
KAMPASI YA TPSC TABORA YATOA MISAADA NA KUFANYA USAFI – KITUO CHA WAZEE IPULI-TABORA
habari
HABARI NA MATUKIO MBALIMBALI


Naibu Mrajis - Uhamasishaji, Consolata Kiluma, amekipongeza chama kikuu cha Ushirika SIMCU (2018) LTD, kwa usimamizi wa ujenzi wa ujenzi na ukarabati wa kiwanda cha kuchakata pamba kilichopo wilayani Maswa mkoa wa Simiyu ambacho kinatarajiwa kuanza kazi musimu huu wa 2026/2027.
Ametoa pongezi hizo leo Februari 21, 2026 alipofanya ziara katika chama hicho kwa lengo kukagua na kuona hatua zilizofikiwa za ujenzi kuelekea uzinduzi wake.
Aidha amewataka viongozi wa SIMCU (2018) LTD, kuendelea kufufua viwanda vingine vinavyomilikiwa na chama ambavyo havifafanyi kazi kwa sasa ikiwa ni sehemu ya kuimarisha ushirika wa viwanda ili kuongeza thamani ya mazao ya wakulima.
Naye, Mwenyekiti wa SIMCU (2018) LTD, Ramadhani Matani, amesema juhudi mbalimbali zinaendelea kuhakikisha kiwanda kinaanza kufanya kazi haraka iwezekanavyo ambapo mpaka sasa wamefikia zaidi ya asilimia 75 ya ujenzi wa kiwanda hicho.


Wakala wa Vipimo Tanzania (WMA) imetoa mafunzo ya vipimo kwa wanafunzi wa Dr. Samia Dodoma Secondary School, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa vipimo sahihi katika biashara na maisha ya kila siku.
Katika zoezi hilo, wanafunzi walipata fursa ya kujifunza kuhusu dhima na majukumu ya Wakala huo, pamoja na namna unavyolinda maslahi ya watumiaji na wafanyabiashara kwa kuhakikisha vipimo vinakuwa sahihi na vya kuaminika.
Akizungumza baada ya mafunzo hayo, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa WMA, Veronica Simba, amesema elimu ya vipimo itatolewa katika mikoa yote ya Tanzania Bara ili kuhakikisha wanafunzi wengi zaidi wanapata uelewa wa matumizi sahihi ya vipimo.
Amesema mpango huo unalenga kukuza uelewa wa masuala ya vipimo kwa vijana, sambamba na kuimarisha utamaduni wa uadilifu na uwajibikaji katika sekta ya biashara nchini.
Kwa upande wake, Meneja wa Wakala wa Vipimo Mkoa wa Dodoma, Said Ibrahim, amesema mafunzo hayo yanaenda sambamba na uanzishwaji wa Klabu za Vipimo mashuleni ili kuendelea kuandaa mabalozi mahiri watakaotoa elimu ya vipimo shuleni na katika jamii kwa ujumla.
“Kwa Dodoma tayari tumeshatoa mafunzo katika shule mbili ambazo ni Shule ya Msingi Mtemi Mazengo na leo tumetoa hapa katika Shule ya Sekondari ya Dkt. Samia Dodoma. Tunaamini mabadiliko katika matumizi ya vipimo sahihi yataongezeka,” amesema Said.
Kwa upande wake, Mwalimu Mussa Madandi, ambaye pia ni mlezi wa Klabu ya Vipimo shuleni hapo, amesema elimu hiyo wamekuwa wakiifundisha darasani, lakini mafunzo yaliyotolewa na WMA yamewapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo, jambo litakalosaidia kuongeza uelewa na kuimarisha matumizi ya vipimo sahihi.
“Vipimo ni somo tunalolifundisha karibu kila darasa, lakini leo wanafunzi wamepata mafunzo kwa vitendo kutoka kwa wataalamu wenyewe. Naamini hali hii itaongeza hamasa ya kuzingatia usahihi katika matumizi ya vipimo na kuwafanya wawe mabalozi wazuri kwa wazazi wao na jamii inayowazunguka,” amesema Mwalimu Madandi.
Naye mwanafunzi Itabangola Elias amesema elimu hiyo imewasaidia kuelewa namna ya kutambua vipimo sahihi na kujikinga dhidi ya udanganyifu unaoweza kujitokeza katika biashara.
Baada ya mafunzo hayo, wanafunzi walishiriki kujibu maswali mbalimbali kuhusiana na vipimo na shughuli za Wakala huo, ambapo waliofanya vizuri walipatiwa zawadi mbalimbali kama sehemu ya kuwahamasisha kuendelea kujifunza na kuwa mabalozi wa matumizi sahihi ya vipimo katika jamii.


Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Jimbo la Kisarawe mkoani Pwani, Dkt. Selemani Jafo, ametangaza mpango wa kuweka kambi maalum katika eneo la ujenzi wa Daraja la Kitomondo lililopo katika barabara ya Mzenga–Gwata, akilenga kuharakisha ukamilishaji wa mradi huo na kuondoa adha wanazokumbana nazo wananchi hasa nyakati za mvua.
Dkt. Jafo alitoa kauli hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi katika Kata za Mzenga na Mafizi ndani ya Jimbo la Kisarawe, ambapo alikagua maendeleo ya mradi huo na kusikiliza changamoto za wananchi wanaotegemea daraja hilo kwa shughuli za kila siku.
Daraja la Kitomondo linajengwa na kampuni ya Neloyt Tanzania Limited kwa gharama ya shilingi milioni 359.67 chini ya usimamizi wa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA), hata hivyo ujenzi wake umechelewa kukamilika hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi wa Mzenga na Mafizi.
Mbunge huyo amesema daraja hilo ni kiungo muhimu kwa wakazi wa kata hizo na vijiji vya Mafizi, Nyani, Gwata na Ving’andi, akieleza kuwa kuchelewa kwake kumeathiri shughuli za kiuchumi na kijamii ikiwemo usafiri wa wanafunzi, wagonjwa na wafanyabiashara.
Amesisitiza kuwa kukamilika kwa daraja hilo kutarahisisha usafiri na usafirishaji wa mazao na bidhaa, hivyo kuchochea maendeleo katika Jimbo la Kisarawe.
Kwa upande wake, Meneja wa TARURA Wilaya ya Kisarawe, Eng. Africano Orota, amemhakikishia Dkt. Jafo kuwa wataongeza usimamizi na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa maelekezo yaliyotolewa ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.



Na.Mwandishi Wetu
Taasisi ya Jafo Education Foundation imefadhili jumla ya vijana 51 kusoma katika Chuo cha FDC Kisarawe - Mzenga, kwa lengo la kuwawezesha kupata ujuzi wa fani mbalimbali za ufundi.
Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua miradi na kuzungumza na wananchi katika Kata ya Mzenga, Mbunge wa Jimbo la Kisarawe Mhe.Dkt. Selemani Jafo, amesema vijana hao 51 watatoka katika kata zote 17 za wilaya hiyo na taasisi hiyo itagharamia ada zao za masomo.
"Hii ni fursa muhimu kwa vijana wa Kisarawe kujipatia ujuzi utakaowawezesha kujiajiri na kuajiriwa, hasa katika kipindi hiki ambacho soko la ajira linahitaji wataalamu wenye ujuzi wa vitendo."amesema Dkt. Jafo
Dkt.Jafo amesema kuwa Chuo cha FDC Kisarawe – Mzenga ni chuo kipya kilichojengwa wilayani humo na tayari kinatoa mafunzo katika fani mbalimbali zikiwemo ufundi magari, ushonaji, ujenzi, mapishi, umeme, kompyuta pamoja na mafunzo ya muda mfupi.
Aidha, Dkt. Jafo ameeleza kuwa tangu mwaka 2010 amefanikiwa kusaidia zaidi ya vijana 500 kutoka familia zenye changamoto kusoma katika ngazi mbalimbali, ikiwemo kidato cha tano, astashahada, stashahada na shahada.
Katika kuendeleza juhudi za kukuza elimu ya ufundi, tarehe 20 Februari, Dkt. Jafo kupitia taasisi yake amekabidhi msaada wa vyerehani vinne vya umeme katika chuo hicho, ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Samia Suluhu Hassan.
Amesema kuwa dhamira kuu ni kuwawezesha vijana katika fani za ufundi ili kujenga msingi imara wa ajira rasmi na zisizo rasmi, pamoja na kuongeza kasi ya maendeleo katika Wilaya ya Kisarawe.















Wakulima wa zao la pamba mkoa wa Simiyu ambao ni wanachama wa Vyama vya Ushirika wameshauriwa kulima kwa tija kwa kutumia teknolojia ya kisasa na kuepukana kilimo cha mazoea ambacho kinawapa hasara.
Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anamringi Macha katika Mkutano wa 8 Chama Kikuu Simiyu, SIMCU (2018) LTD, uliofanyika leo Februari 20, 2026 Wilayani Maswa Mkoa wa Simiyu, pia amewaahakikishia wakulima kuwa Serikali itaendelea kuwawezesha kwa kutoa rudhuku za mbolea, viuatilifu na kutafuta masoko ili kuongeza uzalishaji wa zao hilo.
"Mkulima anapata kilo mia tatu za pamba kwa heka ni hasara na ni upotevu wa muda inabidi tutoke kwenye kilimo cha namna hii..." alisema Mhe. Macha
Akizungumza kwa niaba ya Mrajis wa Vyama vya Ushirika nchini, Consolata Kiluma, ambaye ni Naibu Mrajis - Uhamasishaji, amewasistiza wajumbe wa bodi za vyama vya Ushirika kuwa waadilifu na waaminifu katika kutekeleza majukumu, na kuwa wabunifu kuleta ushindani kwenye biashara kama kauli mbiu isemavyo "Ushirika ni Biashara" ili kuongeza mapato kwa maslahi ya wanaushirika na Wananchi kwa ujumla.
Aidha, Mrajis Msaidizi Mkoa wa Simiyu Godfrey Mpepo amesema Ushirika umeendelea kuimarika tangu kilipoanzishwa chama kikuu SIMCU Ltd mwaka 2018, ambapo awali vyama vya mkoa huo vilikuwa vikisimamiwa na SHIRECU chama kikuu kutoka mkoa wa Shinyanga.
Naye, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Shemsha Mohamed amewataka wajumbe wa Mkutano huo kuepuka na ubadhilifu wa fedha za wanachama jambo ambalo linarudisha Ushirika nyuma kimaendeleo.
Awali, akitoa taarifa ya Utendaji wa SIMCU(2018) LTD, Meneja Mkuu wa chama hicho, Mercy Atanazi alibainisha kuwa mkutano huo umehudhuriwa na wajumbe 625 kati ya wajumbe 675 kutoka vyama wanachama 335.
