HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

*RAIS DKT.SAMIA S. HASSAN KUFUNGUA MKUTANO MKUBWA WA MADINI NOVEMBA 2026*

June 27, 2026 Add Comment



-▪️Ni Mkutano mkubwa wa Madini na Uwekezaji

▪️Washiriki 2000 kutoka mataifa 50 Duniani kushiriki

▪️Kauli Mbiu ya Mkutano inalenga kuongeza thamani madini kwa maendelezo ya Viwanda

▪️Serikali na Sekta Binafsi kushirikiana kuandaa mkutano huo


▪️Waziri Mavunde azindua rasmi maandalizi ya mkutano huo



📍 DAR ES SALAAM. 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Dkt. Samia S. Hassan anatarajiwa kufungua rasmi Mkutano wa Saba wa Madini na Uwekezaji Tanzania (TMIC 2026) utakaofanyika Novemba 19 hadi 21, 2026 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), Dar es Salaam.

Akizungumza leo Juni 27, 2026 wakati wa uzinduzi wa TMIC 2026, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema serikali imeamua kujenga uchumi wa viwanda unaotokana na madini kwa kuwekeza katika uchakataji na uyeyushaji wa madini badala ya kuendelea kuuza malighafi.

Amesema kaulimbiu ya mkutano huo, "Madini Yaliyoongezwa Thamani: Chachu ya Ukuaji wa Viwanda na Uchumi," inaakisi dira ya serikali ya kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha uchakataji wa madini barani Afrika.

Kwa mujibu wa Mhe. Mavunde, amesema Tanzania tayari ina viwanda vinane vya kusafisha dhahabu, huku Mkoa wa Dodoma ukiwa na viwanda tisa vinavyojengwa na vinavyoendelea na uzalishaji pamoja na kiwanda kikubwa cha kuyeyusha madini ya nikeli na shaba.

"Zaidi ya Sh bilioni 600 zinawekezwa katika ujenzi wa kiwanda cha chuma kitakachotumia asilimia 100 ya malighafi za ndani, huku uwekezaji mwingine ukiendelea Kigamboni na Tanga kwa ajili ya uchakataji wa madini ya 'Heavy Mineral Sands' na mradi wa madini ya niobium wa Panda Hill, Mbeya," amesema Mhe. Mavunde

Amesema, katika kuongeza ushiriki wa Watanzania kwenye sekta hiyo,  thamani ya manunuzi kupitia mpango wa 'Local Content' imefikia Sh trilioni 5.1, huku bidhaa 20 zikitakiwa kuzalishwa na wazawa kwa ajili ya kuhudumia migodi mikubwa.

 Amesisitiza wafanyabiashara kuzingatia uaminifu na viwango vya kimataifa ili kunufaika zaidi na fursa hizo.

Amesema sekta ya madini imeendelea kuimarisha mchango wake katika uchumi kwa kuingiza Sh trilioni 1.374 katika Mfuko Mkuu wa Serikali, kiwango kilichovuka lengo la Sh trilioni 1.2 kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Mavunde, amesema Serikali imeidhinisha asilimia 10 ya mapato yote ya sekta ya madini kuelekezwa kwenye utafiti wa kina wa jiofizikia ili kuongeza maeneo yanayofahamika kuwa na madini kutoka asilimia 16 ya sasa hadi asilimia 50 ifikapo mwaka 2030.

Aidha, amesema Serikali inaandaa mfuko maalumu wa mikopo kwa wachimbaji wadogo, ambao licha ya changamoto za mitaji na teknolojia, wanachangia takribani asilimia 40 ya mapato ya sekta ya madini.

Katika hatua nyingine, amesema Serikali inaanza operesheni ya kufuta kidijitali leseni zote za madini zisizotumika. Wamiliki watakaoshindwa kuwasilisha taarifa ndani ya muda uliowekwa watapewa notisi ya siku 30 kabla ya leseni hizo kujifuta moja kwa moja.

Nae, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba, amesema Serikali imejipanga kuhakikisha utajiri wa madini unakuwa chachu ya kukuza viwanda vya ndani, kuongeza ajira na kuimarisha uchumi kupitia uongezaji thamani badala ya kuishia kwenye uchimbaji pekee.

Amesema TMIC 2026 utawakutanisha viongozi wa Serikali, taasisi za fedha, kampuni za madini, wataalamu wa teknolojia, watafiti na wadau wengine kutoka duniani kote kujadili fursa za uwekezaji na maendeleo ya sekta hiyo.

 "Huu ni wakati wa kuingia katika awamu mpya ya uwekezaji, ubunifu na ukuaji wa sekta ya madini nchini," amesema.

Kwa upande wa Katibu Mtendaji wa Chemba ya Migodi Tanzania, Mhandisi Benjamin Mchwampaka, amesema mkutano huo unatarajiwa kuwakutanisha washiriki zaidi ya 2,000 na watoa mada zaidi ya 100 kutoka mataifa zaidi ya 50, huku zaidi ya mada 20 zikijadiliwa zikiwemo sera, kodi, uwekezaji, teknolojia, nishati safi, madini ya kimkakati, uongezaji thamani na masuala ya mazingira, jamii na utawala bora (ESG).

Mchwampaka amesema TMIC 2026 pia utaweka mkazo katika maendeleo ya wachimbaji wadogo pamoja na ushirikishwaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika mnyororo mzima wa uongezaji thamani wa madini. Mkutano huo unatarajiwa kufungwa rasmi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi.

..........




 

MTAKUWWA YAZINDUA KAMPENI Ya 'AMSHA ARI' MIRONGO KUHAMASISHA KUPINGA UKATILII KWA WANAWAKE NA WATOTO

June 27, 2026 Add Comment

 




Mwanza. Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Wanawake na Watoto Mkoa wa Mwanza (MTAKUWWA) imezindua kampeni ya Amsha Ari katika Kata ya Mirongo, ikiwa na lengo la kuhamasisha jamii kushiriki katika malezi bora ya watoto, kuzuia mmomonyoko wa maadili na kutokomeza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Uzinduzi wa kampeni hiyo uliwashirikisha waendesha bodaboda wa Kata ya Mirongo, ambao walieleza utayari wao wa kushiriki kikamilifu katika kuelimisha jamii kuhusu madhara ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto pamoja na kuhamasisha ulinzi wa makundi hayo.

Aidha, waendesha bodaboda hao waliitaka jamii kuendelea kudumisha amani iliyopo nchini na kuwahimiza vijana kuepuka kutumika katika vitendo vya uchochezi vinavyoweza kuhatarisha usalama wa wananchi na mali zao.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mwenyekiti Mwenza wa MTAKUWWA Mkoa wa Mwanza, Yassin Ally, aliwataka waendesha bodaboda kuwa mstari wa mbele katika kufichua vitendo vya ukatili, kutoa elimu kwa jamii kuhusu athari zake na kushiriki kulinda maadili ya jamii.

Kwa upande wao, baadhi ya wajumbe wa MTAKUWWA Mkoa wa Mwanza, akiwemo Twaha Bakari, ambaye ni kiongozi wa dini, na Fatuma Mpinga, Mkaguzi wa Polisi wa Kata ya Mirongo, walisisitiza umuhimu wa kampeni hiyo kwa kuhimiza jamii kushiriki kikamilifu katika malezi ya watoto, kulinda maadili na kuendeleza amani ya nchi.




MWENGE WA UHURU WAKABIDHI GARI LA WAGONJWA LUSHOTO

June 27, 2026 Add Comment

Na Ashrack Miraji, Lushoto

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Bw. Wazo Mwang'onda, amekabidhi gari jipya la kubebea wagonjwa kwa Hospitali ya Wilaya ya Lushoto, akisema hatua hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha huduma za afya na kuwafikisha wananchi huduma muhimu kwa wakati.

Akizungumza wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru yaliyofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Kizala, wilayani Lushoto, Bw. Mwang'onda amesema ujio wa gari hilo unaonesha dhamira ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuboresha sekta ya afya kupitia ujenzi wa vituo vya afya, zahanati pamoja na upatikanaji wa magari ya wagonjwa katika maeneo mbalimbali nchini.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI na Mbunge wa Jimbo la Lushoto, Prof. Riziki Shemdoe, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia wananchi wa Lushoto gari hilo, akieleza kuwa litasaidia kwa kiwango kikubwa kuboresha huduma za rufaa kwa wagonjwa wanaohitaji usafiri wa haraka kwenda kupata matibabu.

Prof. Shemdoe amesema gari lililokuwa likihudumia Hospitali ya Wilaya lilihamishiwa Kituo cha Afya Mlola ili kuimarisha utoaji wa huduma katika eneo hilo, hivyo ujio wa gari jipya unakwenda kuziba pengo lililokuwepo na kuongeza ufanisi wa huduma za afya katika wilaya hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Zephania Sumaye, amesema ujio wa gari hilo la kubebea wagonjwa unaakisi dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi. Amesema uongozi wa wilaya utaendelea kusimamia matumizi sahihi ya gari hilo ili liweze kuwahudumia wananchi kwa ufanisi na kuongeza kasi ya utoaji wa huduma za dharura.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Dkt Ikupa Harrison amesema halmashauri itaendelea kuimarisha huduma za afya kwa kuboresha miundombinu, vifaa tiba na huduma za usafiri wa wagonjwa ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati.

Katika hatua nyingine, Mwenge wa Uhuru umeendelea kutembelea na kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo wilayani Lushoto, ikiwemo mradi wa barabara, hoteli ya kitalii, ukarabati wa matenki ya maji, ujenzi na ukamilishaji wa madarasa, mradi wa kuwawezesha vijana pamoja na Kituo cha Afya. Baada ya kumaliza shughuli zake wilayani humo, Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kukabidhiwa Wilaya ya Korogwe kwa ajili ya kuendelea na mbio zake.







 

TRA KARIAKOO YAENDELEZA UWAJIBIKAJI KWA JAMII KUELEKEA TUZO ZA RAIS KWA WALIPAKODI NA MIAKA 30 YA TRA

June 26, 2026 Add Comment
Kariakoo, 26 Juni 2026

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kariakoo imeendelea na maadhimisho ya miaka 30 ya TRA na maandalizi ya Tuzo za Rais kwa Walipakodi kwa kutekeleza shughuli za uwajibikaji kwa jamii, ambapo leo imekabidhi vifaa tiba katika Hospitali ya Mnazi Mmoja. Msafara huo uliongozwa na Kaimu Meneja wa Mkoa wa Kikodi Kariakoo, Bw. Edson Issanya.

WAZIRI SANGU: SERIKALI ITAENDELEA KUONGEZA WIGO WA FURSA ZA AJIRA

June 26, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu akizungumza wakati wa hafla ya kuwaaga vijana 400 wa Kitanzania waliopata fursa za ajira nje ya nchi iliyofanyika katika Ukumbi wa NSSF Mafao House jijini Dar es Salaam, tarehe 25 Juni, 2026.

MZUMBE YAWAJENGEA UWEZO WATANZANIA KUNUFAIKA NA FURSA ZA PPP

June 26, 2026 Add Comment
CHUO Kikuu cha Mzumbe kimesema mafanikio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yatategemea kwa kiwango kikubwa ushiriki wa sekta binafsi, hususan katika kuzalisha ajira, kuvutia mitaji na kuharakisha ukuaji wa uchumi wa kisasa na wenye ushindani.

KAFULILA: DIRA YA 2050 YAHITAJI NGUVU YA SEKTA BINAFSI

June 26, 2026 Add Comment
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC), David Kafulila amesema Tanzania haiwezi kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kwa kutegemea kodi na mikopo pekee, akisisitiza umuhimu wa kuimarisha ubia kati ya Serikali na sekta binafsi katika kugharamia na kuendesha miradi ya maendeleo.

Oryx gas, kidoti foundation kuhamasisha nishati ya kupikia kwa watoa huduma za saluni

June 26, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu 

KAMPUNI ya Oryx Gas Tanzania kwa kushirikana na taasisi ya Kidodi Foundation wameingia makubaliano ya kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini kwa kulifiki kundi la watoa huduma za Saluni nchini.

UTEKELEZWAJI WA MIPANGO YA KUIMARISHA HAKI NA USTAWI KWA WATU WENYE ULEMAVU WASISITIZWA MWANZA

June 26, 2026 Add Comment

       

Na Mwandishi Wetu, Mwanza.

Serikali imezitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa, watendaji wa sekta mbalimbali pamoja na wadau wa masuala ya Watu wenye Ulemavu kuhakikisha Mpango Kazi wa Taifa wa Haki na Ustawi kwa Watu wenye Ualbino (MTHUWWU) na Mkakati wa Taifa wa Teknolojia Saidizi (NATS) vinatekelezwa kikamilifu ili kuboresha huduma na kulinda haki za Watu wenye Ulemavu nchini. 

NAFUU YA MAFUTA KUANZA KUONEKANA JULAI-WAZIRI NDEJEMBI

June 26, 2026 Add Comment




Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema Watanzania wataanza kushuhudia kushuka kwa bei za mafuta kuanzia mwezi Julai mwaka huu kufuatia kuanza kushuka kwa bei ya mafuta ghafi katika soko la dunia baada ya kusitishwa kwa mapigano ya Mashariki ya Kati.


Akijibu mwongozo wa Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, Bungeni jijini Dodoma leo, Juni 26, 2026, Waziri Ndejembi amesema Serikali imezielekeza EWURA, TPDC na PBPA kuhakikisha manufaa ya kushuka kwa bei za mafuta katika soko la dunia yanawafikia walaji nchini.


Amesema licha ya athari za vita kati ya Iran, Israel na Marekani zilizosababisha usumbufu katika usafirishaji wa mafuta kupitia Mlango wa Hormuz, Tanzania iliendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta bila kukumbwa na uhaba.


Ndejembi amesema hatua za haraka zilizochukuliwa na Serikali zilihakikisha mafuta yanapatikana katika maeneo yote ya nchi, huku Tanzania ikiendelea kuwa miongoni mwa nchi zenye bei nafuu za mafuta katika ukanda wa Afrika Mashariki.


Ameeleza kuwa baada ya makubaliano ya kusitisha mapigano, bei ya mafuta ghafi imeanza kushuka hadi kufikia takribani dola 70 kwa pipa, hali inayotarajiwa kuleta nafuu katika soko la ndani kadri shehena mpya zilizonunuliwa kwa bei ya chini zitakavyoingia nchini.


“Watanzania wataanza kuona punguzo la bei kuanzia mwezi Julai, na kadri shehena mpya za mafuta zilizonunuliwa kwa bei nafuu zitakavyoendelea kuwasili nchini, ndivyo bei zitakavyozidi kushuka,” amesema Waziri Ndejembi.


Aidha, amesema wataalamu wa soko la dunia wanatarajia ndani ya wiki nane hadi 10 bei za mafuta kurejea katika viwango vilivyokuwepo kabla ya kuanza kwa mgogoro huo mwezi Februari mwaka huu.


Waziri Ndejembi ameongeza kuwa Serikali itaendelea kufuatilia mwenendo wa soko la dunia huku ikiimarisha mikakati ya muda mrefu ya kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini, ikiwemo kuongeza vyanzo vya uagizaji wa mafuta na kuharakisha utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa kiwanda cha kusafisha mafuta mkoani Tanga ili kuimarisha usalama wa nishati nchini.

KATIBU MTENDAJI UNCDF ASIFU MCHANGO WA UWEKEZAJI KUPITIA HATIFUNGANI YA TANGA UWASA KWA JAMII

June 26, 2026 Add Comment


Mamlaka ya Majisafi na usafi wa Mazingira Tanga (Tanga UWASA) imepokea ugeni wa viongozi wa kanda na wawakilishi kutoka Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Mitaji (UNCDF) ukiongozwa na Katibu Mtendaji wa Mfuko huo Bw. Pradeep Kurukulasuriya uliolenga kutembelea na kujionea maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji huduma ya maji Tanga awamu ya tatu kupitia ufadhili wa Hatifungani ya Kijani ambapo UNCDF ni miongoni mwa wadau muhimu walioshiriki katika hatua za awali za kufanikisha mradi huo.

Katika ziara hiyo, Katibu Mtendaji na wageni walipokea taarifa ya mradi na mwenendo wa magawio kwa wawekezaji pamoja na kutembelea eneo la mradi na kujionea kasi ya utekelezaji wa shuguli mbalimbali zinazolenga kuongeza na kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika kwa wakazi wa maeneo ya kihuduma ya Tanga UWASA unaotarajiwa kukamilika mapema mwezi Agosti, 2026.

Katibu Mtendaji pamoja na wageni walipata pia fursa ya kufanya kikao na sehemu ya wanufaika wa mradi wa Hatifungani katika Hospiali ya Jiji iliyopo kata ya Masiwani ambapo awali walikuwa wakipata changamoto katika kutoa huduma kutokana na adha ya upatikanaji wa huduma ya maji ya uhakika na kupitia mradi wa Hatifungani wameboreshewa miundombinu hivyo kuimarisha upatikanaji wa uhakika wa huduma ya majisafi.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF Bw. Pradeep Kurukulasuriya  ameipongeza Tanga UWASA kwa uthubutu huo na kwa maendeleo mazuri ya utekelezaji wa mradi lengwa sambamba na kuonesha nia ya kuongeza wigo wa kuendelea kushirikiana.


" Tunajivunia kuwa sehemu ya mchango katika kufanikisha Hatifungani ya Kijani ya Tanga na matarajio yetu ni kwamba mradi huu utaboresha maisha ya jamii na kupitia hili Tanga UWASA imedhihirisha kuwa inawezekana kuhamasisha uwekezaji ndani ya nchi kwani takriban asilimia 65 ya uwekezaji ulitoka kwa wawekezaji wa Kitanzania, na kwa kupitia mpango huu, tumedhihirisha kuwa mitaji ya ndani inaweza kuhamasishwa ili kufadhili miradi muhimu ya maendeleo na kwa sasa tunasoma mfano huu kwa karibu, tunatafuta kuelewa ni nini kilifanya kazi vizuri, changamoto zipi zilizojitokeza, na ni somo gani tunaweza kujifunza ili tuweze kuiga mafanikio ya Hatifungani ya Tanga si tu ndani ya Tanzania bali katika nchi nyingine pia", alisema Bw. Kurukulasuriya.

Awali kabla ya ziara hiyo, Katibu Mtendaji wa UNCDF na wageni wakiongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Tanga UWASA, Eng. Salum Ngumbi walifika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kutoa salamu na kupokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Tanga Mhe. Dadi Kolimba aliyetoa salamu za Mkoa kwa niaba ya Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Buriani Mkuu wa Mkoa wa Tanga






FCC YAHIMIZA WADAU KUUNGANA KULINDA AFYA NA UCHUMI

FCC YAHIMIZA WADAU KUUNGANA KULINDA AFYA NA UCHUMI

June 26, 2026 Add Comment
 

Serikali imetoa wito kwa wazalishaji, waingizaji bidhaa, wasambazaji, wafanyabiashara, vyombo vya habari, vyombo vya dola, mamlaka za forodha, Taasisi za umma, asasi mbalimbali pamoja na wananchi kwa ujumla kuendelea kushirikiana kwa karibu na Tume ya Ushindani (FCC) katika kubaini na kudhibiti bidhaa bandia.

Vilevile, ameipongeza FCC kwa kuendelea kuimarisha juhudi katika kukabiliana na changamoto ya bidhaa bandia na kulipa uzito unaostahili katika mipango ya baadaye ili kuendelea kuboresha mazingira ya biashara Nchi

Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Sixtus Mapunda, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Kudhibiti Bidhaa Bandia Duniani (WACD) 2026.

Aidha, amesema Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kuunga mkono FCC kupitia maboresho ya sera, sheria na mifumo ili kuhakikisha masoko salama na ushindani wa haki ili kukabiliana na athari zake kwa afya za wananchi na uchumi wa taifa.

Mapunda pia amesema FCC inapaswa kupanua matumizi ya teknolojia katika uchunguzi, ufuatiliaji na udhibiti wa bidhaa bandia, hususan katika masoko ya kidijitali na mipaka ya nchi ili kuziba mianya inayotumiwa na wahalifu wa kiuchumi.

Akizungumzia kaulimbiu isemayo, “Linda Maisha na Masoko Dhidi ya Pombe, Vilainishi na Sigara Bandia,” amesema bidhaa bandia zina madhara kwa afya, hupunguza mapato ya Serikali na kudhoofisha biashara halali.

Naye, Kamishna wa Tume Bw. Said Tunda ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa FCC Dkt. Aggrey Mlimuka amesema kampeni za elimu kwa umma na mijadala ya kitaalamu zimeendelea kuongeza uelewa kuhusu athari za bidhaa bandia kwa afya, uchumi na maendeleo ya biashara halali nchini.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa, amesema maadhimisho yanalenga kuongeza uelewa wa umma kuhusu madhara ya bidhaa bandia na kuimarisha ushirikiano wa wadau.

FIDIA ZAANZA KUMWAGIKA PANGANI, WANANCHI 474 KUPISHA MRADI WA SUKARI WA DOLA MILIONI 350

June 26, 2026 Add Comment

 




Na Oscar Assenga, Pangani

SERIKALI imeanza rasmi kulipa fidia kwa wananchi 474 wa vijiji vya Mseko na Kigurusimba, Kata ya Masaika, Wilaya ya Pangani mkoani Tanga, kupisha utekelezaji wa mradi mkubwa wa kilimo cha miwa na ujenzi wa kiwanda cha sukari wenye thamani ya dola za Marekani milioni 350.

Hatua hiyo inaashiria mwanzo wa utekelezaji wa moja ya miradi mikubwa ya uwekezaji nchini inayotarajiwa kuzalisha maelfu ya ajira, kuongeza uzalishaji wa sukari na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Wilaya ya Pangani na taifa kwa ujumla.

Akizindua rasmi zoezi la ulipaji fidia, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Dkt. Batilda Burian, alisema Serikali imeanza kuwalipa wananchi wote waliokamilisha taratibu zinazohitajika ili kuondoa vikwazo vya utekelezaji wa mradi huo.

Alisema zaidi ya wananchi 400 tayari wamekamilisha kusaini nyaraka zinazowaruhusu kupokea malipo yao, huku akibainisha kuwa waliojitokeza mapema watapewa kipaumbele na wengine wataendelea kuhudumiwa kadri watakavyokamilisha taratibu.

"Tunataka zoezi hili lifanyike kwa uwazi, haki na kwa wakati. Serikali imejipanga kuhakikisha kila mwananchi aliyestahili analipwa fidia yake bila kuchelewa," alisema Dkt. Burian.

Aidha, aliwataka wananchi kuendelea kushirikiana na mamlaka zinazoratibu zoezi hilo ili kuhakikisha mradi unaanza kwa wakati na kuleta manufaa yaliyokusudiwa kwa jamii na taifa.

Awali, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo Maalumu ya Kiuchumi Tanzania (TISEZA), Remigius Reverius alisema malipo yanafanyika moja kwa moja kupitia akaunti za benki za wanufaika waliokamilisha uhakiki wa nyaraka zao.

Alisema zoezi hilo limeanza katika Kijiji cha Kigurusimba na litaendelea kwa awamu hadi wananchi wote waliothibitishwa kulipwa fidia watakapopokea stahiki zao.

"Tunawashukuru wananchi kwa ushirikiano wao. Serikali kupitia TISEZA imejipanga kuhakikisha kila aliyefanyiwa tathmini analipwa haki yake. Zoezi hili litaendelea hadi Juni 30 mwaka huu," alisema Reverius.

Aliongeza kuwa wataalamu wanaendelea kuhakiki taarifa za akaunti za benki pamoja na nyaraka mbalimbali ili kuhakikisha malipo yote yanafanyika kwa usahihi na bila dosari.

Mwakilishi wa wakulima wa Kigurusimba, Biligita Batilimeo, alisema kuanza kwa ulipaji wa fidia ni hatua muhimu inayoonyesha dhamira ya Serikali ya kutekeleza mradi huo huku ikilinda maslahi ya wananchi.

Alisema pamoja na fidia, mradi huo unatarajiwa kufungua fursa nyingi za ajira na biashara ambazo zitainua uchumi wa wakazi wa Pangani.

Naye mkazi wa Kigurusimba, Benard Mhagama, aliwasihi wananchi watakaopokea fidia kutumia fedha hizo kwa busara kwa kuwekeza katika shughuli za maendeleo zitakazowanufaisha wao na familia zao kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Masaika, George Mariano, alisema uwekezaji huo utabadilisha sura ya uchumi wa Pangani kwa kuongeza ajira, kuchochea shughuli za biashara na kuongeza mapato ya Serikali.

Mradi huo wa kilimo cha miwa na ujenzi wa kiwanda cha sukari unatekelezwa na TISEZA katika eneo la ekari 22,000 kwa gharama ya dola za Marekani milioni 350, na unatarajiwa kuwa miongoni mwa miradi mikubwa itakayochangia kuongeza uzalishaji wa sukari nchini pamoja na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi katika Mkoa wa Tanga.

Mwisho.