TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI -WAZIRI MKUU ACHUKUA FOMU ZA KUWANIA URAIS

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI -WAZIRI MKUU ACHUKUA FOMU ZA KUWANIA URAIS

June 12, 2015

index 
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amechukua fomu za kuomba kuwania Urais wa Tanzania kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM).
Waziri Mkuu Pinda alikabidhiwa fomu hizo leo (Ijumaa, Juni 12, 2015), saa 4:03 asubuhi kutoka kwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM (Oganaizesheni), Bw. Mohammed Seif Khatib na saa 4:05 akaweka saini kwenye daftari la kupokea nyaraka ili kuthibitisha kuwa amezipokea.
Saa 4:07 alikabidhiwa mkoba wenye nyaraka hizo na Bw. Khatibu na saa 4:08 akaunyanyua juu mbele ya waandishi wa Habari waliokuwepo kwenye ukumbi wa Katibu Mkuu wa CCM kushuhudia akipokea fomu hizo. Kisha saa 4:15 aliingia ukumbi wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) kukutana na wanahabari.
Akizungumza na waandishi wa habari na wanaCCM waliofika ukumbi wa NEC kumsikiliza mara baada ya kuchukua fomu hizo, Waziri Mkuu alisema endapo atafanikiwa kuteuliwa na CCM awanie kiti cha Urais atasimamia utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Uchumi ili unufaishe makundi mengi zaidi ya jamii.
“Ukuaji wa uchumi uko vizuri lakini umaskini unapungua kwa kiasi kidogo, kasi yake hairidhishi… hii ni kwa sababu ukuaji huo umegusa sekta zisizogusa maisha ya watu moja kwa moja kama za ujenzi, utalii, uchukuzi na nyinginezo,” alisema.
“Wataalamu wa mataifa yaliyoendelea wanatuambia ukuaji wa uchumi hauonekani sana kwa sababu unagusa maisha ya watu wachache, sasa hivi wanataka jitihada ziongezwe kwenye jamii kubwa zaidi ambazo ni wakulima, wavuvi, wafugaji, wajasiriamali na warinaasali,” alisema.
“Mimi naamini tukiwagusa hawa impact kubwa itaonekana, ajira zitapatikana kwani viwanda vya usindikaji vitakuwepo; kilimo kikiboreshwa kwa kutumia zana za kisasa wengi watafanya kazi hiyo ambayo hivi sasa kila mtu anaikimbia kwa sababu ya shuruba za kazi yenyewe.”
Alisema Mpango wa Kwanza wa Maendeleo na Ukuzaji Uchumi ulilenga kuimarisha miundombinu zikiwemo barabara, bandari na ndani yake kulikuwa na mpango wa kuunganisha makao makuu ya mikoa yote kwa barabara za lami ifikapo mwaka 2018.
Alisema mpango huo ulioasisiwa na Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa ni wa miaka 25 (2000-2025) lakini ilibidi Rais Kikwete augawanye katika awamu tatu za miaka mitano mitano kuanzia kwama 2011 -2015 sababu muda uliobakia ulikuwa ni miaka 15 tu.
“Kwa maoni yangu kazi iliyokwisha kufanyika ni nzuri lakini tusibweteke. Chini ya Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Uchumi, mambo yatabadilika na ikiwezekana hatutafika 2025 kwa sababu maji, elimu, afya vitakuwa vimeboreshwa tayari,” aliongeza.
Akigusia kuhusu Ilani ya CCM, Waziri Mkuu alisema hawezi kuiongelea kwa sababu bado haijatoka. “Lakini ninaahidi, pindi ikitoka na kupitishwa na Mkutano Mkuu wa CCM, na Mungu akijalia nikapitishwa na chama, sitashindwa kuitekeleza Ilani hiyo. Nina uzoefu wa Ilani zote zilizopita,” alisisitiza.
Alisema kufanya kazi kwa karibu zaidi na Marais wote wanne na uwepo wake kwenye Serikali za Mitaa kwa muda mrefu ni turufu pekee anayoamini itamuwezesha kuwahudumia Watanzania vizuri zaidi kwani anaifahamu nchi kwa undani pamoja na matatizo yanayowakabili Watanzania walio wengi.
Alisema anaamini Mungu peke yake ndiye ajuaye nani amemuandaa kwa ajili ya kuiongoza nchi hii na kwamba hata yeye bado anamtumaini Mungu amuongoze katika safari hiyo. “Mungu peke yake ndiye anajua nani amemuandaa kwa nafasi hii, ni siri yake. Kadri itakavyompendeza, atampa nafasi hiyo yeye amtakaye,” alisema.
IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU,
  1. L. P. 980,
DODOMA.
IJUMAA, JUNI 12, 2015.

KIWANJA CHA MPIRA MAO TSE TUNG-ZANZIBAR CHAFANYIWA UTAFITI KWAAJILI YA KUJENGWA

June 12, 2015

Matayarisho ya awali ya maandalizi ya ujenzi wa Kiwanja cha Michezo cha Mao Tse tung kiliopo Mperani Kikwajuni Mjini Zanzibar yameanza rasmi kwa hatua ya utafiti wa uchunguzi wa udongo wa eneo hilo.
Mhandisi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Ali Mbarouk alieleza hayo wakati akimpatia ufafanuzi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefanya ziara fupi ya kuangalia matayarisho hayo.
Mhandisi Ali Mbaouk alimueleza Balozi Seif kwamba utafiti huo wa udongo unaofanywa kwa kuchukuwa  aina tofauti  za udongo kwenye vishimo 34 vinavyochimbwa  ndani ya eneo la uwanja huo unatarajiwa kuchukuwa muda wa siku 20.
Alisema udongo huo utafanyia utafiti wa kina na wataalamu waliobobea ambao kukamilikwa kwake watatoa ripoti kamili itakayofuatiwa na utangazaji wa tenda kwa Makampuni yatayokuwa tayari kujenga uwanja huo.
Alifahamisha kwamba ujenzi kamili wa uwanja wa Mao Tse Tung unatarajiwa kuanza rasmi mwezi wa Febuari mwaka 2016 chini ya ufadhili wa Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China.
Akitoa ufafanuzi wa Ramani ya  ujenzi  wa uwanja huo Mhandisi Ali Barouk alimueleza Balozi Seif kwamba uwanja huo utakapomalizika utakuwa na Viwanja viwili vya mchezo wa soka, kimoja kitakachokidhi michezo ya Pete pamoja na  Kikapu.
Alieleza kwamba lipo eneo litakalotengwa maalum kwa michezo mbali mbali ya ndani { INDO GAMES }, Majukwaa ya watazamaji eneo la watu Maarufu { VIP } pamoja na ofisi za watendaji wa uwanja huo.
Akielezea furaha yake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kukamilika kwa uwanja wa huo wa Mao Tse Tung kutasaidia kuupunguzia mzigo mkubwa uwanja wa michezo wa Amani.
Balozi Seif alisema uwanja wa Amani kwa sasa ndio pekee unaobeba michezo yote ya Kimataifa na Kitaifa ,Sherehe tofauti ikiwemo ile kubwa ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na matamasha mbali mbali.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kati kati akisalimiana na wataalamu wa Kichina wanaosimamia utafiti wa udongo katika uwanja wa  Mao Tse Tung katika matayarisho ya awali na maandalizi ya ujenzi wake.
 
 Eneo la Uwanja wa Michezo wa Mao Tse Tung likionekana kuwa katika maandalizi ya awali ya matayarisho ya ujenzi mpya unaotarajiwa kugharamiwa na Serikali ya Jamuhuri ya Watu wa China.
 Gari ya Kijiko likiwa katika harakati za uwekaji sawa eneo la Uwanja wa Mao Tse Tung ili kupatana udongo kwa ajili ya kufanyiwa utafiti wa kina kabla ya kuanza rasmi ujenzi wake.
  Mhandisi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Ali Mbarouk  aliyepo kati kati akimuonyesha  Balozi Seif ramani ya uwanja wa Mao utakavyokuwa baada ya kukamilika ujenzi.
Picha na – OPMR – ZNZ.

DKT.MAGUFULI AZIDI KUPATA WADHAMINI KATIKA MIKOA YA KILIMANJARO NA DAR ES SALAAM

June 12, 2015
Waziri wa Ujenzi ambaye pia ni Mbunge wa Chato Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akikabidhiwa fomu yenye orodha ya Wadhamini waliojitokeza kumdhamini katika  mbio za kuwania Urais wa Jamhuri ya Muungano kupitia chama hicho kutoka kwa Katibu wa CCM Wilayani  Moshi mjini Mkoani Kilimanjaro.
 Waziri wa Ujenzi Dkt. John Magufuli akisalimiana na baadhi ya wanachama wa CCM Mkoani Kilimanjaro waliojitokeza kwa wingi kwa ajili ya kumdhamini.
 Waziri wa Ujenzi Dkt. John Magufuli akisaini kitabu cha wageni huku Katibu wa CCM wilaya ya Moshi mjini akihakiki kadi za wanachama kwa ajili ya udhamini.
 Wanachama wa CCM wakimshangilia Waziri wa Ujenzi Dkt. John Magufuli wakati alipofika kwenye ofisi za CCM Wilaya ya Kinondoni.
 Waziri wa Ujenzi ambaye pia ni Mbunge wa Chato Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akikabidhiwa fomu ya wadhamini katika Wilaya ya Kinondoni, mkoani Dar es Salaam.
Waziri wa Ujenzi ambaye pia ni Mbunge wa Chato Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na baadhi ya wanachama wa CCM mkoani Dar es Salaam.

MAKAMBA AITIKISA RUVUMA, UDHAMINI WA WATU 3550 WAVUNJA REKODI

June 12, 2015

 Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Bumbuli, January Makamba amewataka makada wote waliomba ridhaa ya kuteuliwa kugombea nafasi ya urais ndani ya Chama  kuwa wanakiacha chama hicho kuwa salama baada ya mchakato huo kukamilika.

January, aliyasema hayo baada ya kupokea orodha ya wanachama wa chama hicho, katiaka Ofisi ya Chama Cha Mapinduzi Mkoa Ruvuma jana, ambapo wanachama 3500 walijitokeza kumdhamini.

Alisema hivyo kwa vile kuna wapo waomba ridhaa ambao wanadai kuwa endapo hawatateuliwa katika nafasi hiyo kuna hatari chama kikasambaratika.

Alisema, chama hicho kinahitaji kupata mgombea ambaye atahakikisha kuwa nama hicho kinabaki salama na kwambapia atawaongoza watanzania wote bila kujali dini wala kabila zao, akibainisha kuwa yeye ndio sahihi katika kudumisha hayo.

 ”Mimi siamini siasa za kupakana matope kwani wote ni wanachama wa chama kimoja na mwisho wa siku tutapata mgombea mmoja na tutahitajika kumpigia kampeni”alisema Jamuary.

January, alisema kama wagombea watapakana matope katika mchakato huo wa kuomba ridhaa kwa wanachama, anaamini wakati ukifika wa kumfanyia mteule utakuwa mgumu kwani itakuwa siyo rahisi kumfanyia kampeni ambaye tayari umekwisha kumpaka matope.

“Niwaombe muwapime wagombea ambao wameonekana wakiomba nafasi hiyo kwa mbwembwe kwani hatawatakapopata nafasi hiyo wataongoza kwa mbwe jambo ambalo wananchi hawalihitaji”alisema Jamnuary.

January, alisema kuwa chama hicho kiko makini na hakitamteua mgombea kwa woga kama inavyodaiwa na baadhi ya wagombea  kwamba wasipochaguliwa chama hicho kitasambaratika jambo ambalo siyo sahihi.

Alisema kuwa anaamini kuwa chama hicho kitamteuwa mgombea ambaye ni muadilifu, atakuwa rahisi katika kumnadi kwa wananchi.

Akizungumzia, mkoa wa Ruvuma, January, alisema mkoa huo hivi sasa unakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo tatizo la umeme na upande wa hospitali ya Mkoa.

Alisema kwa vile matatizo hayo anayatambua, pindi atakapopewa ridhaa na chama na kuchaguliwa kuwa rais atahakikisha mkoa huo unaingizwa katika gridi ya Taifa kama ilivyo kwa mikoa mingine.

Katika hatua yingine, juzi mkoani Njombe, January alipata wadhamini 84.

January, alisema anaamini atakapokuwa rais atakuwa na uwezo wa kuamua mambo makubwa yanayolihusu taifa ukilinganisha na nafasi aliyosasa kwani inamopaka katika maamuzi ya kushughulikia mambo mbalimbali ya Taifa. 


Mh January Makamba akihutubia wanachi na wanachama wa CCM mkoani Ruvuma mara baada ya kabidhiwa fomu yenye sahihi za wanachama waliomdhamini.
Mh January Makamba akihutubia wanachi na wanachama wa CCM mkoani Ruvuma ndani ya ukumbi wa ofiswi kuu ya chama hicho mkoani Ruvuma. kuanzia kushoto ni mke January Makamba, Ramona Makamba, katibu wa CCM mkoa wa Ruvuma, Verena Shumbusho na kulia ni mwenyekiti wa CCM mkoa, Odo Mwisho.
Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Ruvuma, Odo Mwisho akimkabidhi fomu yenye majina na sahihi za wanachama waliomdhamini mh. January Makamba. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ukumbi wa mikutano katika ofisi kuu ya CCM mkoa wa Ruvuma


 Mh January Makamba na mkewe, Ramona Makamba wakipeana mikono na wanachama wa CCM mkoa wa ruma waliofika katika ukumbi wa  mikutano katika ofisi kuu ya CCM mkoa wa Ruvuma.
Katibu wa CCM mkoa wa Ruvuma, Verena Shumbusho akiwakaribisha mkoani Ruvuma Mh January Makamba na mkewe.

MH. LOWASSA AZIDI KUVUNJA REKODI, APATA WADHAMINI 9516 MKOANI TABORA LEO

June 12, 2015