HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

VIKWAZO VITANO VISIVYO VYA KIKODI VYAPATA UFUMBUZI MPAKA WA TUNDUMA/NAKONDE KUCHOCHEA BIASHARA ZA KIMATAIFA KUSINI MWA AFRIKA

February 23, 2026 Add Comment
Vikwazo vitano visivyo vya kikodi kati ya kumi vilivyokuwa vikisababisha msongamano mkubwa wa malori na usumbufu kwa wafanyabiashara na wasafirishaji katika mpaka wa Tunduma/Nakonde, zimepatiwa ufumbuzi kupitia juhudi za pamoja za Serikali za Tanzania na Zambia. Hatua hiyo inatajwa kuwa chachu ya kuimarisha biashara za kimataifa katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

WAZABUNI WA KILWA, LINDI NA MTWARA WAPATIWA MAFUNZO YA MATUMIZI YA MODULI YA MALALAMIKO, RUFAA KATIKA MFUMO WA NeST

February 23, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Lindi na Mtwara
Katika jitihada za kuongeza uelewa wa matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia Malalamiko na Rufaa kupitia Mfumo wa Kielektroniki wa Ununuzi ya Umma (NeST), Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imetoa mafunzo kwa wazabuni, wajasiriamali na watumishi wa Umma waliopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Mikoa ya Lindi na Mtwara. 
Akielezea kuhusu mafunzo hayo ya siku tano (kuanzia tarehe 16 - 20 Februari, 2026), Meneja wa Usimamizi wa Rufaa na Sheria (PPAA), Bi. Florida Mapunda amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga kutoa elimu kwa wadau wa ununuzi wa Umma kuhusu taratibu za uwasilishaji na ushughulikiaji wa malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST kama ilivyoelekezwa katika Sheria ya Ununuzi wa Umma. 
“Sheria ya Ununuzi wa Umma imeweka sharti la lazima kwa ununuzi wa umma kufanyika katika mfumo wa NeST. Kutokana na sharti hilo, PPAA kwa kushirikiana na PPRA tumejenga moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko katika mfumo wa NeST ili kuwasaidia wadau wa ununuzi wa umma (Wazabuni na Taasisi za Umma) kuwasilisha malalamiko na rufaa kieletroniki,” amesema Bi. Mapunda.
Pamoja na mambo mengine, Bi. Mapunda ameongeza kuwa Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa katika mfumo wa NeST ina manufaa makubwa kwa wazabuni kwani inarahisisha uwasilishaji wa malalamiko ya zabuni kwa njia ya mtandao bila kufika ofisini, jambo linalochangia kuokoa muda, gharama na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika ununuzi wa Umma.
Kwa upande wake Mkuu wa Sehemu ya Rufaa kutoka PPAA, Bi. Violet Limilabo ameeleza kuwa PPAA ina mchango mkubwa katika kulinda haki za wazabuni kwa kuwapa fursa ya kusikilizwa wanapoona hawakutendewa haki katika michakato ya Ununuzi wa Umma. 
Aidha, PPAA imeendelea kuimarisha uwazi na usawa kwa kuhakikisha taratibu za ununuzi wa umma zinafuatwa kwa mujibu wa sheria na kupunguza migogoro kwa kutoa suluhisho la kisheria.
Naye Afisa Ununuzi kutoka ofisi za PPRA Kanda ya Kusini, Bw. Aziz Njovu alitoa mafunzo kuhusu moduli mpya za majadiliano (negotiations) na uandaaji, upekuzi na utiaji saini wa Mkataba (Contract preparation, vetting and signing kwenye mfumo wa NeST, alisema kwa sasa mchakato wa majadiliano na utiaji saini wa mkataba unahitimishwa kwa njia ya mtandao.
“Matumizi ya mfumo wa NeST yameendelea kuimarisha uwajibikaji na kurahisisha ufuatiliaji wa mikataba ya ununuzio wa umma,” amesema Bw. Njovu.
Mafunzo hayo yamewahusisha jumla ya washiriki 322 ambao ni  wataalamu wa sheria, Tehama na ununuzi pamoja na wazabuni, makundi maalum yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye mahitaji maalum pamoja na mafundi wa ndani.
Mafunzo kuhusu Matumizi ya Moduli ya kupokea na Kushughulikia Malalamiko na Rufaa katika Mfumo wa NeST yaligawanyika katika makundi matatu ambapo Kundi la kwanza ni Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa (tarehe 16 Februari, 2026), Mkoa wa Lindi (tarehe 17 na 18 Februari, 2026) na Mkoa wa Mtwara (tarehe 19 na 20 Februari, 2026)
Mafunzo hayo ni mwendelezo wa mafunzo ya awali yaliyofanyika katika Kanda ya Pwani, Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kaskazini, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini pamoja na Kanda ya Kati.
 
 
 
 

WATUMISHI WAPONGEZA UTEKELEZAJI WA MRADI WA EACOP KWA KUZINGATIA UHIFADHI WA MAZINGIRA

February 23, 2026 Add Comment


*Na mwandishi wetu, Tanga.*


Watumishi wa Wizara ya Nishati wameipongeza Serikali na Wanahisa wengine wa EACOP kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi mkubwa wa kimkakati wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP). Pamoja na pongezi hizo Kampuni ya EACOP imepongezwa kwa kuzingatia uhifadhi wa mazingira katika hatua zote za utekelezaji wa mradi hususani viumbe hai katika maeneo yote yanayopitiwa.

Kauli hiyo imetolewa Februari 22, 2026, Chongoleani, Tanga na mwakilishi wa watumishi hao Bw. Benson Lukuta akiwa Mkuu wa Msafara katika ziara iliyofanywa na watumishi wa Wizara ya Nishati kutembelea mradi huo.

Bw. Lukuta pia kwa niaba ya watumishi aliushukuru Uongozi wa Wizara kwa kufanikisha ziara hii muhimu kwa watumishi kufahamu na kujione Miradi inayosimamiwa na Wizara.


Ziara hiyo ililenga kujionea maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo mkubwa, hususan jinsi unavyozingatia uhifadhi wa mazingira, ulinzi wa viumbe hai katika maeneo yanayopitiwa na manufaa kwa jamii katika maisha ya kila siku na ujuzi.

“Utekelezaji wa mradi huu wa kimkakati umezingatia sana uhifadhi wa mazingira na kuleta manufaa kwa jamii zinazouzunguka. Mradi huu unaounganisha Tanzania na Uganda na ni mojawapo ya miradi mikubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki, ukiwa na lengo la kusafirisha mafuta ghafi kutoka Hoima, Uganda hadi Bandari ya Tanga, Tanzania,” alisema Lukuta.

Kwa upande wake, Bw. Thomas De Mauleon Mwakilishi wa Kampuni ya EACOP, alisema mradi huo una manufaa makubwa kwa Watanzania, si tu kiuchumi bali pia kijamii na kitaalamu.

Aidha, amesema mpaka sasa mradi umeweza kutoa ajira za moja kwa moja kwa Watanzania 10,000, huku wananchi 170 wakipatiwa mafunzo maalum ili kufikia viwango vya kimataifa katika ujenzi wa miradi ya mafuta na gesi.

Pia, kupitia miradi ya kijamii, EACOP imeboresha barabara na huduma za maji katika maeneo yanayopakana na Mradi. Takribani kilomita 27 za barabara za changarawe zimeboreshwa, zikiwemo: Barabara ya Kagongwa hadi Sojo (km 18), Handeni kuelekea Kambi Na. 15 (km 2.1), barabara ya kuunganisha eneo kuu la Mradi Chongoleani (km 7.2).

Hatua hizi zinaongeza urahisi wa usafirishaji, kuunganisha jamii na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo yanayopitiwa na mradi.


Waziri Mavunde Apongeza Ushirikiano Benki Ya CRDB na Tume ya Madini Uwezeshaji Wachimbaji Wadogo wa Madini

February 23, 2026 Add Comment

 

Dar es Salaam, 23 Februari 2026 — Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amepongeza kwa ushirikiano wa kimkakati kati ya Benki ya CRDB na Tume ya Madini, akieleza kuwa mpango maalum wa kifedha uliozinduliwa leo kwa ajili ya wachimbaji wadogo ni hatua ya kihistoria itakayobadili kabisa mfumo wa upatikanaji wa mitaji katika sekta ya madini nchini.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa huduma hizo na utiaji saini wa Mkataba wa Makubaliano (MOU) uliofanyika katika hoteli ya Johari Rotana, Waziri Mavunde alisema sekta ya madini imeendelea kukua kwa kasi, ikichangia asilimia 10 ya Pato la Taifa na zaidi ya asilimia 56 ya mapato ya fedha za kigeni kupitia mauzo ya nje yanayozidi dola za Marekani bilioni 5 kwa mwaka.
“Sekta ya madini sasa ni injini ya uchumi wetu. Tunachokishuhudia leo ni daraja linalounganisha maono ya Serikali na nguvu ya mtaji kutoka sekta ya fedha. Ushirikiano huu unaenda moja kwa moja kumgusa mchimbaji mdogo na kumwinua katika uchumi rasmi. Benki ya CRDB hakika mmeonyesha kuwa ni Benki kiongozi katika kuleta suluhisho stahiki kwa sekta mbalimbali. Tunawashukuru sana,” alisema Waziri Mavunde.

Alisisitiza kuwa chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Serikali imekuwa ikitekeleza mageuzi ya kisera, kiusimamizi na kisheria ili kuhakikisha sekta ya madini inawanufaisha Watanzania wengi zaidi, hususan wachimbaji wadogo. Alieleza kuwa azma ya Serikali ni kuona uchimbaji hauishii kwenye kuuza mawe ghafi, bali unapanuka hadi kwenye uchakataji na uongezaji thamani ndani ya nchi.
Mpango uliozinduliwa na Benki ya CRDB unaleta mageuzi makubwa katika mfumo wa dhamana kwa kutambua dhamana mbadala zinazotokana moja kwa moja na shughuli za uchimbaji. Kwa mara ya kwanza katika sekta ya benki nchini, leseni halali za uchimbaji, mikataba ya mauzo ya dhahabu, na akiba ya dhahabu iliyohifadhiwa katika viwanda vya kusafisha pamoja inatambuliwa kama dhamana zinazokubalika kwa ajili ya mikopo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, alisema mpango huo ni mfumo kamili wa kifedha unaogusa mnyororo mzima wa thamani wa sekta ya madini kuanzia uchimbaji, uchakataji, uhifadhi, usafirishaji hadi biashara na masoko ya ndani na nje ya nchi.
“Huu ni muundo mpya wa kifedha unaotambua uhalisia wa sekta ya madini. Tumekubali dhamana zinazotokana na shughuli halisi za wachimbaji badala ya mali zisizohusiana na sekta.

 Hii itafungua milango kwa maelfu ya wachimbaji wadogo waliokuwa nje ya mfumo rasmi wa kifedha,” alisema Nsekela.
Alieleza kuwa mpango huo unajumuisha mikopo ya mtaji kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za uchimbaji, mikopo ya ununuzi wa mitambo na vifaa vya kisasa, mikopo inayodhaminiwa na dhahabu, huduma za bima za migodi na wafanyakazi kupitia CRDB Insurance, pamoja na akaunti maalum za miamala ya madini na dhahabu zitakazorahisisha ufuatiliaji na uwazi wa biashara.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi CRDB, Donald Mmari, alimweleza Waziri wa Madini kuwa Bodi imeweka miongozo ya kimkakati inayolenga kuhakikisha sekta ya madini inakua kwa kuzingatia misingi ya uendelevu, uwajibikaji na uchumi shirikishi.
“Tunataka kuona wachimbaji wadogo wanapanda ngazi kutoka uchimbaji wa jadi hadi kutumia teknolojia bora, kupata masoko rasmi na kushiriki katika uongezaji thamani. Ukuaji wa sekta ya madini lazima uwe endelevu na wenye manufaa kwa jamii,” alisema Dkt. Mmari.

Benki ya CRDB ni miongoni mwa taasisi chache za kifedha zilizowekeza kwa kiwango kikubwa zaidi katika sekta ya madini nchini. Hadi kufikia mwishoni mwa mwaka jana, Benki hiyo imetoa mikopo yenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 186 katika sekta ya madini, ambapo shilingi bilioni 136 zimetolewa kwa wachimbaji wakubwa na shilingi bilioni 50 kwa wachimbaji wadogo.  

Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji, Rais wa Chama cha Wachimbaji Madini Tanzania (FEMATA), John Bina alisema mpango huo umeleta matumaini mapya kwa wachimbaji wadogo waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kukosa dhamana zinazokubalika na taasisi za fedha.
“Leo tunashuhudia mwanzo wa zama mpya. Wachimbaji wadogo tumepewa heshima ya kutambuliwa kama washirika halali wa maendeleo. Tunaishukuru sana Benki ya CRDB kwa kutuletea suluhisho hii, na tunawaahidi tutaendelea kushirikiana nao pamoja na Serikali kuhakikisha tunatumia fursa hii kwa uwajibikaji,” alisema.

Mkataba wa Makubaliano uliosainiwa kati ya Benki CRDB na Tume ya Madini unatarajiwa kuimarisha urasimishaji wa wachimbaji, kuongeza upatikanaji wa mitaji nafuu, kukuza ajira kwa vijana na wanawake katika maeneo ya migodi, pamoja na kuongeza mapato ya Serikali kupitia uwazi wa miamala na ufuatiliaji wa kidijitali.

RC DENDEGO AMPA TANO DKT SAMIA UTEKELEZAJI KWA VITENDO MRADI WA NISHATI SAFI YA KUPIKIA

February 23, 2026 Add Comment




📍Singida


Katika nchi inayokumbwa na changamoto za kiafya, mazingira na umasikini, nishati safi ya kupikia si tu hitaji la msingi bali ni kichocheo cha maendeleo ya kweli kwa watu na Taifa kwa ujumla.


Katika kukabiliana na ukataji miti ambapo takribani asilimia 16 ya eneo la nchi tayari limegeuka kuwa janga, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilizindua mkakati wa kitaifa wa nishati safi ya kupikia unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya watu wanaachana na matumizi ya kuni na mkaa ifikapo mwaka 2034.

Akizungumza ofisini kwake leo tarehe 23 Februari 2026 mara baada ya kupokea ujumbe wa wataalamu kutoka Wakala wa Nishati Vijijini - REA waliopo mkoani Singida kwa ajili ya kuutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku, Mkuu wa Mkoa wa Singida Mhe. Halima Dendego amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara katika utekelezaji wa mkakati wa nishati safi ya kupikia.

Vilevile Mhe Dendego amesema kuwa Rais Samia ni kinara wa utekelezaji wa Nishati safi Afrika hivyo mkoa wa Singida upo tayari na utaanza kugawa majiko hayo banifu katika wilaya zote za mkoa wa Singida ili mpaka kufikia mwaka 2030 mkoa huo uwe umetengeneza alama kubwa kwa wananchi wake kabla hata ya kufikia mwaka 2034.


Pia, amesema kuwa mkoa wa Singida umepokea mitungi ya gesi zaidi ya 18,000 ambayo imesambazwa kwa wananchi ili kutokomeza kabisa nishati chafu ya kupikia.

Kwa upande wake Mhandisi Raya Majallah kutoka REA-Idara ya Nishati Jadidifu na Teknolojia Mbadala akizungumza mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Singida ameutambulisha mradi wa uuzwaji wa majiko banifu kwa bei ya ruzuku katika mkoa huo ambapo amesema kuwa Wakala wa Nishati Vijijini umeandaa mpango huo wa uuzaji wa majiko banifu 200,000 kwa bei ya ruzuku yenye ufanisi mkubwa katika utumiaji wake.

Mradi huo unahusisha usambazaji wa majiko banifu yanayotumia kuni na mkaa kidogo ili kupunguza matumizi ya vyanzo hivyo vya nishati Pamoja na athari za moshi zitokanazo na matumizi katika majiko ya kawaida.

Mhandisi Majallah amesema kuwa mikataba hiyo ilisainiwa Mei 9, 2025 na itatekelezwa ndani ya miezi 15 ambapo gharama ya mradi huo ni Shilingi Milioni 340,288,200 kwa mkoa wa Singida na ruzuku inayotolewa na wakala wa nishati vijijini-REA ni shilingi milioni 289,230,504.47 sawa na asilimia 85 ya gharama ya mradi huku wananchi wakichangia Shilingi 51,057,691.53 sawa na asilimia 15 ya gharama ya mradi.


MWISHO

SERIKALI YATOA BILIONI 8 KUJENGA KITUO CHA UMEME IMALILO-SIMIYU

February 23, 2026 Add Comment


📌 Kituo cha Imalilo kukamilika Mei 2026, kuimarisha ubora wa umeme Bariadi


📌 Serikali yatoa Shilingi Bilioni 8 kugharamia mradi kwa asilimia 100


Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amefanya ziara ya ukaguzi wa miradi ya umeme inayotekelezwa Mkoani Simiyu kwa lengo la kujionea maendeleo ya utekelezaji wa miradi hiyo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati.


Miradi iliyokaguliwa ni pamoja na ujenzi wa Kituo cha Kupokea na Kusambaza Umeme cha Imalilo pamoja na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 220 (220kV) kutoka Shinyanga hadi Simiyu.

Akizungumza mara baada ya ziara hiyo iliyofanyika tarehe 21 Februari 2026, Bw. Twange alisema mradi wa Kituo cha Imalilo ulianza kutekelezwa mwezi Oktoba 2025 na wataalamu wa ndani wa Shirika, na unatarajiwa kukamilika ifikapo Mei 2026.

“Baada ya muda mrefu tumeanza kutekeleza mradi huu kupitia wataalamu wetu wa ndani ambapo tulianza mwezi Oktoba 2025, na tunatarajia kuukamilisha mwezi Mei 2026,” alisema Bw. Twange.


Alifafanua kuwa kwa sasa wananchi wa Bariadi wanategemea umeme kutoka mikoa jirani ya Shinyanga, Mwanza na Mara, hali inayosababisha kupungua kwa ubora wa umeme kutokana na umbali mrefu unaosafiri.

Alisema kukamilika kwa Kituo cha Imalilo kutaondoa changamoto hiyo na kuimarisha miundombinu ya umeme, hivyo kuhakikisha wananchi wa Bariadi wanapata umeme wa uhakika kuanzia Juni 2026.

“Kwa sasa wananchi wa Bariadi wanategemea umeme kutoka mikoa ya Mwanza, Mara na Shinyanga, hali inayosababisha ubora wa umeme kupungua. Ujenzi wa kituo hiki utaimarisha miundombinu na kuondoa changamoto hizo kuanzia Juni 2026,” aliongeza.

Kwa sasa utekelezaji wa mradi wa Kituo cha Kupokea na Kusambaza Umeme cha Imalilo umefikia asilimia 20.75. Mradi huo unagharimu takribani Shilingi bilioni 8, fedha zinazofadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika awamu ya kwanza

TAIFA GAS WAKUTANA NA WADAU KUWEKA MIKAKATI YA KUTOA HUDUMA BORA ZAIDI KWA WATEJA

February 23, 2026 Add Comment

     

Mwenyekiti Mtendaji wa Taifa Gas, Hamis Ramadhan na Meneja Mkuu,Devis Deogratius wakikata utepe kuwakaribisha mawakala wakubwa (Super Dealers) wa kampuni kwenye kiwanda cha kutengeneza mitungi Kibaha.
Mwenyekiti Mtendaji wa Taifa Gas, Hamis Ramadhan akiongea na mawakala wakuu wa kampuni wakati wa hafla hiyo iliyofanyika katika kiwanda cha kutengeneza mitungi kilichopo Kibaha mkoani Pwani.
Katika hafla hiyo mawakala walitunukiwa vyeti kwa kutambua mchango wao
Baadhi ya mawakala katika hafla hiyo
Baadhi ya mawakala katika picha ya pamoja na viongozi wa kampuni ya Taifa Gas

INEC YAWAFUNDA WASIMAMIZI NA WASIMAMIZI WA SAIDIZI WA VITUO VYA KURA JIMBO LA PERAMIHO

February 23, 2026 Add Comment

 

Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 23, 2026 ametembelea mafunzo ya Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na kuzungumza nao ambapo amewasisitiza kutekeleza majukumu yao kwa weledi kwa kufuata Sheria, Kanuni na maelekezo ya Tume.
Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jaji wa Rufaa Jacobs Mwambegele leo Februari 23, 2026 ametembelea mafunzo ya Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma na kuzungumza nao ambapo amewasisitiza kutekeleza majukumu yao kwa weledi kwa kufuata Sheria, Kanuni na maelekezo ya Tume.

Mafunzo hayo ya siku mbili yalifanyika katika Kumbi tatu tofauti za Seminari Kuu Peramiho, Maposeni Sekondari na Ukumbi wa Josephat Mkuwa ni maandalizi ya Uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika Jimbo la Peramiho ambao unatarajiwa kufanyika Februari 26, 2026 na utashirikisha vyama vya siasa 15.

Wajumbe wengine wa Tume walitembelea vituo hivyo vya mafunzo na kuzungumza na washiriki hao. 


Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho.  
Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Uchaguzi kutoka INEC ambaye pia ni Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Kisheria Ndg. Cyprian Mbugano akizungumza jambo. 
Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho. 
Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Peramiho, wilayani Songea mkoani Ruvuma Ndg. Exavery Luyagaza akizungumza jambo wakati wa mafunzo hayo kituo cha Seminari Kuu Peramiho.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi walipotembelewa katika kituo cha mafunzo kilichopo Ukumbi wa Seminari Kuu Peramiho. 
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) Mhe. Balozi Omar Ramadhan Mapuri, leo Februari 23, 2026 ametembelea na kukagua Mafunzo kwa Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi wa Vituo vya Kupiga Kura katika jimbo la Peramiho, Songea mkoani Ruvuma. 

Mjumbe huyo wa Tume amewapongeza washiriki wa mafunzo na kuwataka kuzingatia weledi na kuwakumbusha kuepuka vitendo vinavyoweza kusababisha matatizo kama yaliyojitokeza katika uchaguzi mkuu uliopita uliofanyika Oktoba 29, 2025.

Balozi Mapuri amewasisitiza washiriki wa mafunzo hayo kuwa mafanikio ya uchaguzi yatatokana na wao kuzingatia mafunzo waliyoyapata ili kufanikisha uchaguzi huu mdogo unaotarajiwa kufanyika Februari 26, 2026 kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo la Peramiho Jenista Mhagama.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma waliokua katika kituo cha mafunzo cha Maposeni Sekondari wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi. 
Mjumbe wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Mhe. Magdalena Rwebangira leo tarehe 23 Februari, 2026 ametembelea na kukagua mafunzo kwa makarani wasimamizi na wasimamizi wasaudizi wa vituo vya kupugia kura yaliyofanyika katika ukumbi wa Josephat Mkuwa uliyopo halmashauri ya wilaya Songea Mkoani Ruvuma ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Peramiho utakaofanyika siku ya Alhamisi tarehe 26 Februari, 2026.

Wasimamizi na Wasimamizi Wasaidizi ngazi ya vituo katika Jimbo la Peramiho lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma waliokua katika kituo cha mafunzo cha Josephat Mokuwa wakisikiliza nasaha za viongozi wa Uchaguzi.