GGML: TUPO TAYARI KUSHIRIKIANA NA TANESCO

August 02, 2023

 

Makamu Rais wa AngloGold Ashanti- GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo (kushoto) akichangia mjadala wa nishati kupitia Jukwaa la fikra la Mwananchi uliofanyika juzi jijini Dar es Salaam. Wengine ni washiriki wa mjadala huo ulioenda sambamba na uzinduzi wa mpango mkakati wa miaka 10 wa Tanesco.

***
KAMPUNI ya Geita Gold Mining Limited (GGML) imesema ipo tayari kushirikiana kikamilifu na Shirika la Umeme nchini (Tanesco) kwa kutumia umeme gridi ya Taifa baada ya ujenzi wa kituo cha kupoza umeme na mradi wa kupeleka umeme katika migodi ya kampuni hiyo kukamilika.


Pia imeipongeza Tanesco na wizara ya nishati kwa kuja na mpango mkakati wa miaka 10 ambao utaliwezesha shirika hilo kuanzisha vyanzo vipya vya nishati endelevu kwani ni jambo litakalolisaidia Taifa kutimiza lengo namba saba la Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) linalozungumzia matumizi ya nishati inayofikika, ya gharama nafuu, endelevu na ya kisasa kwa wananchi wake.

Hayo yameelezwa jana na Makamu Rais wa AngloGold Ashanti- GGML anayeshughulikia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo wakati akichangia mjadala wa nishati kupitia Jukwaa la fikra la Mwananchi.

Shayo alisema mpango huo mkakati wa miaka 10, utaifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza kusini mwa nchi za Jangwa la Sahara kutimiza lengo hilo la maendeleo endelevu (SDGs)

"Ni hatua kubwa kwa Tanesco kutafsiri kwenye mkakati wake lile lengo namba saba," alisema.


Alisema licha ya kwamba kampuni nyingi za madini tangu miaka ya 2000 hutumia umeme wanaouzalisha wenyewe, sasa Serikali imekuwa na jitihada za makusudi kufungamanisha sekta ya nishati na sekta kubwa za uzalishaji kwa kuzalisha umeme unaotosheleza mahitaji ya wawekezaji wakubwa.

"Sisi kwa sekta ya madini tunaona hii kama ni baraka kubwa kwa sababu huwezi kuendesha migodi mikubwa kama ya kwetu (GGML) kwa kutumia jenereta," alisema.

Alitoa mfano kuwa GGML hutumia Megawati 29 ambazo huzalisha kwa mafuta lakini sasa wanatamani kuona mradi wa kupeleka umeme wa Tanesco katika mgodi wa kampuni hiyo ukikamilika ili kupunguza gharama za uendeshaji.


"Tukijiunga tu na Tanesco kwenye gridi ya Taifa na kutoka kwenye umeme tunaouzalisha wenyewe, tutapunguza gharama za umeme kwa asilimia 50, tuta-save dola za Marekani milioni 19 kila mwaka. Pia tutapunguza hewa ya ukaa kilotons 81 kufikia 2030," alisema.

Alisema kwa kuwa nchi ipo katika mipango ya kuwekeza pakubwa katika sekta ya madini kwa kuanzisha migodi ya uzalishaji wa madini mengine sehemu mbalimbali nchini, ni Dhahiri kuwa Tanesco itafanikiwa kuongeza mapato makubwa kutokana na mchango wa migodi hiyo kwenye matumizi ya umeme.

Alisema Tanesco wanajenga laini ya kilovolt 220 kutoka Bulyanhulu hadi Geita kisha laini ya kilomita sita yenye kilovolt 33 kuelekea katika mgodi wa GGML ilihali kampuni hiyi ikijenga kituo cha kupoza umeme kwenda kilovolt 11 kwa gharama ya dola za Marekani milioni 24.4.



Awali akizindua mpango huo mkakati wa Tanesco, Waziri wa Nishati, Januari Makamba aliwataka wananchi wawe na subira wakati Shirika hilo linafanya mageuzi ya utendaji kazi wake.

Alisema Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuipa mtaji TANESCO ili itekeleze mipango yake kwa ajili ya kutoa huduma bora kwa wananchi na Afrika kwa ujumla.


Naye Mkurugenzi wa TANESCO, Maharage Chande alisema shirika hilo linakusudia kuendelea na mipango yake ya kuboresha huduma kwa wateja wake, kupitia miradi mbalimbali ikiwemo wa kufua umeme katika Bwawa la Julius Nyerere, ambao unatarajia kuanza kuzalisha umeme Juni 2024.

FCC :YABAINI ASILIMIA 3.4 YA MAKONTENA HAYAJAFATA SHERIA YA ALAMA YA BIDHAA BANDARINI

August 02, 2023




Na Hamida Ramadhan , Dodoma

MKURUNGEZI Mkuu wa Tume ya Ushindani FCC William Erio amesema wameendelea kufanya Kaguzi ili kubaini wanaoingiza bidhaa nchini zilizo kiuka Sheria ya alama za bidhaa.

Pia FCC imefanya kaguzi ya kushtukiza katika Bandari ya Dar es Salaam na Bandari Kavu (ICDs) ambapo 3.4% ya jumla ya makasha (containers) yaliyokaguliwa yenye thamani ya kiasi cha Shilingi Bilioni 20.8 yalikutwa na bidhaa zilizokiuka Sheria ya Alama za Bidhaa .

Mkurungezi huyo ameyasema hayo leo Jijini hapa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu utendajiwa majukumu ya FCC ambapo ameeleza Kaguzi za kushtukiza (Dawn Raids) zilifanyika  bidhaa zenye thamani ya Shilingi Billioni 4.7 zilizokiuka Sheria ya Alama za Bidhaa zilikamatwa na hatua stahiki zilichukuliwa. 

Amesema Kaguzi hizo zilifanyika katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mtwara, Lindi, Ruvuma, Songwe, Kilimanjaro, Pwani, Mwanza, Arusha, Katavi na Mbeya.FCC imefanya uharibifu wa bidhaa bandia zilizokamatwa katika Mikoa ya Mbeya, Iringa na Ruvuma. 

Amebainisha bidhaa zilizoharibiwa ni pamoja na wino wa printa katoni 432 na kilo 1,302 za vifungashio.Kaguzi hizi zinapunguza madhara ya bidhaa bandia ambazo pamoja na mambo mengine, zinaweza kutokuwa salama kwa walaji, zinaikosesha serikali mapato, na zinaweza kuathiri biashara na uwekezaji halali.

"Walaji wanatakiwa kufahamu kuwa, watengenezaji wa bidhaa bandia huwa wanazalisha bidhaa hizi kwenye brands ambazo zinauzika kwa urahisi na zenye kukubalika zaidi sokoni (reputable brands)," Amesema Mkurungezi huyo 

Na kuongeza"Hivyo  ni vizuri walaji wajifunze mbinu za kuzitambua bidhaa bandia kwa kufanya milinganisho ya bei (kati ya bandia na isiyo bandia) pamoja na kufuata maelekezo ya alama za bidhaa zinazotolewa na kampuni husika inayomiliki nembo ya bidhaa halali," amesema. 

Katika kipindi Julai, 2022 hadi Juni, 2023; FCC imefanikiwa kutekeleza na imeidhinisha maombi 56 ya miungano ya kampuni kutoka katika sekta mbalimbali kama vile kilimo, uzalishaji, madini, mawasiliano, mafuta na Gesi. 

Amesema Maombi 51 yalipitishwa bila masharti na maombi matano (5) yalipitishwa kwa masharti. Kwa mujibu wa Sheria, maombi ya miungano yanatakiwa kushughulikia ndani ya siku 90, lakini yamekuwa yakishughulikiwa kwa wastani wa siku 75.

Amesema FCC imetoa msamaha katika mkataba mmoja (1) uliokuwa ukififisha ushindani “exemption to agreement” kati ya Precision Air Services Plc na Kenya Airways Plc kwa lengo la kuendeleza Sekta Ndogo ya Usafiri wa Anga Nchini.

Ameeleza FCC imefanya uchunguzi wa mashauri 20 yanayohusu miungano ya kampuni ambayo haikuidhinishwa na FCC (unnotified mergers).

"Kati ya mashauri haya 4 yameshafungwa na yaliyobaki yako katika hatua mbalimbali za kushughulikiwa. FCC imechunguza Mashauri nane (8) yanayohusu uwezekano wa kuwa na matumizi mabaya ya nguvu ya soko (abuse of market power) ambapo moja limefungwa na mengine yako katika hatua mbalimbali za kushughulikiwa," amesema.

MAFANIKIO YA TUME YA USHINDANI KWA UJUMLA  

Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita (mwaka 2020 - 2023), FCC iliridhia kununuliwa kwa kampuni 14 zenye jumla ya thamani ya bei ya mauziano inayofikia Shilingi Bilioni 49.4 katika sekta ya kilimo kwa lengo la kuruhusu kampuni hizo kuongeza wigo zaidi sokoni, kuongeza mitaji na kupunguza uwezekano wa kampuni hizo kuondoka sokoni.  

Kampuni hizi ni pamoja na Mtanga Foods Limited (yenye biashara zake Iringa), kampuni ya uzalishaji wa Parachichi ya Rungwe Avocado Company Limited, kampuni ya uchenjuaji mpunga (mchele) ya MW Rice Millers Limited na Mring’a Estates Limited. 


Mwisho

MKUTANO WA MAAFISA HABARI WAFANYIKA ZANZIBAR.

August 02, 2023

 Na Rahima Mohamed, Sheha Sheha   Maelezo       1/8/2023

Maafisa habari wametakiwa kutumia vyombo vya habari vya serikali kutoa taarifa za utekelezaji katika  taasisi zao kwa jamii.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Habari na Matukio kutoka shirika la Utangazaji Zanzibar Salum Ramadhan kwa niaba ya Mkurugenzi wa Shirika hilo katika mkutano wa maafisa habari, mawasiliano na uhusiano wa taasisi za Serikali huko Ukumbi wa Sanaa Rahaleo Mkoa wa Mjini Unguja.

Amesema maafisa kuna umuhimu mkubwa kwa viongozi wa taasisi za umma kutumia vyombo vya habari ili wananchi wajue maendeleo yanayofanywa na serikali yao.

Aidha amesema maafisa habari wanatakiwa kutumia njia mbalimbali kutoa taarifa  katika taasisi zao ikiwemo kuandaa Makala, matangazo  na vipindi mbali mbali vinazotoa uchambuzi  zinazoeleza maendeleo ya nchi.

Vilevile, amewashajihisha maafisa habari hao  kuvitumia vipindi vya asubuhi njema na dira vinavyoendeshwa na shirika hilo ambavyo vinatoa nafasi kwaviongozi wa taasisi mbali mbali kuzungumza na Wananchi.

Mkurugenzi Salum ameipongeza Idara ya habari Maelezo  kwa  kusimamia sera ya habari  na kuwakutanisha pamoja  maafisa hao kwa lengo la kujua maendeleo wanayoyafanya na changamoto wanazokumbana nazo katika majukumu yao ya kila siku.

Mkurugenzi wa idara ya Habari Maelezo amewataka wakuu wa taasisi mbalimbali kuwashirkisha maafisa Habari katika kazi zao ili jamii iweze kuhabarika juu ya kazi hizo.

 Aidha amewataka maafisa habari kuwa wabunifu  katika kuandaa kazi zao za kihabari na kuendana na kasi teknolojia ya habari na mawasiliano.

 

Kwa upande wao maafisa habari kutoka taasisi mbali mbali, wamesema kumekuwa na changamoto mbali mbali ambazo zinarejesha nyuma majukumu yao ipasavyo ikiwemo ufinyu wa bajeti na ushirikishwaji mdogo.


Mkurugenzi Habari na Matukio wa Shirika la Utangazaji Zanzibar ZBC Salum Ramadhan Abdalla akitoa hotuba katika Mkutano wa Maafisa Habari,Mawasiliano na Uhusiano uliofanyika katika Ukumbi wa Sanaa Rahaleo Zanzibar.

Afisa Habari wa ZRA Makame Khamis akitoa Taarifa ya Jumuia ya Maafisa Habari wa Serikali katika Mkutano wa Maafisa Habari,Mawasiliano na Uhusiano uliofanyika katika Ukumbi wa Sanaa Rahaleo Zanzibar.

Afisa Uhusiano Mkoa wa Kaskazini Shaame Siami kitoa Mchango wake katika Mkutano wa Maafisa Habari,Mawasiliano na Uhusiano uliofanyika katika Ukumbi wa Sanaa Rahaleo Zanzibar.

RAIS WA ALGERIA AKUTANA KWA MAZUNGUMZO NA WAZIRI TAX

August 02, 2023

 Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, Mhe. Abdelmadjid Tebboune amekutana Kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) alipomtembelea Ikulu Jijini Algiers, Algeria tarehe 1 Agosti 2023.


Mazungumzo hayo yamefanyika pembezoni mwa Mkutano wa Tano wa Tume ya Pamoja ya Kudumu ya Ushirikiano (JPC) kati ya Tanzania na Algeria unaofanyika kuanzia tarehe 30 Julai 2023 hadi 1 Agosti 2023.

Mazungumzo ya viongozi hao yalijikita katika kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kirafiki na kidiplomasia ili kuweza kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa maslahi mapana ya nchi zao.

Aidha, katika kuendelea kuimarisha ushirikiano Waziri Tax pamoja na majukumu mengine, atazindua Ofisi za Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 2 Agosti 2023 Jijini Algiers.

Uzinduzi wa ubalozi huo, ni hatua muhimu hasa wakati huu ambapo viongozi hao wamekubaliana kuinua sekta za uchumi ambazo ni pamoja na biashara, uwekezaji, nishati, madini, elimu, sayansi na teknolojia, afya na utalii.


Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, Mhe. Abdelmadjid Tebboune akisalimiana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Dkt. Stergomena Tax (Mb.) alipomtembelea Ikulu Jijini Algiers, Algeria tarehe 1 Agosti 2023.