TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI: WAZIRI KIGWANGALLA ATENGUA UTEUZI WA WAJUMBE WA BODI YA NGORONGORO

December 19, 2017

WAZIRI MAKAMBA AZINDUA KAMATI YA TAIFA YA USHAURI WA MAZINGIRA

December 19, 2017


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akifungua kikao cha Kamati ya Kitaifa ya Ushauri wa Mazingira hii leo katika Ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma. Kikao hicho kinajumuisha wakumbe kutoka sekta mbalimbali. Wengine katika picha ni Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Butamo Phillip na Katibu Mkuu Mhandisi Joseph Malongo.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akimkabidhi vitendea kazi mmoja ya wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Ushauri wa Mazingira hii leo katika Ukumbi wa Hazina Mjini Dodoma. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Butamo Phillip na Bw. Richard Muyungi Mkurugenzi wa Idara ya Mazingira.
Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini - OMR


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. January Makamba akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Ushauri wa Mazingira mara baada ya ufunguzi uliofanyika katika Ukumbi wa Hazina mjini Dodoma.

Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Ushauri wa Mazingira;
Mhe. Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira;
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira;
Ndugu wajumbe;
Wanahabari;
Mabibi na Mabwana.

Ndugu wajumbe;
Kwanza kabisa, napenda kutumia fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutupa afya njema. Pia nawashukuru nyote kwa kukubali kuja kushiriki katika kikao hiki cha uzinduzi wa Kamati ya Ushauri wa Mazingira (The National Environmental Advisory Committee), licha ya kwamba mnayo majukumu mengi maofisini kwenu. Tunatambua na kuheshimu uwepo wenu hapa na ni ushahidi tosha kuwa sote tuko tayari kukaa pamoja kujadili masuala yenye mustakabali wa Taifa letu.  Nawashukuruni sana wote.
Ndugu wajumbe;
Kama mnavyofahamu, nchi yetu inakabiliwa na changamoto mbalimbali za uharibifu wa mazingira unaotishia juhudi za serikali na wadau katika kufikia maendeleo endelevu. Baadhi ya changamoto hizi ni pamoja na: Uharibifu wa mazingira utokanao na uvamizi wa wafugaji kwenye maeneo ya vyanzo vya maji; Uharibifu wa mazingira kutokana na shughuli za kilimo kisichoendelevu kwenye miteremko ya milima, mabonde na vyanzo vya maji; Uharibifu wa mazingira utokanao na ukataji miti kwa ajili ya kuni na mkaa; upungufu wa maji ya kuendeshea mitambo ya kuzalisha umeme; Uharibifu wa mazingira ya vyanzo vya maji utokanao na moto; Kuenea kwa hali ya jangwa na ukame katika maeneo mengi nchini; Uelewa na ushiriki mdogo wa wananchi katika hifadhi ya mazingira; Migongano katika matumizi ya ardhi baina ya wadau mbalimbali na uharibifu wa mazingira utokanao na shughuli za uchimbaji madini na uchafuzi wa mazingira utokanao na majitaka, taka ngumu na hatarishi zitokanazo na sekta ya viwanda, kilimo na afya. Changamoto hizi za uharibifu wa mazingira zimesababisha athari kadhaa kama vile mabadiliko ya tabianchi, upotevu wa bioanuai za misitu na hivyo kuwepo kwa tishio la kutoweka kwa baadhi ya jamii ya mimea miti na viumbe wengine.

Ndugu wajumbe;
Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imekua ikibuni na kutekeleza hatua kadhaa zenye lengo la kukabiliana na changamoto hizo za uharibifu wa mazingira nchini. Katika kipindi hiki kifupi cha Serikali ya awamu ya tano, tumekabiliana na changamoto hizo na baadhi ya mafanikio yamepatikana ambayo ni pamoja na: Kuanzishwa kwa Carbon Monitoring Centre – SUA; Jumla ya vyeti zaidi ya mia nane (800) vya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) vimeidhinishwa; Viwanda vimeweka mifumo ya kutibu Maji taka na kupunguza uchafuzi wa Mazingira kama vile Viwanda vya Saruji vya Twiga na Lake Cements; Makampuni binafsi mbalimbali yamekidhi matakwa ya hifadhi ya mazingira; Kamati ya Kitaifa ya kusimamia matumizi ya Bioteknolojia ya kisasa imezinduliwa; Mfuko wa mazingira umeanzishwa; Mchakato wa kufanya mapitio ya Sera mpya ya Mazingira unaendelea; Siku ya usafi kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi imepitishwa (Gazetted) na kuwa sheria; Miradi ya hifadhi ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi (Climate Change) yenye thamani ya zaidi Dola milioni Mia moja imeandaliwa na inatafutiwa fedha kwa ajili ya utekelezaji; Serikali kupitia Ofisi Ya Makamu wa Rais imeandaa miradi minne (4) yenye jumla ya Dola za Marekani milioni 28. Fedha za utekelezaji wa Mradi huu zinategemewa kutoka katika Mfuko wa Dunia wa Mazingira (Global Environment Facility – GEF). Miradi hiyo ni pamoja na:
(a)   Mradi wa Kukabiliana na Kasi ya Uharibifu wa Ardhi na Kuongeza Upatikanaji wa Chakula katika Maeneo Kame Nchini (Reversing Land Degradation Trends and Increasing Food Security in Degraded Ecosystems of Semi-arid areas of Tanzania. Mradi huu una thamani ya Dola za Marekani Milioni 7.1. Utekelezaji utafanyika kwa kushirikiana na Mfuko wa Dunia wa Maendeleo ya Kilimo (International Fund for Agricultural Development – IFAD). Utekelezaji wa Mradi huu unatarajiwa kuanza rasmi mwishoni mwa  mwaka 2017.
(b) Mradi Kuhimili mabadiliko ya Tabianchi katika Mifumo-ikolojia ya maeneo ya Vijijini (Ecosystem Based Adaptation for Rural  Resilleience). Thamani ya Mradi huu ni Dola za Marekani milioni 7.57. Utekelezaji utafanyika kwa kushirikiana na Programu ya Mazingira ya Umoja wa Mataifa (United Nations Environment Programme - UNEP). Mradi huu uko katika hatua za awali za utekelezaji.
(c)  Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Usimamizi wa Urejeshwaji wa Maeneo ya Mifumo-ikolojia yaliyoharibika na kuboresha uhifadhi wa bioanuai (Supporting the Implementation of Integrated Ecosystem Management Approach for Landscape restoration and Biodiversity Conservation in Tanzania). Thamani ya Mradi huu ni Dola za Marekani milioni 12.14. Programu ya Mazingira ya Umoja wa Mataifa (United Nations Environment Programme - UNEP). Utekelezaji wa Mradi huu unatarajiwa kuanza rasmi katika kipindi cha mwaka 2017/18.
(d) Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Bonde la Ziwa Nyasa (Sustainable Land Management of the Lake Nyasa Catchment). Thamani ya Mradi huu ni Dola za Marekani milioni 1.3. Utekelezaji utafanyika kwa kushirikiana na Programu ya Mazingira ya Umoja wa Mataifa (United Nations Envionment Programme - UNEP). Mradi huu pia uko katika hatua za awali za utekelezaji.

Ndugu wajumbe;
Uzinduzi wa Kamati hii ya Ushauri wa Mazingira umekuja muda muafaka wakati ambapo serikali inaendelea kushughulikia  changamoto za uharibifu wa mazingira nchini ambazo zinakua kila kuchapo. Ujuzi, utaalamu, weledi na uzoefu wenu katika nyanja mbalimbali unategemewa sana katika kutoa ushauri muafaka katika kukabiliana na changamoto zinazotukabili. Ni matumaini yangu kwamba tutashirikiana vyema katika kazi hii ili kutimiza azma ya serikali ya kuwa na Tanzania ya viwanda bila kuathiri mazingira yetu na hivyo kuchangia katika maendeleo endelevu kwa taifa zima. Sisi kama wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Ushauri wa mazingira tunategemewa kutoa ushauri ambao utasaidia kujikwamua na changamoto za uharibifu wa mazingira nchini. Ni lazima sasa kama taifa tuchukue hatua zenye mtizamo mpya katika kukabiliana na changamoto hizi ili kutimiza azma ya matarajio ya serikali ya awamu ya tano ya Tanzania ya viwanda.
Ndugu wajumbe;
Uwepo wenu katika Kamati hii unatarajiwa kusaidia sana katika kushauri mbinu na mitazamo mipya na bora zaidi ya jinsi ya kukabiliana na kupunguza changamoto za uharibifu wa mazingira nchini. Hili sina shaka nalo kwani nikiangalia mchanganyiko wa wajumbe wa Kamati hii pamoja na uwakilishi mpana kutoka kwenye sekta mbalimbali, ujuzi, majukumu na uzoefu mlio nao naamini kabisa Kamati hii itakua na mchango mkubwa katika kutekeleza majukumu yake.
Ndugu wajumbe;
Jukumu lililo mbele yenu ni kushauri na kusaidia katika kutekeleza Sera, Sheria, Mikakati na Mipango tuliyojiwekea. Ni matumaini yangu leo mtapata fursa ya kupitishwa kwenye masuala mbalimbali ambayo ninyi kama Kamati ya Ushauri kwa Waziri mwenye dhamana ya Mazingira ningependa kupata ushauri wenu wa kitaalamu baada ya kuyajadili kwa pamoja. Mtakavyoendelea kufanya hivyo, Kamati hii itakua na mchango mkubwa katika kushughulikia changamoto za mazingira bila misigano. Napenda kusisitiza kwamba hifadhi ya mazingira na matumizi bora ya rasilimali zake ndio msingi wa maendeleo endelevu, na ni wajibu wetu sote. Sote tuchangie katika namna bora ya kukabiliana na changamoto za uharibifu wa mazingira nchini kwa maendeleo endelevu bila kujali unatoka sekta gani kwani ushauri wenu utatufanya tutoke pale tulipokwama.
Baada ya kusema hayo nawatakia heri katika kazi iliyo mbele yenu na ninayo furaha kuizindua rasmi Kamati hii ya Ushauri wa Mazingira (National Environmental Advisory Commitee – NEAC).

ASANTENI SANA

WAZIRI JAFO: Wakuu wa Wilaya Simamieni kazi zinazofanywa na TARURA

December 19, 2017
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mh. Selemani Jafo amewaagiza Wakuu wa Wilaya wote nchini kusimamia  kazi zinazofanywa na Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA)  ili kuleta matokeo tarajiwa  katika kukuza ustawi wa kiuchimi nchini.
Akifungua kikao cha Wakuu wa Wilaya nchini kote, Mhe. Jafo amewataka Wakuu wa Wilaya kwenda kusiamamia barabara hizo kwa ukaribu ili barabara zitakazo jengwa ziwe na ubora na zitakazo dumu kwa muda mrefu.
Mhe. Jafo amewaambia wakuu hao kuwa uanzishwaji wa Wakala utainua chachu ya uzalishaji wa mazao kutokana na usafiri wa uhakika, ambapo mkulima atakuwa na uhakika wakusafirisha mazao, lakini pia kupunguza gharama za usafiri lakini pia kuboresha hali za maisha za watanzania.
Amesema Serikali imekuwa na changamoto kubwa sana ambapo wakandarasi wanaopatiwa kazi za ujenzi wa barabara kutokuwa waaminifu na kujenga chini ya kiwango, rushwa , hivyo ni kazi ya Mkuu wa Wilaya kusimamia ili kubaini mapungufu hayo kwa haraka na kuokoa fedha za Serikali.
Amesema kuwa baada ya kuifahamu TARURA ni jukumu lao kuibua maovu kwa wafanyakazi wanaofanya maovu ili waweze kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa kufuata sheria na taratibu za utumishi wa umma.
Amesema kuwa Wakuu wa Wilaya ni wawakilishi wa serikali katika maeneo yao, hivyo wanawajibu wa kusimamia kwa ukaribu zaidi katika usimamizi wa mradi ya Ujenzi wa Barabara nchini kwa kuzingatia kuwa asilimia 43 za barabara zinasimamiwa na TARURA zipo katika hali mbaya hivyo Mkuu wa Wilaya anajukumu la kusimamia kazi zinazotekelezwa kuanzia ngazi ya kata ili kuwa na kazi bora katika jamii. 
“Nimezunguka nchi hii karibu kila pembe ya nchi na kila nilipo Wakuu wangu wa Wilaya wamekuwa wakilia juu ya ubovu wa barabara, wengine kukiri kuumwa na migongo, alisema Jafo na kuongeza. “tunahitaji kuunganisha Vijiji, Wilaya na Mikoa kwa mtandao imara utakao wezesha vijiji vyote na maeneo yote ya vijijini na mijini vinafikika kwa wakati” Jafo.
Aidha  mbali  na kuhimiza kusimamia suala zima la barabara, Mhe.Jafo amerudia wito wa Waziri Mkuu wa kuwataka  waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na  Wakuu wa Wilaya kuzisiamamia Halmashauri ili ziweze kuchangia fedha kutoka katika mapato ya ndani.
Wakati huohuo Mkurugenzi Mtendaji Mkuu wa Wakala wa barabara Vijijini na Mijini Bw. Victor Seif amesema imekabidhiwa mtandao wa barabara wenye jumla ya km 108,946.2 ambapo kati ya hizo km 52,946.2 zinatambulika kisheria na km 56,000 mchakato wa kuzihakiki ili zitambulike kisheria unaendelea.
Amesema hali ya mtandao wa barabara nchini hadi kufikia  Disemba, 2016 ilionyesha kuwa asilimia 22.6 ilikuwa na hali nzuri, asilimia 34.2 hali ya wastani na asilimia 43.2 hali mbaya.
Aidha vikao vya kujenga uelewa kuhusu majukumu ya TARURA nchini  vimeeshatolewa kwa Wakuu wa Mikoa, Makatibu  Tawala wa Mikoa,  Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Waheshimiwa Madiwani, Kamati za kudumu za hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na  Kamati ya Serikali za Mitaa.
 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo katika kikao cha  Wakuu wa Wilaya kuhusiana na  kujenga uelewa wa majukumu ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini(TARURA) katika ukumbi wa Hazina Dodoma, leo.
 Baadhi ya Wakuu wa Wilaya waliohudhuria katika kikao cha kujenga uelewa wa majukumu ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini kilichofanyika katika ukumbi wa Hazina Dodoma, leo.