HABARI MPYA
HABARI
SIASA
ELIMU
Recent Posts
WIZARA, RUWASA ZASAINI MIKATABA YA UTENDAJI KUFIKIA VIJIJI 1,575
HABARIRUWASA WAKABIDHIWA CHETI CHA ITHIBATI ISO 9001:2015
HABARINAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA ATEMBELEA KIWANJA CHA UJENZI WA VIWANGO HOUSE ARUSHA
HABARIKAMATI YA BUNGE YAPONGEZA MRADI WA UMEME IGANJO-SAZA
NishatiMwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, ameipongeza Wizara ya Nishati kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa hatua ya kuanza kutekeleza Mradi wa Ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovoti 220 kutoka Iganjo mkoani Mbeya hadi Saza mkoani Songwe, akisema mradi huo utakuwa na manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi.
Mhe. Mgalu amesema hayo tarehe 11 Septemba 2026 katika eneo la Saza, Mkwajuni, Wilaya ya Songwe, Mkoa wa Songwe, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi huo.
Amesema Kamati inaamini kukamilika kwa mradi huo kutachochea shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii, ikiwemo uchimbaji wa madini, kilimo na biashara, sambamba na kuongeza fursa za ajira na kipato kwa wananchi katika maeneo yatakayonufaika na mradi huo.
Mhe. Mgalu amesema Kamati imeendelea kuhimiza utekelezaji wa miradi ya umeme inayolenga kuchochea shughuli za uzalishaji katika maeneo mbalimbali nchini, ikiwemo maeneo yenye shughuli za uchimbaji wa madini.
Ameeleza kuwa Kamati iliielekeza Wizara kuhakikisha umeme wa uhakika unafikishwa katika maeneo ya wachimbaji wa madini ili kupunguza gharama za uzalishaji na kuongeza ufanisi katika shughuli zao, jambo ambalo Wizara ya Nishati imeendelea kulifanyia kazi.
Aidha, Mhe. Mgalu ameishauri Wizara kuangalia uwezekano wa kufikisha umeme wa uhakika mapema katika mkoa huo kupitia miradi mbalimbali wakati wananchi wakiendelea kusubiri Mradi wa Iganjo–Saza unaotarajiwa kutekelezwa kwa kipindi cha miezi 18.
Kuhusu ushauri huo, Serikali tayari ilianza kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kutekeleza mradi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Mwakibete-Mbeya kuelekea Wilaya ya Songwe, ambao unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi huu.

WIZARA , TAASISI ZATAKIWA KUCHUKUA HATUA KUKABILIANA NA MVUA ZA EL NIÑO
HABARI 
OWM –TAMISEMI, Dar es Salaam
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi leo Septemba 11, 2026 amezitaka Wizara, Mamlaka na Taasisi zinazohusika na majanga kuchukua hatua za haraka kujiandaa ili kuzuia na kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua za El Niño zinazotarajiwa kuanza mwezi Oktoba hadi Desemba 2026. 
Makamu wa Rais ametoa maagizo hayo kwa taasisi hizo katika kikao kilichofanyika Ofisi ya Makamu wa Rais Jijini Dar es Salaam, ambapo kwa upande wa Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI yamepokelewa na Waziri Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, mara baada ya ofisi yake na taasisi zinazohusika kuchukua hatua za haraka, kuwasilisha taarifa ya utayari na maandalizi ya Serikali katika kukabiliana na madhara ya mvua hizo, kufuatia tahadhari iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.
Katika kikao kazi hicho, Makamu wa Rais, Mhe. Ndejembi ameagiza wataalamu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Ujenzi pamoja na Taasisi zilizo chini ya Wizara hizo kuhakikisha zinafanya kampeni maalum ya usafi katika miundombinu ya barabara na mifereji ya maji.
“Ifanyike kampeni ya haraka, mikondo na mifereji ya maji izibuliwe, na barabara ziandaliwe,” amesisitiza Makamu wa Rais.
Aidha, Makamu wa Rais Mhe. Ndejembi, ameelekeza taka, tope na udongo unaotolewa baada ya kuzibua mitaro na mifereji katika maeneo mbalimbali kuondolewa mara moja na kutupwa katika maeneo yaliyotengwa, badala ya kuachwa kandokando ya barabara ambako taka, tope na udongo huo zinaweza kurejea kwenye mifereji wakati mvua zinapoanza.
Makamu wa Rais pia amezitaka Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Ujenzi pamoja na Taasisi zilizo chini ya Wizara hizo, kufanya kazi kwa pamoja ya kujiandaa ili kuzuia na kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua za El Niño.
Akipokea maagizo hayo kwa ajili ya utekelezaji, Waziri wa Nchi, OWM – TAMISEMI Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amemueleza Mhe. Makamu wa Rais kuwa ofisi yake imeshaanza kutekeleza maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha usafi wa mazingira katika majiji aliyoyatoa Septemba 02, 2026 wakati akiwaapishwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala aliowateua Agosti 27, 2026.
Prof. Shemdoe amemtaarifu Makamu wa Rais Mhe. Ndejembi kuwa, Septemba 07, 2026 alifanya kikao kazi na Wakuu wa Mikoa yenye majiji, viongozi wa majiji na manispaa za Mkoa wa Dar es Salaam na kuwataka kuhakikisha wanatekeleza kampeni maalum ya wiki mbili ya usafi wa mazingira katika majiji ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais.
Akianisha namna ofisi yake itakavyotekeleza maelekezo ya Makamu wa Rais ya kujiandaa na kukabiliana na athari za mvua za El Niño, Prof. Shemdoe amewasilisha kwa Makamu wa Rais Mhe. Ndejembi, mkakati wa ofisi yake kupitia TARURA ulioandaliwa kwa ajili ya kujiaanda, kuzuia na kupambana na madhara ya uharibifu wa miundombinu ya barabara unaoweza kutokana na mvua za El Niño, ambao umeanisha namna utakavyotekelezwa.
WAFANYABIASHARA WA VIPODOZI KARIAKOO WAPATIWA ELIMU YA KODI
HABARIWANAFUNZI 150 KUNUFAIKA NA UFADHILI WA MASOMO ALGERIA
HABARI
MRADI WA KUSAFIRISHA UMEME KV 220 IGANJO–SAZA KUCHOCHEA UCHIMBAJI MADINI – MHE. SALOME
Nishati
* Ashuhudia utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi kutoka Iganjo, Mbeya hadi Saza, Songwe
* Mradi kutekelezwa kwa miezi 18 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 198.67
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amesema utekelezaji wa Mradi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovoti 220 kutoka Iganjo, Mkoani Mbeya, hadi Saza, Mkoani Songwe, pamoja na ujenzi wa Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Saza, utaimarisha upatikanaji wa umeme katika mikoa hiyo na kuchochea shughuli za uzalishaji, hususan uchimbaji wa madini katika Wilaya za Chunya na Songwe.
Akizungumza Septemba 11, 2026, katika Kijiji cha Saza, Wilaya ya Songwe, wakati wa hafla ya utiaji saini mkataba wa utekelezaji wa mradi huo, Naibu Waziri wa Nishati amesema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kuongeza uzalishaji, kuendeleza kilimo cha kisasa na biashara, pamoja na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa umeme kwa wananchi na katika shughuli mbalimbali za kiuchumi.
Aidha, amesema wakati Mradi wa Iganjo–Saza ukiendelea kutekelezwa, ni muhimu wananchi kufahamu maendeleo ya Mradi wa TAZA (Tanzania–Zambia Transmission Interconnector Project), ambao ni sehemu muhimu ya mipango ya Serikali ya kuimarisha miundombinu ya usafirishaji wa umeme na kukuza biashara ya umeme katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.
“Napenda kuwahakikishia wananchi wa Songwe na Mbeya kwamba Serikali inaona changamoto za upatikanaji wa umeme katika maeneo yenu na inaendelea kuchukua hatua. Utekelezaji wa mradi huu ni kielelezo cha kuendelea kuhakikisha shughuli za kijamii na kiuchumi zinafanyika kwa ufanisi, huku tukijenga mfumo wa umeme ambao utaungana vizuri na kutoa uwezo mkubwa zaidi wa kusafirisha na kusambaza umeme,” amesisitiza Mhe. Salome.
Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Subira Mgalu, amepongeza kazi inayofanywa na Wizara ya Nishati kupitia TANESCO, akisisitiza kuwa mradi huo utakuwa na manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi, ikiwemo kuibua fursa za ajira na kuchochea shughuli za uchimbaji wa madini.
Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO, Mhe. Balozi Zuhura Bundala, amesema TANESCO inaendelea kutekeleza jitihada za kujenga na kuboresha miundombinu ya umeme ili kwenda sambamba na kasi ya ongezeko la mahitaji ya nishati linalochochewa na shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii.
“Utekelezaji wa mradi huu ni sehemu muhimu ya majukumu ya TANESCO ya kuendelea kujenga miundombinu ya umeme ili kumudu mahitaji ya sasa na ya baadaye. Tunahakikisha mradi huu unajengwa kwa ufanisi na kuendana na thamani ya fedha iliyowekwa,” alifafanua Mhe. Balozi Bundala.
Naye Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, anayeshughulikia Mipango, Utafiti na Uwekezaji, Mha. Amos Joas, akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, amesema utekelezaji wa mradi huo utagharimu Shilingi Bilioni 198.67 na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 18.
“Kwa sasa, maeneo ya Chunya na Songwe, hasa upande wa Mkwajuni, yanapata umeme kutoka Mkoa wa Mbeya kupitia Kituo cha Mwakibete kwa kutumia njia ya msongo wa Kilovoti 33 yenye urefu wa zaidi ya kilomita 116. Kutokana na umbali huo mrefu na ongezeko la mahitaji ya umeme, kumekuwa na changamoto katika upatikanaji wa umeme, hivyo utekelezaji wa mradi huu utasaidia kuboresha hali hiyo,” alieleza Mha. Joas.
Mkataba huo umesainiwa kati ya Serikali kupitia TANESCO na Mkandarasi Kampuni ya TBEA kwa ajili ya ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovoti 220 kutoka Iganjo, Mkoani Mbeya, hadi Saza, Mkoani Songwe, pamoja na ujenzi wa Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Saza.

SALOME ASHUHUDIA UTIAJI SAINI MKATABA WA SHILINGI BILIONI 198 KUIMARISHA UMEME SONGWE, CHUNYA
HABARI
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, ameshuhudia utiaji saini wa mkataba wenye thamani ya shilingi bilioni 198.67 kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Njia ya Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovoti 220 kutoka Iganjo mkoani Mbeya hadi Saza mkoani Songwe pamoja na ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme cha Saza, mradi unaotarajiwa kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Songwe na Wilaya ya Chunya.
Akizungumza mara baada ya kushuhudia utiaji saini wa mkataba huo Septemba 11, 2026 katika eneo la Saza-Mkwajuni, Wilaya ya Songwe, Mhe. Salome amesema mradi huo utaimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo hayo ambayo kwa sasa yanategemea umeme unaotoka mkoani Mbeya unaohudumia maeneo mengi kwa umbali mrefu.
Amesema kukamilika kwa mradi huo kutaongeza uwezo wa mfumo wa umeme kukidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye, huku ukiweka mazingira bora zaidi ya uwekezaji na ukuaji wa shughuli za kiuchumi, zikiwemo biashara, kilimo, viwanda na uchimbaji wa madini.Mhe. Salome amesema utekelezaji wa mradi huo ni sehemu ya dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuendeleakuimarisha miundombinu ya nishati ili kuhakikisha wananchi wanapata umeme wa uhakika na kuchochea shughuli za uzalishaji na ukuaji wa uchumi.

Ameeleza kuwa Mradi wa Iganjo–Saza pia ni matokeo ya uwekezaji mkubwa wa Serikali katika Mradi wa Kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kilovoti 400 wa Tanzania–Zambia (TAZA), ambao kwa upande wa Tanzania unahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme kutoka Iringa kupitia Kisada, Iganjo na Tunduma hadi Sumbawanga, yenye urefu wa kilomita 616.
Amesema miundombinu ya Mradi wa TAZA inahusisha pia ujenzi wa Kituo cha Kupokea na Kupoza Umeme cha Iganjo mkoani Mbeya, ambacho ndicho kitakachowezesha kusafirisha umeme kwenda Saza mkoani Songwe ambapo kwa ujumla utekelezaji wa Mradi wa TAZA umefikia asilimia 89.46 na unatarajiwa kukamilika Februari 2027, kabla ya kukamilika kwa Mradi wa Iganjo–Saza.

“Tunataka Songwe, Mbeya, Rukwa, Iringa na mikoa mingine katika ukanda huu iwe na uwezo wa kuvutia uwekezaji, kukuza viwanda, kuongeza shughuli za kilimo, uchimbaji madini na biashara pamoja na kuongeza thamani ya rasilimali zilizopo,” amesema Mhe. Salome
Aidha, Mhe. Salome ameipongeza TANESCO kwa kutumia taasisi yake ya ndani, TANESCO Engineering Consultancy Unit (TANECU), kuwa Mhandisi Mshauri wa mradi huo, akisema hatua hiyo ni muhimu katika kujenga na kuimarisha uwezo wa wataalam wa ndani kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati katika sekta ya umeme.
Pamoja na kuipongeza TANESCO kwa kuendelea kutekeleza miradi inayolenga kuongeza matumizi ya umeme na mapato ya Shirika, Mhe. Salome amesisitiza kuwa Serikali inataka kuona thamani ya fedha, ubora na uzingatiaji wa muda wa mikataba katika utekelezaji wa miradi ya umeme.
“Naielekeza TANESCO na Mkandarasi kuhakikisha kwamba mradi huu unatekelezwa kwa kasi inayostahili, kwa ubora unaotakiwa na kwa kuzingatia masharti yote ya mkataba. Serikali na wananchi wa Songwe hatutegemei kusikia muda wa utekelezaji wa mradi umeongezeka; tutafurahi kuona mradi umekamilika ndani ya wakati na kwa ubora,”amesema.
Vilevile, ameelekeza taratibu za ulipaji fidia kwa wananchi watakaopisha maeneo yao kwa ajili ya utekelezaji wa mradi kufanyika kwa haki na kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa na wananchi wa maeneo yanayozunguka mradi kupewa kipaumbele katika fursa za ajira na utoaji wa huduma mbalimbali wakati wa utekelezaji wake.Katika hatua nyingine, Mhe. Salome amewahakikishia wananchi wa Songwe na Mbeya, hususan maeneo ya Chunya, kuwa Serikali inatambua changamoto za upatikanaji wa umeme wanazokabiliana nazo na inaendelea kuchukua hatua za kuzitatua, mojawapo ni ujenzi wa njia ya umeme kutoka Mwakibete-Mbeya hadi wilayani Songwe ya kV 33 itakayokamilika mwishoni mwa mwezi huu.

Awali, mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Mhandisi Amos Kaihula amesema Mradi wa Iganjo–Saza unaohusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme pamoja na Kituo cha Kupoza Umeme cha Saza,utekelezaji wake unatarajiwa kuchukua miezi 18.
Amesema Kituo cha Saza kitakuwa na transfoma mbili zenye uwezo wa MV 50 kila moja na kwamba mradi huo utaimarisha hali ya upatikanaji wa umeme Songwe na Chunya, maeneo ambayo kwa sasa yanapata umeme kutoka Mbeya unaosafirishwa kwa umbali wa takribani kilomita 116.
Amesema Mkandarasi wa mradi huo ni Kampuni ya TBEA ya China.
Kwa upande wao, wachimbaji wa madini mkoani Songwe kupitia mwakilishi wao, Shadrack Mwakyalabwe, wameipongeza Serikali kwa mradi huo, wakisema utaongeza uhakika wa upatikanaji wa umeme na kuwawezesha kufanya shughuli za uchimbaji kwa ufanisi zaidi. Wamesema kwa sasa baadhi yao wanakabiliwa na gharama kubwa za uzalishaji kutokana na kutegemea mafuta kuendesha shughuli zao.

RAIS DKT. MWINYI AITAKA SERIKALI, WANANCHI KUJIANDAA KUKABILIANA NA MVUA KUBWA ZA EL NIÑO
HABARI 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewataka viongozi na taasisi za Serikali kuongeza utoaji wa elimu na tahadhari kwa wananchi kuhusu hali ya El Niño na mvua kubwa zinazotarajiwa, ili hatua za kujikinga na kupunguza madhara zichukuliwe mapema.
Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo, tarehe 11 Septemba 2026, baada ya Sala ya Ijumaa katika Msikiti wa Masjid Swafaa, Gongoni, Mkoa wa Mjini Magharibi.
Amesema wananchi wanapaswa kufuatilia kwa karibu taarifa na maelekezo yatakayotolewa na Serikali pamoja na mamlaka husika kuhusu mwenendo wa mvua, na kuchukua tahadhari mapema ili kupunguza madhara na usumbufu unaoweza kujitokeza.
Rais Dkt. Mwinyi amewataka wananchi kuchukua tahadhari mapema, hususan kwa kuepuka maeneo ya mabondeni, mikondo na njia za maji, pamoja na kuhama maeneo yenye hatari pale itakapohitajika, huku akisisitiza umuhimu wa kumuomba Mwenyezi Mungu kwa dua sambamba na kuzingatia maelekezo yatakayotolewa na mamlaka husika.
Aidha, amesema Serikali kupitia vikosi na taasisi zake inaendelea na maandalizi ya kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza kutokana na El Niño na mvua kubwa, ikiwemo kuweka utaratibu wa kutoa msaada kwa wananchi watakaoathirika na kuimarisha uwezo wa uokozi pale itakapohitajika.
Rais Dkt. Mwinyi pia amezitaka Manispaa zote za Unguja na Pemba kuhakikisha mifereji, mikondo na njia za kupitisha maji zinasafishwa, ili kupunguza uwezekano wa maji kutuama na madhara ya mafuriko katika maeneo mbalimbali.
Amesema hatua hizo ni sehemu ya maandalizi yanayoendelea kufanywa na Serikali kwa lengo la kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na mvua hizo, huku akitoa wito kwa wananchi kushirikiana na mamlaka husika na kuzingatia taarifa na maelekezo rasmi yatakayotolewa.
Kuhusu upatikanaji wa huduma muhimu, Rais Dkt. Mwinyi amesema Serikali imejiandaa kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata mahitaji ya msingi katika kipindi hicho, ikiwemo chakula na huduma za afya, pamoja na kuhakikisha bohari za dawa zina akiba ya kutosha
Amesisitiza kuwa taasisi na mamlaka zote zinazohusika zinapaswa kuwa katika hali ya utayari wakati wote ili huduma na msaada unaohitajika utolewe kwa wananchi kwa wakati endapo changamoto zitajitokeza.


USHIRIKIANO NI MUHIMU KATIKA MAGEUZI YA KIDIJITALI: KITALI
HABARI
OWM-TAMISEMI, Arusha
Mkurugenzi wa Idara ya TEHAMA Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI), Bw. Erick Kitali, amesema mafanikio ya mageuzi ya kidijitali nchini yanahitaji ushirikiano wa taasisi mbalimbali, uongozi wenye maono na kuwashirikisha wataalamu sahihi katika kufanya maamuzi.
Bw. Kitali ameyasema hayo leo Septemba 10, 2026 jijini Arusha wakati wa mdahalo kuhusu kuimarisha huduma za afya ya msingi kupitia miundombinu ya umma ya kidijitali na safari ya Tanzania ya kuwalipa wahudumu wa afya ya jamii kwa njia za kidijitali.
Amesema ni muhimu Serikali kuhakikisha mifumo mbalimbali inaunganishwa ili kuwezesha upatikanaji wa taarifa kwa wakati na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Tunapaswa kuzungumzia ushirikiano na muunganiko wa mifumo. hakikisheni watu sahihi wanakuwepo kwenye meza ya maamuzi,” amesema.
Bw. Kitali amesema Tanzania imejikita pia katika kutumia wataalamu wa ndani kubuni, kuendeleza na kusimamia mifumo ya kidijitali inayotumika katika huduma za afya, ikiwemo usajili, malipo na utoaji wa taarifa.
Amesema Serikali imeandaa Mpango Elekezi (Blueprint) wa matumizi ya teknolojia katika huduma za wahudumu wa afya ya jamii, ukiwemo mpango wa kuanzisha Dashibodi ya Pamoja itakayounganisha taarifa kutoka mifumo mbalimbali.
Kwa mujibu wa Bw. Kitali, amesema dashibodi hiyo itasaidia kufuatilia huduma na malipo kuanzia ngazi ya jamii hadi taifa, pamoja na kubaini kwa haraka changamoto kama ucheleweshaji wa malipo.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kufanya tafiti na ufuatiliaji wa utekelezaji ili kubaini changamoto mapema na kuchukua hatua kwa wakati.
Amesema ushirikiano wa taasisi, matumizi ya wataalamu wa ndani na mifumo iliyounganishwa ni msingi muhimu wa kuboresha huduma za afya ya msingi na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kwa wakati.










