WANACHAMA MFUKO WA BIMA YA AFYA TANGA WAENDELEA KUONGEZEKA

November 09, 2013
Na Oscar Assenga,Tanga.
IMEELEZWA kuwa idadi ya wanachama wa Mfuko wa Bima ya Afya mkoa wa Tanga(NHIF) katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita imekuwa ikiongezeka toka 17,487 mwaka 2011-2012 hadi kufikia 17,490 mwaka 2013-2014.
Haya yalielezwa na Mkurugenzi wa uhai na takwimu wa  mfuko wa bima ya Afya nchini (NHIF)Michael Mhando wakati akitoa takwimu hizo katika mkutano wa wadau wa NHIF na CHF mkoa wa Tanga uliofanyika katika ukumbi wa mkuu wa mkoa wa Tanga ambao ulifunguliwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga Benedict Ole Kuyani.
Alisema katika kipindi hicho idadi ya wanachama wa CHF imeongezeka kutoka 30,920 hadi 39,932 ambapo ongezeko hilo linadhihirisha kuwa wananchi wamekuwa na hamasa kubwa ya kujiunga na mfuko huo kutokana na kuimarika kwa huduma zake.
Aidha alieleza kuwa kwa kadiri siku zinavyozidi kusogea mbele wananchi wengi zaidi watajiunga na kunufaika na huduma za matibabu kupitia utaratibu wa kuchangia kabla ya kuugua .
Mhando alisema mikutano hiyo ya wadau ni muhimu kwani inawasaidia kubaini matatizo yaliyokuwa yanawakabili wadau wao na hivyo kuwapa nafasi ya kuweka mikakati ya kukabiliana nayo ili kuhakikisha yanakwisha.
Aliongeza kuwa maoni hayo yanawasaidia kufikia maamuzi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufungua wigo kwa watanzania wengi ambapo hadi sasa kila mwananchi anayetaka kujiunga na mfuko huo anaweza kufanya hivyo.
Mkurugenzi huyo aliwaomba viongozi wa mikoa katika ngazi mbalimbali wafanye mijadala kuhusu huduma za NHIF na CHF/TIKA kuwa liwe ni ajenda ya kuduma katika vikao vyao vya maamuzi ili matatizo yanayoweza kukabiliwa katika ngazi hizo yasisubiri maamuzi ya ngazi za juu.