LUKUVI ATOA HATI KWA WANANCHI WA MAKAZI HOLELA MOROGORO.

LUKUVI ATOA HATI KWA WANANCHI WA MAKAZI HOLELA MOROGORO.

October 17, 2016
luv1
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi akimuhoji Afisa ardhi Manispaa ya Morogoro Bw. Abenance Kanomoga (wa kwanza kushoto), kwanini amekaa na hati za wananchi kwa zaidi ya mwaka mmoja bila kuwajulisha wahusika kuja kuzichukua.
luv2
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi akigawa hati kwa wakazi wa Bigwa mkoani Morogoro..
luv3
Baadhi ya wananchi wa mkoani Morogoro wakimsikiliza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi.
luv4
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi ajiongea na wananchi wa mkoani Morogoro.
…………………………………………………………………………
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi katika ziara yake ya mkoani Morogoro (17-10-2016) ameendelea kutekeleza program ya kurasimisha makazi holela kwa wananchi 116, ambapo amegawa hati 60 za awali na kumuagiza Afisa ardhi kuhakikisha anatoa hati zilizobakia ndani ya mwezi mmoja.
Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika mpango wake wa kuboresha maendeleo ya wananchi na makazi yao, imeanzisha program ya kurasimisha makazi holela kwa wananchi. Mpango huu ni wakupima, kupanga na kuwapatia hati wananchi waliojenga katika makazi yasio na mpangilio rasmi.
Akiwa mkoani morogoro Mhe. Waziri alitembelea baadhi ya makazi ya wananchi hao katika kata ya Bigwa na kujionea jinsi wananchi wanavyounga mkono juhudi za serikali katika kurasimisha makazi holela.
Wananchi hao wa Bigwa kwa umoja wao walipima ardhi zao na kufuata utaratibu wa mipango miji kwa mujibu wa taratibu za serikali.
Aidha, Lukuvi alifanya ziara ya kushtukiza katika Masijara ya Ardhi ya Manispaa ya Morogoro, na kukuta idadi kubwa ya hati za wananchi zimekaa zaidi ya mwaka mzima bila ya kuwafikia wahusika. Alihoji juu ya suala hilo, na kutoa agizo kwa Mkurugenzi wa Manispaa hati hizo kuwafikia walengwa ndani ya mwezi mmoja.
Baada ya ziara hiyo Mheshimiwa Waziri aliongea na wananchi wa Morogoro katika ofisi za Manispaa ya Morogoro na kusikiliza kero zao mbalimbali za ardhi na kuzitatua papohapo. Katika mazungumzo yake aliwataka wananchi waunge mkono juhudi za serikali kurasimisha makazi yao ili waweze kuishi katika makazi salama yanayotambulika na pia waweze kufaidika na ardhi yao kama kupata mikopo Benki au katika mambo mengine ya maendeleo yao.

Mkuu wa wilaya ya Iringa Akutana na wamiliki wa Daladala

October 17, 2016





Na Mathias Canal

Mkuu wa wilaya ya Iringa Mh Richard Kasesela amekutana na umoja wa wamiliki wa Daladala Wilayani Iringa katika ukumbi wa Siasa na kilimo kwa lengo la kujadili changamoto mbalimbali zinazo wakabili.

Wakizungumza mbele ya Mkuu wa wilaya hiyo Baadhi ya madereva na Makondakta wameomba kurudishwa katika Stendi ya miyomboni kama ilivyo kuwa hapo awali wakidai kuwa eneo la walilohamishiwa kwa sasa la Mashine tatu ni finyu na lina msongamano mkubwa wa watu jambo ambalo ni hatari kwa usalama wa wananchi.

Dc Kasesela amesema kuwa kurudi katika standi ya miyomboni ni jambo lisilo wezekana kutokana na eneo hilo kuwa dogo na limezungukwa na makazi ya watu pamoja na majengo makubwa ya biashara jambo ambalo linafanya eneo hilo kuwa hatarishi zaidi kama iwapo kunaweza kutokea janga la moto.

"Unajua Miyomboni ni padogo sana pia pamejibana sasa kama ikitokea moto umewaka pale ni ngumu sana kupafikia kwa wepesi lakini pia Watu wa zima moto ndio waliopendekeza kuwa kituo kile kihamishwe sasa nadhani mnafahamu kuwa sheria ya zimamoto huwa ni ngumu kuipinga" Alisema Kasesera

Lakini pia amewataka madereva kuacha kutumika kisiasa kwani wanaofanya hivo wanafanya kwa maslahi yao binafsi.

JAMII ZA WAKULIMA NA WAFUGAJI WILAYANI KILOSA ZATAKIWA KUISHI KWA AMANI

October 17, 2016


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. January Makamba akizungumza na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Kebwe Stephen Kebwe. Waziri Makamba yuko Mkoani Morogoro kwa ziara ya kikazi ya siku mbili.



Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. January Makamba, wa tatu kutoka kulia akiangalia chanzo cha maji kilichovamiwa katika Mto Mambogo



Wananchi wa Kijiji cha Parakuyo wakisalimiana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. January Makamba kabla ya kufanya mkutano wa hadhara kijijini hapo.



Sehemu ya Wananchi wa waliojitokeza katika Mkutano wa hadhara katika kijiji cha Parakuyo Wilayani Kilosa. Wananchi hao walimweleza Waziri changamoto zinazowakabili juu ya Hifadhi ya mazingira



Sehemu ya Wananchi wa waliojitokeza katika Mkutano wa hadhara katika kijiji cha Parakuyo Wilayani Kilosa. 



                      Na Lulu Mussa ,Morogoro


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. January Makamba ameitaka jamii ya watu wa Parakuyo katika Wilaya ya Kilosa kuishi kwa amani, uvumilivu na upendo miongoni mwao kwani ndio misingi ya watanzania.

Rai hiyo imetolewa leo katika Mkutano wa hadhara uliojumuisha jamii za wakulima na wafugaji ambazo zimekuwa na migogoro ya mara kwa mara. Waziri Makamba alizitaka jamii hizo kuishi kwa amani na kuhifadhi mazingira kwa faida ya sasa na vizazi vijavyo.

Miongoni mwa changamoto zilizobainishwa na jamii hiyo ni kutokuwa na elimu juu ya mabadiliko ya Tabianchi na athari zake pamoja na kutokuwepo na matumizi bora ya ardhi.

Waziri Makamba ameuagiza uongozi wa Wilaya na Kijiji kushirikiana pamoja kuunda kamati ya 'Amani' itakayokuwa na wajumbe kutoka pande zote mbili za wakulima na wafugaji na viongozi wa madhehebu ya dini ili kutafuta suluhu ya kudumu baina ya pande mbili ambazo zimekua na migogoro ya mara kwa mara. "Undeni Kamati hii mapema na Ofisi yangu itagharamia mafunzo kwa Kamati husika juu ya namna bora ya kutatua migogoro" alisisitiza Waziri Makamba.

katika jitihada za kukuza uelewa wa masuala ya mazingira na changamoto zake, Waziri Makamba ameitaka Serikali ya Kijiji kuunda Kamati ndogondogo za Mazingira ambazo zipo kwa mujibu wa sheria ya Mazingira na kuahidi kuipati mafunzo Kamati hizo ikiwa ni pamoja na kutengeneza sheria ndogo ndogo zitakazotumika kama nyenzo ya kuhifadhi na kusimamia Mazingira ya maeneo yao.

Aidha, Waziri Makamba amesema kuwa mpango wa matumizi bora ya ardhi ni muhimu sana na kuitaka jamii ya Parakuyo na Twa twa twa kushiriki kikamilifu katika zoezi la kuhakiki na kuhesabu mifugo yako ili kubaini ni ardhi kiasi gani inahitajika kwa wakulima na kiasi gani kwa wafugaji. "ndugu zangu niwasihi, Serikali ina nia ya dhati ya kuhakikisha kuna kuwa na matumizi bora ya ardhi, hivyo nawashauri mmshiriki kikamilifu katika zoezi hilo ili kupata uwiano wa idadi ya mifugo na ardhi iliyopo" Makamba aliongezea.

Awali katika ziara ya kikazi ya siku mbili Mkoani Morogoro Waziri Makamba pia alitembelea chanzo cha maji na kujionea changamoto za kimazingira katika mto Mambogo.