HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

WANDONDI, WANDWEWE WATOA WITO WA KULINDA MAISHA NA AMANI

Kajunason August 10, 2026 Add Comment


Na Mwandishi Wetu.

JAMII ya Wandondi na Wandwewe, imetoa mwito wa kitaifa na kimataifa kwa watu wote wenye nia njema kuungana katika Dua Maalum kwa ajili ya Amani, Umoja, Maridhiano, Mshikamano na Ulinzi wa Maisha ya Binadamu.

Dua hiyo ni mwito wa pamoja unaolenga kuwakutanisha watu wa imani, mila, tamaduni na mitazamo mbalimbali katika kusimama kwa pamoja kutetea amani, utu, uhai, mshikamano na heshima kwa mwanadamu, bila kujali tofauti za dini, kabila, rangi, taifa, utamaduni, itikadi au hali ya kijamii.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Chifu Felix G. L. Mfunda, kwa niaba ya jamii ya Wandondi na Wandwewe amesema dua hiyo itafanyika  Agosti 12, 2026,  ambapo Misa Maalumu ya Kikatoliki itafanyika katika Kanisa Katoliki, Kigango cha Mhangazi, Parokia ya Kitanda, Namtumbo, Ruvuma. huku akitoa  mwito wa amani na maridhiano.

Aidha, kuanzia jioni ya Agosti 13 hadi mchana wa Agosti 14, 2026, kutafanyika dua, na shughuli za jadi zitakazoambatana na ngoma na sanaa mbalimbali za asili za Wandwele na Wandondi.

Jamii mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma, zikiwemo Makumbo, Lizombe na Makiwa, zinatarajiwa kushiriki katika shughuli hizo zinazolenga kuenzi urithi wa tamaduni, kuimarisha undugu na mshikamano, pamoja na kukuza amani kati ya jamii.

Mfululizo huo utakamilishwa Agosti 16, 2026, kwa Dua Maalumu ya Kiislamu itakayofanyika jioni kwa ajili ya kuiombea Tanzania, Afrika na dunia nzima.
Ambapo  amesema Dunia ya leo inakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo migogoro, vita, chuki, migawanyiko ya kijamii, changamoto za kiuchumi, ukosefu wa usawa na athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Katika mazingira haya, tunapaswa kutambua kwamba amani si wajibu wa Serikali pekee; ni wajibu wa kila mwanadamu.Tunatoa mwito kwa viongozi wa kitaifa na kimataifa, viongozi wa dini, viongozi wa kimila, wasomi, vijana, wanawake, mashirika ya kiraia na wananchi wote kutumia nafasi zao kujenga madaraja ya maelewano badala ya kuta za migawanyiko.

“Tunasisitiza umuhimu wa mazungumzo, kusikilizana, kusameheana, kuheshimiana na kutafuta suluhu za amani katika kila tofauti inayojitokeza.”

Aidha amesema ulinzi wa maisha ni wajibu wa pamoja akifafanua maisha ya mwanadamu ni tunu kubwa na hayapaswi kuwekwa rehani kwa sababu ya tofauti za kisiasa, kidini, kikabila, kiuchumi, kijamii au kiitikadi.

Ameongeza kwa msingi huo, wanatoa mwito wa kuheshimiwa kwa utu wa binadamu, haki ya kuishi, usalama wa raia na ulinzi wa watoto, wanawake, wazee na makundi yote yaliyo katika mazingira hatarishi.

“Tunasisitiza tofauti zetu zisigeuke kuwa sababu ya kupoteza maisha ya watu.Kila jamii ina wajibu wa kulinda maisha na kujenga mazingira ambayo kila mwanadamu anaweza kuishi kwa usalama.

Pia amesema kuhusu amani, afya na ulinzi wa mazingira ni kwamba amani ya kweli haiwezi kutenganishwa na afya ya jamii, usalama wa chakula, maji safi, mazingira salama na matumizi endelevu ya rasilimali za asili.

“Uharibifu wa mazingira, ukataji wa misitu, uharibifu wa vyanzo vya maji, upotevu wa bayoanuai na athari za mabadiliko ya tabianchi vinaweza kuongeza changamoto za kijamii na kiuchumi na kuhatarisha maisha ya watu.

“Kwa hiyo, tunatoa mwito wa kuunganisha juhudi za amani, afya, mazingira na maendeleo endelevu kwa ajili ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.

Akieleza zaidi amesema katika dua kwa Watanzania ,Afrika na Dunia amefafanua Tanzania iendelee kuwa taifa la amani, umoja, mshikamano na utulivu na kwa Afrika ipate amani na utulivu wa kudumu.

Pia migogoro na vita duniani zipungue na hatimaye kumalizika na kuongeza viongozi wapate hekima, busara, uadilifu na moyo wa kuhudumia watu.Vijana wapate fursa za elimu, ajira, ubunifu, ujasiriamali na maendeleo.

Kwa watoto walindwe dhidi ya ukatili, unyanyasaji na mazingira yanayohatarisha maisha yao. Wanawake, wazee na makundi yaliyo katika mazingira magumu walindwe na kuheshimiwa.Wagonjwa na wote wanaokabiliwa na changamoto mbalimbali wapate faraja, matumaini na huduma stahiki na mazingira.

Kuhusu ujumbe kwa Watanzania amesema wanawakumbusha Umoja wetu ni nguvu yetu, amani yetu ni utajiri wetu, na maisha ya kila Mtanzania ni sehemu ya thamani ya Taifa letu.

“Tunapaswa kukataa chuki, uchochezi, ubaguzi, vurugu na lugha zinazogawa jamii. Badala yake, tujenge utamaduni wa kusikilizana, kuheshimiana, kusameheana, kusaidiana na kutatua tofauti zetu kwa njia za amani.

“Tanzania yenye amani na mshikamano ni msingi muhimu wa maendeleo ya watu wake na mchango mkubwa kwa amani ya Afrika na dunia.”

SERIKALI YAMTAKA MKANDARASI KUONGEZA KASI UJENZI WA BARABARA YA KAHAMA-KAKOLA UNAOWEZESHWA NA MIGODI YA BARRICK NCHINI

August 10, 2026 Add Comment

  

Waziri wa Nishati na Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga Kiserikali, Mhe. Deogratius Ndejembi akiongozana na Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita na viongozi wengine wa serikali kukagua mradi wa barabara ya Kahama–Bulyanhulu Jct–Kakola unaowezeshwa na migodi ya Barrick-Twiga nchini.
Sehemu ya barabara iliyowekwa lami katika Mradi wa Barabara ya Kahama–Bulyanhulu Jct–Kakola, unaowezeshwa na migodi ya Barrick-Twiga nchini Tanzania.

MAHAKAMA YA RUFAA YAIPA USHINDI IPTL, PAP KATIKA USD 168M MGOGORO DHIDI YA STANDARD CHARTERED

August 10, 2026 Add Comment

  


Na Mwandishi Wetu

Mahakama ya Rufani ya Tanzania imezipa gharama za kisheria Kampuni ya Independent Power Tanzania Limited - IPTL na Pan Africa Power Solutions (T) Limited ya Dola za Kimarekani 8,000,000 kufuatia kufanikiwa kupinga rufaa iliyokatwa na Benki ya Standard Chartered kuhusu mgogoro wa kibiashara wa muda mrefu wa dola za Marekani 168,000,000.

SERIKALI KUJA NA MRADI MAALUMU WA KUSAMBAZA UMEME KWENYE MAENEO YA UZALISHAJI

August 10, 2026 Add Comment




KAHAMA, SHINYANGA


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi, Serikali inaandaa mradi maalumu wa kusambaza umeme katika maeneo ya uzalishaji, hususan maeneo yenye shughuli za uchimbaji wa madini, kwa lengo la kuwawezesha wazalishaji kutumia nishati ya uhakika na kupunguza utegemezi wa dizeli.


Mhe. Ndejembi ameyasema hayo wakati akijibu swali la Mbunge wa Jimbo la Msalala, Mhe. Mabula Magangila, aliyeomba Serikali kupeleka umeme katika maeneo ya uzalishaji, akieleza kuwa baadhi ya wachimbaji madini katika jimbo hilo bado wanatumia dizeli kuendesha shughuli zao za uzalishaji.


Mbunge huyo pia ameieleza Serikali kuwa vitongoji 98 katika Jimbo la Msalala bado havijaunganishwa na huduma ya umeme.

Akijibu hoja hiyo, Mhe. Ndejembi amesema Serikali tayari imeanza maandalizi ya utekelezaji wa mradi huo maalumu kwa kushirikiana na Wizara ya Madini, ambao utalenga kusogeza huduma ya umeme moja kwa moja kwenye maeneo yenye shughuli za uzalishaji, hususan maeneo ya migodi.


Amesema hatua hiyo inalenga kuongeza tija katika uzalishaji, kupunguza gharama zinazotokana na matumizi ya dizeli pamoja na kuwawezesha wachimbaji na wazalishaji kutumia nishati ya umeme iliyo nafuu, ya uhakika na endelevu.

Kuhusu upatikanaji wa umeme vijijini katika Jimbo la Msalala, Mhe. Ndejembi amesema vijiji vyote tayari vimefikiwa na huduma ya umeme, huku Serikali ikiendelea na jitihada za kuwafikishia huduma hiyo wananchi waliopo katika vitongoji ambavyo bado havijaunganishwa, ikiwemo vitongoji 98 vilivyotajwa.


Aidha, akizungumzia upatikanaji wa umeme katika Jimbo la Kahama Mjini, Mhe. Ndejembi amesema tayari amefanya mazungumzo na Mbunge wa Jimbo hilo, Mhe. Benjamini Ngaiwa, kwa lengo la kubainisha maeneo yaliyopo ndani ya Manispaa ya Kahama ambayo, licha ya kuwa ndani ya eneo la mjini, yana sifa na taswira za maeneo ya vijijini.

Amesema maeneo hayo yataangaliwa ili yaweze kunufaika na utaratibu wa Serikali wa kuunganishiwa umeme kwa gharama ya Shilingi 27,000 kwa mteja, kama ilivyoelekezwa.

Mhe. Ndejembi amesema Serikali itaendelea kuweka kipaumbele katika upanuzi wa miundombinu ya umeme na kuhakikisha nishati inafika katika maeneo yenye shughuli za kiuchumi na uzalishaji, ili kuongeza tija, kuchochea uwekezaji na kuboresha maisha ya wananchi.

 NDEJEMBI: BILIONI 6.7 KWA AFYA YA WANANCHI, JENGO LA MAMA NA MTOTO LIKAMILISHWE KWA WAKATI

NDEJEMBI: BILIONI 6.7 KWA AFYA YA WANANCHI, JENGO LA MAMA NA MTOTO LIKAMILISHWE KWA WAKATI

August 10, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu,SHINYANGA

Waziri wa Nishati na Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga Kiserikali, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameitaka Manispaa ya Kahama kuongeza kasi ya ujenzi wa Jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Manispaa ya Kahama, ili likamilike kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mhe. Ndejembi ametoa agizo hilo leo Agosti 9, 2026, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hilo na kubaini kuwa, licha ya taarifa kuonesha mradi umefikia asilimia 80, hali halisi ya utekelezaji hairidhishi na haioneshi kiwango hicho cha maendeleo.

Amesema Serikali imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya, hivyo fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo zinapaswa kutumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kuleta matokeo chanya kwa wananchi.

Ameitaka Manispaa ya Kahama kukaa pamoja na mkandarasi na kupitia changamoto zote zinazokwamisha utekelezaji wa mradi huo, ili zipatiwe ufumbuzi wa haraka na ujenzi uendelee kwa kasi inayostahili.

“Fedha hizi Shilingi bilioni 6.7 si fedha kwa ajili ya Halmashauri kuzichukua na kukaa nazo, ni fedha kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa Kahama kwa huduma bora za afya. Tunatamani kuona fedha hizi zinaongeza thamani kwa wananchi wa Kahama, hivyo mhakikishe mnasimamia jengo hili likamilike kwa wakati,” amesema Mhe. Ndejembi.

Aidha, Mhe. Ndejembi amewapongeza viongozi wa Manispaa ya Kahama kwa hatua wanazochukua katika kutenga na kuelekeza rasilimali katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati inayolenga kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutenga Shilingi bilioni 5.6 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Wagonjwa wa Nje (OPD) pamoja na Jengo la Vipimo katika Hospitali hiyo.

Mhe. Mhita amesema uwekezaji huo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuendelea kuboresha miundombinu na huduma za afya nchini, akieleza kuwa Rais anatambuliwa kwa msisitizo mkubwa anaouweka katika kuboresha afya ya mama na mtoto.

Amesema fedha hizo zimekuwa chachu kwa Mkoa na Halmashauri kuongeza juhudi na kutenga fedha kutoka katika mapato ya ndani kwa ajili ya kuendelea kuboresha huduma za afya, huku akimhakikishia Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga kuwa Mkoa utaendelea kuusimamia kwa karibu mradi huo hadi utakapokamilika.

Aidha, Mhe. Mhita amemshukuru Mhe. Ndejembi kwa kuendelea kuuwezesha Mkoa wa Shinyanga katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati, hususan katika sekta ya nishati, ikiwemo mradi wa umeme unaoendelea katika Wilaya ya Kishapu.



Global Education Link yawafunda wanaokwenda kusoma India

August 10, 2026 Add Comment

Na Mwandishi Wetu

WANAFUNZI 85 wanatarajia kwenda masomoni kwenye vyuo vikuu mbalimbali nchini India kuanzia wiki ijayo kupitia Wakala wa Elimu Nje ya Nchi Global Education Link (GEL).
NM-AIST  KINARA WA MAONESHO YA NANENANE KANDA YA KASKAZINI  2026

NM-AIST  KINARA WA MAONESHO YA NANENANE KANDA YA KASKAZINI  2026

August 09, 2026 Add Comment

Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) imeibuka kinara miongoni mwa Taasisi za Elimu katika Maonesho ya 33 ya Kilimo, Mifugo na Sherehe za Nanenane Kanda ya Kaskazini yaliyofanyika katika Viwanja vya Themi Njiro, Arusha.

Akizungumzia ushindi huo, Prof. Maulilio Kipanyula, Makamu Mkuu wa NM-AIST, amesema bidhaa bora zinahitaji utafiti na NM-AIST kama Taasisi inayotanguliza ubunifu, imeendelea kubadilisha matokeo ya tafiti kuwa teknolojia zinazotoa suluhisho kwa changamoto za wakulima na wafugaji.

Amesema teknolojia mbalimbali zinazooneshwa na Taasisi, ikiwemo Mfumo wa Ng’ombe Smart, zinalenga kuongeza tija katika ufugaji wa ng’ombe wa maziwa kwa kuwezesha ufuatiliaji wa uzalishaji wa maziwa na taarifa muhimu za mifugo.

Aidha, Prof Kipanyula amesema mwaka huu NM-AIST imekuja na teknolojia zinazolenga kuongeza thamani ya mazao, yakiwemo tumbaku, mazao ya chakula pamoja na vyakula vya mifugo kama kuku na ng’ombe.

Prof. Kipanyula amesisitiza kuwa NM-AIST inaendelea kujipanga kuwa kinara katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, hususan katika maeneo ya utafiti na maendeleo, sayansi, teknolojia na ubunifu, pamoja na mabadiliko ya kidijitali.

“Ushindi huu ni chachu ya kuendelea kufanya vizuri zaidi. Mwaka ujao tutakuja na teknolojia mpya kabisa. Mwaka huu tumefanikiwa kuzalisha takribani patent 40, jambo tunalojivunia na linalotupa nguvu ya kuendelea kuzalisha teknolojia na bunifu zenye tija kwa sekta ya kilimo na mifugo.”

RC MAKALLA AIPONGEZA  NM-AIST KWA UBUNIFU NA TAFITI ZINAZOCHOCHEA MAPINDUZI KATIKA KILIMO NA MIFUGO

RC MAKALLA AIPONGEZA NM-AIST KWA UBUNIFU NA TAFITI ZINAZOCHOCHEA MAPINDUZI KATIKA KILIMO NA MIFUGO

August 09, 2026 Add Comment

Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. CPA Amos Makalla, ameipongeza Taasisi ya Afrika ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) kwa tafiti na bunifu mbalimbali zinazolenga kuongeza tija katika sekta za kilimo na mifugo.

Mhe. Makalla amesema kuwa ametembelea banda la NM-AIST na kujionea teknolojia mbalimbali za kilimo na mifugo, pamoja na bunifu zinazolenga kuongeza thamani ya mazao na bidhaa za mifugo.

Amesisitiza kuwa mapinduzi ya kweli hayawezi kufanyika bila utafiti, teknolojia na ubunifu, akieleza kuwa NM-AIST imekuwa ikifanya vizuri katika kuibua na kuendeleza teknolojia zinazolenga kutatua changamoto za jamii.

“Kilimo bila utafiti, teknolojia na dhana za kisasa hakiwezi kuleta mabadiliko makubwa. Taasisi za utafiti zinatuelekeza na kutupeleka kwenye kilimo na ufugaji wenye tija,” amesema Mhe. Makalla.

Aidha, Mhe. Makalla amesema maendeleo ya sekta za kilimo, mifugo na uvuvi hayapaswi kupimwa kwa kuongezeka kwa uzalishaji pekee, bali pia kwa uwezo wa kuzalisha kwa tija, ubora na kuzingatia mahitaji ya soko, kama inavyosisitizwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Ameeleza kuwa Dira hiyo inalenga kujenga uchumi shindani unaoongozwa na maarifa, teknolojia, ubunifu na uongezaji wa thamani, hivyo taasisi za utafiti kama NM-AIST zina nafasi muhimu katika kufanikisha azma hiyo.

Mhe. Makalla ameyasema hayo wakati akihitimisha Maonesho ya 32 ya Kilimo, Mifugo na Sherehe za Nanenane Kanda ya Kaskazini, yaliyofanyika katika Viwanja vya Themi Njiro, Arusha.

BARAZA LA USHINDANI LAJA NA MFUMO WA KIDIJITALI KURAHISISHA RUFAA ZA WANANCHI

BARAZA LA USHINDANI LAJA NA MFUMO WA KIDIJITALI KURAHISISHA RUFAA ZA WANANCHI

August 09, 2026 Add Comment
Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Baraza la Ushindani (FCT limeendelea kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi kwa kutumia teknolojia za kidijitali, likiwataka wananchi na wadau kutumia mfumo wa kielektroniki kuwasilisha mashauri na rufaa zao kwa urahisi na kwa wakati.
Msajili wa Baraza la Ushindani, Mbegu Kaskasi, amesema Baraza hilo lililo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara lina jukumu la kusikiliza na kutatua migogoro ya ushindani wa biashara na udhibiti wa soko inayotokana na maamuzi ya Tume ya Ushindani (FCC) pamoja na mamlaka za udhibiti zikiwemo TCRA, EWURA, LATRA, TURA na TCAA.
Kaskasi amesema Baraza hilo linaundwa na Jaji wa Mahakama Kuu pamoja na wajumbe sita, huku likitumia fursa mbalimbali kuwaelimisha wananchi kuhusu majukumu yake, namna ya kupata huduma na utaratibu wa kuwasilisha mashauri, ikiwemo kupitia mfumo wa kielektroniki wa usikilizaji wa mashauri.
Amesema mfumo huo umewekwa ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi, ambapo kwa sasa wanaweza kuwasilisha mashauri na rufaa zao kwa njia ya kielektroniki bila kulazimika kufika ofisini, hatua inayokwenda sambamba na mabadiliko ya kidijitali nchini.
Kwa upande wake,Afisa Sheria wa baraza hilo ,Hafsa Said, amesema mchakato wa rufaa huanza kwa mhusika kuwasilisha notisi ya rufaa pamoja na kuwapatia nakala wahusika wanaopaswa kujibu rufaa hiyo. Baada ya hapo, mhusika anatakiwa kuwasilisha sababu za rufaa pamoja na kumbukumbu zinazohusiana na shauri hilo.
Amesema baada ya mjibu rufaa kuwasilisha majibu yake, shauri hukamilika kwa ajili ya kusikilizwa, huku Baraza likiwa na utaratibu wa kuhakikisha rufaa inayowasilishwa kikamilifu inasikilizwa na kutolewa uamuzi ndani ya kipindi kisichozidi miezi sita.
Naye Afisa TEHAMA wa Baraza hilo Bw.Athumani Kanyegezi  amewataka wananchi na wadau kutumia mfumo wa kielektroniki unaopatikana kupitia tams.fct.or.tz au tovuti ya Baraza fct.or.tz, akieleza kuwa mfumo huo ni rafiki kwa mtumiaji na umeundwa kuendana na mahitaji ya sasa ya utoaji huduma kwa njia ya kidijitali.
Amesema matumizi ya teknolojia hiyo ni sehemu ya juhudi za Baraza kwenda sambamba na mabadiliko ya kidijitali na kuchangia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050, huku akiwataka wananchi kutumia fursa hiyo kupata huduma kwa urahisi.
Aidha, imeelezwa kuwa uwepo wa Baraza la Ushindani unawapa wananchi fursa ya kukata rufaa pale wanapokuwa hawajaridhishwa na maamuzi ya mamlaka zinazodhibiti sekta mbalimbali. Kwa mfano, mwananchi mwenye malalamiko dhidi ya kampuni ya simu anaweza kwanza kuyawasilisha katika mamlaka husika na, endapo hataridhishwa na uamuzi, anaweza kutumia fursa ya kukata rufaa katika Baraza la Ushindani.
Naye Mdau Vendeline Shekifu,ameeleza kufurahishwa na uwepo wa taasisi hiyo umewapa fursa ya kujifunza kuhusu huduma mbalimbali zinazotolewa na taasisi za Serikali, ikiwemo Baraza la Ushindani.
Awali Diwani wa Kata ya Tamkaleli Clinton Manzi  amesema maadhimisho hayo yamekuwa na manufaa kwa wakazi wa Dodoma kutokana na muda walioupata kujifunza huduma na fursa mbalimbali, huku akimshukuru Rais kwa kuwezesha maadhimisho hayo kufanyika jijini Dodoma.

TBS YAWAFUNGULIA WAJASIRIAMALI NJIA YA MASOKO KUPITIA UBORA WA BIDHAA

August 09, 2026 Add Comment
Wajasiriamali na wananchi wanaoshiriki Maonesho ya Nane Nane Kanda ya Kusini wamepata elimu kuhusu umuhimu wa kuzingatia viwango, kuthibitisha bidhaa na kutumia Alama ya Ubora ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS), hatua inayolenga kuongeza uaminifu wa bidhaa na kufungua fursa zaidi za masoko ndani na nje ya nchi.
WAZIRI NDEJEMBI AMTAKA MKANDARASI KUONGEZA KASI UJENZI WA BARABARA YA KAHAMA- BULYANHULU JCT-KAKOLA

WAZIRI NDEJEMBI AMTAKA MKANDARASI KUONGEZA KASI UJENZI WA BARABARA YA KAHAMA- BULYANHULU JCT-KAKOLA

August 09, 2026 Add Comment




KAHAMA, SHINYANGA

Waziri wa Nishati na Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga Kiserikali, Mhe. Deogratius Ndejembi, amemtaka Mkandarasi wa Barabara ya Kahama–Bulyanhulu Jct–Kakola, M/s China Civil Engineering Construction Corporation (CCECC), kuongeza kasi ya utekelezaji wa mradi huo ili ukamilike kwa wakati na kuwawezesha wananchi kuanza kunufaika na miundombinu hiyo.

Mhe. Ndejembi ametoa agizo hilo leo, Agosti 9, 2026, mkoani Shinyanga, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 73 inayojengwa kwa kiwango cha lami.


Amesema hadi sasa kilomita 32 kati ya 73 zimekamilishwa kwa kuwekwa lami, huku kazi nyingine za ujenzi zikiendelea katika maeneo mbalimbali ya mradi.

SERIKALI YATENGA BILIONI 38 KUPIMA VIJIJI VYOTE TANZANIA, YAAGIZA KLINIKI ZA ARDHI KILA KATA

August 09, 2026 Add Comment

 



Serikali imetangaza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameridhia utoaji wa kiasi cha shilingi bilioni 38 kwa ajili ya kufanikisha mpango wa kupima vijiji vyote nchini ili kumaliza migogoro ya ardhi.

Hayo yameelezwa leo Julai 1, 2026 katika viwanja vya Sokoni Mugumu Wilaya ya Serengeti mkoani Mara na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Kaspar Mmuya alipokuwa akizungumza mbele ya Waziri Mkuu, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba, ambaye yuko katika ziara ya kikazi ya siku tano mkoani humo.

Katika hatua ya haraka ya kusogeza huduma kwa wananchi, Mhe. Mmuya amemuagiza Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Mara pamoja na timu yake, kuhakikisha wanaratibu na kuanzisha kliniki za ardhi katika kila kata.

"Hakikisheni mnaratibu uwepo wa kliniki za ardhi katika kila kata ili muwasikilize wananchi hawa na msione kila changamoto mpewazo ni ya mazoea. Hapana, amekuja kwako kwa sababu ana jambo la kusikilizwa na litatuliwe," alisema Naibu Waziri Mmuya.


Mhe. Mmuya alieleza kuwa wizara ya Ardhi iliwasilisha mpango na maombi ya fedha bungeni kufuatia maelekezo ya awali ya Waziri Mkuu, na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akaidhinisha shilingi bilioni 38 kwa ajili ya kupima jumla ya vijiji 12,333 vya Tanzania.


"Mpaka hivi ninavyoongea, Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi chake kifupi tu ameweza kupima vijiji 4,873. Na ametupatia maelekezo kuwa ndani ya kipindi chake, vijiji vyote vilivyobakia tuvipime." Aliongeza Naibu Waziri Kaspar Mmuya 



Katika hatua nyingine Mhe. Mmuya amesema Wizara ya Ardhi itashirikiana bega kwa bega na Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili kuhakikisha maagizo hayo yanatekelezwa kikamilifu katika vijiji vyote vilivyosalia nchini.


Aidha, Mhe. Mmuya alieleza kuwa Wilaya ya Serengeti ina kata 30 na vijiji 78. Ameuhakikishia uongozi wa wilaya hiyo kuwa vijiji vyote 78 vimeshaingizwa kwenye mpango wa upimaji ndani ya kipindi cha miaka mitano ya Rais Samia Suluhu Hassan.


"Kupima vijiji hivi ndiyo dawa kubwa ya kutatua changamoto ya mipaka kati ya kijiji na kijiji. Lakini ni dawa kubwa ya kutatua changamoto ya kugombania matumizi ya ardhi ya mtu mmoja mmoja, taasisi na taasisi, au serikali na wananchi," alisema Naibu Waziri Kaspar Mmuya.

WAZIRI NDEJEMBI AANZA ZIARA MAALUM MKOANI SHINYANGA

August 09, 2026 Add Comment


Waziri wa Nishati, Mhe. Deogratius Ndejembi (Mb.), amewasili mkoani Shinyanga kwa ziara maalum ya kikazi ya kukagua utekelezaji na kuzindua miradi ya maendeleo, pamoja na kuzungumza na wananchi katika wilaya za Mkoa wa Shinyanga.

Waziri Ndejembi, ambaye ni Mlezi wa Mkoa wa Shinyanga Kiserikali, mara baada ya kuwasili amefika katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga na kupokelewa na Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Mboni Mhita, tarehe 09 Agosti 2026.

Waziri Ndejembi akiwa mkoani hapo, atakagua mradi wa ujenzi wa barabara ya Kahama – Kakola, mradi wa ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama, kukagua ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Shinyanga, pamoja na kuwasha umeme wa REA katika Kitongoji cha Mwanubi, Kolandoto.




AJIRA ZAIDI YA 420 ZAZALISHWA KUPITIA UJENZI WA KITUO CHA EACOP PS4 MBOGWE

August 09, 2026 Add Comment




MBOGWE, 


Zaidi ya wananchi 420 wamepata ajira zisizo za ujuzi kupitia utekelezaji wa ujenzi wa Kituo cha Kuongeza Msukumo wa Mafuta (PS4) cha Mbogwe, kinachotekelezwa chini ya Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP).


Hayo yameelezwa Agosti 8, 2026 na Mkurugenzi wa Mipango na Uwekezaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Bw. Derick Moshi, wakati wa ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho kilichopo Wilaya ya Mbogwe, mkoani Geita.

Bw. Moshi amesema utekelezaji wa mradi huo umeendelea kutoa manufaa kwa Watanzania, ambapo takribani asilimia 80 ya fursa zinazotokana na mradi zimenufaisha Watanzania, ikiwemo ajira, mafunzo na ushiriki wa wazawa katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali.

Amesema zaidi ya ajira hizo, mradi umetoa mafunzo kwa wananchi kupitia Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) na Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO), hatua iliyowawezesha kupata ujuzi na uzoefu unaohitajika katika kushiriki kwenye miradi mikubwa ya kimkakati.

“Mradi huu umeendelea kuwa fursa kwa Watanzania, siyo tu kupitia ajira, bali pia kupitia mafunzo yanayowawezesha vijana kupata ujuzi na uzoefu wa kushiriki katika miradi mikubwa ya kimkakati,” amesema Bw. Moshi.

Aidha, Bw. Moshi ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wa ujenzi wa PS4, ambao umefikia asilimia 88 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 2026.

Amesema utekelezaji wa mradi huo umezingatia pia ushirikishwaji wa jamii inayozunguka mradi kupitia ajira, utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) pamoja na maboresho ya miundombinu, ikiwemo barabara na huduma za maji.

Ameeleza kuwa vituo vya kuongeza msukumo wa mafuta vya Muleba (PS3) na Mbogwe (PS4) ni sehemu muhimu ya miundombinu ya EACOP, kwa kuwa vina jukumu la kupokea na kuongeza msukumo wa mafuta ili yaweze kusafirishwa kwa ufanisi kupitia bomba hilo kuelekea kituo cha mwisho cha Kiteto.



Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Huduma wa EACOP ambaye pia ni Kaimu Meneja wa EACOP Tanzania, Bw. Geofrey Mponda, amesema vituo vya kuongeza msukumo wa mafuta ni miundombinu muhimu katika kuhakikisha usafirishaji wa mafuta kupitia EACOP unafanyika kwa ufanisi na kwa kuzingatia viwango vinavyotakiwa.


Amesema utekelezaji wa Mradi wa EACOP umeendelea kuwa chachu ya fursa kwa Watanzania, hususan vijana, kwa kuwa umetoa ajira kwa wenye ujuzi na wasio na ujuzi, huku ukiwawezesha pia kupata uzoefu wa vitendo katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati.


“EACOP imeendelea kuwa chachu ya fursa kwa Watanzania. Vijana wamepata ajira na wengine wamepata fursa ya kujifunza na kujenga uzoefu ambao utawasaidia kushiriki katika miradi mingine mikubwa ya kimkakati,” amesema Mponda.


Naye Mwakilishi wa Kampuni ya EACOP katika eneo la mradi (EACOP Company Site Representative), Bw. Kamal Maalouli, amesema PS4 ni miongoni mwa vituo vikubwa na muhimu katika utekelezaji wa Mradi wa EACOP.


Amesema kampuni imeendelea kuweka juhudi zote kuhakikisha ujenzi wa kituo hicho unakamilika kwa wakati uliopangwa na kukidhi viwango vinavyohitajika ili kiweze kutekeleza jukumu lake katika mfumo wa usafirishaji wa mafuta kupitia EACOP.


Mradi wa EACOP unahusisha ujenzi wa bomba lenye urefu wa takribani kilomita 1,443 kutoka Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani, Tanga nchini Tanzania, ambapo sehemu kubwa ya bomba hilo inapita nchini Tanzania.