Showing posts with label afya. Show all posts
Showing posts with label afya. Show all posts

NHIF TANGA YATOA ELIMU YA BIMA NA KUFANYA UPIMAJI WA MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA KANISA LA KKKT USHIRIKA WA MAKORORA TANGA

July 06, 2026 Add Comment



Na Oscar Assenga,TANGA

Wazazi, walezi na waajiri nchini wamehimizwa kuhakikisha watoto wanawakatia bima ya afya mapema ili kuwaepusha na changamoto za gharama kubwa za matibabu na kuwawezesha kupata huduma za afya kwa wakati wanapougua.

Wito huo umetolewa leo na Afisa Matekelezo wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga, Macrina Clemens, wakati wa utoaji wa elimu kuhusu bima ya afya ulioambatana na zoezi la upimaji wa afya na usajili wa wanachama wa vifurushi mbalimbali katika Kanisa la KKKT Ushirika wa Makorora, jijini Tanga.

Akizungumza na waumini wa kanisa hilo, Macrina alisema afya ni mtaji muhimu kwa maendeleo ya familia na Taifa, hivyo kujiunga na bima ya afya ni uwekezaji unaowalinda wananchi dhidi ya gharama zisizotarajiwa za matibabu.

Alisema wazazi wanaowakatia watoto wao bima ya afya hupata uhakika wa matibabu wakati wowote mtoto anapougua, jambo linalowapa utulivu wa akili na kuwawezesha watoto kuendelea na masomo bila kukatishwa na changamoto za kifedha.

“Mzazi anapokuwa na bima ya afya kwa mtoto wake anakuwa na uhakika wa kupata matibabu kwa wakati, hivyo kuepuka usumbufu wa kutafuta fedha za dharura kila ugonjwa unapojitokeza,” alisema.

Macrina alisema wanafunzi wanaosoma katika shule mbalimbali wanaweza kujiunga na bima ya afya kupitia shule zao kwa gharama ya Sh50,400 kwa mwaka mzima wa masomo, huku watoto ambao bado hawajaanza shule wakijiunga kupitia vifurushi mbalimbali vinavyotolewa na NHIF.

Alisema Serikali inaendelea kutekeleza azma ya kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na bima ya afya, hivyo akazitaka taasisi za elimu, wazazi, walezi, waajiri na wamiliki wa kampuni binafsi kutumia fursa hiyo kuwaandikisha watoto na wafanyakazi wao.

“Bima ya afya si gharama, ni kinga ya maisha. Ukiwa na bima unakuwa na uhakika wa kupata daktari, dawa na huduma za matibabu bila kubeba mzigo mkubwa wa kifedha pale unapougua,” alisema.

NHIF imeendelea kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya wananchi kuhusu umuhimu wa bima ya afya ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuongeza idadi ya Watanzania wanaonufaika na huduma hiyo na kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya nchini.




ZAIDI YA WANANCHI 6000 KUNUFAIKA NA ZAHANATI YA MUUNGANO,MWENGE WA UHURU WARIDHISHWA NA MRADI

June 23, 2026 Add Comment


Na Oscar Assenga, Muheza

WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 Wazo Mwang'onda alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kutasaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.

Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.

Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.

Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.

Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.

Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.









ZAIDI YA KAYA 7,800 TANGA ZANUFAIKA NA MPANGO WA BIMA YA AFYA KWA WOTE

June 09, 2026 Add Comment

 

Na Oscar Assenga,TANGA

Zaidi ya wananchi 20,000 kutoka kaya masikini mkoani Tanga wameanza kunufaika na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, unaolenga kuboresha upatikanaji wa huduma za matibabu kwa kaya zenye kipato cha chini.

Mpango huo, unaotekelezwa kwa awamu ya kwanza na ya pili, unalenga kuwafikia wananchi walio katika mazingira magumu kiuchumi ili kuwawezesha kupata huduma za afya bila kikwazo cha gharama za matibabu. Ufadhili wa mpango huo unatolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), ukiwa na lengo la kupunguza mzigo wa gharama za matibabu kwa kaya masikini.

Hadi sasa, zaidi ya wanufaika 20,000 kutoka kaya 7,816 wamepatiwa kadi za bima ya afya na wameanza kutumia huduma hizo tangu Machi mwaka huu. Hatua hiyo imeelezwa kuwa imeleta matumaini mapya kwa wananchi wengi ambao hapo awali walikabiliwa na changamoto ya kumudu gharama za matibabu.

Akizungumza katika Maonesho ya Kibiashara ya Mwahako, Daktari Lawi Kupaza kutoka Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga amesema mwitikio wa wananchi umekuwa mkubwa, huku wengi wa walengwa waliostahili tayari wakikabidhiwa kadi zao.

Amesema zoezi hilo linaendelea vizuri katika halmashauri zote za mkoa huo, huku awamu ya pili ikitarajiwa kufikia kaya nyingine 1,300.

“Kwa sasa tunaendelea na ugawaji wa kadi pamoja na uhakiki wa taarifa za wanufaika. Tunawahamasisha wananchi kujitokeza kuhakiki taarifa zao ili waweze kupata huduma kwa wakati,” amesema Dkt. Kupaza.

Hata hivyo, amekiri kuwepo kwa changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ukubwa wa maeneo ya utekelezaji na ratiba za shughuli mbalimbali.

“Kuna changamoto ya kuwafikia wanufaika wote kwa wakati kutokana na ratiba na ukubwa wa eneo la utekelezaji. Hata hivyo, watendaji wa kata na vijiji wanaendelea kusaidia katika uhamasishaji,” ameongeza.

Kwa upande wake, Afisa Madai wa NHIF, Neema Kisinga, ameitaka jamii kuendelea kujiunga na bima ya afya ili kujikinga na gharama kubwa za matibabu.

Amesema mfuko huo una vifurushi mbalimbali vinavyowezesha wananchi kupata huduma za afya kwa gharama nafuu, ikiwemo kifurushi cha Tarangire ambacho kinatoa huduma za matibabu, vipimo na ushauri wa daktari kwa gharama nafuu kwa mwaka mzima.

“Kuwa na bima ya afya kunapunguza mzigo wa kulipia huduma kila unapougua au kuhitaji matibabu. Hii ni njia bora ya kujilinda na gharama zisizotarajiwa za afya,” amesema Kisinga.

Mpango huo unaendelea kuonekana kama hatua muhimu katika juhudi za Serikali za kuhakikisha wananchi wote, hususan wa kipato cha chini, wanapata huduma bora za afya bila kuathiriwa na changamoto za kifedha.

SMZ YATAJA MAFANIKIO YA BIMA YA LAZIMA KWA WAGENI

Kajunason June 07, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Arusha.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetumia Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu-KiliFair 2026 kutangaza mafanikio ya mpango wa bima ya lazima kwa wasafiri, ikieleza kuwa umeimarisha usalama wa wageni na kuchangia ukuaji wa sekta ya afya pamoja na mapato ya utalii visiwani humo.

Mpango huo ulioanza kutekelezwa rasmi Oktoba 1, 2024, unawataka wageni wote wa kimataifa wanaoingia Zanzibar kuwa na bima ya usafiri kabla ya kuwasili. Tangu kuanzishwa kwake, mpango huo umeendelea kuwa chanzo muhimu cha mapato, ukiingiza wastani wa dola za Marekani milioni moja, sawa na zaidi ya Sh bilioni 2.6 kila mwezi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika banda la Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) kwenye viwanja vya Magereza jijini Arusha, Ofisa Mauzo wa shirika hilo, Abdul-Halim Muhammad, alisema maonesho hayo yamewapa fursa ya kutoa elimu kwa watalii, wawekezaji na wadau wa sekta ya utalii kuhusu umuhimu wa bima hiyo.

“Tunashiriki Karibu-KiliFair kuongeza uelewa kuhusu bima hii ya lazima na kueleza namna inavyowanufaisha wageni huku ikichangia maendeleo ya huduma muhimu Zanzibar,” alisema.

Kwa mujibu wa utaratibu huo, wageni wengi wa kimataifa hulipa dola 44 za Marekani kwa kila safari ya kuingia Zanzibar, huku wageni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wakilipia dola 22 pekee. Watoto wenye umri wa miaka mitatu hadi 17 hulipa dola 22, huku walio chini ya umri huo wakisamehewa.

Muhammad alisema bima hiyo inawawezesha wageni kupata huduma za matibabu ya dharura na msaada mwingine muhimu wanapokuwa Zanzibar, hatua inayopunguza changamoto za kifedha na kuhakikisha wanapata huduma kwa haraka wanapozihitaji.

Alisema sehemu ya mapato yanayokusanywa kupitia mfuko huo hutumika kugharamia huduma za afya kwa wageni waliokatiwa bima, huku fedha zinazobaki zikielekezwa katika kuimarisha huduma za afya kwa wananchi na wageni kwa ujumla.
“Mpango huu ulianzishwa baada ya mamlaka kubaini kuwepo kwa matukio ya mara kwa mara ya watalii na wawekezaji kuhitaji matibabu ya dharura huku kukiwa na sintofahamu kuhusu nani angegharamia huduma hizo. Sasa mfumo huu umeondoa changamoto hiyo,” alisema.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa KiliFair Promotions, Dominic Shoo, alisema Karibu-KiliFair 2026 imeendelea kuthibitisha nafasi yake kama maonesho makubwa ya utalii na biashara Afrika Mashariki kwa kuwakutanisha wadau kutoka zaidi ya nchi 40 duniani.

Alisema maonesho hayo yamevutia zaidi ya waoneshaji 500 na wanunuzi wa huduma za utalii wapatao 20,000, hatua inayochochea uwekezaji, ushirikiano wa kibiashara na upanuzi wa masoko ya utalii katika ukanda wa Afrika Mashariki.

“Karibu-KiliFair ni jukwaa muhimu la kuitangaza Tanzania na Afrika Mashariki kimataifa. Kadri wadau wanavyoongezeka kushiriki, ndivyo fursa za biashara, uwekezaji na ukuaji wa sekta ya utalii zinavyozidi kuongezeka,” alisema Shoo. 

NAIBU SPIKA SILLO: MICHANGO YA WADAU MUHIMU KUIMARISHA UPANDIKIZAJI FIGO NA ULOTO KWA WATOTO WENYE SICKLE CELL.

May 20, 2026 Add Comment

NAIBU Spika wa Bunge, Daniel Sillo, ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kushiriki katika kuchangia huduma za matibabu ya upandikizaji Uloto kwa Watoto wenye ugonjwa wa Sicle Cell na upandikizaji figo kwa wenye uhitaji hapa nchini.

Ameyasema hayo wakati wa hafla ya chakula cha jioni tarehe 19 Mei, 2026 katika ukumbi wa Domiya jijini Dodoma, ambapo hafla hiyo imewakutanisha viongozi waandamizi wa mkoa wa Dodoma, wabunge na  wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mfuko wa kusaidia matibabu ya upandikizaji uloto na figo pamoja na huduma nyingine za kibingwa.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana ya huduma hizo za upandikizaji uloto na figo kutolewa hapa nchini na hivyo kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika endapo wananchi wangeenda kutibiwa nje ya nchi.

Alisema kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kuchangia huduma hizo si jukumu la serikali na taasisi pekee, bali ni wajibu wa pamoja kwa kuwa magonjwa ya figo na sickle cell hayachagui mtu kwa nafasi yake, dini wala hali ya maisha.

“Tunaposhiriki katika michango hii si kwa ajili ya taasisi moja, bali tunaunga mkono huduma za kitaifa zinazogusa maisha ya wananchi wengi wanaohitaji matibabu hayo,” alisema Mhe. Sillo.

Alitoa wito kwa wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono juhudi hizo za BMH ili kuwezesha wagonjwa wanaohitaji huduma za upandikizaji viungo na matibabu mengine maalumu kupata huduma kwa wakati.

Ameeleza kutegemea bajeti ya serikali pekee hakuwezi kukidhi mahitaji yote yanayoongezeka ya huduma za kibingwa, hivyo ushirikishwaji wa wadau ni njia muhimu ya kuimarisha sekta ya afya na kuokoa maisha ya Watanzania wengi.

WAZIRI MCHENGERWA ANGOZA UJUMBE WA TZ WHA 79 GENEVA USWISI

WAZIRI MCHENGERWA ANGOZA UJUMBE WA TZ WHA 79 GENEVA USWISI

May 18, 2026 Add Comment






Na John Mapepele, Geneva, Uswisi

Waziri wa Afya Nchini, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa ameongoza ujumbe wa Serikali ya Tanzania katika ufunguzi rasmi wa Mkutano Mkuu wa 79 wa Shirika la Afya Duniani (WHA79) ulioanza leo Mei 18, 2026 mjini Geneva, Uswisi.

Mkutano huo mkubwa duniani katika sekta ya afya unashirikisha zaidi ya nchi 180 katika maeneo mbalimbali ulimwengu umefunguliwa na
Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

“Mkutano wa 79 wa Baraza la Afya Duniani (WHA79) unafanyika kuanzia tarehe 18 hadi 23 Mei 2026 mjini Geneva, Uswisi. Mkutano huu unawakutanisha wajumbe kutoka Nchi Wanachama wa WHO ili kushughulikia shinikizo kubwa linaloikabili mifumo ya afya na kuweka sera za afya za kimataifa, huku ukisisitiza sana huduma ya afya kwa wote, afya ya akili, na athari za mabadiliko ya tabianchi kwa afya.” Amefafanua Mheshimiwa Mchengerwa

Kwa mujibu wa Mheshimiwa Mchengerwa, maeneo makuu ya mjadala katika mkutano wa mwaka 2026 ni pamoja na:
Huduma ya Afya kwa Wote (UHC) na Ufadhili ambapo amesema Nchi wanachama na mashirika ya kiraia wanatoa kipaumbele kwa kuharakisha mifumo ya ufadhili wa afya inayoongozwa na nchi husika, mageuzi ya kidijitali katika mifumo ya afya, na kuhakikisha ushiriki wa kijamii ili kuimarisha mamlaka ya afya ya kitaifa.

Aidha amesisitiza eneo jingine linalopewa mkazo ni Afya ya Akili ambapo amesema kufuatia Mkutano wa Ngazi ya Juu wa Umoja wa Mataifa wa mwaka 2025 kuhusu Magonjwa Yasiyoambukiza (NCDs) na afya ya akili, WHA79 ina kampeni kubwa za utetezi na matukio maalum yanayolenga kutafsiri ahadi za kimataifa kuwa mikakati halisi ya kitaifa ya afya ya akili.

Jambo jingine litakalojadiliwa ni Tabianchi na Afya ambapo amefafanua kuwa ingawa si ajenda maalum ya pekee, athari zinazoendelea za mzozo wa tabianchi na matumizi ya mafuta ya kisukuku ni sehemu muhimu ya mijadala inayohusu afya ya uzazi, magonjwa yasiyoambukiza, na usimamizi wa magonjwa.

Amesem WHO pia inazindua mpango wa kimataifa wa utetezi uliokusudiwa kudumisha msukumo kuelekea mkutano ujao wa COP31 kuhusu tabianchi.
Mkakati wa Kimataifa na Uongozi: Wajumbe wanajadili namna ya kuoanisha mageuzi mbalimbali ya afya ya kimataifa ili kuhakikisha matokeo yenye usawa na uwajibikaji.

Aidha, mkutano huu unaweka msingi wa uchaguzi ujao wa Mkurugenzi Mkuu wa WHO, huku wagombea wakianza kutangazwa rasmi na kundi jipya la nchi likichaguliwa kuingia katika Bodi ya Utendaji.

Pia ameongeza kwamba mkutano huu pia utajadili taarifa na Mikakati ya Magonjwa ambapo ajenda ya muda ya mkutano inajumuisha hatua zinazoendelea kwa mpango wa kutokomeza malaria, Ajenda ya Chanjo 2030, na mkakati wa kumaliza ugonjwa wa kifua kikuu (TB).

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huu ulioongozwa na Mheshimiwa Mchengerwa umeshirikisha Mheshimiwa Balozi Abdala Possi, Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa na Mashirika Mengine ya Kimataifa Mjini Geneva, Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Afya na Ukimwi, Mheshimiwa, Dkt. Johannes Lukumay, Katibu Mkuu Dkt. Seif Shekalaghe, Mganga Mkuu wa Serikali
, Dkt. Grace Magembe na baadhi ya watendaji wa Wizara ya Afya.

Tanzania inatarajia kuwasilisha mawasilisho kadhaa katika mkutano huo na kufanya majadiliano na wadau mbalimbali wa afya pembezoni mwa mkutano huo.

KIPINDI CHA MWAKA 2021-2026 HUDUMA ZA AFYA ZIMEONGEZEKA, ZIMEIMARIKA

May 11, 2026 Add Comment


Na Hassan Kimweri, WAF - Dodoma

Sekta ya afya nchini imepata mafanikio makubwa katika kipindi cha awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan yaliyoongeza upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi kupitia ujenzi wa miundombinu, ununuzi wa vifaa tiba, uoatikanaji wa dawa pamoja na huduma za kibingwa na za dharura nchini.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema hayo leo Mei 11, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara ya Afya kwa mwaka wa fedha 2026/27 katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Spika wa Bunge Mhe. Mussa Azan Zungu.

"Eneo la vituo vya kutolea huduma za afya vimeongezeka kutoka elfu 10,153 mwaka 2021/22 hadi elfu 13,683 kufikia Machi 2026, sawa na ongezeko la vituo 3,530, Zahanati zimeongezeka kutoka elfu 7,189 hadi elfu 8,706 huku hospitali zikiongezeka kutoka mia 404 hadi mia 475 mwaka 2026," amesema Waziri Mchengerwa

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema Serikali imeongeza majengo mapya katika hospitali mbalimbali zikiwemo Hospitali ya Muhimbili, KCMC, BMH, Bugando, Mirembe, pamoja na Kibong'oto huku ikiwa imejenga hospitali mpya 10 za rufaa za mikoa, kukarabati hospitali kongwe 50, kukamilisha maboma 980 ya zahanati na kujenga vituo vya afya 390.

Amesema, katika huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto, Serikali imeongeza wodi za watoto wachanga kutoka 80 hadi 438 pamoja na vituo vya upasuaji wa dharura kutoka 445 hadi 630 ambayo ni mafanikio yaliyochangia kupungua kwa vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 556 mwaka 2016 hadi vifo 104 mwaka 2022 kwa kila vizazi hai 100,000.

"Katika huduma za uchunguzi na matibabu ya kibingwa, Serikali imenunua na kusimika vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi bilioni 241.6 ambapo mashine za MRI zimeongezeka kutoka 7 hadi 13, CT Scan kutoka 12 hadi 45 pamoja na Digital X-ray kutoka 147 hadi 559," amesema Waziri Mchengerea

Kwa upande wa chanjo, amesema watoto waliopata chanjo ya Pentavalent dozi ya tatu wameongezeka kutoka watoto milioni 2,093,412 hadi milioni 3,186,979 huku kiwango cha chanjo kikiongezeka kutoka asilimia 93 hadi 96, juu ya lengo la kimataifa la asilimia 90.

"Upatikanaji wa dawa na bidhaa za afya umeimarika, Serikali imetoa Shilingi trilioni 1.4 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba, viwanda vipya 11 vya dawa na vifaa tiba vimeanzishwa huku 'Tanzania Pharmaceutical Industries kikifufuliwa kwa ajili ya uzalishaji wa dawa za VVU nchini," amesema Waziri Mchengerwa

SERIKALI YATOA BILIONI 48.8 BIMA YA AFYA KWA WOTE

May 11, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu , Dodoma


Serikali imeanza rasmi utekelezaji wa Mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya zisizo na uwezo kwa kutoa Shilingi bilioni 48.8 kwa ajili ya kuwawezesha wananchi wa makundi maalum kupata huduma za afya kwa uhakika. Kupitia utekelezaji huo, jumla ya kaya 172,297 tayari zimefikiwa na kuingizwa kwenye mpango huo, huku wanufaika 463,228 wakianza kupata huduma mbalimbali za matibabu katika vituo vilivyosajiliwa nchini.

Akiwasilisha Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Afya Fungu 52 kwa mwaka 2026/27 Waziri wa Afya Mhe. Omary Mchengerwa amesema kuwa, utekelezaji huu unaonesha dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila kujali hali yake ya kiuchumi, ikiwa ni sehemu ya safari ya kuelekea huduma jumuishi za afya kwa wananchi wote.

Katika kuimarisha sekta ya afya sambamba na utekelezaji wa mpango huo, mabaraza na bodi za kitaaluma yameendelea kusimamia ubora wa huduma kwa kusajili wataalam wa afya 14,310, hatua inayoongeza nguvu kazi muhimu kwa utoaji wa huduma nchini.

Amesema kuwa kuhusu upatikanaji wa huduma za matibabu, jumla ya maduka ya dawa 330 yamesajiliwa pamoja na watarajali 3,004, huku vituo vya kutolea huduma za afya 3,643 vikisajiliwa ili kuongeza upatikanaji wa huduma karibu na wananchi.

Katika kuhakikisha taaluma na maadili yanaendelea kuzingatiwa hususan wakati huu wa kuhudumia wananchi wengi zaidi kupitia mfumo wa Bima ya Afya, vituo binafsi vya afya 654 vimekaguliwa ili kuhakikisha vinakidhi viwango na kutoa huduma salama kwa wananchi.

Mafanikio hayo yanaakisi hatua kubwa ya Serikali katika kujenga mfumo imara wa afya unaojali usawa, ubora na upatikanaji wa huduma kwa wote, huku Bima ya Afya kwa Wote ikiendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

UWEKEZAJI WA SH.BILIONI 50 KITUO CHA MPOMVU WAIMARISHA UPATIKANAJI WA UMEME KANDA YA ZIWA

March 15, 2026 Add Comment


















Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imefanya ziara ya ukaguzi katika Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Mpomvu kilichopo mkoani Geita tarehe 15 Machi 2026, ikiwa ni sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi ya kimkakati ya Nishati inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Subira Mgallu amesema ziara hiyo imelenga kukagua maendeleo ya miradi ya nishati pamoja na kuhakikisha uwekezaji unaofanywa na Serikali unaleta matokeo yaliyokusudiwa kwa wananchi.


“Kama Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini tuna jukumu la kuisimamia Wizara ya Nishati ili kuhakikisha inatekeleza majukumu yake kikamilifu. Tumeridhishwa na uwekezaji uliofanywa katika kituo hiki ambacho kina mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na shughuli za kiuchumi,” amesema Mhe. Mgallu.


Ameongeza kuwa Kituo hicho kina uwezo wa kupokea na kusambaza takribani megawati 90, huku jitihada zikiendelea kuboresha miundombinu ya usambazaji wa umeme ikiwemo mpango wa kuongeza laini maalum kwa ajili ya Mgodi wa dhahabu wa Geita (GGM).


“Mahitaji ya umeme ya mgodi wa GGM yanatarajiwa kufikia takribani megawati 70 ifikapo mwaka 2035 kutoka megawati 36 zinazotumika kwa sasa, hivyo ni muhimu kuendelea kuimarisha miundombinu ya usambazaji wa umeme ili kukidhi mahitaji hayo,” ameongeza.


Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Nishati Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kuimarisha miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Geita kutokana na ukuaji mkubwa wa shughuli za kiuchumi na kijamii hususan katika sekta ya madini.


“Kituo hiki kina mchango mkubwa katika kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Geita pamoja na maeneo ya jirani ikiwemo Biharamulo na Ngara mkoani Kagera, Sengerema mkoani Mwanza na Kakonko mkoani Kigoma,” amesema Mhe. Salome.


Naibu Waziri wa Nishati ameongeza kuwa Kituo cha Mpomvu kimegharimu takribani shilingi bilioni 50, uwekezaji ambao umeongeza uwezo wa usambazaji wa umeme katika eneo hilo linalokua kwa kasi kiuchumi ambapo mahitaji ya sasa ya umeme yamefikia Megawati 73.64.


Awali, Mkoa wa Geita ulikuwa ukipokea umeme kutoka Mkoa wa Shinyanga wenye uwezo wa takribani megawati 4 pekee, kiwango ambacho hakikukidhi mahitaji ya umeme yaliyokuwa yakiongezeka kutokana na shughuli za kiuchumi hususan uchimbaji wa madini.


Kituo cha Kupokea na Kupoza umeme cha Mpomvu kilianza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, kabla ya kuzinduliwa rasmi mwaka 2022 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

DKT.MAGEMBE ATAKA KILA MWAJIRI AHAKIKISHE MTUMISHI WAKE ANAKUWA NA UHAKIKA WA MATIBABU KUELEKEA BIMA YA AFYA KWA WOTE

March 10, 2026 Add Comment




Na Hassan Kimweri, WAF - Dar es Salaam


Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Grace Magembe amewataka waajiri kuhakikisha kila muajiriwa anakuwa na uhakika wa matibabu kuelekea utekelezaji wa Bima ya Afya kwa Wote na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050. 


Dkt. Magembe amesema hayo leo Machi 10, 2026 baada ya wasilisho la maandalizi ya Bima ya Afya kwa Wote kwenye mkutano na Wakurugenzi Wakuu wa Makampuni ya Tanzania (CEO Roundtable of Tanzania – CEOrt) uliofanyika jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha viongozi kutoka serikalini, sekta binafsi na washirika wa maendeleo. 



"Serikali inaendelea kuimarisha utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kuwa na ubunifu wa vyanzo vya fedha pamoja na kuanzisha kitita muhimu kitakachohakikisha kila mwananchi anapata huduma muhimu za afya katika vituo vyote vya kutolea huduma nchini," amesema Dkt. Magembe

Aidha, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanza utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambapo utekelezaji wake unafanyika kwa awamu, awamu ya kwanza ilianza Januari 6, 2025 kwa kuwatambua zaidi ya familia milioni 3.6 kidijitali kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa," amesema Dkt. Magembe

Katika hatua nyingine, Dkt. Magembe amesema Serikali imeanzisha Mfuko wa kugharamia huduma za Afya (Health Equity Fund) utakaosaidia kugharamia huduma za afya kwa wananchi wasio na uwezo wa kumudu gharama za matibabu kupitia vyanzo mbalimbali.

Pia, amesema Serikali imeanza kuchukua hatua za kupunguza utegemezi wa misaada ya wahisani katika sekta ya afya kwa kuimarisha zaidi vyanzo vya ndani vya fedha na kutafuta mbinu mpya za ubunifu zitakazochangia kugharamia huduma za afya nchini.

Hata hivyo, ameeleza dhamira ya Serikali kuimarisha viwanda vya ndani vya dawa na bidhaa za afya ili kuhakikisha upatikanaji wa dawa unakuwa wa uhakika, kuongeza ajira na kukuza sekta binafsi kuelekea utekelezaji wa bima ya afya kwa wote. 

Mwisho, Serikali imewahimiza wawekezaji kutumia fursa zilizopo katika sekta hiyo, huku ikiendelea kukuza ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi katika uzalishaji wa dawa na vifaa tiba nchini.