HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

CHANDE AIPONGEZA WRRB KWA KUWAWEZESHA WAKULIMA KUFIKIA MASOKO

CHANDE AIPONGEZA WRRB KWA KUWAWEZESHA WAKULIMA KUFIKIA MASOKO

August 06, 2026 Add Comment

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, ameipongeza Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala (WRRB) kwa mchango wake katika kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani kupitia Mfumo wa Stakabadhi za Ghala.

Mhe. Chande ameyasema hayo leo Agosti 6, 2026, baada ya kutembelea banda la WRRB katika Maonesho ya 88 yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Malecela, jijini Dodoma.

Amesema WRRB imeendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha biashara ya mazao kwa kuwawezesha wakulima kupata masoko yenye ushindani, kuongeza thamani ya mazao yao na kuchangia ukuaji wa uchumi wa taifa.

Aidha, ameipongeza WRRB kwa kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kutoa wito kwa wadau wa sekta ya kilimo kuendelea kutekeleza kwa vitendo kauli mbiu ya Maonesho ya Nane Nane ya mwaka 2026 isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," kwa kuimarisha mifumo ya masoko, kuongeza tija katika uzalishaji na kuhakikisha wakulima wananufaika na fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa mazao.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Uratibu Huduma ,Bw. Mwita Thomas ameeleza kuwa WRRB itaendelea kuboresha huduma zake, kuimarisha usimamizi wa mfumo huo kwa kushirikiana na wadau ili kuhakikisha sekta ya kilimo inakuwa chachu ya maendeleo ya uchumi na ustawi wa wananchi.

PINDA APONGEZA TVLA KWA KUJENGA UWEZO WA NDANI WA KUZALISHA CHANJO ZA MIFUGO

August 06, 2026 Add Comment
Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda (wa pili kutoka kushoto), akipata maelezo kutoka kwa Meneja wa Wakala ya Maabara ya Veterinari Tanzania (TVLA), Dkt. Japhet Nkangaga kuhusu huduma zinazotolewa na TVLA, wakati alipotembelea banda la TVLA lililopo kwenye banda jumuishi la Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Maonesho ya Kilimo ya NaneNane 2026 yanayoendelea kwenye Viwanja vya John Malecela, Nzuguni jijini Dodoma. Kushoto kwake ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Uvuvi, Prof. Mohammed Ali Sheikh.

MFUMO WA M+2 WAIMARISHA UHAKIKA WA MAFUTA NCHINI

August 06, 2026 Add Comment
DODOMA

Mfumo wa kuagiza mafuta kwa ajili ya matumizi ya miezi miwili inayofuata umeiwezesha Tanzania kuendelea kuwa na bidhaa za mafuta za kutosha, licha ya vita na changamoto nyingine zinazoathiri soko la dunia.
MFUMO WA M+2 WAIMARISHA UHAKIKA WA MAFUTA NCHINI

MFUMO WA M+2 WAIMARISHA UHAKIKA WA MAFUTA NCHINI

August 06, 2026 Add Comment

DODOMA

Mfumo wa kuagiza mafuta kwa ajili ya matumizi ya miezi miwili inayofuata umeiwezesha Tanzania kuendelea kuwa na bidhaa za mafuta za kutosha, licha ya vita na changamoto nyingine zinazoathiri soko la dunia.

Hayo yameelezwa na Mhandisi Rehema Mahundi katika siku ya sita ya Maonesho ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA).

Mhandisi Mahundi alisema moja ya maswali yanayoulizwa zaidi na wananchi ni namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unavyoiwezesha nchi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta, hasa wakati wa migogoro na vita katika maeneo mbalimbali duniani.

Akijibu swali hilo, alieleza kuwa PBPA hutangaza zabuni kila mwezi kwa ajili ya kuagiza mafuta yatakayotumika nchini katika miezi miwili inayofuata. Utaratibu huo unajulikana kama M+2.

“PBPA huingia mikataba na wazabuni walioshinda zabuni hizo ili kuhakikisha bidhaa za mafuta zinafika nchini kwa wakati, hata changamoto zinapojitokeza katika soko la dunia,” alisema Mhandisi Mahundi.

Alisema kupitia mfumo huo, Tanzania imeendelea kuwa na uhakika wa upatikanaji wa mafuta wakati wote na kwa gharama zinazoakisi hali halisi ya soko la dunia.

Katika Maonesho ya Nanenane, PBPA imeendelea kutoa elimu kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja kwa watu kutoka makundi mbalimbali, wakiwamo wanafunzi, wakulima, wajasiriamali, wafanyabiashara pamoja na wawakilishi kutoka taasisi za elimu na sekta binafsi.

Mhandisi Mahundi amewakaribisha wananchi kutembelea Banda la PBPA katika Viwanja vya Nanenane jijini Dodoma ili kupata elimu zaidi kuhusu namna mfumo huo unavyosimamia mnyororo wa uagizaji, usimamizi na upokeaji wa bidhaa za mafuta nchini.

PINDA ARIDHISHWA NA UBUNIFU WA NDEGE NYUKI ZA MATI TECHNOLOGIES

August 06, 2026 Add Comment

 

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda, ameshangazwa na kiwango cha ubunifu wa teknolojia zinazobuniwa na kuzalishwa na kampuni ya Mati Technologies baada ya kutembelea banda la kampuni hiyo katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa ya Kilimo (Nane Nane 2026) yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Mhe. Pinda alitembelea banda hilo leo na kupokea maelezo kutoka kwa viongozi na wataalamu wa Mati Technologies kuhusu shughuli mbalimbali zinazofanywa na kampuni hiyo katika kubuni na kutengeneza teknolojia zinazolenga kuongeza tija katika sekta ya kilimo na maeneo mengine ya maendeleo.

Katika ziara hiyo, alikagua teknolojia mbalimbali zinazotengenezwa na kampuni hiyo, ikiwemo ndege nyuki zinazotumika kunyunyiza viuatilifu na mbolea mashambani kwa usahihi, haraka na ufanisi mkubwa, pamoja na mifumo mingine ya kisasa ya kiteknolojia inayolenga kuboresha uzalishaji wa kilimo.

Baada ya kushuhudia namna teknolojia hizo zinavyofanya kazi, Mhe. Pinda alisema ameridhishwa na hatua kubwa ya ubunifu iliyofikiwa na wataalamu wa Kitanzania.
“Ni jambo la kujivunia kuona Watanzania wakibuni na kuzalisha teknolojia za kisasa zinazotoa suluhisho kwa changamoto mbalimbali za maendeleo, hususan katika sekta ya kilimo,” alisema.

Alisema maendeleo hayo yanaonesha uwezo mkubwa wa wataalamu wa ndani katika kubuni teknolojia zinazokidhi mahitaji ya nchi na kuchangia kukuza uchumi kupitia sekta ya kilimo na viwanda.
Aidha, aliipongeza Mati Technologies kwa kuwekeza katika utafiti, ubunifu na uzalishaji wa teknolojia za ndani, akisisitiza kuwa juhudi hizo zinapaswa kuungwa mkono ili kuharakisha maendeleo ya taifa na kuongeza ushindani wa bidhaa za Kitanzania katika soko la ndani na kimataifa.

Kwa upande wake, uongozi wa Mati Technologies ulisema kampuni itaendelea kubuni na kuzalisha teknolojia zenye ubora wa hali ya juu zitakazorahisisha shughuli za uzalishaji, kuongeza tija kwa wakulima na kuchochea matumizi ya teknolojia katika sekta mbalimbali za uchumi.
Maonesho ya Nane Nane yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuonesha mafanikio ya sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, viwanda na teknolojia, huku yakivutia maelfu ya wananchi, wakulima, wawekezaji, wanafunzi na wataalamu kutoka maeneo mbalimbali nchini.

Kupitia ubunifu wa teknolojia zinazozalishwa hapa nchini, Mati Technologies inaendelea kujijengea sifa kama moja ya kampuni zinazochochea matumizi ya sayansi, teknolojia na utafiti katika kuongeza tija ya uzalishaji na kuchangia maendeleo endelevu ya Tanzania.
DKT. SIMBEYE: WALIMU BORA NDIO NGUZO YA MAFANIKIO YA MTAALA NA ELIMU YA TAIFA

DKT. SIMBEYE: WALIMU BORA NDIO NGUZO YA MAFANIKIO YA MTAALA NA ELIMU YA TAIFA

August 06, 2026 Add Comment

Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye,akizungumza wakati akifungua kikao kazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, leo Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia,

Na.Mwandishi wetu-

Serikali imesisitiza kuwa ubora wa walimu wanaoandaliwa katika vyuo vya ualimu ndio utakaoamua mustakabali wa elimu nchini katika miaka ijayo.

Akifungua kikaokazi cha Wakuu wa Vyuo vya Ualimu vya Serikali na visivyo vya Serikali pamoja na Waratibu wa Taaluma jijini Dodoma, Agosti 6, 2026, kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mkurugenzi wa Uthibiti Ubora wa Shule, Dkt. Ephraim Simbeye, amewataka Wakuu wa vyuo kuimarisha usimamizi wa mafunzo ili kuhakikisha wahitimu wanakuwa na umahiri, maadili na stadi zinazokidhi mahitaji ya Taifa.

Ameongeza kuwa vyuo vya Ualimu vina jukumu kubwa katika utekelezaji wa mtaala kwa kuhakikisha walimu wanaohitimu wanakidhi viwango hitajika.

Dkt. Simbeye ameeleza kuwa kikaokazi hicho kimefanyika katika kipindi muafaka baada ya kukamilika kwa mzunguko wa kwanza wa wahitimu wa Mtaala Ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu ulioanza kutekelezwa mwaka 2023 na kusema kuwa hatua hiyo inatoa nafasi ya kutathmini mafanikio, changamoto na maeneo yanayohitaji maboresho.

Kiongozi huyo amesema kuwa Wakuu wa Vyuo wanapaswa kuwa wabunifu katika matumizi ya rasilimali. Ushirikiano na sekta binafsi pamoja na kuanzisha miradi ya uzalishaji mali bila kuathiri utoaji wa elimu.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kuzingatia miongozo ya Serikali katika utekelezaji wa mtaala, mafunzo kwa vitendo na utoaji wa mafunzo kwa njia ya masafa, ili kuhakikisha nchi inapata walimu wenye viwango vinavyofanana vya umahiri, maadili na uzalendo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Elimu ya Ualimu na Mafunzo, Mathias Mvula, amesema lengo la kikao kazi hicho ni kubadilishana uzoefu uliopatikana katika utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa wa Elimu ya Ualimu.

FCC YALETA MAGEUZI KATIKA BIASHARA KUPITIA ELIMU YA USHINDANI WA HAKI

FCC YALETA MAGEUZI KATIKA BIASHARA KUPITIA ELIMU YA USHINDANI WA HAKI

August 06, 2026 Add Comment

Serikali imewataka wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali nchini kutumia elimu ya ushindani wa haki na ulinzi wa mlaji kama nyenzo ya kuongeza thamani ya bidhaa zao, kupanua masoko na kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Hamad Chande, alipotembelea banda la Tume ya Ushindani (FCC) katika Maonesho ya 33 ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea jijini Nzuguni Dodoma.

Mhe Chande amesema elimu inayotolewa na FCC imekuwa na mchango mkubwa katika kuwajengea uwezo wazalishaji na wafanyabiashara kuzalisha bidhaa zenye ubora unaoweza kushindana katika soko la ndani na la kimataifa.

 "Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kujenga mazingira rafiki ya biashara yanayozingatia ushindani wa haki, fursa sawa kwa washiriki wa soko na ulinzi wa maslahi ya walaji. Msingi huo unachochea uwekezaji, huongeza tija katika uzalishaji na kuimarisha mchango wa sekta mbalimbali katika kukuza uchumi wa Taifa."amesema Mhe.Chande

Hata hivyo amewahimiza wakulima, wafugaji, wavuvi na wajasiriamali kutumia kikamilifu elimu inayotolewa na FCC kwa kuzingatia sheria za ushindani, kuepuka vitendo vinavyopotosha soko na kujikita katika uzalishaji wa bidhaa bora zenye kukidhi mahitaji ya walaji.

"Hatua hiyo itaongeza thamani ya mazao, kuinua kipato cha wazalishaji na kufungua fursa zaidi za biashara ndani na nje ya nchi."amesema 

Aidha, Naibu Waziri huyo ameipongeza FCC kwa kuendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kutoa elimu kwa umma kuhusu haki za walaji na ushindani wa haki, akieleza kuwa juhudi hizo zinaimarisha mazingira ya biashara yenye uwazi na usawa kwa manufaa ya wazalishaji na watumiaji wa bidhaa na huduma.

Amesisitiza kuwa Maonesho ya Nanenane yameendelea kuwa jukwaa muhimu la kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuwapa maarifa yatakayowawezesha kuongeza ubora wa mazao na bidhaa zao.

Ametoa rai kwa FCC kuendeleza kampeni za elimu nchini kote ili Watanzania wengi zaidi wanufaike na fursa zinazotokana na soko lenye ushindani wa haki na hivyo kuchangia kwa kiwango kikubwa maendeleo ya uchumi wa Taifa.