HABARI KUTOKA TFF LEO

HABARI KUTOKA TFF LEO

March 13, 2013
Habari zote na Boniface Wambura,Dar es Salaam.
LIGI YA VODACOM KUENDELEA J’MOSI

Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea Jumamosi (Machi 16, 2013) kwa mechi tatu zitakazochezwa katika miji ya Mwanza, Dar es Salaam na Manungu, Turiani mkoani Morogoro.

Toto Africans inayopigana kukwepa kurudi daraja la kwanza itakuwa mwenyeji wa Mgambo Shooting kutoka Tanga katika mechi itakayochezwa Uwanja wa CCM Kirumba.

Vinara wa ligi hiyo Yanga wataumana na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa wakati Uwanja wa Manungu utakuwa mwenyeji wa mechi ya Mtibwa Sugar na Coastal Union.

UCHAGUZI TAFCA KUFANYIKA MOROGORO
Uchaguzi wa viongozi wa Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA) utafanyika Jumamosi (Machi 16 mwaka huu) mjini Dodoma ambapo wajumbe wanatakiwa kuripoti siku moja kabla ya uchaguzi.

Wagombea waliopitishwa kuwania uongozi na Kamati ya Uchaguzi ya TAFCA chini ya uenyekiti wa Ramadhan Mambosasa ni Oscar Don Koroso (Mwenyekiti), Lister Manyara (Makamu Mwenyekiti) na Katibu (Michael Bundala).

Wengine ni Gabriel Gunda (Katibu Msaidizi), Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania- TFF (Wilfred Kidao) wakati wagombea ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Jemedali Saidi, George Komba na Magoma Rugora.

KIM KUTAJA KIKOSI CHA KUIKABILI MOROCCO
Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Kim Poulsen anatarajia kesho (Machi 13 mwaka huu) kutaja kikosi chake kitakachoivaa Morocco.
Mkutano huo wa Waandishi wa Habari utafanyika saa 5 asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itacheza na Morocco kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Machi 24 mwaka huu.

MECHI YA SIMBA, COASTAL YAINGIZA MIL 37/-
Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Coastal Union iliyochezwa juzi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 36,820,000 kutoka na watazamaji 6,284.

Viingilio katika mechi hiyo namba 138 iliyomalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 8,265,752.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 5,616,610.17.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 4,202,924.97, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 2,521,754.98, Kamati ya Ligi sh. 2,521,754.98, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,260,877.49 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 980,682.49.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
WACHEZAJI 23 WAITWA STARS KUIKABILI MOROCCO

WACHEZAJI 23 WAITWA STARS KUIKABILI MOROCCO

March 13, 2013
Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen ametaja wachezaji 23 watakaoingia kambini Jumamosi (Machi 16 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mechi ya mashindano dhidi ya Morocco.

Mechi hiyo ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwakani nchini Brazil itachezwa Machi 24 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Kocha Kim, wachezaji wa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager wanatakiwa kuripoti kambini katika hoteli ya Tansoma, Machi 17 mwaka huu.

Wachezaji walioitwa ni makipa Juma Kaseja kutoka Simba ambaye pia ndiye nahodha wa Stars, Aishi Manula (Azam), Hussein Shariff (Mtibwa Sugar) na Mwadini Ally (Azam). Mabeki ni Aggrey Morris (Azam), Erasto Nyoni (Azam), Issa Rashid (Mtibwa Sugar), Kelvin Yondani (Yanga), Nadir Haroub (Yanga), Nassoro Masoud Cholo (Simba) na Shomari Kapombe (Simba).

Viungo ni Salum Abubakar (Azam), Athuman Idd (Yanga), Amri Kiemba (Simba), Khamis Mcha (Azam), Frank Domayo (Yanga), Mwinyi Kazimoto (Simba) na Shabani Nditi (Mtibwa Sugar).

Washambuliaji ni John Bocco (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Mrisho Ngasa (Simba), Simon Msuva (Yanga), na Thomas Ulimwengu wa TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC).

Mbali ya Kim, benchi la ufundi la Taifa Stars linaundwa na Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa makipa), Leopold Tasso (Meneja), Dk. Mwanandi Mwankemwa (Daktari wa timu), Frank Mhonda (Mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza vifaa).

SEMINA ELEKEZI COPA COCA-COLA KUFANYIKA MACHI 19
Semina elekezi kwa ajili ya michuano ya Copa Coca-Cola 2013 itafanyika Machi 19 mwaka huu jijini Dar es Salaam. Washiriki wa semina hiyo wanatakiwa kuripoti Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) siku moja kabla (Machi 18 mwaka huu).

Washiriki hao ni makatibu wa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar. Pia waratibu wa mikoa wa mashindano ya Umoja wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA).

Barua za mwaliko kwa ajili ya semina hiyo tayari zimetumwa kwa vyama vya mpira wa miguu vya mikoa.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

PICHA YA UFUNGUZI WA KIKAO CHA TATHIMINI YA DAWATI LA JINSIA NA WATOTO MKOA WA TANGA

March 13, 2013
Katikati ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga,Constatine Massawe akiwa na waandishi wa habari mkoa wa Tanga baada ya ufunguzi wa kikao cha tathimini ya dawati la jinsia na watoto kilichofanyika leo jijini Tanga,kulia ni Katibu wa Klabu ya Waandishi wa habari mkoa wa Tanga,(Tanga Press club),Lulu George na kushoto ni mratibu wa dawati hilo,Yason Mnyanyi,Picha na Mwandishi Wetu,Tanga