HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

PAULINA GEKUL AMBURUZA MTOTO KORTINI, MAHAKAMA YASIMAMISHA KESI

May 26, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu


BABATI — Mahakama ya Mwanzo Wilaya ya Babati mkoani Manyara imesitisha kusikiliza kesi ya jinai namba 291 ya mwaka 2026 iliyofunguliwa na aliyekuwa Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, inayomkabili Brayton Lucas (17), baada ya kujiridhisha kuwa mshtakiwa huyo ni mtoto mwenye umri wa chini ya miaka 18 na hivyo shauri hilo linapaswa kusikilizwa katika Mahakama ya Watoto kwa mujibu wa sheria.

Uamuzi huo ulitolewa baada ya Wakili wa upande wa utetezi, Thadei Lister, kuiomba mahakama kujiridhisha kuhusu umri wa mshtakiwa kwa kuwasilisha nyaraka mbalimbali ikiwemo cheti cha kuzaliwa kilichoonesha kuwa Brayton alizaliwa Novemba 12, 2008 na kwa sasa ana umri wa miaka 17 na miezi sita, tofauti na taarifa zilizokuwa katika hati ya mashtaka zilizomtaja kuwa na miaka 19.




Katika shauri hilo, Paulina Gekul alidai kuwa Brayton Lucas, ambaye alikuwa akichunga mifugo yake, alihusika katika wizi wa mbuzi 15 wenye thamani ya shilingi milioni tatu, kosa linalodaiwa kufanyika chini ya kifungu cha 268 cha sheria ya wizi wa mifugo. Kesi hiyo ilikuwa na jumla ya watuhumiwa watatu.

Mahakama pia ilielezwa kuwa mtoto huyo alikuwa amechanganywa katika shauri moja na watuhumiwa watu wazima, jambo ambalo upande wa utetezi ulidai ni kinyume na sheria zinazolinda haki za mtoto.




Baada ya kupitia nyaraka zilizowasilishwa, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo Babati, Ahmed Mgodo, alisema mahakama imejiridhisha kuwa Brayton Lucas ni mtoto na hivyo haina mamlaka ya kuendelea kusikiliza kesi hiyo. Kutokana na uamuzi huo, mahakama ilisimamisha shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo na kuagiza polisi kuandaa hati mpya ya mashtaka kwa mujibu wa sheria zinazohusu watoto.

Brayton Lucas alipatiwa dhamana huku washtakiwa wawili wengine wakiendelea kushikiliwa. Wakili Thadei Lister amesema wako tayari kuendelea kumtetea mtoto huyo iwapo atafikishwa katika Mahakama ya Watoto.

Akizungumza nje ya mahakama, Wakili Thadei alisema Brayton ni mwanafunzi wa kidato cha nne ambaye alitoweka akiwa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha na wazazi wake walikuwa wakimtafuta kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kupata taarifa kuwa amekamatwa Babati kwa tuhuma za wizi.

Mama mzazi wa Brayton alisema mtoto wake alitakiwa kuwa shuleni baada ya kumaliza kidato cha nne na tayari alikuwa amepangiwa shule, lakini aliondoka nyumbani bila kutoa taarifa na baada ya juhudi za muda mrefu za kumtafuta walipata taarifa kuwa alikuwa Babati akifanya kazi.


Wakati huo huo, Diwani wa Kata ya Maruvango Wilaya ya Arumeru Mashariki, Digna Nassari, amesema taarifa za kupotea kwa mtoto huyo zilikuwa zimetolewa polisi miezi mitatu kabla ya kufunguliwa kesi dhidi yake na Paulina Gekul.

Aidha, Digna amesema Brayton ni miongoni mwa watoto 16 kutoka kata hiyo waliotoroka shule, huku akisisitiza umuhimu wa jamii kushirikiana kuhakikisha watoto wanarudi katika mfumo wa elimu na kupata ulinzi unaostahili

TBS YASISITIZA USALAMA WA CHAKULA KATIKA BIASHARA ZA UOKOAJI (BAKERY)

May 26, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) limetoa mafunzo maalumu kwa wafanyabiashara wa bidhaa za uokaji (bakary) Mkoa wa  Dar es Salaam ili kuongeza uelewa kuhusu masuala ya viwango, kuboresha usalama wa chakula na kuimarisha ushindani wa biashara zao sambamba na kulinda afya za watumiaji.

JAB YAWATAKA WAANDISHI KUTAFAKARI MWELEKEZO WA TASNIA

May 26, 2026 Add Comment

 



Mwenyekiti wa Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB), Bw. Tido Mhando, amewataka Waandishi wa Habari nchini kutafakari upya wajibu wao katika kuijenga jamii kupitia maudhui yenye tija, akieleza kuwa ipo haja ya kurejesha hadhi na nguvu ya taaluma hiyo katika kujenga fikra na maendeleo ya taifa.


Akizungumza jijini Dar es Salaam, Bw. Mhando amesema pamoja na JAB kusimamia utoaji wa ithibati kwa kuzingatia vigezo vya elimu na sheria, bado kuna umuhimu wa Waandishi wa Habari kuendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo ya kitaaluma.

“Tukitazama baadhi ya vyombo vyetu vya habari, iwe ni magazeti, redio au televisheni, mambo ya kufikirisha kwa kiasi kikubwa yamepungua. Waandishi wa Habari wanapaswa kutafakari kama hiyo ndiyo taswira wanayotaka kuiacha katika jamii ya Watanzania,” amesema.

Amesisitiza kuwa vyombo vya habari vina nafasi kubwa ya kuunda mtazamo wa jamii, hivyo kuna wajibu wa kuhakikisha maudhui yanayotolewa yanajenga uelewa, yanakuza maendeleo na yanalinda maslahi ya taifa.

“Tunachosimamia ni kuhakikisha Mwandishi wa Habari anayepata ithibati anakuwa na kiwango cha elimu kisichopungua Diploma, lakini tunataka pia Waandishi wa Habari waendelee kupata mafunzo ili waweze kuimarika zaidi kitaaluma,” amesema.

WAZIRI SANGU AZINDUA BODI YA SABA YA USHAURI YA OSHA.

May 26, 2026 Add Comment
-Asisitiza Utekelezaji wa Viwango vya Kimataifa vya Usalama na Afya katika Maeneo ya Kazi
NAIBU WAZIRI KWAGILWA AHIMIZA USHIRIKIANO USAFI WA MAZINGIRA

NAIBU WAZIRI KWAGILWA AHIMIZA USHIRIKIANO USAFI WA MAZINGIRA

May 26, 2026 Add Comment




Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akiongoza zoezi la usafi wa mazingira lililohusisha uokotaji wa taka na kusafisha mifereji ya maji machafu katika eneo la Taifa Road ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa lei Mei 25, 2026 akipanda mti aina ya mwembe katika eneo la Shule ya Sekondari ya Ndaoya, Mtaa wa Chongoleani jijini Tanga ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.



Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akizungumza na wananchi katika uwanja wa Tangamaano jijini Tanga mara baada ya zoezi la usafi wa mazingira lililohusisha uokotaji wa taka na kusafisha mifereji ya maji machafu katika eneo la Taifa Road ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Reuben Kwagilwa leo Mei 25, 2026 akiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian alipowasili katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa kabla ya zoezi la upandaji miti na usafi wa mazingira ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani ambayo kilele chake kitafanyika jijini Dodoma Juni 05, 2026.

TPDC YAHIMIZA WANANCHI KULINDA MIUNDOMBINU YA BOMBA LA GESI ASILIA

May 25, 2026 Add Comment


Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) limeendelea kuwashirikisha  wananchi katika kulinda miundombinu ya bomba la gesi asilia, likieleza kuwa usalama wa miundombinu hiyo unategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano wa jamii nzima.

Katika kuimarisha ulinzi huo, TPDC inaendelea kutekeleza programu ya utoaji elimu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopitiwa na bomba la gesi asilia mkoani Pwani, hususan katika wilaya za Rufiji, Kibiti na Mkuranga.

 Lengo la programu hiyo ni kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda miundombinu hiyo pamoja na kuwajengea uwezo wa kutambua na kuripoti mapema vitendo au shughuli zinazoweza kuhatarisha usalama wake.


Akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo, Afisa Maendeleo ya Jamii wa TPDC, Bi. Ashura Hoja alisema “Bomba la gesi asilia ni rasilimali ya taifa hivyo  kila mwananchi ana wajibu wa kuwa mlinzi wa miundombinu hii na  kutoa taarifa mapema mnapoona shughuli zisizo za kawaida karibu na bomba la gesi,” alisema Bi. Hoja

Aidha, TPDC imewapongeza wananchi wa maeneo husika kwa mwitikio wao katika kushiriki kulinda miundombinu hiyo, huku ikiwataka kuendelea kuwa makini zaidi kwani uharibifu wowote unaweza kuathiri huduma muhimu pamoja na maendeleo ya taifa kwa ujumla.


Kwa upande wake, mwananchi wa Kijiji cha Jaribu Mpakani, Wilaya ya Kibiti, Bw. Kassimu Iddi alisema elimu inayotolewa na TPDC imeleta mabadiliko makubwa ya mtazamo kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda bomba la gesi.

“Sasa tunaelewa kuwa kulinda bomba la gesi ni kulinda maisha yetu na maendeleo ya taifa letu. Tumeamua kuwa walinzi wa kwanza wa miundombinu hii,” alisema Kassimu

TPDC imeendelea kutoa wito kwa jamii zote zinazoishi karibu na bomba la gesi asilia kushiriki kikamilifu katika mfumo wa ulinzi wa pamoja, ili kuhakikisha miundombinu hiyo inalindwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

TANZANIA KUANDAA MPANGO WA HATUA ZA MAPEMA ZA KUJIANDAA KUKABILIANA NA UKAME - DKT. YONAZI

May 25, 2026 Add Comment


Na Mwandishi wetu - Msumbiji

TANZANIA  inaandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema za kujiandaa, kukabiliana na ukame kwa maeneo yanayokabiliwa na janga hilo kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), ikiwa ni jitihada za kupunguza athari za janga hilo nchini.

Hatua hiyo inaonesha dhamira ya serikali kuachana na utaratibu wa kusubiri madhara yatokee ndipo ichukue hatua, na badala yake kuelekea katika usimamizi wa hatari unaozingatia maandalizi na tahadhari za mapema.


Hayo yameelewa na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu Dkt. Jim Yonazi, katika ziara ya kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Msumbiji kuhusu hatua za mapema kabla ya majanga unaoendelea kwa siku tano kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2026 Mjini Maputo Msumbiji.

Alisema ukame una madhara makubwa katika kilimo, mifugo, rasilimali za maji, usalama wa chakula, maisha ya wananchi, maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla.


“Kwa sasa Tanzania inaendelea kuandaa Mpango wa Kitaifa wa Hatua za Mapema dhidi ya ukame kwa msaada wa WFP, kwa kutambua kuwa bado ni moja ya majanga makubwa yanayoathiri nchi yetu,” alisema Dkt. Yonazi.

Aliongeza kuwa mpango huo utawezesha kuwepo kwa mifumo imara ya tahadhari na utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya majanga hayajatokea.

Kuhusu ziara hiyo, Dkt. Yonazi alisema Tanzania imechagua kujifunza kutoka Msumbiji kutokana na mafanikio yake katika kuanzisha na kutekeleza mifumo ya hatua za mapema dhidi ya majanga, hususan ukame, mafuriko na vimbunga.

Alisema kupitia ushirikiano huo, Tanzania itanufaika kwa kubadilishana uzoefu na mbinu bora, kujifunza mifumo ya uratibu wa taasisi, vigezo vya kuanzisha hatua za mapema pamoja na namna ya kugharamia hatua hizo.

Aidha, alieleza kuwa uzoefu huo utasaidia kuunganisha hatua za mapema ndani ya mifumo ya hifadhi ya jamii ili kuongeza ufanisi katika kukabiliana na majanga.

“Ziara hii ni muhimu kwa Tanzania katika kujifunza kwa vitendo na kupata mafunzo kutokana na mafanikio ya Msumbiji katika utekelezaji wa hatua za mapema kabla ya maafa,” alisema.

=MWISHO=

KARIBU NYUMBANI ILIVYABAMBA OLDUVAI,

May 25, 2026 Add Comment

 Washiriki zaidi ya 300 wameshiriki mbio fupi za kilomita 5 katika  bonde la Olduvai Ngorongoro kwa lengo la kutangaza vivutio vya asili vya Olduvai na Laetoli ambapo historia ya Binadamu wa Kale ilianzia.

Akizungumza kwa Niaba ya Kamishna wa Uhifadhi kwenye tukio hilo, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi anayesimamia Huduma za Utalii na Masoko Mariam Kobelo ameeleza kuwa Ngorongoro kwa kushirikiana na Cape to Cairo Marathon imefanya mbio hizo ili kuonesha utajiri wa utalii wa asili, historia, urithi wa utamaduni na  mambo kale uliopo Olduvai na Laetoli kama Nyumbani kwa asili ya Binadamu. 

Ameongeza kuwa Ngorongoro ni Nyumbani kwa Nyumbu wanaohama kwa kuwa pumzi ya kwanza ya ndama kupigwa mhuri kabla ya kuhamia maeneo mengine safari yao huanzia Ndutu Ngorongoro.

"Ngorongoro ni Nyumbani kwa asili ya binadamu kisayansi, Ni nyumbani kwa Nyumbu wanaohama kila mwaka, ni nyumbani kwa Spinshi ya Ndege zaidi ya 500, ni nyumbani kwa Wanyama wakubwa watano, kiufupi eneo la Ngorongoro ni Nyumbani kwa mkusanyiko wa Vitu vingi ndio maana tunawaambia wadau wote ndani na nje ya Nchi kuwa Wonders Are Calling" ameongeza Kamishna Kobelo.

 Mkurugenzi wa Cape to Cairo Arusha International Marathon, Timothy Mdinka ameeleza kuwa lengo la mbio hizo ni kutangaza mazao mapya  ya Utalii yaliyopo Tanzania na Bara la Africa kwa Ujumla kupitia shughuli mbalimbali ikiwemo  Michezo kama mbio ambayo imefanyika leo Olduvai pamoja na marathon ya Cape to Cairo itakayofanyika tarehe 31 Mei, 2026.

Mbio hizo zimejumuisha wadau mbalimbali wakiwepo Ngorongoro, Cape to Cairo international Marathon, Karatu Runners,  Amani Collection, CRDB, UNDP, NHIF,  Diplomatic and Tourism Police Arusha.












KCMC KUJENGA TAASISI KUBWA YA MOYO KUPUNGUZA RUFAA JKCI

May 25, 2026 Add Comment

 







Na Oscar Assenga, Tanga

HOSPITALI ya Rufaa ya Kanda ya KCMC inatarajia kujenga Taasisi Kubwa ya Moyo ili kupunguza rufaa kwa wagonjwa wanaotoka mikoa ya Kanda ya Kaskazini kwenda Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Cardiac Institute (JKCI) kupata matibabu. 

Ambapo kwa mujibu wa takwimu  zaidi ya asilimia 60 ya wagonjwa wanaopatiwa huduma katika Taasisi hiyo wanatoka katika mikoa hiyo , hali inayoendelea kuchochea ujenzi wa Taasisi kubwa ya Moyo katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC Hospital ili kusogeza huduma karibu na wananchi.

Akizungumza jijini Tanga, Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Batilda Burian wakati wa mkutano wake na wana habari kuelezea harambee ya kuchangia ujenzi wa Taasisi Kubwa ya Moyo katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC utakaofanyika Mei 30 mwaka huu katika Ukumbi wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Jijini Tanga

Alisema serikali pamoja na wadau wa maendeleo wameona umuhimu wa kuimarisha huduma za moyo Kanda ya Kaskazini kutokana na ongezeko kubwa la wagonjwa kutoka eneo hilo wanaohitaji matibabu ya kibingwa.


Alisema mradi huo utakaojengwa KCMC utakuwa na uwezo wa kutoa huduma za kisasa zinazolingana na zile zinazotolewa JKCI, na unatarajiwa kuhudumia wakazi wa mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara.

“Mkoa wa Tanga utaungana na uongozi wa KCMC kuhakikisha mradi huu unakamilika kwa mafanikio,” alisema Burian, akisisitiza kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mkakati wa kuboresha sekta ya afya nchini chini ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Burian aliongeza kuwa tayari zaidi ya Shilingi bilioni 22 zimepatikana kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo, huku Shilingi bilioni 3 zikihitajika kukamilisha ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa.

Kwa mujibu wa taarifa za mradi, ujenzi tayari umeanza na umefikia asilimia 40 ya utekelezaji, huku gharama ya jumla ya mradi ikiwa ni takriban Shilingi bilioni 25.

Kwa upande wake, Meneja Miradi na Afisa Mipango wa KCMC, Emanuel Biyanchi alisema mradi huo utasaidia kupunguza rufaa za wagonjwa kwenda JKCI na nje ya nchi, hivyo kupunguza gharama kubwa kwa wagonjwa na familia zao.

“Karibu asilimia 70 ya wagonjwa wanaopewa rufaa JKCI hushindwa kufika kutokana na changamoto za usafiri na gharama, hivyo huduma zikisogezwa karibu zitakuwa nafuu na rahisi kufikika,” alisema.

Biyanchi aliongeza kuwa taasisi hiyo itakuwa msaada mkubwa katika kupunguza msongamano wa wagonjwa JKCI na kuimarisha huduma za kibingwa nchini.

Alitoa wito kwa wafanyabiashara, wananchi na wadau wa maendeleo wametakiwa kujitokeza kwa wingi  kushiriki katika harambee itakayofanyika Mei 30 mwaka huu Tanga Beach Resort ili kuchangia kukamilisha mradi huo muhimu wa afya.

REA YAANDIKA HISTORIA LUDEWA

May 25, 2026 Add Comment








📌Yawasha umeme ukanda wa Nyasa kitongoji cha Nkanda

📌Yapongezwa kufikisha umeme kwenye mazingira magumu Njombe

📌Bodi ya REA yasisitiza wananchi kuchangamkia fursa uwepo wa nishati ya umeme




Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijni (REA), unaendelea kutekeleza miradi mbalimbali pamoja na kuwasimamia kwa karibu wakandarasi wote waliopewa na watakaopewa zabuni ya kutekeleza miradi ili kuhakikisha kuwa miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kwa ubora uliopangwa ili iweze kuwanufaisha wananchi.

Hayo yamebainishwa leo Mei 25, 2026 na Wajumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), wakati wa hafla ya kukagua miradi, kutembelea na kuwasha umeme kitongoji cha Nkanda kilichopo wilaya ya Ludewa mkoani Njombe mradi uliokuwa unatekelezwa na Suma Jkt Electric Company Ltd.

Mha. Ahmed Chinemba amesema kuwa, mradi wa kupeleka umeme katika vitongoji vya mwambao wilayani Ludewa unatekelezwa na mkandarasi M/S SUMAJKT ELECTRIC COMPANY LTD kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 3.2 ili wananchi wa mwambao wapate huduma ya umeme.

"Mradi huu umelenga kuongeza shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa kitongoji cha nkanda ukiwa na chachu ya kutoa fursa za kibiashara kwa kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi, kurahisiha upatikanaji wa huduma za kijamii na uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo kama mashine za kusaga, mashine za kuchana mbao pamoja na mashine za kuchomelea," Amesema Mha. Chinemba.

Kwa upande wake, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Suma JKT Brigedia Jenerali Shija Lupi, ameishukuru REA kwa kuwapatia kazi hiyo ya kufikisha umeme katika maeneo ya mwambao kikiwemo kitongoji hicho cha Nkanda ambapo kazi imekamilika kwa ubora.

"Sisi Suma JKT tumefanisha kufikisha umeme kwenye mazingira magumu kama haya ambayo yalikuwa na changamoto nyingi lakini tumefanikiwa na sasa tunaona matunda yake, " Amesema Brigedia Jenerali Lupi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Mha. Deogratius Nagu amesema katika kitongoji cha Nkanda takribani shilingi milioni 450 zimetolewa na Serikali kupitia REA ili kufikisha huduma ya umeme katika kitongoji hicho.

Aidha, amewataka wananchi wa Nkanda kuchangamkia fursa ya uwepo wa umeme kwa kuhakikisha wanafanya wiring katika nyumba zao na kuunganisha umeme kwa wingi ili wanufaike na umeme huo katika kitongoji chao.

Naye, Mwakilishi wa Mbunge wa Jimbo hilo Bw. Stanslaus Gowele amesema ujio wa umeme maeneo ya mwambao yanakwenda kuongeza chachu ya Maendeleo kiuchumi na kijamii kwa wananchi hao.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wanufaika wa mradi huo wameeleza namna ambavyo Mradi huo umekuwa mkombozi kwao.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti, baadhi ya wanufaika wa mradi huo wameeleza namna ambavyo Mradi huo umekuwa mkombozi kwao.