HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts

ZAIDI YA SHILINGI BILIONI 19.5 KUTEKELEZA MRADI WA USAMBAZAJI UMEME KWENYE VITONGOJI 127
habari
Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuleta neema ya maendeleo kwa wananchi wa mkoa wa Arusha kwa kuanza utekelezaji wa mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji 127 kwa gharama ya shilingi bilioni 19.5.
Mradi huo unatekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika awamu ya Pili B na unatarajiwa kuwanufaisha wateja 4,086 katika wilaya za Arusha DC, Meru, Karatu, Ngorongoro, Longido na Monduli.
Akizungumza Februari 4, 2026 mkoani Arusha wakati wa hafla ya kumtambulisha mkandarasi aliyeshinda zabuni, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Herini Mhina, amesema utekelezaji wa mradi huo ulianza rasmi Februari 2, 2026 na mkandarasi mzawa Kampuni ya NAKUROI Investment Co. Ltd.
“Tunamshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia utekelezaji wa mradi huu muhimu. Tumewaelekeza wakandarasi kuepuka rushwa, kutumia vibarua wa maeneo husika kwa kazi zisizo za kitaalamu na kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ubora na kwa wakati,” amesema Mhandisi Mhina.
Mhandisi Mhina ameongeza kuwa hadi sasa vitongoji 368 kati ya 1,505 mkoani Arusha vimefikishiwa umeme, huku jitihada zikiendelea kufikisha nishati hiyo katika vitongoji vilivyobaki.
“Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha ifikapo mwaka 2030 vitongoji vyote nchini viwe vimefikishiwa umeme. REA imejipanga kikamilifu kutekeleza dhamira hiyo kupitia miradi mbalimbali ya kimkakati,” amefafanua Mhandisi Mhina.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Makala, ameipongeza REA kwa kutekeleza kwa vitendo maelekezo na dira ya Rais Samia ya kuwaletea wananchi maendeleo.
“Ofisi ya Mkuu wa Mkoa itatoa ushirikiano wa kutosha kwa mkandarasi na REA kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa mafanikio,” amesema Mhe. Makala.
Naye Meneja wa Mradi kutoka Kampuni ya NAKUROI Investment Co. Ltd, Mhandisi Selestine Egongo, ameishukuru Serikali kwa kuwaamini na kuahidi kutekeleza mradi kwa ufanisi kwa kushirikiana na viongozi na wananchi wa maeneo husika.

MCC NA MLEZI WA MKOA WA TANGA HEMED SULEIMAN ABDULLA AWASILI TANGA
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa ambae pia ni Mlezi wa Mkoa wa Tanga Kichama ndugu Hemed Suleiman Abdulla amewasili Mkoani Tanga kuhudhuria katika Maadhimisho ya miaka 49 ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi yanayotarajiwa kufanyika kesho Febuari 5, 2026 katika Uwanja wa Stendi ya Bombani, Wilaya ya Muheza Mkoani Tanga.
SEKTA YA FEDHA YAITWA KUSUKUMA MATUMIZI YA NISHATI SAFI YA KUPIKIA
Nishati*
Serikali imetoa wito kwa wadau kutoka sekta ya fedha nchini kuanzisha huduma na bidhaa za kifedha zitakazowezesha ajenda ya nishati safi ya kupikia kusambaa zaidi, hususan kwa kuwawezesha wajasiriamali wadogo katika maeneo ya pembezoni na vijijini pamoja na wabunifu wa teknolojia za matumizi ya nishati hiyo.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba tarehe 4 Februari 2026 wakati akimwakilisha Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi katika uzinduzi wa mradi wa nishati safi ya kupikia katika shule ya sekondari Bunge Wasichana iliyopo mkoani Dodoma.
"Tanzania imepiga hatua kubwa katika ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia, matumizi ya nishati hii yameongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 na kufikia asilimia 23.2 mwaka 2025. Hata hivyo, bado takribani asilimia 77 ya kaya nchini zinatumia nishati isiyo safi ya kupikia, hivyo natoa wito kwa sekta binafsi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kusukuma ajenda hii kwa kuwezesha upatikanaji wa nishati mbalimbali safi za kupikia katika maeneo ya pembezoni na yale ya vijijini." Amesema Mhe. Salome
Aidha, Mhe. Salome amewasisitiza Wasambazaji wa gesi za mitungi kuongeza vituo vya usambazaji na ujazaji wa gesi za mitungi ili kurahisisha upatikanaji wake kwa watumiaji wengi zaidi, pia Wabunifu na vijana walioko vyuoni kufanya tafiti na kubuni nyenzo na teknolojia zitakazowezesha ajenda hii kusambaa na kuwafikia watu wengi.
Kuhusu mradi wa nishati safi ya kupikia aliouzindua Mhe. Salome amesema kuwa ni utekelezaji wa agizo la Serikali kwa taasisi zinazolisha watu zaidi ya 100 kutumia nishati safi ya kupikia ili kulinda afya za binadamu na kutunza mazingira.
Ameongeza kuwa mfumo huo uliozinduliwa utawezesha chakula kupikwa kwa usafi, kwa haraka, kwa ufanisi, kwa gharama nafuu na bila madhara ya moshi kwa wapishi na wanafunzi huku mazingira yakiendelea kustawi.
Mhe. Salome ameeleza kuwa kuzinduliwa kwa mradi huo ni sehemu ya juhudi za kitaifa zinazoongozwa na Rais, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha asilimia 80 ya watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034 ambapo mpaka sasa tayari asilimia 23.2 ya wananchi wanatumia nishati safi ya kupikia huku taasisi 1,136 zinazolisha zaidi ya watu 100 kwa siku zikihamia katika matumizi ya nishati hiyo.
Akiwa katika shule hiyo ya Wasichana Bunge, Naibu Waziri amezindua pia Klabu ya Nishati Safi ya Kupikia yaani Clean Cooking School Club ambayo ni ya kwanza kuzinduliwa kwa Tanzania ambayo itakuwa mfano wa kuigwa na shule nyingine nchini katika kueneza elimu ya Nishati Safi ya Kupikia.
Wanafunzi watakaojiunga na klabu hiyo watakuwa Vinara wa Nishati Safi ya Kupikia (Clean Cooking Champions) na watashirikiana na Wizara ya Nishati na wadau wengine katika kutoa elimu mashuleni na katika jamii pamoja na kubuni teknolojia za nishati safi ya kupikia zitakazolinda afya na mazingira.
Awali Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Bunge Wasichana, Richard Msana alisema shule hiyo yenye wanafunzi 555 imefanikiwa kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za nishati ya kupikia baada ya kuachana na matumizi ya kuni na kuhamia katika gesi.
Amesema kuanzia Julai 2020 hadi Mei 2022, shule ilikuwa ikitumia takribani shilingi milioni 10.5 kwa kila miezi mitatu kununua kuni. Baadaye walipoanza kutumia mkaa mbadala, gharama zilishuka hadi kufikia shilingi milioni 2.7 na hivi sasa, kupitia mradi wa matumizi ya gesi, shule imenunua tani moja ya gesi iliyotumika kwa miezi miwili, ambapo matumizi ni wastani wa shilingi milioni 1.3 kwa mwezi, kiwango ambacho ni nafuu zaidi kiuchumi.
NACTVET YAENDESHA MAFUNZO KWA MAAFISA UDAHILI NA MITIHANI KUIMARISHA UFANISI WA MIFUMO VYUONI
habari
Meneja wa Utahini na Utunuku wa NACTVET, Dkt. Obeid Mahenya akizungumza wakati akifungua mafunzo maalum kwa Maafisa Udahili na Maafisa Mitihani kutoka katika Vyuo vya Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi nchini Tanzania

MFUMO WA IDRAS KUBORESHA UTOAJI HUDUMA KWA WALIPAKODI
habari
Kaimu Naibu Kamishna wa Huduma kutoka Idara ya Walipakodi wakubwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bi. Rosemary Ruganuza leo 04.02.2026 Jijini Dar es Salaam katika ufunguzi wa mafunzo ya mfumo wa IDRAS kwa walipakodi wakubwa.
.......
Mfumo wa Usimamizi wa Kodi za Ndani (IDRAS) utasaidia kuboresha utoaji wa huduma, kuongeza ufanisi wa kazi na kutumia teknolojia ya kisasa katika kusimamia kodi za ndani.
Hayo yameelezwa na Kaimu Naibu Kamishna wa Huduma kutoka Idara ya Walipakodi wakubwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bi. Rosemary Ruganuza leo 04.02.2026 Jijini Dar es Salaam katika ufunguzi wa mafunzo ya mfumo wa IDRAS kwa walipakodi wakubwa.
Bi. Ruganuza amesema lengo la kuwa na mfumo huo ni kuhakikisha muda mwingi wa watumishi unatumika kutekeleza majukumu ya msingi kwa ufanisi.
Ameeleza mfumo wa IDRAS utawezesha utoaji wa huduma zote za usimamizi wa kodi za ndani kwa njia ya kidijitali, jambo litakalorahisisha mawasiliano kati ya TRA na walipakodi pamoja na kuongeza uwazi na uwajibikaji.
“Tunataka muda wetu mwingi utumike katika kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ili mlipakodi asipate usumbufu wowote wakati wa kupata huduma zetu," amesisitiza Bi. Ruganuza
Vile vile amesema mfumo huo wa IDRAS utatusaidia kutoa huduma bora kwa kutumia teknolojia jambo ambalo litarahisisha mlipakodi kutumia mfumo bila kufika ofisi za TRA.
Ameongeza kuwa kupitia IDRAS, walipakodi watanufaika na huduma zilizo rahisi, haraka na salama, huku Mamlaka ikiimarisha ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa usahihi na ufanisi zaidi.

MAANDALIZI UCHIMBAJI VISIMA VYA GESI ASILIA MTWARA YAFIKIA ZAIDI YA ASILIMIA 90
Nishatichimbaji visima vya gesi asilia Mtwara yafikia zaidi ya asilimia 90*
Maandalizi ya uchimbaji wa visima vitatu vya gesi asilia katika Kitalu cha Mnazi Bay kilichopo mkoani Mtwara yanaendelea vizuri ambapo hadi kufikia Februari 03, 2026 yamefikia zaidi ya asilimia 90.
Hayo yameelezwa na Mhandisi Felista Ndabita kutoka Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), wakati wa ziara ya kikazi iliyofanywa na Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) kwa lengo la kufanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa mradi huo.
Akizungumzia hatua iliyofikiwa, Mha. Felista alieleza kuwa kwa sasa mtambo utakaotumika katika uchimbaji wa gesi asilia umeshasimikwa tayari kuanza uchimbaji wa visima hivyo.
“Kama mnavyoona, kazi ya ufungaji wa mtambo wa kuchimba umekaribia kabisa kukamilika; na vifaa na miundombinu wezeshi ipo katika hatua za mwisho za kukamilika. Matarajio ni kuanza uchimbaji wa visima Februari 09, 2026.” Alieleza Ndabita.
![]() |
Kwa upande wake, Mjiolojia kutoka PURA Bw. Ebeneza Mollel alieleza kuwa PURA kama Mamlaka imeridhishwa na hatua iliyofikiwa na itaendelea kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha kuwa malengo ya kuongeza uzalishaji kutoka katika Kitalu hicho yanafikiwa.
Kwa sasa, Kitalu cha Mnazi Bay kina jumla ya visima vitano (5) vinavyozalisha gesi asilia kwa wastani wa futi za ujazo milioni 90 hadi 100 kwa siku.
Ongezeko la uzalishaji wa gesi asilia unaotarajiwa kufuatia uchimbaji wa visima hivyo utawezesha upatikanaji wa gesi zaidi kwa matumizi mbalimbali yakiwemo kuzalisha umeme, matumizi ya viwandani, majumbani na kwenye magari.






























