HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

KAMPASI YA TPSC TABORA YATOA MISAADA NA KUFANYA USAFI – KITUO CHA WAZEE IPULI-TABORA

February 22, 2026 Add Comment
Katika kuelekea kilele cha maadhimisho ya miaka 25 ya Chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania (TPSC), Kampasi ya Tabora imefanya ziara ya kijamii katika Kituo cha Kulelea Wazee wenye Mahitaji Maalum kilichopo Ipuli, Manispaa ya Tabora. Ziara hiyo ilikuwa ni sehemu ya mikakati ya chuo kuimarisha ushirikiano na jamii.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Tabora, Bi. Asha Churu, kwa kushirikiana na Mkurugenzi wa Kampasi ya Tabora, Dkt. Joseph Mbwillo, wameongoza timu  ya watumishi na wanachuo wa Kampasi ya Tabora kutembelea kituo hicho katika kujali na kusaidia wazee wenye mahitaji maalum.
Lengo kuu la ziara lilikuwa ni kuwapelekea misaada mbalimbali kwa wahitaji hao, ikiwa ni pamoja na mchele, maharage, mafuta ya kupikia na mafuta ya kujipaka, sabuni za kuogea na kufulia, nguo, sukari, mashuka pamoja na nguo katika kuboresha maisha ya wazee hao.
Pamoja na kutoa misaada hiyo, timu hiyo pia ilifanya kazi ya usafi wa mazingira ya makazi ya wazee pamoja na  zoezi la upandaji miti katika eneo hilo kwa lengo la kuimarisha ustawi wao na kuhifadhi mazingira kwa ujumla.
Ziara hii ni sehemu kuelekea kilele cha maadhimisho ya mika 25 ya chuo cha Utumishi wa Umma Tanzania kwa kuonyesha mfano wa jamii inayojali na kuendeleza mazingira kwa manufaa ya wote.
 
 
 
 
 
 
UJENZI WA KIWANDA CHA KUCHAKATA PAMBA SIMCU (2018) LTD WAFIKA ASILIMIA 75

UJENZI WA KIWANDA CHA KUCHAKATA PAMBA SIMCU (2018) LTD WAFIKA ASILIMIA 75

February 21, 2026 Add Comment

Naibu Mrajis - Uhamasishaji, Consolata Kiluma, amekipongeza chama kikuu cha Ushirika SIMCU (2018) LTD, kwa usimamizi wa ujenzi wa ujenzi na ukarabati wa kiwanda cha kuchakata pamba kilichopo wilayani Maswa mkoa wa Simiyu ambacho kinatarajiwa kuanza kazi musimu huu wa 2026/2027.

Ametoa pongezi hizo leo Februari 21, 2026 alipofanya ziara katika chama hicho kwa lengo kukagua na kuona hatua zilizofikiwa za ujenzi kuelekea uzinduzi wake.

Aidha amewataka viongozi wa SIMCU (2018) LTD, kuendelea kufufua viwanda vingine vinavyomilikiwa na chama ambavyo havifafanyi kazi kwa sasa ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirika wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao ya wakulima.

Naye, Mwenyekiti wa SIMCU (2018) LTD, Ramadhani Matani, amesema juhudi mbalimbali zinaendelea kuhakikisha kiwanda kinaanza kufanya kazi haraka iwezekanavyo ambapo mpaka sasa wamefikia zaidi ya asilimia 75 ya ujenzi wa kiwanda hicho.

ELIMU YA VIPIMO YAWAFIKIA WANAFUNZI WA SHULE YA SEKONDARI DR. SAMIA DODOMA

ELIMU YA VIPIMO YAWAFIKIA WANAFUNZI WA SHULE YA SEKONDARI DR. SAMIA DODOMA

February 21, 2026 Add Comment

Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) imetoa mafunzo ya vipimo kwa wanafunzi wa Dr. Samia Dodoma Secondary School, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi katika biashara na maisha ya kila siku.

Katika zoezi hilo, wanafunzi walipata fursa ya kujifunza kuhusu dhima na majukumu ya Wakala huo, pamoja na namna unavyolinda maslahi ya watumiaji na wafanyabiashara kwa kuhakikisha vipimo vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa WMA, Veronica Simba, amesema elimu ya vipimo itatolewa katika mikoa yote ya Tanzania Bara ili kuhakikisha wanafunzi wengi zaidi wanapata uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo.

Amesema mpango huo unalenga kukuza uelewa wa masuala ya vipimo kwa vijana, sambamba na kuimarisha utamaduni wa uadilifu na uwajibikaji katika sekta ya biashara nchini.

Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Dodoma, Said Ibrahim, amesema mafunzo hayo yanaenda sambamba na uanzishwaji wa Klabu za Vipimo mashuleni ili kuendelea kuandaa mabalozi mahiri watakaotoa elimu ya vipimo shuleni na katika jamii kwa ujumla.

“Kwa Dodoma tayari tumeshatoa mafunzo katika shule mbili ambazo ni Shule ya Msingi Mtemi Mazengo na leo tumetoa hapa katika Shule ya Sekondari ya Dkt. Samia Dodoma. Tunaamini mabadiliko katika matumizi ya vipimo sahihi yataongezeka,” amesema Said.

Kwa upande wake, Mwalimu Mussa Madandi, ambaye pia ni mlezi wa Klabu ya Vipimo shuleni hapo, amesema elimu hiyo wamekuwa wakiifundisha darasani, lakini mafunzo yaliyotolewa na WMA yamewapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo, jambo litakalosaidia kuongeza uelewa na kuimarisha matumizi ya vipimo sahihi.

“Vipimo ni somo tunalolifundisha karibu kila darasa, lakini leo wanafunzi wamepata mafunzo kwa vitendo kutoka kwa wataalamu wenyewe. Naamini hali hii itaongeza hamasa ya kuzingatia usahihi katika matumizi ya vipimo na kuwafanya wawe mabalozi wazuri kwa wazazi wao na jamii inayowazunguka,” amesema Mwalimu Madandi.

Naye mwanafunzi Itabangola Elias amesema elimu hiyo imewasaidia kuelewa namna ya kutambua vipimo sahihi na kujikinga dhidi ya udanganyifu unaoweza kujitokeza katika biashara.

Baada ya mafunzo hayo, wanafunzi walishiriki kujibu maswali mbalimbali kuhusiana na vipimo na shughuli za Wakala huo, ambapo waliofanya vizuri walipatiwa zawadi mbalimbali kama sehemu ya kuwahamasisha kuendelea kujifunza na kuwa mabalozi wa matumizi sahihi ya vipimo katika jamii.

JAFO ASISITIZA UKAMILISHAJI WA DARAJA KITOMONDO KUCHOCHEA MAENDELEO KISARAWE

JAFO ASISITIZA UKAMILISHAJI WA DARAJA KITOMONDO KUCHOCHEA MAENDELEO KISARAWE

February 21, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu

MBUNGE wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Dkt. Selemani Jafo, ametangaza mpango wa kuweka kambi maalum katika eneo la ujenzi wa Daraja la Kitomondo lililopo katika barabara ya Mzenga–Gwata, akilenga kuharakisha ukamilishaji wa mradi huo na kuondoa adha wanazokumbana nazo wananchi hasa nyakati za mvua.

Dkt. Jafo alitoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kata za Mzenga na Mafizi ndani ya Jimbo la Kisarawe, ambapo alikagua maendeleo ya mradi huo na kusikiliza changamoto za wananchi wanaotegemea daraja hilo kwa shughuli za kila siku.

Daraja la Kitomondo linajengwa na kampuni ya Neloyt Tanzania Limited kwa gharama ya shilingi milioni 359.67 chini ya usimamizi wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), hata hivyo ujenzi wake umechelewa kukamilika hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi wa Mzenga na Mafizi.

Mbunge huyo amesema daraja hilo ni kiungo muhimu kwa wakazi wa kata hizo na vijiji vya Mafizi, Nyani, Gwata na Ving’andi, akieleza kuwa kuchelewa kwake kumeathiri shughuli za kiuchumi na kijamii ikiwemo usafiri wa wanafunzi, wagonjwa na wafanyabiashara.

Amesisitiza kuwa kukamilika kwa daraja hilo kutarahisisha usafiri na usafirishaji wa mazao na bidhaa, hivyo kuchochea maendeleo katika Jimbo la Kisarawe.

Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Kisarawe, Eng. Africano Orota, amemhakikishia Dkt. Jafo kuwa wataongeza usimamizi na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.

VIJANA 51 KUTOKA KATA ZOTE 17 KISARAWE KUNUFAIKA NA UFADHILI WA MASOMO YA UFUNDI  KUPITIA JAFO EDUCATION FOUNDATION

VIJANA 51 KUTOKA KATA ZOTE 17 KISARAWE KUNUFAIKA NA UFADHILI WA MASOMO YA UFUNDI KUPITIA JAFO EDUCATION FOUNDATION

February 21, 2026 Add Comment

Na.Mwandishi Wetu

Taasisi ya Jafo Education Foundation imefadhili jumla ya vijana 51 kusoma katika Chuo cha FDC Kisarawe - Mzenga, kwa lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa fani mbalimbali za ufundi.

Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi na kuzungumza na wananchi katika Kata ya Mzenga, Mbunge wa Jimbo la Kisarawe Mhe.Dkt. Selemani Jafo, amesema vijana hao 51 watatoka katika kata zote 17 za wilaya hiyo na taasisi hiyo itagharamia ada zao za masomo.

 "Hii ni fursa muhimu kwa vijana wa Kisarawe kujipatia ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiriwa, hasa katika kipindi hiki ambacho soko la ajira linahitaji wataalamu wenye ujuzi wa vitendo."amesema Dkt. Jafo

Dkt.Jafo amesema kuwa Chuo cha FDC Kisarawe – Mzenga ni chuo kipya kilichojengwa wilayani humo na tayari kinatoa mafunzo katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ushonaji, ujenzi, mapishi, umeme, kompyuta pamoja na mafunzo ya muda mfupi.

Aidha, Dkt. Jafo ameeleza kuwa tangu mwaka 2010 amefanikiwa kusaidia zaidi ya vijana 500 kutoka familia zenye changamoto kusoma katika ngazi mbalimbali, ikiwemo kidato cha tano, astashahada, stashahada na shahada.

Katika kuendeleza juhudi za kukuza elimu ya ufundi, tarehe 20 Februari, Dkt. Jafo kupitia taasisi yake amekabidhi msaada wa vyerehani vinne vya umeme katika chuo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan.

Amesema kuwa dhamira kuu ni kuwawezesha vijana katika fani za ufundi ili kujenga msingi imara wa ajira rasmi na zisizo rasmi, pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Wilaya ya Kisarawe.

Oryx Gas Yazindua “Pishi la Kibabe” Ramadhan na Kwaresma

February 20, 2026 Add Comment
Katika kipindi hiki cha Ramadhan na Kwaresma kinachosisitiza ibada, mshikamano na kujitafakari, Oryx Gas Tanzania imezindua kampeni ya “Pishi la Kibabe” yenye lengo la kurahisisha upatikanaji wa nishati safi ya kupikia.

TVLA YATOA ELIMU YA MATUMIZI SAHIHI YA CHANJO ZA MIFUGO KWA WAUZAJI WA PEMBEJEO SINGIDA

February 20, 2026 Add Comment

Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA) Kanda ya Kati, Dodoma, Dkt. Japhet Nkangaga (kushoto), akipokea changamoto mbalimbali zinazowakabili wafugaji kutoka kwa muuzaji wa pembejeo za mifugo Manispaa ya Singida, Bi. Ester Munuo, tarehe 19 Februari 2026 mkoani Singida, wakati wa ziara ya uhamasishaji kwa wauzaji wa pembejeo za mifugo iliyolenga kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya chanjo ya Matone (TEMEVAC) na taratibu za upatikanaji wa leseni za uuzaji wa viuatilifu vya rejareja na jumla.

RUWASA YAKUTANA NA WADAU KUJADILI MPANGO MKAKATI MIAKA MITANO IJAYO

February 20, 2026 Add Comment


Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) imekutana na wadau wake wa ndani na nje ya nchi ikiwemo Wizara ya Maji na Benki ya Dunia katika kikao cha kujadili Mpangomkakati wa miaka mitano wa taasisi hiyo unaotoa mwelekeo wa vipaumbele vya kuimarisha huduma endelevu ya Maji safi ya bomba kwa wakazi wa maeneo ya vijijini katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Akifungua kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Februari 20, 2026, mwakilishi kutoka Wizara ya Maji Mha. Mashaka Sitta ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi wa Uendeshaji na Matengenezo alisema mwelekeo wa RUWASA kuelekeza nguvu zaidi katika kuimarisha huduma endelevu ya maji ni jambo muhimu kwa sasa kwani tayari imeshajenga miradi mingi vijijini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu wa RUWASA Titus Mkapa ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu Mha. Wolta Kirita aliwapongeza na kuwashukuru wadau wote wa maendeleo wanaoshirikiana na taasisi hiyo ambapo alisema baadhi ya vipaumbele katika kipindi cha miaka mitano ijayo ni pamoja na kuhakikisha huduma ya maji vijijini inakuwa imara na endelevu pamoja na kuimarisha eneo la data na takwimu.

Akitoa maelezo ya awali, Mkurugenzi wa Mipango wa RUWASA Enock Wagala alisema kuwa, nyaraka hiyo ya Mpangomkakati wa miaka mitano imeshapitia hatua tofauti za maandalizi na sasa inawasilishwa kwa wadau wa maendeleo hususan wa maji vijijini ili watoe maoni na michango yao katika kuboresha na kuwa sehemu muhimu ya mpangomkakati huo wakati wa utekelezaji wake.

Mkurugenzi Wagala alitaja maeneo makuu Matano ambayo yamepewa kipaumbele zaidi katika Mpangomkakati huo kuwa ni pamoja na uendelevu wa huduma ya maji vijijini, kujenga miradi katika vijiji 1575 vilivyobaki, kuimarisha mbinu za upatikanaji wa fedha, kukamilisha ujenzi wa miradi 878, na kujenga na kuimarisha huduma za usafi wa mazingira vijijini.

Takribani taasisi za wadau 40 walihudhuria kikao hicho ambapo baadhi ya wadau hao ni Wizara ya Maji, Benki ya Dunia, AfDB, Oikos ETS, Water Mission Tanzania, Global Water Center, TAWASANET, Water for Pepople, Netherland Development Organization, UNICEF, CRDB, World Vision Tanzania, Benki ya Equity, NMB, Global Water Partnership Tanzania na DPG WASH Secretariet.








WAKULIMA WA PAMBA WASHAURIWA KUACHA KILIMO CHA MAZOEA NA KULIMA KWA TIJA ZAIDI

WAKULIMA WA PAMBA WASHAURIWA KUACHA KILIMO CHA MAZOEA NA KULIMA KWA TIJA ZAIDI

February 20, 2026 Add Comment
 

Wakulima wa zao la pamba mkoa wa Simiyu ambao ni wanachama wa Vyama vya Ushirika wameshauriwa kulima kwa tija kwa kutumia teknolojia ya kisasa na kuepukana kilimo cha mazoea ambacho kinawapa hasara.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha katika Mkutano wa 8 Chama Kikuu Simiyu, SIMCU (2018) LTD, uliofanyika leo Februari 20, 2026 Wilayani Maswa Mkoa wa Simiyu, pia amewaahakikishia wakulima kuwa Serikali itaendelea kuwawezesha kwa kutoa rudhuku za mbolea, viuatilifu na kutafuta masoko ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo.

"Mkulima anapata kilo mia tatu za pamba kwa heka ni hasara na ni upotevu wa muda inabidi tutoke kwenye kilimo cha namna hii..." alisema Mhe. Macha

Akizungumza kwa niaba ya Mrajis wa Vyama vya Ushirika nchini, Consolata Kiluma, ambaye ni Naibu Mrajis - Uhamasishaji, amewasistiza wajumbe wa bodi za vyama vya Ushirika kuwa waadilifu na waaminifu katika kutekeleza majukumu, na kuwa wabunifu kuleta ushindani kwenye biashara kama kauli mbiu isemavyo "Ushirika ni Biashara" ili kuongeza mapato kwa maslahi ya wanaushirika na Wananchi kwa ujumla.

Aidha, Mrajis Msaidizi Mkoa wa Simiyu Godfrey Mpepo amesema Ushirika umeendelea kuimarika tangu kilipoanzishwa chama kikuu SIMCU Ltd mwaka 2018, ambapo awali vyama vya mkoa huo vilikuwa vikisimamiwa na SHIRECU chama kikuu kutoka mkoa wa Shinyanga.

Naye, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Shemsha Mohamed amewataka wajumbe wa Mkutano huo kuepuka na ubadhilifu wa fedha za wanachama jambo ambalo linarudisha Ushirika nyuma kimaendeleo.

Awali, akitoa taarifa ya Utendaji wa SIMCU(2018) LTD, Meneja Mkuu wa chama hicho, Mercy Atanazi alibainisha kuwa mkutano huo umehudhuriwa na wajumbe 625 kati ya wajumbe 675 kutoka vyama wanachama 335.