HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WAZIRI MAVUNDE AELEKEZA USIMAMIZI THABITI WA SHERIA ILI ASILIMIA 90 YA BIDHAA NA HUDUMA MIGODINI KUFANYWA NA WATANZANIA

July 22, 2026 Add Comment
-Ampongeza Rais Samia kwa kuwa kinara wa ushirikishwaji wa Watanzania migodini

TEA NA UNICEF WATEKELEZA MRADI WA ZAIDI YA SHILINGI BILIONI 1 WA UJENZI WA VITUO 10 VYA ELIMU YA AWALI YA UFUNDI

July 22, 2026 Add Comment
Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), kwa kushirikiana na UNICEF, inaendelea kutekeleza mradi wa ujenzi wa vituo 10 vya Elimu ya Awali ya Ufundi (IPOSA) wenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni moja, kwa lengo la kuwapatia fursa ya mafunzo ya ufundi vijana waliokosa kunufaika na elimu ya msingi kutokana na sababu mbalimbali.

Mradi huo unatekelezwa katika mikoa ya Dodoma, Tabora, Dar es Salaam, Kigoma na Songwe. Kwa sasa, ujenzi unaendelea vizuri na umefikia hatua ya maboma katika maeneo yote ya utekelezaji.

Katika kufuatilia maendeleo ya mradi huo, kuanzia Julai 20 hadi 21, 2026, timu ya wataalamu kutoka UNICEF ikiongozwa na Mhandisi Mohamed Hindi pamoja na Afisa Elimu Bi. Jennifer Mberesero, ilifanya ziara ya ukaguzi katika miradi inayotekelezwa mkoani Dodoma. Baada ya ukaguzi huo, timu hiyo ilifanya kikao kazi na wataalamu wa TEA wanaosimamia utekelezaji wa mradi.

Lengo la kikao hicho lilikuwa kujadili hatua zilizofikiwa, kutathmini maendeleo ya utekelezaji na kuimarisha ushirikiano kati ya pande hizo mbili ili kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotarajiwa.

Aidha, ujumbe huo ulikutana na Mkurugenzi Mkuu wa TEA Dkt. Erasmus Kipesha na kumpa taarifa kuhusu maendeleo ya mradi.

Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, Mkurugenzi Mkuu Dkt. Kipesha aliwashukuru wataalamu wa TEA na UNICEF kwa usimamizi mzuri wa mradi na kuwataka kuendelea kushirikiana kwa karibu ili kuhakikisha malengo yaliyowekwa yanafikiwa ndani ya muda uliopangwa.

WAZIRI NDEJEMBI ATOA ONYO KWA MKANDARASI ANAYETEKELEZA MRADI WA SONGEA–TUNDURU–MASASI

July 22, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu - Tunduru, Ruvuma


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameonesha kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Masasi kupitia Tunduru na kuagiza mkandarasi kuongeza juhudi ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya mradi huo leo Julai 22, 2026, Mhe. Ndejembi amesema Serikali haitakuwa tayari kuona miradi ya kimkakati inayogusa maisha ya wananchi ikicheleweshwa bila sababu za msingi.


Amesema mradi huo ni miongoni mwa miradi muhimu ya Sekta ya Nishati inayopewa kipaumbele na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutokana na mchango wake katika kuimarisha upatikanaji wa umeme na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika ukanda wa Kusini.


“Maendeleo ya mradi huu hayaridhishi ukilinganisha na muda uliopita tangu utekelezaji wake uanze. Serikali inatarajia kuona kasi kubwa zaidi ya utekelezaji katika kipindi kilichobaki. Nimemuagiza Katibu Mkuu kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo haya na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa iwapo hakutakuwa na maboresho yanayoonekana,” amesema Mhe. Ndejembi.


Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Nyasa, Mhe. Boniface Magiri, aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, amesema Mkoa utaendelea kushirikiana na Serikali Kuu katika kufuatilia utekelezaji wa mradi huo ili kuhakikisha unakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati.


Naye Mhe. Sikudhani Chikambo kwa niaba ya wabunge wa Mkoa wa Ruvuma, viongozi hao wameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwekeza katika miundombinu ya umeme ambayo itachochea ukuaji wa uchumi, uwekezaji na kuboresha huduma za kijamii katika maeneo ya Kusini mwa Tanzania.


Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea kupitia Tunduru hadi Masasi unatekelezwa na Mkandarasi Kalpataru Power kutoka India. Mradi huo unatarajiwa kuiunganisha Mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye Gridi ya Taifa pamoja na kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Wilaya ya Tunduru na maeneo jirani.



HUKUMU YA TIKTOKER GHANA -SOMO KWA UHURU WA KUJIELEZA NA WAJIBU WA WATUMIAJI WA MITANDAO

July 22, 2026 Add Comment

 


Hivi karibuni, Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Accra ilimuhukumu Camilla Alhassan, mshawishi maarufu wa TikTok (Tiktoker), kifungo cha mwaka mmoja jerezani. Adhabu hii ilitolewa baada ya mshtakiwa kukiri makosa ya kusambaza taarifa za uongo na kufanya tabia ya kuudhi (offensive conduct) dhidi ya Rais John Dramani Mahama. 


Kesi hii inaashiria hatua kubwa katika udhibiti wa maudhui ya kidijitali barani Afrika na inaibua maswali muhimu kuhusu mipaka ya uhuru wa kujieleza na wajibu wa kisheria wa watumiaji wa mitandao ya kijamii.


Hukumu dhidi ya Alhassan inasimama juu ya *misingi miwili mikuu* ya kisheria inayolenga kulinda usalama wa jamii na sifa za watu


Mosi, Kusambaza Taarifa za Uongo (False News) -  Sheria za Ghana zinakataza utengenezaji au usambazaji wa taarifa ambazo mtengenezaji anajua au ana sababu ya kuamini kuwa ni za uongo, hususan kama zinaweza kusababisha hofu au taharuki miongoni mwa jamii. 


Pili, Tabia ya Kuudhi (Offensive Conduct) - Matumizi ya lugha au madai yanayolenga kudhalilisha, kuchochea chuki, au kuhatarisha amani ya umma—katika muktadha huu, kumhusisha kiongozi wa nchi na matendo ya ushirikina na kafara ya wanyama kwa malengo ya kisiasa.


Sakata hili linaangazia athari kubwa za mitandao ya kijamii katika nyanja za siasa na utulivu wa kijamii:-


*Mmomonyoko wa Imani ya Kisiasa:* Kudai kuwa Rais alifanya matambiko kwa kuzika ng'ombe 32 nchi nzima kulilenga kuchafua sifa yake na kupunguza uaminifu wake mbele ya wapiga kura, jambo linaloweza kuathiri mchakato wa kidemokrasia.


*Silaha ya Algorithm na Ushawishi:* Kama "Tiktoker," Alhassan alitumia nguvu ya ushawishi wake (clout) kupata watazamaji wengi. Katika zama za kidijitali, taarifa za kusisimua na za uzushi husambaa haraka kuliko ukweli, jambo linalofanya madhara yake kuwa makubwa na ya haraka.


*MAANA YA HUKUMU HII KWA MUSTAKABALI WA KIDIJITALI  (IMPLICATIONS)*


Uamuzi wa Jaji kukataa ombi la mawakili wa Alhassan la kupunguza adhabu una ujumbe mzito


Mahakama imeweka wazi kuwa umaarufu wa mtandaoni (social media fame) sio ngao dhidi ya sheria. Kifungo hiki kinatumika kama onyo kwa waundaji wengine wa maudhui (content creators) kuwa uhuru wa kujieleza unaambatana na wajibu.


Aidha, Kesi hii inaongeza msukumo kwa serikali za Kiafrika kuimarisha mifumo ya kufuatilia na kuchukua hatua dhidi ya uhalifu wa kimtandao (cybercrime).


*USHAURI WANGU*


Hukumu ya Camilla Alhassan ni kielelezo cha namna mifumo ya sheria inavyolazimika kubadilika ili kukabiliana na changamoto mpya zinazoletwa na teknolojia. 


Wakati mitandao ya kijamii ikiendelea kuwa jukwaa kuu la mijadala ya umma, kesi hii inakumbusha jamii kuwa maneno yana madhara ya kisheria, na kwamba ulimwengu wa kidijitali unapaswa kuongozwa na ukweli, maadili, na heshima kwa utu wa wengine.


Kama Tanzania Tuna paswa kuchukua hatua za wazi kwa wahalifu wa mitandao na kama nilivyo shauri mara zote tunaweza kupitia hatua tatu ili tuweze kukuza uelewa kwa wananchi na hatimae watakao kaidi zaidi tuwawajibishe kwa mujibu wa sheria za nchi


*Hatua ya Kwanza :* Wahalifu wakwamatwe na kwa uwazi watangazwe na kuonywa kisha waachiwe - Hii itakua somo kwa wengine ambao wana kawaida ya kufata mkumbo kwenye kutenda uhalifu wa kimtandao na wakidhani serikali imelala


*Hatua Ya Pili:* Mhalifu anapo rudia akamatwe tena kwa uwazi na kulipishwa faini kwa mujibu wa sheria zetu - Pesa zitakazo patikana kwneye hili ziwekwe kwenye mfuko maalum utakao saidia kuimarisha udhibiti wa uhalifu mtandao kupitia elimu ya uelewa na nyezo nyingine za udhibiti


*Hatua ya tatu:* Mhalifu anapo rudia mara ya tatu kunakua hakuna tena namna ila ni kufungwa kwa mujibu wa sheria za nchi yetu na hili liwe somo kwa wengine wote.


Naomba kuwasilisha.


*Yusuph Kileo ,*

Mtaalam wa usalama mtandao na Uchunguzio wa makosa ya Kidigitali

Dar Es Salaam, Tnazania

19 - July - 2026.

CCM YATHIBITISHA MSINGI WA KUHUDUMIA WANANCHI KWA VYAMA TAWALA AFRIKA

July 22, 2026 Add Comment

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Mambo ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI), Ndugu Rabia Abdalla Hamid , ameshiriki Mkutano Mkuu wa Chama cha Botswana National Front (BNF) unaofanyika mjini Jwaneng, Botswana, akiwakilisha Chama Cha Mapinduzi.


Akizungumza katika mkutano huo, Ndugu Rabia amesisitiza kuwa kila chama tawala kina wajibu wa kuwatumikia wananchi kwa uadilifu, kuimarisha misingi ya utawala bora, na kuendelea kutoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wananchi bila kuchoka.


Aidha, amekisii Chama cha BNF kuendelea kuzingatia maslahi ya wananchi katika utekelezaji wa sera na maamuzi yake, pamoja na kuhakikisha kuwa hakuna mwananchi anayebaki nyuma katika mchakato wa maendeleo ya taifa.

Aidha,Ndg. Rabia amempongeza Rais wa Chama cha Botswana National Front (BNF) na Rais wa Jamhuri ya Botswana, Mheshimiwa Duma Gideon Boko kwa  ushindi wa Chama chake na kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Jamhuri ya Botswana. 


Ameeleza kuwa kuchaguliwa kwa Rais Boko na Chama cha BNF ni kielelezo cha imani waliyopewa na wananchi wa Botswana na  amewatakia mafanikio katika kuwaletea maendeleo  na ustawi wao.

DC NYAMWESE AWATAKA WAKURUGENZI KUSIMAMIA FEDHA ZA SERIKALI KWA UADILIFU

July 22, 2026 Add Comment

 



Na Oscar Assenga, Tanga


Mwakilishi wa Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Salum Nyamwese, amewataka wakurugenzi wa halmashauri kuhakikisha kila fedha inayotolewa na Serikali kwa ajili ya miradi ya maendeleo inasimamiwa kwa uadilifu na kutumika kulingana na malengo yaliyokusudiwa.

Nyamwese ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Handeni amesema matumizi mabaya ya fedha za umma, rushwa na ubadhirifu vinaweza kuwa kikwazo kikubwa katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050.
Alitoa kauli hiyo mjini Tanga wakati akifungua  warsha ya wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ya maendeleo mkoa wa Tanga iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), iliyowakutanisha wakurugenzi wa halmashauri, wakuu wa taasisi za umma na viongozi mbalimbali kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha uwajibikaji na usimamizi wa rasilimali za umma.

Nyamwese alisema fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi, hivyo viongozi wenye dhamana wanapaswa kuhakikisha kila shilingi inatumika kwa ufanisi na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.
“Fedha zinazotolewa na Serikali ni mali ya wananchi hivyo ni wajibu wa kila mkurugenzi kuhakikisha hakuna hata shilingi moja inayopotea au kutumika nje ya malengo yaliyokusudiwa. Tunapaswa kusimamia miradi kwa uadilifu na kuhakikisha wananchi wanaona thamani ya fedha zinazotolewa,” alisema.

Alisema warsha hiyo imefanyika wakati muafaka ambapo Serikali imeanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kujenga uchumi shindani, taasisi imara, uwajibikaji na matumizi yenye tija ya rasilimali za umma.
Kwa mujibu wa Nyamwese, utekelezaji wa dira hiyo hauwezi kufanikiwa iwapo viongozi hawataweka mbele maslahi ya wananchi na kupambana kikamilifu na vitendo vya rushwa, ubadhirifu na ukiukwaji wa taratibu.

“Rushwa ni adui mkubwa wa maendeleo kwani huhujumu matumizi sahihi ya rasilimali za umma, hudhoofisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, hupunguza ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi na kuondoa imani ya wananchi kwa taasisi za Serikali,” alisema.

Aliwataka wakurugenzi kushirikiana kwa karibu na Takukuru katika kuimarisha mifumo ya udhibiti wa ndani, kuongeza uwazi katika matumizi ya fedha za umma na kuchukua hatua mapema dhidi ya viashiria vya ubadhirifu.
Nyamwese alisema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuelekeza uwekezaji mkubwa katika Mkoa wa Tanga kwa lengo la kuboresha huduma za kijamii na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Alieleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2025/2026, Mkoa wa Tanga umepokea zaidi ya Sh trilioni 3 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali katika sekta za elimu, afya, maji, kilimo, mifugo, uvuvi, biashara, uwekezaji, miundombinu ya barabara, nishati, ardhi na uwezeshaji wananchi kiuchumi.
Hata hivyo, alisema kiasi hicho kikubwa cha fedha hakitakuwa na maana bila kuwepo kwa usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia miradi hiyo.

“Fedha pekee hazileti maendeleo. Kinacholeta maendeleo ni usimamizi mzuri, ufuatiliaji wa karibu na uwajibikaji wa viongozi wanaosimamia utekelezaji wa miradi,” alisisitiza.
Aliwataka wakurugenzi kufanya tathmini za mara kwa mara za miradi inayotekelezwa katika maeneo yao, kuhakikisha kazi zinafanyika kwa viwango vinavyotakiwa na kuchukua hatua dhidi ya watumishi au wakandarasi watakaobainika kukiuka sheria.
Akizungumzia fursa za maendeleo zilizopo mkoani Tanga, Nyamwese alisema mkoa huo unatarajiwa kuwa kitovu kikubwa cha biashara na uwekezaji kutokana na utekelezaji wa miradi ya kimkakati, ikiwemo uboreshaji wa Bandari ya Tanga, reli ya kisasa (SGR) pamoja na Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).

Alisema miradi hiyo itaongeza shughuli za kiuchumi na kuvutia wawekezaji wengi zaidi, hivyo viongozi wa halmashauri wanapaswa kuhakikisha mazingira ya uwazi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali yanaendelea kuimarishwa.
Awali, akizungumza katika warsha hiyo, Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa ( TAKUKURU) Ramadhan Ndwatah alisema taasisi hiyo imefanya tathmini ya miradi inayotekelezwa ndani ya Mkoa wa Tanga na kubaini baadhi ya changamoto zinazotokana na usimamizi usioridhisha.

Alisema changamoto hizo ni pamoja na ucheleweshwaji wa miradi, matumizi yasiyo sahihi ya fedha, ongezeko la gharama zisizo za lazima na kupungua kwa manufaa yaliyotarajiwa kwa wananchi.

“Licha ya mafanikio yaliyopatikana kwenye miradi ya maendeleo, bado kuna changamoto ya udhaifu katika utekelezaji wa miradi, ucheleweshwaji wa miradi kwabaadhi ya wadau wenye dhamana, kuongeza gharama zisizo za lazima na kupunguza manufaa yanayotarajiwa kwa wananchi,” alisema.

Alisema kutokana na changamoto hizo, wameona ni muhimu kukutana na wadau wa usimamizi na utekelezaji wa miradi ili kuwakumbusha wajibu wao katika kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa ufanisi.
Aliwataka wadau wote wenye dhamana ya kusimamia miradi kushirikiana na TAKUKURU ili kutimiza azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo kupitia miradi mbalimbali.

Mkurugenzi Tanga Jiji atoa ushauri kuhusu BOQ

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga, Mhandisi Juma Hamsini, aliiomba Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI kuzingatia thamani halisi ya vifaa vinavyotumika wakati wa kuandaa BOQ za miradi mbalimbali ya ujenzi, ikiwemo madarasa.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha gharama zinazowekwa kwenye miradi zinaendana na hali halisi ya soko na kusaidia utekelezaji wa miradi yenye ubora na thamani kwa wananchi.



TANZANIA MGENI RASMI MAONESHO YA UFUGAJI NYUKI AFRIKA NCHINI ALGERIA

July 21, 2026 Add Comment

  



Balozi wa Tanzania nchini Algeria, Mhe Mobhare Matinyi, akizungumza na vyombo vya habari vya Algeria wakati akitangaza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekubali mwaliko wa kuwa mgeni rasmi katika Maonesho ya Ufugaji wa Nyuki barani Afrika (Africa Bee Expo) yatakayofunguliwa jijini Algiers mnamo Septemba 3, 2026.

WAZIRI SANGU: BONDE LA ZIWA RUKWA NI HAZINA YA AJIRA KWA VIJANA

July 21, 2026 Add Comment
Mbunge wa Jimbo la Kwela ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu akipata Maelezo kutoka kwa msimamizi wa mradi wa ujenzi wa madarasa Noble Helium ambayo Inafanya shughuli za utafiti na uchimbaji wa gesi ya helium Christian Temba (20 Julai 2026) alipokuwa akikagua miradi ya Maendeleo katika Kijiji cha Kinambo Kata ya Milepa Wilaya ya Sumbawanga.

NEWALA KUNUFAIKA NA UMEME WA UHAKIKA

July 21, 2026 Add Comment



📌*Ni baada ya kukamilika kwa njia ya kusafirisha umeme ya kilovoti 33 Masasi - Mtwara*


📌*Mradi umeimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi wa Wilaya ya Newala na maeneo jirani.*


📌*MD Twange asema thamani ya mradi ni takribani shilingi bilioni 4.65*



📍Newala, Mtwara | Julai 22, 2026


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amezindua rasmi mradi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 33 kutoka Masasi hadi Newala, akieleza kuwa mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa wananchi na kuweka mazingira wezeshi kwa ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Wilaya ya Newala.


Akizungumza wakati wa uzinduzi wa njia hiyo, Mhe. Ndejembi amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaendelea kuwekeza katika miradi ya kimkakati ya umeme ili kuhakikisha huduma ya nishati inawafikia wananchi wengi zaidi na kuwa chachu ya maendeleo.

"Njia hii ya umeme ni msingi wa kukuza uchumi, kuongeza uzalishaji, kuvutia uwekezaji na kuboresha upatikanaji wa umeme kwa Wilaya ya Newala," amesema Mhe. Ndejembi.


Aidha, Waziri Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuhakikisha Mikoa ya Lindi na Mtwara inapata umeme wa uhakika ikiwa ni pamoja na kuiunganisha Mikoa hiyo na umeme wa gridi ya Taifa.

Akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Mkuu wa Wilaya ya Newala, Mhe. Mwangi Kundya amesema miradi mbalimbali imeendelea kutekelezwa Mkoa wa Mtwara.


"Mheshimiwa Waziri niipongeze Serikali kwani Vijiji vyote vya Mkoa wa Mtwara 785 vinapata huduma ya umeme". Amesema Mhe. Mwangi.



Ameongeza kuwa katika kuboresha huduma kwa wateja mkoa wa Mtwara umepokea vitendea kazi yakiwemo magari kumi na moja, bajaji nne na pikipiki tisa.

Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba amesema Serikali imekuwa ikiboresha uwekezaji na upatikanaji wa umeme Mikoa ya  Mtwara na Lindi.


"Mahitaji ya Lindi na Mtwara yameendelea kuongezeka na Serikali imewekeza kwenye uzalishaji na hivi sasa Mkoa wa Mtwara tunazalisha zaidi ya megawati 50". Amesema Mha. Mramba.

Awali akitoa taarifa za utekelezaji wa mradi Mkurugenzi Mtendaji TANESCO, Bw. Lazaro Twange amesema ujenzi wa njia hiyo umetekelezwa kwa shilingi bilioni 4.56 kwa umbali wa Kilometa 76 kutoka Masasi hadi Newala.

"Mheshimiwa mgeni rasmi kabla ya mradi huu kutekelezwa Wilaya ya Newala ilikuwa ikipata umeme kutokea Mtwara kupitia Nanyumbu umbali wa kilometa 170, hali iliyochangia tatizo la kukatika kwa umeme mara kwa mara". Amesema Bw. Twange.



Ameongeza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa njia hiyo ya umeme kumeimarisha upatikanaji wa umeme na kuondoa changamoto ya kukatika kwa umeme kwa Wilaya hiyo.



Aidha, Serikali kupitia TANESCO imetenga takribani shilingi bilioni 5.27 kwa ajili ya kujenga kituo cha kubadilishia umeme (Switching Station) kitakacho saidia kuboresha upatikanaji wa umeme na kukidhi mahitaji ya sasa na ya badaye ya wananchi na wawekezaji wa Wilaya ya Newala. 


Mbunge wa Newala Vijijini Dkt. Yahaya Nawanda kwa niaba ya Wabunge wa Mkoa wa Mtwara ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuimarisha upatikanaji wa umeme Mkoa wa Mtwara.