HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
NAIBU KATIBU MKUU UVUVI ATOA WITO KWA WATAALAM KUWA NA MBINU BORA ZA UTEKELEZAJI KATIKA PROGRAMU YA AFDP
habariNa; Mwandishi Wetu - Chato
Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi Profesa Mohammed Ali Sheikh, Ametoa wito kwa wataalam kutoka katika Sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu kuwa na mbinu bora za kiutendaji zitakazowezesha programu hiyo kutekelezeka kwa kasi zaidi.
Ameyasema hayo Wilayani Chato Mkoani Geita Tarehe 12 Juni 2026 alipozungumza na wataalam wa programu wanaofanya kazi ya utekelezaji ya mapitio ya programu mara baada ya ziara yake maalum ya kutembelea kituo cha kuendeleza Ukuzaji viumbemaji cha Rubambagwe kilichopo Wilayani chato.
“Niwapongeze sana kwa kuchukua hatua za haraka baada na maagizo ya kikao cha Mawaziri kukaa pamoja kama wataaalamu na kuyafanyia kazi maagizo yale. Hii ni hatua muhimu sana inayoonesha ni kwa namna gani mnaweza kuwajibika kiutaalamu, mnapewa maelekezo na mnayatekeleza” Alisema.
Naibu Katibu Mkuu Sheikh alibainisha kuwa, kukutana kwa wataalamu hao ni hatua muhimu sana ya kukaa pamoja na kujaribu kujitathmini kuona kila kinachofanyika kinakwenda sawa ama vinginevyo, ‘’Niipongeze sana timu ya Uratibu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kuitisha kikao kazi hiki “Mnapoona kitu hakiendi hebu muitane muone namna ya kukifanyia kazi sisi kama watekelezaji wa Programu hii ni familia moja, Serikali ni moja na tunachotaka ni kufikia malengo na kumsaidia mtanzania katika kilimo na uvuvi kwa ukubwa wake” Alisisitiza
Alibainisha kuwa, kwa kufanya tathmini kunasaidia kujua wapi ulikwama na wapi pa kuboresha. Zaidi aliendelea alisema kuwa, kukua na kubadilika kwa teknolojia kufanya tathmini kunaweza kusaidia kwenda mbele zaidi, “lazima tusaidianae tuje na mbinu bora za utekelezaji katika utendaji wa mradi msione aibu kushauri na kutoa mapendekezo ya kiutendaji kuhusiana na Programu.” Alisema
Akizungumza katika kikao kazi hicho, Mhandisi Enock Nyanda, Mkurugenzi msaidizi sehemu ya Sekta za Uchumi na Uzalishaji Idara ya Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) alisema lengo mahususi ya wataalam kukutana katika kikao kazi hicho ni kuongeza kasi ya utekelezaji wa Programu ili kufikia malengo.

ZFCT YARIDHISHWA NA MAFUNZO YA FCC KUHUSU USIMAMIZI WA MASHAURI YA USHINDANI
habari
Na Mwandishi Wetu
Baraza la Ushindani Halali Zanzibar (ZFCT) limefanya ziara ya mafunzo katika Tume ya Ushindani ya Haki (FCC) kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu katika masuala ya ushindani wa biashara, udhibiti wa bidhaa bandia pamoja na usimamizi wa mashauri yanayohusiana na ushindani.
Ziara hiyo iliyofanyika katika ofisi za FCC Juni 10, 2026 Jijini Dar es Salaam, imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao na kuhakikisha mazingira ya biashara yanakuwa ya haki kwa wadau wote.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa FCC, Bi. Khadija Ngasongwa alisema kuwa kubadilishana uzoefu na taasisi za ndani ya nchi ni muhimu katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa ushindani na kulinda maslahi ya watumiaji dhidi ya vitendo vinavyokiuka sheria za ushindani na biashara.
Alisema ujumbe wa ZFCT unapata fursa ya kujifunza namna FCC inavyotekeleza majukumu yake ya kudhibiti vitendo vya ushindani usio wa haki, kukabiliana na biashara ya bidhaa bandia pamoja na mifumo ya uchunguzi na uendeshaji wa mashauri mbalimbali yanayofikishwa mbele ya taasisi hiyo.
Kwa upande wake, ujumbe wa ZFCT ukiongozwa na Msajili wa Baraza, Bi. Fatma Yahya alieleza kuridhishwa na mafunzo na uzoefu uliopatikana katika ziara hiyo, ukibainisha kuwa utaisaidia taasisi hiyo kuimarisha utendaji wake katika kushughulikia rufaa na mashauri yanayohusiana na ushindani wa biashara Zanzibar.
ZFCT ni chombo kinachoshughulikia mashauri na rufaa zinazotokana na maamuzi ya mamlaka za ushindani, ambapo wadau wasiokubaliana na maamuzi yaliyotolewa huwasilisha kesi zao kwa ajili ya kusikilizwa na kutolewa uamuzi.
Ziara hiyo pia ilitoa nafasi kwa wataalamu kutoka pande zote mbili kujadiliana changamoto na fursa zilizopo katika usimamizi wa ushindani wa biashara, huku wakisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana katika kujenga uwezo wa kitaasisi na kuimarisha utekelezaji wa sheria zinazolinda ushindani wa haki katika soko.

USHIRIKIANO WA WADAU NI MUHIMU KUFIKIA LENGO LA NISHATI SAFI YA KUPIKIA LA 2034"- MHE. SALOME

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba amesema Tanzania imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa agenda ya nishati safi ya kupikia, ambapo upatikanaji wa huduma hiyo umeongezeka kutoka asilimia 6.9 mwaka 2021 hadi asilimia 28.6 mwaka 2025.
Amesema mafanikio hayo yametokana na uongozi thabiti wa Serikali, ushirikiano wa wadau wa maendeleo, sekta binafsi na kuongezeka kwa uelewa wa jamii kuhusu matumizi ya nishati safi.
Akifungua rasmi Mkutano wa Wadau wa Nishati Safi ya Kupikia 2026 uliofanyika Arusha leo Juni 10,2026 Mhe. Salome amesema Serikali imejipanga kufikia lengo la asilimia 80 ya Watanzania kutumia nishati safi ya kupikia ifikapo 2034 kupitia utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024–2034.
‘Miradi mbalimbali imechangia mafanikio hayo ikiwemo usambazaji wa mitungi 452,445 ya LPG, majiko banifu 200,000, pamoja na utekelezaji wa mradi wa CookFund unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kupitia UNCDF, ambao umewezesha kaya zaidi ya 634,000 kupata huduma za nishati safi ya kupikia katika mikoa mbalimbali nchini’.
Pia amewataka wadau wote kuendelea kushirikiana ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanapata nishati safi, salama na nafuu ya kupikia, huku akisisitiza kuwa agenda hiyo ni muhimu kwa afya, mazingira, uchumi wa kaya na maendeleo endelevu ya Taifa.
Mkutano huo ulioandaliwa na UNCDF ukiwa na kwa lengo la kujadili maendeleo, fursa na mikakati ya kuharakisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini Tanzania.






WAKULIMA WA PAMBA IGUNGA WAJITOKEZA KWA WINGI KUFUNGUA AKAUNTI
habari
Wakulima wa zao la pamba kutoka vijiji vya Mbutu, Iyogelo, Ilambakuki, Imalanguzu na Mwamakoma vilivyopo katika Wilaya ya Igunga, Mkoa wa Tabora, wamehamasika kufungua akaunti za benki na kusajili laini za simu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kupokea malipo ya mazao yao kwa njia ya kidijitali. Hatua hiyo inalenga kuongeza uwazi, usalama na uharaka wa malipo kwa wakulima.
Wakulima hao wamefungua akaunti kupitia Benki ya NMB pamoja na kusajili laini kupitia mtandao wa simu wa Mixx by Yas, hatua itakayowawezesha kupokea fedha zao kwa urahisi kupitia mifumo ya benki na huduma za kifedha za simu za mkononi.
Zoezi hilo limefanyika kwa kushirikiana na AMCOS za Ngw'ajojabi, Ngw'asabi na Mwamakoma AMCOS, likitekelezwa kufuatia waraka wa Mrajis wa Vyama vya Ushirika unaoelekeza malipo ya wakulima wa pamba kufanyika kupitia akaunti za benki na huduma za fedha kwa njia ya simu badala ya kutegemea fedha taslimu. Lengo ni kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati, kwa uwazi na kwa usalama zaidi.
Mwitikio wa wakulima umeendelea kuongezeka siku hadi siku kufuatia juhudi za uhamasishaji zinazoendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali. Hadi kufikia Juni 10, 2026, jumla ya wakulima 506 wamejitokeza na kufungua akaunti pamoja na kujiunga na huduma za kifedha za simu, hatua inayoonesha uelewa na utayari mkubwa wa wakulima kupokea mabadiliko ya mfumo wa malipo ya kidijitali.
Aidha, uhamasishaji wa zoezi hilo umefanywa na Mrajis Msaidizi wa Mkoa wa Tabora, Peja Mhoja pamoja na Mrajis Msaidizi (Uhamasishaji), Ibrahim Kadudu, ambao wamekuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wakulima kujiunga na mifumo rasmi ya kifedha ili kunufaika na malipo ya kisasa, salama na yenye tija.

TANESCO YAFUNGUA UKURASA MPYA WA MATUMIZI YA UMEME NCHINI
Nishati
📍Yazindua vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme
📍Wananchi kunufaika na mpango wa ukopeshaji wa majiko ya umeme kupitia LUKU
Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) limezindua mradi wa vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme pamoja na Mpango wa Ukopeshaji wa Majiko ya Umeme kwa Wateja (On-Bill Financing – OBF), hatua inayofungua ukurasa mpya wa matumizi ya umeme nchini na kuharakisha utekelezaji wa ajenda ya nishati safi.
Akizindua miradi hiyo jijini Dodoma, Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb) leo tarehe 11 Juni, 2026 alisema hatua hiyo inaonesha dhamira ya Tanzania kushiriki kikamilifu katika mageuzi ya matumizi ya nishati safi duniani huku ikilenga kuboresha maisha ya wananchi na kukuza uchumi.
“Hatua hii inapanua matumizi ya umeme kutoka kupikia hadi usafiri, kwa lengo la kuboresha maisha ya wananchi, kupunguza gharama za maisha na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa,” alisema Mhe. Ndejembi.
Alisema Serikali imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya nishati, hali iliyowezesha uzalishaji wa umeme nchini kufikia zaidi ya megawati 4,000 na kuweka msingi wa matumizi mapana ya umeme katika sekta mbalimbali za uchumi.
Katika kuimarisha matumizi ya vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme, TANESCO kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) imepokea mashine 50 za kisasa za kuchajia vyombo hivyo kutoka kampuni ya AUTEL ya China. Mashine hizo zitafungwa katika maeneo mbalimbali ya kimkakati nchini ili kurahisisha huduma za uchaji.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, alisema Shirika limejipanga kuongoza mageuzi ya matumizi ya umeme nchini kwa kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa kutosha.
.jpeg)
“Mtazamo wa awali kwamba umeme ni ghali na matumizi yake yanaishia kwenye mwanga pekee umebadilika kwa kiasi kikubwa. Leo, wananchi wengi wanatumia umeme katika kupikia na shughuli mbalimbali za kiuchumi, huku hatua ya kuzindua vituo vya kuchajia vyombo vya usafiri vinavyotumia umeme ikifungua ukurasa mpya wa matumizi ya nishati safi nchini,” alisema Bw. Twange.
Kwa upande wa nishati safi ya kupikia, TANESCO imeanza kutekeleza Mpango wa On-Bill Financing (OBF) utakaowezesha wateja kupata majiko ya umeme kwa mkopo na kufanya marejesho kupitia manunuzi yao ya kawaida ya umeme wa LUKU.

Aidha, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, ameipongeza TANESCO kwa hatua hiyo na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini.
“Nawapongeza TANESCO kwa hatua hii ya kimkakati inayofungua fursa mpya za matumizi ya nishati safi nchini. Ni muhimu kuendelea kuhamasisha wananchi kutumia nishati safi katika usafiri na kupikia ili kuharakisha maendeleo na kuhifadhi mazingira,” alisema Senyamule.
Uzinduzi wa miradi hiyo unaashiria hatua mpya ya kupanua matumizi ya umeme nchini kutoka matumizi ya kawaida ya majumbani hadi sekta za usafiri, kupikia na shughuli za uzalishaji mali, sambamba na juhudi za Taifa kuelekea uchumi wa kijani na maendeleo endelevu.







.jpeg)