
WANDONDI, WANDWEWE WATOA WITO WA KULINDA MAISHA NA AMANI
habari
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI

KAHAMA, SHINYANGA
Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Serikali inaandaa mradi maalumu wa kusambaza umeme katika maeneo ya uzalishaji, hususan maeneo yenye shughuli za uchimbaji wa madini, kwa lengo la kuwawezesha wazalishaji kutumia nishati ya uhakika na kupunguza utegemezi wa dizeli.
Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Msalala, Mhe. Mabula Magangila, aliyeomba Serikali kupeleka umeme katika maeneo ya uzalishaji, akieleza kuwa baadhi ya wachimbaji madini katika jimbo hilo bado wanatumia dizeli kuendesha shughuli zao za uzalishaji.
Mbunge huyo pia ameieleza Serikali kuwa vitongoji 98 katika Jimbo la Msalala bado havijaunganishwa na huduma ya umeme.
Akijibu hoja hiyo, Mhe. Ndejembi amesema Serikali tayari imeanza maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo maalumu kwa kushirikiana na Wizara ya Madini, ambao utalenga kusogeza huduma ya umeme moja kwa moja kwenye maeneo yenye shughuli za uzalishaji, hususan maeneo ya migodi.
Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza tija katika uzalishaji, kupunguza gharama zinazotokana na matumizi ya dizeli pamoja na kuwawezesha wachimbaji na wazalishaji kutumia nishati ya umeme iliyo nafuu, ya uhakika na endelevu.
Kuhusu upatikanaji wa umeme vijijini katika Jimbo la Msalala, Mhe. Ndejembi amesema vijiji vyote tayari vimefikiwa na huduma ya umeme, huku Serikali ikiendelea na jitihada za kuwafikishia huduma hiyo wananchi waliopo katika vitongoji ambavyo bado havijaunganishwa, ikiwemo vitongoji 98 vilivyotajwa.
Aidha, akizungumzia upatikanaji wa umeme katika Jimbo la Kahama Mjini, Mhe. Ndejembi amesema tayari amefanya mazungumzo na Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. Benjamini Ngaiwa, kwa lengo la kubainisha maeneo yaliyopo ndani ya Manispaa ya Kahama ambayo, licha ya kuwa ndani ya eneo la mjini, yana sifa na taswira za maeneo ya vijijini.
Amesema maeneo hayo yataangaliwa ili yaweze kunufaika na utaratibu wa Serikali wa kuunganishiwa umeme kwa gharama ya Shilingi 27,000 kwa mteja, kama ilivyoelekezwa.
Mhe. Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuweka kipaumbele katika upanuzi wa miundombinu ya umeme na kuhakikisha nishati inafika katika maeneo yenye shughuli za kiuchumi na uzalishaji, ili kuongeza tija, kuchochea uwekezaji na kuboresha maisha ya wananchi.






Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) imeibuka kinara miongoni mwa Taasisi za Elimu katika Maonesho ya 33 ya Kilimo, Mifugo na Sherehe za Nanenane Kanda ya Kaskazini yaliyofanyika katika Viwanja vya Themi Njiro, Arusha.
Akizungumzia ushindi huo, Prof. Maulilio Kipanyula, Makamu Mkuu wa NM-AIST, amesema bidhaa bora zinahitaji utafiti na NM-AIST kama Taasisi inayotanguliza ubunifu, imeendelea kubadilisha matokeo ya tafiti kuwa teknolojia zinazotoa suluhisho kwa changamoto za wakulima na wafugaji.
Amesema teknolojia mbalimbali zinazooneshwa na Taasisi, ikiwemo Mfumo wa Ng’ombe Smart, zinalenga kuongeza tija katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa kwa kuwezesha ufuatiliaji wa uzalishaji wa maziwa na taarifa muhimu za mifugo.
Aidha, Prof Kipanyula amesema mwaka huu NM-AIST imekuja na teknolojia zinazolenga kuongeza thamani ya mazao, yakiwemo tumbaku, mazao ya chakula pamoja na vyakula vya mifugo kama kuku na ng’ombe.
Prof. Kipanyula amesisitiza kuwa NM-AIST inaendelea kujipanga kuwa kinara katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan katika maeneo ya utafiti na maendeleo, sayansi, teknolojia na ubunifu, pamoja na mabadiliko ya kidijitali.
“Ushindi huu ni chachu ya kuendelea kufanya vizuri zaidi. Mwaka ujao tutakuja na teknolojia mpya kabisa. Mwaka huu tumefanikiwa kuzalisha takribani patent 40, jambo tunalojivunia na linalotupa nguvu ya kuendelea kuzalisha teknolojia na bunifu zenye tija kwa sekta ya kilimo na mifugo.”


Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Makalla, ameipongeza Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) kwa tafiti na bunifu mbalimbali zinazolenga kuongeza tija katika sekta za kilimo na mifugo.
Mhe. Makalla amesema kuwa ametembelea banda la NM-AIST na kujionea teknolojia mbalimbali za kilimo na mifugo, pamoja na bunifu zinazolenga kuongeza thamani ya mazao na bidhaa za mifugo.
Amesisitiza kuwa mapinduzi ya kweli hayawezi kufanyika bila utafiti, teknolojia na ubunifu, akieleza kuwa NM-AIST imekuwa ikifanya vizuri katika kuibua na kuendeleza teknolojia zinazolenga kutatua changamoto za jamii.
“Kilimo bila utafiti, teknolojia na dhana za kisasa hakiwezi kuleta mabadiliko makubwa. Taasisi za utafiti zinatuelekeza na kutupeleka kwenye kilimo na ufugaji wenye tija,” amesema Mhe. Makalla.
Aidha, Mhe. Makalla amesema maendeleo ya sekta za kilimo, mifugo na uvuvi hayapaswi kupimwa kwa kuongezeka kwa uzalishaji pekee, bali pia kwa uwezo wa kuzalisha kwa tija, ubora na kuzingatia mahitaji ya soko, kama inavyosisitizwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Ameeleza kuwa Dira hiyo inalenga kujenga uchumi shindani unaoongozwa na maarifa, teknolojia, ubunifu na uongezaji wa thamani, hivyo taasisi za utafiti kama NM-AIST zina nafasi muhimu katika kufanikisha azma hiyo.
Mhe. Makalla ameyasema hayo wakati akihitimisha Maonesho ya 32 ya Kilimo, Mifugo na Sherehe za Nanenane Kanda ya Kaskazini, yaliyofanyika katika Viwanja vya Themi Njiro, Arusha.







Serikali imetangaza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameridhia utoaji wa kiasi cha shilingi bilioni 38 kwa ajili ya kufanikisha mpango wa kupima vijiji vyote nchini ili kumaliza migogoro ya ardhi.
Hayo yameelezwa leo Julai 1, 2026 katika viwanja vya Sokoni Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya alipokuwa akizungumza mbele ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ambaye yuko katika ziara ya kikazi ya siku tano mkoani humo.
Katika hatua ya haraka ya kusogeza huduma kwa wananchi, Mhe. Mmuya amemuagiza Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mara pamoja na timu yake, kuhakikisha wanaratibu na kuanzisha kliniki za ardhi katika kila kata.
"Hakikisheni mnaratibu uwepo wa kliniki za ardhi katika kila kata ili muwasikilize wananchi hawa na msione kila changamoto mpewazo ni ya mazoea. Hapana, amekuja kwako kwa sababu ana jambo la kusikilizwa na litatuliwe," alisema Naibu Waziri Mmuya.
Mhe. Mmuya alieleza kuwa wizara ya Ardhi iliwasilisha mpango na maombi ya fedha bungeni kufuatia maelekezo ya awali ya Waziri Mkuu, na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akaidhinisha shilingi bilioni 38 kwa ajili ya kupima jumla ya vijiji 12,333 vya Tanzania.
"Mpaka hivi ninavyoongea, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake kifupi tu ameweza kupima vijiji 4,873. Na ametupatia maelekezo kuwa ndani ya kipindi chake, vijiji vyote vilivyobakia tuvipime." Aliongeza Naibu Waziri Kaspar Mmuya
Katika hatua nyingine Mhe. Mmuya amesema Wizara ya Ardhi itashirikiana bega kwa bega na Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili kuhakikisha maagizo hayo yanatekelezwa kikamilifu katika vijiji vyote vilivyosalia nchini.
Aidha, Mhe. Mmuya alieleza kuwa Wilaya ya Serengeti ina kata 30 na vijiji 78. Ameuhakikishia uongozi wa wilaya hiyo kuwa vijiji vyote 78 vimeshaingizwa kwenye mpango wa upimaji ndani ya kipindi cha miaka mitano ya Rais Samia Suluhu Hassan.
"Kupima vijiji hivi ndiyo dawa kubwa ya kutatua changamoto ya mipaka kati ya kijiji na kijiji. Lakini ni dawa kubwa ya kutatua changamoto ya kugombania matumizi ya ardhi ya mtu mmoja mmoja, taasisi na taasisi, au serikali na wananchi," alisema Naibu Waziri Kaspar Mmuya.
Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb.), amewasili mkoani Shinyanga kwa ziara maalum ya kikazi ya kukagua utekelezaji na kuzindua miradi ya maendeleo, pamoja na kuzungumza na wananchi katika wilaya za Mkoa wa Shinyanga.
Waziri Ndejembi, ambaye ni Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga Kiserikali, mara baada ya kuwasili amefika katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga na kupokelewa na Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Mboni Mhita, tarehe 09 Agosti 2026.
Waziri Ndejembi akiwa mkoani hapo, atakagua mradi wa ujenzi wa barabara ya Kahama – Kakola, mradi wa ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama, kukagua ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Shinyanga, pamoja na kuwasha umeme wa REA katika Kitongoji cha Mwanubi, Kolandoto.
MBOGWE,
Zaidi ya wananchi 420 wamepata ajira zisizo za ujuzi kupitia utekelezaji wa ujenzi wa Kituo cha Kuongeza Msukumo wa Mafuta (PS4) cha Mbogwe, kinachotekelezwa chini ya Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).
Hayo yameelezwa Agosti 8, 2026 na Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Derick Moshi, wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho kilichopo Wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita.
Bw. Moshi amesema utekelezaji wa mradi huo umeendelea kutoa manufaa kwa Watanzania, ambapo takribani asilimia 80 ya fursa zinazotokana na mradi zimenufaisha Watanzania, ikiwemo ajira, mafunzo na ushiriki wa wazawa katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali.
Amesema zaidi ya ajira hizo, mradi umetoa mafunzo kwa wananchi kupitia Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) na Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), hatua iliyowawezesha kupata ujuzi na uzoefu unaohitajika katika kushiriki kwenye miradi mikubwa ya kimkakati.
“Mradi huu umeendelea kuwa fursa kwa Watanzania, siyo tu kupitia ajira, bali pia kupitia mafunzo yanayowawezesha vijana kupata ujuzi na uzoefu wa kushiriki katika miradi mikubwa ya kimkakati,” amesema Bw. Moshi.
Aidha, Bw. Moshi ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa PS4, ambao umefikia asilimia 88 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 2026.
Amesema utekelezaji wa mradi huo umezingatia pia ushirikishwaji wa jamii inayozunguka mradi kupitia ajira, utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) pamoja na maboresho ya miundombinu, ikiwemo barabara na huduma za maji.
Ameeleza kuwa vituo vya kuongeza msukumo wa mafuta vya Muleba (PS3) na Mbogwe (PS4) ni sehemu muhimu ya miundombinu ya EACOP, kwa kuwa vina jukumu la kupokea na kuongeza msukumo wa mafuta ili yaweze kusafirishwa kwa ufanisi kupitia bomba hilo kuelekea kituo cha mwisho cha Kiteto.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Huduma wa EACOP ambaye pia ni Kaimu Meneja wa EACOP Tanzania, Bw. Geofrey Mponda, amesema vituo vya kuongeza msukumo wa mafuta ni miundombinu muhimu katika kuhakikisha usafirishaji wa mafuta kupitia EACOP unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.
Amesema utekelezaji wa Mradi wa EACOP umeendelea kuwa chachu ya fursa kwa Watanzania, hususan vijana, kwa kuwa umetoa ajira kwa wenye ujuzi na wasio na ujuzi, huku ukiwawezesha pia kupata uzoefu wa vitendo katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati.
“EACOP imeendelea kuwa chachu ya fursa kwa Watanzania. Vijana wamepata ajira na wengine wamepata fursa ya kujifunza na kujenga uzoefu ambao utawasaidia kushiriki katika miradi mingine mikubwa ya kimkakati,” amesema Mponda.
Naye Mwakilishi wa Kampuni ya EACOP katika eneo la mradi (EACOP Company Site Representative), Bw. Kamal Maalouli, amesema PS4 ni miongoni mwa vituo vikubwa na muhimu katika utekelezaji wa Mradi wa EACOP.
Amesema kampuni imeendelea kuweka juhudi zote kuhakikisha ujenzi wa kituo hicho unakamilika kwa wakati uliopangwa na kukidhi viwango vinavyohitajika ili kiweze kutekeleza jukumu lake katika mfumo wa usafirishaji wa mafuta kupitia EACOP.
Mradi wa EACOP unahusisha ujenzi wa bomba lenye urefu wa takribani kilomita 1,443 kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani, Tanga nchini Tanzania, ambapo sehemu kubwa ya bomba hilo inapita nchini Tanzania.