HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

SERIKALI YAWEKA MKAKATI WA KUPUNGUZA MUDA WA MELI ZA MAFUTA BANDARINI

August 15, 2026 Add Comment




DAR ES SALAAM. 


Serikali imeweka mkakati wa kupunguza muda ambao meli za mafuta hutumia bandarini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuongeza ufanisi katika upokeaji, uhifadhi na usambazaji wa bidhaa za mafuta nchini.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, anayeshughulikia Mafuta na Gesi Dkt. James Mataragio, amesema hayo wakati wa ziara ya kukagua miundombinu ya mafuta katika eneo la Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Tanzania International Petroleum Reserves Limited (TIPER), Leo Augosti 14,2026 Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mataragio amesema Serikali inalenga kuhakikisha meli zinazowasili nchini zinapata huduma kwa wakati, zinashusha mafuta kwa ufanisi na kuondoka bandarini bila ucheleweshaji usio wa lazima.

“Ni matarajio ya Serikali kuona meli zikifika, zinashusha mafuta na kuondoka. Kila taasisi inapaswa kufahamu jukumu lake na kujipanga ipasavyo,” amesema.


Ameeleza kuwa moja ya changamoto zinazochangia meli kukaa bandarini kwa muda mrefu ni kasi ndogo ya upokeaji na uondoshwaji wa mafuta katika baadhi ya maghala binafsi. Hali hiyo husababisha meli kusubiri na kuongeza msongamano bandarini.

Kutokana na changamoto hiyo, Dkt. Mataragio ameutaka Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA) kuimarisha usimamizi wa wamiliki wa maghala binafsi na kuhakikisha wanaweka miundombinu inayokidhi mahitaji ya uendeshaji.


Amesema wamiliki wa maghala wanapaswa kuboresha pampu na vifaa vingine vinavyotumika kupokea mafuta, hasa vinapokuwa vimechakaa au havina uwezo unaohitajika.



Kwa mujibu wa Dkt. Mataragio, ucheleweshaji wa meli bandarini huongeza gharama za uendeshaji, zikiwemo gharama za meli kusubiri, ambazo hatimaye zinaweza kuathiri bei ya mafuta kwa mwananchi.


Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa PBPA, Bw. Erasto Simon, amesema taasisi hiyo itakutana na wadau muhimu katika sekta ya mafuta, wakiwemo kampuni za uuzaji wa mafuta (OMCs) na TPA, kwa ajili ya kupitia na kuboresha Mwongozo wa Taratibu za Uendeshaji (Standard Operating Procedure Manual).


Amesema mapitio hayo yanalenga kuweka wazi majukumu, muda wa utekelezaji na uwajibikaji wa kila mdau katika mchakato wa upokeaji na uhamishaji wa mafuta.


Hatua hiyo inatarajiwa kuimarisha uratibu kati ya meli na maghala ya kupokea mafuta, kupunguza muda wa meli kukaa bandarini na kudhibiti gharama zinazotokana na ucheleweshaji.


Katika ziara hiyo, Dkt. Mataragio aliambatana na Kamishna wa Mafuta kutoka Wizara ya Nishati, Bw. Goodluck Shirima; Mtendaji Mkuu wa PBPA, Bw. Erasto Simon; Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam, Bw. Abed Gallus Abed; pamoja, Meneja wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) Kanda ya Mashariki, Mhandisi Lorivii Long’idu na wataalam kutoka Wizara ya Nishati.

TAASISI ZAIDI YA 300 KUSHIRIKI WIKI YA ELIMU, UBUNIFU NA UJUZI TANGA

August 14, 2026 Add Comment
Wananchi wa Mkoa wa Tanga na mikoa jirani wanahamasishwa kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ubunifu na Ujuzi, itakayofanyika kuanzia tarehe 15 - 24 Agosti 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga, ili kujifunza, kubadilishana maarifa na kutumia fursa mbalimbali za elimu, ujuzi na ubunifu.

ORYX GAS ZANZIBAR YANOGESHA TAMASHA LA KIZIMKAZI,YAKABIDHI MITUNGI YA GESI 200

August 14, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu ,Zanzibar

ORYX Gas Zanzibar imeeleza hatua mbalimbali inazochukua kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia na katika Tamasha la Kizimkazi kampuni hiyo imetoa mitungi ya gesi 200 huku mkakati kwasasa ni kutoa majenerata yanatotumia gesi ya LPG katika hoteli na viwanda visiwani Zanzibar.
TANGA YAWAITA WANANCHI KUTUMIA FURSA ZA ELIMU, UJUZI NA TEKNOLOJIA

TANGA YAWAITA WANANCHI KUTUMIA FURSA ZA ELIMU, UJUZI NA TEKNOLOJIA

August 14, 2026 Add Comment

Wananchi wa Mkoa wa Tanga na mikoa jirani wanahamasishwa kushiriki katika Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ubunifu na Ujuzi, itakayofanyika kuanzia tarehe 15 - 24 Agosti 2026 katika viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga, ili kujifunza, kubadilishana maarifa na kutumia fursa mbalimbali za elimu, ujuzi na ubunifu.

Akizungumza Agosti 14, 2026, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Rashid Kassim Mchata, amesema maonyesho hayo yatashirikisha taasisi zaidi ya 300 pamoja na wadau wa sekta ya elimu, sayansi na teknolojia. Aidha, kutakuwa na mashindano ya ubunifu na ujuzi katika fani mbalimbali ikiwemo ushonaji, ususi, umeme na mengineyo, ambapo washindi wa kitaifa watapata nafasi ya kushiriki mashindano ya kimataifa.

Mchata ameongeza kuwa wadhamini mbalimbali wakiwemo mabenki wamejitokeza kudhamini miradi ya ubunifu na kuunga mkono wajasiriamali chipukizi.

Kwa upande wake, Prof. Ladislaus Mnyone, Mkurugenzi wa Idara ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, alisema lengo kuu la wiki hiyo ni kuwaleta pamoja wadau kujadili na kuweka mikakati ya pamoja kuhusu elimu, ujuzi na ubunifu.

Amebainisha kuwa matukio makuu yatakuwa ni maonesho ya teknolojia yanayoonyesha mchango wa sayansi katika sekta mbalimbali, pamoja na kongamano la elimu na ubunifu litakalojadili utekelezaji wa Dira 2050.

Prof. Mnyone amefafanua kuwa kongamano hilo litaangazia nyenzo tano kuu: utafiti na maendeleo, sayansi na ubunifu, teknolojia za kidijitali, nishati, na usafirishaji funganishi.

Kupitia mijadala na maonesho hayo, Wizara inalenga kufanikisha malengo ya taifa ikiwemo kufikia uchumi wa dola trilioni 1 ifikapo mwaka 2050, kipato cha wastani cha mtu mmoja kati ya Dola za Marekani 7,000 - 12,000, na ajira zenye staha kwa angalau asilimia 50 ya Watanzania.

WATUMISHI WA WIZARA WATEMBELEA OFISI ZA UBALOZI WA TANZANIA NCHINI INDIA

August 14, 2026 Add Comment
Watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki wanaohudhuria mafunzo maalum ya diplomasia nchini India wametembelea Ofisi za Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jijini New Delhi.

KIRITA AAGIZA KASI MRADI WA MAJI KAHAMA–USHETU: “TUTEMBEE NA MAJI”

August 13, 2026 Add Comment

 

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akizungumza katika moja ya matanki ya maji, Kata ya Ulowa, Halmashauri ya Ushetu.  Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akiwa ameambatana na wataalamu mbalimbali katika moja ya matanki ya maji, Kata ya Ulowa, Halmashauri ya Ushetu.
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akiwa ameambatana na wataalamu mbalimbali katika moja ya matanki ya maji wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa mradi wa maji Kahama - Ushetu. 
Meneja Mradi kutoka RUWASA, John Msengi akieleza kuhusu utekelezaji wa mradi wa maji Kahama–Ushetu.
Muonekano wa sehemu ya mabomba katika mradi wa maji Kahama–Ushetu
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akizungumza wakati wa ziara katika Mradi wa Maji Kahama - Ushetu.

Na Kadama Malunde – Malunde 1 Blog

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mhandisi Wolta Kirita, amewataka Mameneja wa RUWASA ngazi ya mikoa na wilaya kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maji unaenda sambamba na upatikanaji wa huduma, akisisitiza falsafa ya “kutembea na maji” kuwa kipaumbele katika utekelezaji wa miradi hiyo.

RAIS SAMIA AWEKA JIWE LA MSINGI LA SKULI YA SEKONDARI YA UFUNDI KIZIMKAZI

August 13, 2026 Add Comment
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameweka jiwe la msingi na kupanda mti katika Skuli ya Sekondari ya Ufundi Kizimkazi Mkunguni, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.
NAIBU WAZIRI NISHATI AHAMASISHA UMMA KUPATA TAARIFA SAHIHI KUHUSU SEKTA NDOGO YA UMEME

NAIBU WAZIRI NISHATI AHAMASISHA UMMA KUPATA TAARIFA SAHIHI KUHUSU SEKTA NDOGO YA UMEME

August 13, 2026 Add Comment

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, amehimiza umma kupata taarifa sahihi kuhusu hali ya sekta ndogo ya umeme nchini, huku akitoa wito kwa Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuendelea kutoa elimu na taarifa kwa wananchi kuhusu jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali katika kuboresha huduma za umeme.

Mhe. Makamba ametoa wito huo leo, tarehe 13 Agosti 2026, alipotembelea banda la EWURA katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, amesema ni muhimu wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu kuongezeka kwa uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini na hivyo kukidhi mahitaji tuliyonayo.

“Gharama ya umeme nchini Tanzania ni nafuu ikilinganishwa na nchi jirani, na Serikali inaendelea na juhudi za kuboresha na kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi nchini,” aliongeza.

Katika banda la EWURA, Mhe. Makamba alifahamishwa Mamlaka imetumia fursa ya Maonesho hayo kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya udhibiti ikiwemo mikataba ya huduma kwa wateja, matumizi sahihi na salama ya huduma za bidhaa za gesi ya mitungi, gesi asilia, umeme na maji, fursa za uwekezaji katika sekta na mengineyo.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akisaini kitabu  mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

NAIBU WAZIRI MAKAMBA AITAA PBPA KUENDELEA KUTOA ELIMU KWA UMMA

August 13, 2026 Add Comment

 



Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (Mb.), ameitaka Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) kuendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma ili wananchi wawe na uelewa mpana kuhusu majukumu ya Wakala na mchango wake katika kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Mhe. Makamba ametoa wito huo alipotembelea banda la PBPA katika maonesho yanayofanyika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya Tamasha la Kizimkazi 2026.

Amesema ni muhimu wananchi wakaendelea kuelimishwa kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja na namna PBPA inavyotekeleza majukumu yake katika kusimamia uagizaji wa bidhaa za mafuta kwa lengo la kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa hiyo muhimu.


Aidha, Mhe. Makamba ameipongeza PBPA kwa utendaji wake katika kutekeleza majukumu yake na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Mwitazy, amemweleza Naibu Waziri kuwa Wakala unaendelea kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha nchi inakuwa na kiwango cha kutosha cha mafuta ili kukidhi mahitaji ya soko.

Bw. Mwitazy amesema ushiriki wa PBPA katika Tamasha la Kizimkazi umetoa fursa kwa wananchi na wadau mbalimbali kupata elimu na ufafanuzi kuhusu majukumu ya Wakala pamoja na namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unavyofanya kazi.


Ameongeza kuwa PBPA inaendelea kudumisha ushirikiano mzuri na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) katika masuala yanayohusu sekta ya mafuta.


Tamasha la Kizimkazi 2026, ambalo ni msimu wa tatu, linafanyika kuanzia Agosti 12 hadi 14, 2026, likiwa na lengo la kuibua na kufungua fursa mbalimbali za maendeleo, huku likibeba kaulimbiu “Kizimkazi 2026, Fursa na Shangwe.”

KIZIMKAZI 2026: WIZARA YA NISHATI YAENDELEA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI

August 13, 2026 Add Comment


Wataalam wa Wizara ya Nishati wanaendelea kutoa elimu na ufafanuzi kwa wananchi wanaotembelea Banda la Wizara na taasisi zake katika Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026, yanayofanyika Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Wananchi wanapata fursa ya kufahamu shughuli, miradi na huduma mbalimbali zinazotekelezwa katika sekta ya nishati, ikiwemo masuala ya umeme, mafuta, gesi asilia na nishati safi ya kupikia.


Karibu tukuhudumie.



DKT.DOTO BiTEKO ANOGESHA MASHINDANO YA NGALAWA TAMASHA KIZIMKAZI

August 13, 2026 Add Comment




Naibu Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko amesema kuwa mashindano ya ngalawa race ni miongoni mwa matukio makubwa ya kiburudani yanayoipamba Kizimkazi Festival 2026.


Mashindano hayo yamefanyika Kizimkazi, Kusini Unguja Agosti 12, 2026 yaliyokuwa na ushindani mkubwa ambapo Nassor Pandu wa Mkunguni ameibuka mshindi wa mashindano ya ngalawa ikiwa ni sehemu ya shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Tamasha la Kizimkazi.

“ Ni dhahiri kwamba mashindano haya yamekuwa muhimu kwa vijana na jamii kwa ujumla. Tukio hili limewaleta pamoja wadau mbalimbali na kuchangia kwa kiasi kikubwa juhudi za kuboresha mazingira ya michezo na burudani,” amesema Dkt. Biteko.

Dkt. Biteko ameongeza kuwa mashindano ya Ngalawa race Kizimkazi Festival yameendelea kutoa fursa za kiuchumi kwa vijana mbalimbali katika kushindana hadi kupata timu mbili bora za Mchangamle na Mkunguni ambapo kila timu imehusisha manahodha 10.



Mwisho.

KAPINGA: SERIKALI YALENGA HUDUMA ZA AFYA KUMFIKIA KILA MWANANCHI

August 13, 2026 Add Comment
Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.
WAZIRI KAPINGA AHAIDI KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA MTWARA

WAZIRI KAPINGA AHAIDI KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA MTWARA

August 13, 2026 Add Comment

Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.

Hayo yamejiri, katika siku ya tatu ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), mkoani humo, yenye lengo la kukagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Wananchi hao wamesema wanapata huduma za afya kwa wakati na kwa urahisi, jambo walilolieleza kuwa limepunguza changamoto ya kufuata matibabu katika maeneo ya mbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Kapinga amesema Serikali inalenga kuboresha huduma za afya ili wananchi wapate matibabu kwa urahisi na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji, hivyo kuimarisha uchumi wa familia na Taifa.

Amesema kusogeza huduma za afya karibu na wananchi ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu kwa wakati.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa ushirikiano ni msingi wa maendeleo.

Katika siku ya tatu ya ziara hiyo, Waziri Kapinga ametembelea miradi mbalimbali katika Majimbo ya Nanyamba, Mtwara Mjini na Mtwara Vijijini, ikiwemo kuzindua Kituo cha Afya Msangamkuu, kuzindua mabweni mawili na kutoa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule ya Wasichana Mtwara, kukagua ujenzi wa Shule ya Amali Chikota, pamoja na kutembelea Wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba.