
Na Oscar Assenga, MUHEZA
MKUU wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dkt. Batilda Burian, amewataka wananchi 66 wa Kitongoji cha Bago Maisha Plus ,Kijiji cha Msakangoto, Kata ya Kigombe wilayani Muheza, kuondoka katika eneo walilokuwa wakiishi na kuhamia eneo jipya lililotengwa na Serikali ya Kijiji, huku akiahidi kuwa Serikali itaendelea kuwasaidia katika kipindi cha mpito.
Wananchi hao wamekumbwa na changamoto hiyo baada ya nyumba zao kubomolewa kufuatia utekelezaji wa amri ya mahakama iliyotokana na mgogoro wa umiliki wa eneo hilo.
Balozi Burian alitoa kauli hiyo leo alipofanya ziara katika eneo hilo na kukutana na wananchi hao, ambapo alisema Serikali haina mamlaka ya kuzuia utekelezaji wa amri ya mahakama.

Alisema baada ya kubaini kuwa eneo hilo lilikuwa ndani ya hati ya umiliki ya mwekezaji wa Mashamba ya Mkonge ambaye tayari alikuwa amefungua kesi mahakamani na kupata amri ya kuwaondoa wananchi, Serikali ililazimika kuheshimu uamuzi huo.
“Serikali haiwezi kupingana na sheria ya mahakama. Aliyekuja kubomoa alikuwa anatekeleza maelekezo ya mahakama. Hata hivyo, sisi kama Serikali tuliona ni lazima tuzungumze na wananchi na mwekezaji ili kutafuta suluhisho la kibinadamu,” alisema.
Alisema awali wananchi hao walipelekwa katika eneo hilo na Serikali ya Kijiji, huku wakiwa na vielelezo vilivyoonyesha kuwa waliruhusiwa kuishi katika eneo hilo, jambo lililopelekea Serikali ya Mkoa kuingilia kati baada ya mgogoro kujitokeza.
Balozi Burian alisema Serikali ya Mkoa imefanya mazungumzo na mwekezaji kupitia Wizara inayohusika na Uwekezaji, hatua iliyosaidia kuwezesha kupatikana kwa eneo jingine kwa ajili ya kuwahamishia wananchi hao.
Alisema eneo lililotengwa awali kwa ajili ya makazi mapya lilibainika kuwa halifai kutokana na kuwa na maji, hivyo Serikali ililazimika kutafuta eneo jingine.

“Wawakilishi wenu wamekuja ofisini kwangu mara tatu. Hatua ya kwanza ilikuwa kwenda kuzungumza na mwekezaji, hatua ya pili mwekezaji akakubali kutoa Sh200,000 na hatua nyingine ni kuhakikisha hakuna mtu anayewasumbua wakati taratibu za kuwahamisha zikikamilishwa,” alisema.
Balozi Burian alisema maturubai ambayo wanayatumia kwa muda wakati wakijiandaa kujenga makazi yao mapya.
“Kesho asubuhi tutahamisha maturubai hayo kwenda kwenye eneo ambalo mtaenda kuhamia. Mtayatumia kwa mwezi mmoja wakati mkiendelea kujipanga kujenga makazi yenu,” alisema.

Alisema Serikali itaendelea kutafuta wadau na wasamaria wema watakaoweza kusaidia katika ujenzi wa makazi mapya kwa wananchi hao.
Aidha, aliwataka wananchi hao kutokata tamaa na kuacha kuchukua hatua zinazoweza kuwaingiza katika mgogoro mwingine wa kisheria.

“Ndugu zangu, mchakato mzima nimewaeleza. Sina mamlaka ya juu zaidi ya hapa. Kila mhimili una kiwango chake cha kushughulikia jambo. Likishafika mahakamani, Serikali haiingilii tena,” alisema.
Alisema wananchi wanapaswa kuanza maisha katika eneo jipya huku wakiamini kuwa Serikali itaendelea kushirikiana nao katika kutafuta suluhisho la changamoto zinazowakabili.
Akizungumza kwa niaba ya wananchi hao, Ally Mohamed, mkazi wa Maisha Plus, alisema suala la fidia limekuwa miongoni mwa changamoto kubwa zilizowafanya kuwa na wasiwasi kuhusu kuhamia eneo jipya.

Alisema baadhi yao walitumia mafao waliyopata kutoka Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kujenga nyumba zao, hivyo kubomolewa kwa nyumba hizo kumewasababishia hasara kubwa.
“Baadhi yetu tulitumia mafao yetu ya NSSF kujenga nyumba. Sasa nyumba zimebomolewa na tunajiuliza tutaanzaje maisha upya,” alisema.
Akijibu suala hilo, Balozi Burian alisema wananchi waliokuwa na madai ya fidia wakati shauri likiendelea walikuwa na nafasi ya kuyawasilisha mahakamani.
Hata hivyo, alisema Serikali ya Mkoa imeendelea kufanya mazungumzo na mwekezaji kwa lengo la kutafuta namna ya kuwasaidia wananchi hao katika kipindi hiki cha mpito.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kigombe (CCM) Shahongwe Mgandi aliishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua iliyochukua, akisema viongozi wa kata watahakikisha wananchi hao wanapata usalama na huduma muhimu katika eneo jipya.
Alisema Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limeanza maandalizi ya kufikisha huduma ya umeme katika eneo hilo, ikiwa ni pamoja na kusimika nguzo.

Alisema pia maeneo ambayo wananchi hao watahamia yatatambuliwa kisheria na kutambuliwa kama kitongoji, huku Serikali ikiendelea kuboresha barabara na huduma nyingine muhimu.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Maisha Plus alishukuru Serikali ya Mkoa kwa hatua hiyo na kuiomba iruhusu wananchi hao, inapowezekana, kuhamisha baadhi ya miti waliyokwishaipanda katika eneo la awali ili kuitumia katika mazingira ya makazi mapya.
Hatua hiyo, alisema, itawasaidia wananchi hao kuanza maisha mapya huku wakitunza mazingira katika eneo watakalohamia.
