HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

INNOIP YAFUNGUA FURSA MPYA KWA WABUNIFU

August 22, 2026 Add Comment

 



Na OSCAR ASSENGA, Tanga


SERIKALI imezindua programu ya InnoIP Tanzania, inayolenga kuwasaidia zaidi ya wabunifu 5,000 nchini kulinda kazi zao kisheria, kuzigeuza kuwa fursa za biashara na kuchochea uundaji wa ajira.


Programu hiyo pia inalenga kukabiliana na changamoto ya wizi wa mawazo na ubunifu inayowakabili wabunifu wengi, hasa wanaoweka wazi mawazo yao kabla ya kuchukua hatua za kuyakinga kisheria.


Uzinduzi huo umefanywa Agosti 22, 2026, na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batilda Burian, katika maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayoendelea katika Viwanja vya Usagara, jijini Tanga.




Akizungumza na mamia ya wadau wa sekta ya sayansi na ubunifu, Dkt. Batilda alisema Tanzania inapaswa kuhakikisha ubunifu wa ndani unalindwa kisheria na kuunganishwa na masoko makubwa ili kuongeza thamani ya bidhaa na teknolojia zinazozalishwa na Watanzania.

Alisema baadhi ya wabunifu hupoteza fursa kwa kuweka wazi mawazo yao mapema bila kuwa na makubaliano yanayoeleweka kuhusu umiliki wa ubunifu huo.


Kwa mujibu wa Dkt. Batilda, hali hiyo inaweza kumsababishia mbunifu kukosa ulinzi wa kisheria wa kazi yake na kuwafanya wawekezaji kusita kuwekeza katika kampuni changa ambazo hazina uthibitisho wa umiliki wa haki zao za miliki bunifu.


FURSA WOMEN KULENGA WANAWAKE


Sambamba na uzinduzi wa InnoIP Tanzania, Mkuu wa Mkoa alitangaza kuanza kwa programu ya Fursa Women, inayolenga kuwawezesha wanawake wajasiriamali kutumia teknolojia na mifumo ya kidijitali kukuza biashara zao.


Dkt. Batilda alisema matumizi ya teknolojia yanaweza kupunguza gharama za uendeshaji wa biashara na kuwawezesha wafanyabiashara kuwafikia wateja wengi kwa haraka zaidi.

Aidha, alizitaka vyuo vikuu na taasisi za utafiti kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinageuzwa kuwa bidhaa na suluhisho halisi zinazowanufaisha wananchi, badala ya kuishia kwenye makabrasha na makabati.



Pia aliwataka wawekezaji na taasisi za fedha kushirikiana na wabunifu wa Kitanzania kwa kununua bidhaa zao, kuwekeza katika teknolojia zao na kuwawezesha kupata mitaji kwa ajili ya kukuza biashara.


Akizungumzia ushiriki wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Mkurugenzi wa Miliki, Loy Mhando, aliyemwakilisha Afisa Mtendaji Mkuu, alisema InnoIP Tanzania haimaanishi kuwa kila ubunifu lazima upatiwe hataza (Patent).


Alisema programu hiyo itawasaidia wabunifu kutambua aina sahihi ya ulinzi wa kisheria kulingana na aina ya ubunifu wao, ikiwemo hataza, alama za biashara, hakimiliki na siri za biashara.


Alifafanua kuwa InnoIP inasimamiwa na BRELA na kuratibiwa na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), kupitia atamizi za Dar Teknohama Business Incubator (DTBi) na Buni Innovation Hub.


Programu hiyo inalenga kuwasaidia kampuni changa, watafiti, wanafunzi wa vyuo vikuu, biashara ndogo na za kati pamoja na wajasiriamali kutambua, kulinda na kubiasharisha haki zao za miliki bunifu.


Mhando alisema katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji, programu hiyo inalenga kufanya uchambuzi wa kina wa mahitaji ya wabunifu 120 wa awali, ambao watasaidiwa kisheria na kifedha kulinda kazi zao na baadaye kuunganishwa na wawekezaji.



Alisema uteuzi wa wabunifu hao utazingatia vigezo mbalimbali, ikiwemo umuhimu wa ubunifu husika kwa jamii pamoja na uwezo wake wa kuzalisha faida.


Kwa mujibu wa Mhando, programu hiyo itawasaidia wabunifu kupitia hatua saba: utambuzi na uhamasishaji; mafunzo na warsha za vitendo; uchambuzi wa mahitaji; maandalizi ya ramani ya ulinzi; uwasilishaji wa maombi ya usajili; ubiasharishaji kwa kuwaunganisha na wawekezaji; pamoja na ufuatiliaji endelevu.


Aliwataka wabunifu na kampuni changa kutumia fursa hiyo mapema badala ya kusubiri hadi mgogoro wa umiliki unapotokea, mawazo yao yanaponakiliwa au mwekezaji anapohitaji uthibitisho wa kisheria kuhusu umiliki wa biashara.

 

Naye Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dkt. Amos Nungu, alisema miliki bunifu si suala la kisheria pekee, bali ni rasilimali muhimu ya kiuchumi inayoweza kuwa msingi wa kuvutia uwekezaji, utoaji wa leseni kwa viwanda vingine, uhamishaji wa teknolojia na ujenzi wa biashara zinazoweza kukua hadi masoko ya kimataifa.


“Changamoto yetu kuu kwa sasa nchini si ukosefu wa mawazo; ni kuhakikisha kuwa mawazo mazuri ya vijana, watafiti na wabunifu wetu yanalindwa kisheria, yanaendelezwa na hatimaye yanafikishwa sokoni,” alisema Dkt. Nungu.


Alisema mafanikio ya InnoIP hayatapimwa kwa idadi ya watu watakaohudhuria mafunzo na semina pekee, bali kwa matokeo, ikiwemo kuongezeka kwa idadi ya ubunifu unaolindwa kisheria, teknolojia mpya kuingia sokoni, biashara kukua, uwekezaji kuvutiwa na ajira mpya kuzalishwa.



Akizungumzia programu ya Fursa Women, Dkt. Nungu aliishukuru Airtel Tanzania kwa kushirikiana na COSTECH katika kufadhili programu hiyo.


Alisema ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja katika kujenga jamii yenye ujuzi wa kidijitali.


Alifafanua kuwa kupitia Fursa Women, wanawake watajengewa uelewa kuhusu matumizi sahihi na salama ya mifumo ya kidijitali katika kutangaza bidhaa, kuwafikia wateja, kufanya na kupokea malipo mtandaoni pamoja na kuhifadhi kumbukumbu za biashara zao.


Dkt. Nungu alitoa wito kwa wawekezaji na sekta binafsi kutambua kuwa ubunifu wa Kitanzania ni fursa ya uwekezaji ambayo bado haijatumika kikamilifu.


Aliwaalika kushirikiana na Serikali katika kujaribu, kununua na kupanua matumizi ya teknolojia pamoja na suluhisho mbalimbali zinazozalishwa na Watanzania.


Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanatarajiwa kufungwa Jumatatu na Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba.

KAMBARAGE VIJANA CHOIR YAANDAA TAMASHA LA UIMBAJI “NIMEBEBA USHUHUDA”

August 22, 2026 Add Comment


Mwenyekiti wa Kambarage Vijana Choir, Heri Ndaki, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tamasha la Uimbaji Mubashara ‘Nimebeba Ushuhuda’ linalotarajiwa kufanyika Oktoba 16, 2026 katika Kanisa la AIC Kambarage, Manispaa ya Shinyanga.
Mwenyekiti wa Kambarage Vijana Choir, Heri Ndaki, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tamasha la Uimbaji Mubashara ‘Nimebeba Ushuhuda’ linalotarajiwa kufanyika Oktoba 16, 2026 katika Kanisa la AIC Kambarage, Manispaa ya Shinyanga.

Na Elizabeth Cosmas - Shinyanga

Kwaya ya Vijana ya Kanisa la AIC Kambarage, maarufu kama Kambarage Vijana Choir (KVC), imeandaa Tamasha la Uimbaji Mubashara litakalobeba jina la “Nimebeba Ushuhuda”, huku likilenga kuunganisha waumini wa madhehebu mbalimbali na kuhamasisha jamii kudumisha amani, upendo na mshikamano.

MANYARA TANZANITE MARATHON YALENGA SH1.5 BILIONI KUOKOA WATOTO NJITI

Kajunason August 22, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu, Manyara

MBIO za hisani za Manyara Tanzanite Marathon 2026 zimefanyika leo katika Mji wa Babati, mkoani Manyara, huku waandaaji wakiwa na lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zilizoendeshwa chini ya kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti”, zimewakutanisha wananchi, wanariadha na wadau mbalimbali kutoka maeneo tofauti nchini, kwa lengo la kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto njiti.

Mgeni rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, amepongeza Mkoa wa Manyara kwa kuanzisha mbio hizo, akisema ni ubunifu unaolenga kushirikisha jamii katika kuchangia huduma za afya.

Sillo amesema Manyara Tanzanite Marathon ni mfano wa namna matukio ya michezo yanavyoweza kutumika katika kuhamasisha jamii na wadau kuchangia miradi yenye manufaa kwa wananchi, hususan katika sekta ya afya.

Amesema jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono na maeneo mengine nchini ili kuongeza ushiriki wa jamii katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.
MBIO za hisani za Manyara Tanzanite Marathon 2026 zimefanyika leo katika Mji wa Babati, mkoani Manyara, huku waandaaji wakiwa na lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum ya kuwahudumia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati.

Mbio hizo zilizoendeshwa chini ya kaulimbiu “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti”, zimewakutanisha wananchi, wanariadha na wadau mbalimbali kutoka maeneo tofauti nchini, kwa lengo la kuunga mkono juhudi za kuboresha huduma za afya kwa watoto wachanga na watoto njiti.

Mgeni rasmi kwa niaba ya Waziri Mkuu, Mhe. Mwigulu Nchemba, ambaye ni Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Daniel Sillo, amepongeza Mkoa wa Manyara kwa kuanzisha mbio hizo, akisema ni ubunifu unaolenga kushirikisha jamii katika kuchangia huduma za afya.

Sillo amesema Manyara Tanzanite Marathon ni mfano wa namna matukio ya michezo yanavyoweza kutumika katika kuhamasisha jamii na wadau kuchangia miradi yenye manufaa kwa wananchi, hususan katika sekta ya afya.
Amesema jitihada hizo zinapaswa kuungwa mkono na maeneo mengine nchini ili kuongeza ushiriki wa jamii katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Jafari Rajabu, amesema mbio hizo zina umuhimu mkubwa katika juhudi za kuokoa maisha ya watoto, huku akiwataka wananchi na wadau kuendelea kuunga mkono mipango inayolenga kuboresha huduma za afya.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewashukuru wadau walioshiriki katika maandalizi na utekelezaji wa mbio hizo, akisema ushirikiano wao umewezesha kufanikisha tukio hilo lenye lengo la kuchangisha fedha kwa ajili ya watoto wanaohitaji huduma maalumu za afya.
Sendiga amesema fedha zitakazopatikana kupitia mbio hizo zitaelekezwa katika kufanikisha ujenzi na uwezeshaji wa wodi maalum kwa ajili ya kuwahudumia watoto njiti, ambao huhitaji huduma za kitaalamu na vifaa maalumu tangu wanapozaliwa.

Baadhi ya washiriki wa mbio hizo wamesema walishiriki si kwa ajili ya mazoezi na afya zao pekee, bali pia kuchangia juhudi za kuokoa maisha ya watoto wachanga na watoto njiti.

Wamesema Manyara Tanzanite Marathon imewapa fursa ya kuunganisha michezo na shughuli za kijamii, huku wakitoa wito kwa wananchi wengine kushiriki katika matukio yenye malengo ya kuboresha afya na ustawi wa jamii.

Manyara Tanzanite Marathon 2026 imeweka lengo la kukusanya Sh1.5 bilioni, ikiwa ni sehemu ya kampeni ya “Hatua Moja, Okoa Maisha ya Mtoto Njiti” inayolenga kuongeza uwezo wa huduma za afya kwa watoto wanaozaliwa kabla ya wakati mkoani Manyara.

RAIS SAMIA AZINDUA RASMI KITUO CHA KUZALISHA UMEME CHA BWAWA LA JULIUS NYERERE

August 22, 2026 Add Comment



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amezindua rasmi Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Julius Nyerere (JNHPP) chenye uwezo wa kuzalisha megawati 2,115 leo, tarehe 22 Agosti 2026, katika eneo la mradi lililopo Rufiji, mkoani Pwani.


Viongozi mbalimbali wameungana na Rais Samia katika uzinduzi huo, akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi,Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba; Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Mhe. Moustafa Madbouly; Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi; pamoja na viongozi wengine.


Uzinduzi wa JNHPP ni kilele cha utekelezaji wa mradi mkubwa wa kimkakati uliotekelezwa kwa kutumia fedha za ndani za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mradi huo umegharimu takribani shilingi trilioni 7.452, sawa na dola za Marekani bilioni 3.35. Ujenzi wake ulianza Juni 2019 na kukamilika Machi 2025.


JNHPP imeongeza uwezo wa uzalishaji wa umeme nchini na kuimarisha usalama wa nishati. Kwa sasa, uwezo wa mitambo ya kuzalisha umeme nchini umefikia takribani megawati 4,075, ambapo JNHPP pekee inachangia zaidi ya nusu ya uwezo huo.