JIJI TANGA WAENDELEA KUNYANYASA SHIMISEMITA DODOMA.

November 01, 2013


Na Twahiru Mdimu,Dodoma. 

TIMU ya Mpira wa Miguu ya Halmashauri ya Jiji la Tanga leo Imefanikiwa kukata tiketi ya kucheza hatua ya nusu fainali ya mashindano ya Serikali za Mitaa nchini (Shimisemita)baada ya kuibamiza Mtwara Mikindani mabao 2-0,kwenye mchezo wa robo fainali uliochezwa dimba la Jamhuri mkoani Dodoma.

Mchezo huo ambao ulikuwa wa aina yake huku timu ya Halmashauri ya Jiji la Tanga ikionekana kuutawala kipindi cha kwanza na cha pili kwa kucheza kwa umakini mkubwa na kufanikiwa kuandika bao lao la kwanza ambalo lilifungwa na Ibrahim Mustapha katika dakika ya 8.

Mpaka timu zote zinakwenda mapumziko,Halmashauri ya Jiji la Tanga ilikuwa ikiongoza katika mchezo huo ambapo kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku kila timu ikionekana kujipanga vema .

Wakionekana kucheza kwa umakini na umahiri mkubwa Halmashauri ya Jiji la Tanga waliweza kupeleka mashambulizi mara kwa mara langoni mwa Mtwara Mikindani na kufanikiwa kupata bao lao la pili kwenye dakika ya 80 ambalo lilifungwa nyota wa mchezo huo Ibrahim Mustapha.

Akizungumza na Tanga Raha mara baada ya kumalizika mchezo huo,Mweka Hazina wa timu ya Jiji la Tanga,Twahiru Mdimu aliwapongeza wachezaji wa timu hiyo kwa kuendelea kulipa heshima jiji hili kwa kufanya vizuri kwenye michezo yao wanayokuwa wakicheza.

Licha ya kuwapongeza wachezaji hao ,aliwataka kuhakikisha wanaendelea kuilinda heshima ya jiji la Tanga kwa kufanya vizuri kwenye mechi yao ya nusu fainali ambayo itachezwa kesho kati yao na timu ya Kyela.

Akizungumzia hali za wachezaji wa timu ya Tanga,Mdimu alisema wanaendelea vizuri isipokuwa wachezaji wawili ambao wamepata majeraha katika mechi yao ya leo ambapo ni Daudi Kiweri.

TAARIFA KUTOKA SHIRIKISHO LA SOKA TFF LEO

November 01, 2013

Release No. 189
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Novemba 1, 2013

MECHI YA SIMBA, KAGERA YAINGIZA MIL 32
Mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Kagera iliyochezwa jana (Oktoba 31 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 32,726,000.

Washabiki waliohudhuria mechi hiyo namba 81 iliyomalizika kwa timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 walikuwa 5,541 ambapo viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000.

Mgawo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh. 4,992,101.69, gharama za kuchapa tiketi sh. 3,183,890 wakati kila klabu ilipata sh. 7,242,252.45.

Wamiliki wa uwanja walipata sh. 3,682,501.25, gharama za mchezo sh. 2,209,500.75, Bodi ya Ligi sh. 2,209,500.75, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,104,750.37, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 859,250.29.

VPL YAENDELEA RAUNDI YA 12
Raundi ya 12 ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) ambayo ipo katika raundi yake ya 12 inaendelea kesho (Novemba 2 mwaka huu) kwa mechi nne zitakazochezwa katika miji minne tofauti.

Mgambo Shooting na Coastal Union zitaoneshana kazi kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, Mbeya City na Ashanti United zitaumana kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya, Azam na Ruvu Shooting (Azam Complex, Dar es Salaam), na Mtibwa Sugar na Rhino Rangers (Uwanja wa Manungu, Morogoro).

Raundi hiyo itakamilika Novemba 3 mwaka huu kwa mechi moja ambapo Tanzania Prisons itakuwa mwenyeji wa Oljoro kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Mechi za kukamilisha mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo zitachezwa Novemba 6 na 7 mwaka huu. Novemba 6 ni JKT Ruvu vs Coastal Union, Ashanti United vs Simba, Kagera Sugar vs Mgambo Shooting, na Ruvu Shooting vs Mtibwa Sugar.

Novemba 7 mwaka huu, Azam itacheza na Mbeya City, Yanga itacheza na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Rhino itakuwa mwenyeji wa Tanzania Prisons.

Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

TIMU ZA HALMASHAURI YA JIJI LA TANGA ZAENDELEA KUTESA SHIMISEMITA

November 01, 2013


Na Twahiru Mdimu ,Dodoma.
MASHINDANO ya Shirikisho za Serikali za Mitaa(Shimisemita) yanayoendelea kutimua vumbi mkoani Dodoma yameingia hatua ya robo fainali huku timu kutoka Halmashauri ya Jiji la Tanga zikiendelea kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Timu za Halmashauri ya Jiji la Tanga kutokana na kufanya vizuri katika mashindano hayo leo zimefanikiwa kuingia hatua ya robo fainali ambapo mechi hizo zitaanza majira ya saa nane mchana.

Kwa mujibu wa taarifa zilizoifikia blog ya Tanga Raha zimeeleza kuwa timu ya Halmashauri ya Jiji la Tanga leo jioni itakuwa na kibarua kizito kuweza kuwakabili timu ya Halmashauri ya Mtwara Mikindani kwenye mchezo wa mpira wa miguu.

Katika mchezo mwengine unaotarajiwa kuwa na upinzani wa hali ya juu ni wa pete ambapo timu ya Halmashauri ya Jiji la Tanga watakapowakabiliana wenzao kutoka Halmashauri ya wilaya ya Kyela.

Licha ya kuchezwa mchezo huo kutakuwa na mechi nyengine ambayo itachezwa saa kumi jioni Halmashauri ya wilaya ya Kinondoni watacheza na Halmashauri ya wilaya ya Ulanga kwenye michezo ambao unatazamiwa kuwa na upinzani mkubwa.

DC DENDEGO KUFUNGUA PAZIA LA LIGI YA UVCCM CUP MABAWA

November 01, 2013


Na Oscar Assenga,Tanga.
MKUU wa wilaya ya Tanga,Halima Dendego anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa Ligi ya Umoja wa Vijana kata ya Mabawa (UVCCM)itakayoanza kutimua vumbi Jumapili wiki hii kwenye viwanja wa soka Mikanjuni Sekondari.

Akizungumza leo,Mwenyekiti wa UVCCM Kata ya Mabawa, Ramadhani Hanaph alisema maandalizi ya kuelekea mashindano hayo yanaendelea vizuri na kinachosubiriwa ni kuanza kwake.

Hanaph alisema mashindano hayo yatashirikisha timu kumi na tatu ambazo zitagawanywa katika makundi mawili ambayo itachezwa kwa mfumo wa ligi.

Alisema mashindano hayo yatafunguliwa Jumapili kuanza majira ya saa tisa mchana ambapo zitaanza shamrashamra kwa timu zote kumi na tatu kujipanga kwenye mstari ili kusubiri kukaguliwa na mgeni rasmi.

Mwenyekiti huyo alisema lengo la mashindano hayo ni kuinua vipaji katika kata hiyo na kuhamasisha vijana kupenga michezo na kujiepusha kutumia madawa ya kulevya.