HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

SERIKALI YARIDHIA UCHIMBAJI WA BAUXITE MAGAMBA, LESENI 45 ZASITISHWA

February 18, 2026 Add Comment



Waziri Mkuu, Mwigulu Nchemba, ameielekeza kampuni ya Abanyambo Enterprises & General Supplies Ltd kuendelea na shughuli za uchimbaji wa madini ya bauxite katika Kata ya Magamba, Wilaya ya Lushoto, mkoani Tanga.

Hatua hiyo imekuja kufuatia utekelezaji wa agizo lililokuwa limetolewa awali na Waziri Mkuu mstaafu, Kassim Majaliwa, ambaye alisitisha uchimbaji huo hadi tathmini ya athari kwa mazingira na binadamu itakapofanyika na kukamilika.

Akizungumza wakati wa ziara yake mkoani humo, Waziri Mkuu alisema kampuni hiyo, ambayo inamiliki leseni nne halali, imeruhusiwa kuendelea na uzalishaji baada ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kujiridhisha na kutoa kibali rasmi cha tathmini ya athari kwa mazingira.


Alitoa kauli hiyo alipokuwa akijibu swali la aliyekuwa Mwenyekiti wa Kitongoji cha Magamba, Mahamud Kotti, ambaye alitaka kujua msimamo wa Serikali kuhusu mradi huo.  licha ya uchimbaji huo kuwa chanzo cha ajira na mapato kwa kijiji na halmashauri.

Hata hivyo Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali haitavumilia uvunjaji wa sheria katika sekta ya madini, akieleza kuwa wawekezaji wote wanapaswa kufuata taratibu zilizowekwa ili kulinda rasilimali za taifa pamoja na mazingira.

Katika hatua nyingine, alitangaza kusimamishwa kwa leseni 45 zilizokuwa zikitaka kufanya shughuli katika mgodi huo kinyume na sheria na masharti ya uchimbaji.

 Alifafanua kuwa uamuzi huo umefikiwa baada ya kubainika kuwepo kwa ukiukwaji wa taratibu ambao ungeweza kuhatarisha usalama wa mazingira na kusababisha upotevu wa mapato ya Serikali.

“Hatutakuwa tayari kuona rasilimali za nchi zinachimbwa bila kufuata sheria. Lazima kila mmoja aheshimu utaratibu,” alisisitiza Waziri Mkuu.

Aidha, amemuagiza Afisa Madini Mkoa wa Tanga kusimamia kikamilifu utekelezaji wa agizo hilo na kuhakikisha kuwa kampuni ya Abanyambo pekee ndiyo inayoendelea na shughuli za uchimbaji katika eneo hilo.

Ziara hiyo ni sehemu ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo na shughuli za kiuchumi unaofanywa na Waziri Mkuu, kwa lengo la kuhakikisha sheria, uwazi na uwajibikaji vinazingatiwa katika usimamizi wa rasilimali za taifa.

MAGEUZI YA ELIMU KULETA DOUBLE COHORT KWA KIDATO CHA KWANZA

MAGEUZI YA ELIMU KULETA DOUBLE COHORT KWA KIDATO CHA KWANZA

February 18, 2026 Add Comment

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda,akizungumza katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya uliofanyika   wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani.

......

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema kuwa jukumu kubwa la Wathibiti Ubora wa Shule ni kuhakikisha utekelezaji wa sera, sheria, miongozo na mikakati ya elimu unafanyika kwa ufanisi.

Akizungumza  wilayani Bagamoyo Mkoani Pwani katika ufunguzi wa mafunzo elekezi ya Wathibiti Ubora wa Shule ngazi ya wilaya, ameeleza kuwa watendaji wanapaswa kusaidia katika utekelezaji wa sera na kuhakikisha wanazielewa kikamilifu, hususani zinazohusu elimu ya amali na elimu ya lazima.

Profesa Mkenda amesema wathibiti Ubora wa Shule wanapaswa kutoa taarifa juu ya changamoto zinazojitokeza shuleni ikiwemo ukosefu wa vifaa au madarasa kwa Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya ili hatua za kutatua changamoto hizo zichukuliwe haraka.

Akizungumzia mageuzi makubwa ya Sekta ya Elimu, Waziri amesema kuwa kuanzia mwaka wa masomo 2027/2028, elimu ya msingi itaanza kutolewa kwa Miaka Sita badala ya Saba na elimu ya lazima itakuwa miaka kumi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne.

"Mabadiliko haya yataleta “double cohort,” ambapo wanafunzi wa darasa la saba (mfumo wa zamani) na darasa la sita (mfumo mpya) wataingia kidato cha kwanza kwa wakati mmoja. Hata hivyo, hali hiyo ni ya mpito na mfumo utarejea katika “single cohort” baada ya muda,'amefafanua Waziri Mkenda.

Amesema Serikali inawekeza katika shue za ufundi, lakini bado kuna uhaba wa karakana, vifaa na walimu wenye sifa huku akisisitiza Halmashauri kupanga bajeti kwa umakini ili kuzuia shule kufungwa kutokana na ukosefu wa mahitaji ya msingi.

Mkurugenzi Msaidizi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Monica Mpululu, amesema kuwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imekuwa ikitekeleza majukumu yake kwa kasi na kwa ushirikiano wa karibu na Wathibiti Ubora wa shule nchini.

Mkurugenzi huyo ameeleza kuwa wizara imeendelea kuwawezesha wathibiti Ubora wa shule kwa kuwapatia rasilimali muhimu, ikiwemo fedha na vifaa vya kazi ambayo inasaidia kuboresha usimamizi na ufuatiliaji wa shule katika maeneo mbalimbali ya nchi na kuongeza ufanisi wa kazi za uthibiti ubora.

Mpululu amesema kuwa ushirikiano wa wadau wote wa elimu ni msingi wa mafanikio ya sekta, na kwamba juhudi zinazofanywa sasa ni matokeo ya kazi ya pamoja inayolenga kuinua kiwango cha elimu kwa manufaa ya taifa.

MAVUNDE AWATAKA WANUFAIKA WA BILIONI 2/- MTUMBA KUTUMIA MIKOPO KUJIKWAMUA KIUCHUMI

MAVUNDE AWATAKA WANUFAIKA WA BILIONI 2/- MTUMBA KUTUMIA MIKOPO KUJIKWAMUA KIUCHUMI

February 17, 2026 Add Comment

Na.Alex Sonna-DODOMA

WAZIRI  wa Madini na Mbunge wa Jimbo la Mtumba Mhe. Anthony Mavunde , amevitaka vikundi vilivyonufaika na mkopo wa shilingi bilioni mbili uliotolewa kwa wajasiriamali wa jimbo hilo, kutumia fedha hizo kama zilivyokusudiwa ili kujikwamua kiuchumi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mikopo hiyo jijini Dodoma, Mhe.Mavunde amesema kuwa  azma ya serikali ni kuhakikisha wananchi wanapata nyenzo na mitaji ya kuwawezesha kupanua na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Amesema kuwa  Mkopo huo umefadhiliwa na CRDB Bank kupitia CRDB Bank Foundation katika programu ya imbeju inayolenga kuwawezesha wajasiriamali wadogo na wa kati.

"Tumieni vizuri  mikopo hiyo kwa kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za ujasiriamali ili iweze kuleta tija, kuwaimarisha kiuchumi na hatimaye kurejeshwa kwa manufaa ya wengine."amesema Mhe.Mavunde

Mhe.Mavunde amesema kuwa  mikopo hiyo ni kama mbegu inayohitaji kutunzwa na kuendelezwa ili izae matunda yenye manufaa kwa mkopaji na jamii kwa ujumla.

“Mikopo hii ni mbegu. mkizitumia vizuri zitazaa matunda na kuwainua kiuchumi, lakini pia zitawawezesha wengine kupata fursa kama hii baada ya ninyi kurejesha kwa wakati,” amesisitiza 

Aidha ameongeza kuwa dhamira yake ni kuona wananchi wa mtumba wanaachana kabisa na mikopo umiza maarufu kama ‘mikopo ya kausha damu’ na badala yake wanatumia fursa rasmi za kifedha zenye masharti nafuu na rafiki kwa maendeleo yao.

“Wananchi wa mtumba wakae mkao wa kula. kuna mipango mingi ya kuwawezesha kiuchumi inaendelea kuja, na lengo letu ni kuhakikisha kila mmoja anapata fursa ya kujikwamua,” ameongeza

Hata hivyo amewataka wanufaika kuchangamkia fursa hizo kila zinapojitokeza na kuhakikisha wanarejesha mikopo kwa wakati ili wengine nao wapate kunufaika na mpango huo.

kwa upande wake, Mkurugenzi mtendaji wa CRDB Bank Foundation,Bi. Tully Esther Mwambapa, amesema kuwa  taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na serikali kupitia programu mbalimbali zinazolenga kuyawezesha makundi tofauti ya wananchi kiuchumi.

Amesema kuwa  lengo la programu ya imbeju ni kuwajengea uwezo wajasiriamali kwa kuwapatia mitaji pamoja na elimu ya usimamizi wa biashara ili waweze kuendesha miradi yao kwa tija na ufanisi.

" Hadi sasa taasisi hiyo imetoa mikopo ya mitaji wezeshi yenye thamani ya shilingi bilioni 22.1, huku zaidi ya wajasiriamali milioni moja wakinufaika nchini kote."amesema 

Amesema kuwa  mikopo hiyo imekuwa chachu ya kuboresha ustawi wa kiuchumi wa jamii na kuchangia katika ukuaji wa pato la taifa kupitia shughuli za uzalishaji mali zinazofanywa na wanufaika.

Baadhi ya wanufaika wa mikopo hiyo wameishukuru CRDB  kwa kuwagusa moja kwa moja katika maisha yao na kuahidi kuitumia mikopo hiyo katika shughuli za uzalishaji mali pamoja na kuirejesha kwa wakati ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini.

hafla hiyo imeelezwa kuwa sehemu ya jitihada za kuimarisha uchumi wa wananchi wa mtumba na kuongeza mchango wao katika maendeleo ya taifa.

Dkt. MSEMWA ATOA SHULE YA UWEKEZAJI KWA VIJANA WA CBE

February 17, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu - Dar es Salaam


Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais (Uwekezaji) Dkt. Fred Msemwa ametoa wito kwa vijana hususani walioko vyuo vikuu kujenga utamaduni wa kujifunza kuhusu uwekezaji, kwa kuwa wana faida ya kuwa na uwezo wa kiutendaji na utimamu wa kimwili.

Dkt. Msemwa, ametoa wito huo leo katika hafla ya uzinduzi wa Klabu ya Uwekezaji kwa Vijana (YIC) katika Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), Dar es Salaam, ambapo amesisitiza kuwa Dira 2050 imewapatia vijana umuhimu mkubwa kwa kuwaona wao kama rasilimaliwatu Muhimu.

“Dira inawatambua nyinyi kama rasilimali muhimu ya Taifa, inasisitiza kuwaandaa kuwa na ujuzi wa hali ya juu ili muiwezasha nchi kushindana kimataifa.” Alisema Dkt. Msemwa.

Katika mazungumzo yake na vijana hao, aliwapa changamoto ya kujiwekea msingi imara wa kiuchumi, akawafundisha nguzo nne muhimu zilizohusisha; kuwa na malengo, kujenga mtizamo sahihi, kujifunza kuweka akiba na kuwekeza, na kujifunza tabia ya kufanya zaidi.

Vile vile, Katibu Mkuu amewakumbusha kuwa Elimu ya Fedha, Ujasiriamali, Uwekezaji kwenye mifuko ya kijamii, na ujuzi wa Kuanzisha na Kusimamia Biashara, iliyokuwa ikitolewa katika hafla hiyo ilikuwa muhimu kwa kuwa inajibu changamoto zao binafsi na za jamii.

Ufunguzi wa Klabu hiyo, ni sehemu ya utekelezaji wa program ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA) unaolenga kukuza elimu ya fedha, ujasiriamali na utamaduni wa uwekezaji miongoni mwa vijana na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu nchini.










SERIKALI YAZINDUA AWAMU YA KWANZA YA MRADI WA KUPELEKA NISHATI SAFI YA KUPIKIA KWA TAASISI ZINAZOHUDUMIA WATU ZAIDI YA 100

February 17, 2026 Add Comment




📌*Unahusisha Shule za Sekondari 52 na Chuo kimoja cha VETA*


📌*Ni sehemu ya mradi wa Shilingi bilioni 25.8 wa kupeleka nishati safi ya kupikia kwa taasisi 453*


Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba,  amezindua awamu ya kwanza ya mradi wa kusambaza nishati safi ya kupikia katika taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100, unaohusisha shule 52 za sekondari pamoja na chuo kimoja cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika mikoa 18 ya Tanzania Bara.

Mradi huo ni sehemu ya mpango mkubwa wa kuunganisha miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika taasisi 453 wenye thamani ya Shilingi bilioni 25.8, ambapo gharama zote zinagharamiwa kwa asilimia 100 na Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

 Mhe. Salome Makamba amezindua mradi huo tarehe 17 Februari 2026 katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kondoa, mkoani Dodoma, ambayo imekuwa taasisi ya kwanza kufungiwa mfumo wa nishati safi ya kupikia kupitia mradi husika.


Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Salome amesema  kuwa mradi unahusisha usimikaji wa mifumo ya gesi ya LPG, ufungaji wa majiko banifu  pamoja na usambazaji wa mkaa mbadala katika taasisi 453.

Ameeleza kuwa katika awamu ya kwanza, taasisi 53 zitanufaika, huku awamu ya pili ikihusisha taasisi 400 zilizopo katika mikoa yote nchini.


Ametanabaisha kuwa, kuwepo kwa mradi huo ni  utekelezaji wa azma ya Serikali inayoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100 zinatumia nishati safi ya kupikia.

"Ili mradi huu uwe endelevu, nitoe wito kwa Serikali za Mitaa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na TAMISEMI kusimamia mifumo iliyofungwa ili iwe endelevu  suala litakalohamasisha jamii kuiga mfano wa taasisi za umma kuhamia katika nishati safi ya kupikia.” amesema Mhe. Salome



Aidha, ameitaka sekta binafsi kuona na kuchangamkia fursa iliyopo katika uzalishaji na usambazaji wa nishati safi ya kupikia ili kuongeza upatikanaji na kupunguza gharama kwa wananchi.


Vilevile, Mhe. Salome ameitaka REA kuchochea matumizi ya nishati safi ya kupikia katika maeneo ya minada, stendi na masoko. kwani tafiti zinaonesha kuwa kuna minada ya awali na upili ipatayo 13,763 pamoja na masoko ya samaki yapatayo 1,229 nchini, ambayo yanapaswa kufikiwa kutokana na kuhudumia kundi kubwa la wananchi.


Vilevile, amesisitiza uwekaji wa miundombinu ya nishati safi ya kupikia katika shule zote za umma na binafsi ili kutimiza azma ya Serikali kwa taasisi zinazohudumia zaidi ya watu 100 kutumia nishati hiyo.


Kwa walimu na wanafunzi, ametoa wito wawe mabalozi wa mabadiliko kwa kuanzisha klabu za nishati safi ya kupikia shuleni ili kupeleka ujumbe huo katika familia na jamii zinazowazunguka.


Kwa upande wake, Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Jonas Mbunda, amemshukuru Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha na kugharamia mpango wa nishati safi ya kupikia, akieleza kuwa unalinda afya za wananchi na mazingira.


Naye, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati ambaye ni Mkurugenzi wa Nishati Safi ya Kupikia, Nolasco Mlay, amesema mradi huo utapunguza matumizi ya kuni na mkaa katika taasisi za elimu, kuchangia uhifadhi wa mazingira, kuboresha afya na usalama wa wapishi pamoja na kuongeza ufanisi wa uendeshaji wa shule.


Aidha, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Jones Olotu, amesema takwimu zinaonesha kuwa matumizi ya nishati isiyo safi yamepelekea takribani hekta 46,606 za misitu kuharibiwa kila mwaka kwa ajili ya kuni na mkaa, watu zaidi ya 33,000 wakifariki kutokana na matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia na  wanawake na watoto wa kike kutumia saa 4 hadi 8 kutafuta kuni, jambo linaloathiri muda wa shughuli za maendeleo.


Amesema Serikali ilitambua changamoto hizo na hivyo kuja na mkakati wa nishati safi ya kupikia ili kulinda mazingira, afya na muda wa kufanya shughuli za maendeleo.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Nishati Jadidifu na Teknolojia za Nishati Mbadala kutoka REA, Mhandisi Advera Mwijage, amesema mradi wa nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kondoa umegharimu Shilingi milioni 54.


Amesema katika shule hiyo, limefungwa tanki la gesi lenye ujazo wa tani moja linaloweza kuhudumia upishi kwa takribani miezi miwili, pamoja na mfumo wa mkaa mbadala unaotokana na mabaki ya miwa.


Mkuu wa shule hiyo, Mwl. Flora Nusu, ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa mradi huo, akieleza kuwa utaondoa athari za kiafya kwa wapishi na muda uliokuwa ukipotea katika kutafuta kuni, na pia kupunguza gharama za uendeshaji kwa asilimia 40.

DKT.MATARAGIO AENDELEA NA MAJUKUMU JIJINI DODOMA

February 17, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu,


Katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi Asilia, Dkt. James Mataragio amepokelewa katika Ofisi za Wizara ya Nishati jijini Dodoma baada ya kuanza majukumu yake jijini Dar es salaam baada ya kupokelewa rasmi na Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi mwishoni mwa wiki iliyopita.


Jijini Dodoa amepokelewa na Wajumbe wa Menejimenti wakiongozwa na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bi. Ziana Mlawa pamoja na watumishi wote wa Wizara ya Nishati, mapema leo tarehe 17 Februari, 2026.

Dkt. Mataragio anatarajiwa kuongoza timu ya Wizara ya Nishati katika kusimamia sekta ya mafuta na gesi asilia nchini, kuhakikisha usalama wa mafuta na gesi asilia pamoja na kukuza matumizi ya nishati safi na endelevu; Pia Dkt. Mataragio anatarajiwa kuchangia katika kuendeleza sekta hiyo ili kuleta maendeleo endelevu kwa taifa letu na wananchi kwa ujumla.

Pia Dkt. Mataragio ameishukuru menejimenti na watumishi wa Wizara kwa mapokezi mazuri, ameahidi kufanya kazi kwa bidii, ushirikiano mzuri ili kuleta matokeo chanya katika sekta ya mafuta na gesi asilia nchini.

TRA YASIFU MATUMIZI MAZURI YA FEDHA UJENZI WA BWAWA LA JULIUS NYERERE

February 17, 2026 Add Comment


📌 Yasema mradi huo ni ushahidi wa thamani ya kodi za wananchi katika kuchochea maendeleo ya nchi 


📌Yahimiza ulipaji wa kodi kwa hiari na wakati kuwezesha utekelezaji endelevu wa miradi mingine inayoendelea nchini 


Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) imesifu matumizi sahihi ya fedha za kodi za watanzania katika Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere kufuatia ziara yao ya kikazi Februari 14, 2026, ikieleza kuwa mradi huo unaonyesha namna kodi zinavyochochea maendeleo kwa kuongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.


Ziara hiyo ilihusisha Viongozi na Maafisa Elimu na Mawasiliano kutoka vituo vyote nchini vya Mamlaka hiyo wakiwa na lengo la kujifunza na kujionea namna kodi za wananchi zilivyowezesha utekelezaji wa mradi huo mkubwa wa kimkakati wa taifa.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Mkurugenzi wa Elimu na Mawasiliano wa TRA, Bw. Richard Kayombo, alisema ziara yao katika Mradi wa Bwawa la Julius Nyerere ilikuwa muhimu kwa kuwa TRA ndiyo taasisi inayokusanya kodi, hivyo walitaka kujionea jinsi fedha za wananchi zinavyotumika na matokeo yake kwa maendeleo ya nchi.

Bw. Kayombo alisema mradi wa Bwawa la Julius Nyerere unaonyesha jinsi kodi zinavyobadilisha maisha ya wananchi kwa kuongeza umeme wa uhakika, kukuza biashara, uwekezaji na ukuaji wa uchumi, hivyo kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato ya Serikali.


Aliongeza kuwa, ongezeko la uzalishaji wa umeme nchini linasaidia kupunguza changamoto za mgao wa umeme na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na sekta binafsi. 


“ Mradi huu unatupa ushahidi kuwa kodi za wananchi zinapotumika ipasavyo katika kuleta matokeo makubwa yanayoonekana na kugusa maisha ya jamii moja kwa moja,” alisema Bw. Kayombo.


Kwa upande wao, Maafisa Elimu na Mawasiliano wa TRA walieleza kuwa, ziara hiyo imewapa uelewa mpana kuhusu uwekezaji uliofanywa na Serikali katika sekta ya nishati na kuahidi kuwa mabalozi wazuri wa kuhamasisha ulipaji wa kodi kwa hiari na wakati. 


Aidha, wameahidi kuendelea kuwaelimisha wananchi kuwa kodi wanazolipa zina mchango mkubwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo mfano , Bwawa la Julius Nyerere, ambalo sasa ni moja ya vyanzo muhimu vya umeme katika Gridi ya Taifa likichangia takribani jumla ya megawati 2115. 


Akizungumza kwa niaba ya uongozi wa kituo, Kaimu Meneja Uendeshaji na Udhibiti wa Mifumo wa Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere, Mha. Elinainyi Kalalu, alisema ziara hiyo imekuwa na tija kwa kuwa imewapa fursa ya kujionea namna fedha za wananchi zinavyotumika na matokeo yake kurudi kwao kupitia huduma bora ya umeme.


“ Ziara hii imekuwa na tija kubwa , nipende kusisitiza kuwa, Kituo kitaendelea kuzalisha umeme kwa weledi na ufanisi ili kuhakikisha huduma ya uhakika kwa wananchi. Ni muhimu pia kwa TRA kuendelea kuhamasisha ulipaji wa kodi, kwani ndizo zinazoziwezesha Serikali kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo nchini ,” alisisitiza Mha. Kalalu.


Ziara hiyo imekuwa ya mafanikio kwani imeimarisha uelewa kuwa ulipaji wa kodi kwa hiari na kwa wakati ni msingi wa utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo, ikiwemo uwekezaji katika sekta muhimu ya nishati ya umeme, kwa ustawi wa Taifa.

WAZIRI NDEJEMBI AKUTANA NA BALOZI WA OMAN,WAJADILI MASUALA YA MAFUTA NA GESI

February 17, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Oman nchini Tanzania, Mhe. Saud Al-Shidhani yaliyolenga kuimarisha na kuendeleza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili katika sekta ya nishati. Mazungumzo hayo yamefanyika leo, tarehe 17 Februari 2026, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati jijini Dar es Salaam.

Katika mazungumzo hayo, wamejadili kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo kubadilishana uzoefu wa kitaalamu, mafunzo kwa wataalamu, teknolojia ya uchimbaji pamoja na usimamizi wa miradi ya gesi na mafuta kwa lengo la kuharakisha maendeleo kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) na Shirika la Maendeleo ya Mafuta la Oman (PDO).