HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts

KAMATI YA BUNGE YAISHAURI SERIKALI KUONGEZA RUZUKU KWA TBA
HABARIKamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeiomba Serikali kuongeza ruzuku kwa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), ili kuwezesha kuongeza kasi ya ujenzi wa nyumba za makazi ya watumishi wa umma nchini.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Selemani Kakoso, wakati wa ziara ya kukagua miradi ya nyumba za watumishi inayotekelezwa na TBA katika maeneo ya Kisasa na Nzuguni jijini Dodoma, ikiwa ni sehemu ya ziara ya kutathmini utekelezaji wa miradi ya miundombinu nchini.
Kakoso amesema Kamati imejiridhisha na juhudi zinazofanywa na Serikali pamoja na TBA katika kukabiliana na changamoto ya makazi kwa watumishi wa umma, huku akisisitiza umuhimu wa kuongeza kasi ya ujenzi kutokana na mahitaji makubwa ya nyumba nchini.
Amesema eneo la Nzuguni lenye takribani ekari 630 lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa makazi ni hatua muhimu katika kuendeleza mji mpya wa Serikali, kwa kuwa uwepo wa nyumba hizo utawasaidia watumishi, wakiwemo walio katika ngazi za chini, kupata makazi yaliyo karibu na maeneo yao ya kazi.
“Tunawapongeza Serikali kwa juhudi kubwa zilizofanyika na pia TBA kwa mipango mizuri ya kuandaa nyumba za makazi ya watumishi. Tumekagua eneo la Kisasa na tumeona maboresho makubwa katika nyumba zilizojengwa,” amesema Kakoso.
Hata hivyo, Kamati imeishauri Serikali kuharakisha upatikanaji wa wabia kupitia utaratibu wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), ili kuongeza uwezo wa TBA kutekeleza miradi mikubwa ya nyumba kwa wakati na kukidhi mahitaji ya watumishi.
Kwa mujibu wa Kamati hiyo, ushirikishwaji wa sekta binafsi utawezesha kupatikana kwa mitaji na utaalamu zaidi, huku Serikali ikiendelea kusimamia miradi hiyo kuhakikisha inatoa huduma bora na nyumba zenye viwango vinavyokidhi mahitaji ya watumishi.
Kuhusu huduma ya maji, Kamati imepongeza TBA kwa kuanzisha mfumo wake wa maji bila kutegemea kikamilifu huduma kutoka Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dodoma (DUWASA).
Hata hivyo, imeitaka TBA kuongeza juhudi za kuchimba visima na kuimarisha mifumo ya majitaka ili kukidhi mahitaji ya eneo hilo kwa muda mrefu.
Aidha, Kamati imeishauri TBA kuangalia uwezekano wa kutumia nishati ya jua kama chanzo mbadala cha umeme, hatua ambayo itasaidia kupunguza utegemezi wa mfumo wa kawaida wa umeme na kuhakikisha huduma zinaendelea kupatikana wakati changamoto za umeme zinapotokea.
Vilevile, Kamati imeitaka Wizara ya Ujenzi kushirikiana na Ofisi ya Rais-TAMISEMI, TANROADS, TARURA pamoja na TBA katika ujenzi wa miundombinu bora ya barabara katika maeneo hayo, hususan barabara za lami, ili kuongeza mvuto wa makazi hayo na kurahisisha usafiri.
Kamati imesisitiza kuwa ujenzi wa nyumba za watumishi ni uwekezaji wa muda mrefu unaopaswa kuzingatia thamani ya fedha, ubora wa majengo na mahitaji ya wananchi, ili miundombinu hiyo iwe na tija kwa Serikali na kizazi cha sasa na kijacho.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Miliki wa TBA, Said Rajabu Mndeme, aliyemwakilisha Mtendaji Mkuu wa TBA, amesema mradi huo unatekelezwa katika eneo lenye takribani ekari 640, ambapo ujenzi wa nyumba 150 tayari umekamilika.
Amesema nyumba nyingine 110 zipo katika hatua mbalimbali za ujenzi, zikiwemo nyumba 50 za chini zilizofikia hatua ya mwisho na zinatarajiwa kuanza kutumika. Aidha, majengo mawili ya ghorofa tano yako katika hatua ya msingi, ambapo kila jengo litakuwa na uwezo wa kuhudumia familia 30.
Kwa mujibu wa Mndeme, TBA imeanza kushirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa mradi huo baada ya eneo hilo kutangazwa na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi kuwasilisha mapendekezo ya kushirikiana na Wakala.
Amesema mradi huo umepangwa kuwa na huduma muhimu zikiwemo shule za awali, shule mbili za msingi, maeneo ya biashara pamoja na vyuo.
Mndeme amesema mahitaji ya nyumba katika Jiji la Dodoma ni makubwa, akifichua kuwa wakati ujenzi wa nyumba 150 za awali ulipokuwa ukiendelea, TBA ilipokea zaidi ya maombi 1,000 kutoka kwa watumishi waliokuwa wakihitaji makazi.
Amesema hadi sasa, Meneja wa TBA Mkoa wa Dodoma ana maombi zaidi ya 8,000 ya nyumba kutoka kwa watumishi na wananchi, hali inayoonyesha ukubwa wa changamoto ya makazi katika jiji hilo.
Mndeme ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita na Wizara ya Ujenzi kwa kuendelea kuiwezesha TBA kupitia ruzuku, akisema mradi huo ulioanza mwaka 2021 umeendelea kutekelezwa kwa ufadhili wa Serikali.
Amesema TBA sasa inalenga kuongeza kasi ya ushirikishwaji wa sekta binafsi ili kuharakisha ukamilishaji wa mpango wa ujenzi wa nyumba 3,500 na hivyo kupunguza changamoto ya makazi katika Jiji la Dodoma.

KAIRUKI AITAKA TTCL KUSIMAMIA KWA UKALI WAKANDARASI WA MRADI WA FAIBA
HABARI
Na Mwandishi Wetu - DAR ES SALAAM,
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki, ameitaka TTCL kuhakikisha wazabuni na wakandarasi wanaotekeleza Awamu ya Pili ya Mradi wa Faiba Mlangoni Kwako wanasimamiwa kwa ufanisi ili kazi zikamilike kwa wakati, kwa ubora na kwa kuzingatia thamani ya fedha.
Mhe. Kairuki amesema usimamizi wa mradi ni muhimu katika kuhakikisha uwekezaji wa Serikali na Shirika unazalisha miundombinu inayodumu na inayotoa huduma bora kwa wananchi.

Ametoa maelekezo hayo wakati wa uzinduzi wa Awamu ya Pili ya mradi huo katika Ukumbi wa Johari Rotana jijini Dar es Salaam.
Amesema mafanikio ya mradi hayatakiwi kuishia katika kujenga Home Pass, bali yanapaswa kuonekana katika huduma zinazotolewa kwa wananchi, kasi ya intaneti na kuridhika kwa wateja.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, CPA Moremi Marwa, amesema utekelezaji wa Awamu ya Pili unafanyika kwa ushirikiano na makandarasi wa ndani na wa kimataifa wakiwemo Huawei, ZTT na Visoll.
Amesema Awamu hiyo inalenga kuongeza zaidi ya Home Pass 400,000, ikiwa ni hatua inayotarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za intaneti ya kasi.
Marwa amesema TTCL pia imeendelea kutumia teknolojia ya GPON kuongeza ufanisi na kuboresha ubora wa huduma.









BALOZI SALUM AZITAKA FCC, TBS NA WMA KUPAMBANA NA BIDHAA BANDIA NA DUNI
habariRC BURIAN ATOA MWELEKEO KWA WANANCHI 66 WA MSAKANGOTO
habari
Na Oscar Assenga, MUHEZA
MKUU wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi 66 wa Kitongoji cha Bago Maisha Plus ,Kijiji cha Msakangoto, Kata ya Kigombe wilayani Muheza, kuondoka katika eneo walilokuwa wakiishi na kuhamia eneo jipya lililotengwa na Serikali ya Kijiji, huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kuwasaidia katika kipindi cha mpito.
Wananchi hao wamekumbwa na changamoto hiyo baada ya nyumba zao kubomolewa kufuatia utekelezaji wa amri ya mahakama iliyotokana na mgogoro wa umiliki wa eneo hilo.
Balozi Burian alitoa kauli hiyo leo alipofanya ziara katika eneo hilo na kukutana na wananchi hao, ambapo alisema Serikali haina mamlaka ya kuzuia utekelezaji wa amri ya mahakama.
Alisema baada ya kubaini kuwa eneo hilo lilikuwa ndani ya hati ya umiliki ya mwekezaji wa Mashamba ya Mkonge ambaye tayari alikuwa amefungua kesi mahakamani na kupata amri ya kuwaondoa wananchi, Serikali ililazimika kuheshimu uamuzi huo.
“Serikali haiwezi kupingana na sheria ya mahakama. Aliyekuja kubomoa alikuwa anatekeleza maelekezo ya mahakama. Hata hivyo, sisi kama Serikali tuliona ni lazima tuzungumze na wananchi na mwekezaji ili kutafuta suluhisho la kibinadamu,” alisema.
Alisema awali wananchi hao walipelekwa katika eneo hilo na Serikali ya Kijiji, huku wakiwa na vielelezo vilivyoonyesha kuwa waliruhusiwa kuishi katika eneo hilo, jambo lililopelekea Serikali ya Mkoa kuingilia kati baada ya mgogoro kujitokeza.
Balozi Burian alisema Serikali ya Mkoa imefanya mazungumzo na mwekezaji kupitia Wizara inayohusika na Uwekezaji, hatua iliyosaidia kuwezesha kupatikana kwa eneo jingine kwa ajili ya kuwahamishia wananchi hao.
Alisema eneo lililotengwa awali kwa ajili ya makazi mapya lilibainika kuwa halifai kutokana na kuwa na maji, hivyo Serikali ililazimika kutafuta eneo jingine.
“Wawakilishi wenu wamekuja ofisini kwangu mara tatu. Hatua ya kwanza ilikuwa kwenda kuzungumza na mwekezaji, hatua ya pili mwekezaji akakubali kutoa Sh200,000 na hatua nyingine ni kuhakikisha hakuna mtu anayewasumbua wakati taratibu za kuwahamisha zikikamilishwa,” alisema.
Balozi Burian alisema maturubai ambayo wanayatumia kwa muda wakati wakijiandaa kujenga makazi yao mapya.
“Kesho asubuhi tutahamisha maturubai hayo kwenda kwenye eneo ambalo mtaenda kuhamia. Mtayatumia kwa mwezi mmoja wakati mkiendelea kujipanga kujenga makazi yenu,” alisema.
Alisema Serikali itaendelea kutafuta wadau na wasamaria wema watakaoweza kusaidia katika ujenzi wa makazi mapya kwa wananchi hao.
Aidha, aliwataka wananchi hao kutokata tamaa na kuacha kuchukua hatua zinazoweza kuwaingiza katika mgogoro mwingine wa kisheria.
“Ndugu zangu, mchakato mzima nimewaeleza. Sina mamlaka ya juu zaidi ya hapa. Kila mhimili una kiwango chake cha kushughulikia jambo. Likishafika mahakamani, Serikali haiingilii tena,” alisema.
Alisema wananchi wanapaswa kuanza maisha katika eneo jipya huku wakiamini kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili.
Akizungumza kwa niaba ya wananchi hao, Ally Mohamed, mkazi wa Maisha Plus, alisema suala la fidia limekuwa miongoni mwa changamoto kubwa zilizowafanya kuwa na wasiwasi kuhusu kuhamia eneo jipya.
Alisema baadhi yao walitumia mafao waliyopata kutoka Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kujenga nyumba zao, hivyo kubomolewa kwa nyumba hizo kumewasababishia hasara kubwa.
“Baadhi yetu tulitumia mafao yetu ya NSSF kujenga nyumba. Sasa nyumba zimebomolewa na tunajiuliza tutaanzaje maisha upya,” alisema.
Akijibu suala hilo, Balozi Burian alisema wananchi waliokuwa na madai ya fidia wakati shauri likiendelea walikuwa na nafasi ya kuyawasilisha mahakamani.
Hata hivyo, alisema Serikali ya Mkoa imeendelea kufanya mazungumzo na mwekezaji kwa lengo la kutafuta namna ya kuwasaidia wananchi hao katika kipindi hiki cha mpito.
Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kigombe (CCM) Shahongwe Mgandi aliishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua iliyochukua, akisema viongozi wa kata watahakikisha wananchi hao wanapata usalama na huduma muhimu katika eneo jipya.
Alisema Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeanza maandalizi ya kufikisha huduma ya umeme katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na kusimika nguzo.
Alisema pia maeneo ambayo wananchi hao watahamia yatatambuliwa kisheria na kutambuliwa kama kitongoji, huku Serikali ikiendelea kuboresha barabara na huduma nyingine muhimu.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Maisha Plus alishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua hiyo na kuiomba iruhusu wananchi hao, inapowezekana, kuhamisha baadhi ya miti waliyokwishaipanda katika eneo la awali ili kuitumia katika mazingira ya makazi mapya.
Hatua hiyo, alisema, itawasaidia wananchi hao kuanza maisha mapya huku wakitunza mazingira katika eneo watakalohamia.