NSSF KUANDAA UTARATIBU WA KUWAKOPESHA WANACHAMA WAKE.

August 06, 2013

Na Oscar Assenga, Tanga.
MFUKO wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), unaandaa utaratibu wa kuwakopesha wanachama wake sehemu ya michango yao wanayolipa kila mwezi ili kuwasaidia kuboresha maisha na kupambana na umasikini.

Sanjari na hilo, mfuko huo umewataka wananchi nchini kubadili mitizamo yao ya kuchangia harusi na sherehe mbalimbali za kijamii na badala yake wawekeze sehemu ya fedha wanazozipata, katika mifuko ya hifadhi ya jamii.

Akizungumza katika semina ya siku tatu kwa Jumuiya ya Wanawake nchini (UWT) inayofanyika Jijini Tanga, Meneja wa NSSF mkoa wa Tanga, Frank Maduga, alisema kuwa mfuko huo unaandaa utaratibu utawawezesha wananchama kukopeshwa fedha kukidhi mahitaji yao.

“Wadhamini wa mfuko wanaandaa utaratibu ambao utawawezesha kukopa kile wanachochangia kila mwezi,hii itawasaidia wanachama wetu kuona ni namna gani wanaweza kupambana na umasikini,” alisema Maduga.

Alisema wananchi hapa nchini lazima wafahamu maisha yamekuwa na changamoto nyingi hivyo suala la kuhifadhi fedha katika mifuko ya jamii ni suala la kisheria ambalo wanatakiwa walipe kipaumbele kwa ajili ya kuwasaidia hapo baadae.

“Wananchi lazima waweke kipaumbe katika suala la akiba kwa maisha ya baadaye…Hii michango ya harusi wanayojali zaidi haina faida faida wajue maisha yamekuwa na changamoto nyingi kwa sasa ni bora wakajali na kuwekeza katika mifuko ya jamii,” alisema Maduga.

Hata hivyo, alikemea tabia ya jamii ya watu wa mkoa wa Tanga, kila inapofika wakati wa sikukuu na mwanzoni mwa mwaka, wanajitoa kuchangia katika mfuko huo na kuchukua fedha zao kwa ajili ya matuminzi ya wakati huo akieleza kwamba hayana faida.

Alisema ni vema wananchi wakaendelea kuchangia kwa faida ya baadaye kuliko kuchangia kisha kuchukua fedha hizo kwa lengo la kujitoa akieleza kwamba matokeo yake, hawawezi kujiwekea akiba ya mbeleni.

Miongoni mwa wajumbe katika semina hiyo Mbunge Viti maalum Singida,Martha Mlata aalisema mafunzo hayo yametolewa muda muafaka kwani yameweza kuwajenga kisiasa.

Alisema kuwa watahakikisha wanakwenda kuhamasisha wanachama ili waone umuhimu wa kujiunga na mfuko huo kuweza kupata mafao ya uzeeni sambamba na matibabu pindi wanapougua.
MWISHO

RUKSA 3PILLARS KUCHEZA MECHI ZA KIRAFIKI

August 06, 2013
Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.
  
Timu ya 3Pillars Football Club ya Nigeria sasa inaruhusiwa kucheza mechi za kirafiki nchini baada ya kupata idhini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu la Nigeria (NFF).

Awali tuliikatalia timu hiyo kucheza mechi za kirafiki nchini kwa vile haikuwa na barua kutoka NFF, lakini sasa Shirikisho hilo limetoa idhini hiyo. 

Pia ziara yake haikuwa inaratibiwa na wakala wa mechi anayetambuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) au mwanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Klabu hiyo kutoka Jimbo la Lagos ilipanga ziara hiyo kwa kuwasiliana na chama cha mpira wa miguu cha jimbo hilo ambacho nacho kilitakiwa kuomba idhini NFF kwa niaba ya 3Pillars.

Hivyo timu hiyo inaweza kucheza mechi, kwani ziara hiyo sasa inaratibiwa na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) ambaye ni mwanachama wetu.

Tunapenda kukumbusha kuwa watu pekee wanaotakiwa kuandaa mechi za kirafiki za kimataifa ni mawakala wa mechi wanaotambuliwa na FIFA au wanachama wa TFF.

USAJILI WA WACHEZAJI HATUA YA KWANZA WAMALIZIKA

August 06, 2013
Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.
Hatua ya kwanza ya usajili wa wachezaji kwa msimu wa 2013/2014 imefungwa rasmi jana (Agosti 5 mwaka huu) ambapo klabu zote za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) zimewasilisha usajili wa vikosi vyao ndani ya wakati.

Baadhi ya klabu zimefanya makosa madogo madogo katika usajili ambapo zimepewa siku ya leo (Agosti 6 mwaka huu) kufanyia marekebisho kasoro hizo. Hivyo kesho (Agosti 7 mwaka huu) majina ya vikosi vyote yatabandikwa kwenye mbao za matangazo za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kwa ajili ya kipindi cha pingamizi kitakachomalizika Agosti 12 mwaka huu.

Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa itakutana Agosti 13 na 14 mwaka huu kupitia na kufanyia uamuzi usajili wa wachezaji wenye matatizo.

Hatua ya pili ya usajili itaanza tena Agosti 14 mwaka huu ikihusisha wachezaji ambao watakuwa hawajasajiliwa katika Ligi Kuu ya Vodacom msimu huu na wale kutoka nje ya Tanzania. Hivyo, dirisha la uhamisho kwa wachezaji wa kimataifa litafungwa baada ya hatua ya pili ya usajili kumalizika Agosti 29 mwaka huu.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

AURORA :HAKUNA TIMU ITAKAYOTUTISHA MSIMU UJAO.

August 06, 2013
Na Oscar Assenga,Tanga.
MWENYEKITI wa Klabu ya Coastal Union ya Tanga,Hemed Aurora (pichani juu kushoto)amesema hakuna timu yoyote itakayowasumbua katika msimu mpya wa Ligi kuu Tanzania bara ambayo itaanza Agosti 24 mwaka huu kutokana na timu yao kusheheni wachezaji wenye viwango vizuri.

Aurora alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki wakati wa futari iliyoandaliwa na timu hiyo kwa ajili ya wachezaji wa timu hiyo na viongozi wake iliyofanyika Raskazone Hotel jijini Tanga na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali.

Alisema kikosi kilichosajiliwa na timu hiyo msimu huu ni kizuri ambacho kitaleta upinzani mkubwa kwenye mechi mbalimbali za ligi hiyo ambayo inashirikisha timu 14 kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini huku akiwataka wapenzi,mashabiki wa timu hiyo wakiwemo wanachama kutarajia makubwa kutoka kwao.

Mwenyekiti huyo alisema kipimo tosha cha kwamba kikosi chao kimeiva na kipo imara ni ushindi walioupata kwenye mechi mbili za majaribio ambapo waliifunga Simba na URA ya Uganda ambapo kwenye michezo hiyo kikosi hicho kilionyesha uwezo wa hali ya juu.

    "Tunataka kurudisha historia ya mwaka 1988 ya kuchukua ubingwa wa ligi kuu Tanzania bara kwani hilo linawezekana na tunaima litafanikiwa kwa asilimia kubwa ili kuweza kuwapa raha wapenzi wa soka mkoani hapa "Alisema Aurora.

Aidha Aurora alisema wanaamini kuwa pointi tatu muhimu kwenye mechi yao ya ufunguzi wa kuu hapa nchini dhidi yao na JKT Oljoro haina ubishi kwani watakachokifanya katika mchezo huo ni kupambana kufa na kupona ili kuanza vema msimu mpya.

Ligi kuu ya soka Tanzania bara itaanza Agosti 24 mwaka huu ambapo jumla ya viwanja saba vitawaka moto kwa mabingwa watetezi wa

Kombe hilo Yanga kuvaana na Ashante United iliyopanda ligi kuu msimu huu kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam,Mtibwa Sugar watacheza na Azam Fc kwenye uwanja wa Manungu mkoani Morogoro,JKT Oljoro na Coastal Union mchezo utakaopigwa katika dimba la

Sheirh Amri Abeid mkoani Arusha,Mgambo Shooting na JKT Ruvu uwanja wa Mkwakwani,Rhino Rangers iliyopanda daraja msimu huu  itakipiga na Simba kwenye uwanja wa Ally Hassani Mwinyi mkoani Tabora.

Mechi nyengine zitakazofungua pazia la michuano hiyo ni Mbeya City nayo iliyopanda daraja msimu huu itacheza na Kagera Sugar kwenye uwanja wa Sokoine mkoani Mbeya huku mechi ya mwisho ikiwa ni Ruvu Shooting na Tanzania Prison kwenye dimba la Mabatini Mlandizi mkoani Pwani.

Mwisho.