HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WALAJI KUNUFAIKA NA UZALISHAJI WA VIFAA VYA UJENZI WENYE VIWANGO

March 11, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam.

Tume ya Ushindani (FCC) imesema wazalishaji wa vifaa vya ujenzi wana wajibu wa kumlinda mlaji kwa kuhakikisha wanazalisha na kuuza bidhaa zenye ubora unaolingana na thamani ya fedha anayolipa mnunuzi.

FCC imeeleza kuwa ni muhimu kwa wazalishaji kuzingatia viwango vinavyotakiwa katika uzalishaji wa vifaa vya ujenzi ili kuepusha uwepo wa bidhaa zisizo na ubora sokoni, ambazo zinaweza kusababisha hasara kwa watumiaji na kudhoofisha imani ya wananchi katika bidhaa hizo.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa semina kwa wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuelekea kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani, Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa Inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC, Bi. Magdalena Utouh, kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, amesema ulinzi wa mlaji ni miongoni mwa majukumu makuu ya Tume hiyo.

Amesema FCC itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la bidhaa za ujenzi ili kuhakikisha haki za walaji zinalindwa na wananchi wanapata bidhaa salama na zenye ubora unaokidhi viwango vinavyotakiwa.

Bi. Utouh amewataka wazalishaji wa vifaa vya ujenzi kuendesha biashara zao kwa kuzingatia sheria na kanuni za ushindani wa haki, hatua ambayo itasaidia kujenga soko lenye ushindani wa kweli unaolinda maslahi ya walaji pamoja na kuchochea maendeleo ya sekta ya ujenzi nchini.

Ameeleza kuwa sekta ya ujenzi ni mhimili muhimu wa ukuaji wa uchumi wa taifa, hivyo uzalishaji wa vifaa vya ujenzi unapaswa kufanyika kwa kuzingatia viwango stahiki na thamani halisi ya fedha inayolipwa na mlaji.

“FCC ina jukumu la kufuatilia mwenendo wa ushindani katika soko ili kuhakikisha hakuna makubaliano ya kupanga bei miongoni mwa wafanyabiashara ambayo yanaweza kumuathiri mlaji,” amesema Bi.Magdalena

Amesema Tume haitavumilia vitendo vyovyote vinavyomuumiza mlaji, akisisitiza kuwa sheria na miongozo ya ushindani ipo wazi na wazalishaji wanapaswa kuizingatia kikamilifu.

Hata hivyo amesema mikutano na majadiliano kati ya FCC na wadau wa sekta ya ujenzi itaendelea kufanyika mara kwa mara ili kuimarisha ushindani wa soko na kuhakikisha walaji wanapata bidhaa na huduma bora.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa Shirikisho la Wamiliki wa Viwanda Tanzania (CTI), Bi. Neema Mhondo, amesema sekta ya ujenzi ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi pamoja na kutoa ajira kwa wananchi.

Hata hivyo, amesema wazalishaji wa ndani wanakabiliwa na changamoto ya uwepo wa bidhaa bandia sokoni, hali inayofanya viwanda vya ndani kupata ugumu katika ushindani kutokana na gharama kubwa za uzalishaji na uendeshaji wa biashara.

Semina hiyo ya siku moja imefanyika Machi 11, 2026 katika Ukumbi wa Mikutano wa Ngorongoro katika Ofisi za FCC, Jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh akizungumza wakati akifungua Semina ya Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.Meneja wa Kumlinda Mlaji wa FCC Joshua Msoma akitoa mada kwa wadau wa uzalishaji wa vifaa vya Ujenzi ikiwa ni muendelezo wa FCC kukutana na wadau kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani,jijini Dar es Salaam.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa FCC,Bi. Roberta Feruzi akitoa maelezo kuhusiana na Semina ya wadau uzalishaji wa vifaa vya Ujenzi ikiwa ni muendelezo wa FCC kukutana na wadau kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mlaji Duniani,jijini Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Huduma za Wanachama wa CTI Neema Mhondo akizungumza kwa niaba ya wadau kuhusiana na semina ya Wadau wa Uzalishaji wa wa vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.

Semina ikiendelea

Picha ya pamoja ya makundi mbalimbalj ya Mkurugenzi wa Udhibiti wa Mienendo ya Bidhaa inayokatazwa na Sheria ya Ushindani wa FCC Bi.Magdalena Utouh na Wadau wa Uzalishaji wa Vifaa vya Ujenzi ,jijini Dar es Salaam.

KILA MKUU WA MKOA ATATOA TAARIFA KUHUSU UKUZAJI BIASHARA - WAZIRI MKUU

March 11, 2026 Add Comment


 


*Asema waandae mapendekezo kuhusu utitiri wa taasisi za udhibiti na kodi
*Ataka yawasilishwe kwa Waziri wa Fedha, yaingizwe katika Muswada wa Sheria ya Fedha wa mwaka huu

WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba amewataka Wakuu wa Mikoa na watendaji wao katika mikoa yote nchini wajipange kutoa taarifa kuhusu uwekezaji na ukuzaji wa biashara kwenye mikoa yao kila wanapotoa taarifa kwa viongozi wa kitaifa.

“Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala na Wakurugenzi wa Halmashauri mbebe jukumu la kuwa mabalozi wa kwanza wa uwekezaji katika maeneo yenu kwa kutambua na kutangaza fursa mbalimbali zilizopo katika maeneo yenu.”



“Tubebe hili jukumu, kila Mkuu wa Mkoa anapotoa taarifa atapaswa aseme ameongeza uwekezaji kwa kiasi gani, amekuza biashara kwa kiasi gani na katika kuongeza biashara mpya

Ametoa wito huo leo jioni (Jumatano, Machi 11, 2026) wakati akifunga Mkutano wa Kuhakiki Rasimu ya Pili ya Mpango wa Kuboresha Mazingira ya Biashara na Uwekezaji (Mkumbi II) uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage, HAZINA, jijini Dodoma.

Amesema mapendekezo yote yaliyowasilishwa na washiriki wa mkutano huo ambao ni Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa pamoja na Wakurugenzi yaandaliwe katika mfumo wa mkakati wa utekelezaji ili kuwezesha utekelezaji wake kwa ufanisi.



“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alishasema isiwepo sheria inayoleta kikwazo katika utendaji kazi wa serikali. Haya tuliyoyabaini, tuyaweke kwenye majedwali na kubainisha lipi ni kikwazo na lipi limefanyika. Leteni hayo mapendekezo.”

“Kuhusu suala la utitiri wa taasisi za udhibiti na kodi, andaeni mapendekezo mahsusi na yawasilishwe kwa Waziri wa Fedha ili yaweze kuingizwa katika Muswada wa Sheria ya Fedha (Finance Bill) wa mwaka huu. Hatua hii inalenga kuwa sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini,” amesema.



Pia amezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa zihakikishe zinaondoa urasimu katika kuanzisha biashara mpya au viwanda vipya katika maeneo yao. “Kufanya hivyo, kutasaidia kuchochea upatikanaji wa ajira mpya kwa vijana, kukuza kipato kwa wawekezaji na wafanyabiashara pamoja na kukuza pato la Taifa.”

Amezitaka mamlaka hizo ziweke mikakati ya kushughulikia changamoto mbalimbali zikiwemo za tozo zisizo rafiki kwa sekta binafsi. “Ni dhahiri kuwa Serikali pekee haiwezi kufanikisha malengo haya bila ushiriki mpana na madhubuti wa sekta binafsi,” amesema.

Mapema, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof. Kitila Mkumbo aliwashukuru Wakuu wa Mikoa yote kwa ushirikiano wao na jinsi walivyolipa kipaumbele suala la uwekezaji kwenye maeneo yao.

Alisema ofisi yake kwa kushirikiana na Waziri wa Nchi, OWM – TAMISEMI wanaandaa nyenzo za kushindanisha mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa (Ease of Doing Competitive Business) katika kuvutia uwekezaji na kulinda biashara.

“Kupitia hii kila mkoa utapimwa jinsi wanavyowezesha biashara na kuvutia uwekezaji ili kuona wanakuza vipi biashara katika maeneo yao. Na watapimwa ufanisi wao kila mwaka mara moja,” alisema.

Naye, Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar aliwaeleza washiriki wa mkutano huo kwamba matarajio ya Serikali kwenye utekelezaji wa DIRA 2050 unaendana na MKUMBI II kwenye maeneo yao.

“Uchumi wa nchi yetu kwa sasa ni dola za Marekani bilioni 100 tukichanganya uzalishaji wa bidhaa zetu zote, huduma na biashara za ndani na za nje angalau kwa hesabu za mwaka jana. Katika miaka 25 ijayo, tunataka tufikie dola za Marekani trilioni moja, maana yake tukue zaidi ya mara 10.”

“Ili tufike huko hatupaswi kwenda kama ilivyo sasa, tunapaswa kubadilika sana na tuongeze bidii siyo tu uchumi ukue bali uwe wa kisasa pia,” alisema.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
JUMATANO, MACHI 11, 2026.

BALOZI MBUNDI AKUTANA NA WASHIRIKI WA KOZI YA 14 KUTOKA CHUO CHA TAIFA CHA ULINZI (NDC)

March 11, 2026 Add Comment

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Stephen Mbundi amekutana na Washiriki wa Kozi ya 14 kutoka Chuo cha Taifa cha Ulinzi  (NDC) waliotembelea Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mtumba jijini Dodoma kwa ziara ya Mafunzo.


Akizungumza katika kikao na wanachuo hao Mhe. Balozi Mbundi alieleza kufurahishwa kwake na ziara hiyo ambayo inawapatia mafunzo kwa vitendo wanachuo hao na kusisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa, majadiliano ya kimkakati, na mbinu za pamoja kama nyenzo za kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia.

Alisema kuwa mazingira ya usalama duniani yanabadilika kutokana na changamoto mbalimbali kama za mivutano ya kisiasa kati ya mataifa, uhalifu wa kuvuka mipaka, ugaidi, vitisho vya mtandao, mabadiliko ya tabianchi na za kiuchumi.

Aliongeza kuwa ni matumaini yake ziara hiyo itachangia kuimarisha uelewa wa washiriki kuhusu uhusiano kati ya diplomasia, usalama wa taifa na ushirikiano wa kimataifa na kuimarisha ushirikiano kati ya Wizara ya Mambop ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Chuo hicho.

Katika kikao hicho Balozi Mbundi alielezea kwa ufupi historia, majukumu, dira na dhamira ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki katika kusimamia sera ya mambo ya nje, kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia, na kukuza ushirikiano wa kikanda kupitia taasisi kama Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Afrika.

Naye Mwakilishi wa Mkuu wa Chuo cha NDC,  Brigedia Jenerali Selemani Bakari Gwaya alieleza kuridhishwa kwao na mchango wa Wizara katika kufanikisha kozi mbalimbali zinazotolewa na chuo hicho ambao unakiwezesha kukua kimataifa na kuaminika kama  taasisi ya kimkakati.

Amepongeza juhudi za Wizara kwa kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi kwa weledi na Vitendo licha ya changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika siasa za kimataifa.

Wanachuo 72 wa Kozi ya 14 ya NDC kutoka nchi 17 za Tanzania, Bangladesh, Botswana, Burundi, Misri, Ethiopia,India, Kenya, Malawi, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sierra Leone, Afrika Kusini, Uganda, Zambia na Zimbawe waliambatana na Wakufunzi na Viongozi wao walifika Wizarani kwa lengo la kujifunza jinsi Wizara inavyotekeleza majukumu yake.

WAZIRI NDEJEMBI AFANYA KIKAO KAZI NA TAASISI ZILIZOPO CHINI YA WIZARA YA NISHATI

March 11, 2026 Add Comment

 


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, leo Machi 11, 2026 amefanya kikao kazi cha pamoja na taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati zinazoshughulikia masuala ya mafuta. Kikao hicho kimefanyika katika Ofisi za Wizara ya Nishati, Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, Mkurugenzi Mtendaji wa EWURA, Dkt. James Mwainyekule, pamoja na wataalamu kutoka wizarani na taasisi za TPDC na PBPA.


Lengo la kikao hicho ni kuimarisha ufanisi na usimamizi katika utekelezaji wa majukumu ya taasisi hizo, ili kuboresha utendaji na maendeleo ya sekta ya mafuta nchini.



REA YATOA ZAIDI YA BILIONI 5 KUZALISHA UMEME WA MAJI LUPALI

March 11, 2026 Add Comment





Na Mwandishi Wetu - Njombe

Wakala wa Nishati Vijijini (REA), imetoa kiasi cha shilingi bilioni 5.4 kwenye mradi wa kuzalisha umeme wa maji Lupali wenye uwezo wa kuzalisha kilowati 317 unaotekelezwa na shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent Imiliwaha.

Hayo yamebainishwa leo Machi 11, 2026 wakati wa ziara ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) walipotembelea mradi wa Lupali unaotumia nguvu ya maporomoko madogo ya maji ya mto Lupali katika kuzalisha umeme mkoani Njombe.


Akiwaeleza TEF utekelezaji wa mradi huo, Kaimu Meneja Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji wa Mradi kutoka REA, Mha. Emmanuel Yessaya amesema Serikali kupitia REA imetoa ruzuku kwa awamu tano zenye jumla ya shilingi za kitanzania bilioni 5.4.


Ameongeza kuwa, mradi wa kuzalisha umeme wa Lupali wenye uwezo wa kuzalisha Kilowati 317 unatekelezwa na Shirika la Benedictine Sisters of St. Gertrud Convent Imiliwaha.


Aidha, fedha zilizotolewa na REA zimewezesha ujenzi wa kituo cha uzalishaji wa umeme na miundombinu ya usambazaji kwenye kituo cha Imiliwaha Sisters Convent pamoja na vijiji vya jirani vya Boimanda, Kitulila na Matola sambamba na kuwezesha tafiti za mradi huo.

Vile vile utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 99 ambapo kazi zilizotekelezwa hadi sasa ni pamoja na ujenzi wa kizuizi cha maji na mtaro wa kupitisha maji ya mafuriko ambao tayari umekamilika.


Naye, Mwenyekiti wa TEF, Bw. Deodatus Balile ameipongeza REA kwa kuweka kiasi kikubwa cha fedha takribani shilingi bilioni 5.4 za kuendeleza na kutekeleza mradi huo ambao unakwenda kuongeza ubora na upatikanaji wa umeme mkoa wa Njombe.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi Sista Imakulata Mlowe, amesema kuwa mara baada ya mradi kukamilika, umeme utakaozalishwa utauzwa moja kwa moja kwa TANESCO ambapo tayari mkataba wa kuuziana umeme umeshasainiwa.

Ameongeza faida za mradi utakapokamilika utaongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa wananchi kwa matumizi ya nyumbani na biashara na kupinguza matumizi ya nishati isiyo rafiki na mazingira.


Ziara hiyo ya TEF mkoani Njombe imelenga kupitia utekelezaji wa miradi ya REA inayotekelezwa katika huo sambamba na kupitia maendeleo ya waendelezaji wadogo wa miradi ya kuzalisha umeme hapa nchini na kupatiwa ufumbuzi.

.

MARY CHATANDA ATIMIZA AHADI YA NG'OMBE WAWILI KWA MAGEREZA

March 11, 2026 Add Comment


Na: Mwandishi Wetu, KOROGWE

Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa (MCC) na Mbunge wa Viti Maalum wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM, Mary Chatanda, ametimiza ahadi yake ya kutoa ng'ombe wawili wa maziwa kwa Magereza mawili ya wilayani Korogwe mkoani Tanga.

Hafla hiyo imefanyika Machi 09, 2026, ambapo viongozi wa CCM ngazi ya wilaya walimwakilisha Chatanda Katika kukabidhi ng'ombe hao. Katika Gereza la Kwamngumi viongozi wa Chama walikabidhi ng'ombe wa maziwa kwa kikundi cha wake wa Askari Magereza huku ng'ombe mwingine akikabidhiwa kwa uongozi wa Gereza la Manundu.

Akizungumza katika makabidhiano hayo, Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Korogwe, Thobias Nyakusagira alisema "Utoaji wa ng'ombe hawa ni utekelezaji wa ahadi ya Mama Mary Pius Chatanda baada ya kufanya ziara Magerezani na akapokea changamoto na leo tupo hapa kutekeleza ahadi yake." 

Kwa upande wa Katibu wa CCM wilaya Korogwe Mjini, Evarist Mluge alisema "Mama Chatanda wakati wa ziara yake ya kuimarisha Chama, alitembelea makundi maalum yakiwemo wanawake na wafungwa ambapo alipokea maombi ya ng'ombe wa maziwa na leo tuna furaha kuwa ahadi yake ameitekeleza kwa vitendo."


Katika hatua nyingine, viongozi wa kikundi cha wake wa Askari Magereza wamemshukuru Mama Chatanda kwa kuwaunga mkono katika jitihada zao za kujikomboa kiuchumi kwani ng'ombe huyo atawasaidia kuongeza kipato chao. Katika hatua nyingine, uongozi wa Gereza la Manundu wameahidi kumtunza ng'ombe huyo kwani atasaidia kupatikana maziwa yatakayosaidia kuimarisha afya za wafungwa.

Viongozi wengine waliohudhuria hafla hiyo ni pamoja na Mwenyekiti wa UWT wilaya, Faida Bayagumu, Katibu wa UWT wilaya, Suzan Mandia na Diwani wa Kata ya Kilole ambaye pia ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Korogwe Ally Mkwavingwa. Viongozi hao wamesisitiza kushirikiana na Magereza hayo katika kutatua changamoto zao kwani hayo ndiyo maelekezo ya Chama chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake Taifa, Dk. Samia Suluhu Hassan ya kutatua changamoto za wananchi kwa wakati ili kujenga ustawi wao.