GST YAHITIMISHA WIKI YA MAAFA DUNIANI

October 13, 2023














*Zaidi ya wananchi 2500 wapata elimu ya Majanga ya Asili Manyara*


Maadhimisho ya Wiki ya Maafa Duniani yamefikia kilele chake leo Oktoba 13, 2023 katika viwanja vya Stendi ya Zamani Mkoani Manyara ambapo zaidi ya wananchi 2500 wametembelea banda la Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) ili kupata elimu ya Majanga ya Asili ya jiolojia.


Akizungumza kwa niaba ya Mtedaji Mkuu wa GST, Meneja wa Sehemu ya Mapping Economic Geology na Mkuu wa Kitengo cha Majanga ya Asili ya Jiolojia Gabriel Mbogoni ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa wananchi wote wanaoishi katika maeneo yenye miinuko yenye mawe na majabali kuchukua tahadhali ya Majanga ya Asili hususan katika kipindi hiki kinachotarajiwa kutokea kwa mvua za Elnino.


Mbogoni amesema, kwa mujibu wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 na Marekebisho yake ya Mwaka 2017 na 2019, GST ina jukumu la kufanya Menejimenti ya Majanga ya Asili ya Jiolojia kwa lengo la kuhakikisha madhara yatokanayo na Majanga hayo yanapungua.


Mbogoni ameyataja baadhi ya Majanga ya Asili ya jioloia yakiwemo matetemeko ya ardhi, milipuko ya volkano, sunami, kutitia kwa ardhi na maporomoko ya ardhi ambapo amesema GST imeshiriki katika maonyesho hayo ili kutoa elimu ya namna ya kupunguza madhara na kuepuka maafa yanayoweza kusababishwa na Majanga ya Asili ya Jiolojia.


Maadhimisho ya Wiki ya Maafa Duniani 2023 yenye Kauli Mbiu isemayo "Imarisha Usawa kwa Uthabiti Endelevu" yamefanyika Mjini Babati katika Mkoa wa Manyara ambapo yameenda sambamba na Wiki ya Vijana pamoja na Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru.

OFISI YA WAKILI MKUU WA SERIKALI YAOKOA ZAIDI YA BILIONI 600 NA DOLA ZA KIMAREKANI ZAIDI YA MILIONI 37

October 13, 2023

Wakili Mkuu wa Serikali Dkt Boniphace Luhende akizungumza wakati akifungua kikao cha cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/2024 kilichofanyika Jijini Tanga.
Wakili Mkuu wa Serikali Dkt Boniphace Luhende akizungumza wakati akifungua kikao cha cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/2024 kilichofanyika Jijini Tanga.
Makamu Mwenyekiti wa Baraza, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mark Mulwambo  akizungumza wakati wa akifungua kikao cha cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/2024 kilichofanyika Jijini Tanga.

Na Oscar Assenga, TANGA

SERIKALI kupitia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imefanikiwa kuokoa zaidi ya Sh Bilioni 600 na dola za Kimarekani milioni thelathini na saba nukta tatu nne ambazo zingelipwa kwa wadaiwa endapo Serikali ingeshindwa kwenye mashauri hayo.

Hayo yalibainishwa leo na Wakili Mkuu wa Serikali Dkt Boniphace Luhende wakati akifungua kikao cha cha Baraza la Pili la Wafanyakazi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/2024 kilichofanyika Jijini Tanga.

Alisema wanamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu kwa kuiendelea kuiwezesha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kutekeleza vema majukumu yake ya kuiwakilisha Serikali na Taasisi zake kwenye mashauri ya madai na usuluhushi ndani na nje ya nchi.

Aidha alisema majukumu hayo ni kuratibu, kusimamia na kuendesha mashauri ya madai na usuluhishi yanayofunguliwa dhidi au kwa niaba ya Serikali na Taasisi zake ndani na nje ya nchi.

“Tunamshukuru Rais Dkt Samia Suluhu kwani amekuwa akiendelea kuiwezesha Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kutekeleza vema majukumu yake ya kuiwakilisha Serikali na Taasisi zake kwenye mashauri ya madai na usuluhushi ndani na nje ya nchi”Alisema

Aliongeza kwamba katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2022/2023 Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali imeendesha mashauri 7,392 ambapo kati ya mashauri hayo 7,255 ni ya madai na 137 ni ya usuluhishi ambapo kati ya mashauri hayo 7,350 ni ya ndani ya nchi na 42 ni ya nje ya nchi.

Dkt Luhende alisema kwa kipindi hicho hicho Ofisi hiyo imemaliza jumla ya mashauri 620 ambapo mashauri 579 yalimalizika kwa njia za kimahakama na mashauri 41 yalimalizika kwa njia ya majadiliano nje ya mahakama.

Alisema kwamba wameshuhudia ongezeko la bajeti yao bungeni kwa ajili ya uendeshaji wa majukumu ya Serikali kuwatumikia wananchi kwa mwaka wa fedha 2023/2024 ambapo katika kipindi hicho ofisi ya wakili mkuu wa Serikali kupitia Wizara ya Katiba na Sheria ilifanikiwa kuongezewa bajeti kutoka zaidi ya Bilioni 12 kwa mwaka wa fedha 2022/2023 hadi kufikia zaidi ya Sh.Bilioni 17 kwa mwaka wa fedha 2023/2024 ambapo ongezeko hilo ni asilimia 25.

Awali akizungumza katika kikao hicho Makamu Mwenyekiti wa Baraza, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mark Mulwambo alisema katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ofisi hiyo imejiwekea vipaumbele mbalimbali ni pamoja na kuendelea kuratibu, kusimamia na kuiwakilisha serikali na taasisi zake katika kuendesha mashauri ya madai yanayofunguliwa dhidi ya Serikali kwenye mahakama au mabaraza mbalimbali ndani na nje ya nchi .

Alisema pia kuendelea kukamilisha ujenzi wa makao makuu ya ofisi ya wakili mkuu wa serikali unayoendelea mji wa serikali Mitumba mji Dodoma wanaishukuru serikali kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi huo.

Alisema pia wataendelea kuwajengea uwezo watumishi kwa kutoa mafunzo ya muda mrefu na mfupi ikiwemo mafunzo ya kibobevu katika maeneo maalumu ikiwemo ya sekta ya mafuta na gesi pamoja na usuhuluhi wa kimataifa kuimarisha ofisi za mkoa na hivi sasa wanaendelea kufungua ofisi nyengine mkoani Manyara.