HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

DKT.BITEKO AMPONGEZA WAZIRI WA NISHATI KWA UONGOZI MAHIRI,AZINDUA JENGO JIPYA LA TANESCO BUKOMBE

August 03, 2026 Add Comment




Bukombe, Geita


Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Dkt. Doto Biteko, amempongeza Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, kwa uongozi wake mahiri na usimamizi mzuri wa sekta ya nishati, akisema utekelezaji wa miradi unaonyesha dhamira ya Serikali ya kutekeleza kwa vitendo maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.


Dkt. Biteko ametoa pongezi hizo leo Agosti 3, 2026 wakati wa uzinduzi rasmi wa jengo jipya la Ofisi ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Bukombe.

“Kwa kweli nampongeza sana Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Deogratias Ndejembi, pamoja na wasaidizi wake kwa jinsi wanavyofanya kazi kwa weledi na kujituma katika kutekeleza maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Dkt. Biteko.

Aidha, amemshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo zinazowezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuboresha huduma kwa wananchi nchini.


Amesema ujenzi wa jengo hilo ni ushahidi wa mafanikio ya Serikali katika kuimarisha utoaji wa huduma za umma na kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa TANESCO, jambo litakaloongeza ufanisi wa utoaji wa huduma kwa wananchi wa Bukombe na maeneo jirani.

Dkt. Biteko amesisitiza kuwa pamoja na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika sekta ya nishati na miundombinu ya huduma za umma, ni wajibu wa kila mtumishi kulinda na kutunza mali za umma ili ziendelee kutoa huduma bora kwa vizazi vya sasa na vijavyo.


“Tunzeni jengo letu jipya la TANESCO ili liendelee kutoa huduma bora kwa muda mrefu. Miundombinu hii imejengwa kwa gharama kubwa kwa manufaa ya wananchi, hivyo inahitaji kutunzwa na kulindwa wakati wote,” amesisitiza Dkt. Biteko.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe, Eng. Paskasi Muragili, amesema Serikali imeendelea kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta ya nishati ili kusogeza huduma karibu na wananchi, kuongeza upatikanaji wa umeme na kuchochea shughuli za kiuchumi pamoja na maendeleo ya jamii.


Naye Meneja wa TANESCO Wilaya ya Bukombe, Eng. Valerian Myula, amesema jengo hilo la kisasa limejengwa kwa fedha za ndani za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kwa gharama ya shilingi milioni 285, ikiwa ni sehemu ya jitihada za shirika hilo za kuendelea kuboresha huduma za umeme na kuongeza ufanisi wa kuwahudumia wananchi.

WAZIRI NDEJEMBI AONGOZA KIKAO MAALUM KUIMARISHA USALAMA WA UPATIKANAJI WA MAFUTA NCHINI

August 03, 2026 Add Comment



Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, leo Agosti 3, 2026 ameongoza kikao kazi cha pamoja na taasisi zinazoshughulikia sekta ya mafuta na gesi katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Nishati, jijini Dar es Salaam.


Lengo la kikao hicho lilikuwa kuweka mikakati madhubuti ya kuimarisha usalama wa upatikanaji na usambazaji wa mafuta nchini, sambamba na kuendelea kuhakikisha nchi inakuwa na akiba ya kutosha ya mafuta katika kipindi hiki cha mgogoro wa vita ya Mashariki ya kati kuliko pelekea kufungwa kwa mlango bahari wa Hormuz na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika soko la kimataifa.


Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio; Kamishna wa Mafuta, Bw. Godluck Shirima; Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Bw. Salum Mnuna; Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC, Bw. Mussa Makame; Mkurugenzi Mtendaji wa PBPA, Bw. Erasto Simon; pamoja na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati na taasisi zake.




NAIBU MTENDAJI SUMA JKT ATEMBELEA BANDA LA MALIASILI NANE NANE

August 03, 2026 Add Comment

     

📌Aipongeza Wizara kwa kushirikisha wadau wa mazao ya misitu na nyuki

📌Asema kazi ya uhifadhi inafanyika kwa weledi mkubwa

Na Neema Chalila Mbuja, Dodoma

NAIBU Mkurugenzi Mtendaji wa SUMA JKT  Brigedia Jenerali  Shija Lupi leo Agosti 03, 2026 ametembelea Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii kujionea wadau mbalimbali wanaoshirikiana na wizara kwenye uzalishaji wa bidhaa za misitu na asali na kuipongeza wizara kwa kushirikiana na wadau hao.

WIZARA YA NISHATI YAHAMASISHA WANANCHI KUTUMIA CNG KUTOKANA NA UNAFUU WAKE

August 03, 2026 Add Comment


Matumizi ya Gesi Asilia Iliyoshindiliwa (Compressed Natural Gas – CNG) kwenye vyombo vya usafiri yanaendelea kuwavutia wananchi kutokana na manufaa yake ya kiuchumi, huku kilo moja ya gesi hiyo ikiuzwa kwa Shilingi 1,550 pekee.

 Hayo yameelezwa na Mjiolojia Nuru Helambili kutoka Wizara ya Nishati wakati akitoa elimu kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Nishati katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni, jijini Dodoma.

Helambili amesema matumizi ya CNG husaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa vyombo vya usafiri na ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuhamasisha matumizi ya nishati safi, salama na yenye gharama nafuu kwa wananchi.

Aidha, amesema Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) imetenga Shilingi bilioni 22.06 katika Mwaka wa Fedha 2026/27 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vinavyohamishika vya kujazia gesi asilia (CNG Mobile Stations) vitakavyojengwa katika mikoa ya Dar es Salaam (vituo viwili), Morogoro (kituo kimoja) na Dodoma (vituo viwili).

Amesema ujenzi wa vituo hivyo unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za CNG nchini na kuchochea matumizi ya nishati hiyo katika sekta ya usafiri.

Wizara ya Nishati inaendelea kutumia Maonesho ya Nanenane kama jukwaa la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu miradi mbalimbali inayotekelezwa na Serikali kupitia Wizara na taasisi zake, kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu fursa na huduma zinazopatikana katika sekta ya nishati.



MAKAMU WA RAIS AVUTIWA NA MAFANIKIO YA UWEZESHAJI WA TADB

August 03, 2026 Add Comment
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi, ametembelea Banda la Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) akiwa ameambatana na Waziri wa Kilimo, Mhe. Daniel Chongolo, katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea kwenye Viwanja vya Mhe. John Malechela, Nzuguni – Dodoma.
WAZIRI SANGU: BANDARI YA UVUVI KILWA MASOKO KUFUNGUA FURSA ZA AJIRA KWA VIJANA

WAZIRI SANGU: BANDARI YA UVUVI KILWA MASOKO KUFUNGUA FURSA ZA AJIRA KWA VIJANA

August 03, 2026 Add Comment

Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu (aliyekaa) akikagua chumba maalum cha Kamera za Usalama na mifumo ya Mawasiliano alipofanya ziara katika Bandari ya Uvuvi iliyopo Kilwa Masoko, Mkoani Lindi Wakati wa Ziara ya Kikazi ya ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo leo Agosti 3, 2026.

Na. OWM (KAM) - Kilwa, Lindi

Vijana mkoani Lindi amewahimiza kuchangamkia fursa zitakazotokana na kukamilika kwa Mradi wa Kimkakati wa Bandari ya Uvuvi ya Kilwa Masoko ikiwemo ajira, biashara na masoko ya mazao ya uvuvi, ili kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya Taifa kwa ujumla.

Wito huo umetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu wakati akizungumza na wananchi wa Kilwa Masoko mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa bandari ya uvuvi iliyojengwa na serikali.

Mhe. Sangu amesema kuwa mradi huo ni fursa muhimu kwa wananchi kupata ajira akitaja jumla ya ajira 30,000 ambazo zitapatikana mara ujenzi utakapokamilika na kusema Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuona uchumi wa buluu ukichangia uchumi wa taifa.

" Kupitia bandari hii tumeona zaidi ya ajira 30,000 zitaenda kuzalishwa kwa kundi la vijana na wanachi wengine kutokana na bandari kuwa na uzalishaji wa zaidi ya tani 60,000 za samaki watakaovuliwa kwa mwaka" amesema Waziri Sangu.

Katika hatua nyingine Waziri Sangu amesema ujenzi wa bandari ya Kilwa ni utekelezaji wa Dira 2050 ambayo inaelekeza sekta binafsi kuchangia ukuaji wa uchumi ambapo serikali inakusudia kuzalisha ajira zaidi ya milioni nane (8).

Vile vile, ameongeza kuwa sekta ndogo ya uvuvi kwa sasa inachangia asilimia 2.2 ya pato la taifa ambapo lengo la Dira ya 2050 ni kufikia asilimia 9.8 .

Akiwasilisha taarifa ya mradi, Msimamizi wa mradi huo Mhandisi George Kwandu toka Wizara ya Mifugo na Uvuvi amesema ujenzi wa bandari ya uvuvi Kilwa Masoko umefikia asilimia 100 ambapo jumla ya shilingi bilioni 225 kati 280 zimetolewa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Kadhalika, amesema mradi huo umezalisha ajira 1,270 zilipatikana wakati wa ujenzi wa mradi huku ajira za moja kwa moja 300 zikitarajiwa wakati wa utekelezaji wa mradi na pia zaidi ya ajira 30,000 zitapatikana kipindi chote za mradi huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kilwa Mohamed Nyundo ameshukuru Serikali kwa kuona fursa ya bandari ya Kilwa Masoko na kuamua kutekekeleza mradi huo wa kimkakati ambao utakuwa na manufaa makubwa kwa wananchi wa mkoa huo na taifa kwa ujumla.

“Kilwa Masoko tayari imeanza kazi ya kuelimisha vijana kupitia makongamano ili watambue fursa za kiuchumi zitakazotokana na mradi huu wa bandari ya uvuvi,” amesema

Naye, Mbunge wa Kilwa Kusini Mhe. Hasnain Dewji amesema kukamilika kwa mradi huo wa bandari ya uvuvi kutavutia wafanyabiashara katika sekta ya uvuvi ambapo hadi sasa nchi mbalimbali ikiwemo Somalia, Kenya na Msumbiji tayari zimeonesha utayari wa kuja kutumia bandari hiyo.

Mbunge huyo pia, amesema manufaa mengine ya kukamilika kwa mradi huo ni kuongezeka kwa mapato ya ndani ya halmashauri kutoka shilingi Bilioni 10 za sasa hadi Bilioni 25.

Waziri Sangu ameanza ziara ya kikazi ya siku tano (5) ya kukakagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na serikali pamoja na kuzungumza na wananchi wa Mkoa wa Lindi.

Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu (aliyekaa) akikagua chumba maalum cha Kamera za Usalama na mifumo ya Mawasiliano alipofanya ziara katika Bandari ya Uvuvi iliyopo Kilwa Masoko, Mkoani Lindi Wakati wa Ziara ya Kikazi ya ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo leo Agosti 3, 2026.

Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Clement Sangu (aliyekaa) akikagua maeneo mbalimbali katika Bandari ya Uvuvi iliyopo Kilwa Masoko, Mkoani Lindi Wakati wa Ziara ya Kikazi ya ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo mkoani humo, leo Agosti 3, 2026

DC TABORA, KIGOMA, WAITAKA EWURA KUONGEZA HAMASA NISHATI SAFI, VITUO VYA MAFUTA VIJIJINI

DC TABORA, KIGOMA, WAITAKA EWURA KUONGEZA HAMASA NISHATI SAFI, VITUO VYA MAFUTA VIJIJINI

August 02, 2026 Add Comment

Meneja wa EWURA Kanda ya Magahribi, Mha. Karim Ally (kulia) akimweleza Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Mh. Upendo Wella (kushoto), Mamlaka inavyoendelea kutoa elimu na kuhamasisha ujenzi wa vituo maeneo ya vijijini ambapo uhitaji bado ni mkubwa hususan katika maeneo ya pembezoni na hivyo kuendelea kuwepo uuzaji holela wa bidhaa za petroli, ambao ni hatari kwa afya, mazingira na maisha ya watu, wakati kiongozi huyo alipotembelea banda la EWURA, katika maonesho ya NaneNane, viwanja vya Ipuli, Tabora, leo, 02/08/2026.

Na.Mwandishi Wetu-Tabora

Wakuu wa Wilaya za Tabora, Mh. Upendo Wella, na Kigoma, Mh. Dkt. Rashid Chuachua, wameipongeza EWURA kwa usimamizi mzuri wa huduma za nishati na maji nchini. Wametoa pongezi hizo walipotembelea banda la EWURA, katika maonesho ya NaneNane yanayoendelea viwanja vya Ipuli, Tabora, leo, 02.08.2026.

Viongozi hao wameitaka EWURA kuongeza hamasa kwa wananchi ili kubadili mtazamo na kuhamia katika matumizi ya nishati safi ya kupikia ili azma ya kufikia 80% ya watumiaji ifikapo 2034 itimie.

Aidha, wameisisitiza EWURA kuendelea kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta maeneo ya vijijini, wakieleza kuwa huduma hiyo inahitajika kutokana na kushamiri shughuli za kilimo, ufugaji na uvuvi.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magharibi, Mha. Karim Ally, alitumia fursa hiyo kueleza nafasi ya EWURA ya kuweka mazingira wezeshi ya kupata wasambazaji wakubwa wa gesi ya mitungi (LPG) katika eneo la Kanda ya Magharibi linalohudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Katavi na Kigoma, ambapo kwa sasa ni 19 pekee.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magaharibi, Mha. Karim Ally(kushoto) akitoa maelezo ya majukumu yanayotekelezwa na Mamlaka kwa Mkuu wa Wilaya ya Kigoma, Mh. Dkt. Rashid Chuachua(kulia) ikiwemo utoaji wa leseni na vibali vya ujenzi wa vituo vya mafuta, vituo vya CNG, utatuzi wa migogoro na malalamiko na nafasi ya EWURA katika kuweka mazingira wezeshi ya kupata wasambazaji wakubwa wa gesi ya mitungi ( LPG) katika eneo la Kanda ya Magharibi linalohudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Katavi na Kigoma, wakati kuongozi huyo alipotembelea banda la EWURA katika maonesho ya NaneNane yanayoendelea viwanja vya Ipuli, Tabora, leo 02/08/2026.

Meneja wa EWURA Kanda ya Magahribi, Mha. Karim Ally(kulia) akimweleza Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Mh. Upendo Wella (kushoto), Mamlaka inavyoendelea kutoa elimu na kuhamasisha ujenzi wa vituo maeneo ya vijijini ambapo uhitaji bado ni mkubwa hususan katika maeneo ya pembezoni na hivyo kuendelea kuwepo uuzaji holela wa bidhaa za petroli, ambao ni hatari kwa afya, mazingira na maisha ya watu, wakati kiongozi huyo alipotembelea banda la EWURA, katika maonesho ya NaneNane, viwanja vya Ipuli, Tabora, leo, 02/08/2026.

TEKNOLOJIA NA UBUNIFU KUWA MSINGI WA MAGEUZI YA ELIMU

August 02, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SERIKALI itaendelea kuwekeza katika maendeleo ya kitaaluma ya walimu, wakufunzi na wahadhiri kupitia mafunzo endelevu, tafiti na matumizi ya teknolojia za kisasa ili kuhakikisha mfumo wa elimu unazalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya soko la ajira na uchumi wa kidijitali.

PSSSF KUTOA HUDUMA NA ELIMU MAONESHO YA NANENANE 2026 KATIKA KANDA TANO ,IKIWEMO ZANZIBAR

August 02, 2026 Add Comment


AFISA Kumbukumbu za Wanachama wa Mfuko wa PSSSF Bw.Alex Bwanakunu (kulia) akimsikiliza mwananchi aliyetembelea Banda la PSSSF kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Ziwa Magharibi yanayofanyika uwanja wa Nyamhongolo Jijini Mwanza Agosi 2,2026


Dodoma, Agosti 2, 2026

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) unashiriki katika Maonesho ya Nanenane 2026 kwa kutoa huduma mbalimbali na elimu kuhusu Hifadhi ya Jamii  kwa wanachama wake na wananchi kupitia mabanda yake yaliyopo katika kanda tano nchini, ikiwemo Zanzibar.

Msanii maarufu nchini ,Mrisho Mpoto (wa pili kushoto) akiwa ameshika mkanda ,moja ya bidhaa zinazozalishwa katika kiwanda cha KLICL,Kinachomilikiwa na PSSSF kwa ushirikiano na Jeshi la Magereza ,alipotembelea Banda la Mfuko wa PSSSF kwenye maonesho ya Nanenane yanayofanyika Kitaifa kwenye viwanja vya Nzunguni Jijini Dodoma Agosti 2,2026,kushoto ni Afisa Mkuu wa Uhusiano wa Mfuko wa PSSSF Bw.Abdul Njaidi na kulia ni Afisa Mauzo kiwanda cha KLICL ,Bi,Mary Muna    


Kwa mujibu wa Afisa Uhusiano Mkuu wa Mfuko wa PSSSF, Bw. Abdul Njaidi, PSSSF imeshiriki maonesho hayo katika Kanda ya Kati viwanja vya Nanenane mkoani Dodoma, ambako Maonesho ya Nanenane 2026 yanafanyika kitaifa na tayari yamezinduliwa na Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, Agosti 1, 2026. Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘Tambua Soko; Ongeza Tija na Thamani ya Kuelekea Dira 2025’.



Wanachama wa Mfuko wa PSSSF wakihudumiwa kwenye Banda la Mfuko huo kwenye Maonesho ya Nanenane yanayofanyika Kitaifa kwenye viwanja vya Nzunguni Jijini Dodoma Agosti2,2026

Katika maonesho ya mwaka huu, PSSSF inashiriki; Zanzibar katika viwanja vya Dole, Kanda ya Magharibi mkoani Tabora katika viwanja vya Ipuli Mnadani, Kanda ya Ziwa jijini Mwanza katika viwanja vya Nyamhungolo, Kanda ya Kusini mkoani Lindi katika viwanja vya Ngongo na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini jijini Mbeya, viwanja vya Nanenane.

Afisa Matekelezo wa Mfuko wa PSSSF Bi.Esther Mpemba (kulia ) akimuunganisha Mwanachama wa PSSSF ,Bi.Maliasa Sajoho na Mfumo wa PSSSF Member Portal ambao unamuwezesha kupata huduma za mfuko Kidijitali,kwenye maonesho ya Nanenane Viwanja vya Nzunguni Jijini Dodoma Agosti 2,2026


"Tunawakaribisha wanachama wetu na wananchi wote kutembelea mabanda ya PSSSF katika kanda hizo ili kupata huduma mbalimbali ikiwa ni pamoja na elimu kuhusu mafao, kuhakiki taarifa zao na michango, pamoja na kuwaunganisha katika huduma zetu za kidijitali, huku tukiwahakikisha kesho ya uhakika wanachama wetu’" alisema Bw. Njaidi.



Afisa Huduma kwa Wateja wa Mfuko wa PSSSF ,Bi .Saluna Ally (kushoto) akimuhudumia Mstaafu anayepokea Pensheni PSSSF ,Bw.Mwakibete G.Kasilati,kwenye banda la mfuko huu katika  maonesho ya Nanenane Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwenye viwanja vya Nanenane Jijini Mbeya,Agosti 2,2026

Aidha, watakaotembelea kwenye mabanda ya PSSSF watapata nafasi ya kuona fursa za uwekezaji wa Mfuko ambazo ni pamoja na bidhaa za ngozi zinazotengenezwa na Kiwanda cha KLICL na nyama kutoka machinjio ya Kimataifa ya Nguru.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt Mwigulu Nchemba akitoa hotuba ya ufunguzi wa Maonesho ya Nanenane Kitaifa katika viwanja vya Nzunguni Jijini Dodoma Agosti 1,2026

Meneja wa PSSSF Kanda ya Magharibi Bw.Eliadi Mndeme akitoa elimu kwa mwanachama wa PSSSF wakati wa Maonesho ya Nanenane Kanda ya Magharibi ambayo yanafanyika viwanja vya Ipuli mkoani Tabora Agosti 2,2026

Mwisho.

MZUMBE YATOA USHAURI WA UCHAGUZI WA KOZI KATIKA KAMBI YA UDAHILI MLIMANI CITY

August 02, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

CHUO Kikuu Mzumbe kimewahimiza wanafunzi na wazazi kutumia fursa ya kambi maalumu ya udahili inayoendelea katika viwanja vya Mlimani City ili kupata ushauri wa kitaaluma na kufanya maamuzi sahihi kuhusu uchaguzi wa kozi za masomo ya juu.

MKAKATI WA BARRICK WA KUWEKEZA KUPATA WATAALAMU WA TASNIA YA MADINI WAUNGWA MKONO NA WANAZUONI NA WADAU KATIKA SEKTA

August 02, 2026 Add Comment
Washiriki wakifuatilia mada mbalimbali wakati wa mdahalo huo
Wadau mbalimbali katika sekta ya madini nchini walioshiriki katika mkutano wa wa jukwaa la tano la utekelezaji na ushirikishwaji wa watanzania katika sekta ya madini uliomalizika jijini Mwanza wametoka na maazimio mbalimbali mojawapo likiwa ni kuwekeza kupata rasilimali watu wenye ujuzi wa kisasa kwendana na mabadiliko ya sayansi na teknolojia na ukuaji wa sekta kama ambavyo kampuni ya Barrick nchini yenye ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga tayari imeanza kutekeleza.

Standard Chartered Foundation Yatoa TZS Milioni 21.4 Kuwezesha Wanawake Kiuchumi Kupitia Programu ya Mabinti ya CCBRT

August 02, 2026 Add Comment

 

Standard Chartered Foundation, kupitia Standard Chartered Tanzania, imetoa mchango wa TZS 21,456,431.52 kwa ajili ya kuunga mkono Programu ya Mabinti ya CCBRT, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya Benki ya kuendelea kukuza ujumuishaji wa kiuchumi na kuongeza fursa kwa makundi yaliyo katika mazingira magumu nchini Tanzania.

Mchango huo utagharamia programu ya wiki sita itakayowanufaisha wanawake 40 kupitia mafunzo ya stadi za kazi, usimamizi wa biashara na elimu ya fedha, pamoja na ununuzi wa mashine za kushona zitakazowawezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli za kujiongezea kipato.

Kupitia ufadhili huo, washiriki watapatiwa mafunzo ya ushonaji wa bidhaa za crochet, urembaji wa nguo (embroidery), usimamizi wa biashara na elimu ya fedha. Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea wanawake ujuzi wa vitendo na maarifa ya ujasiriamali yatakayowawezesha kujitegemea kiuchumi. Aidha, mashine za kushona zitakazonunuliwa kupitia mchango huo zitawasaidia kuongeza uzalishaji na kipato baada ya kuhitimu mafunzo.

Programu ya Mabinti inayotekelezwa na CCBRT inawalenga wanawake walio katika mazingira magumu, wakiwemo wanawake wenye ulemavu, manusura wa fistula ya uzazi, wasichana walioacha shule na wanawake wanaokabiliwa na changamoto za kiuchumi na kijamii. Kupitia mafunzo ya ujuzi na usaidizi wa ujasiriamali, programu hiyo inawawezesha wanawake kujitegemea kifedha na kuboresha maisha yao.

Ushirikiano huu unaendelea kudhihirisha dhamira ya Standard Chartered ya kuwekeza katika maendeleo ya jamii inazohudumia. Mapema mwaka huu, katika kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake, wafanyakazi wa Standard Chartered Tanzania walitembelea Kituo cha Mabinti na kukabidhi mashine 12 za kushona pamoja na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanufaika wa programu hiyo. Hatua hiyo ilionesha dhamira ya Benki ya kuwawezesha wanawake kupitia msaada wa vitendo na kuwajengea uwezo.

Mchango huu pia umetolewa katika mwaka ambao Standard Chartered inaadhimisha miaka 20 ya Mpango wa Kujitolea wa Wafanyakazi, unaotambua mchango wa wafanyakazi wake ambao kwa kipindi cha miongo miwili wamekuwa wakitumia muda, ujuzi na uzoefu wao kuleta mabadiliko chanya katika jamii duniani.

Akizungumza kuhusu mchango huo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Tanzania, Geofrey Mchangila, alisema:

"Tunajivunia kuendeleza ushirikiano wetu na CCBRT katika kuunga mkono Programu ya Mabinti ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika kuwawezesha wanawake. Hii ni mara ya pili kushirikiana na CCBRT. Mapema mwaka huu, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wanawake, timu yetu ilitembelea kituo hicho, ambapo tulikabidhi mashine 12 za kushona na kutoa mafunzo ya elimu ya fedha kwa wanawake wanaoshiriki katika programu hiyo.

Leo tunaimarisha zaidi dhamira yetu kwa kutoa TZS milioni 21.4 kwa ajili ya kugharamia mafunzo ya stadi za kazi, usimamizi wa biashara na fedha kwa wanawake 40, pamoja na ununuzi wa mashine zaidi za kushona. Tunaamini kuwa programu kama hii zinawapa wanawake ujuzi, maarifa na rasilimali muhimu za kujenga maisha ya kujitegemea na mustakabali wenye fursa zaidi."

Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Tanzania, Geofrey Mchangila akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la CCBRT Brenda Msangi mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi  (TZS) 21,456,431.52 kwa ajili ya kuunga mkono Programu ya Mabinti ya CCBRT, ikiwa ni sehemu ya dhamira ya Benki ya kuendelea kukuza ujumuishaji wa kiuchumi na kuongeza fursa kwa makundi yaliyo katika mazingira magumu nchini Tanzania.

Mchango huo utagharamia programu ya wiki sita itakayowanufaisha wanawake 40 kupitia mafunzo ya stadi za kazi, usimamizi wa biashara na elimu ya fedha, pamoja na ununuzi wa mashine za kushona zitakazowawezesha kuanzisha na kuendeleza shughuli za kujiongezea kipato.
Afisa Mtendaji Mkuu na Mkuu wa Kitengo cha Coverage wa Standard Chartered Tanzania, Geofrey Mchangila akioneshwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la CCBRT Brenda Msangi baadhi ya bidhaa zinazotengenezwa na baadhi ya Wanawake waliopo kwenye taasisi hiyo.



WAZIRI KAPINGA: UWEKEZAJI WA AZANIA GROUP UTAONGEZA AJIRA NA KUKUZA UCHUMI WA TAIFA

August 02, 2026 Add Comment
Serikali imeipongeza Azania Group kwa kutimiza miaka 25 ya mafanikio katika sekta ya viwanda na biashara, huku ikieleza kuwa kampuni hiyo imeendelea kuwa mfano wa uwekezaji wa wazawa baada ya kutangaza mpango wa kuwekeza zaidi ya Shilingi trilioni moja katika miradi mbalimbali ya uzalishaji nchini.

KAPINGA: WAKULIMA WASIZALISHE BILA UHAKIKA WA SOKO

August 02, 2026 Add Comment
Serikali yaweka mkakati wa kuondoa tatizo la wakulima kuvuna mazao bila kuwa na uhakika wa soko, ikisisitiza kuwa kuanzia sasa uzalishaji wa mazao, mifugo na uvuvi unapaswa kuongozwa na mahitaji ya soko badala ya utaratibu wa kuzalisha kwanza na kuanza kutafuta wanunuzi baada ya mavuno.

KATIBU MKUU CCM AONGOZA KIKAO CHA SEKRETERIETI YA HALMASHAURI KUU YA CCM

August 01, 2026 Add Comment


Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro, akiongoza Kikao cha Sekreterieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, wakati wa kuwapokea na kuwatambulisha wajumbe walioteuliwa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), hivi karibuni. Katika kikao hicho kilichofanyika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam, leo Jumamosi, tarehe 1 Agosti 2026, pia Balozi Dkt. Migiro alishuhudia makabidhiano ya ofisi na majukumu kati ya viongozi wapya na wanaoondoka 

Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Bara, Ndugu Aggrey Mwanri akipokewa na kusalimiana kwa tabasamu na bashasha na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Ndugu John Mongella, leo Jumamosi, tarehe 1 Agosti 2026, Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam, wakati wa mapokezi ya Wajumbe wa Sekreterieti ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, walioteuliwa hivi karibuni.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dkt. Asha-Rose Migiro (katikati) akishuhudia makabidhiano ya ofisi na majukumu, kati ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Komredi Aggrey Mwanri (kushoto pichani) na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CCM Bara, Komredi John Mongella (kulia pichani), yaliyofanyika Ofisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Lumumba, jijini Dar Es Salaam, leo Jumamosi, tarehe 1 Agosti 2026.





TFC YAHAMASISHA MATUMIZI YA MBOLEA KWA TIJA YA KILIMO

TFC YAHAMASISHA MATUMIZI YA MBOLEA KWA TIJA YA KILIMO

August 01, 2026 Add Comment

Mkurugenzi wa Uendeshaji Biashara wa Kampuni ya Mbolea Tanzania, Lameck Borega,akizungumza na waandishi wa habari kwenye Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt.John Samuel Malecela jijini Dodoma.

Na.Alex Sonna-DODOMA

Kampuni ya Mbolea Tanzania (TFC) imewahimiza wakulima nchini kuachana na dhana potofu kuhusu matumizi ya mbolea, ikisisitiza kuwa kilimo cha kisasa kinahitaji matumizi sahihi ya mbolea ili kuongeza uzalishaji na tija mashambani.

Wito huo umetolewa na Mkurugenzi wa Uendeshaji Biashara wa Kampuni ya Mbolea Tanzania, Lameck Borega, wakati wa Maonesho ya 49 ya Kilimo ya Nane Nane yanayoendelea kitaifa katika viwanja vya Dkt.John Samuel Malecela jijini Dodoma.

Bw.Borega amesema TFC, ambayo inamilikiwa kwa asilimia 100 na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imefika katika maonesho hayo ikiwa na lengo la kutoa elimu kwa wakulima kuhusu umuhimu wa kutumia mbolea bora na zinazokidhi mahitaji ya mazao pamoja na aina mbalimbali za udongo.

Amesema kampuni hiyo inasambaza mbolea za aina mbalimbali ikiwemo DAP kwa ajili ya kupandia, Urea na CAN kwa ukuaji wa mazao, pamoja na NPK na SA zinazosaidia kukomaza mazao, huku akisisitiza kuwa uchaguzi wa mbolea unapaswa kuzingatia mahitaji halisi ya udongo na zao husika.

"Kilimo bila mbolea ni kilimo kisicho na tija. Ili mkulima apate mavuno mengi na yenye ubora ni lazima atumie mbolea sahihi," amesema Borega.

Amefafanua kuwa maafisa wa TFC wanaendelea kuwafikia wakulima katika mikoa yote nchini kwa kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya mbolea, sambamba na kuwasaidia kuelewa aina za mbolea zinazofaa kwa maeneo yao.

Aidha, amesema maonesho ya Nane Nane yamekuwa jukwaa muhimu la kuonesha tofauti ya uzalishaji kati ya mashamba yanayotumia mbolea na yale yasiyotumia kupitia mashamba darasa (demo plots) yaliyoandaliwa na kampuni hiyo.

"Anayetembelea banda letu anaweza kujionea mwenyewe tofauti ya ukuaji wa mazao yaliyotumia mbolea na yale ambayo hayajatumia. Huo ni ushahidi wa moja kwa moja wa faida za matumizi ya mbolea," amesema

Borega pia amewataka wakulima kupuuza imani kwamba mbolea huharibu udongo, akieleza kuwa udongo hutofautiana kwa kiwango cha virutubisho na kwamba mbolea huongeza virutubisho vinavyokuwa vimepungua kutokana na matumizi ya muda mrefu na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Amekumbusha kuwa Kampuni ya Mbolea Tanzania ilianzishwa mwaka 1968, miaka minane baada ya Uhuru, ikiwa na dhamira ya kuhakikisha wakulima wanapata mbolea bora kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa mazao na kuimarisha usalama wa chakula nchini.

"Tunawaalika wakulima wote kutembelea banda letu katika maonesho ya Nane Nane na kufika katika vituo vyetu vilivyopo nchini kote ili kupata mbolea bora zilizothibitishwa na mamlaka husika kwa ajili ya kilimo chenye tija," amesema  Borega.

POMBE YA MITISHAMBA YAZUA GUMZO!

August 01, 2026 Add Comment

 

Dar es Salaam | 31 Julai 2026

Kwa wiki kadhaa, swali moja limekuwa likiulizwa kila sehemu—mitandaoni, kwenye WhatsApp, hata pale unapokutana na marafiki kwenye baa.

Watu wamekuwa wakiuliza: "Kwa nini mitishamba inazungumzwa sana hivi karibuni?"

WAZIRI SANGU ASISITIZA NIDHAMU NA UADILIFU KWA BODI YA WADHAMINI PSSSF

August 01, 2026 Add Comment
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, akizungumza wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa HIfadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) jijini Dar es Salaam, Agosti 1, 2026.


Ataka Uwekezaji wenye Tija

Na: Mwandishi Wetu - Dar eÅ› Salaam 

Bodi ya Wadhamini wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) imeelekezwa kutekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali ili kuhakikisha mfuko unaendelea kuwa imara, endelevu na wenye uwezo wa kutoa huduma bora kwa wanachama.

Amesema hayo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Deus Sangu wakati wa hafla ya uzinduzi wa Bodi ya Mfuko huo wa PSSSF iliyofanyika leo Agosti 1, 2026, PSSSF Commercial Complex, Jijini Dar es Salaam.

Aidha, Mhe. Sangu amesema jukumu kuu la bodi ni kusimamia shughuli za mfuko kama ilivyoainishwa katika Sheria ya PSSSF, kifungu cha 11 hususan katika maeneo makuu ya usimamizi ikiwemo huduma kwa wanachama, ukusanyaji wa michango, uwekezaji wa rasilimali za mfuko na ulipaji wa mafao.


Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu (Katikati) akibonyeza kitufe kuashiria uzinduzi wa Bodi ya Wadhamini ya Mfuko wa PSSSF jijini Dar es Salaam Agosti 1, 2026

Vile vile, amesisitiza kuwa katika kutekeleza majukumu hayo, bodi inapaswa kuzingatia kikamilifu sheria, kanuni na miongozo ya Serikali pamoja na Mpango Mkakati wa PSSSF, ambao umeanza kutekelezwa pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

“Wajumbe mmeingia katika kipindi muhimu ambapo mfuko umeanza kutekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano. Huu ndio utakaokuwa mwongozo wa utekelezaji wa majukumu na kufanikisha malengo ya mfuko,” amesema.



Kadhalika, amewataka wajumbe kuzingatia misingi ya uadilifu, uwajibikaji, uwazi na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yao, akibainisha kuwa Serikali ina matarajio makubwa kwa PSSSF katika kuhakikisha mfuko huo unakuwa imara.

Kuhusu uwekezaji, Waziri alisema fedha za wanachama zinapaswa kuwekezwa kwa umakini na weledi ili kulinda thamani yake na kuhakikisha zinazalisha faida itakayowezesha mfuko kutimiza wajibu wa kulipa mafao kwa wakati, hata baada ya miongo kadhaa.

Viongozi waliohudhuria hafla hiyo


“Fedha za wanachama zinawekwa leo kwa matarajio ya kulipa mafao miaka ijayo. Hivyo, ni muhimu ziwekezwe katika miradi yenye tija, salama na inayozingatia miongozo ya uwekezaji iliyowekwa na Serikali,” alisisitiza.

Viongozi waliohudhuria hafla hiyo