HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

TUCTA-MWRC KUWAPA MWONGOZO WAFANYAKAZI WANAOTAFUTA AJIRA NJE YA NCHI

June 11, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) kwa kushirikiana na Shirika la Kazi la Umoja wa Mataifa (ILO) limezindua Kituo cha Msaada kwa Wafanyakazi Wahamiaji Tanzania (TUCTA-MWRC) kwa lengo la kuwapatia taarifa, ushauri na msaada wafanyakazi wanaotafuta ajira ndani na nje ya nchi.

WAZIRI PROF,MKUMBO ATAJA MAENEO MATANO YA KIPAUMBELE MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA WA MWAKA 2026/27

June 11, 2026 Add Comment

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Mipango na Uwekezaji, Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amewasilisha Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2026/27 akisisitiza vipaumbele vitano vya utekelezaji wake.

Akitaja vipaumbele hivyo, amesema mosi ni kuimarisha utawala bora, demokrasia, amani, na utulivu na pili ni kujenga uchumi imara, jumuishi na shindani na kipaumbele cha tatu ni, kuimarisha uwezo wa watu na maendeleo ya jamii.

Akiendelea kufafanua vipambele hivyo, Mhe. Waziri amesema kipaumbele cha nne ni kuimarisha uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu kwa mabadiliko ya tabianchi na cha tano kikiwa kusimamia utekelezaji wa vichocheo vya mageuzi ambavyo ni pamoja na nishati, miundombinu ya usafiri na usafirishaji, utafiti na maendeleo, na mageuzi ya kidigitali.

Prof Kitila amesesema utekelezaji wa vipaumbele hivyo ni hatua za kuyatekeleza malengo makuu ya Dira 2050, na vimezingatia Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2026/27 – 2030/31 wenye dhima ya “Mageuzi kwa ajili ya Ukuaji Jumuishi wa Uchumi na Uzalishaji Ajira” ambao ni wa kwanza katika utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu 2026/27 – 2050/51.

Aidha katika kutekeleza maeneo ya vipaumbele hivyo, Serikali imepanga kuanza kutekeleza programu na miradi mbalimbali ikiwemo miradi shikizi 38 kati ya 51 iliyopo katika programu saba (7) za kielelezo zilizoainishwa katika Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano.





BALOZI MATINYI AKABIDHI HATI KWA RAIS WA ALGERIA

June 11, 2026 Add Comment

 

Mheshimiwa Balozi Mobhare Matinyi akisalimiana na Mheshimiwa Abdelmadjid Tebboune, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria, mara baada ya kukabidhi hati za utambulisho wa kibalozi katika hafla iliyofanyika kwenye Ikulu ya Algiers tarehe 10 Juni, 2026. Katikati ni Mheshimiwa Ahmed Attaf, Waziri wa Mambo wa Nje wa Algeria.

MAGAVANA WA BENKI KUU SADC WAKUTANA DAR KUJADILI HATARI ZA KIUCHUMI KIKANDA

June 11, 2026 Add Comment
MAGAVANA wa Benki Kuu za nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana jijini Dar es Salaam kujadili mikakati ya kukabiliana na changamoto za kiuchumi zinazoendelea kujitokeza duniani, huku migogoro ya kimataifa na mfumuko wa bei vikitajwa kuwa miongoni mwa vihatarishi vikubwa vya ukuaji wa uchumi wa ukanda huo.

RAIS MSTAAFU DKT JAKAYA KIKWETE ATETA NA MSHAURI MWANDAMIZI WA RAIS DONALD TRUMP KATIKA MKUTANO WA OSLO FORUM NORWAY

June 11, 2026 Add Comment

 

Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Massad Boulos, mwanadiplomasia na Mshauri Mwandamizi wa Rais Donald Trump kuhusu masuala ya Afrika, nchi za Kiarabu na Mashariki ya Kati, baada ya kufanya mazungumzo pembezoni mwa Mkutano wa Oslo Forum unaofanyika Oslo, Norway.

Mkutano huo, unaofanyika kuanzia tarehe 10 hadi 12 Juni, 2026, umewakutanisha viongozi, wanadiplomasia waandamizi na wadau wa masuala ya amani, diplomasia na usuluhishi kutoka nchi mbalimbali zenye ushawishi duniani.

MKUU WA WILAYA CHATO AMESEMA AFDP NI MKOMBOZI WA UCHUMI WA WANANCHI

June 11, 2026 Add Comment

Na; Mwandishi wetu – Chato


Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Louis Peter Bura Amepongeza Programu ya kuendeeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu kwa Uratibu wa Kituo cha kuendeleza ukuzaji Viumbemaji Rubambagwe Kilichopo wilayani Chato Mkoani Geita kinachosimamiwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Ametoa Pongezi hizo Tarehe 10 Juni 2026 Wilayani Chato alipofanya ziara maalum ya kutembelea kituo hicho akiwa pamoja na timu ya wataalam waliokutana katika Wilaya hiyo wakiwa katika kazi maalum ya kufanya mapitio ya mpangokazi wa Program hiyo.



Mkuu wa Wilaya Bura, alisema kuwa Wilaya yake inawajibu wa kutoa elimu kwa wafugaji kupitia kituo cha Rubambagwe hivyo amewaasa wataalam kutoka katika sekta zinazotekeleza mradi kufanya kazi kwa ushirikianao na Wilaya hiyo, ili kuweza kuleta matokeo chanya katika uchumi wa Wilaya na Taifa kwa Ujumla na Kuongeza mnyororo wa thamani.


“Tutakuwa tunazalisha vifaranga vya samaki pale, haitatosha hiyo pia tutakuwa tunazalisha vyakula vya samaki, na hayo yote yamenipa mimi wakati mzuri na sababu ya kujifunza haya yote, na tunashukuru mradi huu kwenda kwa kasi na ni wakati sasa wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja . “Alibanisha

Sambamba na hilo Mkuu huyo wa Wilaya alisisitiza ushirikishwaji mzuri baina ya sekta zinazotekeleza Programu hiyo nchini pamoja na Wilaya husika.’katika dhana nzima ya ushirikishwaji kuna mambo mengi ambayo Wilaya inaweza kuyasimamia na kuyatekeleza kwa ukaribu zaidi, hapa Chato wananchi wanajihusisha Zaidi na uuzaji wa samaki tuna soko kubwa la samaki hapa linaitwa Chato beach, wananchi wanapata chakula na pia wanauza sehemu nyingine nje ya Chato.’ Alifafanua.


Kwa upande wake Mratibu wa Programu Hiyo kutoka Ofisi ya waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Bw. Salimu Mwinjaka alisema pamoja na mambo Mengine kwa upande wa bahari kuu, Progamu hiyo inakusudia kujenga  viwanda vya samaki Tanzania Zanzibar katika eneo la Fungurefu na Wilayani Kilwa Mkoani Lindi na  kuweza kukabili hali ya upotevu wa mazao ya samaki baada ya kuvuna kwa kujenga vyumba vya ubaridi vya kuhifadhi mazao ya uvuvi, mitambo wa kuzalisha barafu, vichanja na mahema yakukaushia dagaa au samaki kwa kutumia mionzi ya jua. 


Akiongelea kuhusu ufugaji samaki, Bw. Mwinjaka alisema kupitia progamu hiyo kuna vituo vinne ambavyo vipo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambavyo ni Pamoja na vituo vya kuendeleza ukuzaji viumbemaji cha Rubambagwe kilichopo Wilayani Chato, Mwamapuli Wilayani Igunga, Kingolwira Wilayani Morogoro na kituo cha Ruhila Wilayani Songea.



Akiongea katika ziara hiyo, Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi Mkomanile Mahundi alisema kituo cha Kuendeleza Ukuzaji Viumbemaji Rubambagwe kitakuwa na kazi ya kuzalisha na kusambaza vifaranga bora vya samaki aina ya sato na kambale, pamoja na kutoa mafunzo kwa wakuzaji viumbemaji katika maeneo ya mikoa ya Geita, Mwanza, Kagera, Shinyanga, Simiyu na Mara.


Aliongeza kusema pia, baada ya kituo kukamilika kitakuwa na uwezo wa kuchakata chakula cha samaki ambapo itapelekea wigo wa kuongeza ajira kwa wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum.

“Wizara ya Mifugo na uvuvi kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) itawezesha uwepo wa dirisha maalum katika taasisi za kifedha kama vile Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kuwawezesha wakuzaji viumbemaji kupata mkopo yenye riba nafuu ya pembejeo na zana za ukuzaji viumbemaji.” Alisem

Ujenzi wa Kituo hicho cha Rubambagwe umefikia Asilimia 85 mpaka sasa ambapo umehusisha Jengo la utawala, karakana, nyumba za wafanyakazi jengo la kitotoleshi cha samaki, ujenzi wa mabwawa ya kufugia samaki, chanzo cha maji yaani tenki maalum la kutunza maji, kuchuja na kusafirisha maji hayo kwenda kwenye mabwawa ya kufugia samaki, kitotoleshi pamoja na maeneo mengine yanayotumia maji kituoni hapo.


                                   xxxxx MWISHO xxxxxxxxx

DAWASA, JIJI, TARURA WAZIBUA MITARO YA MAJI TAKA INAYOZUNGUKA SOKO LA KARIAKOO.

June 10, 2026 Add Comment
Shirika la Masoko ya Kariakoo kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA), Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) na Halmashauri ya Jiji ya Dar es Salaam wameshirikiana kuzibua mitaro ya maji taka inayozunguka Soko Kuu la Kariakoo.

DKT. MAULID AHAMASISHA VIONGOZI WA SHULE KUTUMIA MAARIFA KUBORESHA UTENDAJI

June 10, 2026 Add Comment
Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt Maulid J. Maulid leo umefungua Mafunzo ya Uongozi wa Kimkakati (Strategic Leadership) kwa viongozi wa shule za sekondari wa Manispaa ya Shinyanga, yakiwakutanisha washiriki 44 wakiwemo Wakuu wa Shule za Sekondari 22 na Makamu Wakuu wa Shule 22. 

WAZIRI MKUU DKT.MWIGULU ATETA NA MBUNGE WA JIMBO LA KILINDI

June 10, 2026 Add Comment

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Mwigulu Nchemba akimsikiliza Mbunge wa jimbo la Kilindi Mhe.Salehe Mbwana Mhando leo Jumatano Juni 10,2026 bungeni jijini Dodoma.



CBE YAINGIZA AKILI MNEMBA (AI) KATIKA MABORESHO YA MITAALA

June 10, 2026 Add Comment
Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kipo katika mchakato wa kupitia na kuhuisha mitaala tisa ya masomo ili iendane na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023), pamoja na mahitaji ya sasa ya soko la ajira nchini.

MAKALA -UCHUMI WA NYUKLIA :UCHAMBUZI WA AKIBA YA URANI YA MKUJU NA MAONO YA RAIS SAMIA YA KINU CHA KWANZA MWAKA 2029

June 10, 2026 Add Comment


Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Urusi

Kwa miaka mingi, mazungumzo kuhusu nishati nchini Tanzania yamekuwa yakitawaliwa na vyanzo vya maji, gesi asilia, na sasa nishati jadidifu kama jua na upepo. 

Hata hivyo, kauli ya hivi karibuni ya Rais Samia Suluhu Hassan akiwa nchini Urusi imethibitisha kuwa Tanzania sasa imedhamiria kuingia kwenye Klabu ya Nyuklia ifikapo mwaka 2029. 

Hili si jambo la kubahatisha bali ni mkakati unaoendeshwa na uwepo wa akiba kubwa ya madini ya urani katika Bonde la Mto Mkuju mkoani Ruvuma, mradi unaosubiriwa kwa hamu kubwa kuwezesha fursa ya maendeleo. Mkakati huu unalenga kuipa nchi vyanzo mbadala na imara vya nishati ili kukabiliana na changamoto za kukatika kwa umeme na kukua kwa kasi kwa sekta ya viwanda.

Historia ya mradi wa urani wa Mkuju River uliopo ndani ya mfumo wa ikolojia wa Selous na Nyerere kusini mwa Tanzania inaonyesha kuwa unatajwa kuwa miongoni mwa hifadhi kubwa zaidi za urani ambazo hazijachimbwa duniani kote.

Mradi huu unamilikiwa na kampuni ya Mantra Tanzania, ambayo ni kampuni tanzu ya Uranium One inayomilikiwa na Shirika la Nishati la Atomiki la Urusi liitwalo Rosatom. 

Ugunduzi wa madini haya ulileta matumaini makubwa tangu miaka ya 2010 ambapo tafiti za kijiolojia zilionyesha kuwa eneo hilo lina hifadhi inayokadiriwa kufikia tani milioni 152 za miamba yenye madini hayo inayoweza kuzalisha mamilioni ya ratili za urani iliyosafishwa kwa kiasi fulani kwa miaka zaidi ya 12 hadi 20 ya uhai wa mgodi huo.

Hata hivyo, mradi huo ulikabiliwa na changamoto mbalimbali zilizosababisha usitishwaji wa muda ikiwemo kuanguka kwa bei ya urani duniani baada ya ajali ya nyuklia ya Fukushima nchini Japani mwaka 2011. 

Mahitaji ya urani duniani yalishuka sana na kupelekea bei kuporomoka hali iliyofanya uchimbaji wa Mkuju kutokuwa na tija ya kibiashara kwa wakati huo. 

Changamoto nyingine ilikuwa ni mazingira na udhibiti kwa kuwa eneo la mradi lilikuwa ndani ya Hifadhi ya Selous ambayo ni eneo la Urithi wa Dunia, jambo lililolazimisha serikali kufanya mabadiliko ya mipaka ili kuruhusu uchimbaji bila kuathiri ikolojia nzima ya eneo hilo.

Baada ya usingizi wa muda mrefu, mradi wa Mkuju sasa unafufuka kwa kasi kubwa kutokana na kupanda upya kwa bei ya urani duniani na msukumo wa kisiasa kutoka kwa serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa sasa, Mantra Tanzania na Uranium One wamekamilisha hatua za majaribio ya teknolojia ya uchenjuaji iitwayo In-Situ Recovery au majaribio ya kinu cha majaribio. 

Teknolojia hii ni ya kisasa na salama zaidi kimazingira kwani haihusishi kuchimba mashimo makubwa bali huingiza vimiminika maalum ardhini vinavyoyeyusha urani na kuivuta juu ikiwa kimiminika.

Mazingira ya sasa yanaonyesha kuwa miundombinu ya msingi ikiwemo barabara za kuingia eneo la mradi, mifumo ya ulinzi wa mionzi, na kambi za wafanyakazi zimeshaimarishwa huku serikali kupitia Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania ikifanya ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha usalama wa mionzi unazingatiwa kabla ya uchimbaji kuanza kikamilifu.

Ukimya wa miaka kadhaa uliacha maswali mengi lakini sasa wananchi na wadau wa kiuchumi wanasubiri kwa shauku kubwa kuanza kwa mgodi huu kwa sababu ya fursa za ajira na uchumi wa ndani. 

Wakazi wa mikoa ya Kusini hasa Ruvuma na Lindi wanatarajia fursa za ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja pamoja na kukuza biashara za ndani kupitia usambazaji wa bidhaa mgodini. 

Mradi huu pia unatajwa kuwa chanzo kipya na kikubwa cha mrabaha na kodi kwa serikali utakaosaidia kufadhili miradi mingine ya kijamii kama afya na elimu huku kukiwa na matumaini ya uhuru wa nishati kwani kauli ya Rais Samia kuwa urani hii itatumiwa kuzalisha umeme nchini inaleta matumaini mapya kuwa Tanzania haitakuwa tu msafirishaji wa mali ghafi bali itakuwa mtumiaji wa mwisho wa teknolojia hiyo.

Uthibitisho mkubwa zaidi unaoonyesha kuwa Tanzania inaenda kuwa na kinu cha nyuklia kwa siri na umakini mkubwa ni kuwepo kwa mkataba wa faragha ambao unazuia pande mbili yaani Shirika la Umeme Tanzania na Shirika la Rosatom la Urusi kusema chochote wakati wa mazungumzo mpaka yafikie mwisho. 

Wataalamu wa sekta ya nishati na sheria nchini wameeleza kuwa mkataba huu wa kisheria wa kutosambaza taarifa ni wa kawaida lakini wa kiwango cha juu sana unapohusisha masuala nyeti ya usalama na nishati ya kimkakati kama nyuklia. 

Siri hii kubwa inalinda maslahi ya taifa na kuzuia kuingiliwa kati kwa mazungumzo hayo na mataifa mengine au washindani wa kijiografia kabla ya makubaliano kamili kukamilika. 

Hatua hii ya usiri inatafsiriwa na wachambuzi kama ishara ya wazi kwamba pande zote mbili ziko katika hatua za mwisho za kiufundi na kisheria kufanikisha ujenzi wa kinu hicho bila kuleta taharuki.

Ili kufikia maono ya mwaka 2029 ya kuwa na kinu cha nyuklia, Tanzania inakabiliwa na kibarua kizito cha kujenga udhibiti madhubuti wa kisheria na kitaalamu. 

Rais Samia akizungumza na waandishi wa habari mjini St Petersburg, Urusi wakati akihudhuria Jukwaa la Uchumi la Kimataifa la Petersburg, alibainisha kuwa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania sasa itakuwa na kazi kubwa inayohusiana na masuala ya matumizi ya nyuklia kwa amani kama inavyoelekezwa na Shirika la Kimataifa la Nguvu za Atomiki. 

Ushirikiano mpya na Urusi hautalenga tu kununua mitambo bali kuhamisha teknolojia kwa kutoa mafunzo ya wahandisi wa kiasili yanayofadhiliwa kwa sasa nchini Urusi, jambo ambalo ni la msingi sana kwani usalama wa kinu cha nyuklia unategemea kwa asilimia mia moja uwezo, maarifa, na umakini wa wanadamu wanaokiongoza.

Wataalamu wa nishati kutoka serikalini wanasisitiza kuwa hatua hii ya sasa ya kimkakati itaiwezesha nchi kuwa na uhakika kamili wa nishati ya viwanda ambayo haitayumba kutokana na mabadiliko ya tabianchi kama ilivyo kwa nishati ya maji. 

Kauli za wataalamu hao zilianikizwa na Rais Samia Suluhu Hassan aliyesema jwamba ni lengo la serikali kuwa na taifa ambalo linazalisha jumla ya megawati 8000 ili kuwa na ziada ya uhakika ya kuuza nchi za nje.

Mazungumzo yanayoendelea chini ya mkataba wa faragha yanalenga kuhakikisha kuwa ujenzi wa kinu hicho unazingatia viwango vyote vya kimataifa na gharama zinazohimilika kwa uchumi wa Tanzania. 

Hii inaonyesha kuwa serikali haikurupuki bali inasonga mbele kwa hatua madhubuti zilizofanyiwa utafiti wa kina ili kulinda maslahi ya kizazi cha sasa na kijacho.

Safari ya kuelekea mwaka 2029 imeshaanza kwa kasi kubwa na ya kimyakimya chini ya usimamizi thabiti Rais Samia Suluhu Hassan ambapo ziara yake nchini Urusi pamoja na kuwa na mafanikio makubwa kisiasa na kiuchumi, imewezesha kuwepo kwa mikataba ya makubaliano kadha yanayogusa teknolojia ya nyukilia.

Urani ya Mkuju si hadithi tena ya madini yaliyolala ardhini bali ni mtaji wa kimkakati unaokwenda kubadilisha kabisa ramani ya nishati katika ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati. 

Kama ahadi ya Rais Samia itatimizwa na mazungumzo ya siri yaliyopo sasa yakazaa matunda yaliyokusudiwa, ifikapo mwaka 2029 moshi na mwanga kutoka kwenye kinu cha kwanza cha nyuklia cha Tanzania utakuwa ndio ushahidi tosha wa nchi iliyoamua kuikumbatia nishati ya kesho kwa ajili ya maendeleo endelevu ya leo.

mwisho

UJUMBE WA TANZANIA WASHIRIKI MAADHIMISHO YA KUZUIA UTUMIKISHWAJI WA MTOTO GENEVA

June 10, 2026 Add Comment
Mkurugenzi Mkuu wa ILO, Bw. Gilbert Houngbo akihutubia wakati  wa Maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Kupinga Utumikishwaji wa Mtoto yaliyofanyika katika Ukumbi wa Tempus, Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, tarehe 9 Juni, 2026, Geneva, Uswizi.

MAKALA- RAIS DKT.SAMIA -TANZANIA HAIFUNGAMANI NA UPANDE WOWOTE ,INASAKA FURSA ZA KIUCHUMI KILA PEMBE YA DUNIA

June 10, 2026 Add Comment


Na Beda Msimbe, TBN, aliyekuwa Petersburg, Urusi


Ulimwengu wa sasa wa diplomasia ya kijiografia unatawaliwa na ushindani mkubwa wa nguvu za kisiasa na kiuchumi kati ya mataifa makubwa ya Magharibi na yale ya Mashariki. 

Katika mazingira haya, mataifa yanayoendelea mara nyingi hujikuta yakitazamwa kwa darubini ya shaka pale yanapochukua hatua za kimkakati kupanua wigo wa washirika wao wa kimaendeleo. 

Ziara ya hivi karibuni ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini Urusi, imezua minong'ono na hisia mbalimbali miongoni mwa wachambuzi wa mambo, wengi wao wakihofia kuwa huenda Tanzania sasa inabadili mwelekeo wake wa sera ya mambo ya nje kwa kuitupa mkono Magharibi na kugeukia upande wa Mashariki. 

Hofu hii haina msingi wowote, kwani majibu thabiti na ya kizalendo aliyoyatoa Rais Samia mbele ya waandishi wa habari pembezoni mwa Jukwaa la Kimataifa ya Uchumi la St. Petersburg (SPIEF) nchini Urusi, yanadhihirisha ukomavu wa diplomasia ya Tanzania inayojali maslahi ya taifa kwanza kabisa.

Katika mazungumzo hayo maalum yaliyowashirikisha waandishi wa habari 13 walioambatana naye, akiwemo mwakilishi kutoka Mtandao wa Bloggers Tanzania (TBN), Rais Samia alikuwa wazi na alinyoosha maelezo bila kusita. 

Alifafanua kuwa Tanzania haihamishi nguvu zake kutoka upande mmoja kwenda mwingine, bali inaongeza wigo wa washirika ili kuhakikisha malengo ya maendeleo ya kiuchumi yanatimizwa kwa faida ya wananchi wake. 

Hii ina maana kwamba wale wote wenye hofu au mashaka kuhusu ushirikiano wa karibu kati ya Tanzania na Urusi wanapaswa kuondoa shaka hiyo mara moja, kwani serikali haifuati mtu au upande wowote wa kiitikadi, bali inafuata yeyote mwenye nia njema ya kushirikiana katika kuinua maisha ya Watanzania.

Msimamo huu wa Rais Samia si jambo geni wala la kubahatisha, bali ni muendelezo wa misingi imara ya kihistoria iliyowekwa na Muasisi wa Taifa letu, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. 

Miaka 57 iliyopita, Mwalimu Nyerere alipotembelea Urusi (wakati huo ikiwa Muungano wa Sovieti), alitamka maneno yaleyale yanayosikika leo kutoka kwa Rais Samia: kwamba Tanzania ni nchi isiyofungamana na upande wowote. Mwalimu alisisitiza kuwa Tanzania itajichanganya na marafiki zake kwa jinsi marafiki hao wanavyotaka kuwa na Tanzania, mradi tu hawataingilia uhuru na mamlaka ya nchi. Falsafa hiyo ya kihistoria ndiyo inayomwongoza Rais Samia hadi leo katika ulimwengu huu unaozidi kuwa na vitovu vingi vya nguvu ya kiuchumi na kiteknolojia.

Sera ya Tanzania ya kutofungamana na upande wowote (Non-Aligned Policy) imekuwa silaha kuu ya kulinda uhuru wa Tanzania wa kufanya maamuzi ya kimkakati. Katika kile kinachoitwa Diplomasia ya Maslahi ya Kitaifa (National-Interest Diplomacy), kigezo kikuu cha kupima ubora wa uhusiano wa kimataifa si itikadi za kisiasa, bali ni mchango gani uhusiano huo unaingiza katika uchumi wa nchi, ajira kwa vijana, na uhamishaji wa teknolojia. 

Rais Samia alifafanua kuwa ziara yake nchini Urusi ilikuja na maombi saba ya kimkakati kutoka Tanzania, na wenyeji wao wa Urusi wakavutiwa kiasi cha kuongeza maombi mengine mawili na kufanya jumla ya maeneo tisa ya ushirikiano. Hii inadhihirisha kuwa pande zote mbili zinazungumza lugha moja inayolenga ustawi wa kiuchumi na maendeleo ya jamii.

Ili kuelewa kwa nini Tanzania inapaswa kuendelea kushirikiana na Urusi pamoja na ulimwengu mzima, ni lazima kuangalia uwiano wa washirika wetu duniani kote. 

Serikali ya Awamu ya Sita haijafunga milango kwa mataifa ya Magharibi; badala yake washirika wetu wa kitamaduni wanaendelea kuwa nguzo muhimu. Kwa mfano, Marekani bado ni mshirika mkubwa sana wa kiuchumi na kibiashara nchini Tanzania, ikiongoza katika kuleta watalii wengi na kuwekeza kupitia kampuni kubwa zaidi ya 500 zilizopo nchini, hususan katika sekta ya madini na uwekezaji mbalimbali wa kimkakati. Vivyo hivyo, mataifa ya Ulaya yameendelea kuwa washirika  wakuu katika biashara na utoaji wa misaada pamoja na uwezeshaji wa kifedha. Uhusiano huu wa karibu na Magharibi haujatikisika, na unazidi kuimarika kila uchao.

Wakati huo huo, Tanzania imeendelea kunufaika na uhusiano mkubwa na mataifa ya Asia. China imekuwa mshirika  mkuu wa kihistoria na wa sasa katika kuwezesha miradi mikubwa ya miundombinu ya usafirishaji na uchukuzi, huku India nayo ikiwa miongoni mwa washirika wakubwa wa kibiashara .

Japan haikuachwa nyuma, kwani imeendelea kuwekeza kwa nguvu katika sekta za nishati, elimu, na ujenzi wa miundombinu ya kijamii. Hata mataifa mengine kama Australia, Uingereza, na Ufaransa yamekuwa yakija nchini kwa kasi kupitia mipango mbalimbali kama vile mpango wa Matei wa Ufaransa ili kuwezesha maendeleo ya kiuchumi. 

Kwa mtazamo huu, Urusi inaingia kama mshirika mwingine muhimu wa kimkakati baada ya Tanzania kumaliza changamoto zilizotokana na masharti magumu ya mabadiliko ya kiuchumi ya Benki ya Dunia katika miaka ya 1980, ambayo wakati huo yalilazimu Tanzania kuangalia upande mmoja tu wa mlango.

Ni dhahiri kuwa Diplomasia ya sasa ya Tanzania inatawaliwa na ukomavu na uhuru wa kuchagua. Kama alivyowahi kunukuu Waziri wa Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, kuhusu methali maarufu ya kiuchumi: "Tanzania haihitaji kujua rangi ya paka, mradi tu paka huyo ana uwezo wa kukamata panya." 

Maneno haya yana maana kwamba Tanzania haichagui wala haibagui mshirika kwa kuangalia sura au mfumo wake wa kisiasa, bali inaangalia uwezo na utayari wa mshirika huyo kushirikiana nayo katika kutatua changamoto za umaskini na kukuza uchumi. Kila taifa linaloheshimu mamlaka ya Tanzania na liko tayari kuchangia katika ustawi linakaribishwa kwa mikono miwili.

Mkakati huu wa kutafuta washirika wengi kwa wakati mmoja una umuhimu mkubwa sana katika kulinda usalama wa kiuchumi wa Tanzania. Hakika kuweka mayai yote kwenye kikapu kimoja ni hatari kubwa katika ulimwengu wa sasa uliopasuka kutokana na vikwazo vya kiuchumi na migogoro ya kikanda. Kuwa na washirika mbalimbali kunatoa nguvu kubwa ya majadiliano (bargaining power) kwenye meza za kimataifa, kwani hatutegemei chanzo kimoja tu cha mitaji au teknolojia. Kama soko moja likiyumba au kukiwa na mabadiliko ya kisiasa upande mmoja, Tanzania inaweza kuendelea kusonga mbele kwa kutumia milango mingine iliyo wazi.

Kwa kuwa, dira yetu ya maendeleo ya taifa ya 2050 ndiyo dira kuu inayoongoza Tanzania hivi sasa ni vyema kama taifa kutumia diplomasia ya kiuchumi kutekeleza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2050, lengo likiwa ni kukuza uchumi kwa kiwango kikubwa na kufikia thamani ya uchumi wa dola bilioni 1,000 (trilioni moja) ifikapo mwishoni mwa utekelezaji wake. 

Ili kufikia lengo hili kubwa la kihistoria, serikali inahitaji mitaji mikubwa, miundombinu ya kisasa, na teknolojia ya hali ya juu kutoka kila kona ya dunia. Tanzania haiwezi kufikia malengo hayo makubwa kwa kujifungia milango au kwa kuchagua upande mmoja wa kidunia. Ndiyo maana Rais Samia anapiga hatua kwa ujasiri, akifungua milango kila mahali—iwe ni Washington, Beijing, Brussels, au Moscow—kuhakikisha kuwa maslahi ya taifa yanalindwa na fursa za kiuchumi zinawafikia wananchi wote.

mwisho

KOMANYA: UHURU WA VYOMBO VYA HABARI UENDE SAMBAMBA NA UWAJIBIKAJI

Kajunason June 10, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu

Weledi, maadili na uelewa wa sheria kwa waandishi wa habari vimetajwa kuwa nyenzo muhimu katika kulinda haki za wananchi na kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi kuhusu masuala ya kisheria, haki za binadamu na ukatili wa kijinsia.

Hayo yameelezwa na Mjumbe wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Wakili Ladislaus Komanya, tarehe 09 Juni 2026 wakati akiwasilisha mada kuhusu "Uhuru wa Vyombo vya Habari katika Enzi ya Kidijiti: Wajibu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari" katika mafunzo ya waandishi wa habari yaliyoandaliwa na Wizara ya Katiba na Sheria wilayani Tarime, mkoani Mara.

Wakili Komanya amesema uhuru wa vyombo vya habari unaenda sambamba na uwajibikaji wa mwandishi katika kuthibitisha taarifa, kuzingatia maadili ya taaluma na kuheshimu sheria za nchi. 

Ameongeza kuwa waandishi wa habari wanapaswa kutumia fursa zinazotolewa na teknolojia za kidijiti kwa kuzingatia weledi na maadili ili kuhakikisha taarifa wanazozitoa zinachangia upatikanaji wa haki, maendeleo ya jamii na ustawi wa wananchi.

"Mwandishi wa habari anapaswa kuzingatia misingi ya taaluma, maadili na sheria ili kuhakikisha taarifa anazozitoa zinachangia upatikanaji wa haki na maendeleo ya jamii," amesema Wakili Komanya.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa waandishi wa habari kuthibitisha taarifa kabla ya kuzichapisha au kuzirusha, hususan wanaporipoti masuala yanayohusu sheria, haki za binadamu na makundi maalumu katika jamii. 

Amesema matumizi ya teknolojia za kidijiti yanapaswa kwenda sambamba na uwajibikaji ili kulinda hadhi ya taaluma ya habari na maslahi ya umma.

Akifungua mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, amesema mafunzo hayo yataongeza tija katika utoaji wa habari za kisheria na kusaidia wananchi kutambua haki zao kupitia vyombo vya habari.

Amesema pia kuwa ongezeko la matukio ya ukatili wa kijinsia yanayoripotiwa katika vyombo vya sheria linahitaji ushiriki mkubwa wa waandishi wa habari katika kutoa elimu na taarifa sahihi kwa wananchi ili kusaidia juhudi za kuyatokomeza.

"Endapo mtatumia mafunzo haya kwa ufasaha, yataongeza tija katika kuhabarisha wananchi kuhusu mafanikio ya huduma za msaada wa kisheria pamoja na changamoto zinazojitokeza katika jamii zetu," amesema Gowele.

Kwa upande wake, Mratibu wa mafunzo hayo kutoka Wizara ya Katiba na Sheria, Wakili wa Serikali Athumani Msosole, amesema mafunzo hayo yatawawezesha waandishi wa habari kutambua namna bora ya kuripoti masuala ya ukiukwaji wa haki za binadamu, changamoto za kisheria pamoja na hatua zinazochukuliwa na mamlaka mbalimbali katika kutatua matatizo hayo ndani ya jamii.

Msosole amesema uandishi sahihi wa habari za masuala ya sheria una mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu haki zao na huduma mbalimbali za msaada wa kisheria zinazotolewa nchini.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Wanahabari Tarime, Jacob Karoli, amesema mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka kwani yatawajengea waandishi wa habari uwezo wa kuandika habari za kisheria kwa usahihi zaidi na hivyo kuongeza manufaa ya habari hizo kwa wananchi.

Jumla ya waandishi wa habari 40 kutoka Wilaya ya Tarime wanashiriki mafunzo hayo yanayolenga kuwawezesha kuwa mabalozi wa elimu ya sheria, haki za binadamu na mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia katika maeneo yao.

RAIS MSTAAFU DKT.JAKAYA KIKWETE NA RAIS WILLIAM RUTO WA KENYA MKUTANONI JUKWAA LA AMANI LA OSLO 2026

June 10, 2026 Add Comment

 


Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na Rais wa Kenya Mhe. William Samoei Ruto walipokutana wakati wa mkutano wa Jukwaa la Amani la Oslo 2026 (Oslo Forum 2026) unaofanyika mjini Oslo, Norway, tarehe 10–11 Juni 2026.  

Mkutano huo wa kimataifa wa kila mwaka unawaleta pamoja wasuluhishi wa migogoro, viongozi wa ngazi za juu, na wataalamu wa amani kutoka zaidi ya nchi 50 duniani. 



Mwaka huu, Oslo Forum inajadili kauli mbiu yenye uzito wa kipekee: "Gharama ya Vita, Thamani ya Amani" ("The Cost of War, the Price of Peace").



MAHUNDI AIELEZA DUNIA HATUA ZA TANZANIA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

MAHUNDI AIELEZA DUNIA HATUA ZA TANZANIA KATIKA KULINDA HAKI ZA WATU WENYE ULEMAVU

June 10, 2026 Add Comment




Na Jackline Minja, New York, Marekani

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Mhandisi Maryprisca Mahundi, ameieleza Jumuiya ya Kimataifa hatua kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Tanzania katika kulinda na kuendeleza haki za watu wenye ulemavu, wakati aliposhiriki Mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (COSP19) unaofanyika katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, Jijini New York, Marekani.

Mhe. Mahundi, ambaye amemuwakilisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge na Uratibu na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Palamagamba John Kabudi, amesema Tanzania imeendelea kuimarisha mifumo ya kisheria, kisera na kiutendaji ili kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata haki, fursa na huduma stahiki kama wananchi wengine.

Akiwasilisha taarifa ya nchi, Mhe. Mahundi amesema Tanzania imepiga hatua kubwa kupitia Sheria ya Watu Wenye Ulemavu Na. 9 ya mwaka 2010 kwa Tanzania Bara pamoja na Sheria Na. 8 ya mwaka 2022 ya Zanzibar, ambazo zimeweka msingi imara wa kulinda haki na ustawi wa watu wenye ulemavu.

“Masuala ya ulemavu yamejumuishwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na mipango mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha hakuna anayebaki nyuma katika safari ya maendeleo ya taifa na kusema kuwa Serikali imeendelea kupanua upatikanaji wa elimu jumuishi, huduma za afya, huduma za urekebishaji na tiba, teknolojia saidizi, programu za uwezeshaji kiuchumi pamoja na huduma za hifadhi ya jamii kwa watu wenye ulemavu” amesema Mhe. Mahundi

Aidha Mhe. Mahundi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa uongozi wake madhubuti na dhamira ya dhati ya kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata huduma bora na fursa zinazowawezesha kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya nchi.

“Serikali ya Tanzania itaendelea kushirikiana na nchi wanachama, Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia na watu wenye ulemavu wenyewe katika kuharakisha utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu na kujenga jamii jumuishi inayoheshimu usawa, utu na haki za kila mtu,” amesema Mhe. Mahundi

Mkutano huo wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu umebeba kaulimbiu inayosema “CRPD at 20: Celebrating and Consolidating Achievements and Shaping the Next Phase of Implementation in a Changing World,” ukilenga kutathmini mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 20 tangu kuanzishwa kwa mkataba huo na kuweka mikakati ya kuendeleza utekelezaji wake duniani.  

WRRB YANADI UFANISI WA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA MISRI, YAFUNGUA MILANGO YA BIASHARA YA MIFUGO

WRRB YANADI UFANISI WA MFUMO WA STAKABADHI ZA GHALA MISRI, YAFUNGUA MILANGO YA BIASHARA YA MIFUGO

June 10, 2026 Add Comment
 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB), Asangye Bangu, ameshiriki Jukwaa la Tanzania na Misri la Utalii, Biashara na Uwekezaji na kueleza kuwa Tanzania imeongeza biashara ya mifugo na mazao ya mifugo katika Mfumo wa Stakabadhi za Ghala kwa kuwa unazingatia uwazi, ubora na uaminifu katika biashara.

Akizungumza katika jukwaa hilo (Tanzania–Egypt Tourism, Trade and Investment Forum) lililofanyika nchini Misri na kuwakutanisha wadau wa biashara, uwekezaji na utalii, Bangu amesema mfumo unaotumika kusimamia biashara ya mazao ya kilimo sasa uko tayari kuhudumia pia sekta ya mifugo.

Akifafanua ufanisi wa matumizi ya mfumo huo katika moja ya mijadala iliyokuwepo kwenye jukwaa hilo, Bangu amesema wamefanya kikao kifupi na ujumbe wa Misri ambao wameonesha nia kubwa ya kufanya biashara ya mifugo na bidhaa zitokanazo na mifugo kutoka Tanzania.

“Tunawakaribisha wafanyabiashara wa Misri kuja kufanya biashara Tanzania. Mfumo wetu wa Stakabadhi za Ghala ni wa kuaminika na umejengwa kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na usalama kwa pande zote,” amesema.

Amesisitiza kuwa ushirikiano kati ya Tanzania na Misri katika biashara ya mifugo na mazao mengine unaweza kuongeza thamani ya biashara kati ya nchi hizo mbili na kuwanufaisha wazalishaji, wafanyabiashara na uchumi wa Taifa kwa ujumla.

Awali, amefafanua kuwa WRRB haihusiki na hatua ya uzalishaji wa mazao bali huingia baada ya uzalishaji kukamilika kwa kusimamia mnyororo wa biashara unaohakikisha bidhaa zinahifadhiwa, zinakaguliwa na kuuzwa kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.

Bangu amesema kwa sasa WRRB inashirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Nafaka na Mazao Mchanganyiko (COPRA), vyama vya ushirika pamoja na wafanyabiashara binafsi katika kuwezesha biashara ya mazao kupitia maghala yaliyosajiliwa na kusimamiwa kisheria.

Ameeleza kuwa bidhaa zinazopelekwa kwenye maghala hayo hukaguliwa ubora na kiasi chake na wataalamu mbalimbali kabla ya kuingizwa katika mfumo rasmi wa biashara.

“Maghala haya yanamilikiwa na sekta binafsi, vyama vya ushirika au Serikali, lakini yote husajiliwa na kusimamiwa na WRRB ili kuhakikisha yanazingatia viwango vinavyotakiwa,” amesema.

Kwa mujibu wa Bangu, mfumo huo unahusisha wataalamu wa ukaguzi wa ubora, usimamizi wa taarifa na ufuatiliaji wa bidhaa kuanzia zilikotoka hadi zinapowekwa ghalani, jambo linaloongeza uaminifu kwa wanunuzi wa ndani na nje ya nchi.

Ameongeza kuwa hatua ya mwisho ni kuandaliwa kwa taarifa kamili za bidhaa husika (catalogue) ambazo huwapatia wafanyabiashara taarifa muhimu kabla ya kufanya maamuzi ya ununuzi.

Bangu amesema WRRB pia inashirikiana na Soko la Bidhaa Tanzania (TMX) kupitia mfumo wa kidijitali unaowezesha wafanyabiashara kutoka sehemu mbalimbali duniani kuona bidhaa zilizopo maghalani na kufanya biashara kwa urahisi.

MRAMBA AITANGAZA TANZANIA CANADA,ASEMA NI KITOVU CHA UWEKEZAJI WA NISHATI

June 10, 2026 Add Comment



Calgary, Canada


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mha. Felchesmi Mramba, ameendelea kuitangaza Tanzania kimataifa kwa lengo la kuvutia uwekezaji zaidi katika Sekta ya Nishati akieleza kuwa Tanzania ni kitovu cha uwekezaji wa nishati barani Afrika.


Mramba amesema hayo wakati wa Mkutano wa Dunia wa Nishati ya Jotoardhi (World Geothermal Congress – WGC 2026) unaoendelea  Calgary nchini Canada.


Amesema Tanzania ni kiungo muhimu katika biashara ya umeme kikanda kupitia ushiriki wake katika masoko ya umeme ya Jumuiya ya Nchi za Afrika Mashariki (EAPP) na Kusini mwa Afrika (SAPP), jambo linalotoa fursa kwa wawekezaji kufikia masoko mengi nje ya mipaka ya nchi.


Katika mkutano huo Mha.Mramba amewasilisha fursa mbalimbali za uwekezaji zilizopo nchini Tanzania, akibainisha kuwa Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na kuimarisha miundombinu ya nishati ili kukidhi ongezeko la mahitaji ya umeme linalochochewa na ukuaji wa viwanda, shughuli za uchimbaji madini, sekta nyingine za kiuchumi na matumizi ya mwananchi mmoja mmoja.


Kuhusu nishati ya jotoardhi Mha. Mramba amebainisha kuwa Tanzania ina hazina kubwa ya nishati hiyo kutokana na uwepo wake ndani ya Ukanda wa Ufa wa Afrika Mashariki, wenye uwezo kuzalisha zaidi ya megawati 5,000 za umeme. 


Amesema pamoja na Serikali kuendelea na juhudi za  kuendeleza miradi ya jotoardhi, inakaribisha ushiriki wa wawekezaji katika utafutaji, uendelezaji na matumizi ya rasilimali hiyo.



Aidha, amewahamasisha wawekezaji wa Canada kuwekeza katika maeneo mbalimbali ya sekta ya nishati ikiwemo jotoardhi, gesi asilia, nishati ya jua, mifumo ya kuhifadhi nishati pamoja na maendeleo ya miundombinu ya umeme.


Kwa upande mwingine, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Canada katika mafunzo ya wataalam, uhamishaji wa teknolojia na uwekezaji wa pamoja katika miradi ya nishati safi na endelevu.


Mkutano huo wa Kimataifa wa Jotoardhi ni sehemu pia ya jitihada za kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi na uwekezaji kati ya Canada na nchi za Afrika, hususan katika sekta ya nishati, kwa lengo la kuharakisha upatikanaji wa nishati safi, ya uhakika na endelevu.

MBUNGE ANNE KILANGO AONGOZA MAPOKEZI YA SHUJAA WA AFCON U -17 SAME MASHARIKI

June 10, 2026 Add Comment



Mamia ya wananchi wa Kata ya Kalemawe, Kijiji cha karamba wilayani Same, wamejitokeza kwa wingi kumpokea nyumbani kwao nyota chipukizi wa soka, Issa Chole, ambaye ni mchezaji wa timu ya taifa ya vijana ya Serengeti Boys chini ya umri wa miaka 17.

Mapokezi hayo yaliongozwa na Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, Anne Kilango, pamoja na viongozi mbalimbali wa eneo hilo na wananchi waliokusanyika kumpongeza kijana huyo kwa kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya AFCON 2026 kwa vijana chini ya miaka 17.



Shangwe na nderemo zilitawala katika kijiji hicho huku wananchi wakionesha fahari yao kwa mafanikio ya Issa Chole, ambaye ameibuka kuwa mmoja wa vijana wanaolipeperusha bendera ya Tanzania kimataifa kupitia mchezo wa soka.

Akizungumza katika hafla hiyo, Anne Kilango alisema mafanikio ya Issa Chole ni jambo kubwa kwa wakazi wa Same Mashariki na Taifa kwa ujumla kwani yanaonesha kuwa vijana wa eneo hilo wana uwezo wa kufikia ndoto zao wanapopewa fursa sahihi.


Alisema ujio wa mchezaji huyo nyumbani ni heshima kubwa kwa jimbo hilo na ushahidi kwamba uwekezaji katika michezo unaweza kuzaa matokeo chanya kwa vijana na jamii kwa ujumla.

Kilango alibainisha kuwa Issa Chole ni miongoni mwa vijana waliopitia mashindano ya Samia Cup, yanayoandaliwa kila mwaka katika Jimbo la Same Mashariki kwa lengo la kuibua na kukuza vipaji vya michezo.


Kwa mujibu wa mbunge huyo, zaidi ya timu 91 kutoka maeneo mbalimbali ya jimbo hilo hushiriki mashindano hayo, ambayo yamekuwa jukwaa muhimu la kuwapa vijana nafasi ya kuonesha uwezo wao.


Alisema kupitia mashindano hayo, vijana wengi wameanza kuonekana katika ngazi za juu za soka na wengine wamepata nafasi ya kujiendeleza katika taaluma ya michezo.


“Leo tunashuhudia matunda ya Samia Cup. Issa ametufanya tujivunie kama wananchi wa Same Mashariki na kama Watanzania. Hii ni ishara kwamba tuna vijana wengi wenye vipaji ambao wanahitaji kuungwa mkono,” alisema Kilango.


Aliongeza kuwa ataendelea kuimarisha mashindano hayo ili kuhakikisha vipaji zaidi vinaibuliwa na kupata nafasi ya kuiwakilisha Tanzania katika mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa.


Mbunge huyo pia aliahidi kuanzisha na kuendeleza michezo mingine ikiwemo mpira wa miguu kwa wasichana na mpira wa pete, kwa lengo la kuwapa vijana na watoto wa kike fursa zaidi za kukuza vipaji na kujenga ajira kupitia michezo.


Kwa upande wake, Issa Chole aliwashukuru wananchi wa Kalemawe pamoja na Anne Kilango kwa mapokezi makubwa aliyoyapata, akisema hakuwahi kutarajia kupokelewa kwa namna hiyo baada ya kurejea kutoka majukumu ya timu ya taifa.


Alisema mafanikio yake yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na mashindano ya Samia Cup yaliyompa nafasi ya kuonekana na kuanza safari yake ya soka la ushindani, huku akiwataka vijana wengine kushiriki mashindano hayo kwa nidhamu, kujituma na kuwa na malengo makubwa maishani.


Baba mzazi wa mchezaji huyo, Mzee Musa Chole, alisema anajivunia maendeleo ya mwanawe katika soka na kusisitiza kuwa nidhamu, mazoezi na kujituma ndiyo msingi wa mafanikio katika mchezo huo.Aidha, alimuomba Mbunge Anne Kilango kuendelea kuunga mkono vijana kupitia Samia Cup ili vipaji zaidi viweze kuibuliwa na kuendelezwa.


Naye mmoja wa wananchi wa Kata ya Kalemawe alisema jitihada za mbunge huyo katika kuendeleza michezo zimekuwa na manufaa makubwa kwa vijana, kwani zimewapa hamasa ya kujituma, kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya, ulevi na vitendo vingine vinavyoweza kuharibu maisha yao, huku akimpongeza kwa kujitokeza kushiriki mapokezi hayo ambayo yameonesha mshikamano mkubwa kati ya viongozi na wananchi.

STANDARD CHARTERED YAONGOZA TUKIO LA UPANDAJI MITI BAGAMOYO.

June 09, 2026 Add Comment

 

Kama sehemu ya dhamira yake ya kukuza uendelevu wa mazingira na uhifadhi wa mazingira, Standard Chartered Tanzania imeongoza shughuli ya upandaji miti katika Shule ya Sekondari Nianjema, Wilaya ya Bagamoyo.

Shughuli hiyo inaakisi juhudi zinazoendelea za benki katika kuunga mkono hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuhamasisha uelewa wa masuala ya mazingira na kuchangia katika uhifadhi wa mifumo asilia ya ikolojia ya Tanzania.

Mpango wa mwaka huu una umuhimu wa kipekee kwani unaadhimisha miaka 20 ya kujitolea kwa wafanyakazi wa Standard Chartered, ukiashiria miongo miwili ya hatua za pamoja, mchango kwa jamii na ushiriki wa wafanyakazi katika shughuli za kijamii na kimazingira.

Tukio hilo liliwakutanisha wafanyakazi wa benki, viongozi wa eneo husika, wanafunzi na wanajamii katika juhudi za pamoja za kuongeza uoto wa kijani na kuimarisha umuhimu wa utunzaji wa mazingira, Kupitia ushiriki huo, benki inalenga si tu kurejesha mazingira bali pia kuhamasisha utamaduni wa uendelevu kwa vizazi vijavyo.

Mpango huo uliongozwa rasmi na wawakilishi wa serikali za mitaa, jambo lililoonesha umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kusukuma mbele vipaumbele vya taifa katika masuala ya mazingira.

Akizungumza kabla ya tukio hilo, Mkuu wa Transaction Banking Tanzania, Busara Raymond, alisema

“Mazingira ni msingi wa uhai wetu ndiyo chanzo cha hewa ya oksijeni tunayopumua, malighafi tunazotegemea na mifumo ya ikolojia inayodumisha maisha. Hii ndiyo sababu uhifadhi wa mazingira ni muhimu sana, na kwa nini Standard Chartered inaendelea kuweka kipaumbele katika mipango inayolinda na kuhifadhi mazingira yetu.”

“Huu ni mwaka wetu wa tano mfululizo kupanda miti Bagamoyo, jambo linalodhihirisha dhamira yetu ya muda mrefu kwa jamii hii. Mwaka jana tulipanda miche 2,000 katika Shule ya Msingi Fukayosi, na tunajivunia kuendelea kujenga juu ya mafanikio hayo, Mbali na upandaji miti, tunaendelea kushiriki kikamilifu katika shughuli nyingine za kujitolea kwa jamii, ikiwemo kikao cha hivi karibuni cha ushauri na uongozi kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Pugu Boys.”

Tukio hilo pia lilihudhuriwa na Katibu Tawala wa Wilaya (DAS) wa Bagamoyo, jambo lililoonesha ushirikiano imara kati ya sekta ya umma na binafsi katika kuendeleza mipango ya uendelevu wa mazingira.

Kupitia ushirikiano huo, benki imefanikiwa kupanda zaidi ya miti 10,000 katika Wilaya ya Bagamoyo pekee na zaidi ya miti 30,000 katika Mkoa wa Dar es Salaam, hatua iliyochangia kuboresha uendelevu wa mazingira na kuunga mkono malengo ya upandaji miti nchini.

Kwa miaka mingi, benki imekuwa ikitekeleza programu mbalimbali zinazolenga jamii kwa lengo la kuimarisha ustahimilivu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi na kuhamasisha maendeleo endelevu.