HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

JAFO KUJA NA HOJA BINAFSI KUPENDEKEZA MPANGO MAALUM WA AJIRA ZA MUDA MFUPI KWA VIJANA

JAFO KUJA NA HOJA BINAFSI KUPENDEKEZA MPANGO MAALUM WA AJIRA ZA MUDA MFUPI KWA VIJANA

April 09, 2026 Add Comment

Mbunge wa Jimbo la Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo,akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27  leo Aprili 9,2026 bungeni jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

Mbunge wa Kisarawe, Dkt. Selemani Jafo, amedhamiria kuwasilisha hoja binafsi bungeni itakayolenga kuishauri Serikali kuanzisha mpango maalum wa mikataba ya ajira za muda mfupi kwa vijana ili kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira nchini.

Akichangia makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zake kwa mwaka wa fedha 2026/27 bungeni, Jafo alisema mpango huo unaweza kuwa na mfumo wa Ajira za muda (part time employment) utakaodumu kwa kipindi cha miaka mitatu mitatu hadi ifikapo mwaka 2050  ambapo vijana watapata ajira za mikataba na kujipatia uzoefu wa kazi.

Alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi kubwa za kuongeza fursa za ajira kwa vijana tangu aingie madarakani, akisema serikali imefanya kazi kubwa katika kuwawezesha wananchi, lakini bado kuna haja ya kuja na mikakati mipya ya kukabiliana na wimbi la vijana wasio na ajira.

Jafo alibainisha kuwa changamoto ya ajira bado ni kubwa, huku akitoa mfano wa vijana wengi waliopo kwenye shughuli zisizo rasmi kama bodaboda, baadhi yao wakiwa na elimu ya juu ikiwemo stashahada,  shahada na kuendelea. Alipendekeza mpango maalum utakaolenga wahitimu hao ili kuwapa nafasi ya kupata ajira za muda na mikataba ya miaka mitatu.

Kwa mujibu wa mapendekezo yake, kila mwaka vijana 50,000 wanaweza kuingizwa kwenye mpango huo, ambapo asilimia 20 wawe wahitimu wa stashahada na asilimia 80 wawe wahitimu wa shahada na kuendelea. Aidha, alipendekeza malipo ya kujikimu ya Shilingi 500,000 kwa wenye stashahada na Shilingi 700,000 kwa wahitimu wa shahada.

Alisema gharama ya utekelezaji wa mpango huo inakadiriwa kufikia Shilingi bilioni 396, huku akisisitiza kuwa mpango huo utasaidia kukuza ujuzi wa vijana, kuongeza uzoefu wa kazi na kupunguza tatizo la ajira nchini.

Pia alipendekeza asilimia 10 zitoke katika mapato ya ndani ya kila Halmashauri, 10 ya gawio la Serikali kutoka kwenye mashirika ya umma, na fedha zingine zitokane na kubana maeneo mengine ya matumizi ya kawaida ya serikali(Recurrent Expenditure) ili zitumike kufadhili mpango huo. Aidha, alishauri mpango huo usimamie kupitia serikali za mitaa na Taasisi za Umma ili kurahisisha upatikanaji wa ajira katika halmashauri mbalimbali na Taasisi hizo za Umma.

Jafo alisisitiza kuwa mpango huo, kama utapitishwa, utaisaidia Serikali kuongeza wigo wa ajira na kuwawezesha vijana wengi zaidi kunufaika na fursa za kiuchumi nchini.

NGORONGORO NI NYUMBANI KWA KILA BINADAMU - KAMISHNA BADRU.

April 09, 2026 Add Comment

 Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Bw. Abdul-Razaq Badru leo tarehe 9 Aprili, 2026 amepuliza rasmi Kipenga cha shindano la mwezi mmoja la Safari Field Challenge akisisitiza kwamba Ngorongoro ni nyumbani kwa kila binadamu kutokana na chimbuko la historia linalobainishwa kisayansi.


Akizindua shindano hilo Kamishna Badru amewashukuru washiriki nane (8) wa shindano hilo kwa kuitika wito wa Ngorongoro na kuwaeleza kuwa Hifadhi ya Ngorongoro ni zaidi ya Kreta hasa kutokana na kuwa na utamaduni, asili, chimbuko la binadamu wa kale, siri ya Binadamu na maisha yake, Nyayo za Laetoli zenye umri za zaidi ya miaka milioni 3.6, mchanga unaohama, kushuhudia pumzi ya kwanza ya Nyumbu eneo la Ndutu, kuona Wanyama wakubwa watano katika eneo moja, mlima Lolmalasian ambao wa tatu kwa urefu Tanzania, misitu, mimea na ndege mbalimbali.

“Karibuni Ngorongoro ambapo ni nyumbani kwa sisi sote, mtapata uzoefu ya maajabu mbalimbali, kuyahisi, kuyaishi, kufurahia, kuyahadithia na kuwasaidia kupata ujuzi ambao utawafanya muwe mabalozi wazuri kuwaelezea watu wengine mkusanyiko wa maajabu yaliyoko Ngorongoro” Alisema Kamishna Badu.

Kamishna Badru amewapa changamoto washiriki wa shindano hilo kuwa watundu wa kuifahamu Ngorongoro, kuisemea Ngorongoro kwa mtazamo mpya wa sauti moja ambapo kwa kushirikiana na Azam Media hadithi, historia, maajabu ya Ngorongoro itasimuliwa na kufika pembe nne za dunia kuwa Ngorongoro sio kivutio cha utalii pakee bali ni Nyumbani kwa kila Binadamu ambapo historia yao ilianza.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi anayesimamia Huduma za Utalii na masoko Mariam Chuma Kobelo amewaeleza washiriki wa Safari Field Challenge kuwa Tanzania ina vitu vingi vya Kujivunia,lakini Ngorongoro kuna vingi zaidi na kuwasisitiza washiriki wa shindano hilo kwenda kujifunza, kuifahamu na kuisimulia Ngorongoro kuwa ni zaidi ya Kasoko ya Ngorongoro.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tanzania Tour Guide Fondation (TTGF) Mosses Njole ameleza kuwa washiriki wote 8 wako timamu na wamejiandaa kikamilifu kushiriki shindano hilo na kuwapongeza Ngorongoro kwa kuwa wadhamini wakuu na wadau wengine wakiwepo Azam Media ambayo imekuwa sehemu ya kusimulia maajabu ya Ngorongoro.







SERIKALI YAZINDUA KUKOSI KAZI CHA TAIFA CHA UFUATILIAJI,TATHMINI NA UTOAJI TAARIFA

April 09, 2026 Add Comment


Na  OWM-SBUU -Morogoro


Serikali imezindua Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kwa lengo kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa Ufuatiliaji na Tathmini katika kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali.


Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 09 Aprili, 2026 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. James Kilabuko  wakati akifungua Kikao Kazi Cha Kikosi Kazi cha Taifa cha Ufuatiliaji, Tathmini na Utoaji Taarifa (ME&R National Task Force) kilichofanyika mkoani Morogoro.

Dkt. Kilabuko amesema, Ufuatiliaji na Tathmini ni dhana muhimu ya usimamizi inayotumika kwa lengo la kuhakikisha uwajibikaji na uwazi katika utekelezaji wa afua za maendeleo.

“Kikosi Kazi hiki kitakuwa chombo cha kitaalamu cha kusaidia kuratibu utekelezaji wa Mwongozo Jumuishi wa U&Tc, kuoanisha mifumo ya kitaifa ya utendaji, kuimarisha ubora wa takwimu na taarifa za Serikali na  kuandaa mapendekezo ya sera na maboresho ya kiutendaji” alisema Naibu Katibu Mkuu huyo.

Ameeleza kuwa, kikao kazi hicho ni fursa ya kipekee ya kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuweka mikakati ya pamoja ya namna bora ya kutekeleza majukumu ya  Ufuatiliaji na Tathmini nchini.

“Matarajio yangu ni kwamba, baada ya kikao hiki tutaboresha uratibu na kuoanisha viwango vya kitaifa vya Ufuatiliaji na Tathmini (M&E) katika Wizara, Idara na Wakala (MDAs), Sekretarieti za Mikoa (RSs) na Mamlaka za Serikali za Mitaa (LGAs) ni hatua muhimu katika kuhakikisha uwiano na ufanisi wa utekelezaji wa shughuli za maendeleo” amefafanua.

 


Vilevile, Dkt. Kilabuko amebainisha kuwa ipo haja ya  kuoanisha viashiria vya taasisi na maeneo muhimu ya matokeo ya Kitaifa ili kuhakikisha kuwa juhudi za taasisi mbalimbali zinaendana na vipaumbele vya Taifa.

 


“ Katika hili, ni muhimu kuimarisha mwingiliano na utangamano wa Mfumo wa Kupima Utendaji Kazi wa Watumishi wa Umma na Taasisi (PEPMIS), PIPMIS na Mfumo wa Kitaifa wa Usimamizi wa Miradi ya Maendeleo na Programu (NPMIS) ili kuwezesha mtiririko mzuri wa taarifa na matumizi ya data kwa ufanisi” ameeleza.

 



Aidha, amebainisha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inataka kuona taarifa za U&T zikitumika kufanya maamuzi,  miradi inakamilika kwa wakati na kwa thamani halisi ya fedha na maisha ya wananchi yanaboreshwa kutokana na kazi zinazotekelezwa.

 


“Haya yote yatawezekana ikiwa tutazingatia misingi ya Ufuatiliaji na Tathmini kama inavyoelekezwa katika Mwongozo Jumuishi. Tumieni muda huu vizuri kujadili masuala yatakayokuwa na maslahi mapana kwa nchi yetu na kuwa na Ufuatiliaji na Tathmini wenye tija” ameongeza Dkt. Kilabuko.



*MWISHO*

CCM YATAKA MAENEO YA KUKUSANYIA TAKA SOKO LA MGANDINI YABORESHWE

April 09, 2026 Add Comment

 


Na Oscar Assenga, TANGA

Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga kimetoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.

Agizo hilo lilitolewa na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Tanga Rajab Abdurhaman wakati wa ziara yake ambapo alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu.

Ziara hiyo ilikuwa ni kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo ambapo viongozi wa Jiji hilo walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo hayo ya CCM.

“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.

Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.

Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.

“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.

Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.

Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.

Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.

Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.

Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.

Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.

Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.

Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.

Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.

Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.

Kwa upande wake, Naibu Meya Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Mwisho.

WATENDAJI OFISI YA WAZIRI MKUU WAKUMBUSHWA KUIMARISHA WELEDI KUTIMIZA DIRA YA TAIFA 2050

April 08, 2026 Add Comment




Na. MWANDISHI WETU -DODOMA



Watendaji wa Ofisi ya Waziri Mkuu wamekumbushwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, ufanisi na kujituma ili kuhakikisha wanachangia kikamilifu katika kufanikisha malengo ya Dira ya Taifa 2050, hususan katika maeneo ya sera, uratibu na usimamizi wa utekelezaji wake.


Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Mhe. Prof. Palamagamba J.A. Kabudi, wakati akizungumza na watumishi wa Ofisi hiyo mara baada ya kuwasili rasmi na kupokelewa na uongozi na watumjshi wa Ofisi hiyo katika Jengo la Ngome Jijini Dodoma tarehe 8 Machi, 2026

Prof. Kabudi alisisitiza umuhimu wa ushirikiano na ubunifu miongoni mwa watumishi ili kuongeza ufanisi wa utendaji kazi.

“Ni muhimu tushirikishane mawazo na kufanya kazi kwa pamoja ili kumsaidia Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufanikisha adhima ya maendeleo yenye kuleta ustawi na furaha kwa Watanzania," alisema Prof. Kabudi


Aliongezea kuwa upo umuhimu wa kushikamana ili kuendelea kuimarisha utendaji wetu ili kumwezesha Mheshimiwa Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi zaidi.


Aidha, Waziri Kabudi alibainisha kuwa mazingira ya kazi yenye mshikamano na mahusiano ya kifamilia hayapaswi kuwa chanzo cha uzembe au utovu wa nidhamu, bali yawe kichocheo cha kuongeza uwajibikaji na kufikia viwango vya juu vya utendaji.

Katika hatua nyingine, Waziri Kabudi aliwataka watumishi kuendelea kumuombea aliyekuwa Waziri wa Nchi katika Ofisi hiyo, Marehemu William Vangimembe Lukuvi, ili Mwenyezi Mungu amrehemu na kumpa pumziko la milele.

“Nitaendeleza, kadri nitakavyoweza, misingi na jitihada zilizoanzishwa na mtangulizi wangu katika kuijenga Ofisi hii,” aliongeza.

Awali, Naibu Waziri wa Ofisi hiyo, Mhe. Ummy Nderiananga, alimpongeza Prof. Kabudi kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kushika nafasi hiyo, akiahidi ushirikiano wa dhati kutoka kwa watumishi wote katika utekelezaji wa majukumu yake.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu), Dkt. Jim Yonazi, naye alimpongeza Waziri Kabudi kwa uteuzi huo na kusisitiza kuwa watumishi wako tayari kuongozwa na kushirikiana naye katika kuendelea kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.



=MWISHO=

RC DKT BATILDA BUNGENI DODOMA

April 08, 2026 Add Comment


 Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Batilda Burian Leo Aprili 8.2026 akiwa bungeni na Baadhi ya Wakuu wa Mikoa wamewasili Bungeni Jijini Dodoma, kwa ajili ya kufuatilia na kusikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge wakiwa wanachangia bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na ofisi ya Bunge ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na ofisi ya Bunge ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2026/2027 iliwasilishwa Bungeni siku ya Tarehe 1.4.2026 siku ya Jumanne ili Wabunge wapate nafasi ya kuchangia.

SAME UTALII FESTIVAL YAWAINUA WANANCHI KIUCHUMI

April 08, 2026 Add Comment



Wananchi wa wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro wamewaomba viongozi kuhakikisha tamasha la utalii la Same Utalii Festival linafanyika kila mwaka kutokana na mchango wake mkubwa katika kukuza uchumi wa jamii.

Wito huo umetolewa leo na kina mama lishe wakati wa joggin ya kuhamasisha tamasha hilo linalotarajiwa kufanyika Aprili 10 hadi 12 mwaka huu, likiwa ni msimu wa tatu tangu kuanzishwa kwake.

Akizungumza katika joggin hiyo, Anna Mzava, ambaye ni mama lishe katika stendi ya mabasi wilayani Same, alisema tamasha hilo limekuwa msaada mkubwa kwao kiuchumi.

Alisema mbali na kuhamasisha utalii, tamasha hilo limeongeza kipato kwa wafanyabiashara wadogo kutokana na ongezeko la watu wanaohudhuria.

“Tunaomba tamasha hili liwe endelevu kwani sisi wananchi wa chini tunafaidika nalo. Biashara zetu zinaenda vizuri na tunapata fedha zaidi. Kwa mfano, badala ya kupika mchele kilo tatu, wakati wa tamasha napika hadi kilo 10 na zote zinaisha,” alisema Mzava.

Kwa upande wake, Jumanne Idd alisema tamasha hilo limekuwa chachu ya kutangaza utalii wa wilaya ya Same pamoja na vyakula vya asili vya kabila la Wapare.

Aliongeza kuwa tukio hilo limechangia kuitangaza wilaya hiyo kitaifa na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi wakati wa msimu wa tamasha.

Akizungumza katika joggin hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Same, Yusto Mapande, alisema wamejipanga kuhakikisha tamasha hilo linakuwa endelevu ili kuendelea kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo wilayani humo.

Alisema halmashauri itaendelea kubuni na kuibua vivutio vipya ili kuongeza fursa za kiuchumi kwa wananchi.

“Faida kubwa tunazotarajia ni za kiuchumi.Panapokusanyika watu wengi ni fursa, kwani wanahitaji huduma mbalimbali na hivyo kuongeza kipato kwa wananchi,” alisema Mapande.

RAIS MHE. DKT. SAMIA SULUHU HASSAN AWAAPISHA VIONGOZI MBALIMBALI IKULU YA CHAMWINO MKOANI DODOMA

April 08, 2026 Add Comment

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Profesa Palamagamba John Aidan Kabudi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Profesa Palamagamba John Aidan Kabudi kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Festo John Dugange kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Kwagilwa Reuben Nhamanilo kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Kwagilwa Reuben Nhamanilo kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akimuapisha Mhe. Gerson John Mdemu kuwa Kamishna wa Tume ya Utumishi wa Mahakama kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026.
Viongozi wateule wakiapa Kiapo cha Maadili kwenye hafla iliyofanyika Ikulu ya Chamwino mkoani Dodoma tarehe 08 Aprili, 2026

KASULU YAZIDI KUNUFAIKA NA MALIASILI NA UTALII

April 08, 2026 Add Comment


Na Sixmund Begashe, Dodoma
Wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wameendelea kunufaika na uwepo wa mwekezaji katika kitalu cha Makere Forest Reserve kwa kupata mgao wa fedha za maendeleo ya jamii zaidi ya Shilingi Milioni 12 kila mwaka kinacholipwa na mwekezaji kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya vijiji.

Hayo yamesemwa Bungeni Jijini Dodoma na Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji, alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Edibil Kazala Kinyoma alipotaka kujua "Je, ni kwa kiasi gani wananchi wa Jimbo la Kasulu Vijijini wananufaika na uwepo wa Mwekezaji wa kitalu cha Makere Forest Reserve".

Dkt. Kijaji amesema kuwa kwa kuzingatia vipaumbele vya vijiji husika katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 Vijiji vya Kagera Nkanda, Chekenya na Kabulanzwili vililipwa Shilingi 4,356,435.67 kila kimoja.

"Vilevile, mgao wa fedha zinazotokana na asilimia 25 ya ada ya wanyamapori wanaowindwa katika kitalu husika kwa mujibu wa Kifungu cha 137 cha Sheria ya Fedha ya Mwaka 2025 zinalipwa na Serikali kwa Halmashauri husika". Alifafanua Dkt. Kijaji

Ameongeza kuwa asilimia 60 ya fedha hizo hutumika kutekeleza miradi ya maendeleo na asilimia 40 shughuli za uhifadhi katika vijiji vinavyozunguka kitalu husika.

"Sambamba na manufaa yaliyotajwa, katika kipindi cha mwaka 2024/25 na 2025/26 mwekezaji kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) wamechangia miradi ya jamii yenye thamani ya shilingi 166,475,000". Aliongeza Dkt. Kijaji

Aidha, Dkt. Kijaji amesema kuwa fedha hizo zimetumika kufadhili kambi ya huduma ya matibabu ya macho katika Halmashauri ya Kasulu, madawati 100 katika Shule za Msingi Chekenya (25), Nyakasanda (25) na Nyantuku (50) na uchimbaji wa visima vya maji sita (6) katika Shule za Msingi Kamganza, Kasasa, Mwitiri, Chekenya na Nyantuki pamoja na Kituo cha Afya cha Kagerankanda.