Na Mwandishi wetu Boston
Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, jana aliwasili Zanzibar akitokea Ughaibuni baada ya kukamilisha awamu ya pili ya ziara yake ya Mataifa mbalimbali Ulimwenguni.
Wazanzibari wakimsikiliza Maalim Seif (Picha na swahilivilla.Blog)
Katika awamu hiyo ya pili, Maalim Seif alitembelea Marekani na kupata nafasi ya kuzungumza na Wazanzibari katika jimbo la Massachusetts. Ifuatayo ni sehemu ya mwisho ya mfululizo wa makala zetu za "Maalim Seif azungumza na Wazanzibari Boston"
Akiwa mwishoni mwishoni mwa hotuba yake, Mwanasiasa huyo Mkongwe alikariri msimamo wa CUF wa kutoitambua serikali ya Zanzibar iliyoko madarakani kwa vile haikupata ridhaa ya wananchi, akisisitiza kuwa serikali hiyo pia haitambuliki Kimataifa.
"Hatuitambui serikali ya Dakta Shein, na hakuna taifa hata moja linaloitambua", alisisitiza.
Maalim Seif alielezea kwamba, wakati wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar, wafanyazi wa serikali walikuwa wakipokea mishahara yao kwa wakati. Lakini matokeo ya serikali hiyo kugomewa na wanchi na kutengwa kimataifa, kumezidisha hali ya kiuchumi kuwa mbaya kiasi kwamba serikali inashindwa kuwalipa mishahara wafanyakazi wake kwa wakati.
"Tulifikia hatua nzuri, kiasi kwamba tarehe 22-23 watu walikuwa wameshapata mishahara yao. Sasa hali imezidi kuwa mbaya kiuchumi kiasi kwamba inafika mpaka tarehe 3 watu hawajalipwa", alisisitiza.
Kama Wahenga walivyosema: "Baada ya dhiki faraja", Maalim Seif naye aliwataka Wazanzibari kuwa wavumilivu katika kipindi hiki kigumu cha mpito, akiwahakikishia kuwa serikali iliyopo madarakani haitodumu.