KINANA KUTUA TANGA SEPTEMBA 23 KWA AJILI YA ZIARA YA MKOA MZIMA.

September 21, 2014
TANGA.
KATIBU MKUU wa Chama cha Mapinduzi Taifa (CCM), Abdulrahamani Kinana anatarajiwa kuwasili mkoani Tanga Septemba 23 mwaka huu kwa ajili ya ziara yake ya kutembelea majimbo 11 mkoani Tanga na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo kisha kuweka mawe ya msingi.

Akizungumza na TANGA RAHA OFISINI KWAKE, Katibu wa CCM Mkoa wa Tanga, Shija Othumani alisema katibu huyo atapokelewa wilaya ya Handeni akitokea mkoani Pwani ambapo baadaye atazindua miradi ya kuweka mawe ya msingi eneo la Mkata pamoja na kushiriki kwenye mradi wa maji, ujenzi wa maabara kwenye shule za sekondari wilayani humo.

Alisema kuwa licha ya hayo atashiriki kwenye ujenzi wa matawi ya chama na majengo ya makao makuu kwa baadhi ya kata atakazozitembelea ambapo akiwa wilayani humo atashiriki kwenye ujenzi wa tawi la Kwenjugu mashariki.

Aidha alisema kuwa akiwa wilayani Korogwe, Kinana ataweka jiwe la msingi ofisi ya Chama hicho Kata ya Mashewa ikiwemo kufanya mikutano ya ndani pamoja na kuzungumza kupitia halmashauri kuu za wilaya.

Aliongeza kuwa licha ya kufanya kazi hizo, Katibu huyo atashiriki kwenye kazi mbalimbali ikiwemo za kufyetua matofauli kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vya maabara kwenye wilaya ambavyo zimepangwa kufanya hivyo.

  “Katibu Mkuu Kinana atawasili mkoani hapa Septemba 23 mwaka huu na atapokelewa kata ya Mkata wilayani Handeni hivyo wananchi na wakazi wa maeneo jirani hakikisha mnajitokeza kwa wingi kumlaki kiongozi huyo “Alisema


 Mwisho.