Na Mwandishi wa diGOtv, Tanga
WAZIRI wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Musa Omar (Mb) anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi katika hafla kubwa na ya kihistoria ya ugawaji wa miguu bandia 100 kwa watu wenye ulemavu mkoani Tanga, iliyoandaliwa na Ofisi ya Mbunge wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Mhandisi Mwanaisha Ulenge.
Hafla hiyo kubwa inatarajiwa kufanyika *Jumanne, tarehe 14 Julai 2026*, katika ukumbi wa *Regal Naivera* jijini Tanga kuanzia saa 2:00 asubuhi.
Hatua hii inamfanya Mhe. Mhandisi Ulenge kuweka rekodi ya kuwa Mbunge wa kwanza mkoani Tanga kufanya shughuli kubwa za kijamii na kugusa maisha ya watu moja kwa moja tangu kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu mwaka jana. Utendaji huu unaendelea kumuweka karibu zaidi na makundi mbalimbali mkoani humo kutokana na utu wake na dhamira ya dhati ya kulipa fadhila kwa kura nyingi alizopigiwa.
Akizungumzia msukumo wake wa kuandaa tukio hilo linalogusa maisha ya wanyonge, Mhe. Ulenge ameweka wazi kuwa yeye ni mtumishi wa wananchi na anachokifanya ni kurudisha fadhila kwao.
"Hii nafasi niliyokuwa nayo ni ya watu. Kurejesha kidogo ninachopata pamoja na wadau wangu ni jambo kubwa kwangu, kwa sababu watu ndiyo walionifikisha hapa," alisema Mhe. Ulenge kwa hisia.
*Mafunzo ya Sheria ya Asilimia 30 (Manunuzi ya Umma)*
Ukiachilia mbali zoezi la ugawaji wa miguu hiyo bandia ili kuwarudishia uwezo wa kutembea, hafla hiyo itakwenda sambamba na utoaji wa mafunzo maalum kwa makundi maalum (Vijana, Wanawake, na Watu wenye Ulemavu).
Kwa kuwa Mgeni Rasmi ni Waziri wa Fedha anayesimamia sera za kiuchumi, mafunzo hayo yatalenga kuwajengea uwezo washiriki namna ya kunufaika na *Sheria ya asilimia 30 (30%) ya Manunuzi ya Umma*. Lengo ni kuwapa uelewa utakaowawezesha kupata zabuni za kiserikali na kujikwamua kiuchumi badala ya kutegemea misaada pekee.
Wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo wanaendelea kupongeza hatua hii ya Mhe. Ulenge, huku maandalizi ya kumpokea Waziri wa Fedha na kukamilisha zoezi hili yakiwa yamepamba moto jijini Tanga.


































