HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

BONDIA MASHUHURI KUTOKA MAREKANI ATUA KUFANYA "ROYAL TOUR" TANZANIA

May 24, 2026 Add Comment
Bondia mashuhuri kutoka Marekani mwenye rekodi ya kushika mikanda yote minne ya dunia katika uzito wake ukiwemo wa welterweight, Terence “Bud” Crawford, ametua nchini Tanzania leo Mei 24, 2026, kuanza “Royal Tour.”

TADB YAIMARISHA USHIRIKIANO NA REDIO ZA KIJAMII KUKUZA KILIMO

May 24, 2026 Add Comment
Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) inaendesha semina kwa wamiliki na wahariri wa redio za kijamii zipatazo 50 toka Tanzania Bara na Zanzibar kuanzia tarehe 23 hadi 25,Mei 2026, Lengo kuu likiwa ni kukuza uelewa juu ya majukumu ya TADB pamoja na kuonesha fursa zinazopatikana katika benki hiyo.

SERIKALI YARIDHISHWA NA MWENENDO WA KIWANDA CHA SATURN CORPORATION

May 24, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Serikali imesema mafanikio yaliyofikiwa na kiwanda cha kuunganisha magari aina ya Howo kinachomilikiwa na Saturn Corporation Limited ndani ya kipindi cha miaka miwili ni ushahidi wa ukuaji wa sekta ya viwanda nchini, huku uzalishaji, ajira na mapato ya Serikali vikiongezeka kwa kasi.

Vyuo vikuu 9 vya Malasyia kushiriki maonesho Dar

May 24, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

TANZANIA inatarajiwa kupokea ujumbe mkubwa wa viongozi wa elimu ya juu kutoka Malaysia, wakiwemo viongozi kutoka Wizara ya Elimu ya Malaysia, Education Malaysia Global Services (EMGS), pamoja na wawakilishi wa vyuo vikuu tisa.

MRADI WA BARRICK - TWIGA WAJENGA MADARASA SEKONDARI ULAYASI , NJOMBE

May 24, 2026 Add Comment

Kiongozi wa Mbio za Mwenge kitaifa, Wazo Michael Mwang’onda akikagua moja ya madarasa yaliyojengwa kupitia mradi wa Barrick-Twiga Future Forward Education Program katika moja ya Shule ya Sekondari Kongwe ya Ulayasi iliyopo Ludewa Mkoani Njombe.

DKT. SAJAD HABIB RAI AISHAURI SERIKALI KUANZISHA MFUKO WA MAFUTA

May 24, 2026 Add Comment

     

SERIKALI imeshauriwa kuanzisha Mfuko maalumu wa kuhimili bei ya Nishati ya mafuta nchini ambao pamoja na mambo mengine utasaidia kupunguza makali ya bei wakati wa dharura zinazosababishwa na sababu mbalimbali.

UPATIKANAJI UMEME KUENDELEA KUIMARIKA MKOANI IRINGA— MHE. SALOME

May 24, 2026 Add Comment



Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali inaendelea kufanya jitihada mbalimbali ili kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Iringa.


Amesema tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aingie madarakani, Mkoa wa Iringa umepokea zaidi ya shilingi bilioni 124 kwa ajili ya kuimarisha huduma ya umeme na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanafikiwa na huduma hiyo kwa lengo la kuwawezesha kujiletea maendeleo ya kiuchumi.


Mhe. Salome ameyasema hayo leo Mei 23, 2026 wakati akijibu hoja za wananchi mkoani Iringa, wakati wa ziara ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba.


Amesema changamoto za umeme zilizokuwa zikikabili baadhi ya maeneo ikiwemo Kata ya Mafifi tayari zimeshapatiwa ufumbuzi na wananchi wanaendelea kupata huduma ya umeme wa uhakika. Hata hivyo, amesema katika Mtaa wa Mosi huduma hiyo bado haijafika ipasavyo ambapo tayari maelekezo yametolewa kwa TANESCO na REA kuhakikisha wananchi wa eneo hilo wanaunganishiwa umeme kwa wakati.


Pia ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuweka mazingira rafiki ya wananchi kuunganishiwa umeme kwa gharama nafuu ya shilingi elfu 27,000 tu, huku akielekeza kuwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya mjini lakini kiuhalisia wanaishi mazingira ya vijijini waunganishiwe umeme kwa gharama hiyo pia.


Katika kuimarisha zaidi huduma ya umeme mkoani Iringa, amesema Serikali kupitia Wizara ya Nishati inaendelea kuongeza uwezo wa Kituo cha Kupokea na Kusambaza Umeme cha Mufindi ambapo Mkoa huo utaanza kupata umeme kutoka megawati 60 hadi megawati 260.


Ameongeza kuwa Serikali inaendelea kubadilisha transfoma katika maeneo mbalimbali ya uwekezaji ili kuwezesha viwanda kufanya kazi muda wote na wananchi kuendelea kupata umeme wa uhakika.

Sambamba na hayo, Mhe. Salome amesisitiza umuhimu wa matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia kwa wananchi wa Mkoa wa Iringa ili kulinda mazingira na kuboresha afya na maisha ya wananchi.


Amesema Serikali inaendelea kutoa ruzuku ya majiko ya gesi na majiko banifu kwa wananchi wa vijijini na kuwahamasisha kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.




RAIS MSTAAFU DKY JAKAYA MRISHO KIKWETE AKUTANA NA MAKUNDI YA UPINZANI CHINI SUDAN KUSINI JIJINI DAR ES SALAAM

May 24, 2026 Add Comment

Pichani, Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya wajumbe wa makundi yaliyoshiriki mikutano hiyo, yakiwemo United People’s Alliance (UPA), SSOMA, SPLM-IO, pamoja na People’s Coalition for Civil Action na Federal Democratic Party.


Picha na Issa Michuzi



Mikutano ya ngazi ya juu iliyohusisha makundi mbalimbali ya upinzani nchini Sudan Kusini imefanyika jijini Dar es Salaam tarehe 21 na 22 Mei, 2026 ikiwa ni sehemu ya juhudi mpya za kufufua mchakato wa amani jumuishi baada ya kusuasua kwa utekelezaji wa makubaliano ya amani ya mwaka 2018.

Mazungumzo hayo yaliongozwa na Rais wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, ambaye ni Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Afrika kwa Ukanda wa Pembe ya Afrika na Bahari ya Shamu.

Majukumu yake makuu yanajumuisha: Upatanishi wa Amani: Kusimamia diplomasia ya kuzuia migogoro na kuongoza mazungumzo jumuishi ili kutatua changamoto za kisiasa na kiusalama katika ukanda huo.

Ushirikiano wa Kikanda: Kufanya kazi kwa karibu na jumuiya na taasisi mbalimbali kama vile IGAD na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) ili kujenga misingi thabiti ya amani na usalama.

Kwa ujumla, mikutano hiyo ilionyesha dhamira ya Umoja wa Afrika na wadau wa kikanda katika kuimarisha mazungumzo ya kisiasa na kuhakikisha mazingira ya amani na utulivu yanaimarishwa kuelekea uchaguzi mkuu baadaye mwaka huu nchini Sudan Kusini.

Mikutano hiyo pia ililenga kuisaidia Umoja wa Afrika kupata picha kamili ya hali ya kisiasa na kiusalama nchini Sudan Kusini kabla ya uchaguzi uliotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huo wa 2026.

NLD YATETEA MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA NCHINI

May 24, 2026 Add Comment

 



>Sheria Isichague Chama

NA OSCAR ASSENGA, TANGA

Katibu Mkuu wa Chama cha NLD, Doyo Hassan Doyo, amesema mjadala unaoendelea kuhusu hatua zinazochukuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa umeonyesha jinsi baadhi ya Watanzania wanavyotoa hukumu za haraka bila kutafakari misingi ya sheria.

Doyo alisema kumekuwa na mtazamo kwamba Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inalenga zaidi vyama vya upinzani, huku ukweli ukiwa ni kwamba taasisi hiyo inasimamia sheria bila kuangalia itikadi ya chama husika.

Akizungumza wakati wa ziara ya chama hicho mkoani Tanga, alisema hatua zilizochukuliwa hivi karibuni dhidi ya baadhi ya viongozi wa kisiasa zinatokana na matamshi yaliyotafsiriwa kuwa na viashiria vya uvunjifu wa sheria za vyama vya siasa.

“Sheria iko wazi. Chama au kiongozi anayekiuka taratibu anaweza kupewa adhabu ya faini, kusimamishwa shughuli au hata kuchukuliwa hatua nyingine za kisheria. Hii siyo kwa chama fulani pekee,” alisema.



Alieleza kuwa baada ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutoa kauli zilizozua mjadala, Ofisi ya Msajili iliwaandikia barua ya kutaka maelezo. Hatua hiyo, kwa mujibu wa Doyo, ilitafsiriwa vibaya na baadhi ya wananchi pamoja na wanaharakati waliodai kuwa upinzani unaonewa.

Hata hivyo alisema hali hiyo imebadilika baada ya mmoja wa viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) naye kuandikiwa barua kufuatia matamshi yake ya kisiasa.

“Watu walidhani sheria inafanya kazi kwa upande mmoja, lakini sasa imeonekana wazi kuwa anayevunja sheria ndiye anayechukuliwa hatua, bila kujali anatoka chama gani,” alisema.

Doyo alisema vyama vya siasa vinapaswa kutambua kuwa vimesajiliwa kwa mujibu wa sheria na hivyo vina wajibu wa kuendesha shughuli zake ndani ya mipaka ya kisheria.

Alionya kuwa siasa zisizo na nidhamu zinaweza kupelekea uvunjifu wa amani na kuhatarisha usalama wa Taifa.

“Ukianza kufanya siasa nje ya sheria, maana yake unaondoka kwenye misingi ya kisiasa na kinachofuata ni migogoro na vurugu. Taifa haliwezi kujengwa kwa misingi ya shinikizo na vitisho,” alisema.



Aidha, aliitaka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuendelea kusimamia sheria kwa uthabiti bila kuogopa presha za kisiasa kutoka kwa wanasiasa au wanaharakati.

Kwa mujibu wa Doyo, uwepo wa taasisi imara zinazotekeleza sheria kwa haki ndiyo msingi wa kulinda amani na utulivu wa nchi.

Katika ziara hiyo ya NLD iliyoanzia Pangani na kuelekea Lushoto, chama hicho kimesema kinaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kuheshimu sheria, taratibu na kanuni za kisiasa ili kuimarisha demokrasia na mshikamano wa Taifa.

KILO 504 ZA HEROIN ZATEKETEZWA, DCEA YAIMARISHA ELIMU NA HUDUMA KWA WARAIBU

May 24, 2026 Add Comment
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza kilogramu 504.36 za dawa za kulevya aina ya heroin katika kiwanda cha saruji cha Dangote kilichopo mkoani Mtwara. Uteketezaji huo umefanyika kufuatia amri ya Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mtwara baada ya kukamilika kwa hatua za kisheria dhidi ya watuhumiwa waliohusika na dawa hizo.

TUME YA MADINI YAANZA KUTUMIA MFUMO WA IDRAS KUONGEZA UFANISI, MAPATO

May 22, 2026 Add Comment
Arusha

Tume ya Madini imeanza rasmi kutumia Mfumo Jumuishi wa Kodi za Ndani (IDRAS) unaolenga kurahisisha utoaji wa huduma, kuongeza ufanisi wa utendaji na kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali katika sekta ya madini.

ZIARA KWA VITENDO ZAWANOA WADAU WA MAZIWA MBEYA

May 22, 2026 Add Comment
Washiriki wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wadau wa Tasnia ya Maziwa mkoani Mbeya wamepata fursa ya kujifunza kwa vitendo kupitia ziara maalum zilizofanyika katika kiwanda cha maziwa cha Chuo Kikuu Cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) pamoja na shamba la ng’ombe wa maziwa la Gereza la Songwe, ikiwa ni sehemu ya kuimarisha uelewa wao kuhusu uzalishaji, uchakataji na usimamizi wa ubora wa maziwa.

SERIKALI YA AWAMU YA SITA YAENDELEA KUBORESHA MASLAHI YA WATUMISHI WA UMMA

May 22, 2026 Add Comment







WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete, leo ameshiriki ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Ngurdoto, mkoani Arusha.


Mkutano huo umefunguliwa rasmi na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, na umewakutanisha zaidi ya wanachama 5,050 wa TAPSEA kutoka Serikali Kuu, Serikali za Mitaa, taasisi mbalimbali za umma pamoja na wajumbe kutoka Tanzania Bara na Zanzibar.


Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Makamu wa Rais Dkt. Nchimbi aliwataka wajumbe wa mkutano huo, ambao pia unatarajiwa kuchagua viongozi wapya wa chama hicho, kuzingatia haki, mshikamano na maslahi ya taasisi yao, huku akisisitiza umuhimu wa kuepuka migogoro na mambo yanayoweza kukipotezea mwelekeo chama hicho muhimu kwa maendeleo ya utumishi wa umma nchini.


Kwa upande wake, Mhe. Ridhiwani Kikwete, akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, aliwakumbusha wajumbe hao juu ya juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha ustawi wa watumishi wa umma nchini.


Alieleza kuwa Serikali imeendelea kupandisha madaraja watumishi, kuboresha miundo na vyeo vya kazi, pamoja na kulipa madeni mbalimbali ya mishahara na stahiki za watumishi, huku akiahidi kuwa juhudi hizo zitaendelea kadri hali ya bajeti ya Serikali itakavyoruhusu.


“Tumekuwa tukifanya maboresho haya hatua kwa hatua, na dhamira yetu ni kuhakikisha watumishi wa umma wanaendelea kunufaika na matunda ya Serikali yao,” alisema Mhe. Ridhiwani.


Mkutano huo wa TAPSEA unatarajiwa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya taaluma ya uandishi na uendesha ofisi pamoja na mustakabali wa chama hicho nchini.




SALOME: NGUZO ZA ZEGE NA CHUMA KUTUMIKA KUKABILI CHANGAMOTO YA KUANGUKA KWA NGUZO ZA UMEME ZA MITI.

May 22, 2026 Add Comment



NAIBU Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kubadilisha nguzo chakavu kwa kuweka nguzo imara zaidi, zikiwemo nguzo za zege na chuma, pamoja na kuimarisha misingi ya nguzo katika maeneo yenye udongo laini ili kukabili changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme.

Salome ameeleza hayo leo, Mei 22, 2026, Bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mhe. Sara Msafiri Ally, Mbunge wa Mvomero, aliyetaka kujua ni lini Serikali itatatua changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika Tarafa ya Mgeta.

Akijibu swali hilo, Salome amesema Serikali inatambua uwepo wa changamoto ya kuanguka kwa nguzo za umeme katika baadhi ya maeneo ya Tarafa ya Mgeta kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo mvua nyingi, uwepo wa udongo usiohimilivu pamoja na uchakavu wa baadhi ya nguzo.Amesema Serikali kupitia TANESCO inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa miundombinu ya umeme ili kubaini na kushughulikia changamoto hizo mapema pindi zinapojitokeza.

Aidha, Salome amefafanua kuwa Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetenga bajeti maalum ya kubadilisha nguzo za miti katika maeneo yote yenye unyevunyevu pamoja na maeneo yenye shughuli mbalimbali za kibinadamu.

Kadhalika, ametoa wito kwa wananchi kuacha matumizi mabaya ya ardhi, ikiwemo kuchoma moto ovyo mashambani, jambo ambalo limekuwa likiathiri miundombinu ya umeme kwa kuunguza nguzo za umeme.

WAZIRI DKT. GWAJIMA ASISITIZA UWAJIBIKAJI NA MAZINGIRA BORA YA KAZI KWA WATUMISHI

May 22, 2026 Add Comment



Na WMJJWM – Dodoma

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima, amewataka watumishi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa bidii, kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya Utumishi wa Umma ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi. Dkt. Gwajima amesema hayo Mei 22, 2026 wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi uliofanyika katika Ukumbi wa Royal Village Hotel jijini Dodoma.

Katika hotuba yake, Dkt. Gwajima amesisitiza kaulimbiu yake ya “Kasi Zaidi, Karibu Zaidi na Wananchi; Kasi Zaidi, Karibu Zaidi na Watumishi – KAZA KAZAWA,” akieleza kuwa inalenga kuongeza uwajibikaji, uwazi na ufanisi wa watumishi pamoja na kuimarisha mazingira bora ya kazi. Aidha, ameitaka Menejimenti ya Wizara kuendelea kutoa motisha kwa watumishi wanaotekeleza majukumu yao kwa ubunifu, weledi na kuzingatia maadili mema ya utumishi wa umma.
Aidha, Dkt. Gwajima amesisitiza umuhimu wa kuwashirikisha watumishi katika mijadala ya bajeti na utekelezaji wa mipango ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2026/27. Vilevile, ametoa wito kwa watumishi kujiepusha na tabia hatarishi zinazosababisha maambukizi ya UKIMWI huku akiagiza Menejimenti kuendelea kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza tija na ufanisi kazini.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Eliakim Chacha Maswi, amesema Serikali itaendelea kuimarisha fikra chanya katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kuanzia ngazi ya msingi ili kuhakikisha jamii inanufaika na huduma zinazotolewa kwa ufanisi. Amesema mafanikio ya Wizara yanategemea ushirikiano, uwajibikaji na ubunifu wa watumishi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Aidha, Maswi amesema Wizara itaendelea kuimarisha malezi ya familia pamoja na matunzo ya watoto ili kuhakikisha kizazi kinachokua kinapata maadili mema na mazingira bora ya maendeleo. Pia amesema Serikali imejipanga kuhakikisha makundi maalum yanapata huduma na fursa za kuwawezesha kukuza uchumi wao na kujitegemea kupitia programu mbalimbali za maendeleo ya jamii.

“Hatuwezi kuendesha taasisi kama mali binafsi, tunapaswa kufanya kazi kwa kuzingatia maslahi ya wananchi na Taifa kwa ujumla,” amesema Maswi huku akiongeza kuwa Dira ya Taifa ya 2050 inahitaji watumishi wenye motisha, ubunifu na uwezo wa kuendana na mabadiliko ya teknolojia ili kutoa matokeo chanya katika jamii.

MWISHO

NDEJEMBI AZUNGUMZA NA BALOZI WA NORWAY NCHINI TANZANIA

May 22, 2026 Add Comment



Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Norway nchini Tanzania, Mhe. Tone Tinnes yaliyolenga kuimarisha na kuendeleza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili katika sekta ya nishati.

Mazungumzo hayo yamefanyika leo Mei 22, 2026 katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati zilizopo jijini Dar es Salaam.

Viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya nishati ikiwemo mashirikiano ya kimkakati katika uendelezaji wa gesi, umeme, nishati jadidifu pamoja na kubadilishana uzoefu wa kitaalamu na juhudi za kukuza sekta ya nishati kwa nchi hizo mbili.Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Kamishna wa Mafuta na Gesi kutoka wizara ya nishati, Bw. Goodluck Shirima, Mkurugenzi wa Maendeleo na Uzalishaji kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Paschal Njiko pamoja na wataalamu wengine.

DCEA YATUNUKIWA TUZO KWA KUIMARISHA NYUMBA ZA UPATAJI NAFUU

May 22, 2026 Add Comment
Mtandao wa Wamiliki wa Nyumba za Upataji Nafuu nchini, Tanzania Network for Voice of Sober House Tanzania, umemkabidhi tuzo ya shukrani Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), Aretas Lyimo, kwa kutambua mchango wake mkubwa katika mapambano dhidi ya dawa za kulevya hususan katika eneo la usimamizi, uratibu na uwezeshaji wa nyumba za upataji nafuu nchini.

MD TWANGE AELEZA KUTORIDHISHWA NA KASI YA MKANDARASI WA MRADI WA HALE

May 22, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu, Korogwe, Tanga


Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO Bw. Lazaro Twange ameeleza kutoridhishwa na kasi ya mkandarasi anayetekeleza mradi wa maboresho ya Kituo cha Kufua Umeme cha Hale kutokana na kuchelewa kukamilika kwa Mradi huo ulioanza kutekelezwa tangu mwaka 2022.

Bw. Twange ameyasema hayo leo Aprili 22, 2026 wakati wa ziara yake ya ukaguzi katika mradi wa Hale pamoja na mradi wa usafishaji wa bwawa la Mto Pangani iliyopo katika Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga ambapo amemtaka mkandarasi wa Mradi wa Hale kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ikiwa ni pamoja na kuongeza wafanyakazi pamoja na muda wa kufanya kazi ili ukamilike kwa wakati.

“Siridhishwi sana na mwenendo wake. Mkandarasi amewahi kuomba nyongeza ya muda mara mbili na nimepata taarifa kuwa yuko kwenye hatua za kuomba nyongeza nyingine ya tatu. Ndio maana nimekuja kuona kuna nini,” amesema Bw. Twange.

Amesema mradi huo una maeneo saba ya utekelezaji ambapo maeneo mawili tayari yamekamilika huku mengine yakiendelea na utekelezaji.

“Nimezungumza na msimamizi wa mradi, mhandisi mshauri pamoja na mkandarasi na nimewaelekeza wakae pamoja kuhakikisha ifikapo mwisho wa mwezi Julai mradi huu uwe umekamilika,” amesema Bw. Twange

Aidha, kuhusu mradi wa usafishaji wa bwawa la Pangani, Bw. Twange amesema matarajio ya TANESCO ni kuhakikisha kazi hiyo inakamilika ndani ya muda uliopangwa ili kuepusha changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa msimu wa mvua.

“Matarajio yetu ni kutoupitiliza mwaka mmoja ili tumalize kabla ya msimu unaokuja wa mvua,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Bw. Twange amesema TANESCO kwa sasa inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ya umeme nchini yenye thamani ya zaidi ya shilingi trilioni 13.4.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi wa Mradi wa Hale Mha. Kulwa Byemelo amesema maagizo yaliyotolewa na Mkurugenzi Mtendaji yatatekelezwa ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

“Mradi huu utakapokamilika utaimarisha upatikanaji wa umeme katika wilaya mbalimbali zinazochukua umeme kutoka kituo cha Hale pamoja na wilaya za Handeni, Muheza na Korogwe,” amesema Byemelo.

Ziara hii ni moja ya mikakati ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali ya umeme pamoja na kubaini changamoto zinazojitokeza na kuhakikisha zinatatuliwa kwa wakati na miradi ina kamilika ili watanzania waweze kuendelea kufurahia upatikanaji wa umeme wa uhakika.







TUME YA TAIFA YA MIPANGO YAWAKUTANISHA WADAU MAJADILIANO ATHARI ZA MGONGORO UKANDA WA GHUBA KWA TANZANIA

May 22, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa UNDP leo Mei 22, imefanya mjadala uliyowakutanisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabiliana na athari za mgogoro wa ukanda wa Ghuba.

Akifungua mjadala huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Mhe. Prof. Kitila Mkumbo amesema kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua madhubuti na za kimkakati ili kupunguza athari zinazotokana na mgogoro wa Ghuba kiuchumi na kwa wananchi.

Mhe. Mkumbo amesema hayo leo Mei, 22 jijini Dar es Salaam katika mjadala wa kitaalamu ulioandaliwa na Tume ya Taifa ya Mipango kwa kushirikiana na Umoja wa Mataifa UNDP kwa lengo la kujadili athari, uhimilivu na fursa zinazotokana na mgogoro huo.

Akitaja hatua hizo, Prof. Mkumbo amesema kuwa ni pamoja na kufuatilia kwa karibu bei na upatikanaji wa mafuta, chakula, mbolea na usafiri, kulinda kaya zilizo katika mazingira hatarishi, kuimarisha akiba na usambazaji wa biadhaa muhimu.

“tutahakikisha wananchi wanaendelea kupata chakula cha kutosha na mbolea kwa bei himilivu, vile vile tutaendelea kufanya uthibiti wa gharama za nishati, ikiwa ni pamoja na kutumia fursa za maliasili tulizonazo kama Gesi asilia, madini, utalii na fursa ya miundombinu ya usafiri kuimarisha uchumi wa taifa” amesema Prof. Mkumbo.

Hatua hizo, zinalenga kukabiliana na athari kama vile kupanda kwa bei ya mafuta, usafirishaji na mbolea kunakoweza kuathiri maisha ya wananchi, uzalishaji na bajeti ya Serikali, hivyo Serikali itaendelea kuchukua hatua za haraka ili kuwalinda.

Aidha, Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa pamoja na changamoto hizo, mgogoro huo wa Ghuba unatoa fursa ya kipekee ya kiuchumi kwa Tanzania na bara la Afrika kwa ujumla, hasa katika kuvutia uwekezaji mpya kwenye sekta ya nishati.

"Mgogoro huu unatoa mwanya mkubwa wa uwekezaji katika miundombinu ya mafuta, ikiwemo ujenzi wa viwanda vya kikanda vya kusafisha na kuchakata mafuta (regional refineries)," amesema Prof. Mkumbo.

Awali akimkaribisha Mhe. Waziri, Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Mipango na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango Dkt. Tausi Kida alieleza kuwa mkutano huo unahusisha wadau wa maendeleo, sekta binafsi, asasi za kiraia, watafiti na taasisi za elimu ya juu kujadili hatua mbalimbali na afua zinazoweza kutumika ili kukabilia na athari za mgogoro huo.

Majadiliano hayo yalihudhuriwa na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa Bi. Susan Namondo na Mwakalishi Mkaazi wa Umoja wa Mtaifa, na Mwakilishi Mkazi wa UNDP Tanzania Bw. Shigeki Komatsubaram.






FCC YABAINI VIPURI NA VILAINISHI BANDIA SOKONI

May 22, 2026 Add Comment
Wizara ya Viwanda na Biashara imeendelea kupambana na bidhaa bandia nchini kupitia operesheni maalum zilizofanywa na Tume ya Ushindani (FCC), ambapo hadi Aprili 2026 jumla ya chupa 4,251 za pombe bandia, chupa tupu 286 na katoni tupu 250 zilikamatwa jijini Dar es Salaam.

TBS YAFANIKIWA KUPATA ITHIBATI YA UMAHIRI YA KIWANGO CHA KIMATAIFA

May 22, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limefanikiwa kupata ithibati ya umahiri ya kiwango cha kimataifa cha ISO/IEC 17020 katika ukaguzi wa bidhaa, hatua inayotajwa kuwa chachu ya kuimarisha biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

SERIKALI KUIMARISHA MAABARA ZA VIWANDA

May 22, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DODOMA

Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) imeendelea kuimarisha sekta ya viwanda nchini kwa kufanya tathmini ya viwanda, kuboresha maabara za kisasa pamoja na kuendeleza teknolojia za uzalishaji zinazolenga kuongeza thamani ya rasilimali za ndani.

Akizungumza leo Mei 22, 2026 bungeni jijini Dodoma wakati akiwasilisha hotuba ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2025/2026, Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga amesema TIRDO imeendelea kutekeleza zoezi la tathmini ya viwanda na kubaini fursa za uwekezaji katika maeneo mbalimbali nchini.

Amesema tathmini hiyo inalenga kubaini idadi ya viwanda, ajira, uwezo wa uzalishaji, teknolojia zinazotumika pamoja na maeneo yenye fursa za uwekezaji ili kuchochea maendeleo ya viwanda na kuongeza thamani ya rasilimali za ndani.

Kwa mujibu wa Kapinga, zoezi hilo limefanyika katika mikoa miwili mipya na kufanya jumla ya mikoa iliyofikiwa kufikia tisa ambayo ni Pwani, Morogoro, Dar es Salaam, Kilimanjaro, Tanga, Arusha, Manyara, Mwanza na Shinyanga.

Aidha, amesema taarifa zote zilizokusanywa zimeingizwa katika mfumo wa kanzidata za viwanda ambapo hadi Aprili 2026 kulikuwa na jumla ya viwanda 25,650 vilivyosajiliwa.

“Kati ya viwanda hivyo, 482 ni vikubwa, 625 vya kati, 8,980 vidogo na 15,563 ni viwanda vidogo sana,” amesema Kapinga.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo amesema TIRDO imeendelea kuimarisha maabara zake kwa ajili ya utoaji wa huduma za kitafiti katika maendeleo ya viwanda.


Ameeleza kuwa maabara ya chakula iliyopata ithibati mwaka 2025 imeboreshwa kwa kuongeza huduma kutoka tatu hadi sita pamoja na kuongeza wigo wa bidhaa kutoka moja hadi nne.


Bidhaa hizo ni pamoja na vyakula vilivyotayari kwa matumizi, nyama na bidhaa zake, samaki na bidhaa zake pamoja na sampuli za usufi wa nyuso.


Kapinga amesema hatua hiyo itaongeza uwezo wa maabara kutoa huduma za kuaminika zaidi huku ikipunguza utegemezi wa huduma kutoka nje ya nchi.


Pia amesema TIRDO inaendelea na jitihada za kuanzisha Maabara ya Nishati na Madini katika Mkoa wa Njombe ili kusogeza huduma karibu na maeneo yenye shughuli za uzalishaji na rasilimali za madini.


Amesema maabara hiyo itahudumia mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Ruvuma, Mbeya na Rukwa, huku ikitarajiwa kufanya vipimo vya ubora wa makaa ya mawe, kemikali, madini pamoja na nishati mbadala ikiwemo biomasi na mkaa mbadala.


“Hadi Aprili 2026, Shirika limefanikiwa kumpata mzabuni wa kusambaza na kusimika vifaa vya kisasa pamoja na kutoa mafunzo kwa wataalam watakaoendesha maabara hiyo,” amesema.


Kapinga aliongeza kuwa kukamilika kwa maabara hiyo kutachochea uchumi wa viwanda unaozingatia nishati safi na rafiki kwa mazingira.

Sambamba na hayo, amesema TIRDO inaendelea na mchakato wa kupata ithibati kwa maabara zake za mazingira, kemia, makaa ya mawe, mafuta na gesi ili kuongeza ubora wa huduma zinazotolewa.

Katika eneo la ubunifu na teknolojia, Waziri Kapinga alisema Wizara kupitia Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) imefanikiwa kuhawilisha teknolojia nane za uchakataji wa mazao na uzalishaji.

Teknolojia hizo ni pamoja na mashine za kutengeneza mkaa mbadala, kusafisha mafuta ya alizeti, kuzalisha chakula cha samaki, kubangua korosho, kukamua mafuta ya nazi pamoja na mashine za kusaga mawe yenye madini.

Aidha, amesema SIDO kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Viwanda la Umoja wa Mataifa (UNIDO) imetengeneza mashine tatu za kuzalisha mkaa mbadala na kuanzisha teknolojia mpya kutoka Japan katika maeneo ya Ifakara, Kahama na Mwanjelwa.

TBS YASOGEZA HUDUMA KARIBU, YAJENGA MAABARA MPYA DODOMA, MWANZA NA ARUSHA

May 22, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, 

WIZARA ya Viwanda na Biashara kupitia Shirika la Viwango Tanzania (TBS) imeendelea kuimarisha udhibiti wa ubora wa bidhaa za chakula na vipodozi nchini kwa kusogeza huduma karibu na wananchi pamoja na kupanua miundombinu ya maabara katika kanda mbalimbali.

RAIA WA IRAN APATIKANA NA HATIA YA KUSAFIRISHA DAWA ZA KULEVYA

May 22, 2026 Add Comment
Raia wa Iran, Jan Mohammed Millan, aliyekuwa nahodha wa jahazi la Al Arab, amehukumiwa kifungo cha jumla ya miaka 60 jela baada ya kupatilana na hatia ya kusafirisha dawa za Kulevya kilogramu 504.36 za heroin na kilogramu 355 za methamphetamine katika Bahari ya Hindi ndani ya eneo la kiuchumi la Tanzania.

WAHASIBU, WACHUMI WATAKIWA KUFUATA SHERIA KUEPUKA UDUKUZI WA MIFUMO

May 21, 2026 Add Comment
-Arusha

Wahasibu na wachumi wametakiwa kujijengea nidhamu ya kitaaluma kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni zilizowekwa ili kujiepusha na vitendo vya udukuzi wa mifumo ya kielektroniki na kulinda taarifa za Serikali.

KUELEKEA KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA NYUKI DUNIANI MKOANI TABORA

May 21, 2026 Add Comment
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi leo Mei 21, 2026 amekagua maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yanayotarajiwa kufanyika Kitaifa katika Uwanja wa Vita mkoani Tabora.

TANZANIA YAJIPANGA KUIMARISHA TEKNOLOJIA YA NYUKLIA

May 21, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu-Kigali, Rwanda


TUME ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia Barani Afrika (NEISA 2026) uliofanyika Mei 19, 2026 mjini Kigali, Rwanda, ukiwakutanisha viongozi wa kitaifa, wataalamu wa nishati, wawekezaji pamoja na mashirika ya kimataifa kujadili mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika.

Mkutano huo ulilenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nyuklia pamoja na kuvutia uwekezaji katika miradi ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uchumi endelevu.

Katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alisema Tanzania inaendelea kutathmini matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuongeza vyanzo vya nishati nchini.

Rais Samia alieleza kuwa teknolojia mpya za Small Modular Reactors (SMRs) na Micro Modular Reactors (MMRs) zinaweza kuwa suluhisho sahihi kwa nchi zinazoendelea kutokana na uwezo wake wa kuzalisha nishati kwa ufanisi na usalama zaidi.

Aidha, alitaja maeneo muhimu yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kuwa ni pamoja na mifumo imara ya udhibiti, wataalamu wenye ujuzi pamoja na usimamizi madhubuti wa usalama kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati yanahitaji maandalizi ya mifumo ya udhibiti, uwezo wa taasisi, upatikanaji wa fedha, uelewa wa wananchi na ushirikiano wa kikanda.

Katika ushiriki wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Profesa Najat Kassim Mohammed alihudhuria mkutano huo akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Nyuklia na Huduma za Ufundi, Dkt. Remigius Kawala.

Profesa Najat alipata fursa ya kushiriki kikao cha ndani kilichoongozwa na Rais Samia ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya nyuklia nchini pamoja na miradi inayotekelezwa na TAEC kwa kushirikiana na International Atomic Energy Agency.

Miongoni mwa mipango hiyo ni Rays of Hope unaolenga kuimarisha huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani nchini, Atoms4Food unaohamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta ya kilimo pamoja na ushiriki wa TAEC katika mpango wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa uzalishaji wa umeme.

Profesa Najat alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti, usalama na mafunzo ya wataalamu ili kuhakikisha matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda, utafiti wa madini na uzalishaji wa nishati.

Kupitia mkutano huo, TAEC ilipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu usalama wa nyuklia, mifumo ya udhibiti wa teknolojia za nyuklia pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kisasa ya nishati.

Aidha, ushiriki wa Tanzania katika NEISA 2026 uliendana na maono ya serikali ya kukuza sekta ya nishati na kuimarisha ushirikiano wa kikanda ndani ya Afrika Mashariki.

Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa Afrika walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza miradi ya nyuklia, kuongeza uwekezaji na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kwa ujumla, ushiriki wa TAEC katika NEISA 2026 umeiwezesha Tanzania kuendelea kujijengea nafasi katika mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika pamoja na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, kiteknolojia na kiuchumi kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Mkutano wa NEISA 2026 uliandaliwa kwa ushirikiano wa International Atomic Energy Agency, United Nations Economic Commission for Africa, World Nuclear Association pamoja na Rwanda.

MCHENGERWA: MAPAMBANO YA MALARIA YANAHITAJI NGUVU YA PAMOJA

May 21, 2026 Add Comment

Na John Mapepele,Geneva, Uswisi

Waziri wa Afya wa Tanzania, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kikanda katika mapambano dhidi ya malaria na Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele (NTDs), katika kikao maalum cha ngazi ya juu kilichofanyika sambamba na Mkutano wa 79 wa Shirika la Afya Duniani (WHA),akisisitiza kuwa udhibiti wa magonjwa hauwezi kufanikiwa bila hatua za pamoja zinazovuka mipaka ya mataifa.

MRADI WA NJIA YA KUSAFIRISHA UMEME CHALINZE–DODOMA KUKAMILIKA AGOSTI 2026 : MD TWANGE

May 21, 2026 Add Comment



Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Zuzu, Dodoma, unatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti 18, 2026.

Akizungumza Mei 20, 2026 wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo katika mikoa ya Morogoro na Dodoma, Bw. Twange amesema mradi huo ni muhimu kwa kuwa unasafirisha umeme unaozalishwa moja kwa moja kutoka katika Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere ambao unapita Chalinze hadi Dodoma.

Amesema utekelezaji wa mradi huo unaenda sambamba na upanuzi wa vituo vya kupokea na kupoza umeme vya Chalinze na Zuzu, Dodoma, ambapo kukamilika kwake kutaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme kwa ajili ya shughuli za uwekezaji pamoja na kuongeza fursa mbalimbali za kiuchumi nchini.

Amesema Serikali Chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa kiasi cha Shilingi Bil 514 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi huo ambao utachochea shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii kuendana na kasi ya ongezeko la mahitaji.

“Leo tumefanya ukaguzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma. Njia hii ni muhimu kwa kuwa inaongeza uwezo wa kusafirisha umeme kutoka Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere kwenda kwa watumiaji mbalimbali. Idadi ya watu imeongezeka na shughuli za kiuchumi zimeongezeka hivyo tumeingia makubaliano sasa mradi huu utakamilika Agosti 18, 2026,” alisisitiza Bw. Twange.

Ameeleza kuridhishwa na hatua iliyofikiwa huku akimtaka mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

“Tumekubaliana kuongeza wataalamu na vifaa vya kutosha ili kuhakikisha mradi huu unakamilika ndani ya muda ulioainishwa ,” ameongeza.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi, Mhandisi Newtone Lingstone, amesema mradi huo wenye urefu wa kilometa 345 Kutoka Chalinze hadi Dodoma unafadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Tanzania, huku kazi za upanuzi wa vituo vya kupokea na kupoza umeme vya Chalinze na Dodoma zikiendelea vizuri.

Kukamilika kwa mradi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma wenye msongo wa Kilovoti 400 utaimarisha na hali ya upatikanaji wa umeme si kwa Mkoa wa Dodoma pekee, bali katika maeneo mbalimbali nchini.