HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

TANZANIA YAJIPANGA KUIMARISHA TEKNOLOJIA YA NYUKLIA

May 21, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu-Kigali, Rwanda


TUME ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) imeshiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia Barani Afrika (NEISA 2026) uliofanyika Mei 19, 2026 mjini Kigali, Rwanda, ukiwakutanisha viongozi wa kitaifa, wataalamu wa nishati, wawekezaji pamoja na mashirika ya kimataifa kujadili mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika.

Mkutano huo ulilenga kujadili namna bora ya kuongeza upatikanaji wa nishati ya umeme, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kusaidia maendeleo ya viwanda, kukuza ubunifu wa teknolojia za nyuklia pamoja na kuvutia uwekezaji katika miradi ya nishati kwa ajili ya kuimarisha uchumi endelevu.

Katika mkutano huo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan alisema Tanzania inaendelea kutathmini matumizi ya nishati ya nyuklia kama sehemu ya mkakati wa muda mrefu wa kuongeza vyanzo vya nishati nchini.

Rais Samia alieleza kuwa teknolojia mpya za Small Modular Reactors (SMRs) na Micro Modular Reactors (MMRs) zinaweza kuwa suluhisho sahihi kwa nchi zinazoendelea kutokana na uwezo wake wa kuzalisha nishati kwa ufanisi na usalama zaidi.

Aidha, alitaja maeneo muhimu yanayopaswa kupewa kipaumbele katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ya nyuklia kuwa ni pamoja na mifumo imara ya udhibiti, wataalamu wenye ujuzi pamoja na usimamizi madhubuti wa usalama kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.

Alisisitiza kuwa matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika uzalishaji wa nishati yanahitaji maandalizi ya mifumo ya udhibiti, uwezo wa taasisi, upatikanaji wa fedha, uelewa wa wananchi na ushirikiano wa kikanda.

Katika ushiriki wake, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Profesa Najat Kassim Mohammed alihudhuria mkutano huo akiwa ameambatana na Mkurugenzi wa Teknolojia ya Nyuklia na Huduma za Ufundi, Dkt. Remigius Kawala.

Profesa Najat alipata fursa ya kushiriki kikao cha ndani kilichoongozwa na Rais Samia ambapo alitoa ufafanuzi kuhusu maendeleo ya nyuklia nchini pamoja na miradi inayotekelezwa na TAEC kwa kushirikiana na International Atomic Energy Agency.

Miongoni mwa mipango hiyo ni Rays of Hope unaolenga kuimarisha huduma za uchunguzi na matibabu ya saratani nchini, Atoms4Food unaohamasisha matumizi ya teknolojia ya nyuklia katika sekta ya kilimo pamoja na ushiriki wa TAEC katika mpango wa matumizi ya teknolojia ya nyuklia kwa uzalishaji wa umeme.

Profesa Najat alisisitiza umuhimu wa Tanzania kuendelea kuwekeza katika utafiti, usalama na mafunzo ya wataalamu ili kuhakikisha matumizi salama na endelevu ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, viwanda, utafiti wa madini na uzalishaji wa nishati.

Kupitia mkutano huo, TAEC ilipata nafasi ya kubadilishana uzoefu na wataalamu kutoka mataifa mbalimbali kuhusu usalama wa nyuklia, mifumo ya udhibiti wa teknolojia za nyuklia pamoja na uwekezaji katika miundombinu ya kisasa ya nishati.

Aidha, ushiriki wa Tanzania katika NEISA 2026 uliendana na maono ya serikali ya kukuza sekta ya nishati na kuimarisha ushirikiano wa kikanda ndani ya Afrika Mashariki.

Katika mkutano huo, viongozi mbalimbali wa Afrika walisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza miradi ya nyuklia, kuongeza uwekezaji na kujenga uwezo wa wataalamu wa ndani.

Kwa ujumla, ushiriki wa TAEC katika NEISA 2026 umeiwezesha Tanzania kuendelea kujijengea nafasi katika mjadala wa kimataifa kuhusu mustakabali wa nishati ya nyuklia barani Afrika pamoja na kufungua fursa mpya za ushirikiano wa kitaalamu, kiteknolojia na kiuchumi kwa maendeleo endelevu ya taifa.

Mkutano wa NEISA 2026 uliandaliwa kwa ushirikiano wa International Atomic Energy Agency, United Nations Economic Commission for Africa, World Nuclear Association pamoja na Rwanda.

MCHENGERWA: MAPAMBANO YA MALARIA YANAHITAJI NGUVU YA PAMOJA

May 21, 2026 Add Comment

Na John Mapepele,Geneva, Uswisi

Waziri wa Afya wa Tanzania, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano wa kikanda katika mapambano dhidi ya malaria na Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele (NTDs), katika kikao maalum cha ngazi ya juu kilichofanyika sambamba na Mkutano wa 79 wa Shirika la Afya Duniani (WHA),akisisitiza kuwa udhibiti wa magonjwa hauwezi kufanikiwa bila hatua za pamoja zinazovuka mipaka ya mataifa.

MRADI WA NJIA YA KUSAFIRISHA UMEME CHALINZE–DODOMA KUKAMILIKA AGOSTI 2026 : MD TWANGE

May 21, 2026 Add Comment



Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Chalinze hadi Zuzu, Dodoma, unatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti 18, 2026.

Akizungumza Mei 20, 2026 wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya mradi huo katika mikoa ya Morogoro na Dodoma, Bw. Twange amesema mradi huo ni muhimu kwa kuwa unasafirisha umeme unaozalishwa moja kwa moja kutoka katika Bwawa la Kufua Umeme la Julius Nyerere ambao unapita Chalinze hadi Dodoma.

Amesema utekelezaji wa mradi huo unaenda sambamba na upanuzi wa vituo vya kupokea na kupoza umeme vya Chalinze na Zuzu, Dodoma, ambapo kukamilika kwake kutaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme kwa ajili ya shughuli za uwekezaji pamoja na kuongeza fursa mbalimbali za kiuchumi nchini.

Amesema Serikali Chini ya Rais Dkt Samia Suluhu Hassan imetoa kiasi cha Shilingi Bil 514 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi huo ambao utachochea shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii kuendana na kasi ya ongezeko la mahitaji.

“Leo tumefanya ukaguzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma. Njia hii ni muhimu kwa kuwa inaongeza uwezo wa kusafirisha umeme kutoka Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere kwenda kwa watumiaji mbalimbali. Idadi ya watu imeongezeka na shughuli za kiuchumi zimeongezeka hivyo tumeingia makubaliano sasa mradi huu utakamilika Agosti 18, 2026,” alisisitiza Bw. Twange.

Ameeleza kuridhishwa na hatua iliyofikiwa huku akimtaka mkandarasi kuongeza kasi ya utekelezaji ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati.

“Tumekubaliana kuongeza wataalamu na vifaa vya kutosha ili kuhakikisha mradi huu unakamilika ndani ya muda ulioainishwa ,” ameongeza.

Kwa upande wake, Meneja wa Mradi, Mhandisi Newtone Lingstone, amesema mradi huo wenye urefu wa kilometa 345 Kutoka Chalinze hadi Dodoma unafadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Tanzania, huku kazi za upanuzi wa vituo vya kupokea na kupoza umeme vya Chalinze na Dodoma zikiendelea vizuri.

Kukamilika kwa mradi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Chalinze hadi Dodoma wenye msongo wa Kilovoti 400 utaimarisha na hali ya upatikanaji wa umeme si kwa Mkoa wa Dodoma pekee, bali katika maeneo mbalimbali nchini.



CCM, CPC na Vyama vya Ukombozi Afrika waimarisha ushirikiano wa maendeleo

May 20, 2026 Add Comment
Kibaha, Pwani

CCM leo imekuwa mwenyeji wa mkutano kati ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) na Vyama Sita Rafiki vya Ukombozi Kusini mwa Afrika uliofanyika katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Julius Nyerere (MJNLS), Kibaha.

KAPINGA AIPONGEZA SBC KWA KUUNGA MKONO DIRA YA UCHUMI WA VIWANDA

May 20, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewahimiza wawekezaji na wafanyabiashara nchini kuhakikisha wanalinda haki na usalama wa watumiaji kwa kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia ununuzi wa malighafi, usafirishaji hadi uchakataji wa bidhaa ili kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora vinavyokidhi matakwa ya walaji.

Dk . Komba: tafiti zitoe majibu ya changamoto za wananchi

May 20, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amezitaka taasisi za elimu ya juu nchini kuhakikisha tafiti, ubunifu pamoja na matumizi ya teknolojia vinaelekezwa katika kutoa suluhisho la changamoto halisi zinazowakabili wananchi na kuchochea maendeleo ya taifa.

NAIBU SPIKA SILLO: MICHANGO YA WADAU MUHIMU KUIMARISHA UPANDIKIZAJI FIGO NA ULOTO KWA WATOTO WENYE SICKLE CELL.

May 20, 2026 Add Comment

NAIBU Spika wa Bunge, Daniel Sillo, ametoa wito kwa wananchi na wadau mbalimbali kushiriki katika kuchangia huduma za matibabu ya upandikizaji Uloto kwa Watoto wenye ugonjwa wa Sicle Cell na upandikizaji figo kwa wenye uhitaji hapa nchini.

Ameyasema hayo wakati wa hafla ya chakula cha jioni tarehe 19 Mei, 2026 katika ukumbi wa Domiya jijini Dodoma, ambapo hafla hiyo imewakutanisha viongozi waandamizi wa mkoa wa Dodoma, wabunge na  wadau mbalimbali kwa lengo la kujadili namna ya kuimarisha mfuko wa kusaidia matibabu ya upandikizaji uloto na figo pamoja na huduma nyingine za kibingwa.

Amesema licha ya mafanikio yaliyopatikana ya huduma hizo za upandikizaji uloto na figo kutolewa hapa nchini na hivyo kuokoa fedha nyingi ambazo zingeweza kutumika endapo wananchi wangeenda kutibiwa nje ya nchi.

Alisema kila mwananchi anapaswa kutambua kuwa kuchangia huduma hizo si jukumu la serikali na taasisi pekee, bali ni wajibu wa pamoja kwa kuwa magonjwa ya figo na sickle cell hayachagui mtu kwa nafasi yake, dini wala hali ya maisha.

“Tunaposhiriki katika michango hii si kwa ajili ya taasisi moja, bali tunaunga mkono huduma za kitaifa zinazogusa maisha ya wananchi wengi wanaohitaji matibabu hayo,” alisema Mhe. Sillo.

Alitoa wito kwa wananchi, taasisi na wadau mbalimbali kuendelea kuunga mkono juhudi hizo za BMH ili kuwezesha wagonjwa wanaohitaji huduma za upandikizaji viungo na matibabu mengine maalumu kupata huduma kwa wakati.

Ameeleza kutegemea bajeti ya serikali pekee hakuwezi kukidhi mahitaji yote yanayoongezeka ya huduma za kibingwa, hivyo ushirikishwaji wa wadau ni njia muhimu ya kuimarisha sekta ya afya na kuokoa maisha ya Watanzania wengi.

QWARAY AVUTIWA NA UBUNIFU WA TEHAMA RIDC

May 20, 2026 Add Comment


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Regina Ndege Qwaray (Mb), amefanya ziara ya kikazi katika Kituo cha Utafiti, Ubunifu na Uendelezaji wa Serikali Mtandao (Research, Innovation and Development Centre – RIDC) kilichopo jijini Dodoma, ambapo amekagua miradi mbalimbali ya TEHAMA inayotekelezwa na kituo hicho kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma Serikalini.

Katika ziara hiyo iliyofanyika mapema wiki hii, Mhe. Qwaray alipata fursa ya kutembelea na kujionea miradi ya kiteknolojia inayolenga kutoa suluhisho kwa changamoto katika sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya na utawala.

Aidha, miradi hiyo inahusisha matumizi ya teknolojia zinazochipukia kama vile Internet of Things (IoT) na Akili Mnemba (AI), katika kurahisisha utendaji kazi Serikalini na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Qwaray ameipongeza Mamlaka ya Serikali Mtandao (e-GA) kwa juhudi zake za kuibua na kuendeleza vipaji vya vijana, kupitia tafiti na ubunifu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA yenye mchango mkubwa katika maendeleo ya taifa.

“Niwapongeze e-GA kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kukuza ubunifu na tafiti za teknolojia. Dunia ya sasa inabadilika kwa kasi kubwa kutokana na maendeleo ya teknolojia, hivyo ni muhimu kuendelea kujifunza, kufanya tafiti na kubuni mifumo mipya itakayokwenda sambamba na mabadiliko hayo,” amesema Mhe. Qwaray.

Amesisitiza kuwa, bunifu zote zinazotengenezwa zinapaswa kuwa na tija kwa jamii na kuchangia moja kwa moja katika kuboresha huduma zinazotolewa kwa wananchi pamoja na kuongeza ufanisi ndani ya taasisi za Serikali.

Sambamba na hilo, Mhe. Qwaray amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya e-GA, vyuo vikuu na sekta binafsi ili kuongeza uwekezaji katika tafiti, ubunifu na maendeleo ya teknolojia zinazoweza kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa e-GA, Mhandisi Benedict Ndomba, amesema kituo hicho kimeendelea kuwa chachu ya mageuzi ya kidijitali Serikalini kupitia ujenzi wa mifumo mbalimbali inayotumika katika taasisi za umma.

Ametaja baadhi ya mifumo hiyo kuwa ni Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao vya Bodi na Menejimenti (e-Board) pamoja na Mfumo wa Uendeshaji wa Vikao Kidijitali (e-Mikutano), ambayo imekuwa ikisaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za Serikali.

“Kituo hiki kimekuwa na manufaa makubwa kwa taifa kutokana na kazi zake za utafiti, ubunifu na maendeleo ya mifumo ya TEHAMA. Pia, kimefungua fursa kwa wanafunzi na vijana wenye taaluma ya TEHAMA kushiriki katika tafiti na bunifu mbalimbali kwa maslahi ya taifa,” amesema Mha.Ndomba.

Katika kuonesha dhamira ya Serikali kuendelea kuimarisha kituo hicho, Mhe. Qwaray ameahidi kuwa Wizara itaendelea kushirikiana na e-GA kutatua changamoto zinazoikabili RIDC ili kuongeza fursa kwa vijana wengi zaidi wa Kitanzania kupata nafasi ya kujifunza, kufanya tafiti na kushiriki katika ubunifu wa teknolojia mbalimbali za kisasa.







CRDB Yaongeza Ushirikiano na Majeshi Kupitia Mkutano wa Kimataifa

May 20, 2026 Add Comment

 

MONACO - Benki ya CRDB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kuunga mkono maendeleo ya Taifa kupitia sekta mbalimbali kwa kushiriki katika Mkutano Mkuu wa 81 wa Michezo ya Majeshi Duniani (81st CISM General Assembly) uliofanyika nchini Monaco kuanzia tarehe 1 hadi 9 Mei 2026.

Mkutano huo wa kimataifa uliwakutanisha viongozi wa kijeshi na wadau wa michezo kutoka zaidi ya nchi 130 duniani kwa lengo la kuimarisha mshikamano, diplomasia ya michezo na amani kupitia kaulimbiu ya “Friendship Through Sport.”
Benki ya CRDB, ikiwa miongoni mwa wadau wakubwa wa maendeleo nchini, imeendelea kuunga mkono jitihada za vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na michezo ya majeshi, hatua inayoimarisha ushirikiano wake na taasisi za Serikali katika kukuza ustawi wa askari na familia zao.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo uliongozwa na Brigedia Jenerali Saidi Hamisi Saidi, akisaidiana na Luteni Kanali Penina Anthony Igwe. Kutoka CRDB, ujumbe unajumuisha Meneja wa Kitengo cha Wateja Maalum, Crispin Sichalwe pamoja na Meneja Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma, Emmanuel Tupeligwe.
Akizungumza kwenye mkutano huo, Sichalwe alisema CRDB imeendelea kutoa huduma maalum za kifedha kwa wanajeshi ndani na nje ya nchi, ikiwemo mikopo nafuu, bima na huduma za kifedha zinazowafikia popote walipo.

“Tunatambua mchango mkubwa wa majeshi katika usalama wa Taifa, hivyo tunahakikisha wanapata huduma bora na za haraka kupitia kitengo chetu maalum,” alisema.
Kwa upande wake, Tupeligwe alisisitiza kuwa CRDB itaendelea kushirikiana kwa karibu na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kupitia elimu ya fedha na huduma zinazowafikia wanajeshi hata wakiwa katika maeneo ya mbali au majukumu ya kimataifa.

Aidha, benki hiyo imeendelea kuimarisha ushirikiano wake wa kimkakati na JWTZ ili kuhakikisha wanajeshi wanapata huduma bora za kifedha kwa urahisi, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika maendeleo na usalama wa Taifa.

BALOZI MATINYI AWASILI ALGERIA

May 19, 2026 Add Comment

     


Balozi Mobhare Matinyi akisalimiana na Mwenyekiti wa Mabalozi wa nchi wanachama za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) waliopo Algeria, Balozi Ndumiso Ndima Ntshinga wa Afrika Kusini, mara baada ya kupokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Houri Boumediene jijini Algiers, Jumanne, tarehe 19 Mei, 2026.
Balozi Mobhare Matinyi akisalimiana na Balozi Abdellatif Ellayeh wa Misri, mara baada ya kupokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Houri Boumediene jijini Algiers, Jumanne, tarehe 19 Mei, 2026. Katikati ni Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Suleiman Mussa Rashid.
Balozi Mobhare Matinyi akisalimiana na Balozi Toko Diakenga Serão wa Angola, mara baada ya kupokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Houri Boumediene jijini Algiers, Jumanne, tarehe 19 Mei, 2026. Katikati ni Balozi Ndumiso Ndima Ntshinga wa Afrika Kusini.

****

Balozi Mobhare Matinyi amewasili jijini Algiers, Jumanne, tarehe 19 Mei, 2026, tayari kuanza majukumu ya kuiwakilisha Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Watu wa Algeria.

MCC RAJABU AONGOZA KIKAO CHA KAMATI YA SIASA YA HALMASHAURI KUU YA CCM MKOA TANGA

May 19, 2026 Add Comment

 


Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga na Mjumbe wa Kamati Kuu Ndugu Rajabu Abrahmani Abdallah ameongoza Kikao Maalum Cha Kamati ya Siasa ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Tanga Leo Tarehe 19.05.2026.



TANZANIA NA RWANDA ZASAINI MAKUBALIANO YA USHIRIKIANO WA NISHATI MBELE YA RAIS SAMIA NA KAGAME

May 19, 2026 Add Comment




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na Rais wa Jamhuri ya Rwanda, Mhe. Paul Kagame leo Mei 19, 2026 wameshuhudia zoezi la utiaji saini wa ushirikiano wa masuala ya sekta ya nishati baina ya Tanzania na Rwanda hatua inayolenga kuimarisha ushirikiano wa kikanda na usalama wa nishati kwa nchi hizo mbili.

Zoezi hilo la utiaji saini limefanywa na Waziri wa Nishati wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi na Waziri wa Miundombinu wa Rwanda, Mhe. Dkt. Jimmy Gasore kwenye ukumbi wa mikutano wa Kigali Convention Center (KCC) unapofanyika Mkutano wa Pili wa Uvumbuzi wa Nishati ya Nyuklia barani Afrika (NEISA 2026) unaofanyika jijini Kigali, Rwanda.

Makubaliano hayo yanaangazia maeneo kadhaa ya ushirikiano ikiwemo kubadilishana umeme kati ya Tanzania na Rwanda ili kuimarisha usalama wa nishati, utekelezaji wa miradi ya pamoja ya miundombinu ya umeme, pamoja na kuendeleza biashara ya umeme baina ya nchi hizo mbili.


Aidha maeneo mengine ya ushirikiano ni pamoja na utafutaji na uendelezaji wa mafuta na gesi asilia, usambazaji wa bidhaa za petroli, fursa zilizopo katika miradi ya LNG pamoja na matumizi ya teknolojia za kisasa ikiwemo akili bandia katika Sekta ya Nishati.


Miongoni mwa viongozi waliohudhuria hafla hiyo ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Waziri wa Fedha, Mhe Balozi Khamis Omar, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini wa Zanzibar, Mhe. Dkt. Seif Pandu, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mha. Felchesmi Mramba pamoja na wataalamu kutoka serikali zote mbili.








TET KUSHIRIKIANA NA DUCE KUIMARISHA ELIMU KUPITIA TAFITI

May 19, 2026 Add Comment
NA NOEL RUKANUGA, DAR ES SALAAM

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Dkt. Aneth Komba, amefungua maonesho ya Wiki ya Utafiti na Ubunifu ya Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu Dar es Salaam (DUCE), huku akiahidi kushirikiana na chuo hicho katika kutumia matokeo ya tafiti kuimarisha ufundishaji nchini.

ARBAB VILLAGE IN TANGA KUFANYIWA MABORESHO MAKUBWA, CEO AMTAJA BAKHRESA

May 19, 2026 Add Comment

 



Na Oscar Asenga Tanga

Ikiwa ni zaidi ya miezi sita  tangu kuzinduliwa rasmi kwa Arbab Village mjini Tanga mnamo Desemba 6, 2025, eneo hilo sasa limeendelea kuwa gumzo kubwa kwa wakazi wa Tanga na wageni kutoka maeneo mbalimbali kutokana na muonekano wake wa kisasa, ubunifu wake wa kipekee na namna lilivyobadilisha kabisa taswira ya eneo hilo.

Mkurugenzi wa Arbab Village, Mbwana Imamu, amesema mafanikio makubwa yaliyopatikana ndani ya muda mfupi ndiyo sababu kubwa iliyowasukuma kuanza mpango wa maboresho makubwa zaidi ili kufanya eneo hilo liendelee kuwa kivutio kikubwa zaidi ndani ya Tanga na nje ya Tanzania 🇹🇿 

Kwa sauti yenye kujiamini, Arbab amesema jambo lililompa nguvu zaidi ni namna wananchi wa Tanga walivyoikubali Arbab Village kwa haraka, tofauti na matarajio ya watu wengi waliokuwa hawaamini kama eneo hilo lingeweza kubadilika na kuwa sehemu ya kisasa yenye mvuto mkubwa wa biashara na burudani.

“Watu wengi hawakuwahi kufikiria kama hapa panaweza kuwa sehemu kama hii. Wapo waliowahi kujaribu kufanya uwekezaji lakini walishindwa. Mimi nilikuja na maono tofauti… niliamua kutumia ubunifu mkubwa na kufanya kitu ambacho watu watakikumbuka,” amesema Arbab.

Ameeleza kuwa hakutaka kufanya biashara ya kawaida kama zilivyo sehemu nyingine, bali alitaka kuleta utofauti ambao ungeifanya Arbab Village kuwa na hadhi yake ya kipekee ndani ya jiji la Tanga.

“Biashara kama hizi zipo sehemu nyingi, lakini nilikaa nikafikiria… nifanye nini ambacho kitawafanya watu wajisikie tofauti wakifika hapa? Ndiyo maana nikaja na ubunifu mkubwa ambao leo watu wameukubali na wengine kuvutiwa sana na kuiga”, amesema.

Kutokana na mwitikio mkubwa wa wateja kila siku, Arbab amesema tayari wameanza mipango ya kufanya maboresho makubwa zaidi yatakayoongeza hadhi na ubora wa huduma zinazotolewa katika eneo hilo.

Amesema maboresho hayo hayajasukumwa na malalamiko ya wateja, bali ni sehemu ya maono yangu  ya kuhakikisha kila anayefika Arbab Village anapata uzoefu bora na mpya zaidi.

“Sisi hatusubiri kuambiwa na wateja ndipo tubadilike. Tunataka kila siku tuwe bora zaidi kuliko jana,” amesema kwa msisitizo.

Katika mazungumzo yake, Arbab pia alitoa somo kwa vijana wanaotamani kuingia kwenye biashara, akisisitiza kuwa mafanikio hayapatikani kwa mihemko wala kushindana na watu, bali kwa kusikiliza mahitaji ya wateja na kuwa mbunifu.

“Ukitaka kuwa mfanyabiashara mzuri usipoteze muda kushindana na mfanyabiashara mwingine. Angalia wateja wako wanahitaji nini… hakikisha unawapa,” amesema.

Ameongeza kuwa vijana wengi wanaharibu safari zao za biashara kwa kuendeshwa na presha za mitandaoni na kutaka mafanikio ya haraka badala ya kujenga biashara kwa utulivu, ubunifu na uvumilivu, Arbab Village sio night club kwa maana tunapiga disco hapana, Arbab Village ni sehem tulivu yenye music wa wastan sio makelele huku ukipata chakula na vinywaji. 

Akizungumzia watu waliompa hamasa katika safari yake ya biashara, Arbab hakusita kumtaja mfanyabiashara maarufu wa Tanzania Said Salim Bakhresa kuwa mmoja wa watu waliomvutia kupitia maneno yake ya motisha.

“Niliwahi kumsikia Bakhresa akisema mfanyabiashara lazima ujaribu kila kitu na usikate tamaa. Pia lazima ujitume mwenyewe na upambane binafsi. Yale maneno yalinijenga sana,” amesema.

Arbab amesema leo hii wengi wanashangazwa na namna anavyofanikiwa kufanya mambo makubwa akiwa hana makundi ya vijana wenye mihemko au makelele, bali anaamini katika kazi, nidhamu, ubunifu na kujenga heshima ya biashara yake kupitia matokeo.

Kwa sasa, Arbab Village imeendelea kuwa moja ya sehemu zinazovuta watu wengi zaidi jijini Tanga, huku wengi wakisubiri kwa hamu kuona maboresho mapya yatakayofanyika katika eneo hilo ambalo tayari limeanza kubadilisha sura ya burudani na biashara ndani ya mkoa huo.

TUME YA MADINI YAPATA HATI SAFI YA UKAGUZI, YAKUSANYA MADUHULI TSH. TRILIONI 1.192

May 19, 2026 Add Comment

 




ARUSHA


Tume ya Madini imeendelea kuonesha mafanikio makubwa katika usimamizi wa rasilimali za umma baada ya kupata hati safi ya ukaguzi kwa Hesabu za Mwaka wa Fedha 2024/2025 sambamba na kukusanya maduhuli yaliyofikia Shilingi Trilioni 1.192, sawa na asilimia 99 ya lengo la mwaka.

Akizungumza Mei 19, 2026 mkoani Arusha wakati wa kikao kazi cha wahasibu na wachumi wa Tume, Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Tume ya Madini, CPA. Idfonce Masoud, amesema hati safi hiyo imetokana na ukaguzi uliokamilika na kuwasilishwa kwa Mheshimiwa Rais na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) mwezi Machi 2026.

CPA. Masoud amesema mafanikio hayo yanatokana na juhudi, nidhamu ya kazi na weledi wa timu ya wahasibu na wachumi waliotekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Kanuni za Kimataifa za Uandaaji wa Hesabu za Sekta ya Umma (IPSAS), hatua iliyosaidia kupunguza hoja za ukaguzi na kuimarisha uwazi wa kifedha.

Amezipongeza pia Ofisi za Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa kwa mchango wao mkubwa katika ukusanyaji wa maduhuli pamoja na usimamizi madhubuti wa Katibu Mtendaji wa Tume, uliowezesha kufikiwa kwa kiwango kikubwa cha mapato ya Serikali.

“Natumia fursa hii kuwashukuru na kuwapongeza sana kwa juhudi mlizozifanya katika kusimamia ukusanyaji wa maduhuli hadi kufikia kiasi kilichokusanywa kufikia tarehe 15 Mei 2026,” amesema CPA. Masoud.

Aidha, amewataka washiriki wa kikao kazi hicho kutumia ipasavyo mafunzo na mada zitakazowasilishwa ili kuendelea kuimarisha utendaji kazi na kuongeza ufanisi wa Taasisi.

Kwa upande wake, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Arusha, Godson Kamihanda, amesema kikao kazi hicho ni jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto za kiutendaji na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha utoaji huduma.

Amesema majadiliano yatakayofanyika yanatarajiwa kuzaa matokeo chanya yatakayochangia maendeleo ya Tume ya Madini na Taifa kwa ujumla.

Kikao kazi hicho kinajumuisha mafunzo katika maeneo mbalimbali ikiwemo matumizi ya Mfumo mpya wa Kodi (IDRAS), uandaaji na utunzaji wa taarifa za madeni ya maduhuli, uandaaji wa hesabu, usimamizi wa bajeti na matumizi ya fedha pamoja na maadili na uwajibikaji mahali pa kazi.