ROYAL TOUR YAPAISHA MAPATO YA TANAPA
SHILINGI TRILIONI 1.4 KUTUMIKA KUKABILIANA NA MAGONJWA YA MALARIA, UKIMWI NA KIFUA KIKUU
Na WAF- Dodoma
Serikali ya Tanzania imepokea jumla ya dola za kimarekani milioni 602 sawa na trilioni 1.4 za kitanzania kwa ajili ya kukabiliana na magonjwa ya Malaria, Kifua Kikuu na UKIMWI katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2024 hadi 2026.
Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. John Jingu leo Machi 21, 2024 jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa mkakati wa utekelezaji wa fedha hizo kupitia mradi mpya wa Mfuko wa Dunia mzunguko wa saba.
Dkt. Jingu amesema fedha zilizopokelewa zimetokana na jitihada za Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha huduma za afya ili ziweze kuwafikia wananchi katika maeneo yao bila kikwazo.
“Mkutano huu umeandaliwa kwa wakati muafaka ili uwe chachu ya kuhakikisha utekelezaji wa mradi huu unakua na ufanisi uliokusudiwa huku lengo letu ni kuangalia na kufanyia kazi mambo muhimu tuliyojiwekea kwenye mikakati itakayoongoza utekelezaji wa mradi huu katika kipindi chote cha utekelezaji”. Amesema Dkt. Jingu
Aidha, Dkt. Jingu amefafanua kuwa Serikali kwa kushirikiana na Wadau imeendelea kutenga rasilimali zinazotumika kugharamia utekelezaji wa afua mbalimbali za kudhibiti UKIMWI, Kifua Kikuu, Malaria na Uimarishaji wa Mifumo ya Afya hivyo ameushukuru mfuko wa dunia kuweza kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa afua zilizopangwa.
“Tunatakiwa kuongeza kasi ya utekelezaji na kuongeza uwajibikaji kwa lengo la kuboresha hali ya utoaji wa huduma za Afya nchini. Ili kufikia malengo haya, wote tunao wajibu wa kusimamia na kutekeleza ipasavyo mipango tuliyojiwekea na kuwezesha shughuli zote za mradi ambazo zimepangwa kutekelezwa kwa kipindi cha mwaka 2024-2026 zinakamilika kwa asilimia mia moja”. Amesisitiza Dkt. Jingu.
Akitoa salamu za Serikali ya Marekani, Mwakilishi wa Serikali ya Marekani Dkt. Etruda Temba, ameishukuru Serikali kwa kuandaa mkutano huo na kusema wadau wa Maendeleo wanatambua mchango wa Serikali huku akitoa angalizo wakati wa utekelezaji kuepuka ubadhirifu wa fedha ili kupata matokeo yaliyokusudiwa.
Naye, Mwakilishi wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Subisya Kabuje, amesema Wizara yao imekuwa mnufaika mkubwa wa fedha za Mfuko wa Dunia ambapo katika kipindi cha awamu ya sita TAMISEMI ilipokea shilingi Bilioni 39.9 zilizofanikisha ukamilishaji wa mfumo wa taarifa za afya wa GoTHOMIS ambao umekuwa kichocheo kikubwa katika kusimamia huduma za afya kwenye ngazi za Mikoa na Vituo vya afya.
Mapema akimkaribisha Katibu Mkuu kufungua Mkutano huo, Maganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu, amesema ni lazima nchi kujipanga kufikia malengo ya dunia namba tatu lakini pia kukamilisha lengo kwenye sekta ya Afya mkakati wa tano, ili ifikapo 2026 nchi iweze kujipima kikamilifu mafanikio iliyopata.
UJENZI WA KIWANJA CHA NDEGE CHA MSALATO SEHEMU YA KWANZA KUKAMILIKA DISEMBA, 2024
Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa ameeleza kuwa ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Msalato - Dodoma umefikia asilimia 54.1 kwa sehemu ya kwanza inayohusisha ujenzi wa barabara ya kuruka na kutua ndege, maegesho ya ndege, barabara za maungio na barabara za kuingia na kutoka kiwanjani ambapo unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Disemba, 2024.
Bashungwa ameeleza hayo leo, Machi 21, 2024 wakati akiwasilisha Utekelezaji wa Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2023/24 na Makadirio ya Mpango na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2024/25 kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu.
"Nikuhakikishie Mwenyekiti kuwa ujenzi wa uwanja huu sehemu ya kwanza unaendelea vizuri na mkandarasi anaendelea na kazi, sehemu ya pili inayohusisha ujenzi wa jengo la abiria na majengo mengine nayo imefikia asilimia 17.1", amesema Bashungwa.
Aidha, Bashungwa amebainisha kuwa ukarabati, upanuzi na uboreshaji wa viwanja vya ndege vingine umefikia hatua mbalimbali ambapo Iringa (90%), Musoma (55%), Tabora (38%), Shinyanga (11%), Sumbawanga (6%) na Kiwanja cha Ndege cha Kigoma Mkandarasi yupo katika maandalizi ya kuanza ujenzi.
Bashungwa ameeleza kuwa Wakala wa Barabara (TANROADS) imefanikiwa kujenga barabara kwa kiwango cha lami zenye urefu wa kilometa 134.75 za barabara kuu, kilometa 23.11 za barabara za Mikoa na ukarabati kwa kiwango cha changarawe kilometa 253.67 katika kipindi cha utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2023/24.
Bashungwa ametaja baadhi ya miradi iliyotekelezwa ikiwemo ujenzi wa Daraja la Kigongo-Busisi (km 3.2) na barabara unganishi (km 1.66) umefikia asilimia 85, ujenzi wa miundombinu ya Mabasi Yaendayo Haraka Awamu ya Pili (km 20.3) umefikia asilimia 99.
Ameeleza miradi mingine ni ujenzi wa barabara ya mzunguko wa nje Dodoma (km 112.3) sehemu ya kwanza umefikia asilimia 68.3 na sehemu ya pili ya utekelezaji umefikia asilimia 56.32, upanuzi wa madaraja ya kibamba, kiluvya na mpiji yamekamilika pamoja na upanuzi wa barabara ya Kimara-Kibaha (km 19.2) njia nane.
Halikadhalika, Bashungwa amesema Wizara kupitia Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA) imekamilisha ukarabati wa vivuko nane (8) ambavyo vinaendelea kutoa huduma maeneo mbalimbali, ukarabati wa vivuko vitatu (3) vipo katika hatua mbalimbali ya utekelezaji pamoja na ujenzi wa vivuko vipya sita vinaendelea.
Vilevile, Bashungwa amesema kuwa Wizara kupitia Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB) imesajili Mkandarasi 1,192 ambapo Mkandarasi wa ndani ni 1,155 na wa nje ni 37 sawa na asilimia 99.3 ya lengo kwa mwaka 2023/24.
Hata hivyo, Bashingwa ameeleza Wizara kupitia Wakala wa Majengo (TBA) inaendeleza ujenzi wa majengo yenye uwezo wa kuchukua familia nyingi kutoka familia 4 hadi 114 katika maeneo yaliyokuwa chini ya usimamizi wa TAMISEMI ikiwemo Temeke Kota, Magomeni Kota na Ghana Kota.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mhe. Selemani Kakoso ameitaka Wizara kuendelea kusimamia na kutekekeleza miradi yote iliyoahidiwa na Serikali ili wananchi kupata huduma stahiki zinazotarajiwa.
Kadhalika, Kakoso ameisitiza Wizara hiyo kuendelea kufuatilia mchakato wa upatikanaji wa fedha ili kulipa madeni ya Makandarasi na kusaidia miradi mingine kuweza kutekelezwa kwa wingi na kwa wakati.
TGNP-UWAKILISHI WA WANAWAKE NAFASI ZA UONGOZI BADO CHANGAMOTO
NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
TAKWIMU zinaonesha bado hakuna uwakilishi wa kutosha wa wanawake katika nafasi za uongozi, za kuchaguliwa au kuteuliwa katika ngazi mbalimbali za uongozi na hata hivyo ukilinganisha na tulipotoka, kuna mabadiliko chanya katika ushiriki wa wanawake na uongozi.
Lengo namba 5 la Malengo ya Maendeleo Endelevu linataka wanawake washiriki kikamilifu na kwa tija na fursa sawa katika uongozi na ngazi zote za maamuzi katika siasa, uchumi na Maisha kwa ujumla.
Hayo yamebainishwa leo Machi 21, 2024 na Mkurugenzi Mkuu wa Mtandao wa Jinsia Tanzania- TGNP, Bi. Lilian Liundi wakati akifungua warsha ya waandishi wa habari ngazi ya jamii iliyofanyika katika Ofisi za TGNP Mabibo Jijini Dar es Salaam.
Amesema kutokana na mila na mitizamo kandamizi ambayo inadai kuwa wanawake hawana nafasi kwenye umma, madai yanayopewa nguvu na maarifa duni waliyonayo wanawake na uelewa mdogo wa haki zao,
"Kwa wale waliofanikiwa kuwa viongozi walau katika nafasi ndogo za maamuzi, wamekuwa wakiacha nafasi hizo kutokana na kukosekana kwa mfumo wa kuungwa mkono (supportive mechanism) kuanzia kwenye ngazi ya familia hadi jamii kwa ujumla". Amesema
Aidha amesema pamoja na kujivunia kuwa na wanawake viongozi katika nafazi za juu za maamuzi katika mihimili miwili ( Serikali na Bunge) pamoja na maeneo mengine, bado kuna changamoto kubwa katika kufikia 50/50.
Ameeleza kuwa bado hakuna mifumo rasmi na wezeshi ya kikatiba , kisheria na kisera, katika usawa katika nafasi za uongozi. Mila kandamizi, desturi na mitizamo hasi dhidi ya ushiriki wa wanawake katika maamuzi bado ni changamoto kubwa katika jamii yetu.
Kwa upande wake Mwandishi wa habari kutoka Rufiji FM, Bi. Kaundime Bakari amesema vyombo vya habari ni vyanzo vikubwa kupeleka taarifa eneo husika, hivyo atatumia chombo chake cha habari kuhakikisha wanatengeneza programu mbalimbali ambazo zinachochea wanawake kushiriki katika uongozi.
"Tunapoelekea kwenye kipindi cha uchaguzi, nitawashawishi wanawake wenzangu kuhakikisha wanashiriki katika kugombea nafasi ya uongozi mbalimbali na wasiweze kukaa nyuma". Amesema
Nae Mdau wa habari nchini, Bw. Meshack Michael amesema licha ya uwepo wa taasisi mbalimbali ambazo zinahimiza wanawake kushiriki katika uongozi, kuna jukumu la muhimu kwa waandishi wa habari nao wakatoa ushirikiano wa kutosha kwa taasisi hizo ili kundi kubwa la wanawake waweze kujitokeza katika kugombea nafasi za uongozi.
UCRT YAZINDUA MRADI WA UHIFADHI JUMUISHI WA MAZINGIRA NA KUBORESHA MAISHA YA JAMII YA MBULU
MGODI WA BARRICK BULYANHULU WAONGEZEWA MUDA WA LESENI YA UCHIMBAJI