TAIFA STARS YAKALISHWA 2-0 NA BURUNDI, SAMATTA, ULIMWENGU NJE!

TAIFA STARS YAKALISHWA 2-0 NA BURUNDI, SAMATTA, ULIMWENGU NJE!

September 07, 2014


TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, chini ya kocha mkuu Mholanzi, Mart Nooij imetandikwa kwa mara nyingine tena mabao 2-0 dhidi ya timu ya taifa ya Burundi katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki uliomalizika muda mfupi uliopita mjini Bujumbura.
Mabao ya Burundi yamefungwa na nahodha Said Ntibanzikiza katika sekundi ya 40 tu na la pili lilifungwa na Yussuf Ndikumana katika dakika ya 24.
Stars iliingia katika mchezo wa leo ikiwa na kumbukumbu ya kufungwa mabao 3-0 na Burundi katika mechi maalumu ya kuadhamisha miaka 50 ya Muungano, iliyopigwa April 26 mwaka huu uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam.
Katika mechi ya leo, Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta hawakuwepo katika kikosi cha Stars kwasababu walikosa usafiri wa kuunganisha ndege kutoka Zambia ilipo kambi ya TP Mazembe kwenda Lubumbashi na hatimaye Bujumbura.
Stars itarejea kesho baada ya kuumizwa kwa mara nyingine tena na kuwapa huzuni Watanzania walioshuhudia timu yao iakitolewa katika michuano ya kuwania kufuzu hatua ya makundi kusaka tiketi za kucheza fainali za mataifa ya Afrika, AFCON mwakani nchini Morocco dhidi ya Msumbiji.
Nooij aliwaanzisha Deo Munish ‘Dida;, Said Mourad, Shomari Kapombe, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Joram Mgeveke, Erasto Nyoni, Mrisho Ngasa, Mwinyi Kazimoto, Mwagane Yeya, Amri Kiemba na Khamis Mcha ‘Vialli’.

Wachezaji wa Burundi walioanza walikuwa ni: Mbonihankuy Innocent, Ntibanzonkiza Said, Kiza Fataki, Hakizimana Issa, Rachid Leo, Ndikumana Yussuf, Pierre Kwizera, Steve Ndikumasabo, Hussein Shaaban, Didier Kavumbangu na David Nshirimana.

DC TANGA AONGOZA MAPOKEZI YA COASTAL UNION, WANANCHI WAJITOKEZA BARABARANI KUWALAKI, ASEMA HATASITA KUWACHUKULIA HATUA WANAOLETA MIGOGORO

September 07, 2014


 Kulia ni Kocha Mkuu wa Coastal Union,Yusuph Chippo akisalimia na Mkuu wa wilaya ya Tanga,Halima Dendego mara baada ya kuwasili uwanja wa Ndege Tanga akiwa ameambana na timu hiyo wakitokea Pemba walipokuwa wamweka kambi wa kwanza kulia anayemtabulisha ni Meneja wa Coastal Union Akida Machai na kushoto ni Katibu Mkuu wa Coastal Union Kassim El Siagi,Picha KWA HISANI YA COASTAL UNION
 Msafara wa Coastal Union ukiongozwa na pikipiki na Baiskeli zisizokuwa na idadi wakipita katika mitaa mbalimbali jijini Tanga kabla ya kuelekea kwenye Kambi yao iliyopo Raskazoni Jijini Tanga.
Mkuu wa wilaya ya Tanga,Halima Dendego akizungumza na waandishi wa habari katika uwanja wa Ndege jijini Tanga mara baada ya timu ya Coastal Union kuwasili katika uwanja huo ikitokea visiwani Pemba ilipokuwa imeweka kambi ya mwezi mmoja ikijiandaa na msimu mpya wa Ligi kuu soka Tanzania bara

Na Mwandishi Wetu, Tanga.
MKUU wa wilaya ya Tanga,Halima Dendego leo ameongeza mapokezi ya timu ya Coastal Union yaliyofanyika kwenye uwanja wa Ndege jijini Tanga ambapo timu hiyo ilikuwa ikitokea Visiwani Pemba ilipokuwa imeweka kambi kwa muda wa mwezi mzima.

Akizungumza wakati wa mapokezi hayo DC Dendego amesema kuwa serikali ya wilaya hiyo haitasita kuchukulia hatua watu wote wanaoleta migogoro na chokochoko ndani ya klabu ya Coastal Union kwa sababu wasiposhughulikiwa wanaweza kupelekea kuwagawa wanachama,wapenzi na mashabiki hivyo kudhoofisha maendeleo.

Wachezaji hao walitua uwanja wa ndege Tanga wakitumia ndege mbili tofauti ambapo baada ya hapo Mkuu huyo wa wilaya aliweza kuongoza msafara wa magari zaidi ya 50,pikipiki na baiskeli zisizokuwa na idadi zilizunguka maeneo mbalimbali jijini Tanga huku wananchi wakijitokeza kwa wingi kuilaki kila ilipokuwa ikipita kwa kuimba nyimbo za kuisifu timu hiyo.

Baada ya mzunguko huo ambao ulichukua takribani saa moja ndipo wachezaji wa timu hiyo wakawasili kambini eneo la Raskazone Hotel Pembezoni mwa bahari ya hindi ilipo kambi yao hivyo.

Dendego amesema kuwa lazima wao kama serikali wahakikisha klabu zao mkoani hapa zinakuwa na utulivu kila wakati kwa hiyo inapotokea inakwenda kunyume chake basi wao watachukua hatua kali ili iweza kuwa fundisho kwa watu wengine ambao wanaweza kufanya hivyo kipindi kingine.

  Hata hivyo amesema kuwa lazima wapenzi ,wanachama na mashabiki kuhakikisha wanakuwa na mshikamano wa thati ili kuweza kuhakikisha timu hiyo inafikia malengo yake waliojiwekea kwenye msimu mpya wa Ligi kuu soka Tanzania bara.

Kwa upande wake,Katibu Mkuu wa Coastal Union,Kassim El Siagi amesema kuwa timu hiyo ilifanya usajili mzuri msimu huu hivyo wana matumaini makubwa ya kufanya vizuri kwa kuanzia na mechi yao na Simba ambao haiwapi wasiwasi wa aina yoyote ile.

El Siagi amesema kutokana na maandalizi timu hiyo walioifanya wakiwa visiwani Pemba wana matumaini makubwa ya kuibuka na pointi tatu muhimu mbele ya Simba mechi ya ufunguzi wa Ligi kuu itakayochezwa uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Awali akizungumza katika mapokezi hayo,aliyekuwa Mwenyekiti wa Coastal Union,Hemed Aurora amewataka wapenzi ,wanachama kudumisha na kuendeleza mshikamano ili kuiwezesha timu hiyo kuweza kufikia malengo yao ya kuchukua ubingwa wa Ligi kuu msimu ujao.

     “Umoja na mshikamano ndio siri ya mafanikio yoyote yale hivyo nawasihi wapenzi ,mashabiki na wanachama muenzi mshikamno kwa sababu ndio nuru ya mafanikio kwenu “Alisema Aurora.