MPINA ATOA MAAGIZO KWA KIWANDA CHA SUKARI MTIBWA

September 30, 2017

 
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Luhaga Mpina akiangalia chanzo cha maji katika milima ya Urugulu, Mjini Morogoro, akiwa katika ziara ya mkikazi Mkoani Morogoro Mpina alielezwa kuwa chanzo hico cha maji kinaharibiwa na shughuli za binadamu.
Kulia Mratibu wa Mazingira kanda ya mashariki kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC Bw. Jafari Chimgege akiongea jambo wakati wa Oparesheni ya ukaguzi wa mazingira katika kiwanda cha Sukari Mtibwa.
Katikati Naibu Waziri Mpina akisukuma toroli baada ya kumaliza zoezi la usafi wa mazingira wilayani Mvomero, kushoto ni Mkuu wa Wilaya hiyo Bw. Mohammed Mussa Utali.
Mkuu wa Wilaya hiyo Bw. Mohammed Mussa Utali  akitoa taarifa ya wilaya hiyo kwa Naibu Waziri Mpina kabla ya kuanza zoezi la usafi wilayani humo.

NA EVELYN MKOKOI - MVOMERO

Akiwa katika ziara ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa sheria ya mazingira ya mwaka 2004 na kanuni zake Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Luhaga Mpina ametoa maagizo  kwa kiwanda cha Mtibwa sukari kuieleza serikali kwa nini bado kiwanda hicho kinaendelea kutumia magogo katika uzalishaji wake licha ya maelekezo aliyowahi kuyatoa kiwanda hapo katika ziara yake mwaka mmoja iliyopita iliyowataka kutumia mfumo rafiki kwa mazingira.

Alipokuwa ziarani kiwandani hapo mwaka Jana. Mpina aliagiza kiwanda hicho kutoka katika mfumo wa uzalishaji kwa kutumia njia hiyo ya magogo ambayo si rafiki kwa mazingira ambapo kiwanda kilipewa muda wa mwaka mmoja kubadilisha mfumo huo sambamba na mfumo wa utiririshaji wa majitaka toka kiwandani hapo jambo ambalo wamelitekeleza kwa kujenga mfumo wa kisasa wa uondoshwaji wa maji taka,hatua ambayo imempelekea Naibu Waziri Mpina kukipongeza kiwanda hicho. 

Kwa Upande Wake Meneja uzalishaji wa kiwanda hicho Bw. Abel Magese alimueleza Mpina kuwa kiwanda hicho kipo katika hatua ya kujenga mabwawa makubwa ya kisasa ya kutunzia maji ya uzalishaji.

Kufuatia taarifa hiyo,Mpina aliwataka waandike barua Kwa mamlaka husika yaani NEMC kupitia Serikali ya Mkoa na bonde la Wami Ruvu ili kuweza kufanyika Kwa tathmini kwa athari ya mazingira na kuwezesha mchakato huo kwenda kwa haraka.

Mpina pia alikipongeza kiwanda hicho kwa ongezeko kubwa la uzalishaji wa sukari kutoka Tani 15,000 kwa mwaka jana. mpaka tani 30,000 za sukari kwa mwaka huu, na kusema kuwa ongezeko hilo litachangia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa sukari nchini

Aidha, Mpina pia alipongeza  uongozi wa kiwanda hicho kwa kuajiri wahitimu kutoka vyuo vikuu mbalimbali nchini pamoja na kuwachukua wanafunzi wa mafunzo kwa vitendo.

Wakati huo huo, Naibu waziri Mpina Alitembelea vyanzo vya maji vya milima ya Urugulu na Ruaha mpakani mwa wilaya ya Mvomero na Kilosa akiwa na lengo la kujionea utunzanji wa vyanzo hivyo vya maji na misitu ya hifadhi inavyotekelezeka.

Mpina amemaliza Ziara yake ya siku mbili Mkoani Morogoro leo.

USIKOSE IBADA ZA LEO IKIWA NI SIKU YA MWISHO YA MKUTANO WA INJILI JIJINI MWANZA

September 30, 2017

DC SHINYANGA AWEKA JIWE LA MSINGI NA KUENDESHA HARAMBEE UJENZI WA BWALO LA CHAKULA SHULE YA LITTLE TREASURES

September 30, 2017

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro leo Jumamosi Septemba 30,2017 ameweka jiwe la msingi katika jengo la Bwalo la Chakula katika shule ya msingi Little Treasures “Little Treasures Nursery & Primary School” iliyopo katika kijiji cha Bugayambelele kata ya Kizumbi katika manispaa ya Shinyanga.
Mbali ya kuweka jiwe la msingi pia ameendesha harambee kwa ajili ya kupata shilingi milioni 200 kwa ajili kukamilisha ujenzi huo,ambapo wazazi na walezi wameshiriki katika harambee hiyo. 
Akizungumza katika shule hiyo,Matiro aliwapongeza wazazi na walezi wa wanafunzi kwa kujitoa kwa hali na mali kusaidia shule hiyo ambayo imejizolea sifa lukuki kwa utoaji wa elimu bora. 
“Shule hii imejizolea sifa nzuri,hii ni miongoni mwa shule bora kabisa nchini,kila mzazi anapenda mtoto wake asome kwenye shule nzuri,ukifika Shinyanga ukauliza shule gani nzuri,utatajiwa shule hii,nimeambiwa siri ya mafanikio haya inatokana na maono na utayari wa wazazi na marafiki kuisaidia shule hii”,alifafanua Matiro. 
“Sisi kama serikali tunaunga mkono sekta binafsi,kutokana na shule hii kufanya vizuri,ni ukweli usiopingika kuwa imeleta ushindani mkubwa kwa shule zetu za serikali,nasi kwa upande wa shule zetu za serikali hatuna budi kuiga, tuje kujifunza nini wanafanya hapa Little Treasures”,aliongeza Matiro. 
Aliwaasa wazazi na walezi mkoani Shinyanga kupeleka watoto shule kwani urithi pekee kwa watoto ni elimu na wala siyo mali ambazo hupotea kirahisi sana. 
Katika hatua nyingine alizitaka shule za taasisi binafsi kutoza ada zinazoendana na hali ya uchumi wa wazazi huku akiwasihi wazazi kutoa ushirikiano katika shule akitolea mfano wa shule ya Little Treasures ambayo imekuwa karibu zaidi na wazazi na walezi wa wanafunzi. 
Mkurugenzi wa shule ya msingi Little Treasures,Lucy Dominic alisema ili kukamilika kwa jengo la bwalo la chakula jumla ya shilingi milioni 200 zinahitajika na tayari uongozi wa shule umetenga shilingi milioni 50 hivyo bado zinahitajika shilingi milioni 150. 
Naye Meneja wa shule hiyo,Wilfred Mwita alisema pindi jengo hilo litakapokamilika litatumika kama sehemu ya wanafunzi na wafanyakazi wa shule hiyo kula chakula lakini pia kwa ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo michezo na mikutano. 
Akisoma risala,Mkuu wa shule hiyo,Paul Kiondo alisema shule hiyo yenye mchepuo wa Kiingereza ina wanafunzi wa bweni na kutwa ilianza na wanafunzi wanne pekee na sasa ina jumla ya wanafunzi 662 kati yao,wavulana ni 304 na wasichana 318 na imekuwa ikifanya vizuri katika mitihani mbalimbali.
Jumla ya shilingi milioni 15 zimepatikana katika harambee hiyo ya kuchangia ujenzi wa bwalo la chakula,ambapo wazazi na walezi pamoja na marafiki wa shule hiyo wamechangia huku Mkuu wa wilaya Shinyanga Josephine akitoa shilingi Milioni 2 pamoja na mifuko 30 ya saruji.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro (wa pili kulia) akiwasili katika shule ya msingi Little Treasures “Little Treasures Nursery & Primary School”.-Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiweka jiwe la msingi katika jengo la Bwalo la Chakula katika shule ya msingi Little Treasures “Little Treasures Nursery & Primary School”.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akisoma maandishi baada ya kuweka jiwe la msingi katika jengo la Bwalo la Chakula katika shule ya msingi Little Treasures.
Maandishi yakisomeka kwa lugha ya Kiingereza yakiwa na maana ya 'Jiwe la Msingi limewekwa na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Josephine Matiro leo Septemba 30,2017'.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akipanda mti wa kumbukumbu baada ya kuweka jiwe la msingi katika jengo la Bwalo la Chakula katika shule ya msingi Little Treasures.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akimwagilia maji mti alioupanda katika shule ya Little Treasures.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiondoka katika eneo panapojengwa jengo la Bwalo la chakula katika shule ya msingi Little Treasures.Kulia ni Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo,Tilulindwa Sulusi.
Wanafunzi wa shule ya msingi Little Treasures wakimwongoza Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro katika maaandamano kuelekea eneo la mkutano kwa ajili ya harambee kuchangia ujenzi wa bwalo la chakula katika shule hiyo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akiwa katika maandamano hayo.Wa kwanza kushoto mbele ni Mkurugenzi wa shule ya msingi Little Treasures,Lucy Dominic,kulia ni Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo,Tilulindwa Sulusi.
Meza kuu: Katikati ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.Kulia ni Mkurugenzi wa shule ya msingi Little Treasures,Lucy Dominic,kushoto ni Mwenyekiti wa bodi ya shule hiyo,Tilulindwa Sulusi.

SEKTA BINAFSI ZAONGEZA NGUVU KATIKA KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA SINGIDA.

September 30, 2017
 Mratibu wa Ukimwi Mkoa wa Singida Dkt Mohamed Mbalazi akitoa mada katika mkutano ulijadili uboreshaji wa ushirikiano baina ya serikali na wadau wa sekta binafsi zinazotoa huduma ya Afya Mkoani Singida.
 Afisa Lishe Mkoa wa Singida Teda Sinde akifafanua jambo katika mkutano ulijadili uboreshaji wa ushirikiano baina ya serikali na wadau wa sekta binafsi zinazotoa huduma ya Afya Mkoani Singida.
 Mratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma Mkoa wa Singida Dkt Evans Mlay (wa kwanza kushoto) akipitia dondoo, kabla ya kuwasilisha mada iliyoonyesha mchango mkubwa wa wadau Sekta ya Afya katika mapambano dhidi ya Kifua Kikuu Singida, Kulia kwake ni Afisa Mradi wa AMREF Mkoa wa Singida Donathapeace Kayoza.
 Mwakilishi wa Kaimu Katibu Tawala Mkoa, Cosmas Sikali akizungumza na wadau wa sekta binafsi zinazotoa huduma katika Mkoa wa Singida.

  Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Salum Manyatta akisikiliza kwa makini maoni na michango mbalimbali ya wadau ambao ni taasisi na mashirika binafsi yanayotoa huduma za Afya Mkoani Singida.
Meneja Mradi wa EGPAF Kanda ya Kati Dkt Joseph Obedi akiandika baadhi ya mapendekezo ya kuboresha ushirikiano kati ya sekta binafsi na serikali katika uboreshaji wa huduma za Afya Mkoa wa Singida.
Wadau mbalimbali wa sekta binafsi wameweza kuongeza nguvu katika kuboresha sekta ya Afya Mkoani Singida kutokana na ushirikiano mzuri ulipo baina yao na serikali.

Hayo yamebainishwa katika mkutano maalumu wa siku mbili uliohitimishwa jana Mjini Singida, ambapo viongozi wa serikali, taasisi na mashirika 15 yanayotoa huduma za Afya na Ustawi wa jamii Mkoani hapa wamejadiliana namna ya kuboresha ushirikiano baina yao.

Mratibu wa Ukimwi Mkoa wa Singida Dkt Mohamed Mbalazi amesema katika mapambano dhidi ya Ukimwi na Virusi vya Ukimwi (VVU) Mkoani hapa, Sekta binafsi zimekuwa na mchango mkubwa.

Dkt Mbalazi amesema wadau hao wameweza kutoa dawa za kupunguza makali ya VVU, tiba lishe, mafunzo kwa watoa huduma wa afya, ufuatiliaji wa watumia wa dawa za VVU pamoja na kuandaa takwimu jambo ambalo limeboresha mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi.

“Sisi kama watendaji wa serikali tunathamini na kutambua mchango wa wadau wa sekta afya kwakuwa ni nguzo muhimu sana, mfano wadau wetu shirika la EGPAF, wametenga bilioni 1.6 kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ukimwi na maambukizi ya VVU” Mkoani Singida”, amesema na kuongeza kuwa,
“Fedha hizo zitaongea nguvu pale ambapo kuna changamoto au bajeti inakuwa haitoshelezi, lakini pia tunaendelea kutoa wito kwa wadua wengine waendelee kuongea nguvu na wigo wa ushirikiano kwakuwa lengo letu ni moja yaani kumsaidia mwananchi apate huduma bora za afya”, amesisitiza Dkt Mbalazi.

Naye Afisa Lishe Mkoa wa Singida Teda Sinde amesema wadau wamekuwa watekelezaji wazuri wa masuala ya Lishe Mkoani hapa hasa kwa ngazi ya jamii hivyo ushirikiano kati yao umekuwa wa manufaa makubwa.

Teda amesema mkutano huo wa wadau umewawezesha watendaji na viongozi wa serikali kuelewa kwa upana zaidi kazi wanazofanya wadau pamoja na changamoto wanazopitia ili waweze kusaidiana katika kuboresha hali ya Lishe Mkoani hapa.

“Mkutano huu umeongeza na kuboresha ushirikiano baina yetu na wadau wetu ambao wengi wao wanatoa chakula lishe na elimu ya lishe kwa akina mama wajawazito, watoto wenye umri wa miezi sita mpaka 59 na akina mama wanaonyonyesha watoto chini ya miezi sita”, ameeleza Teda.

Ameongeza kuwa mkutano huo umeweza kusaidia katika kupanga mikakati ya utoaji huduma ili kuepusha wadau wanaotoa huduma ya aina moja kutoelekeza nguvu katika maeneo yanayofanana au ambayo hayana uhitaji mkubwa kuliko mengine.

Akifungua Mkutano huo Mwakilishi wa Kaimu Katibu Tawala Mkoa, Cosmas Sikali aliwataka wadau kujadili sera, sheria, kanuni, maeneo ya kipaumbele katika miradi mbalimbali, mafanikio na changamoto katika utekelezaji wa mipango mikakati inayosisitiza ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na binafsi.

Sikali amesema endapo nguvu hizi kwa pamoja zitaunganishwa na kuratibiwa vizuri kwa kiasi kikubwa changamoto zilizopo katika sekta ya afya na ustawi wa jamii pamoja na maradhi kwa wananchi yataweza kupungua.

Ameongeza kuwa serikali peke yake haitaweza kufikia malengo ya kupunguza vifo vya watoto, akina mama wajawazito na kuweza kudhibiti magonjwa ya kuambukiza  na yasiyoambukiza, pamoja na  kuboresha afya ya mazingira  na kupata maji safi na salama bila kushirikiana na Sekta binafsi.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Salum Manyatta amesema mkutano huo umeshirikisha wadau wote muhimu wanatoa huduma za afya na ustawi wa jamii mkoa wa Singida.
Dkt Manyatta amesema mkutano huo umeweka malengo na maazimio ya pamoja na wadau wa sekta binafsi ili kuimarisha sekta ya afya na ustawi wa jamii Mkoani Singida.