ZIARA YA NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS MH. UMMY MWALIMU MTWARA

December 10, 2014
Afisa Uhusiano wa kampuni ya SBS, Bw. Geofrey Kanenge  (katikati) akitoa maelezo kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (Mb) (wa pili kushoto)  kuhusu udhibiti wa utiririshaji wa maji taka yatokanayo na usafishaji wa mapipa yenye kemikali unavyofanywa na kampuni hiyo wakati wa ziara ya ukaguzi wa mazingira mkoani Mtwara.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (katikati) akipata maelezo kuhusu ubanguaji wa korosho kutoka kwa Uongozi wa Kiwanda cha Micronix  kilichopo mkoani Mtwara wakati wa ziara aliyoifanya mkoani humo.

Sehemu ya Wananchi wakimsikiliza Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mheshimiwa Ummy Mwalimu (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kukagua hali ya Mazingira ya viwanda  aliyoifanya mkoani Mtwara

Eneo la bwawa la asili la Mdenga lililofukiwa kinyume cha sheria na kampuni ya SBS inayojishughulisha na urejelezaji wa taka mkoani Mtwara na kusababisha uharibifu wa mazingira katika eneo hilo.

Na Mwandishi Wetu, Dar
NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira, Ummy Mwalimu, ameutaka uongozi wa kiwanda cha OK Plastic kilicho jijini Dar es Salaam, kuwasilisha mara moja ripoti ya mwaka ya ukaguzi wa mazingira kwa baraza la Usimamizi wa Mazingira (NEMC).
Alisema hayo Jumatano wiki hii alipofanya ziara katika kiwanda hicho ikiwa ni sehemu ya ziara zake katika viwanda mbalimbali nchini kuangalia hali ya utunzwaji wa mazingira hasa baada ya wananchi kulalamika kuwepo kwa uchafu wa mazingira katika maeneo ya viwanda katika mikoa mbalimbali.
Aidha, Ummy alitoa agizo kwa kiwanda hicho kusimamisha mara moja kutupa taka ngumu katika dampo la Kinyamwezi, kwa sababu ni hatari kwa afya za wakazi wa eneo hilo.
“Kwanini mnafanya hivi, naagiza msitishe mara moja kutupa taka ngumu katika dampo wala msichome mabaki ya taka katika eneo la kiwanda na mkiendelea nitahakikisha hatua za kisheria zinachukuliwa juu yenu kwa sababu mambo haya si ya kuyaacha yapite ivihivi,” alisema Ummy.
Aliongeza kuwa agizo hilo si kwa kiwanda cha OK Plastic peke yake bali ni viwanda vyote vya ndani na nje ya jiji hili kuhakikisha vinatunza mazingira na kuacha kuchoma taka za viwandani kwani moshi unaofuka husambaza hewa ya semu kwa wakazi wa jirani na viwanda hivyo hali inayohatarisha afya za binadamu.
Jumatatu wiki hii Ummy, alikuwa katika ziara kwenye mikoa ya Kusini hasa Mkoani Mtwara katika eneo la Mdenga, Manispaa ya Mtwara kwa lengo la kuitikia wito wa wananchi waliotoa malalamiko kwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, alipofanya ziara katika mikoa hiyo na kulalamika kuhusu uchafuzi wa mazingira.
Katika ziara hiyo Naibu Waziri huyo alitembelea viwanda vidogo vya ubanguaji korosho na maeneo mengine kama bwawa la asili la Mdenga mablo kwa sasa limefukiwa kutokana na shughuli zinazoendeshwa na kiwanda cha SBS kinachoshugulika na kuzirudisha taka katika matumizi (Recycling).
Ziara hizo ni muendelezo wa ziara nyingi zinazoendelea kufanywa na viongizi wa Ofisi ya Makamu wa Rais, zikiwa na lengo la kuhakikisha mazingira yanahifadhiwa na kutunzwa.