HABARI

SIASA

ELIMU

Recent Posts

KIRITA AAGIZA KASI MRADI WA MAJI KAHAMA–USHETU: “TUTEMBEE NA MAJI”

August 13, 2026 Add Comment

 

Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akizungumza katika moja ya matanki ya maji, Kata ya Ulowa, Halmashauri ya Ushetu.  Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akiwa ameambatana na wataalamu mbalimbali katika moja ya matanki ya maji, Kata ya Ulowa, Halmashauri ya Ushetu.
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akiwa ameambatana na wataalamu mbalimbali katika moja ya matanki ya maji wakati wa ziara yake ya kukagua utekelezaji wa mradi wa maji Kahama - Ushetu. 
Meneja Mradi kutoka RUWASA, John Msengi akieleza kuhusu utekelezaji wa mradi wa maji Kahama–Ushetu.
Muonekano wa sehemu ya mabomba katika mradi wa maji Kahama–Ushetu
Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA, Mhandisi Wolta Kirita, akizungumza wakati wa ziara katika Mradi wa Maji Kahama - Ushetu.

Na Kadama Malunde – Malunde 1 Blog

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), Mhandisi Wolta Kirita, amewataka Mameneja wa RUWASA ngazi ya mikoa na wilaya kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maji unaenda sambamba na upatikanaji wa huduma, akisisitiza falsafa ya “kutembea na maji” kuwa kipaumbele katika utekelezaji wa miradi hiyo.

RAIS SAMIA AWEKA JIWE LA MSINGI LA SKULI YA SEKONDARI YA UFUNDI KIZIMKAZI

August 13, 2026 Add Comment
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameweka jiwe la msingi na kupanda mti katika Skuli ya Sekondari ya Ufundi Kizimkazi Mkunguni, Wilaya ya Kusini, Mkoa wa Kusini Unguja.
NAIBU WAZIRI NISHATI AHAMASISHA UMMA KUPATA TAARIFA SAHIHI KUHUSU SEKTA NDOGO YA UMEME

NAIBU WAZIRI NISHATI AHAMASISHA UMMA KUPATA TAARIFA SAHIHI KUHUSU SEKTA NDOGO YA UMEME

August 13, 2026 Add Comment

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Na Mwandishi Wetu

Naibu Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Salome Makamba, amehimiza umma kupata taarifa sahihi kuhusu hali ya sekta ndogo ya umeme nchini, huku akitoa wito kwa Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kuendelea kutoa elimu na taarifa kwa wananchi kuhusu jitihada mbalimbali zinazofanywa na Serikali katika kuboresha huduma za umeme.

Mhe. Makamba ametoa wito huo leo, tarehe 13 Agosti 2026, alipotembelea banda la EWURA katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, amesema ni muhimu wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu kuongezeka kwa uzalishaji na upatikanaji wa umeme nchini na hivyo kukidhi mahitaji tuliyonayo.

“Gharama ya umeme nchini Tanzania ni nafuu ikilinganishwa na nchi jirani, na Serikali inaendelea na juhudi za kuboresha na kuimarisha miundombinu ya umeme ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma hiyo kwa uhakika, hatua itakayochochea maendeleo ya kiuchumi nchini,” aliongeza.

Katika banda la EWURA, Mhe. Makamba alifahamishwa Mamlaka imetumia fursa ya Maonesho hayo kutoa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya udhibiti ikiwemo mikataba ya huduma kwa wateja, matumizi sahihi na salama ya huduma za bidhaa za gesi ya mitungi, gesi asilia, umeme na maji, fursa za uwekezaji katika sekta na mengineyo.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akisaini kitabu  mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

 

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe.Salome Makamba,akipata maelezo mara baada ya kutembelea  banda la Mamlaka ya Udhibiti Huduma za Nishati na Maji (EWURA) katika Maonesho ya Kizimkazi yanayoendelea katika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar.

NAIBU WAZIRI MAKAMBA AITAA PBPA KUENDELEA KUTOA ELIMU KWA UMMA

August 13, 2026 Add Comment

 



Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba (Mb.), ameitaka Wakala wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja (PBPA) kuendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa umma ili wananchi wawe na uelewa mpana kuhusu majukumu ya Wakala na mchango wake katika kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.

Mhe. Makamba ametoa wito huo alipotembelea banda la PBPA katika maonesho yanayofanyika Viwanja vya Dimbani, Kizimkazi, Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya Tamasha la Kizimkazi 2026.

Amesema ni muhimu wananchi wakaendelea kuelimishwa kuhusu Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja na namna PBPA inavyotekeleza majukumu yake katika kusimamia uagizaji wa bidhaa za mafuta kwa lengo la kuhakikisha nchi inakuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa hiyo muhimu.


Aidha, Mhe. Makamba ameipongeza PBPA kwa utendaji wake katika kutekeleza majukumu yake na kuhakikisha upatikanaji wa mafuta nchini.


Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkaguzi wa Mafuta wa PBPA, Bw. Issa Mwitazy, amemweleza Naibu Waziri kuwa Wakala unaendelea kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha nchi inakuwa na kiwango cha kutosha cha mafuta ili kukidhi mahitaji ya soko.

Bw. Mwitazy amesema ushiriki wa PBPA katika Tamasha la Kizimkazi umetoa fursa kwa wananchi na wadau mbalimbali kupata elimu na ufafanuzi kuhusu majukumu ya Wakala pamoja na namna Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja unavyofanya kazi.


Ameongeza kuwa PBPA inaendelea kudumisha ushirikiano mzuri na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati Zanzibar (ZURA) katika masuala yanayohusu sekta ya mafuta.


Tamasha la Kizimkazi 2026, ambalo ni msimu wa tatu, linafanyika kuanzia Agosti 12 hadi 14, 2026, likiwa na lengo la kuibua na kufungua fursa mbalimbali za maendeleo, huku likibeba kaulimbiu “Kizimkazi 2026, Fursa na Shangwe.”

KIZIMKAZI 2026: WIZARA YA NISHATI YAENDELEA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI

August 13, 2026 Add Comment


Wataalam wa Wizara ya Nishati wanaendelea kutoa elimu na ufafanuzi kwa wananchi wanaotembelea Banda la Wizara na taasisi zake katika Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2026, yanayofanyika Kizimkazi, Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar.

Wananchi wanapata fursa ya kufahamu shughuli, miradi na huduma mbalimbali zinazotekelezwa katika sekta ya nishati, ikiwemo masuala ya umeme, mafuta, gesi asilia na nishati safi ya kupikia.


Karibu tukuhudumie.



DKT.DOTO BiTEKO ANOGESHA MASHINDANO YA NGALAWA TAMASHA KIZIMKAZI

August 13, 2026 Add Comment




Naibu Waziri Mkuu Mstaafu na Mbunge wa Jimbo la Bukombe, Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko amesema kuwa mashindano ya ngalawa race ni miongoni mwa matukio makubwa ya kiburudani yanayoipamba Kizimkazi Festival 2026.


Mashindano hayo yamefanyika Kizimkazi, Kusini Unguja Agosti 12, 2026 yaliyokuwa na ushindani mkubwa ambapo Nassor Pandu wa Mkunguni ameibuka mshindi wa mashindano ya ngalawa ikiwa ni sehemu ya shughuli mbalimbali zinazoendelea katika Tamasha la Kizimkazi.

“ Ni dhahiri kwamba mashindano haya yamekuwa muhimu kwa vijana na jamii kwa ujumla. Tukio hili limewaleta pamoja wadau mbalimbali na kuchangia kwa kiasi kikubwa juhudi za kuboresha mazingira ya michezo na burudani,” amesema Dkt. Biteko.

Dkt. Biteko ameongeza kuwa mashindano ya Ngalawa race Kizimkazi Festival yameendelea kutoa fursa za kiuchumi kwa vijana mbalimbali katika kushindana hadi kupata timu mbili bora za Mchangamle na Mkunguni ambapo kila timu imehusisha manahodha 10.



Mwisho.

KAPINGA: SERIKALI YALENGA HUDUMA ZA AFYA KUMFIKIA KILA MWANANCHI

August 13, 2026 Add Comment
Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.
WAZIRI KAPINGA AHAIDI KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA MTWARA

WAZIRI KAPINGA AHAIDI KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA MTWARA

August 13, 2026 Add Comment

Wananchi mkoani Mtwara wameishukuru Serikali kwa kuendelea kujenga na kuboresha miundombinu ya huduma za afya, hatua iliyowarahisishia upatikanaji wa huduma hizo bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.

Hayo yamejiri, katika siku ya tatu ya ziara ya kikazi ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga (Mb), mkoani humo, yenye lengo la kukagua na kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita.

Wananchi hao wamesema wanapata huduma za afya kwa wakati na kwa urahisi, jambo walilolieleza kuwa limepunguza changamoto ya kufuata matibabu katika maeneo ya mbali.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Waziri Kapinga amesema Serikali inalenga kuboresha huduma za afya ili wananchi wapate matibabu kwa urahisi na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji, hivyo kuimarisha uchumi wa familia na Taifa.

Amesema kusogeza huduma za afya karibu na wananchi ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma muhimu kwa wakati.

Aidha, amewataka wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo, akisisitiza kuwa ushirikiano ni msingi wa maendeleo.

Katika siku ya tatu ya ziara hiyo, Waziri Kapinga ametembelea miradi mbalimbali katika Majimbo ya Nanyamba, Mtwara Mjini na Mtwara Vijijini, ikiwemo kuzindua Kituo cha Afya Msangamkuu, kuzindua mabweni mawili na kutoa taulo za kike kwa wanafunzi wa Shule ya Wasichana Mtwara, kukagua ujenzi wa Shule ya Amali Chikota, pamoja na kutembelea Wodi ya Wazazi katika Hospitali ya Wilaya ya Tandahimba.

ALC GROUP YATOA MSAADA KWA WANAFUNZI WENYE MAHITAJI MAALUM PU­GU

August 13, 2026 Add Comment

    

Jamii, kampuni binafsi na wadau mbalimbali wametakiwa kuongeza juhudi za kusaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum kwa kuwapatia huduma za afya, vifaa saidizi na mahitaji ya kielimu ili kuwawezesha kupata elimu bora na kutimiza ndoto zao.

Wito huo umetolewa na Elvis Lyimo, Mkuu wa Idara ya Elimu Maalum katika Shule ya Sekondari Pugu, wakati ALC Group, wauzaji wa vilainishi vya Flying Horse Lubricant, ilipofika shuleni hapo na kutoa msaada kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Kupitia msaada huo, wanafunzi 50 wamepatiwa bima ya afya, huku baadhi yao wakipatiwa viti mwendo pamoja na kompyuta kwa ajili ya kuwawezesha kushiriki vizuri zaidi katika masomo na shughuli zao za kila siku.

Lyimo amesema msaada huo una umuhimu mkubwa kwa wanafunzi wenye ulemavu, hususan wale wanaotoka katika familia zenye uwezo mdogo kiuchumi na ambao mara nyingi hukabiliwa na changamoto ya kupata huduma za afya na vifaa muhimu vya kuwasaidia katika ujifunzaji.
“Msaada huu utawasaidia wanafunzi wenye ulemavu wa viungo na changamoto ya kuandika, ambao wengi wao wanatoka katika familia zenye hali duni kiuchumi,” amesema Lyimo.

Amesema baadhi ya wanafunzi wenye mahitaji maalum hukabiliwa na changamoto za kupata viti mwendo, magongo ya kutembelea, magodoro, vifaa vya kujifunzia na mahitaji mengine muhimu, huku gharama za matibabu zikiwa changamoto kwa familia nyingi.

Kwa mujibu wa Lyimo, Shule ya Sekondari Pugu ina jumla ya wanafunzi 85 wenye mahitaji maalum, hali inayofanya mahitaji ya huduma na vifaa kuwa makubwa zaidi licha ya Serikali kuendelea kutoa huduma mbalimbali.
Amesema ushiriki wa wadau zaidi ni muhimu katika kuziba pengo lililopo na kuhakikisha wanafunzi hao wanapata fursa sawa ya elimu na maendeleo.

WAZAZI WATAKIWA KUTOWAFICHA WATOTO WENYE ULEMAVU

Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Pugu, Patrick Sinyinza, amewataka wazazi na walezi kutowaficha watoto wenye ulemavu majumbani, bali kuwapeleka shuleni ili wapate elimu na fursa ya kuendeleza vipaji na uwezo wao.

Sinyinza amesema watoto wenye mahitaji maalum wana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri kitaaluma iwapo watapewa mazingira rafiki, msaada na fursa zinazostahili.

Amesema msaada uliotolewa na ALC Group umefika wakati muafaka kwa kuwa wanafunzi wenye ulemavu wanahitaji huduma za afya mara kwa mara pamoja na vifaa vinavyowawezesha kushiriki kikamilifu katika masomo.

“Wazazi wasiwanyime watoto wenye ulemavu haki yao ya kupata elimu kwa kuwaficha nyumbani. Watoto hawa wana uwezo mkubwa wa kufanya vizuri kitaaluma,” amesema Sinyinza.
Ameeleza kuwa Serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeendelea kuboresha miundombinu na mazingira ya shule ili kuwawezesha wanafunzi wenye na wasio na ulemavu kusoma pamoja katika mazingira yanayozingatia mahitaji yao.

Shule ya Sekondari Pugu ina jumla ya wanafunzi 989 na walimu 74, ambapo walimu 26 wamepatiwa mafunzo maalum ya elimu ili kuwawezesha kuwahudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum.

MWANAFUNZI MWENYE MAHITAJI MAALUM APATA ALAMA SABA

Sinyinza amesema mafanikio ya wanafunzi wenye mahitaji maalum katika shule hiyo ni ushahidi kuwa ulemavu si kikwazo cha kufikia mafanikio ikiwa mwanafunzi atapatiwa msaada unaostahili.

Ametoa mfano wa mwanafunzi wa Kidato cha Sita aliyefanya mtihani mwaka huu na kupata alama saba na Daraja la Kwanza, akisema mafanikio hayo yanaonyesha uwezo mkubwa walionao wanafunzi wenye mahitaji maalum.

“Hii inaonyesha uwezo mkubwa walionao watoto hawa. Wapo wanafunzi wasio na ulemavu ambao hawakupata alama saba, lakini mwanafunzi mwenye mahitaji maalum ameweza kufanya hivyo. Wanachohitaji ni msaada na fursa,” amesema.

ALC GROUP YAAHIDI KUENDELEA KUSAIDIA

Akizungumza wakati wa makabidhiano ya msaada huo, Emmanuel Shija, Balozi wa ALC Group, wauzaji wa vilainishi vya Flying Horse Lubricant, ambaye pia ni Bingwa wa WBC Muay-Thai Tanzania, amesema mchango huo ni sehemu ya utekelezaji wa wajibu wa kampuni kwa jamii.

Shija amesema kampuni imeamua kuanza na wanafunzi 50 kwa kuwapatia bima za afya, viti mwendo na kompyuta, huku ikiweka mkakati wa kuendelea kusaidia wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Amesema watu wenye ulemavu na wanaoishi katika mazingira magumu mara nyingi husahaulika katika jamii, hivyo ALC Group imeona umuhimu wa kutumia sehemu ya mafanikio yake kusaidia kuboresha maisha ya kundi hilo.

“Watu ambao wana changamoto au wanaoishi katika mazingira magumu mara nyingi husahaulika na jamii. Tumeamua kuanza na wanafunzi 50 kwa kuwapatia bima za afya, viti mwendo na kompyuta kwa sababu tunaamini ni muhimu kuwakumbuka na kuwasaidia wanaohitaji msaada,” amesema Shija.

Amesema ALC Group itaendelea kugharamia bima za afya kwa baadhi ya wanafunzi wenye mahitaji maalum ili kuwawezesha kupata matibabu kwa wakati na kupunguza mzigo wa gharama kwa familia zao.

Aidha, amesema kampuni hiyo itaendelea kutoa vifaa vya usafiri kwa baadhi ya wanafunzi, ikiwemo baiskeli za magurudumu matatu, ili kuwawezesha wanafunzi wenye changamoto za ulemavu wa viungo kusafiri kwa urahisi na kushiriki kikamilifu katika shughuli za kila siku.

Shija amesema lengo la kampuni si kutoa msaada wa mara moja pekee, bali kujenga utamaduni endelevu wa kuirudishia jamii sehemu ya mafanikio yanayopatikana kupitia shughuli za kampuni.

“Lengo letu si kutoa msaada wa mara moja, bali kujenga utamaduni wa kutoa na kuirudishia jamii sehemu ya mafanikio tunayoyapata. Tunaamini kila taasisi ina nafasi ya kuleta mabadiliko chanya katika maisha ya watu wenye mahitaji maalum,” amesema.

WANAFUNZI WASHUKURU MSAADA

Kwa upande wa wanafunzi, Thobias Masumbulko, aliyewakilisha wanafunzi wenzake, ameishukuru ALC Group kwa msaada huo na kusema vifaa vilivyotolewa vina umuhimu mkubwa katika maisha yao.

Amesema wakati mwingine watu wanaweza kuona msaada kama huo kuwa ni mdogo, lakini kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum una thamani kubwa kwa sababu unawapatia vitu ambavyo hapo awali walikosa.

“Tunawashukuru kwa kile mlichotupatia. Mnaweza kufikiri ni kidogo, lakini kwetu ni kitu kikubwa kwa sababu ni vitu ambavyo hatukuwa navyo kabla,” amesema.

Masumbulko amewataka wazazi na jamii kwa ujumla kutowatenga watoto wenye ulemavu, akisisitiza kuwa wana uwezo wa kufanya mambo makubwa iwapo watapewa fursa na msaada unaostahili.

Ameeleza pia kuwa walimu wa shule hiyo wamekuwa na mchango mkubwa katika kuwajengea wanafunzi wenye mahitaji maalum kujiamini na kuwahamasisha kuangalia uwezo wao badala ya kujikita katika changamoto zao.