Bukombe, Geita
Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa uongozi wake mahiri na usimamizi mzuri wa sekta ya nishati, akisema utekelezaji wa miradi unaonyesha dhamira ya Serikali ya kutekeleza kwa vitendo maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo leo Agosti 3, 2026 wakati wa uzinduzi rasmi wa jengo jipya la Ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Bukombe.
“Kwa kweli nampongeza sana Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Deogratias Ndejembi, pamoja na wasaidizi wake kwa jinsi wanavyofanya kazi kwa weledi na kujituma katika kutekeleza maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Dkt. Biteko.
Aidha, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo zinazowezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuboresha huduma kwa wananchi nchini.
Amesema ujenzi wa jengo hilo ni ushahidi wa mafanikio ya Serikali katika kuimarisha utoaji wa huduma za umma na kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa TANESCO, jambo litakaloongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi wa Bukombe na maeneo jirani.
Dkt. Biteko amesisitiza kuwa pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika sekta ya nishati na miundombinu ya huduma za umma, ni wajibu wa kila mtumishi kulinda na kutunza mali za umma ili ziendelee kutoa huduma bora kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
“Tunzeni jengo letu jipya la TANESCO ili liendelee kutoa huduma bora kwa muda mrefu. Miundombinu hii imejengwa kwa gharama kubwa kwa manufaa ya wananchi, hivyo inahitaji kutunzwa na kulindwa wakati wote,” amesisitiza Dkt. Biteko.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Eng. Paskasi Muragili, amesema Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya nishati ili kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza upatikanaji wa umeme na kuchochea shughuli za kiuchumi pamoja na maendeleo ya jamii.
Naye Meneja wa TANESCO Wilaya ya Bukombe, Eng. Valerian Myula, amesema jengo hilo la kisasa limejengwa kwa fedha za ndani za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya shilingi milioni 285, ikiwa ni sehemu ya jitihada za shirika hilo za kuendelea kuboresha huduma za umeme na kuongeza ufanisi wa kuwahudumia wananchi.































.jpeg)


.jpeg)









