokeza jambo ambalo siyo jema kujitokeza hapa nchini. 

Kuhusu taarifa ya bwana miti aliyetuhumiwa kujenga nyumba pembeni ya msitu wa hifadhi Luteni mstaafu Gallawa alimuagiza mkuu wa wilaya ya Lushoto Alhaj Majid Mwanga kuhakikisha kwamba anakamatwa mara moja kwa mahojiano juu ya vitendo ambavyo vinadaiwa kuwa na baraka zake. 

Awali akizungumza kabla ya ufungwaji wa mkutano huo mkuu wa wilaya ya Korogwe Mrisho Gambo aliwaasa viongozi wa wilaya ya Lushoto anayopakana nayo kujitahidi kutoruhusu vitendo vya uharibifu wa mazingira havifanyika katika maeneo yaliyo mipakani mwa wilaya zao ambapo alisisitiza akisema hatua za kali za kisheria zitawabana watu wote bila kujali vyeo vyao,itikadi za kisiasa wala dini. 

Kama vile haitoshi naye mkuu wa wilaya ya Lushoto Alhaj Majid Mwanga alitanabaisha kuwa ushirikiano zaidi unahitajika baina ya pande zote mbili kwa kuwashirikisha viongozi wa wilaya za Korogwe na Lushoto katika masuala yote yanayolenga kuongeza tija kwa jamii ambapo alitilia mkazo juu ya kushirikishana kwenye suala la utozaji ushuru wa mazao.