HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

SERIKALI YAONGEZA NGUVU KATIKA MIKAKATI YA KUHAKIKISHA UPATIKANAJI ENDELEVU WA MAFUTA NCHINI

March 28, 2026 Add Comment

Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratias Ndejembi amekutana na kufanya mazungumzo na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Nishati  zinashughuliki mafuta na gesi nchini katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es salaam.


Kikao hicho kilichofanyika leo, tarehe 28 Machi 2026, ni sehemu ya juhudi za Serikali kuendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha usalama na upatikanaji wa mafuta.

Uhaba wa mafuta unaoshuhudiwa unatokana na changamoto za usambazaji katika soko la kimataifa, zilizochochewa na vita inayoendelea katika ukanda wa Mashariki ya Kati. 

Hali hiyo imeathiri njia muhimu za usafirishaji wa mafuta, ikiwemo kupungua kwa upitishaji wa shehena kupitia Mlango wa Bahari wa Hormuz, jambo lililosababisha kucheleweshwa kwa usafirishaji na hatimaye kupungua kwa upatikanaji wa mafuta katika baadhi ya maeneo.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, Kamishna wa Mafuta na Gesi, Bw. Goodluck Shirima, Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt. James Mwainyekule, Mkurugenzi Mtendaji wa TPDC Bw. Musa Makame, Mtendaji Mkuu wa PBPA Bw. Erasto Simon na wataalamu kutoka Wizara ya Nishati kwa lengo la kupokea taarifa ya hali ya upatikanaji wa mafuta nchini.

TANZANIA YANG’ARA KIMATAIFA KWA USIMAMIZI BORA WA DENI LA SERIKALI

March 28, 2026 Add Comment

  Na Joseph Mahumi, WF


Serikali ya Tanzania imeendelea kung’ara katika jukwaa la kimataifa baada ya kuibuka mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.

Ushindi huo mkubwa unatokana na juhudi za Serikali katika kuimarisha mifumo ya usimamizi wa deni la umma, ikiwemo kuunganisha vyema mifumo ya kifedha ya Serikali na kuboresha upatikanaji wa rasilimali fedha kwa ajili ya maendeleo, ambapo Jopo huru la wataalamu lililochambua mawasilisho kutoka nchi mbalimbali za Jumuiya ya Madola lilizingatia vigezo vya ubunifu, uimara na uendelevu katika kutoa tuzo hizo.

Akifungua hafla ya utoaji tuzo hizo, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal, alisisitiza umuhimu wa nchi wanachama kuendelea kubuni mbinu madhubuti za kusimamia deni la umma ili kulinda uchumi dhidi ya misukosuko ya kifedha duniani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola, Bi. Ruth Kattumuri, aliipongeza Tanzania kwa mageuzi makubwa iliyoyafanya katika kuimarisha usimamizi wa deni la umma.

Alieleza kuwa mafanikio hayo ni kielelezo cha dhamira ya dhati ya nchi katika kujenga uchumi imara na unaostahimili mishtuko ya kiuchumi.

Aidha, Bi. Kattumuri, alisema kuwa Sekretarieti ya Jumuiya ya Madola itaendelea kuisaidia Tanzania katika juhudi zake za kuboresha sera na mifumo ya usimamizi wa deni, sambamba na utekelezaji wa maazimio ya Kikao cha 72 cha Kundi la Mawaziri wa Jumuiya ya Madola.

Mkutano huo wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola uliofanyika kwa muda wa wiki moja uliwakutanisha wataalamu wa usimamizi wa deni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola kwa lengo la kubadilishana uzoefu, kujifunza na kujadili mbinu bora za kukopa, kusimamia na kulipa deni la umma, na umeandaliwa ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Jumuiya ya Madola wa Deni Imara, Bunifu na Endelevu, ambapo Tanzania imejitokeza kama kinara na mfano wa kuigwa barani Afrika na katika Jumuiya nzima ya Madola.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) akiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola, Bw. Tanmaya Lal (kushoto) na  Mkurugenzi Mkuu Mwandamizi wa Idara ya Uchumi, Maendeleo, Biashara na Uwekezaji wa Sekretarieti ya Jumuiya hiyo, Bi. Ruth Kattumuri.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama, akionesha tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza.
Kamishna Msaidizi Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Omary Khama (Katikati) Aakiwa ameshika tuzo mbili ambazo Tanzania imepata kwa kuibuka Mshindi wa jumla wa mwaka katika Tuzo za Usimamizi wa Deni la Umma za Jumuiya ya Madola na Tuzo ya Ofisi Bora Kanda ya Afrika kupitia Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha (Debt Management Division), ambazo zilitangazwa tarehe 26 Machi 2026 wakati wa Mkutano wa Jukwaa la Jumuiya ya Madola kuhusu Usimamizi wa Deni la Umma, uliofanyika jijini London, nchini Uingereza. Wengine katika picha ni washindi wenngine wa tuzo hizo kutoka nchi ya Barbados ambayo iliibuka mshindi wa Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Caribbean na Sri Lanka Msimamizi bora wa deni katika ukanda wa nchi za Asia.

FCC, TBS wakutana na wadau wa Pombe kutatua changamoto bidhaa hafifu na bandia

March 28, 2026 Add Comment
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) kwa kushirikiana na Tume ya Ushindani (FCC) wamekutana na wadau wa bidhaa za pombe nchini kwa lengo la kuwajengea uelewa juu ya matakwa ya sheria, kanuni na viwango vinavyosimamia sekta hiyo.

WAZIRI WA NISHATI AKABIDHI VITENDEA KAZI KWA TANESCO MKOA WA SHINYANGA

March 28, 2026 Add Comment



Na Mwandishi Wetu, Kahama


Naibu Waziri wa Nishati Mh. Salome Makamba amekabidhi vitendea kazi vya usafiri kwa TANESCO Mkoa wa Shinyanga kwa lengo la kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi na kutatua changamoto zao kwa haraka.

Akizungumza tarehe 27, Machi 2026 wakati wa hafla ya kukakabidhi vitendea kazi hivyo iliyofanyika katika Manispaa ya Kahama Mkaoni Shinyaga Mhe. Salome amesema hatua hiyo ya kukabidhi vitendea kazi hivyo ni kuyaishi maono ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za Umeme wa uhakika.

WAZIRI NDEJEMBI NA WAZIRI CHIKOTE WA ZAMBIA WAJADILI USHIRIKIANO SEKTA YA NISHATI

March 27, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Nishati wa Zambia, Mhe. Makozo Chikote, leo tarehe 27 Machi 2026 katika Jiji la Lusaka, Zambia.

Katika kikao hicho kilichowashirikisha wataalam kutoka nchi hizo mbili, Viongozi hao wamejadili masuala mbalimbali yaliyolenga kuimarisha na kuendeleza ushirikiano katika sekta ya nishati, hususan sekta ndogo ya mafuta na gesi.

Kikao hicho kimehudhuriwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Mafuta na Gesi, Dkt. James Mataragio, Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Luteni Jeneral Mathew Edward Mkingule pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Nishati na taasisi zilizo chini yake.

Tanzania na Zambia zimekuwa na historia ya ushirikiano wa karibu katika sekta ya nishati, ikiwemo usimamizi na matumizi ya Bomba la Mafuta la TAZAMA, ambalo ni kiungo muhimu katika usafirishaji wa mafuta kutoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda Zambia.


Ushirikiano huo umeendelea kuchangia kuimarika kwa usalama wa nishati na kukuza uchumi wa nchi zote mbili.

KUTOKA KUNI HADI GESI :JANGWANI SEC NA DIAMOND PRIMARY ZAPIGA HATUA KUBWA NISHATI SAFI

March 27, 2026 Add Comment


Serikali imezidi kusisitiza matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa taasisi za umma, huku Shule ya Sekondari Jangwani na Shule ya Msingi Diamond jijini Dar es Salaam zikiwa miongoni mwa Taasisi za mfano kwa utekelezaji wa ajenda hiyo muhimu ya kitaifa.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa mifumo ya nishati safi Machi 26, 2026, Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu Wizara ya Nishati, Mhandisi Innocent Luoga, alizitaka taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100 kwa siku kuachana na kuni na mkaa, na badala yake kutumia teknolojia safi za kupikia.

Alieleza kuwa hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi (2024–2034), unaolenga kuhakikisha asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034, chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan


“Ninaziomba sekta binafsi ziungane na Serikali katika kufanikisha mkakati huu mkubwa wa miaka kumi, ambao tayari umeanza kuleta matokeo chanya katika taasisi mbalimbali,” alisema Luoga.

Katika ziara hiyo, alibainisha kuwa mifumo ya nishati safi hiyo imewezeshwa kupitia programu ya CookFund inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya, tayari imeanza kusambazwa katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma na Mwanza. Hadi sasa, taasisi 45 zikiwemo shule, hospitali na vyuo vikuu zimefungiwa mifumo hiyo ya kisasa.

Aidha, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imeingia makubaliano na taasisi za umma kama Magereza na Jeshi la Wananchi ili kuhakikisha wanatumia nishati safi ya kupikia.

Mhandisi Luoga amesisitiza kuwa matumizi ya nishati safi yameleta manufaa makubwa, ikiwemo kupunguza gharama za uendeshaji, kulinda mazingira kwa kupunguza hewa ukaa, pamoja na kuboresha afya za wapishi.

Alitoa pongezi kwa Umoja wa Ulaya kupitia mradi wa CookFund kwa mchango wao, akieleza kuwa juhudi zinaendelea kupanua mradi huo ili kufikia taasisi nyingi zaidi nchini.



BALOZI KAGANDA ASHIRIKI MDAHALO WA VIONGOZI WAANDAMIZI ZIMBABWE, AELEZA MCHANGO WA TANZANIA KIKANDA

March 27, 2026 Add Comment


Balozi wa Tanzania nchini Zimbabwe, Kamishna wa Polisi (CP) Suzan Kaganda, ameshiriki mdahalo wa viongozi waandamizi uliofanyika katika Chuo Kikuu cha Zimbabwe, jijini Harare ambapo Mdahalo huo ulikuwa na kaulimbiu isemayo “Uhuru wa Kimkakati: Kusawazisha Maslahi ya Afrika katika Mabadiliko ya Kijiografia na Kisiasa.”

Mdahalo huo uliwakutanisha viongozi waandamizi wa Serikali ya Zimbabwe, wanadiplomasia, wachumi na wanasiasa kutoka maeneo mbalimbali nchini humo, Washiriki walipata fursa ya kubadilishana uzoefu na kujadili mikakati ya kulinda na kuendeleza maslahi ya bara la Afrika katika mazingira ya mabadiliko ya kisiasa na kiuchumi duniani.

Katika mdahalo huo, Mheshimiwa Kaganda aliwasilisha mada kuhusu mchango wa Tanzania katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda kupitia uanachama wake katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) na Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), akieleza kuwa Tanzania imeendelea kuwa mhimili muhimu katika kukuza mshikamano wa kikanda na maendeleo ya pamoja barani Afrika.

Aidha, alibainisha kuwa Tanzania imekuwa mfano bora kwa nchi wanachama wa SADC kwa kuwekeza katika ujenzi wa miundombinu ya kisasa ambapo aliitaja miradi hiyo kama vile barabara, reli ya kisasa (SGR), pamoja na upanuzi wa bandari kuwa imeongeza ufanisi wa usafirishaji na kuifanya Tanzania kuwa lango muhimu la biashara katika ukanda wa Kusini mwa Afrika.

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Kaganda alifanya mazungumzo na Kaimu Mkuu wa Idara ya Elimu na Utafiti wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA), Profesa Maulid Matawala, ambaye yuko nchini Zimbabwe kwa ziara ya kikazi. Mazungumzo yao yalijikita katika kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu ya juu kati ya Tanzania na Zimbabwe.

Vilevile Profesa Matawala anatarajiwa kukutana na viongozi wa vyuo vikuu mbalimbali vya Zimbabwe, ikiwemo Chuo Kikuu cha Zimbabwe (UZ), kwa lengo la kujadili fursa za ushirikiano katika elimu, utafiti na ubadilishanaji wa wataalamu.


FANYENI KAZI KWA BIDII, UPENDO NA USHIRIKIANO KUBORESHA UTOAJI HUDUMA KWA WANANCHI - PROF. SHEMDOE

March 27, 2026 Add Comment





Na OWM – TAMISEMI, Dodoma


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM– TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amewataka watumishi wa OWM- TAMISEMI kufanya kazi kwa bidii, upendo, ushirikiano, pamoja na ubunifu katika utendaji wao ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.


Prof. Shemdoe ametoa wito huo jana Machi 26, 2026 wakati akifungua
Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa OWM– TAMISEMI uliofanyika Jijini Dodoma.


Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa baraza hilo litumike kama jukwaa muhimu la kuimarisha mshikamano miongoni mwa watumishi na kuleta ushirikiano kati ya menejimenti na wafanyakazi katika utekelezaji wa majukumu ya taasisi.


“Baraza hili lina nafasi kubwa ya kukuza upendo na ushirikiano ili kuongeza ufanisi katika utendaji wa kazi zetu za kila siku,” amesema Prof. Shemdoe.


Prof. Shemdoe amesisitiza kuwa mabaraza ya wafanyakazi yameanzishwa kwa mujibu wa sheria kwa lengo la kushughulikia masuala ya msingi mahali pa kazi, ikiwa ni pamoja na utatuzi wa migogoro, maslahi ya watumishi, na kuboresha mazingira ya kazi. Aidha, amewataka watumishi kuzingatia haki, wajibu pamoja na maadili ya Utumishi wa Umma.


Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe amewahimiza wajumbe wa baraza hilo kujadili kwa kina mpango na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27 kwa kuzingatia vipaumbele vya taasisi, akisisitiza kuwa usimamizi madhubuti wa utekelezaji wake ni nguzo muhimu ya kufikia malengo yaliyokusudiwa.


Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Sinyamule, amesema mabaraza ya wafanyakazi yameendelea kuwa kiunganishi muhimu kati ya uongozi na watumishi, huku akiwapongeza wajumbe kwa juhudi zao katika kuboresha utendaji kazi.


Awali, akitoa neno la utangulizi, Mwenyekiti wa Baraza hilo ambaye pia ni Katibu Mkuu wa OWM- TAMISEMI, Bw. Adolf Nduguru amesema mabaraza ya wafanyakazi ni vyombo vya kisheria vinavyolenga kuongeza tija, uwajibikaji, na kutoa fursa kwa watumishi kujadili masuala muhimu yanayohusu utendaji wao pamoja na maslahi yao.


Naye, mmoja wa wajumbe wa baraza hilo Bw. Elias Mabele, amesema anayo imani kubwa kuwa baraza hilo litafanya kazi ya kuboresha bajeti ya OWM- TAMISEMI pamoja na Tasisi zake ili kupeleka tabasamu kwa wananchi hususan katika sekta zinazosimamiwa na Ofisi ya OWM-TAMISEMI kama Elimu, Afya, Miundombinu pamoja na Utawala Bora.








BODI YA WAKURUGENZI BONDE LA PANGANI WATEMBELEA VYANZO VYA MAJI MABAYANI TANGA

March 27, 2026 Add Comment






Na Oscar Assenga, TANGA


BODI ya Wakurugenzi ya Bonde la Pangani leo wamefanya ziara ya kukagua maeneo vyanzo vya maji ikiwemo Bwawa la Mabayani na Mtambo wa Kutibu Maji wa Mowe na kujiridhisha kuhusiana na kazi zinazotelezwa na menejimenti pamoja na wateja wao namna wanavyopokea huduma.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Bonde la Pangani,Mhandisi Ruth Koya alisema kwamba bodi hiyo na menejimenti wamefanya ziara hiyo kwa ajili ya kufuatilia utekelezaji wa maelekezo na majukumu wanayowalekeza menejimenti kwamba wanayafuatilia na kuyafanya kwa uhakika.

Katika ziara hiyo Bodi hiyo wametembelea Bwawa la mabayani wamejionea shughuli Zinazofanyika ikiwemo utunzwaji wa Bwawa la mabayani pamoja na kumtembelea mteja wao mkubwa Tanga Uwasa wameona yupo vizuri na kazi inafanyika kwa waledi

Alisema kwamba wameona bwawa limewekwa alama na wameipokea taarifa kwamba wananchi nao wanashirikishwa kutokana na uwepo wa jumuiya za watumia maji ambao wamekuwa chachu kubwa kuhakikisha vyanzo hivyo vinalindwa na kutunzwa.

Aidha alitoa wito kwa watumishi na kusisitiza kuwasimamia wadau wao wakiwemo Tanga Uwasa ili kuendelea kutunza chanzo cha maji kikubwa ambacho ni muhimu kwa ajili ya Jiji la Tanga na kushirikiana na wadau Tanga Uwasa na wengineo .

Alisema kwamba lakini wamepata taarifa Tanga Uwasa wanazidi kupanua uzalishaji maji hadi kufikia lita milioni 70 ina maana utunzaji ni nzuri ndio maana wameweza kuwekeza zaidi kupitia hat fungani yao walioipata hivi karibuni.

Awali akizungumza Mkurugenzi wa Bonde la Pangani Segule segule alisema kwamba ziara ya Bodi hiyo ni kutembelea maeneo ya uwandani na kukakgua maeneneo mbalimbali na kujiridhisha kuhusiana na kazi zinazotekelzwa na menejimenti lakini kupata kujua kuhusu wateja wao mbalimbali wanavyopokea huduma zao.

Alisema kwamba bodi imeona ipite kwenye eneo la mnufaika mkubwa wa maji Mto Zigi ambao ni wenzao wa Tanga Uwasa ambapo wametembelea maeneo mbalimbali ambayo Tanga Uwasa wanafaidika nayo wamenza ikiwemo Bwawa la Mabayani ambalo wao ndio wamiliki na yeye ndio mteja wao.

Aidha alisema kwamba wamejionea mazingira yanavyotunzwa na wametumia fursa hiyo kupata maelekezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Tanga Uwasa kuhusiana na mradi wa Hati Funfani ambao unatumia chanzo kwa ajili ya kuboresha huduma ya maji Tanga .

Alieleza kwamba na ziara ilitoa fursa kwa wajumbe wa bodi,menejimenti kuona mchango wao kama bonde mchango wao kwenye mradi Hatifungani kwamba wakitunza vyanzo vyema wenzao wa Tanga Uwasa wataweza fikia matarajio yao na kwa gharama walizokadiria.

Aliongeza kwamba bwawa hilo wanalitunza na moja walishaanza kuweka alama za mipaka kuainisha mita 500 na kama sheria za usimamizi rasilimali za maji zinaelekeza mita 60 za chanzo lakini wanatoa mamlaka kwa taasisi na wao kama mabonde kuomba nyongeza kwa bwawa la mabayani wamehifadhi mita 500 .

Alieleza kwa sasa hiyo inatoa fursa hata nyongeza za miradi kutokana na mahitaji ya maji wanaweza kuhifadhi hivyo mkakakati wao ni kuendelea kuimraisha baada ya kuweka alama za mipaka katika yale maeneo walioweka mipaka watu wasifanye shughuli za kibinadamu ili kupunguza uchafuzi kwenda kwenye bwawa.

Aliongeza kwamba lakini upande wa juu wa bwawa wanaendelea kuimarisha utunzaji wa jumuiya za watumiaji maji ambao wote wanakuwa watumiaji maji na mkakati wa kuziimarisha huku wenzao Tanga Uwasa wameimarisha utunzaji wa vyanzo vya maji .

Hata hivyo alisema kwamb hali ya vyanzo vya maji ukilinganisha na miaka ya nyuma ni nzuri changamoto zipo lakini hawajafika wakati wa kusema hali iliyopo imehataraisha vyanzo kukauka na kushindwa kuwahudumua watu.

Aliongeza kwamba lazima waendelee kuimarisha na shughuli zinaongezeka kutokana na mahitaji ya ardhi kuna jitihada kubwa za watu kutokana na uhaba wa ardhi na watu wanaongezeka na kutaka kusogelea vyanzo wao wanaendelea kuimarisha jumuiya za watumiaji maji ili kuweza kuhakikisha vyanzo vya maji vilivyopo vinatunzwa na kuvilindwa.

Naye kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Tanga Uwasa Mhandisi Geofrey Hilly alisema kwamba ameshiriki katika ziara hiyo ya Bodi ya Bonde la Pangani ambao wanatembelea kuangalia vyanzo vya maji vinavyotunzwa ikiwemo bwawa la mabayani ambalo ndio chanzo kikubwa wanachotumia Tanga Uwasa katika kusambaza maji kinahudumia Tanga, Muheza na Mkinga .

Mhandisi Hilly alisema wameongeza uzalishaji wa maji kuhakikisha wanawafikia vema wananchi ili kutekeleza malengo yao mbalimbali ya nchi ifikapo 2030 watu wote wawe wamepata maji mijini na Tanga Uwasa na wenzao Ruwasa wananchi waweze kupata maji.

Alisema kwa hiyo mahitaji na matumizi ni makubwa wao kwa kushirikiana na Bodi la Bonde la Mto Pangani wanaweka juhudi kubwa katika utunzaji chanzo cha maji kutokana na kuwa wanufaika wakubwa wa bonde hilo.

Alieleza hivyo wana wajibu kuhakikisha chanzo hicho kinalindwa na kutunzwa wanashirikiana kwenye maeneo mbalimbali ya mto,bwawa la mabayani wana mpaka kamati za uhifadhi na utunzaji wa mazingira ikiwemo uwamakizi kuhakikisha vinaendelea kuwa imara.

“Kwa mfano mradi wa hati fungani miongoni mwa fedha zinakwenda kwenye chanzo cha maji na sasa wana mkakati wa kupanda miti laki moja katika maeneo hayo na mpaka sasa wamepanda miti zaidi 50,000”Alisema

Hata hvyo alieleza pia wameendelea na mradi wa hati fungani kuongeza uzalishaji maji huku wakieleza mipango yao ni kuongeza uwezo bwawa tuta eneo la kupita utoro wa maji na kazi za mazingira zitafanyika na hivyyo itawasadia kuwa na uhakika wa usambazaji wa maji hata ikitokea mabadiliko ya tabia ya nchi na wakati wa ukame.



Mwisho.




 FCC YATIA MKAZO HAKI ZA MLAJI KATIKA SEKTA YA FEDHA

FCC YATIA MKAZO HAKI ZA MLAJI KATIKA SEKTA YA FEDHA

March 27, 2026 Add Comment

TUME  ya Ushindani (FCC) kupitia Kanda ya Ziwa imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kwa kutoa elimu ya ulinzi wa mlaji kupitia Kliniki ya Mlaji inayofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mkendo, Manispaa ya Musoma.

Katika kuimarisha uelewa wa wadau mbalimbali, FCC haikuishia kwa wananchi pekee bali pia ilifanya ziara maalum kwa baadhi ya taasisi zinazotoa huduma ndogo za fedha katika manispaa hiyo, kwa lengo la kuzielimisha juu ya wajibu wao wa kuzingatia sheria na kanuni katika utoaji wa huduma.

Akiongoza zoezi hilo, Mkuu wa Kanda ya Ziwa,Bw. Frank Mdimi, akishirikiana na Afisa Biashara wa Manispaa ya Musoma, Joshua Mlole pamoja na maafisa wengine, walitembelea taasisi za Enokwe, Pongeza na Ohura na kufanya mazungumzo ya moja kwa moja na watoa huduma hao.

Katika ziara hiyo, maafisa wa FCC wamesisitiza umuhimu wa kuandaa mikataba ya huduma kwa uwazi na haki, wakielekeza taasisi hizo kuzingatia matakwa ya  Sheria ya Ushindani inasimamia na kudhibiti Mikataba ya Mlaji inayoandaliwa na watoa huduma

Watoa huduma kutoka taasisi hizo walionesha utayari mkubwa wa kupokea maelekezo hayo, wakieleza kufurahishwa kwao na hatua ya FCC kuwafuata na kuwapatia elimu kwa vitendo. Wamesisitiza kuwa elimu hiyo itawasaidia kuboresha huduma zao na kujenga uaminifu kwa wateja wao.

Aidha, taasisi hizo zimeahidi kushirikiana kwa karibu na FCC kwa kuhakikisha zinazingatia sheria, kanuni na miongozo ya Serikali, pamoja na kudumisha mawasiliano ya mara kwa mara ili kuboresha zaidi sekta ya huduma ndogo za fedha.

Zoezi la utoaji elimu kupitia Kliniki ya Mlaji linaendelea Machi 27, ambapo wananchi wataendelea kupatiwa elimu kuhusu haki zao, wajibu wao na namna bora ya kujilinda wanapotumia huduma mbalimbali sokoni.