📍Yapokea cheti cha pongezi kwa mchango wake katika kuendeleza elimu jumuishi
📍Utambuzi watolewa katika hafla maalum ya kuwapongeza wadau wa maendeleo wa UDSM
Na Mwandishi Wetu
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limetambuliwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kama miongoni mwa sekta wezeshi zinazochangia maendeleo ya elimu jumuishi na ustawi wa wanafunzi chuoni hapo.
Utambuzi huo umetolewa Mei 26, 2026, wakati wa hafla maalum ya kuwatambua na kuwapongeza wadau wa maendeleo wa chuo hicho iliyofanyika katika Ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe.Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, amesema mchango wa wadau mbalimbali wakiwemo TANESCO una mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na maendeleo ya kitaaluma kwa wanafunzi.
“Tunapowasaidia wanafunzi hawa, hatuwafanyii fadhila. Tunathibitisha uwezo wao, utu wao na nafasi yao halali katika elimu ya juu,” amesema Dkt. Kikwete.
Aidha, ameshukuru wadau wote wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na chuo hicho katika kuhakikisha upatikanaji wa elimu jumuishi kwa wanafunzi wote, wakiwemo wenye mahitaji maalum.
Kwa upande wa TANESCO, cheti hicho cha utambuzi na pongezi kilipokelewa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja, Irene Gowelle, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji Lazaro Twange.
Utambuzi huo umetolewa ikiwa ni ishara ya kuthamini mchango wa TANESCO katika kuboresha mazingira ya kujifunzia na kujisomea kwa wanafunzi pamoja na wakufunzi wenye changamoto mbalimbali za ulemavu na mahitaji maalumu chuoni hapo.
Hafla hiyo ilibebwa na kaulimbiu isemayo “Kujenga Mazingira Jumuishi ya Kujifunzia kupitia Ushirikiano wa Kimkakati”, ikiwa na lengo la kuhamasisha ushirikiano kati ya taasisi, wadau wa maendeleo na jamii katika kuendeleza elimu jumuishi nchini.
Katika hafla hiyo pia, Dkt. Kikwete alizindua rasmi mbio za “UDSM Marathon 2026” zitakazofanyika Desemba 5, 2026, zikiwa na lengo la kukusanya rasilimali kwa ajili ya kusaidia elimu jumuishi, ustawi wa wanafunzi na programu za kuwasaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum.























.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)


.jpeg)










.jpeg)


.jpeg)




