HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

NM-AIST YAWASILISHA ZAIDI YA BUNIFU 20 WIKI YA ELIMU, UJUZI NA UBUNIFU.

NM-AIST YAWASILISHA ZAIDI YA BUNIFU 20 WIKI YA ELIMU, UJUZI NA UBUNIFU.

August 23, 2026 Add Comment

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi na washiriki wa Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu inayofanyika jijini Tanga kuhusu bunifu mbalimbali zinazozalishwa na watafiti na wabunifu wanaoshirikiana na taasisi hiyo.

Katika maadhimisho hayo, NM-AIST imewasilisha jumla ya bunifu 20, ambazo nyingi zimetokana na tafiti na kazi za watafiti wa ndani ya taasisi, huku nyingine zikiwa zimezalishwa na wabunifu wa nje wanaopatiwa malezi, mafunzo na mwongozo kupitia taasisi hiyo. Bunifu hizo zinaonesha jitihada za NM-AIST katika kuunganisha utafiti, ubunifu na mahitaji halisi ya jamii.

Aidha, taasisi hiyo imewashirikisha wawakilishi wa vikundi vya wanawake wanaopatiwa msaada na mwongozo katika kuboresha bidhaa zao na kuongeza thamani. Hatua hiyo inalenga kuwawezesha kutumia maarifa na teknolojia kuongeza ubora, tija na ushindani wa bidhaa zao sokoni.

Katika hatua nyingine, NM-AIST imewasilisha kampuni tatu zilizoanzishwa kutokana na bunifu na tafiti zilizofanyika ndani ya taasisi. Kampuni hizo ni Nano Filter, inayojihusisha na teknolojia ya uchujaji wa maji; AfriTech, inayotumia teknolojia inayotokana na mabaki ya korosho katika uchakataji wa ngozi; na Uji Chap Chap, inayolenga kuchangia afya bora kupitia bidhaa za lishe.

Ushiriki wa NM-AIST katika maonyesho hayo unaendelea kutoa fursa kwa wananchi kujifunza namna ambavyo matokeo ya utafiti na ubunifu yanaweza kubadilishwa kuwa bidhaa na huduma zenye manufaa kwa jamii. Aidha, ushiriki huo unaonesha mchango wa taasisi katika kukuza matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu kama nyenzo muhimu za maendeleo ya Tanzania.

NM-AIST inaendelea kuthibitisha dhamira yake ya kuifikia jamii, kuwatamia wajasiriamali na kukuza ubunifu kwa maendeleo endelevu.

NM-AIST KUTEKELEZA DIRA 2050 KUPITIA UTAFITI, UBUNIFU NA UJASIRIAMALI

NM-AIST KUTEKELEZA DIRA 2050 KUPITIA UTAFITI, UBUNIFU NA UJASIRIAMALI

August 23, 2026 Add Comment
 

Mkuu wa Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela Mhe. Omari Issa atunuku shahada za umahiri na uzamivu kwa wahitimi 138 katika Mahafali ya 12 ya Taasisi ya Nelson Mandela yaliyofanyika Leo tarehe 20 Agosti 2026, NM-AIST Tengeru Arusha.

Mwenyekiti wa Baraza la Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST), Balozi Maimuna Tarishi, amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha tafiti, teknolojia na ubunifu unaozalishwa na Taasisi unatafsiriwa kuwa bidhaa, huduma na suluhisho halisi kwa changamoto za jamii, sambamba na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050.

Akizungumza katika Mahafali ya 12 ya Taasisi (NM-AIST), Balozi Tarishi amesema ubunifu haupaswi kuishia kwenye makaratasi au usajili wa hati miliki, bali unapaswa kutumika kutatua changamoto katika sekta za kilimo, ufugaji, biashara, mazingira na uchumi.

“Ubunifu usiishie kwenye makaratasi wala usajili BRELA; twende tukautafsiri kwa vitendo ili kujibu changamoto mbalimbali za jamii,” amesema Balozi Tarish.

Aidha, amewataka wahitimu kutumia maarifa na ujuzi walioupata NM-AIST kujitolea kuitumikia jamii ya Tanzania na Afrika, badala ya kutumia elimu kwa manufaa binafsi pekee.

Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa NM-AIST, Prof. Maulilio Kipanyula, amesema jumla ya wahitimu 138 wamehitimu katika mahafali hayo, wakiwa wamezalisha machapisho 219 ya kisayansi na hati miliki saba.

Amesema NM-AIST itaendelea kuhamasisha wanafunzi na watafiti kuzalisha bidhaa, kufanya ugunduzi na kuchapisha tafiti katika majarida ya kimataifa. 

Pia, Profesa Maulilio Kipanyula amesema watafiti 19 wa NM-AIST wametambuliwa katika tuzo za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia zinazohusisha machapisho katika majarida ya kisayansi yenye hadhi ya juu duniani.

NM-AIST inaendelea kubadili maarifa kuwa ubunifu, ubunifu kuwa bidhaa na huduma, na tafiti kuwa suluhisho la changamoto za jamii sambamba na utekelezaji wa Dira 2050.

MVUA YAWAPA KAZI VIJANA BUNIFU

August 23, 2026 Add Comment

 




Na Oscar Assenga, TANGA

VIJANA wameanza kutumia maarifa ya Sayansi, Teknolojia, Uhandisi na Hisabati (STEM) kubuni suluhisho za changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii, kupitia mradi wa Vijana Bunifu unaotekelezwa chini ya programu ya Tanga Yetu

Mradi huo unaolenga kuwajengea watoto na vijana hamasa ya kujifunza masomo ya STEM, pia umekuwa ukitoa nafasi kwa vijana wenye mawazo ya kibunifu kuyabadilisha kuwa bidhaa au suluhisho zinazoweza kutumika katika maisha ya kila siku.

Akizungumza kuhusu mradi huo, Mkufunzi wa Masomo ya STEM kutoka Project Inspire,Mohamed Mohamed,  alisema lengo ni kuwajengea watoto na vijana msingi wa elimu ya STEM tangu wakiwa wadogo, huku wakiandaliwa kwa taaluma mbalimbali za baadaye.

Alisema Project Inspire inatekeleza mradi huo kupitia mfumo wa STEM Career Radar, unaolenga kumsaidia mtoto kutambua na kukuza uwezo wake katika nyanja za STEM, ikiwamo udaktari, uhandisi na Sayansi ya Kompyuta.

“Lengo letu ni kutengeneza interest kwa watoto katika kujifunza masomo ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati, kisha kuwasaidia kuchukua mawazo waliyonayo kichwani na kuyaweka katika uhalisia,” alisema Mohamed.

Alisema katika hatua ya kwanza, mradi unawahusisha watoto wenye umri wa chini ya miaka mitatu hadi 12, ambao hufundishwa masomo ya STEM kwa njia ya vitendo ili kuwawezesha kuelewa kwa urahisi na kujenga hamasa ya kujifunza.

Kwa mujibu wa Mohamed, hatua nyingine inalenga vijana wenye umri wa miaka 13 hadi 18, ambapo vijana wenye mawazo ya kutatua changamoto mbalimbali katika jamii hupewa nafasi ya kuyafanyia kazi.

Alisema vijana hao hushiriki programu mbalimbali, ikiwamo Boot Camp, inayowapa fursa ya kujifunza, kubadilishana mawazo na kutengeneza bunifu zinazolenga kutatua changamoto halisi.

Bunifu ya nyumba ‘inayohisi’ mvua

Miongoni mwa bunifu zilizotengenezwa na vijana hao ni mfumo wa nyumba unaoweza kutambua mvua na kusaidia kuzuia nguo zilizofuliwa  na kuanikwa nje kutokulowana.

Mohamed alisema mfumo huo umewekewa kihisi (sensor) kinachoweza kutambua uwepo wa mvua.

Alisema mvua inapoanza kunyesha, mfumo huo hufanya kazi ya kupeleka sehemu ya kukaushia nguo upande ambao hauna mvua, hivyo kusaidia kuzuia nguo kulowana.

“Mfano, mtu amefua nguo na anatamani kuzivaa kwenye kikao, ametoka lakini mvua imeanza kunyesha. Mfumo unatambua kuwa kuna mvua na nguo zinarudishwa upande ambao hakuna mvua,” alisema.

Alisema mvua inapokatika, mfumo huo hutambua hali hiyo na kuirudisha sehemu ya kukaushia nguo upande wenye jua ili nguo ziendelee kukauka.

Mohamed alisema bunifu hiyo ni mfano wa namna vijana wanavyofundishwa kutumia STEM kutatua changamoto zinazojitokeza katika maisha ya kila siku.

Kutoka mshiriki hadi mlezi wa vijana

Kwa upande wake, Mboni Zahoro, mmoja wa wanufaika wa mradi huo, alisema safari yake ya kutumia STEM ilianza akiwa mwanafunzi na mshiriki wa programu ya Boot Camp.

Alisema baada ya kumaliza masomo, aliamua kujitolea na kujifunza zaidi namna ya kuwasaidia vijana wenzake kutumia sayansi, teknolojia na ubunifu katika kukuza ujuzi wao.

Mboni alisema baada ya kuanza kwa mradi wa Vijana Bunifu alipata nafasi ya kuwa STEM Communicator, akitumia uzoefu na maarifa aliyoyapata kuwasaidia vijana wengine kukuza mawazo yao.

“Nilianza kama mwanafunzi na mshiriki wa Boot Camp. Baada ya kumaliza masomo nilijitolea kujifunza namna ya kuwasaidia vijana wenzangu kutekeleza sayansi, teknolojia na ubunifu,” alisema.

Alisema kwa sasa anawasaidia vijana kuchukua mawazo waliyonayo na kuyakuza kupitia teknolojia ili yaweze kuwa suluhisho la changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Mboni alisema anaamini kuendelea kuwafundisha vijana masuala ya sayansi, teknolojia, uhandisi na hisabati kutawasaidia kufikia mbali zaidi na kutumia ujuzi wao kuleta mabadiliko katika jamii.

Alisisitiza umuhimu wa vijana kujifunza kwa vitendo, akisema njia hiyo inawapa nafasi ya kuonyesha uwezo wao, kukuza ubunifu na kutengeneza suluhisho zinazolenga changamoto halisi za jamii.

ADEM YAENDESHA MAFUNZO YA UONGOZI NA USIMAMIZI WA UTEKELEZAJI WA MTAALA ULIOBORESHWA

August 23, 2026 Add Comment
23 Agosti 2026. | 📍Bagamoyo, Tanzania.

Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) umeendelea kutoa mafunzo maalum ya siku mbili kuhusu Uongozi na Usimamizi wa Utekelezaji wa Mtaala Ulioboreshwa, yakilenga kuimarisha uwezo wa Wakuu wa Shule za Sekondari katika kusimamia kwa ufanisi mabadiliko ya mtaala.

HUDUMA ZA DHARURA ZIMEIMARIKA NCHINI- DKT. SYLVANUS

August 23, 2026 Add Comment

Na Cletus Sanga, WAF – Kibiti

Huduma za dharura nchini zimeendelea kuimarika kupitia hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali katika kuimarisha mfumo wa huduma za dharura, ikiwemo kuongeza na kuboresha magari ya wagonjwa ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi wanaohitaji msaada wa haraka.

INNOIP YAFUNGUA FURSA MPYA KWA WABUNIFU

August 22, 2026 Add Comment

 



Na OSCAR ASSENGA, Tanga


SERIKALI imezindua programu ya InnoIP Tanzania, inayolenga kuwasaidia zaidi ya wabunifu 5,000 nchini kulinda kazi zao kisheria, kuzigeuza kuwa fursa za biashara na kuchochea uundaji wa ajira.


Programu hiyo pia inalenga kukabiliana na changamoto ya wizi wa mawazo na ubunifu inayowakabili wabunifu wengi, hasa wanaoweka wazi mawazo yao kabla ya kuchukua hatua za kuyakinga kisheria.


Uzinduzi huo umefanywa Agosti 22, 2026, na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, katika maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.




Akizungumza na mamia ya wadau wa sekta ya sayansi na ubunifu, Dkt. Batilda alisema Tanzania inapaswa kuhakikisha ubunifu wa ndani unalindwa kisheria na kuunganishwa na masoko makubwa ili kuongeza thamani ya bidhaa na teknolojia zinazozalishwa na Watanzania.

Alisema baadhi ya wabunifu hupoteza fursa kwa kuweka wazi mawazo yao mapema bila kuwa na makubaliano yanayoeleweka kuhusu umiliki wa ubunifu huo.


Kwa mujibu wa Dkt. Batilda, hali hiyo inaweza kumsababishia mbunifu kukosa ulinzi wa kisheria wa kazi yake na kuwafanya wawekezaji kusita kuwekeza katika kampuni changa ambazo hazina uthibitisho wa umiliki wa haki zao za miliki bunifu.


FURSA WOMEN KULENGA WANAWAKE


Sambamba na uzinduzi wa InnoIP Tanzania, Mkuu wa Mkoa alitangaza kuanza kwa programu ya Fursa Women, inayolenga kuwawezesha wanawake wajasiriamali kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kukuza biashara zao.


Dkt. Batilda alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara na kuwawezesha wafanyabiashara kuwafikia wateja wengi kwa haraka zaidi.

Aidha, alizitaka vyuo vikuu na taasisi za utafiti kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinageuzwa kuwa bidhaa na suluhisho halisi zinazowanufaisha wananchi, badala ya kuishia kwenye makabrasha na makabati.



Pia aliwataka wawekezaji na taasisi za fedha kushirikiana na wabunifu wa Kitanzania kwa kununua bidhaa zao, kuwekeza katika teknolojia zao na kuwawezesha kupata mitaji kwa ajili ya kukuza biashara.


Akizungumzia ushiriki wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Mkurugenzi wa Miliki, Loy Mhando, aliyemwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu, alisema InnoIP Tanzania haimaanishi kuwa kila ubunifu lazima upatiwe hataza (Patent).


Alisema programu hiyo itawasaidia wabunifu kutambua aina sahihi ya ulinzi wa kisheria kulingana na aina ya ubunifu wao, ikiwemo hataza, alama za biashara, hakimiliki na siri za biashara.


Alifafanua kuwa InnoIP inasimamiwa na BRELA na kuratibiwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), kupitia atamizi za Dar Teknohama Business Incubator (DTBi) na Buni Innovation Hub.


Programu hiyo inalenga kuwasaidia kampuni changa, watafiti, wanafunzi wa vyuo vikuu, biashara ndogo na za kati pamoja na wajasiriamali kutambua, kulinda na kubiasharisha haki zao za miliki bunifu.


Mhando alisema katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji, programu hiyo inalenga kufanya uchambuzi wa kina wa mahitaji ya wabunifu 120 wa awali, ambao watasaidiwa kisheria na kifedha kulinda kazi zao na baadaye kuunganishwa na wawekezaji.



Alisema uteuzi wa wabunifu hao utazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo umuhimu wa ubunifu husika kwa jamii pamoja na uwezo wake wa kuzalisha faida.


Kwa mujibu wa Mhando, programu hiyo itawasaidia wabunifu kupitia hatua saba: utambuzi na uhamasishaji; mafunzo na warsha za vitendo; uchambuzi wa mahitaji; maandalizi ya ramani ya ulinzi; uwasilishaji wa maombi ya usajili; ubiasharishaji kwa kuwaunganisha na wawekezaji; pamoja na ufuatiliaji endelevu.


Aliwataka wabunifu na kampuni changa kutumia fursa hiyo mapema badala ya kusubiri hadi mgogoro wa umiliki unapotokea, mawazo yao yanaponakiliwa au mwekezaji anapohitaji uthibitisho wa kisheria kuhusu umiliki wa biashara.

 

Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema miliki bunifu si suala la kisheria pekee, bali ni rasilimali muhimu ya kiuchumi inayoweza kuwa msingi wa kuvutia uwekezaji, utoaji wa leseni kwa viwanda vingine, uhamishaji wa teknolojia na ujenzi wa biashara zinazoweza kukua hadi masoko ya kimataifa.


“Changamoto yetu kuu kwa sasa nchini si ukosefu wa mawazo; ni kuhakikisha kuwa mawazo mazuri ya vijana, watafiti na wabunifu wetu yanalindwa kisheria, yanaendelezwa na hatimaye yanafikishwa sokoni,” alisema Dkt. Nungu.


Alisema mafanikio ya InnoIP hayatapimwa kwa idadi ya watu watakaohudhuria mafunzo na semina pekee, bali kwa matokeo, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya ubunifu unaolindwa kisheria, teknolojia mpya kuingia sokoni, biashara kukua, uwekezaji kuvutiwa na ajira mpya kuzalishwa.



Akizungumzia programu ya Fursa Women, Dkt. Nungu aliishukuru Airtel Tanzania kwa kushirikiana na COSTECH katika kufadhili programu hiyo.


Alisema ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja katika kujenga jamii yenye ujuzi wa kidijitali.


Alifafanua kuwa kupitia Fursa Women, wanawake watajengewa uelewa kuhusu matumizi sahihi na salama ya mifumo ya kidijitali katika kutangaza bidhaa, kuwafikia wateja, kufanya na kupokea malipo mtandaoni pamoja na kuhifadhi kumbukumbu za biashara zao.


Dkt. Nungu alitoa wito kwa wawekezaji na sekta binafsi kutambua kuwa ubunifu wa Kitanzania ni fursa ya uwekezaji ambayo bado haijatumika kikamilifu.


Aliwaalika kushirikiana na Serikali katika kujaribu, kununua na kupanua matumizi ya teknolojia pamoja na suluhisho mbalimbali zinazozalishwa na Watanzania.


Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanatarajiwa kufungwa Jumatatu na Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba.

KAMBARAGE VIJANA CHOIR YAANDAA TAMASHA LA UIMBAJI “NIMEBEBA USHUHUDA”

August 22, 2026 Add Comment


Mwenyekiti wa Kambarage Vijana Choir, Heri Ndaki, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tamasha la Uimbaji Mubashara ‘Nimebeba Ushuhuda’ linalotarajiwa kufanyika Oktoba 16, 2026 katika Kanisa la AIC Kambarage, Manispaa ya Shinyanga.
Mwenyekiti wa Kambarage Vijana Choir, Heri Ndaki, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tamasha la Uimbaji Mubashara ‘Nimebeba Ushuhuda’ linalotarajiwa kufanyika Oktoba 16, 2026 katika Kanisa la AIC Kambarage, Manispaa ya Shinyanga.

Na Elizabeth Cosmas - Shinyanga

Kwaya ya Vijana ya Kanisa la AIC Kambarage, maarufu kama Kambarage Vijana Choir (KVC), imeandaa Tamasha la Uimbaji Mubashara litakalobeba jina la “Nimebeba Ushuhuda”, huku likilenga kuunganisha waumini wa madhehebu mbalimbali na kuhamasisha jamii kudumisha amani, upendo na mshikamano.

MANYARA TANZANITE MARATHON YALENGA SH1.5 BILIONI KUOKOA WATOTO NJITI

Kajunason August 22, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu, Manyara

MBIO za hisani za Manyara Tanzanite Marathon 2026 zimefanyika leo katika Mji wa Babati, mkoani Manyara, huku waandaaji wakiwa na lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zilizoendeshwa chini ya kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti”, zimewakutanisha wananchi, wanariadha na wadau mbalimbali kutoka maeneo tofauti nchini, kwa lengo la kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto njiti.

Mgeni rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, amepongeza Mkoa wa Manyara kwa kuanzisha mbio hizo, akisema ni ubunifu unaolenga kushirikisha jamii katika kuchangia huduma za afya.

Sillo amesema Manyara Tanzanite Marathon ni mfano wa namna matukio ya michezo yanavyoweza kutumika katika kuhamasisha jamii na wadau kuchangia miradi yenye manufaa kwa wananchi, hususan katika sekta ya afya.

Amesema jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono na maeneo mengine nchini ili kuongeza ushiriki wa jamii katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
MBIO za hisani za Manyara Tanzanite Marathon 2026 zimefanyika leo katika Mji wa Babati, mkoani Manyara, huku waandaaji wakiwa na lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zilizoendeshwa chini ya kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti”, zimewakutanisha wananchi, wanariadha na wadau mbalimbali kutoka maeneo tofauti nchini, kwa lengo la kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto njiti.

Mgeni rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, amepongeza Mkoa wa Manyara kwa kuanzisha mbio hizo, akisema ni ubunifu unaolenga kushirikisha jamii katika kuchangia huduma za afya.

Sillo amesema Manyara Tanzanite Marathon ni mfano wa namna matukio ya michezo yanavyoweza kutumika katika kuhamasisha jamii na wadau kuchangia miradi yenye manufaa kwa wananchi, hususan katika sekta ya afya.
Amesema jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono na maeneo mengine nchini ili kuongeza ushiriki wa jamii katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zina umuhimu mkubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, huku akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono mipango inayolenga kuboresha huduma za afya.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau walioshiriki katika maandalizi na utekelezaji wa mbio hizo, akisema ushirikiano wao umewezesha kufanikisha tukio hilo lenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.
Sendiga amesema fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zitaelekezwa katika kufanikisha ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum kwa ajili ya kuwahudumia watoto njiti, ambao huhitaji huduma za kitaalamu na vifaa maalumu tangu wanapozaliwa.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema walishiriki si kwa ajili ya mazoezi na afya zao pekee, bali pia kuchangia juhudi za kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema Manyara Tanzanite Marathon imewapa fursa ya kuunganisha michezo na shughuli za kijamii, huku wakitoa wito kwa wananchi wengine kushiriki katika matukio yenye malengo ya kuboresha afya na ustawi wa jamii.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeweka lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti” inayolenga kuongeza uwezo wa huduma za afya kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati mkoani Manyara.