HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

AJIRA ZA WAZAWA ZILINDWE : CI NYAKUNGA

July 12, 2026 Add Comment
Na. OWM (KAM), Dar es Salaam

Kamishna wa Uhamiaji wa Divisheni ya Usimamizi na Udhibiti wa Mipaka, CI Fakih Nyakunga, ameiomba Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) kupitia Idara ya Kazi kuhakikisha vibali vya kazi vinatolewa kwa raia wa kigeni wenye ujuzi ambao haupatikani nchini Tanzania ili kulinda ajira za wazawa.

DKT. BATILDA BURIAN ATOA WITO WA KUTEMBELEA BANDA LA OFISI YA WAZIRI MKUU

Kajunason July 12, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian ametoa wito kwa wananchi kuendelea kujitokeza kupata elimu ya masuala mbalimbali katika Banda Jumuishi la Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara (Sabasaba 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam. 

Ametoa wito huo hii leo (12 Julai, 2026)
alipotembelea na kujionea namna ofisi hiyo inavyoendelea kutoa huduma kwa wananchi na kuwasihi waendelee kujitokeza kwa wingi na kupata taarifa na huduma zinazotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zake.
Dkt. Batilda amepongeza namna Ofisi ya Waziri Mkuu ilivyojipanga na kuhakikisha inawafikia wananchi kwa utoaji wa huduma bora na kuzingatia viwango huku wakiendelea kutatua changamoto mbalimbali kwa jamii kupitia maonesho hayo.

Aidha amewakumbusha watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kuwa na program mbalimbali za elimu kwa umma ili kuifikia jamii kwa ukumbwa wake na kuendelea kutangaza huduma zinazotolewa.
Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam yanaendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere chini ya kaulimbiu isemayo, "Maonesho ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba ni Fahari ya Tanzania," yakilenga kukuza biashara, uwekezaji na ubunifu, nchini.

KWAGILWA AFUNGIA KIWANDA CHA HANGJIN STEEL MKURANGA KWA UKIUKWAJI WA SHERIA ZA MAZINGIRA

July 12, 2026 Add Comment
Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Reuben Kwagilwa, amesimamisha shughuli za Kiwanda cha Hangjin Steel kinachojihusisha na uzalishaji wa nondo kwa kutumia vyuma chakavu, kilichopo Wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani, baada ya kubainika kukiuka masharti ya Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira.

WAZIRI WA FEDHA MGENI RASMI HALFA YA ULENGE KUGAWA MIGUU BANDIA 100 TANGA,MBUNGE AFUNGUKA "NAREJESHA FADHILA"

July 12, 2026 Add Comment



Na Mwandishi wa diGOtv, Tanga


WAZIRI wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Musa Omar (Mb) anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika hafla kubwa na ya kihistoria ya ugawaji wa miguu bandia 100 kwa watu wenye ulemavu mkoani Tanga, iliyoandaliwa na Ofisi ya Mbunge wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Mhandisi Mwanaisha Ulenge.


Hafla hiyo kubwa inatarajiwa kufanyika *Jumanne, tarehe 14 Julai 2026*, katika ukumbi wa *Regal Naivera* jijini Tanga kuanzia saa 2:00 asubuhi.


Hatua hii inamfanya Mhe. Mhandisi Ulenge kuweka rekodi ya kuwa Mbunge wa kwanza mkoani Tanga kufanya shughuli kubwa za kijamii na kugusa maisha ya watu moja kwa moja tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu mwaka jana. Utendaji huu unaendelea kumuweka karibu zaidi na makundi mbalimbali mkoani humo kutokana na utu wake na dhamira ya dhati ya kulipa fadhila kwa kura nyingi alizopigiwa.


Akizungumzia msukumo wake wa kuandaa tukio hilo linalogusa maisha ya wanyonge, Mhe. Ulenge ameweka wazi kuwa yeye ni mtumishi wa wananchi na anachokifanya ni kurudisha fadhila kwao.


"Hii nafasi niliyokuwa nayo ni ya watu. Kurejesha kidogo ninachopata pamoja na wadau wangu ni jambo kubwa kwangu, kwa sababu watu ndiyo walionifikisha hapa," alisema Mhe. Ulenge kwa hisia.


*Mafunzo ya Sheria ya Asilimia 30 (Manunuzi ya Umma)*

Ukiachilia mbali zoezi la ugawaji wa miguu hiyo bandia ili kuwarudishia uwezo wa kutembea, hafla hiyo itakwenda sambamba na utoaji wa mafunzo maalum kwa makundi maalum (Vijana, Wanawake, na Watu wenye Ulemavu). 


Kwa kuwa Mgeni Rasmi ni Waziri wa Fedha anayesimamia sera za kiuchumi, mafunzo hayo yatalenga kuwajengea uwezo washiriki namna ya kunufaika na *Sheria ya asilimia 30 (30%) ya Manunuzi ya Umma*. Lengo ni kuwapa uelewa utakaowawezesha kupata zabuni za kiserikali na kujikwamua kiuchumi badala ya kutegemea misaada pekee.


Wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo wanaendelea kupongeza hatua hii ya Mhe. Ulenge, huku maandalizi ya kumpokea Waziri wa Fedha na kukamilisha zoezi hili yakiwa yamepamba moto jijini Tanga.

MBUNGE KILINDI,KITETO WAENDELEZA UJIRANI MWEMA MIRADI YA MAENDELEO

July 12, 2026 Add Comment


Katika kuonesha ujirani mwema Mbunge wa Kiteto Edward Ole Lekaita na Mbunge wa Kilindi Salehe Mhando wameamua kushirikiana kuhakikisha barabara ya Lengatei- Songe inatengenezwa kwa kiwango cha changarawe na kupitika kwa mwaka mzima.

Mbali ya kushirikiana kusimamia Ujenzi wa barabara hiyo pia Wabunge hao wameshiriki shughuli ya uzinduzi wa shule ya awali na msingi Kijiji cha Lesiot Kata ya Lengatei Kiteto.



MAGOTI AIPONGEZA TET KWA MABORESHO YA MITAALA

July 12, 2026 Add Comment
Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Mhe. Petro Magoti ameipongeza Taasisi ya Elimu Tanzania kwa namna ilivyofanya maboresho ya mitaala ya Elimu nchini yenye lengo la kumfanya muhitimu kuweza kujiajiri au kuajiriwa mara anapomaliza masomo yake.

Mhe. Magoti ameyasema hayo leo tarehe 13/7/2026 katika maonesho ya Sabasaba ambapo amesema kuwa TET inafanya kazi nzuri ya kuboresha elimu nchini.

"Kwa kweli nawapongeza kwa kazi nzuri ya kuboresha Elimu nchini hasa hivi karibuni katika maboresho ya mitaala yaliyofanyika, ni tumaini langu kwamba wanafunzi nchi nzima wataendelea kufanya vyema, "amesema mhe. Magoti.

Pia ameeleza, anafurahia namna wanafunzi wanaendelea kupatiwa vitendea kazi kama vitabu vinavyowapelekea kuendele kufanya vyema wakati wa masomo yao na kuendelea kuipongeza TET kwa uratibu mzuri na upatikanaji wa vitabu mashuleni.

TET inashiriki katika maonesho ya Kimataifa ya biashara maarufu kama Sabasaba yaliyoanza tarehe 28,Juni ambapo yanatarajiwa kufungwa hapo kesho,Julai 13.

UBIA WA BARRICK NA TWIGA WAZIDI KUWA KIOO CHA USHIRIKIANO WA SERIKALI NA SEKTA BINAFSI TASNIA YA MADINI

July 12, 2026 Add Comment

  

Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dk. Melkiory Ngido, akipokea Tuzo ya Rais ya Mlipakodi Kinara kwa niaba ya Barrick Mining Corporation kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, wakati wa hafla ya utoaji wa Tuzo za Rais kwa Walipakodi Wakubwa iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mpango wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI), Profesa Riziki Shemdoe akisalimia wakazi wa Kibaigwa wakati wa hafla ya uzinduzi wa awamu ya pili ya mpango wa Barrick–Twiga Future Forward Education Program katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaigwa, mkoani Dodoma. Kushoto ni
Meneja Mkazi wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido.

**

MYCOELY BALOZI MPYA WA MAZINGIRA NCHINI

July 12, 2026 Add Comment
Msanii wa Mziki wa Bongo fleva nchini Michael Muganda (Mycoely) amesaini hati ya makubaliano na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ya kuwa Balozi wa Mazingira nchini.

UTORO NA VIGODORO VYATAJWA KUCHANGIA UFAULU HAFIFU, POLISI KATA YAISHUKURU TANGAYETU

July 12, 2026 Add Comment


Polisi Kata wa Kata ya Nguvumali, Jiji la Tanga, Inspekta Sharifu Kiswamba, amesema utoro wa wanafunzi na tabia ya kukesha kwenye vigodoro ni miongoni mwa sababu zinazochangia kushuka kwa kiwango cha ufaulu katika shule za sekondari.

Inspekta Kiswamba alitoa kauli hiyo wakati wa mafunzo maalumu ya kuwajengea wanafunzi mbinu za kujifunza kwa ufanisi na kujiandaa vizuri kwa mitihani, yanayoendeshwa na Tanzania Centre for Education (TCE) kwa kushirikiana na Botnar Foundation na Inovex kupitia Mradi wa TangaYetu.


Alisema mradi huo unahusisha shule 10 zilizobainika kuwa na changamoto ya matokeo hafifu ya kitaaluma, ukiwa na lengo la kuwajengea wanafunzi uwezo wa kujifunza kwa ufanisi na kuongeza kiwango cha ufaulu.


"Kama Polisi Kata tunaushukuru Mradi wa TangaYetu pamoja na wadau wake kwa kuanzisha mafunzo haya. Tunaamini yatasaidia kubadilisha mtazamo wa wanafunzi, kuongeza nidhamu na hatimaye kuinua ufaulu katika shule zetu," alisema.


Alieleza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kushirikiana na viongozi wa kata, walimu na jamii kuhakikisha wanafunzi wanaotoroka masomo wanafuatiliwa na kurejeshwa shuleni ili wasikose haki yao ya elimu.


"Tunatoa onyo kwa wanafunzi wanaotoroka masomo. Tutakaowakuta wakizurura wakati wa vipindi vya masomo watachukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu, ikiwemo kupelekwa ofisini kwa hatua zaidi za kinidhamu," alisema.


Inspekta Kiswamba alisema pia tabia ya wanafunzi kushinda vijiweni na kukesha kwenye vigodoro imeendelea kuwa changamoto inayochangia kuporomoka kwa nidhamu na kuathiri maendeleo yao kitaaluma.


"Hatutavumilia tabia hii. Tutaendelea kufanya doria na kushirikiana na viongozi wa mitaa pamoja na wazazi kuhakikisha wanafunzi wanazingatia masomo na kujiepusha na mazingira yanayoharibu mustakabali wao," alisisitiza.


Aidha, aliwataka wazazi na walezi kutekeleza wajibu wao wa kufuatilia maendeleo ya watoto wao kwa kuhakikisha wanahudhuria masomo, wanapata muda wa kujisomea na kuepuka vitendo vinavyoweza kuhatarisha elimu yao.


Alisema mafanikio ya sekta ya elimu yanahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wazazi, walimu, viongozi wa serikali za mitaa, Jeshi la Polisi na wadau wa maendeleo, akieleza kuwa jitihada zinazofanywa na Mradi wa TangaYetu ni sehemu ya suluhisho la changamoto zinazolikabili eneo hilo.


Mafunzo hayo ni sehemu ya jitihada za Mradi wa TangaYetu za kuboresha matokeo ya kitaaluma katika shule zenye changamoto kwa kuwajengea wanafunzi stadi za kujifunza, nidhamu na maandalizi bora ya mitihani.









JAB YAHIFADHI URITHI WA TASNIA YA HABARI KUPITIA ITHIBATI YA MAISHA

Kajunason July 12, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu.

Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imezindua rasmi Mwongozo wa Kisheria wa Utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa Waandishi wa Habari Wakongwe, hatua inayolenga kutambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari waliolitumikia Taifa kwa muda mrefu na kwa utumishi uliotukuka katika maendeleo ya sekta ya habari nchini.

Uzinduzi huo umefanyika leo, Julai 11, 2026, wakati wa maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika katika Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwenye Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba).

Kupitia hotuba yake iliyosomwa na Dkt. Egbert Mkoko, Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Bw. Tido Mhando, alisema mwongozo huo umeandaliwa kwa kuzingatia mamlaka iliyopewa Bodi chini ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229 pamoja na Kanuni zake, ili kuweka utaratibu wa utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa waandishi wa habari wakongwe waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya taaluma hiyo.

Alisema mwongozo huo unawahusu waandishi wa habari ambao wakati Sheria ya Huduma za Habari ilipoanza kutumika mwaka 2016 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi na walikuwa tayari wametoa mchango mkubwa katika sekta ya habari, lakini hawakupata fursa ya kujiendeleza hadi kufikia sifa za kitaaluma zinazohitajika kwa mujibu wa sheria.

"Mwongozo huu unalenga kuhifadhi historia ya tasnia ya habari, kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe na kuhakikisha uzoefu wao unaendelea kuwa sehemu ya urithi wa taaluma ya uandishi wa habari nchini," ilieleza sehemu ya hotuba ya Mwenyekiti.

Bw. Mhando alisisitiza kuwa mwongozo huo hauondoi wala haupunguzi masharti ya msingi yaliyowekwa na Sheria ya Huduma za Habari kuhusu sifa za kupata ithibati kwa waandishi wa habari, bali unaweka utaratibu wa kutekeleza mamlaka ambayo sheria imeipa Bodi kuhusu utoaji wa Ithibati ya Maisha kwa watu wenye utumishi uliotukuka na waliotoa mchango wa kipekee katika maendeleo ya sekta ya habari.

Aidha, aliipongeza Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuendelea kuiwezesha Bodi kutekeleza majukumu yake na kuimarisha ushirikiano unaolenga kukuza weledi, uwajibikaji na maadili katika taaluma ya uandishi wa habari.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alisema uzinduzi wa mwongozo huo ni hatua muhimu katika utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari na unaonesha dhamira ya Bodi ya kuimarisha viwango vya taaluma huku ikitambua na kuthamini mchango wa waandishi wa habari wakongwe waliolitumikia Taifa kwa uaminifu, uzalendo na weledi.

Sambamba na uzinduzi huo, JAB iliendesha mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya habari kujadili maendeleo ya sekta ya habari nchini, utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari pamoja na mafanikio na changamoto zilizojitokeza katika mwaka mmoja wa utekelezaji wa mfumo wa utoaji wa ithibati kwa waandishi wa habari waliokidhi vigezo vya sheria.

MBUNGE ADO SHAIBU AKUTANA NA TANZANIA ONE KUTOKA TUNDURU

July 11, 2026 Add Comment


Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini Mh. Ado Shaibu Ado amekutana na kufanya mazungumzo na Ndugu Biriat Yafet Biriat ambaye kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa na Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) kwa ngazi ya kidato cha sita ndiye kinara wa kufaulu nchi nzima (Tanzania One)

Mh. Ado amesema ameamua kukutana na mwanafunzi huyo aliyehitimu shule ya Ndanda Wilayani Masasi akitokea Wilayani Tunduru kwa sababu ufaulu wake ambao haujawahi kutokea kwa kiwango hicho Wilayani Tunduru umeiletea heshima kubwa wilaya ya Tunduru.



Mbali na kumpongeza Mh. Ado alikubali maombi ya Ndugu Biriat kusaidiwa simu, laptop na fedha za kujikimu na kushughulikia michakato yote hadi pale atapojiunga rasmi na kupata mkopo wa Serikali. Ndugu Ado alimnunulia simu, kumkabidhi fedha taslimu milioni moja na kumpa ahadi ya kumuagizia laptop. Amesema kuwa atatoa ushirikiano kwa mahitaji mengine ya kielimu yatayoibuka.


Kwa upande wake Ndugu Biriat amemshukuru Ndugu Ado kwa msaada wake akiamini hatua hiyo inafungua milango zaidi kwa wadau wengine.

TEA YAHIMIZWA KUENDELEA KUIMARISHA SEKTA YA ELIMU

July 11, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

MKURUGENZI wa Idara ya Elimu Mbadala na Elimu ya Watu Wazima Zanzibar, Mashavu Ahmada Fakih, ameipongeza Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha sekta ya elimu nchini, huku akiwataka wadau wa maendeleo na wananchi kuendelea kuchangia Mfuko wa Elimu ili kuongeza ubora wa elimu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

TEA YATAKA RASILIMALI ZAIDI KWA AJILI YA MAENDELEO YA ELIMU

July 11, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imezitaka taasisi za maendeleo, sekta binafsi na wananchi wenye uwezo kujitokeza kuchangia Mfuko wa Taifa wa Elimu ili kuongeza rasilimali zitakazowezesha kuboresha miundombinu ya elimu na kuimarisha uwekezaji katika elimu ya amali nchini.

DIAMOND APONGEZA USIMAMIZI WA JAB KATIKA SEKTA YA HABARI

Kajunason July 11, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Mkurugenzi Mtendaji wa Wasafi Media, Nasib Abdul maarufu Diamond Platnumz, amesema utekelezaji wa Sheria ya Huduma za Habari unaweka mazingira bora ya kukuza uwekezaji katika sekta ya habari kwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaendeshwa kwa kuzingatia sheria, weledi na viwango vya taaluma.

Diamond alitoa kauli hiyo tarehe 11 Juni, 2026 alipotembelea Banda la Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba), kufuatia mwaliko wa Bodi hiyo ili kujionea huduma na elimu inayotolewa kwa waandishi wa habari pamoja na wananchi.

Alisema uwekezaji katika sekta ya habari unahitaji nidhamu, maono, subira na uongozi unaozingatia sheria, akibainisha kuwa usimamizi unaofanywa na JAB unasaidia wawekezaji kuelewa matakwa ya kisheria na namna ya kuyazingatia bila kuhisi kuwa biashara zao zinakwamishwa.

"Utekelezaji na usimamizi wa Sheria ya Huduma za Habari unaonesha ni kwa kiwango gani Serikali inaunga mkono uwekezaji wa vijana katika sekta ya habari. Kazi ya Bodi si kuzuia watu kufanya biashara, bali kuwaelekeza kufuata matakwa ya sheria na kuwahamasisha kuongeza elimu na kukidhi vigezo vinavyotakiwa," alisema Diamond.

Aliongeza kuwa utekelezaji wa sheria unahitaji busara, maarifa na uwezo wa kuwaelimisha wadau ili waelewe mabadiliko ya taratibu bila kujenga hofu au kuona kuwa wanawekewa vikwazo.

"Kazi hii inahitaji busara na maarifa ya kuwafundisha watu, kuwaelekeza na kuwafanya waelewe taratibu mpya pasipo kuona kwamba wameharibiwa biashara zao. Nimeona Bodi ina timu nzuri inayounga mkono maono ya uongozi wake katika kusimamia sekta hii," alisema Diamond.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari, Wakili Patrick Kipangula, alimpongeza Diamond kwa uwekezaji wake katika sekta ya habari na kwa Wasafi Media kuendelea kuzingatia matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari.

Alisema JAB itaendelea kushirikiana na wamiliki wa vyombo vya habari na wadau wengine kuhakikisha sheria inatekelezwa kwa njia inayokuza weledi, uwajibikaji na maendeleo ya sekta ya habari, huku ikitoa elimu na ushauri unaowawezesha wadau kutekeleza matakwa ya sheria kwa ufanisi.

Ziara ya Diamond katika Banda la JAB ilikuwa sehemu ya maadhimisho ya JAB Day yaliyofanyika ndani ya Banda la Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam, ambapo Bodi imekuwa ikitoa huduma za ithibati, elimu kuhusu Sheria ya Huduma za Habari na ushauri kwa waandishi wa habari, wamiliki wa vyombo vya habari na wananchi.