HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

MATUMIZI YA NISHATI SAFI YAPUNGUZA UKATAJI WA MITI MVOMERO

March 05, 2026 Add Comment




Na Mwandishi Wetu,


Wananchi wa Mvomero wamesema kuwa utekelezaji wa agizo la Serikali la kuhamasisha matumizi ya nishati safi umeanza kuleta matokeo chanya, ikiwemo kupungua kwa ukataji wa miti na uchomaji wa mkaa katika baadhi ya maeneo.


Hayo yameelezwa na baadhi ya wananchi wa Wilaya ya Mvomero wakati wa ziara ya timu kutoka Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF), iliyofika wilayani humo kutoa elimu kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia. 

Kampeni hiyo imefanyika katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Morogoro kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya nishati salama.

Wameeleza kuwa wananchi wengi sasa wameanza kuhamia katika matumizi ya gesi na umeme kwa ajili ya kupikia, jambo linalowasaidia kuokoa muda katika shughuli zao za kila siku pamoja na kujikinga na madhara ya kiafya yanayotokana na moshi wa kuni na mkaa.

Katika kampeni hiyo, wananchi wamepata fursa ya kushuhudia maonesho ya matumizi ya majiko ya gesi na umeme, ambapo walioneshwa jinsi yanavyoweza kupika chakula kwa haraka, kwa gharama nafuu na kuhifadhi ubora pamoja na ladha ya chakula. Hali hiyo imeongeza mwitikio wa wananchi wengi kuanza kutumia nishati safi ya kupikia.



TBA YASHIRIKI KLINIKI YA KUTATUA KERO ZA WANANCHI DODOMA

TBA YASHIRIKI KLINIKI YA KUTATUA KERO ZA WANANCHI DODOMA

March 05, 2026 Add Comment

Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Mkoa wa Dodoma unashiriki katika Kliniki maalum ya kutatua kero na changamoto mbalimbali za wananchi iliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, inayofanyika tarehe 3 hadi 6 Machi, 2026 katika viwanja vya Nyerere Square jijini Dodoma.

Kupitia kliniki hiyo, TBA inakutana na wateja wake ambao ni wapangaji wa nyumba zake kwa lengo la kusikiliza na kutatua changamoto pamoja na kero mbalimbali zinazojitokeza katika maeneo wanayoishi.

Aidha, kliniki hiyo imekuwa fursa kwa taasisi mbalimbali za Serikali kutoa elimu kwa wananchi pamoja na kueleza mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa majukumu yao ndani ya siku 100 za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu kuingia madarakani.

Katika kliniki hiyo, TBA kama zilivyo taasisi nyingine za Serikali imeweka banda maalum kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kuhusu majukumu yake pamoja na kueleza miradi mbalimbali iliyotekelezwa na wakala huo katika kipindi hicho.

Akitembelea mabanda ya taasisi mbalimbali katika viwanja hivyo leo Machi 5, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule, ameipongeza TBA kwa kutekeleza miradi mikubwa ya Serikali katika mkoa wa Dodoma, ikiwemo ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na mradi wa ujenzi wa nyumba 3,500 za makazi ya watumishi wa umma katika eneo la Nzuguni.

Kwa upande wao, wananchi waliotembelea banda la TBA wamepongeza utekelezaji wa mradi wa nyumba za makazi katika eneo la Nzuguni, wakisema umechangia kusogeza huduma za kijamii na biashara karibu na wananchi pamoja na kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

WAZIRI NDEJEMBI AKUTANA NA CHAMA CHA WAAGIZAJI NA WASAMBAZAJI WA MAFUTA TAOMAC

March 05, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Chama cha Waagizaji na Wasambazaji wa Mafuta Tanzania (TAOMAC) kwa lengo la kuboresha na kukuza sekta ya mafuta nchini pamoja na kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali na wadau wa sekta hiyo.

Kikao hicho kimefanyika leo, Machi 5, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati zilizopo jijini Dar es Salaam.


Katika Kikao hicho wamejadili masuala mbalimbali yanayolenga kuimarisha usimamizi, ufanisi na maendeleo ya sekta ya mafuta nchini kwa manufaa ya uchumi na wananchi kwa ujumla.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Kamishna wa Mafuta kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Goodluck Shirima; Mtendaji Mkuu wa PBPA, Bw. Erasto Simon; Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Mwainyekule; pamoja na viongozi na wanachama wa TAOMAC.






MAKATIBU WAKUU VYAMA VYA UKOMBOZI WAJADILI HALI YA KISIASA KUSINI MWA AFRIKA

March 05, 2026 Add Comment


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeongoza Kikao cha 12 cha Makatibu Wakuu wa Vyama vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, ambapo, pamoja na mambo mengine, vimejadili hali ya siasa, ukombozi wa kiuchumi na kuboresha hali za wananchi katika nchi zao. 

Kikao hicho kilichofanyika leo tarehe 5 Machi 2026, Kibaha, mkoani Pwani, kilihusisha Makatibu Wakuu wa Vyama 6 vya Ukombozi Kusini mwa Afrika, ambavyo ni ANC (Afrika Kusini), CCM (Tanzania), FRELIMO (Msumbiji), SWAPO (Namibia), ZANU-PF (Zimbabwe) na MPLA (Angola).

Akizungumza na vyombo vya habari baada ya mkutano huo, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Asha-Rose Migiro, amesema kuwa katika kikao hicho wamepitia maazimio ya Mkutano Mkuu wa Wakuu wa Vyama hivyo uliofanyika mwaka jana, nchini Afrika ya Kusini. 

Alisema mijadala ilijikita kuangalia hali ya kisiasa katika ukanda wa Kusini mwa Afrika, hususan kulinda uhuru wa kisiasa na kiuchumi, kutathmini malengo ya harakati za ukombozi pamoja na kuendelea kulinda na kuimarisha uhuru uliopatikana.


Dkt. Migiro amesema jukumu kubwa la vyama hivyo ni kuimarisha mshikamano na umoja wao pamoja na kujadili changamoto mbalimbali zinazoikabili kanda hiyo ikiwemo mabadiliko ya tabianchi. Aidha, walijadili namna ya kutatua migogoro katika nchi wanachama na kuchochea maendeleo ya kiuchumi, kisiasa na kijamii.


Katika kikao hicho pia walifanya mapitio ya maendeleo yaliyopatikana katika nchi zao, ikiwa ni pamoja na kuimarisha huduma za jamii, kuboresha miundombinu pamoja na kuweka mikakati ya kujenga uchumi stahimilivu na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Masuala mengine yaliyojadiliwa ni pamoja na umuhimu wa kuongeza ajira kwa vijana, kuwawezesha wanawake pamoja na kujenga uchumi jumuishi na stahimilivu kwa maendeleo ya Ukanda wa Kusini mwa Afrika.


#Ends

EWURA KANDA YA KASKAZINI YAWANOA VIONGOZI WA WILAYA YA KOROGWE

EWURA KANDA YA KASKAZINI YAWANOA VIONGOZI WA WILAYA YA KOROGWE

March 05, 2026 Add Comment

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kupitia Kanda ya Kaskazini, leo tarehe 5 Machi 2026 imetoa elimu kwa viongozi wa Wilaya ya Korogwe katika semina iliyofanyika katika ukumbi wa GMCC.

Akimkaribisha Mgeni Rasmi, Meneja wa EWURA Kanda ya Kaskazini, George Mhina, alisema lengo ni kuwajengea viongozi uelewa kuhusu majukumu ya EWURA na maeneo inayoyadhibiti ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Katika semina hiyo, washiriki walipatiwa elimu kuhusu umuhimu wa uvunaji wa maji ya mvua, matumizi ya nishati safi ya kupikia, leseni za mafundi umeme, ujenzi wa vituo vya mafuta vijijini pamoja na namna ya kutatua migogoro katika sekta za maji na nishati.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Mhe. William Mwakilema amewasisitiza viongozi hao kuwa mabalozi wa elimu waliyoipata kwa kuhakikisha wanaifikisha kwa wananchi ili kuongeza uelewa na matumizi sahihi ya huduma za maji na nishati.

 

SHEIKH MKUU WA TANZANIA AWAHAMASISHA WANAWAKE KUMILIKI ARDHI BAADA YA KUPATA HATI SAMIA ARDHI KLINIKI

March 05, 2026 Add Comment
Dar es salaam –
Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, ametoa wito kwa Watanzania kujitokeza kwa wingi kutumia fursa ya huduma za ardhi zinazotolewa kupitia Samia Ardhi Kliniki, akisisitiza umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi kama njia ya kujikomboa kiuchumi.
Mufti Zubeir alitoa kauli hiyo baada ya kufika katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika katika Ofisi za Ardhi za Mkoa wa Dar es Salaam, ambapo alipata hati ya ardhi huku akishuhudia namna wananchi wanavyohudumiwa katika kliniki hiyo ambayo inaendelea nchi nzima.
Akizungumza mara baada ya kupata huduma hiyo, Mufti Zubeir alisema hatua ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kuandaa Samia Ardhi Kliniki yenye kulenga kuwapa kipaumbele wanawake ni jambo muhimu linalosaidia kuongeza usawa katika umiliki wa rasilimali muhimu kama ardhi.
Alisema wanawake wanapaswa kutumia kikamilifu fursa hiyo ili waweze kupata hati za ardhi na kujiimarisha kiuchumi.
“Wanawake wana haki ya kumiliki mali mbalimbali ikiwemo magari na mali nyingine, hivyo hakuna sababu ya kuwanyima nafasi ya kumiliki ardhi. Ni muhimu jamii, hususan wanaume, kuachana na mila kandamizi zinazowazuia wanawake kumiliki rasilimali,” alisema Mufti Zubeir.
Aidha, aliwataka wanaume kuwapa nafasi wanawake kumiliki ardhi ili kuongeza idadi ya wanawake wenye umiliki rasmi wa ardhi nchini, jambo ambalo litasaidia kuimarisha ustawi wa familia na jamii kwa ujumla.
Katika hatua nyingine, Mufti Zubeir alipongeza maandalizi mazuri yaliyofanywa na Ofisi ya Mkoa wa Dar es Salaam katika uendeshaji wa kliniki hiyo, kuanzia mapokezi hadi utoaji wa huduma kwa wananchi.
Alisema namna wateja wanavyohudumiwa kwa ufanisi ni jambo jema lenye manufaa kwa jamii na lina thawabu kubwa mbele za Mwenyezi Mungu, hususan katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Mufti Zubeir pia aliwaombea heri watumishi wanaotoa huduma katika kliniki hiyo ili waendelee kuwahudumia wananchi kwa uadilifu na bidii.
Samia Ardhi Kliniki zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini kwa lengo la kurahisisha upatikanaji wa huduma za ardhi, hususan kwa wanawake, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa Machi 8 kila mwaka.
 
 
SERIKALI, SEKTA BINAFSI KUIMARISHA HUDUMA ZA DHARURA KUCHOCHEA AJIRA NCHINI

SERIKALI, SEKTA BINAFSI KUIMARISHA HUDUMA ZA DHARURA KUCHOCHEA AJIRA NCHINI

March 05, 2026 Add Comment






Na Abduly Iddy, Dar es Salaam

Serikali imesema ushirikiano kati yake na Sekta binafsi utaendelea kuwa chachu muhimu ya kuimarisha huduma za afya nchini, hususan katika kuboresha huduma za dharura kupitia mpango wa kuanzisha uzalishaji wa magari ya wagonjwa (ambulance) mkoani Tanga.

Akizungumza Machi 5, 2026 jijini Dar es Salaam katika kikao cha maandalizi ya kuanzisha uzalishaji wa magari hayo, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe.Batilda Burian, amesema Serikali inakaribisha uwekezaji huo unaofanywa kwa kushirikiana na SO Company Limited kwani utaimarisha upatikanaji wa huduma za dharura za afya nchini hususan magari ya wagonjwa.

Amesema uzalishaji wa ambulance ndani ya nchi utaongeza upatikanaji wa magari ya kisasa ya kuwahudumia wagonjwa na kupunguza muda wa kuwafikia wananchi wanaohitaji msaada wa haraka wa kitabibu, hatua itakayosaidia kuokoa maisha ya watu.

“Mradi huu ni hatua muhimu tunapoimarisha mfumo wetu wa huduma za afya. Kupatikana kwa ambulance zinazozalishwa hapa nchini kutarahisisha usambazaji wake katika maeneo mbalimbali, hususan ya pembezoni,” amesema, RC Batlida.

Aidha, amesema mradi huo pia utaleta manufaa ya kiuchumi kwa kufungua fursa za ajira kwa vijana, kukuza wazalishaji wa ndani wa vipuri na kuchochea maendeleo ya sekta zinazohusiana na uzalishaji wa vifaa vya magari na huduma za afya.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Dharura na Maafa kutoka Wizara ya Afya, Dkt. Erasto Sylvanus, amesema Serikali itaendelea kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji ili kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kwa ufanisi na kuchangia maendeleo ya sekta ya afya pamoja na uchumi wa taifa.

Mradi huo unatarajiwa kuimarisha huduma za dharura za afya huku ukifungua fursa mpya za ajira na maendeleo ya kiuchumi nchini.

SENYAMULE AIPA KONGOLE WIZARA YA ARDHI KUANZISHA SAMIA ARDHI KLINIKI

SENYAMULE AIPA KONGOLE WIZARA YA ARDHI KUANZISHA SAMIA ARDHI KLINIKI

March 05, 2026 Add Comment

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule ameipongeza Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa kuendesha zoezi la Samia Ardhi Kliniki linalofanyika nchi nzima.

Mhe. Senyamule ametoa pongezi hizo leo Machi 5, 2026 alipotembelea kliniki hiyo inayoendelea katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Dodoma.

“Nimekaa sijawahi kuona ubunifu wa jambo hili, na nimeambiwa linafanyika nchi nzima ya Tanzania. Hiki ni kitu cha pekee sana,” amesema Senyamule.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa mkoa wa Dodoma, awali aliposikia kuhusu kliniki hiyo alijiuliza kama kutapatikana wanawake wa kutosha kwenda kutatuliwa kero zao za ardhi, lakini hali imekuwa tofauti.

“Nilijiuliza kama wanawake watapatikana kwa wingi, lakini leo nimeshangaa kuona na kushuhudia kuwa sasa wanawake wengi wanamiliki ardhi,” amesema Senyamule.

Aidha, amesema kuwa kama jambo hilo lingefanyika miaka kumi au ishirini iliyopita, isingekuwa rahisi kupata wanawake wengi kwa sababu wengi hawakuwa na uelewa wa haki yao ya kumiliki ardhi.

“Kama ungelifanya jambo hili miaka kumi au ishirini iliyopita na kusema wanawake waje washughulikie kero zao za ardhi na kupata hati, usingewapata wengi kwa sababu wakati huo hatukuwa na uelewa kuwa sisi pia tunastahili kumiliki ardhi,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mhe. Senyamule amewaasa wanawake kutunza vizuri hati zao za ardhi, akieleza kuwa ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa inayoongezeka kila siku.

“Ukishapata hati yako, itunze vizuri kwa sababu ardhi ya Dodoma ina thamani kubwa na thamani yake inaendelea kuongezeka kila siku,” amesema.

Sambamba na hilo, Mhe. Senyamule pia amekabidhi hati miliki kwa baadhi ya wanawake waliofika katika kliniki hiyo iliyofanyika katika viwanja vya Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Dodoma.

Samia Ardhi Kliniki ilianza rasmi tarehe 2 Machi 2026 katika mikoa yote nchini na inatarajiwa kuhitimishwa tarehe 7 Machi 2026 yenye Kauli Mbiu, Mwanamke; Haki Yako, Miliki Ardhi sasa.