UMITASHUMTA mkoa wa Tanga kutimua vumbi leo

UMITASHUMTA mkoa wa Tanga kutimua vumbi leo

June 12, 2013
Na Oscar Assenga, Tanga.
MASHINDANO ya Umoja wa shule za Msingi nchini (Umitashumta) ngazi ya Mkoa wa Tanga yanatarajiwa kuanza kutimua leo katika viwanja vitatu vilivyopo mkoani hapa.

Akizungumza na blog hii, Mratibu wa Mashindano hayo, Rajabu Dimoso alisema maandalizi ya mashindano hayo yanaendelea vizuri na yatashirikisha wanamichezo kutoka shule za wilaya tisa zilizopo mkoani hapa na baadae kupatikana timu ambayo itashiriki ngazi ya Taifa.

Dimoso alizitaja wilaya hizo kuwa ni Kilindi,Handeni,Pangani, Lushoto,Korogwe mjini na Korogwe vijijini,Muheza,Mkinga na Tanga na kueleza mashindano hayo msimu huu yanatarajiwa kuwa ya aina yake kutokana na ushindani uliokuwepo kwa timu hizo ngazi ya wilaya zao.

Aidha aliitaja michezo itakayokuwa ikichezwa kwenye mashindano hayo kuwa ni mpira wa miguu,Pete, mpira wa mikono ,wavu na riadha ambapo washindi watakabidhiwa zawadi zao baada ya kumalizika michezo hiyo.

Alivitaja viwanja ambavyo michezo hiyo itachezwa kuwa ni Mkwakwani, Popatlaly Sekondari na Shule ya Sekondari Tanga Ufundi (Tanga School) ambapo michuano hiyo itashirikisha wanamichezo wapatao 1098 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Afisa elimu Taaluma Mkoa wa Tanga.

Mwisho.

“Bosnia kuzichapa na Ally Baba”

Na Oscar Assenga, Tanga.

BONDIA Chipukizi Ally Bosnia wa Tanga anatarajiwa kupanda ulingoni kuzichapa na Ally Baba wa Kilimanjaro katika pambano la nane lenye uzito wa kg71 lisilokuwa na ubingwa litakalifanyika Julai 7 mwaka huu kwenye uwanja wa Mkwakwani mjini hapa.

Akizungumza jana, Muandaaji wa Pambano hilo, Promota Abbasi Mwazoa alisema maandalizi ya pambano hilo yanaendelea vizuri na kueleza kuwa siku hiyo pia kutakuwa na mabondia ambao watacheza michezo kadhaa ya utangulizi.

Mwanzoa aliwataja mabondia hao kuwa ni Khamisi Mwakinyo atachuana na Said Mundi katika pambano la raundi nane lenye uzito wa kg61 ambalo linatarajiwa kuwa la aina yake kabla ya Haji Juma kupanda ulingoni kuzichapa na J.J.Ngotiko kwenye pambano litakalo kuwa la kg 55 raundi sita.

Promota Mwanzoa aliyataja mapambano mengine kuwa ni Athumani Boxers atakuwa na kibarua kizito dhidi ya mpinzani wake Saimoni Zabron litakalouwa na raundi sita lenye uzito wa kg 61 huku Rajabu Mahoja nae akipanda jukwaani kuzichapa na Jumanne Mohamed pambano la raundi sita lenye uzito wa kg 59.

Pambano lengine litakalofanyika siku hiyo kuwa ni bondia Zuberi Kitandula atazichapa na Hemed Kangeta litakalo kuwa la raundi 4 lenye uzito wa kg 55 wakati Abdalla Mapoka naye atapambana na Ibrahimu Habibu pambano lenye uzito na raundi sawa na mabondia hao.

Mwanzoa aliwataka wadau wa mchezo masumbwi mkoani Tanga kujitokeza kwa wingi kushuhudia mapambano hayo ambayo yatakuwa na upinzani mkubwa kutokana na uwezo walionao mabondia hao.

Mwisho.
KIKOSI CHA IVORY COAST KUWASILI JUNI 13

KIKOSI CHA IVORY COAST KUWASILI JUNI 13

June 12, 2013
KIKOSI CHA IVORY COAST KUWASILI JUNI 13
Msafara wa timu ya Taifa ya Ivory Coast (The Elephants) wa watu 80 wakiwemo wachezaji 27 unatarajiwa kuwasili nchini kesho (Juni 13 mwaka huu) kwa ndege maalum kwa ajili ya mechi dhidi ya Taifa Stars.

Mechi hiyo itachezwa Jumapili (Juni 16 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 9 kamili alasiri, na itachezeshwa na Charef Mehdi Abdi kutoka Algeria.

Kikosi hicho kitawasili Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 2.50 usiku na kitafikia hoteli ya Bahari Beach iliyoko nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam. Timu hiyo inatarajia kuondoka saa chache baada ya mechi hiyo.

Wachezaji walioko katika kikosi hicho ni Abdoul Razak, Akpa Akpro Jean-Daniel Dave Lewis, Angoua Brou Benjamin, Arouna Kone, Aurier Serge Alain Stephane, Bamba Souleman, Barry Boubacar, Boka Etienne Arthur, Bolly Mathis Gazoa Kippersund, Bony Wilfried Guemiand, Cisse Abdoul Karim, Diarrassou Ousmane Viera na Dja Djedje Brice Florentin.

Doumbia Seydou, Gbohouo Guelassiognon Sylvain, Gosso Gosso Jean-Jacques, Kalou Salomon Armand Magloire, N’dri Koffi Christian Romaric, Sangare Badra, Serey Die Gnonzaroua Geoffroy, Sio Giovanni, Tiote Cheik Ismael, Toure Yaya Gnegneri, Traore Lacina, Ya Konan Didier, Yao Kouassi Gervais na Zokora Deguy Alain Didier.

Taifa Stars iko kambini hoteli ya Tansoma tangu iliporejea kutoka Marrakesh, Morocco ambapo leo na kesho itafanya mazoezi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 9 kamili alasiri. Ijumaa itapumzika, na itafanya mazoezi ya mwisho Jumamosi kwenye uwanja huo huo kuanzia saa 10 kamili.

Makocha wa timu zote mbili (Taifa Stars na The Elephants) watakutana na waandishi wa habari Jumamosi (Juni 15 mwaka huu) saa 4 asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa TFF kuzungumzia jinsi walivyojiandaa kwa mechi hiyo.

KIINGILIO MECHI YA STARS, IVORY COAST 5,000/-
Kiingilio cha chini katika mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Ivory Coast (The Elephants) itakayochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya kijani.

Viti vya kijani katika uwanja huo wenye uwezo wa kumeza watazamaji 60,000 viko 19,648. Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu ambavyo viko 17,045 ni sh. 7,000. Kiingilio kwa viti vya rangi ya chungwa ambavyo viko 11,897 ni sh. 10,000.

Viingilio vya daraja la juu ni kama ifuatavyo; VIP C yenye watazamaji 4,060 ni sh. 15,000 wakati sh. 20,000 ni kwa VIP B yenye watazamaji 4,160. VIP A yenye watazamaji 748 kiingilio chake ni sh. 30,000.

Tiketi kwa ajili ya mechi hiyo itakayoanza saa 9 kamili alasiri zitaanza kuuzwa siku mbili kabla ya mchezo (Ijumaa na Jumamosi) katika vituo vifuatavyo; Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.

Katika vituo hivyo tiketi zitauzwa katika magari maalumu. Magari hayo pia yatafanya mauzo ya tiketi uwanjani siku ya mechi. Tunapenda kuwakumbusha watazamaji kutonunua tiketi mikononi mwa watu au katika maeneo yasiyohusika ili kuepuka kununua tiketi bandia, hivyo kukosa fursa ya kushuhudia mechi hiyo.

Utaratibu katika mechi hiyo utakuwa kama ilivyokuwa katika mchezo wa Simba na Yanga, ambapo hayataruhusiwa kuingia uwanjani isipokuwa kwa yale yatakayokuwa na sticker maalumu kutoka TFF.

HATUA YA TATU RCL KUCHEZWA JUMAMOSI
Mechi za kwanza za hatua ya tatu ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) kuwania nafasi tatu za kupanda Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu ujao zitachezwa Jumamosi (Juni 15 mwaka huu) wakati za marudiano zitachezwa Jumatano ya Juni 19 mwaka huu.


Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ilikutana jana (Juni 11 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kupitia ripoti za michezo iliyopita na kufanya uamuzi mbalimbali ikiwemo mechi ya marudiano kati ya Mpwapwa Stars na Machava FC ambayo haikuchezwa.

Machava FC ambayo ilishinda mechi ya kwanza iliyochezwa mjini Moshi kwa mabao 2-0 inaendelea katika hatua ya tatu kwa vile haikuhusika katika kukwamisha mchezo wa marudiano uliopangwa kuchezwa Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dodoma (DOREFA) kiliuhamishia mchezo huo kwenye Uwanja wa Mgambo mjini Mpwapwa kinyume na maelekezo ya Kamati ya Mashindano ya TFF. Kamati katika kikao chake cha awali iliekeleza kuwa mechi zote za RCL zitachezwa makao makuu ya mikoa isipokuwa kwa Morogoro ambapo timu ya Techfort FC iliruhusiwa kutumia Uwanja wa CCM Mkamba mjini Ifakara.

Hivyo timu nane zilizofuzu kucheza raundi hiyo ni Friends Rangers ya Dar es Salaam, Kariakoo ya Lindi, Katavi Warriors ya Katavi, Kimondo SC ya Mbeya, Machava ya Kilimanjaro, Njombe Mji ya Njombe, Polisi Jamii ya Mara na Stand United FC ya Shinyanga.

Wakati timu nyingine zimefuzu kwa kushinda mechi zao za raundi ya mbili, Njombe Mji imeingia hatua hiyo kwa kuwa timu yenye uwiano mdogo wa kufungwa (best looser) katika hatua ya pili.

Katika hatua hiyo mechi ni ifuatavyo; Kariakoo vs Friends Rangers, Machava FC vs Stand United FC, Polisi Jamii vs Katavi Warriors, na Kimondo SC vs Njombe Mji. Timu zilizoanza kutajwa ndizo zinazoanzia nyumbani.

Vilevile Kamati ya Mashindano imeagiza Kamishna wa mechi ya marudiano kati ya Mpwapwa Stars vs Machava FC, Mwijage Rugakingira wa Tanga ambaye alikwenda Uwanja wa Mgambo badala ya Uwanja wa Jamhuri kinyume na maelekezo ya TFF aondolewe kwenye orodha ya makamishna.

Pia waamuzi wa mechi hiyo ambao nao walikwenda Mpwapwa badala ya Dodoma Mjini wamepelekwa Kamati ya Waamuzi ya TFF kwa ajili ya kuchukuliwa hatua kutokana na tukio hilo.

Kamati ya Mashindano imekumbusha kuwa RCL ni mashindano yanayosimamiwa na TFF, hivyo maelekezo yoyote kuhusiana na mashindano hayo pia yatatoka TFF na si mahali pengine popote. Hivyo, msimamizi wa kituoa hana mamlaka ya kubadili uwanja.

Hatua ya nne ya RCL itachezwa kati ya Juni 23 na 23 mwaka huu wakati mechi za marudiano zitachezwa kati ya Juni 29 na 30 mwaka huu.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)