HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

SHULE YA VIZIWI NJOMBE YAHAMIA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

March 16, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu,Njombe

SHULE ya Sekondari ya Viziwi mkoani Njombe imetekeleza agizo la Serikali la kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ili kuepukana na madhara ya kiafya yanayosababishwa na moshi wa nishati chafu.

Akizungumza wakati wa ziara ya timu ya wataalamu kutoka Wizara ya Nishati iliyotembelea shule hiyo kukagua utekelezaji wa agizo hilo, Mjiolojia kutoka Kitengo cha Nishati Safi ya Kupikia,  Nsajigwa Maclean, amesema shule hiyo imefanikiwa kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Amesema hatua hiyo ni sehemu ya kampeni ya utoaji wa elimu kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Njombe.

 Maclean amefafanua kuwa matumizi ya nishati mbadala kama gesi, majiko banifu na umeme yana mchango mkubwa katika kupunguza uharibifu wa misitu unaotokana na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Aidha, amesema moshi unaotokana na matumizi ya nishati za jadi umekuwa ukichangia kusababisha magonjwa ya mfumo wa upumuaji kwa wapishi na wanafunzi, hivyo matumizi ya nishati safi yanasaidia kulinda afya pamoja na kuboresha mazingira ya kujifunzia shuleni.

Amezipongeza shule ambazo tayari zimeanza kutumia nishati safi ya kupikia, akisema hatua hiyo inaunga mkono juhudi za Serikali za kulinda mazingira na kuboresha afya za watumiaji.

Amesema Wizara ya Nishati itaendelea kutoa elimu na kuhamasisha taasisi mbalimbali, ikiwemo shule, hospitali na magereza, kuachana na matumizi ya kuni na mkaa na badala yake kutumia nishati safi na salama kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Viziwi,  Rosemary Mbuya, amesema kufuatia agizo la Serikali, shule hiyo iliamua kuachana na matumizi ya kuni na mkaa kutokana na gharama kubwa za upatikanaji wake.

“Gharama ya kununua kuni na mkaa ilikuwa kubwa sana, na mara nyingi tulilazimika kuvifuata mbali. Pia wapishi wetu walikuwa wakikumbwa na changamoto za kiafya mara kwa mara kutokana na moshi,” amesema Mbuya.

Ameongeza kuwa tangu kuanza kutumia nishati safi ya kupikia, kumekuwa na maboresho makubwa katika ufanisi wa shughuli za jikoni pamoja na afya za wapishi.

 Amesema matumizi ya gesi yamepunguza muda wa kupika chakula kwa wanafunzi na kupunguza gharama zilizokuwa zikitumika kununua kuni na mkaa mara kwa mara.

Mwalimu Mbuya pia amebainisha kuwa hatua hiyo imechangia kulinda mazingira kwa kupunguza utegemezi wa ukataji wa miti kwa ajili ya kuni.


JANUARI MAKAMBA ATOA FUTARI KWA TAASISI ZA DINI TANGA

March 16, 2026 Add Comment



Na Mashaka Mhando, TANGA


MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Januari Makamba, ametoa msaada wa futari kwa taasisi nane za kidini jijini Tanga, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono waumini katika mwezi mtukufu wa Ramadhan.


Zoezi hilo lililofanyika  Machi 15 Jijini Tanga, limenufaisha taasisi za TAMTA, Maawal Chumbageni, Zahara Rashad, Shamsi Maarifa, Sururu, Noor-Hudaa, Abutwalib pamoja na Anisa.



Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Makamba amesema hatua hiyo inalenga kuimarisha mshikamano, upendo na utamaduni wa kusaidiana, hususan kwa makundi yenye uhitaji katika kipindi hiki cha funga.



“Taasisi za dini zina nafasi kubwa katika kulea maadili mema kwa vijana na jamii kwa ujumla. Ni muhimu kuendelea kuzisaidia na kushirikiana nazo ili zijikite katika kutoa malezi bora,” amesema Makamba.



Kwa upande wao, viongozi na wanafunzi wa taasisi hizo wameishukuru hatua hiyo wakieleza kuwa msaada huo utasaidia kupunguza mahitaji ya chakula kwa wanafunzi na waumini wanaofanya ibada katika vituo hivyo.



Kwa mujibu wa mratibu wa msaada huo wa futari, Salimu Bawazir alisema, utoaji huo wa futari ni umekuwa sehemu ya utaratibu wa Makamba kushirikiana na jamii ya Tanga katika masuala ya kijamii na kidini ili kuchochea maendeleo na umoja mkoani hapa.



Bawazir alisema baada ya kupita na kugawa futari katika taasisi za dini, Jumatatu Machi 16 mhe Malamba ameandaa futari kwenye hoteli ya Kitalii ya Tanga Beach Resort kwa watu mbalimbali waliopewa mialiko maalum.





KUTOKA NDOTO HADI FURAHA: UMEME KUMFIKIA BIBI SESILIA

March 16, 2026 Add Comment

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, alipata nafasi ya kusikiliza ombi la Bibi Sesilia Charles wakati wa mazungumzo na wananchi katika Kitongoji cha Elimu, Kijiji cha Mushinde, Kata ya Buwangongo wilayani Geita. Bibi Sesilia alimueleza kuwa licha ya umeme kufikishwa katika kitongoji chao, bado nyumba yake haijaunganishiwa huduma hiyo.

Katika mazungumzo hayo, Bibi Sesilia alimuelekeza Naibu Waziri kwa kidole akionyesha ilipo nyumba yake, akieleza kuwa nguzo ya umeme tayari imesimamishwa karibu na eneo hilo na kuomba kusaidiwa ili naye aweze kuunganishiwa umeme. Akijibu ombi hilo, Naibu Waziri alisema, “Pole sana Bibi, ombi hili nalifanyia kazi hapa hapa.”

Bila kupoteza muda, Naibu Waziri alimuita Mhandisi wa REA na kumuelekeza kwenda pamoja na Bibi Sesilia nyumbani kwake ili kumsaidia kufanya taratibu za maombi ya kuunganishiwa umeme na kuhakikisha anaunganishiwa haraka iwezekanavyo.

Akitekeleza maelekezo hayo, Mhandisi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) aliahidi kuchukua hatua mara moja na kuhakikisha Bibi Sesilia anapata huduma hiyo muhimu.

Baada ya kupata matumaini ya kuunganishiwa umeme, Bibi Sesilia alionekana mwenye furaha kubwa akicheza kwa shangwe na kusema, “Mama Samia oyeee! Sasa na mimi naletewa umeme mpaka ndani.”

Tukio hilo lilitokea tarehe 14 Machi 2026 wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ilipozindua mradi wa upelekaji umeme katika vitongoji 15 kwa kila jimbo la uchaguzi (HEP 2A) kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika kitongoji hicho.

WATAALAMU WA UFUATILIAJI NA TATHMINI WANOLEWA KUHUSU NAMNA YA KUTATHMINI MIRADI INAYOTEKELEZWA NA SERIKALI

March 16, 2026 Add Comment




Na Mwandishi wetu- Dodoma

 Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea na hatua ya tatu ya kujengewa uwezo  wa namna ya kufanya tathmini za programu na miradi kupitia programu ya Kuendeleza  Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II)  ili kuwawezesha watalaam wa ufuatiliaji na tathmini kupata uelewa na namna ya kutathmini miradi na programu mbalimbali zinazotekelezwa katika taasisi za umma.


Hayo yamesemwa leo tarehe 16 Machi 2026, jijini Dodoma na Mkurugenzi wa Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Bi. Sakina Mwinyimkuu   wakati akifungua mafunzo yanayofanyika kwa siku nne Jijini Dodoma yakihusisha washiriki kutoka wizara zinazotekeleza  program ya ASDP II na washiriki kutoka nchini Zimbabwe na Malawi kwa lengo la kujifunza chini ya Twendembele Initiative ambapo Tanzania ni mshirika.

 


Bi. Sakina amewasisitiza washiriki kuzingatia mafunzo kwani yatawasaidia katika kuimarisha eneo la tathmini kwa ujumla yanayotolewa na Watathmini wazawa wa Kampuni ya Auxim na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine mkoani Morogoro huku yakiratibiwa  na Clear Initiatives kwa ufadhili kutoka Global Evaluation Initiative iliyopo chini ya Benki ya Dunia.

 “Mabadiliko ya sekta ya kilimo yanaendelea kuwa msingi wa mikakati ya maendeleo katika Afrika Mashariki na Kusini, ambapo mifumo ya kilimo cha wakulima wadogo ina jukumu muhimu katika kudumisha maisha ya vijijini, kuhakikisha usalama wa chakula, na kuchochea ukuaji wa uchumi wa kitaifa” amesema Mkurugenzi huyo.

 


Ameongeza kuwa, mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo Awamu ya Pili (ASDP II) unasimama kama mpango wa ushirikiano wa wadau wengi, ukiwa na lengo la kuongeza uzalishaji wa kilimo, kukuza ujumuishaji wa masoko, kuendeleza uendelevu wa mazingira, na kuimarisha ushiriki jumuishi wa kiuchumi miongoni mwa wakulima wadogo na jamii za vijijini.

 


“Mnamo Desemba 2024, Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Sera, Mipango na Uratibu (PMO-PPCD) iliingia katika ushirikiano na kituo cha kujifunza kuhusu tathmini na matokeo – Afrika ya Anglophone (CLEAR-AA) cha Global Evaluation Initiative (GEI) katika Wits School of Governance pamoja na Taasisi ya Ujerumani ya Tathmini ya Maendeleo (DEval) ili kufanya tathmini ya matokeo ya ASDP II,” ameongeza.

 


Vilvile amefafanua kwamba, ushirikiano huo unaonyesha dhamira ya makusudi ya kuzingatia viwango vya kimataifa vya tathmini huku ukihakikisha kuwa mchakato wa tathmini unabaki katika umiliki wa kitaifa na unachangia kujifunza kwa taasisi.

 “Mfumo huu wa ushirikiano umeundwa kuunganisha umakini wa kitaalamu, uimara wa mbinu, na mbinu bora za kimataifa, huku ukihakikisha kuwa serikali zinazoshiriki zinabaki na umiliki kamili wa mchakato na matokeo yake,” alieleza Mkurugenzi huyo.

 

Pia ameeleza kwamba, warsha hiyo  inawaleta pamoja wawakilishi kutoka nchi mbalimbali. wakiwemo wadau wakuu wa kitaasisi  ambao ni pamoja na Serikali ya Tanzania, inayowakilishwa na PMO-PPCD na Wizara zinazoongoza Sekta ya Kilimo zinazohusika katika utekelezaji wa program,  Serikali ya Zimbabwe kupitia Ofisi ya Rais na Baraza la Mawaziri – Kurugenzi ya Tathmini, Kujifunza na Utafiti,  na Serikali ya Malawi, inayowakilishwa na Wizara ya Fedha, Mipango ya Uchumi na Ugatuzi.

 


“Mtandao wa kikanda wa tathmini wa Twende Mbele unashiriki pia, ukichangia utaalamu wa kulinganisha na kuwezesha ujifunzaji wa pamoja kati ya mifumo ya tathmini barani Afrika. Muundo huu wa utawala wa wadau wengi unaonyesha dhamira inayokua ya kikanda ya kuingiza utamaduni wa tathmini ndani ya mifumo ya kitaifa,” amesema.


Aidha, ameeleza kwamba  sifa mojawapo muhimu ya tathmini  inayoongozwa na Nchi (Country-Led Evaluation) ni ujumuishaji wa makusudi wa maendeleo ya uwezo wa kitaasisi kama sehemu kuu ya mchakato, badala ya kuwa shughuli ya ziada kwani maendeleo endelevu katika utawala unaotumia ushahidi hayategemei tu uzalishaji wa matokeo ya tathmini, bali pia kuimarisha uwezo wa taasisi kuagiza, kusimamia na kutumia tathmini kwa muda mrefu.


RAIS SAMIA ATOA BILIONI 5.2 KUBORESHA CHUO CHA UHAMIAJI TRITA

March 15, 2026 Add Comment





Na Mwandishi Wetu,KILIMANJARO

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Patrobas Katambi amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imepeleka Kiasi cha Shilingi Bilioni 5.2 kwa Idara ya Uhamiaji ili kuboresha Chuo cha Uhamiaji cha Kikanda(TRITA) kilichopo Kilimanjaro ambapo Waziri Katambi ameweka wazi nia ya kuanzisha kutoa elimu katika ngazi ya Shahada,Uzamili na Uzamivu ambapo kwa sasa chuo hicho cha masuala ya uhamiaji kikitoa elimu ngazi ya Diploma.

Ametoa kauli hiyo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo,Najma Murtaza Giga(Mb), kwa ajili ya ukaguzi wa Miradi iliyopo chini ya wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

“Ni chuo ambacho kimejikita zaidi kwenye taaluma ya soft skills(ujuzi laini) ila mafunzo ya medani yanatolewa Chuo cha Raphael Kubaga kilichopo Wilayani Mkinga,Mkoani Tanga kwa hapa tunakusudia kama tutafanya vizuri zaidi na kwa kuwa Mheshimiwa Rais anaviwezesha Vyombo vilivyopo chini ya wizara kifedha basi tuna matumaini ya kufika kwenye hatua ya kutoa elimu ngazi ya Shahada,Uzamili na Uzamivu inawezekana kwa eneo hili ukiwepo urahisi wa kufika na tunapata wanafunzi kutoka nchi za jirani” amesema Waziri Katambi

Akizungumza katika ziara hiyo Kamishna Jenerali wa Uhamiaji, Dkt.Anna Makakala amesema Idara sasa inatoa mafunzo ya Kijeshi kwenye Chuo kilichopo wilayani Mkinga Mkoani Tanga ambapo hapo awali walikua wakitumia Vyuo vya Majeshi mengine kutoa mafunzo mbalimbali ya ukakamavu ikiwemo Shule ya Polisi,Magereza na Jeshi la Kujenga Taifa ambapo Mkuu wa Chuo hicho cha kikanda, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji, Hoja Mahiba akitaja wazi kutolewa kwa elimu ngazi ya Diploma sambamba na mafunzo mbalimbali kwa Maafisa Uhamiaji katika kuwajengea uwezo,kutoa mafunzo kwa wadau wanaopokea wageni wakiwemo watalii na watumishi wa serikali ikiwemo watendaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Akizungumza katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje Ulinzi na Usalama,Najma Murtaza Giga(Mb) ameitaka Idara ya Uhamiaji kuweka mifumo ya teknolojia ili kusaidia maeneo mengine huku Mjumbe wa Kamati hiyo,Nape Nnauye(Mb) akishauri uanzishwaji pia wa elimu masafa ili kuweza kuwafikia wanafunzi wengi zaidi.








MIKAKATI MIPYA YAWEKWA KUONGEZA UTAFUTAJI WA MAFUTA NA GESI NCHINI

March 15, 2026 Add Comment


Katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia mafuta na Gesi asilia Dkt. James Mataragio amewaelekeza Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kuimarisha shughuli za utafutaji akibainisha kuwa shughuli hizo zimepungua kwa kiasi kikubwa katika miaka ya hivi karibuni

Katika Kikao chake na Menejimenti ya Mamlaka hiyo mwishoni mwa Juma hili  jijini Dar es Salaam amesema moja ya maeneo yanayohitaji kipaumbele kwa hivi sasa ni utafutaji wa Gesi asilia.


Ameeleza kuwa miaka ya nyuma shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia zilikuwa zinafanyika kwa kasi kubwa, ambapo mikataba ya uzalishaji na ugawanaji wa mapato (PSA) ilikuwa zaidi ya 26, lakini kwa sasa imepungua na kufikia mikataba 11 pekee.

“Pia tukichunguza kwa kina, hata katika mikataba hiyo iliyobaki, ni kampuni chache zinazotekeleza kikamilifu majukumu yao ya kuendelea kufanya utafutaji wa mafuta na gesi asilia. Hali hii hairidhishi na inahitaji mikakati madhubuti ya kuchochea shughuli za utafutaji nchini,” alisema Dkt. Mataragio.

Aliongeza kuwa kupungua kwa shughuli za utafutaji ni hatari kwa mustakabali wa upatikanaji wa gesi asilia nchini, kwa kuwa utafutaji ndiyo hatua muhimu inayochochea ugunduzi wa rasilimali hizo na hatimaye kupelekea uzalishaji wake.

“Kwa sasa tumejipanga kama Wizara kuhakikisha tunaweka juhudi kubwa katika eneo hili pamoja na kuboresha mazingira wezeshi yatakayochochea uwekezaji na ustawi wa shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia,” alisisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Mhandisi Charles Sangweni, amesema mamlaka imeendelea kutekeleza mikakati ya kuendeleza utafutaji wa mafuta na gesi asilia nchini ikiwa ni pamoja na kuingia mikataba na makampuni ya kijiofizikia yaliyobobea katika ukusanyaji wa takwimu za petroli (Multi-Client Geophysical Companies) ili kuimarisha utafiti katika maeneo ya bahari kuu na nchi kavu.

Kikao hicho kimehudhuriwa na viongozi mbalimbali, akiwemo Kamishna Msaidizi wa Petroli kutoka Wizara ya Nishati, Mhandisi Antelimi Raphael, Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Mhandisi Charles Sangweni, pamoja na maafisa wengine kutoka Wizara ya Nishati na PURA.