HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MTAKUWWA MAGU YAKUMBUSHWA KUELIMISHA JAMII DHIDI YA UKATILI WA KIJINSIA

July 01, 2026 Add Comment


Rai imetolewa kwa Kamati ya Kupinga Ukatili wa Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) Wilayani Magu kuweka mkazo  elimu kwa Jamii kuhusu namna ya kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia ambavyo vimeshamiri wiilayani humo.

Rai hiyo imetolewa leo Julai 1, 2026 na Mwenyekiti mwenza wa Kamati ya MTAKUWWA ngazi ya mkoa wa Mwanza Bw. Yassin Ally wakati wa kikao cha pamoja na Kamati ya wilaya hiyo kilicjofanyika kwenye ukumbi wa mikutsno wa Halmashauri ya Magu,amesema vitendo vya ukatili vimekuwa tishoo katika maendeleo ya wananchi

Ametolea mfano katika sekta ya elimu bado kunahitsjika jitihafa za ziada kutokana na baadhi ya walimu kuzikimbia shule wanazofindisha kutokana na kuingiliwa kimwili kishirikina hali ambayo imesababisha taharuki.

"Hali ni mbaya tushikamane kutokomeza hali hii tusikae maofisini twendeni tukawape elimu jamii,vinginevyo tutazidi kurudi nyumba kimarndeleo" amesisiriza Mwenyekiti mwenza.

Ameongeza kuwa baadhi ya wazazi wanatoa mafundisho potofu kwa watoto zao wa kike kuchora madudu kwenye mitihani yao ya kumaliza ili wajifelishe kwa makusudi na waishie kuolewa.

Afisa Ustawi wa Jamii mkoani Mwanza Baraka Makona amesema Kamati hiyo ya MTAKUWWA Mkoa wa Mwanza inafanya ziara kwenye wilaya zote mkoani humo ili kuona mipango ya utekelezaji na changamoto wanazokabiliana nazo.

Awali akitoa taarifa fupi ya utekelezaji wa MTAKUWWA Wiilayani Magu AFISA Ustawi wa Jamii wiilayani humo Bi.Coletha Sanga amesema katika kupambana na umasikini ndani ya jamii wametoa mikopo kwa vikundi 13 wenye gharama ya zaidi ya shs.milioni 143.

Kamati ya MTAKUWWA ngazi ya mkoa itaendelea na ziara yake Alhamisi hii kwa kutembelea Halmashauri ya Ilemela.



 

MTAKUWWA YATAKA ELIMU ZAIDI DHIDI YA UKATILI MAGU .

July 01, 2026 Add Comment

Kamati ya Kupinga Ukatili wa Wanawake na Watoto (MTAKUWWA) Wilayani Magu imetakiwa kuongeza juhudi za kutoa elimu kwa jamii ili kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyoendelea kushamiri wilayani humo.

Rai hiyo imetolewa leo Julai 1, 2026 na Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya MTAKUWWA Mkoa wa Mwanza, Yassin Ally, wakati wa kikao na Kamati ya MTAKUWWA Wilaya ya Magu kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Amesema vitendo vya ukatili vimeendelea kuwa kikwazo kwa maendeleo ya wananchi na vinahitaji ushirikiano wa wadau wote kuvimaliza.

Amesema bado kuna changamoto katika sekta ya elimu, akieleza kuwa baadhi ya walimu hukimbia vituo vyao vya kazi kutokana na vitisho na matukio ya ushirikina, hali inayosababisha taharuki na kuathiri utoaji wa huduma za elimu.

Aidha, ameeleza kuwa baadhi ya wazazi huwapa watoto wa kike mafundisho potofu ya kujifelisha kwa makusudi katika mitihani ya kuhitimu ili waolewe mapema, akisisitiza kuwa tabia hiyo inapaswa kukemewa.

Kwa upande wake, Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Mwanza, Baraka Makona, amesema Kamati ya MTAKUWWA Mkoa inaendelea na ziara katika wilaya zote za mkoa huo kwa lengo la kufuatilia utekelezaji wa mipango ya kupambana na ukatili wa kijinsia pamoja na kubaini changamoto zinazojitokeza.

Awali, Afisa Ustawi wa Jamii Wilaya ya Magu, Coletha Sanga, amesema kupitia jitihada za kuwawezesha wananchi kiuchumi, Halmashauri imetoa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 330 kwa vikundi 28 ili kusaidia kupunguza umasikini na kuongeza ustawi wa jamii.








 

NIDA yakabidhi Serikali zaidi ya shilingi bilioni 61

Kajunason July 01, 2026 Add Comment

 Dar es Salaam, 1 Julai 2026 Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) inapenda kuufahamisha Umma wa Watanzania kuwa tarehe 30 Juni 2026, imekabidhi Serikalini mchango wa TZS 61,053,535,363 ikiwa ni fedha za makusanyo yake katika kuunga mkono jitihada za Serikali ya Jamuhuriy a Muungano wa Tanzania ya kuleta maendeleo kwa wananchi. 

Mchango huo ulikabidhiwa kwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika hafla ya upokeaji wa gawio na michango ya Taasisi za Umma iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam. 

Katika hafla hiyo, NIDA pia ilipata heshima ya kutunukiwa tuzo baada ya kushika nafasi ya pili miongoni mwa Taasisi zilizofanya vizuri katika kuwasilisha mchango wake Serikalini. Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Mheshimiwa Rais, ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wa NIDA katika kuimarisha mapato ya Serikali na kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa manufaa ya wananchi. 

Akizungumza baada ya hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, James Kaji amesema mafanikio hayo ni matokeo ya kuendelea kuimarishwa kwa mifumo ya utoaji huduma kwa wananchi. 

“Tunapokea heshima hii kwa unyenyekevu mkubwa. Mchango huu siyo tu takwimu za kifedha, bali ni matokeo ya uboreshaji wa huduma za utambuzi wa Taifa ambapo ni nyenzo muhimu katika kuimarisha usalama, kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi na kichocheo cha mapato katika sekta binafsi na Umma,” amesema Kaji. 

NIDA inaendelea kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kusajili na kuwatambua wananchi kwa kutoa Namba ya Utambulisho wa Taifa (NIN) na Vitambulisho vya Taifa, pamoja na kuwezesha matumizi ya taarifa sahihi za utambuzi katika sekta mbalimbali za huduma za umma na binafsi.

 Utambuzi wa Taifa ni msingi muhimu katika kuwezesha Serikali na Sekta Binafsi kupanga, kuhudumia wananchi au wateja wake kwa ufanisi, kuimarisha usalama, kudhibiti mianya ya udanganyifu na kuongeza tija katika utoaji wa huduma. NIDA inatoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maono, miongozo na uwekezaji unaoendelea kufanywa katika kuimarisha mifumo ya utambuzi nchini.

  Aidha, NIDA inawashukuru wananchi, wadau, taasisi za Serikali na sekta binafsi kwa kuendelea kushirikiana na Mamlaka katika kujenga Taifa lenye utambuzi sahihi, huduma bora na maendeleo jumuishi. Imetolewa na: Kitengo cha Mawasiliano na Hifadhi Hati 



Rostam Azizi apokea tuzo ya heshima kwa kukuza uwekezaji nchini

Kajunason July 01, 2026 Add Comment

 Mwenyekiti wa Taifa Group na mfanyabiashara mashuhuri, Bw. Rostam Azizi, ametunukiwa Tuzo ya Juu ya Heshima ya Chemba ya Taifa ya Biashara Tanzania (TNCC) kwa kutambua mchango wake katika kukuza uwekezaji, kuunda ajira, kuboresha huduma za jamii na kuchochea maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Tuzo hiyo ilikabidhiwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mwigulu Nchemba, aliyekuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Biashara na Uwekezaji la Mwaka 2026 lililoandaliwa na TNCC katika Hoteli ya Johari Rotana, Dar es Salaam.

Akizungumza katika kongamano hilo, Dkt. Mwigulu alisema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji kupitia maboresho ya sera, sheria, kanuni na mifumo ya utoaji huduma ili kuiwezesha sekta binafsi kuwa injini ya ukuaji wa uchumi na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

"Ajenda ya sekta binafsi ni ajenda ya Taifa. Hatuwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 bila sekta binafsi yenye nguvu na inayoshirikiana kwa karibu na Serikali," amesema.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kushughulikia mapendekezo ya sekta binafsi ili kuondoa vikwazo vya biashara na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kupitia uwekezaji wake katika sekta mbalimbali, Bw. Rostam Azizi amechangia uundaji wa maelfu ya ajira, kukuza uwekezaji na kuboresha huduma za jamii, hatua zilizochangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza baada ya kupokea tuzo hiyo, Bw. Rostam Azizi aliishukuru Serikali na TNCC kwa kutambua mchango wake, akisema tuzo hiyo ni motisha ya kuendelea kushiriki katika maendeleo ya Taifa.

"Ninapokea tuzo hii kwa heshima kubwa.

Naihusisha na juhudi za pamoja kati ya sekta binafsi na Serikali katika kujenga uchumi imara. Nawapongeza pia wadau wote waliotunukiwa tuzo mbalimbali leo kwa mchango wao katika kuimarisha sekta binafsi na kukuza uchumi wa Taifa," amesema.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu pia alikabidhi tuzo mbalimbali kwa wadau wengine, akiwemo Bi. Emma Kawawa, Bw. David Mwaibula, Bw. Imani Kajula, Bw. Elibariki Mmasi na Bi. Mercy Emmanuel Sila, kwa mchango wao katika kuendeleza sekta binafsi, kuboresha mazingira ya biashara na kuimarisha shughuli za TNCC.

Katibu Mkuu CCM akutana na Balozi wa Umoja wa Ulaya Kujadili Ushirikiano wa Maendeleo

July 01, 2026 Add Comment

 

 Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ndugu Asha-Rose Migiro, amefanya mazungumzo na Mheshimiwa Christine Grau, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Tanzania, katika Ofisi ya Katibu Mkuu wa CCM, Lumumba, Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yamefanyika jana Juni 30,2026, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kumuaga Balozi Grau anayehitimisha kipindi chake cha uwakilishi nchini Tanzania. Viongozi hao walitathmini ushirikiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya na kujadili namna ya kuuendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, viongozi hao walibadilishana mawazo kuhusu umuhimu wa kuimarisha misingi ya utawala bora, amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa kama nguzo ya maendeleo endelevu ya Taifa. Katika muktadha huo, CCM ilisisitiza dhamira yake ya kuendelea kujenga Taifa linaloongozwa kwa misingi ya haki, uwajibikaji na utulivu wa kisiasa.

Pia, ilitambua changamoto zilizojitokeza nchini katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu uliopita na umuhimu wa hatua ambazo Serikali inaendelea kuzichukua katika kuimarisha imani ya wananchi, ikiwemo kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi, Tume ya Upelelezi wa Jinai na hatua nyingine za kisheria zinazolenga kuhakikisha ukweli, uwajibikaji na haki vinaendelea kutawala katika kulinda amani na mshikamano wa Taifa.

Aidha, ilielezwa kuwa ajenda ya kuendelea kuimarisha demokrasia nchini, ikiwemo mchakato wa Katiba Mpya ambao umeainishwa katika Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2025–2030, inabaki kuwa sehemu muhimu ya maono ya muda mrefu ya kuimarisha utawala bora na mshikamano wa Taifa.

Viongozi hao pia walitambua nafasi ya vijana katika mustakabali wa maendeleo ya Tanzania na umuhimu wa kuhakikisha kizazi hicho kinaendelea kuwa sehemu ya safari ya Taifa kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na ujenzi wa uchumi wenye ushindani na maendeleo jumuishi.

CCM inathamini ushirikiano wake na Umoja wa Ulaya na inaamini kuwa ushirikiano huo utaendelea kuimarika kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, maslahi ya pamoja na dhamira ya pamoja ya kuendeleza maendeleo endelevu ya Tanzania.







RC BATILDA AZIELEKEZA HALMASHAURI TANGA KUDHIBITI CHANZO CHA HOJA ZA CAG

July 01, 2026 Add Comment

 


HALMASHAURI za Wilaya, Miji na Jiji mkoani Tanga, zimeagizwa kuzuia vyanzo vinavyosababisha hoja zinazoibuliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). 

Agizo hilo limetoa leo Juni 30, 2026 na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt Batilda Burian, alipozungumza kwenye vikao maalum vya kujadili hoja za CAG katika Baraza la Madiwani wa Halmashauri za Lushoto na Bumbuli.

Amesema, taarifa za CAG kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, inaonesha halmashauri hizo zimefanikiwa kupata hati inayoridhisha, ikiwa ni Ishara ya ufanisi, weledi na kujituma kwa watumishi na watendaji.

Amesema, hali hiyo inapaswa kuendelezwa ili kufikia malengo msingi ya Serikali katika kutoa huduma bora kwa wananchi.


Hata hivyo, Mhe. Balozi Dkt Batilda amesema, pamoja na mafanikio hayo, halmashauri hizo zinatakiwa kudhibiti vitendo vinavyosababisha hoja za ukaguzi.

Awali, taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Nje, Mkoa wa Tanga, Hamu Mwakasola, ilieleza kuwa kutolewa hati inayoridhisha haimaanishi kuwepo mifumo mizuri ya udhibiti wa ndani, bali kutokuwepo dosari kubwa wakati wa ukaguzi.

“Inamaanisha hapakuwa dosari kubwa zilizobainika wakati wa ukaguzi ambazo zingemzua Mkaguzi kutoa maoni, au kumlazimu kutoa hati yenye mashaka au hati mbaya,” amesema

Naye Katibu Tawala Mkoa (RAS) wa Tanga, Rashid Mchatta, pamoja na mambo mengine, amewahimiza watumishi na umma, kuendeleza mahusiano mema ili kuongeza ufanisi na tija mahali pa kazi.

Amesema, viongozi, watendaji na watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wanapaswa kutambua ‘uzito’ wa hadhi ya Ofisi ya CAG katika ukaguzi wa hesabu uliopo katika ngazi za kimataifa.

Mchatta amesema utambuzi wa ubora huo utachangia kuboresha utendaji kazi na kupunguza kwa kiasi kikubwa hoja za ukaguzi, hali itakayoifanya CAG kutekeleza vema wajibu wake wa ushauri wa kitaalamu kwa taasisi husika.  




Mwisho

WATANZANIA KUNUFAIKA NA UMEME WA UHAKIKA; MRADI WA CHALINZE–DODOMA WAFIKIA ASILIMIA 89 YA UTEKELEZAJI

July 01, 2026 Add Comment

 


📌 utaimarisha upatikanaji wa umeme kwa wananchi, viwanda na shughuli za kiuchumi

📌 Wananchi wanatarajiwa kunufaika na huduma ya umeme yenye uhakika zaidi baada ya kukamilika kwa mradi

📌 TANESCO yavunja rekodi kwa kuunganisha zaidi ya wateja laki nane mwaka 2025/26

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

Watanzania katika maeneo mbalimbali nchini wanatarajiwa kunufaika na huduma ya umeme yenye uhakika zaidi kutokana na maendeleo makubwa ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Chalinze hadi Dodoma, ambayo sasa imefikia asilimia 89 ya utekelezaji.

Mradi huo wenye urefu wa kilometa 345 unatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026 na utaongeza uwezo wa kusafirisha umeme kutoka vyanzo vikubwa vya uzalishaji kwenda maeneo yenye mahitaji makubwa ya nishati, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

Akikagua maendeleo ya mradi huo Julai 1, 2026, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb), amesema mradi huo ni uwekezaji muhimu unaolenga kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika kwa matumizi ya nyumbani, biashara ndogo na kubwa, pamoja na shughuli za uzalishaji.

Amesema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuimarisha Gridi ya Taifa na kuwezesha umeme unaozalishwa katika Kituo cha Kufua Umeme cha Julius Nyerere chenye uwezo wa megawati 2,115 kuwafikia wananchi na sekta mbalimbali za uchumi kwa ufanisi zaidi.

“Umeme wa uhakika una maana ya maisha bora zaidi kwa wananchi, biashara kukua, viwanda kufanya kazi bila kukatika kwa huduma na huduma za kijamii kama hospitali na shule kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuwekeza katika miradi ya umeme ili kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma ya nishati inayowawezesha kuongeza kipato na kuboresha ustawi wao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Razalo Twange, amesema ongezeko la uwekezaji katika miundombinu ya umeme limechangia kuongezeka kwa kasi ya uunganishaji wa wateja wapya, jambo linaloonesha namna umeme unavyoendelea kuwa sehemu muhimu ya maisha na maendeleo ya wananchi.

Amesema katika mwaka wa fedha 2025/26, TANESCO imeweka rekodi mpya kwa kuunganisha zaidi ya wateja laki nane, idadi ambayo haijawahi kufikiwa tangu Tanzania ipate uhuru.

“Kila mteja mpya anayepata umeme ni fursa mpya ya biashara, elimu bora kwa watoto, huduma bora za afya na ongezeko la kipato kwa familia. Hii ndiyo maana ya uwekezaji huu mkubwa wa Serikali katika sekta ya umeme,” amesema Bw. Twange.

Awali, Meneja wa Mradi, Mha. Newton Mwakifamba, amesema kazi zinaendelea vizuri na zinatarajiwa kukamilika Agosti 21, 2026 kwa mujibu wa ratiba ya mkataba, na hivyo kufungua ukurasa mpya wa upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa Watanzania wengi zaidi.






OFISI YA WAZIRI MKUU NA TAASISI YA CHAKULA NA LISHE TANZANIA KUSHIRIKIANA KUANDAA MPANGO WA LISHE TAIFA

July 01, 2026 Add Comment

 Na Mwandishi wetu- Dodoma 




Na Mwandishi Wetu- Dodoma


Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Chakula na  Lishe  Tanzania  (TFNC) Bi. Debora Charwe amesema, Serikali ipo katika mchakato wa kuandaa Mpango wa Muda Mrefu wa Lishe wa Taifa (NN-LTP)  ili kuongeza jitihada za sekta mtambuka  katika kuboresha utekelezaji wa  lishe kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.


Bi. Debora ameyasema hayo leo tarehe 30 Juni, 2026 wakati akifungua Warsha ya mafunzo kuhusu kuandaa mpango wa muda mrefu wa lishe wa Taifa (National Nutrition Long Term  Plan  2026-2050) ambayo  inafanyika jijini Dodoma kwa siku tatu kuanzia Juni 30 hadi Julai 02, 2026

Amesema, mafunzo hayo yanatolewa kwa Wataalam  kutoka ngazi ya Wizara mbalimbali kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu uandaaji wa  mipango ya muda mrefu  wa lishe  inayojumuisha sekta mtambuka pamoja na  kubadilishana uzoefu kusaidia katika usanifu, muundo na taratibu za utekelezaji wa Mpango wa muda mrefu wa Lishe wa Taifa.








Vilevile Bi. Debora amefafanua kuwa, mpango huo  unaandaliwa chini ya usimamaizi wa Ofisi ya Waziri  Mkuu  kwa kushirikiana na Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (TFNC)  na wadau wengine wa maendeleo kwa kuzingatia haja ya  kuifanya lishe kuwa moja ya kichocheo  na kipimo katika  kufikiwa kwa malengo ya Dira  ya Maendeleo ya Tanzania kufikia 2050. 

 Aidha, warsha hiyo imehusisha Afisa viungo wa lishe kutoka Wizara mbalimbali zikiwemo Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Ofisi ya Rais Maendeleo ya Vijana, Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) pamoja na  Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Viwanda, Wizara ya Maji na Wizara ya Mambo na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

==MWISHO==