Assenga Atunukiwa Tuzo.

March 08, 2013
Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Five Brothers,Nassoro Makau akimpa tuzo ya kutambua mchango wake,Mmiliki wa Blogi hii Oscar Assenga mwenye miwani kwenye halfa iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo katikati ya Jiji la Tanga,Picha na Mwandishi Wetu.
MIKAKATI YA KUENDELEZA MPIRA WA MIGUU KWA WANAWAKE

MIKAKATI YA KUENDELEZA MPIRA WA MIGUU KWA WANAWAKE

March 08, 2013
Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.

 Utangulizi:

Awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya kamati ya utendaji ya TWFA kuwashukuru wajumbe wa mkutano mkuu kwa kutupa ridhaa ya kuongoza chama kwa kipindi cha miaka minne.

Pia napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wadau wote wa mpira wa miguu kwa kutuwezesha kufika hapa tulipo. Napenda niwashukuru wadau wote kwa ujumla wao na pia kuishukuru serikali kwa namna ya pekee zaidi kwa mchango wake ,na mashirika na makampuni ambayo yamekuwa karibu sana nasi NMB, SERENGETI, NSSF, PPF, na Bakheresa Group of Companies.

Tunaamini kabisa kuwa vyombo vya habari ni washirika wetu wakubwa katika kuendeleza mpira wa miguu wanawake. Napenda kuvishukuru vyombo vyote vya habari hapa nchini na hata vile vya nje vilivyoweza kutoa nafasi katika ujenzi wa mpira wa miguu wanawake.

 Maendeleo ya mpira
 Kutekeleza na kuendeleza mpango wa grassroot.

Kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa miguu Tanzania,Chama cha Mpira  wa Miguu wanawake  na vyama vya mikoa na wadau mbalimbali  tutaendelea kuendeleza mradi wa mpira wa miguu kwa watoto wa kike na wa kiume Grassroot programme.(umri wa miaka 06-12).kwa mwaka 2013 mradi huu utatekelezwa katika mikoa  mitano (5) mikoa hiyo ni  Tanga,Pwani.Mwanza,Mtwara na Lindi. Mradi huu unaendeshwa kupitia shule za msingi.Kwa mwaka 2012 Mradi huu umeendeshwa katika mkoa wa Dar es Salaam na  watoto wapatao 8766 (wasichana 4909 na wavulana 3857 ) na walimu 26 wameshirikishwa.

Mafunzo ,semina na makongamano
Kwa mwaka 2013 tunatengemea kuendesha mafunzo mbalimbali katika nyanja kuu nne za maendeleo ya mpira wa miguu yaani Utawala na uongozi,Ualimu(Ukocha)  Uamuzi na utabibu katika mpira wa miguu .Katika mwaka mwaka 2013 mafunzo yatafanyika zaidi katika nyanja ya uongozi ili kuwajengea stadi za uongozi viongozi wengi ambao wameingia madarakani katika chaguzi zilizofanyika kwa mwaka 2012/2013.Mafunzo ya utawala na uongozi yatafanyika katika mikoa nane:Dar es Salaam,Pwani,Morogoro,Mwanza,Musoma,Shinyanga,Kilimanjaro na Tanga.Katika mafunzo hayo baadhi ya washiriki watateuliwa kutokana na uwezo wao kwa kuzingatia vigezo vitakavyowekwa na watahudhuria semina itakayo andaliwa kwa kushirikiana na shirikisho la mpira wa miguu Tanzania.

Mafunzo kwa walimu katika ngazi mbalimbali na uratibu wa utekelezaji wa mafunzo yaliyofanyika yatapewa kipau mbele.

Mafunzo kwa waamuzi yatalenga zaidi kuibua vipaji vya watoto wa kike walioko mashuleni na wachezaji wanaomaliza/waliomaliza muda wao.Mafunzo yatafanyika kwa awamu mbili katika mkoa wa Dar es Salaam.

Madaktari  wa michezo  ni muhimu sana katika maendeleo ya mpira na afya za wachezaji kwa kushirikiana na vyombo husika mafunzo kwa mwaka 2013 yatafanyika kwa awamu mbili na yatafanyika katika mkoa wa Dar es Salaam. 
Wanahabari wenye uweledi katika mpira wa miguu wa wanawake ni chachu ya maendeleo ya mpira huo.Nafasi ya wanahabari ni kubwa katika kuendeleza mpira wa miguu ili kuwajengea ujuzi zaidi kutakuwa na mafunzo kwa wanahabari yatakayofanyika Dar es Salaam.

Uongozi na utawala bora
Maendeleo ya mpira wa miguu kwa wanawake yanahitaji viongozi bora na waliopewa ridhaa na vyombo husika.Chaguzi zimefanyika katika  mikoa 16 kati 25  ya mikoa ya Tanzania Bara. Pia tunahimiza mikoa ambayo haijafanya uchaguzi ifanye chaguzi mapema.  Mikoa hiyo ni: Dar es salaam, Mwanza, Kilimanjaro, Rukwa, Arusha, Geita, Simiyu, Njombe, Katavi na Mbeya.

Katika chaguzi hizo kuna baadhi nafasi zote hazikujazwa ni matumaini yetu kuwa  zitajazwa katika mikutano ijayo ya vyama husika.
Pia nichukue nafasi hii kuwahamasisha kina mama wengi wenye sifa kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali katika vyama vya mikoa na taifa pale uchaguzi utakapoitishwa.

Mashindano
Mashindano mbalimbali ndio moyo wa mpira wa miguu bila mashindano  hakuna anayeweza kutambua  ubora na kiwango chakena pia ni kipimo cha maendeleo.
Kutakuwa na mashindano mbalimbali katika ngazi ya  mikoa,taifa na kimataifa.
Mashindano hayo pia yatahusisha shule za msingi na sekondari  na vyuo mbalimbali.Kwa kushirikiana na vyombo husika kutakuwa na ufuatiliaji wa karibu wa michezo ya UMISSETA toka ngazi ya mkoa hadi Taifa na kuwa na mpango endelevu wa kuwaendeleza wale wenye vipaji ambao wamechaguliwa /wanaweza kuchaguliwa kwenye timu za taifa.

Ligi itachezwa katika ngazi za mikoa na baadaye kuunda kombaini ya mkoa itakayoshiriki mashindano ya taifa.

Kwa mwaka 2013 tunatengemea mikoa kuchezesha ligi isiyopungua timu tano kwa mikoa 15 itakuwa na timu  10 na timu itaruhusiwa kusajili wachezaji 25 kwa mwaka 2013 tunatengemea watoto/wasichana  3750 kushiriki katika mpira wa miguu. Idadi hii ukizidisha mara nne unapata jumla ya wachezaji 15,000.Endapo tutakuwa na benki ya wachezaji hawa tutaweza kuunda timu bora za umri tofauti na zenye kiwango cha juu.

Pia mikoa inahimizwa kuanzisha mashindano mbalimbali yatakayoamsha ari kwa watoto wa kike na wasichana kushiriki katika mpira wa miguu.

Uratibu wa mikoa
Wajumbe wa kamati ya utendaji pamoja na  majukumu yao kama wajumbe watakuwa na jukumu la kuratibu shughuli za  maendeleo ya mpira wa miguu katika mikoa:Uratibu huo utakuwa kama ifuatavyo:
Rose Kissiwa
Makamu Mwenyekiti
Tabora, Dodoma, Rukwa, Kigoma, Pwani
Amina Karuma
Katibu
Lindi, Mtwara, Iringa, Njombe, Ruvuma
Zena Chande
Mjumbe
Dar es Salaam, Morogoro, Katavi, Shinyanga, Mbeya
Triphonia Temba
Mjumbe
Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Singida
Sophia Charles
Mjumbe
Mara, Kagera, Simiyu, Geita, Mwanza
Kwa mujibu wa katiba ya TWFA  ibara ya 37  inatoa nafasi kwa kamati ya utendaji kuunda kamati ndogo za kuendeleza mpira wa miguu wanawake kamati hizo ni kamati ya Fedha na mipango,kamati ya Ufundi,kamati ya ngingine itakayoonekana inafaa.Kamati ya utendaji kwa pamoja ilikubaliana kuunda kamati ya habari na masoko.
Kamati ya Fedha na Mipango
1.     Rose Kissiwa       - Mwenyekiti
2.     Evans Aveva
3.     Sophia Tigalyoma
4.     Sophia Mukama
5.     Asha Baraka
Kamati ya Ufundi
1.     Tryphonia Temba – Mwenyekiti
2.     Florence Ambonisye
3.     Miraji Fundi
4.     Dr. Leonia Kaijage
5.     Furaha Francis
6.     Richard Muhotoli
Kamati ya Habari na Masoko
1.     Zena Chande – Mwenyekiti
2.     Beatrice Mgaya
3.     Mohamed Mkangara
4.     Florian Kaijage
5.     Somoe Ng’itu

Masoko na Habari
Mpira wa miguu wanawake hauna udhamini na pia vyanzo rasmi vya kupata mapato.Kwa kupitia kamati ya habari na masoko ,tunaamini kutakuwa na mikakakti mbalimbali ya kuelimisha ,kuhamasisha wadau na watanzania wote kuwiwa na kujitoa kuendeleza mpira wa miguu .

 Asanteni
Lina P.Kessy
Mwenyekiti Chama cha Mpira wa miguu wanawake 
TAARIFA KUTOKA SHIRIKISHO LA SOKA NCHINI (TFF).

TAARIFA KUTOKA SHIRIKISHO LA SOKA NCHINI (TFF).

March 08, 2013
Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.

"TFF BADO YASISITIZA KUMUONA WAZIRI MUKANGARA"

RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amemshukuru Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mukangara kwa kukubali ombi la Shirikisho la kutaka kukutana naye kwa mazungumzo na kumsihi asitishe hatua anazodhamiria kuchukua hadi hapo kikao hicho kitakapofanyika.

Waziri Mukangara ameiagiza TFF kuitisha Mkutano Mkuu wa marekebisho ya katiba ifikapo tarehe 15 Aprili 2013 na Mkutano Mkuu wa Uchaguzi ifikapo tarehe 25 Mei 2013 na kwamba tamko la TFF kutekeleza maagizo hayo liwe limetolewa katika muda wa siku tano zinazoishia Jumatatu (Machi 11, 2013).

Katika barua pepe ambayo amemuandikia Waziri ambaye kwa sasa yuko nje ya nchi, Rais Tenga ameeleza kuwa alikwenda ofisini kwake tarehe 7 Machi 2013 kujaribu kumuona lakini akaambiwa amesafiri, hivyo kuomba kukutana na Katibu Mkuu wa Wizara, ambaye pia hakuwepo ofisini na hatimaye akakutana na Naibu Katibu Mkuu.

Katika barua hiyo pepe, Rais Tenga ameeleza madhumuni ya kutaka kuonana na Waziri Mukangara kuwa ni kwanza “kukushukuru kwa kukubali kuonana na ujumbe wa TFF ulioongozwa na mjumbe wetu wa Kamati ya Utendaji, Bw. Alex Mgongolwa, akiongozana na Katibu Mkuu wa TFF, Bw. Angetile Osiah, jana tarehe 6 Machi 2013.
“Kukushukuru kwa kukubali kukutana nasi tena siku ya tarehe 19 Machi, kwa ajili ya mazungumzo juu ya maagizo yako.
“Kukuarifu kuwa nimepokea maagizo yako uliyoyatoa jana kupitia kwa Mjumbe wetu wa Kamati ya Utendaji na kwa njia ya barua; na
“Kwa heshima na taadhima, kukuomba usitishe hatua yoyote ile unayodhamiria kuchukua hadi hapo tutakapokutana na kupata maelezo yetu, TFF, juu ya maamuzi na maagizo uliyoyatoa.”

Tenga, ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu la Afrika (CAF) aliondoka jana (Machi 7 mwaka huu) kwenda Marrakech, Morocco kuhudhuria kikao cha kamati hiyo na pia Mkutano Mkuu wa CAF ambao umepangwa kufanyika Machi 10 mwaka huu ukihusisha pia ajenda ya uchaguzi wa rais.

Mwisho.

Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.

"KAIJAGE KOCHA MPYA TWIGA STARS"

ROGASIAN Kaijage ameteuliwa kuwa kocha mpya wa timu ya taifa ya mpira wa miguu ya wanawake, Twiga Stars baada ya kocha wa zamani, Charles Boniface Mkwasa kujiuzulu katikati ya mwaka jana.

Mkwasa, ambaye alikuwa nyota wa Yanga na Taifa Stars, alijiengua kufundisha timu hiyo aliyoiongoza kwa muda mrefu, baada ya Twiga Stars kuondolewa katika kinyang’anyiro cha kuwania tiketi ya kucheza fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) zilizofanyika nchini Equatorial Guinea.

Twiga ilipata bao muhimu la ugenini jijini Addis Ababa ilipofungwa na wenyeji wao Ethiopia mabao 2-1, lakini ikiwa na matumaini ya kutumia vyema bao la ugenini ilijikuta ikilala bao 1-0 kwenye Uwanja wa Taifa katika mchezo wa marudiano na hivyo kukosa tiketi ya kurudi tena kwenye fainali hizo.

Kaijage ambaye kwa sasa anajihusisha na mradi wa vijana (grassroots) pamoja na programu nyingine za kukuza vipaji zilizo chini ya TFF, aliteuliwa na Kamati ya Ufundi ya TFF kufanya kazi hiyo na ameita kikosi cha Twiga Stars kwa mazoezi ya siku kumi kuanzia Machi 10 hadi 23 mwaka huu Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam.

Wachezaji walioitwa ni Amina Ally (Lord Barden), Asha Rashid (Mburahati Queens), Aziza Mwadini (Zanzibar), Esther Chabruma (Sayari), Esther Mayalla (TSC Academy), Etoe Mlenzi (JKT), Evelyn Sekikubo (Mbarahati Queens), Fatuma Bushiri (Simba Queens), Fatuma Mustafa (Sayari) na Fatuma Omari (Sayari).

Flora Kayanda (Tanzanite), Hamisa Athuman (Marsh Academy), Hellen Maduka (Bujora), Hellen Peter (JKT), Irene Ndibalema (TSC Academy), Maimuna Said (JKT), Mwajuma Abdallah (Tanzanite), Mwanaidi Tamba (Mburahati Queens), Mwanahamis Omari (Mburahati Queens) na Mwapewa Mtumwa (Sayari).

Nabila Ahmed (Marsh Academy), Nasiria Hashim (Zanzibar), Pulkeria Charaji (Sayari), Rukia Khamis (Sayari), Semeni Abeid (Tanzanite), Sharida Boniface (Makongo Sekondari), Sophia Mwasikili (Luleburgaz Gucu Spor, Uturuki), Theresa Yona (TSC Academy), Vumilia Maarifa (Evergreen) na Zena Khamis (Mburahati Queens).

Mwisho.

Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.
 
"YANGA, TOTO AFRICANS KUUMANA DAR"

MICHUANO ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo vinara Yanga watakuwa wenyeji wa Toto Africans kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi wa mechi hiyo namba 135 atakuwa Andrew Shamba kutoka Pwani akisaidiwa na Abdallah Mkomwa na Abdallah Rashid pia wote kutoka Pwani. Kamishna ni Salim Singano kutoka Tanga wakati Mtathmini wa waamuzi ni Alfred Lwiza.

Nayo Polisi Morogoro itakuwa mgeni wa Azam kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam. Azam katika mechi hiyo namba 136 na nyingine mbili zinazofuata itakuwa bila kocha wake Steward John Hall ambaye Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemfungia mechi tatu.

Charles Komba kutoka Dodoma ndiye atakayekuwa Kamishna wa mechi hiyo namba 136 itakayochezeshwa na mwamuzi Simon Mberwa kutoka mkoani Pwani.

Ligi hiyo itaendelea tena keshokutwa (Machi 10 mwaka huu) ambapo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utashuhudia mechi kati ya Simba na Coastal Union ya Tanga. Waamuzi wa mechi hiyo ni Martin Saanya akisaidiwa na Jesse Erasmo na Vicent Mlabu wote kutoka Morogoro.

Mwisho.

Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.
 
"RHINO, KANEMBWA ZASAKA TIKETI VPL"

KINDUMBWENDUMBWE cha Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kinaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) katika makundi yote matatu, lakini macho na masikio ya washabiki wa mpira wa miguu yakiwa kwenye mechi za Rhino Rangers ya Tabora na Kanembwa JKT ya Kigoma.

Timu hizo ndizo ziko katika nafasi nzuri ya kupata tiketi ya kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao kutoka kundi hilo la C. Tayari Mbeya City ya Mbeya na Ashanti United ya Dar es Salaam zimeshapata tiketi za kucheza VPL msimu ujao kutoka kundi A na B.

Rhino Rangers itaikaribisha Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, wakati Kanembwa JKT itakuwa mgeni wa Pamba kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mechi nyingine za kundi C ni Mwadui vs Polisi Tabora (Kambarage, Shinyanga), na Morani vs Polisi Mara (Kiteto, Manyara). Mechi za kundi A ni Majimaji vs JKT Mlale (Majimaji, Songea), Mkamba Rangers vs Mbeya City (Sokoine, Mbeya) na Polisi Iringa vs Burkina Faso (Samora, Iringa).

Mshikeshike ya kundi B ni Ndanda vs Ashanti United (Nangwanda Sijaona, Mtwara), Villa Squad vs Green Warriors (Karume, Dar es Salaam), Polisi Dar vs Transit Camp (Mabatini, Mlandizi) wakati Tessema na Moro United zitacheza Machi 10 mwaka huu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

Mwisho.


MABAO 191 na Kadi 163 zapatikana ligi ya wilaya ya Tanga.

MABAO 191 na Kadi 163 zapatikana ligi ya wilaya ya Tanga.

March 08, 2013

Na Mwandishi Wetu,Tanga.
Katika hatua ya mchujo ya Ligi wilaya ya Tanga iliyoanza mwishoni mwa mwezi septemba mwaka jana na kumalizika Januari 6 mwaka huu jumla ya mabao 191 yalifungwa na timu zilizokuwa zikishiriki ligi hiyo.

Katibu Msaidizi wa Chama cha soka wilaya ya Tanga (TDFA) Salim Carlos alisema kuwa mabao hayo yalitokana na michezo 64 iliyochezwa kwenye hatua hiyo ambayo ilikuwa ikishirikisha timu 41 ambazo zilikuwa zimegawanywa kwenye makundi kumi.

Carlos alisema baada ya kumalizika hatua hiyo kila kundi tiyari limekwisha kutoa washindi wawili ambao wanaendelea na ligi hiyo katika msimu mpya wa mwaka 2012-2013.

Alisema pia katika hatua hiyo jumla ya kadi zipatazo163 ambapo kati ya hizo kadi za njano zilikuwa ni 143 wakati kadi nyekundu zilikuwa 20 na  timu iliyoongoza kupewa kadi nyingi za njano ni Raidon ambapo timu hiyo ilipewa kadi 8.

Aidha alisema katika hatua hiyo wachezaji Hussein Salim wa timu ya Donge Fc Rubein Desideri na wa Younga Rovers waliongoza kwa kufunga mabao ambapo kila mmoja alifunga mabao 15.

Akizungumzia changamoto ambazo zilijiotokeza katika hatua hiyo, Katibu huyo alisema uhaba wa fedha za uendeshaji ni moja kati ya vitu ambavyo vilijitokeza hali iliyopelekea kushindwa kuwalipa waamuzi na pesa za kulipia uwanja kwa wakati.

Katibu huyo aliwataka wadau mbalimbali wa soka mkoani hapa kukisaidia chama hicho ili kiweze kufanikisha ligi yao msimu huu kwani wamedhamiria kuinua kiwango cha soka wilayani hapa.

Mwisho.
TIMU 13 kushiriki ligi ya Mkoa wa Tanga"

TIMU 13 kushiriki ligi ya Mkoa wa Tanga"

March 08, 2013
Na Mwandishi Wetu, Tanga.
JUMLA ya timu 13 zimefunzu kucheza Ligi ya Mkoa wa Tanga mzunguko wa pili baada ya kufanya vizuri mzunguko wa kwanza na itachezwa kwa mfumo wa nyumbani na ugenini.

Akizungumza na Blogi hii Katibu wa chama cha soka Mkoa wa Tanga (TRFA), Beatrice Mgaya alisema maandalizi ya hatua hiyo yamekamilika na mzunguko huo utaanza Machi 9 mwaka huu.

Mgaya alisema katika ufunguzi wa mzunguko huo, timu za soka Lushoto Shooting na Korogwe United zinatarajiwa kuonyeshana kazi katika uwanja wa soka Lushoto na unatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa.

Alisema mchezo mwengine utakaochezwa siku hiyo utafanyika kwenye uwanja wa Mkwakwani ambapo timu ya maafande wa jeshi la magereza mkoani hapa Small Prison watakapoikabili Viva Dynamo ya Maramba wilayani Mkinga.

Katibu huyo alizitaka timu zinazoshiriki ligi hiyo kuonyesha nidhamu ya hali ya juu ili kuweza kuleta ushindani pamoja na kuziasa zifanye maandalizi ya kutosha kabla ya mechi zao.

Mgaya alizitaja timu zinazoshiriki kuwa ni Lushoto Shooting, Korogwe United,Halmashauri Fc,Lushoto Star,Small Prison,Viva Dynamo, ,Veteran FC,Monga Star,African Sports,Black Burn,Eagle Rangers na Moa Original na Makorora Star.

Timu hizo zitachukuana ili kuweza kupatikana bingwa wa mkoa katika msimu huu ambapo ataweza kushiriki mashindano ya mabingwa wa mikoa itakayochezwa baada ya kumalizika ligi za mikoa.

Mwisho.

"Bondo United watwaa ubingwa wa Kombe la Diwani Handeni"
 
Na Mwandishi Wetu,Handeni

LIGI ya soka kuwania kombe la Diwani kata ya Kwamgwe wilayani hapa,juzi ilifikia tamati kwa mchezo kati ya Bondo United na Mungano FC ambapo matokeo ya mchezo huo Bondo ilitwaa ubingwa kwa njia ya penati kwa kuwanyuka wapinzani wao kwa 3 - 0.

Katika mchezo huo wa fainali uliofanyika uwanja wa Kwedigongo hadi muda wa kawaida unamaizika hakuna mbabe ambapo mwamuzi wa mchezo huo Mohamed Chombo aliongeza muda wa nyongeza dk 15 ambazo pia hazikutoa mshindi hadi hatua ya penati.

Waliofanikiwa kuzikwamisha wavuni penati za Bondo ni Charles Ernest,Hemed Athumani na Hamisi Mohamed wakati ile ya Muungano ilifungwa na mchezaji Enock Juma matokeo ambayo yaliifanya Bondo United kuwa bingwa baada ya penati tano tano kupigwa.

Bingwa wa ligi hiyo ambayo hufanyika kila mwaka aliweza kuzawadiwa kikombe,jezi seti moja na Tsh 100,000, wakati mshindi wa pili timu ya Muungano ilizawadiwa Tsh 70,000 na mshindi wa tatu Tsh 50,000 ambazo zilikwenda jkwa klabu ya soka ya Mbogoni FC.

Mratibu wa mashindano hayo ambaye ni diwani wa kata ya Kwamgwe Sharrifa Abebe akizungumza baada ya mchezo huo kumalizika alisema,amefurahishwa na wachezaji pamoja na mashabiki wa timu zilizoshiriki kuzingatia suala la nidhamu mchezoni.

Alisema mashindano hayo yameweza kutoa timu ya kata ainayoundwa na wachezaji wapatao 40  ambao watakuwa chini ya mwalimu wao msaidizi aliyemtaja kwa jina la Hamza Manulanula huku jitihada za kumtafuta kocha mkuu zikiendelea kufanywa.

"Nimefurahi ligi kumalizika kwa amani na sasa tunaangalia suala la timu yetu ya kata,mwalimu msaidizi amepatikana...mimi na wafadhili wengine tunasaka kocha mkuu ili kuwanoa vyema vijana wetu,tutakuwa na mechi nyingi za majaribio"alisema Sharrifa.

Alisema,lengo la kuanzishwa ligi hiyo ni kukuza vipaji sanjari na kutengeneza ajira kwa vijana huku akibainisha kuwa kupitia ichezi pia vijana itawasaidia kuepukana na mazingira ambayo yanaweza kuwatumbukiza katika vitendo hatarishi na kuharibu maisha yao.

Mwisho.