HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
RC MTANDA AKABIDHI PIKIPIKI 18 KWA VIKUNDI 2 VYA VIJANA BUCHOSA
WIZARA YA NISHATI YASISITIZA USHIRIKIANO KUFIKIA ASILIMIA 80 YA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA IFIKAPO 2034
habari
Wizara ya Nishati imesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo katika kufanikisha lengo la Taifa la kufikia asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Wito huo umetolewa na Mjiolojia Mkuu wa Wizara ya Nishati, Bw. Ngereja Mgejwa, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, wakati akifungua Maonesho na Kongamano la Nishati Safi ya Kupikia 2026 (Clean Cooking Expo 2026), Juni 23, 2026 katika Ukumbi wa EACLC jijini Dar es salaam.
Akizungumza katika kongamano hilo, Bw. Mgejwa amesema nishati safi ya kupikia ni ajenda muhimu ya kitaifa inayohitaji ushirikiano wa wadau wote ili kuleta mabadiliko ya kudumu katika sekta ya nishati. Amesema matumizi ya nishati safi yana mchango mkubwa katika kulinda afya za wananchi, hususan wanawake na watoto, kuhifadhi mazingira, kuinua elimu kwa watoto wa kike na kuongeza tija ya kiuchumi.
Ameeleza kuwa kazi iliyopo mbele ni kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi ya kupikia iliyo nafuu, salama na endelevu ikiwemo gesi oevu (LPG), majiko banifu, gesi asilia, umeme, bayogesi na bayoethanoli.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya nishati safi pamoja na kutoa elimu kwa umma ili kubadili matumizi ya nishati za jadi kwenda kwenye nishati safi.
Bw. Mgejwa amepongeza Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TABWA) kwa kuandaa kongamano hilo, akisema majadiliano yatakayofanyika yataibua suluhisho na mapendekezo yatakayochochea ongezeko la matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.
Ameongeza kuwa kongamano hilo litahitimishwa kwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitakazotumika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi kwa afya na uhifadhi wa mazingira.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ya Wafanyabiashara Wanawake Tanzania(TABWA) Bi. Noreen Mawalla amesema maonesho hayo yameandaliwa chini ya kaulimbiu ya "Linda Afya, Hifadhi Mazingira, Okoa Muda kwa Uchumi Endelevu" kwa lengo la kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia na kuunga mkono utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia.
Amebainisha kuwa Clean Cooking Expo 2026 itafanyika kwa siku tatu na itajumuisha mafunzo, mijadala na maonesho ya teknolojia mbalimbali za nishati safi zitakazowakutanisha wadau kutoka sekta ya umma na binafsi.
Amewakaribisha wananchi kutembelea mabanda ya maonesho ili kupata elimu na taarifa sahihi kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia, huku akieleza kuwa Mbio za Nishati Safi ya Kupikia zitafanyika Jumamosi na zinatarajiwa kuongozwa na Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi.





ZAIDI YA WANANCHI 6000 KUNUFAIKA NA ZAHANATI YA MUUNGANO,MWENGE WA UHURU WARIDHISHWA NA MRADI
afya
Na Oscar Assenga, Muheza
WANANCHI 6,258 wa Kijiji cha Muungano, Wilaya ya Muheza, wanatarajiwa kunufaika na huduma bora za afya kufuatia kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Muungano, mradi ambao umepokelewa na kuridhiwa na Mwenge wa Uhuru 2026 baada ya kukaguliwa na kupokea taarifa ya utekelezaji wake.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2026 Wazo Mwang'onda alisema kukamilika kwa zahanati hiyo kutasaidia kusogeza huduma za matibabu karibu na wananchi na kupunguza changamoto ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za afya.
Alisema Serikali tayari imepeleka vifaa tiba pamoja na watumishi wa afya watakaotoa huduma katika zahanati hiyo, hatua inayoonesha dhamira ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya, hususan katika maeneo ya vijijini.

“Mradi huu ni muhimu kwa wananchi wa Muungano na maeneo jirani kwa sababu unasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kuongeza ustawi wa jamii,” alisema.
Kiongozi huyo aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo yametokana na ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa maendeleo, hususan Taasisi ya Islamic Help, iliyochangia ujenzi wa zahanati hiyo, huku Serikali ikigharamia vifaa tiba na watumishi wa afya.
Aliwashukuru wadau wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya kijamii, na kuwataka kuendeleza ushirikiano huo ili kusaidia kuboresha huduma muhimu kwa wananchi.

Aidha, aliwahimiza wananchi kuendelea kulinda amani na utulivu wa nchi, akisema kuwa mazingira hayo yanawezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuvutia wadau zaidi kushirikiana na Serikali.
Kwa upande wake, akitoa taarifa ya mradi huo, Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza, Dk. Fani Mussa, alisema ujenzi wa Zahanati ya Muungano ulianza Machi 2, 2025 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 165.94.

Alieleza kuwa kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 141.55 zilitumika kwa ujenzi, huku Shilingi milioni 24.39 zikitumika kununua vifaa tiba.
Kwa mujibu wa Dk. Mussa, zahanati hiyo itahudumia wakazi 6,258 wa Kijiji cha Muungano, wakiwemo wanaume 3,089 na wanawake 3,169, na inatarajiwa kwa kiasi kikubwa kuboresha upatikanaji wa huduma za afya katika eneo hilo.

Baada ya ukaguzi huo, Mwenge wa Uhuru 2026 ulieleza kuridhishwa na ubora wa utekelezaji wa mradi huo, ukibainisha kuwa ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za afya karibu na wananchi na kuunga mkono jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya afya nchini.
TEA YATAKIWA KUONGEZA ELIMU KWA UMMA KUHUSU FURSA ZA MFUKO WA ELIMU WA TAIFA
habari
MADIWANI WA MPANDA NA NSIMBO WAIPONGEZA SERIKALI KWA UWEKEZAJI MKUBWA KATIKA KITUO CHA KUFUA UMEME CHA JULIUS NYERERE
Nishati
Na Mwandishi wetu,
Rufiji – Pwani
Madiwani wa Halmashauri za Wilaya za Mpanda na Nsimbo mkoani Katavi, wakiongozana na baadhi ya wabunge na viongozi wengine, wamepongeza uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP) baada ya kujionea kwa karibu uendeshaji wa kituo hicho na mchango wake katika maendeleo ya sekta ya nishati nchini.
Viongozi hao walitembelea kituo hicho tarehe 20 Juni 2026 kwa lengo la kujionea uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali, kufahamu namna kituo kinavyoendeshwa pamoja na kupata uelewa wa mchango wake katika kuimarisha upatikanaji wa umeme nchini. Ziara hiyo ilihusisha madiwani 22 pamoja na baadhi ya wabunge na viongozi wengine kutoka Mkoa wa Katavi.
Akizungumza baada ya ziara hiyo, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Mpanda, Charles Philipo, aliishukuru Serikali kwa juhudi kubwa inazoendelea kufanya katika kuimarisha sekta ya nishati na kuipongeza TANESCO kwa kuwapatia viongozi hao fursa ya kujionea kituo hicho.
“Tunaishukuru Serikali yetu kwa namna ambavyo imejikita kutatua changamoto ya umeme. Nipende kuwashukuru TANESCO kwa niaba ya waheshimiwa madiwani wa Mpanda na Nsimbo kwa kuona namna ya sisi kuja hapa na kujionea kituo hiki,” alisema Philipo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Nsimbo, Mhe. Anna Mpembe, alisema ameoneshwa kuvutiwa na ukubwa wa kituo hicho na kiwango cha uwekezaji kilichowekwa katika kuhakikisha Tanzania inakuwa na umeme wa kutosha kwa maendeleo ya taifa.
“Leo tunaona maajabu na miujiza kupitia Kituo cha Julius Nyerere. Jinsi kilivyojengwa ni kitu cha thamani kubwa sana katika nchi yetu ya Tanzania,” alisema Mhe. Mpembe.
Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mpanda, Joseph Lwamba, alisema maendeleo ya sekta ya umeme yameendelea kubadilisha maisha ya wananchi kwa kuongeza fursa za kiuchumi na kijamii katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Katavi.
“Namshukuru Mwenyezi Mungu kwamba katika wilaya yetu ya Mpanda karibu vijiji vyote sasa vina umeme. Wananchi wanaweza kufanya shughuli zao za maendeleo kupitia umeme huu,” alisema Lwamba.
Akielezea lengo la ziara hiyo, Mhandisi wa Usafirishaji Umeme Mkoa wa Katavi, Victor Ngw’igulu, alisema viongozi hao wameletwa katika kituo hicho ili kujionea kwa macho maendeleo makubwa yanayofanywa na Serikali kupitia sekta ya nishati na kuwa mabalozi wa kueleza wananchi mafanikio hayo.
“Wananchi wanapaswa kujua nini kinafanywa na TANESCO kupitia Wizara ya Nishati na hii ni sehemu nzuri ya kuona maendeleo yanayofanywa katika nchi yao. Kupitia Mkoa wa Katavi tumewaleta waheshimiwa hawa ili wajionee kwa macho kile walichokuwa wanakisikia kuhusu Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere, namna kinavyofanya kazi na kuchangia katika uchumi wa taifa,” alisema Ngw’igulu.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere, Mhandisi Elinainyi Kalalu, alisema ujio wa viongozi hao una mchango mkubwa katika kuendelea kuhamasisha uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kituo hicho na nafasi yake katika maendeleo ya taifa.
“Tumewapitisha katika maeneo mbalimbali na kuwaonyesha miundombinu inayotumika katika uzalishaji wa umeme. Tuna imani kwamba wataichukulia ziara hii kama chachu ya maendeleo na watakuwa wajumbe wazuri huko waendako, hasa katika kuelezea mchango wa Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere katika maendeleo ya taifa,” alisema Kalalu.
Ziara hiyo imewapa madiwani wa Mpanda na Nsimbo pamoja na viongozi wengine kutoka Mkoa wa Katavi fursa ya kujionea kwa karibu uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika sekta ya nishati kupitia Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere. Aidha, viongozi hao wameeleza kuridhishwa na hatua zilizofikiwa na kuahidi kuendelea kuhamasisha wananchi kutambua mchango wa kituo hicho katika kuimarisha upatikanaji wa umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.

MWENGE WA UHURU KUPITIA MIRADI YA SH.BILIONI 1.5 MUHEZA
habariNa Oscar Assenga, Muheza
MWENGE wa Uhuru 2026 unatarajiwa kuingia Wilaya ya Muheza kesho saa 4:00 asubuhi na kukimbizwa kupitia miradi saba ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 1.5, huku viongozi wa wilaya wakitoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo.
Mwenge huo utapokewa katika eneo la Kilapura, Kijiji cha Muungano, Kata ya Mlingano na utapitia miradi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi inayolenga kuboresha maisha ya wananchi wa wilaya hiyo.
Akizungumza kuhusu maandalizi ya ujio wa Mwenge huo, Mkuu wa wilaya ya Muheza Ayoub Sebabili alisema kati ya miradi saba itakayopitiwa, miwili itazinduliwa rasmi, miwili itawekewa mawe ya msingi na mitatu itatembelewa na kukaguliwa.
Alisema mradi wa kwanza ni Zahanati ya Muungano, ikifuatiwa na mradi wa maji wa Kijiji cha Magoda unaolenga kuongeza upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi.
Pia Mwenge wa Uhuru utazindua mabweni ya Shule ya Sekondari Mangenya pamoja na kuweka jiwe la msingi katika darasa jipya linalojengwa kwa ajili ya maandalizi ya kupokea wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka 2027.
Mbali na miradi hiyo, viongozi wa mbio za Mwenge watatembelea Klabu ya Wapinga Rushwa ya wanafunzi ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha maadili mema na mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa katika jamii.
Katika kuunga mkono juhudi za serikali za matumizi ya nishati safi, Mwenge wa Uhuru pia utashuhudia utoaji wa mitungi ya gesi kwa wananchi ili kuhamasisha matumizi ya nishati mbadala na kulinda mazingira.
Ratiba hiyo itahusisha pia uzinduzi wa boksi kalavati katika Kijiji cha Tongwe, Kata ya Tongwe, kabla ya kutembelea kikundi cha vijana wa Kijiji cha Magila, Kata ya Genge, waliopata mkopo wa asilimia 10 kutoka mapato ya halmashauri kwa ajili ya shughuli za maendeleo.
Aidha, Mwenge huo utafungua rasmi Hoteli ya Harvest Inn, mradi wa uwekezaji wa mwananchi wenye thamani ya Sh milioni 950, unaotarajiwa kuongeza fursa za ajira na kuchochea ukuaji wa sekta ya utalii na huduma wilayani Muheza.
Baada ya shughuli za miradi kukamilika, mbio za Mwenge wa Uhuru zitahitimishwa katika viwanja vya Mkesha Jitegemee, ambapo kutafanyika maonesho mbalimbali ya utalii, biashara za wajasiriamali, burudani kutoka kwa wasanii wa ndani na nje ya wilaya pamoja na maonesho ya vipaji vya vijana.
Vilevile, wananchi watapata fursa ya kupatiwa elimu kuhusu mapambano dhidi ya rushwa, matumizi ya dawa za kulevya, maambukizi ya UKIMWI, malaria na masuala mengine ya kijamii yanayogusa maendeleo ya taifa.
Wananchi wa Muheza wametakiwa kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio hizo za Mwenge wa Uhuru, zinazobeba kaulimbiu ya kuhamasisha uzalendo, uwajibikaji na maendeleo ya wananchi.
LINDI,MTWARA,KAGERA NA RUKWA KUPATA UMEME WA GRIDI NDANI YA MWAKA WA FEDHA 2026/2027
NishatiSerikali imesema katika mwaka wa fedha 2026/2027 itatekeleza miradi mbalimbali ya umeme ikiwemo kuunganisha mikoa ya Lindi, Mtwara, Kagera na Rukwa kwenye gridi ya taifa ya umeme ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma hiyo nchini.
Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 bungeni jijini Dodoma Juni 22, 2026, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema umeme si anasa tena bali ni hitaji la msingi kwa maisha ya wananchi jambo linaloiifanya Serikali kuendelea kuwekeza fedha nyingi katika sekta hiyo.
Amesema Serikali imeendelea kuimarisha miundombinu ya uzalishaji, usafirishaji na usambazaji wa umeme nchini ili kuhakikisha nishati hiyo inawafikia wananchi katika maeneo mbalimbali.
Waziri Ndejembi ameeleza kuwa umeme unaozalishwa katika Bwawa la Julius Nyerere unasafirishwa kupitia Chalinze kuelekea Morogoro na Dodoma, huku pia ukiunganishwa kwenye njia ya usafirishaji umeme ya Zuzu ili uweze kufika mikoa ya Singida, Tabora, Shinyanga, Simiyu, Geita na Mwanza.
Ameongeza kuwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 Serikali itahakikisha mkandarasi anayetekeleza mradi wa njia ya umeme ya Songea–Tunduru–Masasi–Mahumbika anatekeleza kazi kwa wakati huku Serikali ikiendelea kutoa malipo yatakayomwezesha mkandarasi huyo kufanya kazi bila kukwama na hivyo kuwezesha mikoa ya Lindi na Mtwara kupata umeme kutoka gridi ya taifa.
Aidha, amesema Serikali inaendelea kukamilisha miradi ya njia za kusafirisha umeme kutoka Iringa kwenda Mbeya, Songwe na Rukwa pamoja na mradi wa Benako–Kyaka ambao unalenga kuimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo husika.
Kwa upande wa usambazaji wa umeme vijijini, Mhe.Ndejembi amesema Serikali imepanga kupeleka umeme katika vitongoji 9,009 huku idadi ya vitongoji vitakavyofikiwa na huduma hiyo ikiendelea kuongezeka katika miaka inayofuata.
Amesema lengo la Serikali ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote nchini vinafikiwa na huduma ya umeme, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kwa wananchi.
“Ni kazi kubwa ambayo inakwenda kufanywa, lakini Serikali imejipanga kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata huduma ya umeme wa uhakika." Amesisitiza Waziri Ndejembi
MAFANIKIO YA USAMBAZAJI UMEME -MHANDISi MRAMBA AIPONGEZA REA NA TANESCO
📌*Wakandarasi wa umeme wakaribishwa Zambia kutekeleza miradi*
Dar es Salaam
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba, amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika upatikanaji wa huduma ya umeme, kutoka hatua ya kusambaza umeme kwenye mikoa hadi kufikia ngazi ya vitongoji, ambapo amewapongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa mchango wao katika mafanikio hayo.
Mhandisi Mramba ametoa pongezi hizo leo Juni 22, 2026, jijini Dar es Salaam wakati wa hafla ya utoaji wa tuzo na vyeti kwa wasimamizi wa miradi kutoka REA na wakandarasi waliotekeleza miradi ya umeme vijijini na vitongojini na kuikamilisha kwa wakati.
Amesema hadi sasa asilimia 62 ya vitongoji nchini vimefikiwa na huduma ya umeme, huku Serikali ikilenga kuhakikisha vitongoji vyote vinaunganishwa na umeme ifikapo mwaka 2030 kupitia mpango wa kuunganisha wateja wa mwisho (Last Mile Household Electrification).
Katika hafla hiyo, Mhandisi Mramba amewataka wakandarasi wote wanaotekeleza miradi ya umeme nchini kuhakikisha wanazingatia muda, ubora na gharama, akisisitiza kuwa Wizara itaendelea kufuatilia kwa karibu utendaji wao.
Amesema Serikali haitaacha kujadiliana na wakandarasi pale changamoto zinapotokea lakini kwa watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo hawatapewa fursa ya kushiriki miradi mingine ya Serikali.
Katika kikao hicho, Mhandisi Mramba pia alimkaribisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati ya Zambia anayeshughulikia masuala ya umeme, Mhandisi Arnold Simwaba ambaye yupo nchini pamoja na ujumbe wake kwa ziara ya kikazi katika miradi ya umeme.
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Nishati nchini Zambia amesema wakandarasi walioonyesha uwezo mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya umeme nchini Tanzania wanakaribishwa pia kushiriki katika utekelezaji wa miradi ya umeme nchini Zambia.
Kwa upande wake, mwakilishi wa wakandarasi ambaye kampuni yake ya Derm Electric imefanya vizuri katika miradi ya umeme vijijini na vitongojini, Ridhuani Mringo amesema wakandarasi wazawa wanapaswa kuendelea kutekeleza miradi kwa uadilifu, weledi na uaminifu ili kuendelea kujenga imani ya Serikali na kuongeza nafasi ya kampuni za ndani kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa na ya kimkakati.
BARRICK NORTH MARA YAADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE KATIKA MADINI KWA KUTOA MSAADA GEREZA LA TARIME NA KWENYE JAMII
habariABBASI AONGOZA KIKAO CHA PILI CHA BODI YA USIMAMIZI WA MRADI WA FORLAND
habariMWENYEKITI MPYA WA BODI YA USHAURI ADEM DKT. DACHI AONGOZA KIKAO CHAKE CHA KWANZA,
habari
RAIS DKT. SAMIA AMUAGA RAIS WA NAMIBIA DKT. NETUMBO NDAITWAH
habari
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Namibia Mhe. Dkt, Netumbo Nandi-Ndaitwah katika viwanja vya Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 22 Juni, 2026. Rais Mhe. Dkt. Ndaitwah amehitimisha Ziara yake ya Kitaifa ya siku 4 nchini Tanzania ambapo pamoja na kufanya mazungumzo na Rais Mhe. Dkt. Samia pia alitembelea Kambi ya Kihistoria ya Wapigania Uhuru wa nchi yake, Kongwa mkoani Dodoma.

WATALAAM WA REA ZAMBIA KUJIFUNZA MAFANIKIO YA TANZANIA KATIKA USAMBAZAJI UMEME VIJIJINI
NishatiViongozi wa Mamlaka ya Nishati Vijijini (REA) kutoka nchini Zambia wamewasili nchini kwa ajili ya ziara ya kujifunza na kubadilishana ujuzi na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).
REA Zambia ambao wameongozwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Zambia anayeshughulikia Umeme, Mhandisi Arnold Simwaba wamewasili leo Juni 21, 2026 katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere na kupokelewa na Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati Tanzania, Wilson Nyamanga pamoja na Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kiutoka REA Tanzania, Mhandisi Jones Olotu, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa REA Tanzania, Renatus Msangira.
Uongozi wa REA Zambia utakuwa nchini kwa ziara ya kikazi ya Siku 7 ambapo pamoja na vikao vya kubadilishana ujuzi, wajumbe hao wanatarajiwa kutembelea miradi mbalimbali ya umeme vijijini inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini.























