HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WANANCHI MSIHOFU KUTUMIA NISHATI YA UMEME KATIKA VYOMBO VYA USAFIRI-

June 20, 2026 Add Comment

 WANANCHI MSIHOFU KUTUMIA NISHATI YA UMEME KATIKA VYOMBO VYA USAFIRI -MD TWANGE



📌Asema TANESCO inajenga vituo vya kuchajia vyombo hivyo nchi nzima


📌Aeleza mpango wa kusambaza majiko sanifu ya umeme  takribani Mil 1


📌Awapongeza Wafanyakazi kwa ubunifu na jitihada za kuwahudumia wateja kwa ufanisi.


Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), Bw. Lazaro Twange, amewaondoa hofu wananchi kuhusu matumizi ya nishati ya umeme katika vyombo vya usafiri, akisema kuwa TANESCO imejipanga kujenga vituo vya kuchajia vyombo hivyo nchi nzima.


Mkurugenzi huyo amesema hayo Juni 19, 2026, alipotembelea banda la TANESCO katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, mkoani Dodoma.


Amesema shirika linatambua kuwa mahitaji ya umeme yanaendelea kuongezeka kutokana na kukua kwa shughuli za kiuchumi, hivyo jitihada zinaendelea kufanyika kuhakikisha umeme unawafikia wananchi kwa ubora na uhakika kwa matumizi mbalimbali ya kijamii na kiuchumi.

“TANESCO inafanya kazi kubwa ya kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia. Aidha, sasa tunashuhudia matumizi ya umeme katika vyombo vya usafiri. Sisi kama wazalishaji wa umeme tunaonesha njia kwa kuwa tuna vyombo vingi vya usafiri vinavyotumia umeme. Tumejipanga kujenga vituo vya kuchajia vyombo hivyo nchi nzima,” alifafanua Bw. Twange.


Bw. Twange pia amefafanua kuhusu mpango wa ukopeshaji wa majiko sanifu ya umeme kwa wananchi, unaowawezesha kulipa kidogo kidogo kupitia manunuzi ya Luku. Amesema kuwa, kwa kushirikiana na wadau , takribani majiko milioni 1 yatasambazwa katika kipindi cha miaka miwili hadi mitatu.



“Tunatumia mbinu mbalimbali kuwaelimisha wananchi na kuwaondoa hofu kuhusu matumizi ya  umeme  kupikia. Tunawakopesha majiko ya umeme  na wanalipa kidogo kidogo kupitia mfumo wa manunuzi ya Luku. Wadau kutoka sekta binafsi wametuunga mkono, na tunatarajia kusambaza majiko karibu milioni 1 katika kipindi cha miaka miwili hadi mitatu,” aliongeza Bw. Twange.


Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala, Bi. Beatrice Kimoleta, Licha ya kumpongeza Mkurugenzi Mtendaji kwa kutembelea Banda la TANESCO  kujionea namna wananchi wanavyohudumiwa, amesema Shirika linajivunia watendaji  wenye dhamira ya kuwahudumia wananchi kwa ubunifu na weledi mkubwa.


“Tunaomba wateja wetu muendelee kutuamini, Tunafahamu kuwa umeme ni huduma muhimu kwa kila Mtanzania, hivyo tunaendelea kuongeza jitihada za kutoa huduma bora, ya uhakika na yenye ufanisi zaidi, tunaimani na watumishi wetu katika kuhakikisha wananchi wananufaika na nishati ya umeme katika fursa mbalimbali ,” alisisitiza Bi. Kimoleta.


Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma Kitaifa kwa mwaka 2026 yanaendelea kufanyika katika Viwanja vya Chinangali, mkoani Dodoma, na yanatarajiwa kuhitimishwa rasmi  Juni 23, 2026.

WAZIRI KAPINGA AIPONGEZA TBS KWA KUIWEKA TANZANIA KWENYE RAMANI YA UBORA

WAZIRI KAPINGA AIPONGEZA TBS KWA KUIWEKA TANZANIA KWENYE RAMANI YA UBORA

June 20, 2026 Add Comment

Na.Alex Sonna-DODOMA

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limepongezwa kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi cha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, huku likitakiwa kuendelea kwenda sambamba na maendeleo ya teknolojia na mabadiliko ya soko la dunia ili kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania kimataifa.

Pongezi hizo zimetolewa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga,wakati wa maadhimisho ya kilele cha miaka 50 ya shirika hilo yaliyofanyika katika ofisi zake zilizopo Njedengwa jijini Dodoma, sambamba na uzinduzi wa kitabu kinachoelezea historia, mafanikio na mchango wa taasisi hiyo katika kukuza ubora wa bidhaa na huduma nchini.

Waziri Kapinga amesema TBS imekuwa nguzo muhimu katika kulinda afya na usalama wa wananchi kupitia usimamizi wa viwango vya bidhaa mbalimbali, huku ikichangia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa sekta za uzalishaji, biashara na viwanda nchini.

Ameeleza kuwa katika kipindi hiki ambacho dunia inaendelea kubadilika kwa kasi kupitia teknolojia na ubunifu, TBS inapaswa kuwa na dhana ya kujitegemea zaidi kwa kuimarisha mifumo ya kisasa ya utoaji huduma na kuongeza uwezo wake wa kitaalamu ili kukidhi mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi.

"Tunapoadhimisha miaka 50 ya TBS, tunashuhudia mchango mkubwa wa taasisi hii katika kujenga imani ya bidhaa za Tanzania. Hata hivyo, ni muhimu kuendelea kuwekeza katika teknolojia, ubunifu na ushirikiano na sekta binafsi ili kuhakikisha bidhaa zetu zinakidhi viwango vya kimataifa," amesema Kapinga.

Aidha, Waziri huyo amesisitiza umuhimu wa TBS kuendelea kufanya kazi kwa karibu na sekta binafsi ili kuongeza ubora wa bidhaa zinazozalishwa nchini na kusaidia kutafsiri kwa vitendo maono ya Tanzania ya kuwa taifa lenye uchumi wa viwanda unaozalisha bidhaa zenye ushindani mkubwa katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Dkt. Ashura Katunzi,amesema  maadhimisho hayo  ni fursa ya kutathmini mafanikio yaliyofikiwa na kuweka mikakati mipya ya kuifanya taasisi hiyo kuwa ya kisasa zaidi na yenye uwezo mkubwa wa kukabiliana na changamoto za karne ya 21.

Dkt. Katunzi amesema TBS itaendelea kuimarisha maabara za kisasa, kuongeza matumizi ya teknolojia za kidijitali na kuwekeza katika rasilimali watu ili kuhakikisha huduma za viwango zinakuwa bora zaidi, za haraka na zenye kuaminika.

"TBS inatambua kuwa dunia inabadilika kwa kasi kubwa, huku teknolojia na mazingira ya biashara vikibadilika, hivyo shirika hilo linapaswa kuendelea kuwa imara, bunifu na lenye uwezo wa kujibu changamoto mpya zinazoibuka."aamesema Dkt. Katunzi

Amebainisha kuwa kwa kipindi cha nusu karne, TBS imekuwa mhimili muhimu wa maendeleo ya viwanda na biashara nchini kwa kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa na kuuzwa zinazingatia viwango vinavyotakiwa, jambo ambalo limeongeza imani ya walaji na kufungua fursa za biashara katika masoko mbalimbali duniani.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo, Mariam Ditopile Mzuzuri, amesema TBS imekuwa mhimili muhimu katika kulinda maslahi ya walaji, kuimarisha ushindani wa bidhaa za Tanzania na kuchochea ukuaji wa sekta za uzalishaji nchini.

 Ditopile amesema ipo haja ya kufanyika kwa mapitio ya kina ya Sera ya Ubora wa Bidhaa ili iweze kuakisi mabadiliko makubwa yaliyotokea katika nyanja za sayansi, teknolojia, biashara na uzalishaji tangu sera hiyo ilipoanzishwa.

"Tunapoipongeza TBS kwa mafanikio ya miaka 50, ni muhimu pia kuangalia mbele na kufanya maboresho yatakayoiwezesha taasisi hii kuendelea kuwa nguzo ya maendeleo ya viwanda, biashara na kilimo katika mazingira ya sasa ya kiteknolojia," amesema Ditopile.

Ditopile amesema imejijengea rekodi ya kuwa taasisi muhimu katika kuhakikisha bidhaa zinazozalishwa, kuuzwa na kutumiwa nchini zinakidhi viwango vinavyotakiwa kwa ajili ya kulinda afya, usalama na maslahi ya watumiaji.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Viwango Afrika (ARSO), Dkt. Hermogene Nsengimana, amesema Julai 2026 Tanzania itakuwa nchi ya saba barani Afrika kupata Alama ya Ubora ya Afrika (Africa Quality Mark) kwenye bidhaa zake.

Amesema kwa hatua hiyo, Tanzania itaungana na Rwanda, Togo, Senegal, Ethiopia, Nigeria na Zimbabwe katika nchi zinazotumia alama hiyo ya ubora inayolenga kuimarisha viwango vya bidhaa barani Afrika.

Amesema Shirikisho la Viwango Afrika limekwisharatibu na kuoanisha takribani viwango 2,600 vinavyolenga sekta za kipaumbele ikiwemo usindikaji wa mazao ya kilimo, sekta ya magari, dawa na bidhaa za afya, usafirishaji na ugavi, pamoja na nguo na bidhaa za ngozi.

Ameeleza kuwa kwa sasa takribani bidhaa 500 katika ngazi ya Afrika zinapitiwa ili kupata Alama ya Ubora ya Afrika, hatua itakayosaidia kurahisisha biashara ndani ya Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA).

Amesema bidhaa za Tanzania ambazo kwa sasa zinabeba alama ya TBS, zitapata fursa ya kuwekewa alama ya ubora ya Afrika, jambo litakaloongeza ushindani na upatikanaji wa masoko katika nchi mbalimbali za bara hilo.

WAZIRI SANGU: SERIKALI INATHAMINI MCHANGO WA TAASISI ZA DINI KATIKA KUJENGA AMANI NA MAENDELEO YA TAIFA

June 19, 2026 Add Comment
SERIKALI imeendelea kuthamini mchango mkubwa unaotolewa na taasisi za kidini nchini katika kuimarisha amani, mshikamano na maendeleo ya taifa.

RAIS WA NAMIBIA AWASILI KWA ZIARA YA KITAIFA

June 19, 2026 Add Comment
Rais wa Jamhuri ya Namibia, Mhe. Dkt. Netumbo Nandi-Ndaitwah, amewasili nchini kwa Ziara ya Kitaifa ya siku tatu kuanzia tarehe 19 hadi 21 Juni 2026, kwa mwaliko wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

PPAA YAJIVUNIA MAFANIKO MODULI YA MALALAMIKO, RUFAA

June 19, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Mamlaka ya Rufani ya Zabuni za Umma (PPAA) imeendelea kujivunia mafanikio ya matumizi ya Moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa kieletroniki kupitia mfumo Mfumo wa Ununuzi wa Umma wa Tanzania (NeST).

Mafanikio hayo yamebainishwa na Katibu Mtendaji wa PPAA, Bw. James Sando alipotembelea banda la Mamlaka hiyo kwenye maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, Jijini Dodoma.

Bw. Sando amesema kuwa moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa ilianzishwa ili kutatua changamoto mbalimbali zilizokuwa zinajitokeza kwenye utatuzi wa migogoro kwenye michakato ya ununuzi wa umma.

“Changamoto tulizoziondoa kwa wazabuni na taasisi nunuzi ni pamoja kuokoa muda, gharama, uwazi na uwajibikaji pamoja na kumbukumbu sahihi za malalamiko na rufaa zinazowasilishwa na wazabuni,” amesema Bw. Sando.

Bw. Sando amebainisha kuwa ili PPAA iweze kufanya maamuzi kuhusu shauri lililowasilishwa kwa Mamlaka hiyo ni lazima kuwa na kumbukumbu sahihi za shauri hilo, hivyo kupitia moduli PPAA imeweza kupata nyaraka mbalimbali zinazohitajika kwa wakati. 

“moduli ya kupokea na kushughulikia malalamiko na rufaa imeziunganisha taasisi nunuzi na PPAA, faida zote hizi zimeletwa na moduli hii,” ameongeza Bw. Sando


“Kwa Mwaka wa fedha 2025/26 hadi sasa malalamiko takribani 157 yamewasilishwa kupitia moduli hiyo kwa taasisi nunuzi, na kati ya malalamiko hayo mashauri 37 yamewasilishwa PPAA na kutolewa uamuzi, hivyo matumizi ya moduli yanaendelea vyema,” ameongeza Bw. Sando

PPAA inampango wa kuunganisha sekta ya utoaji haki katika ununuzi wa umma na mfumo wa utoaji haki wa Mahakama ya Tanzania kwa mwaka wa fedha ujao ili kuongeza uwazi na uwajibikaji zaidi.

MADEREVA WANAOSAFIRISHA KEMIKALI WAZINGATIE MAFUNZO

June 19, 2026 Add Comment
NA Oscar Nkembo

Msimamizi wa Dawati la Ukaguzi wa Kemikali wa Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Ofisi ya Kanda ya Kati, Suitbert Sinduhije amesema Mamlaka imedhibiti Kemikali ya Sulphur iliyomwagika eneo la Mikumi na amewataka Madereva kuzingatia mafunzo wanayopata huku akiwasihi Wananchi kutoa taarifa kwa Mamlaka pindi ajali za Kemikali zinapotokea.

NEMC YACHOCHEA UWAJIBIKAJI JUMUISHI: SEKTA YA MAZINGIRA

June 19, 2026 Add Comment
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) linaendelea kuhimiza ushiriki wa wadau mbalimbali katika uhifadhi na usimamizi wa mazingira, likieleza kuwa mafanikio katika sekta hiyo yanategemea ushirikiano wa wananchi, taasisi za umma, sekta binafsi na washirika wa maendeleo.

DC NGUBIAGAI AONGOZA VITA DHIDI YA UVUVI HARAMU UKEREWE

June 19, 2026 Add Comment

  

Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe Cde. Christopher Ngubiagai akihutubia wananchi wa Gana katika mkutano
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe Ndg. Vicent Mbua akizungumza na wananchi wa Gana kuachana na uvuvi haramu

Na Mwandishi Wetu - Ukerewe

Mikakati ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ya kuimarisha usimamizi wa rasilimali za taifa na kuhakikisha sekta ya uvuvi inachangia kikamilifu ukuaji wa uchumi inaendelea kuzaa matunda, ambapo Wilaya ya Ukerewe imeendelea kuchukua hatua madhubuti dhidi ya uvuvi haramu.

WALIPAKODI MCHIKICHINI WAPONGEZWA KWA MCHANGO WAO KATIKA MIAKA 30 YA MAFANIKIO YA TRA

June 19, 2026 Add Comment
Kariakoo, 18 Juni, 2026

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kikodi Kariakoo imewapongeza walipakodi wa eneo la Mchikichini kwa mchango wao mkubwa ambao umekuwa sehemu muhimu ya mafanikio ya Mamlaka, katika kipindi cha miaka 30 tangu kuanzishwa kwake.

WAAJIRI WANAOZINGATIA SHERIA ZA KAZI WAPONGEZWA

June 18, 2026 Add Comment
Na OWM-KAM, Mwanza

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano), Mhe. Deus Sangu, amepongeza waajiri nchini wanaotekeleza wajibu wao kwa kuzingatia sheria za kazi, ikiwemo kuwasilisha michango ya wafanyakazi katika Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) kwa lengo la kulinda maslahi ya wafanyakazi dhidi ya madhara yanayotokana na kazi.
MKURUGENZI WA UCHAGUZI APONGEZA UFANISI NA UWAZI WA MFUMO WA UAGIZAJI MAFUTA KWA PAMOJA

MKURUGENZI WA UCHAGUZI APONGEZA UFANISI NA UWAZI WA MFUMO WA UAGIZAJI MAFUTA KWA PAMOJA

June 18, 2026 Add Comment
 

Na Mwandishi Wetu

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Bw. Ramadhan Kailima, amepongeza ufanisi na uwazi wa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unaosimamiwa na Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja, akieleza kuwa mfumo huo umechangia kuimarisha ukusanyaji wa mapato ya Serikali na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Bw. Kailima alitoa pongezi hizo Juni 18, 2026 alipotembelea banda la PBPA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Akizungumza baada ya kupata maelezo kuhusu utekelezaji wa mfumo huo, alisema kuwa umejengwa katika misingi ya uwazi na ushindani, jambo linalosaidia kupunguza gharama za uagizaji wa mafuta na kuongeza ufanisi katika usimamizi wa sekta hiyo muhimu kwa uchumi wa nchi.

Akitoa ufafanuzi kwa mgeni huyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Mwitazy, alisema kuwa katika mfumo wa uagizaji mafuta kwa pamoja, ushindani hujikita katika gharama za usafirishaji wa mafuta (Premium).

Alieleza kuwa wazabuni hushindanishwa kwa kuwasilisha bei za usafirishaji wa bidhaa za petroli, dizeli na mafuta ya taa, ambapo mzabuni mwenye gharama nafuu zaidi hupatiwa zabuni husika.

“Utaratibu huu umetuwezesha kuhakikisha upatikanaji wa mafuta ya kutosha nchini wakati wote na wakati huohuo kuipa Serikali taarifa sahihi za kiasi cha mafuta na hivyo kuwezesha ukusanyaji wa mapato yatokanayo na biashara ya mafuta,” alisema.

Aliongeza kuwa mikataba ya uagizaji wa mafuta husainiwa mapema kabla ya bidhaa kuwasili nchini, jambo linaloiwezesha Serikali kufanya makadirio sahihi ya mapato yatokanayo na sekta hiyo.

Kwa mujibu wa Mwitazy, mafanikio ya mfumo huo yameifanya PBPA kuwa kitovu cha huduma za uagizaji mafuta kwa nchi kadhaa za ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, zikiwemo Malawi, Rwanda, Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambazo huleta mahitaji yao kupitia mfumo wa uagizaji wa mafuta kwa pamoja.

Ziara ya Bw. Kailima katika banda la PBPA ni sehemu ya shughuli za Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayolenga kuonesha mafanikio, huduma na ubunifu unaotekelezwa na taasisi za umma katika kuwahudumia wananchi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Wananchi Dodoma Wajifunza Haki Zao Kupitia Elimu ya Vipimo Sahihi

Kajunason June 18, 2026 Add Comment

 Na Mwandishi Wetu, Dodoma


Wananchi waliotembelea banda la Wakala wa Vipimo (WMA) katika Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park, Dodoma, wameeleza kufurahishwa na elimu wanayoipata kuhusu matumizi sahihi ya vipimo na kuahidi kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuhakiki vipimo katika shughuli za kila siku.

Siku ya tatu ya maonesho hayo yaliyofunguliwa Juni 16 na yanayotarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026, banda la WMA limeendelea kuvutia idadi kubwa ya wananchi wanaotaka kujifunza namna Serikali inavyohakikisha vipimo vinavyotumika katika biashara na huduma mbalimbali vinakuwa sahihi na vya kuaminika.

Mmoja wa wananchi hao, Bw. Bilson Vedastus, alisema elimu aliyopata imemsaidia kuelewa mambo muhimu ya kuzingatia anaponunua mafuta, gesi ya kupikia na bidhaa nyingine zinazopimwa.

“Awali sikuwa naelewa mambo haya kwa kina, lakini sasa najua ninachopaswa kuangalia ninapojaza mafuta, kununua sukari au gesi ya kupikia,” alisema.

Kwa upande wake, Bi. Asha Siyaya alisema elimu hiyo imewapa uwezo wa kutambua udanganyifu unaoweza kufanywa kupitia vipimo visivyo sahihi na kuahidi kutoa taarifa pale watakapobaini ukiukwaji.

“Tumeona jinsi pampu za mafuta, mizani na vifaa vingine vinavyohakikiwa ili kuhakikisha vinapima kwa usahihi. Hatuwezi kukaa kimya tukiona mteja anadhulumiwa. Tutawaeleza wengine na kuripoti udanganyifu popote tutakapouona,” alisema.

Wataalamu wa WMA, Albogast Kajungu, Mbwana Amani na Said Ibrahim, waliwaeleza wananchi kuwa huduma za uhakiki wa vipimo zinagusa sekta nyingi zinazohusiana moja kwa moja na maisha ya kila siku ya wananchi.

Walifafanua kuwa pampu za mafuta huhakikiwa na kuwekewa alama za uthibitisho, huku mizani inayotumika sokoni na madukani kupimia bidhaa mbalimbali ikikaguliwa mara kwa mara ili kuhakikisha watumiaji wanapata kiwango stahiki cha bidhaa wanazonunua.

Aidha, mita za maji na umeme zinazotumika majumbani na katika biashara huhakikiwa ili kuhakikisha wateja wanalipia matumizi halisi, huku mitungi ya gesi ya kupikia, bidhaa zilizofungashwa pamoja na mizani za kupimia uzito wa magari barabarani nazo zikiendelea kufanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara.

Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja Mawasiliano wa Wakala wa Vipimo, Bi. Veronica Simba, alisema lengo la WMA ni kuhakikisha kila mwananchi anapata thamani halisi ya fedha anayolipia bidhaa na huduma mbalimbali.

Alitoa wito kwa wananchi kuendelea kutembelea banda la WMA katika maonesho hayo ili kupata elimu zaidi kuhusu haki zao na umuhimu wa matumizi ya vipimo sahihi katika shughuli za kijamii na kiuchumi.