MKUTANO MKUU WA ALAT TAIFA WAANZA LEO MKOANI TANGA KUFUNGULIWA KESHO NA WAZIRI MKUU

May 13, 2014

Baadhi ya Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Jumuia ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT), wakiwa kwenye siku ya kwanza ya mkutano wa siku tatu wa kuadhimisha miaka 30 ya Serikali za mitaa ulioanza jijini Tanga leo.

UVCCM TANGA WATOA SOMO KWA VIONGOZI MIZIGO.

May 13, 2014
NA OSCAR ASSENGA,TANGA.
KATIBU wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Tanga(UVCCM)Mwajuma Rashid ametoa wito kwa viongozi wa ngazi mbalimbali mkoani hapa waliochaguliwa na wananchi na kushindwa kutekeleza wajibu wao wasihangaike kuchukua fomu za kuwania nafasi hizo kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu na uchaguzi mkuu 2015 kwani hawatawaunga mkono.

Mwajuma alitoa wito huo mwishoni mwa wiki wakati wa kikao cha kamati ya utekeleza ya Jumuiya ya Umoja wa Vijana Mkoa kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chama cha Mapinduzi uliopo mjini hapa .

Alisema katika kikao hicho waliweza kujadili mambo mbalimbali kubwa likiwemo suala la uchaguzi mkuu ujazo na kukubaliana kuwa vijana wenye uwezo wa kuwania nafasi mbalimbali za uongozi walijitokeze kwani wao watawaunga mkono kwa asilimia kubwa lengo likiwa kuleta mabadiliko na chachu ya maendeleo kwenye jamii.

Aidha alisema vijana wanapaswa kujithatiti na kuangalia namna ya
kuweza kuwania nafasi hizo kuanza ngazi za serikali za mitaa,udiwani na ubunge kwa malengo ya kuwapa maendeleo wananchi wanaowapa ridhaa ya kuwaongoza.

Alisema viongozi ambao walikuwa ni mizigo kwa kushindwa kuwajibika watambue kuwa jumuiya hiyo haitawaunga mkono hivyo ni bora waache kuchukua fomu na kusisitiza ikiwezekana watawafuata na kuwaeleza zaidi kuwa hawatoshi kugombea.

     “Tupo mbioni kuwaambia ukweli wagombea ambao hawajatekeleza wajibu wao kwani hatupo tayari kukiona chama kinashindwa kupata ridhaa ya kuwaongoza wananchi kwa sababu ya kiongozi ambaye hatekelezi wajibu wake “Alisema Mwajuma.

Hata hivyo alizungumzia suala la makundi ambapo alisema hali hiyo
haiwezi kuzuilika ila wanapaswa kusubiri na kuwa na uvumilivu kwa sababu makundi ya tokea mwaka 2005 mpaka leo yapo lakini wanapaswa kuyavunja na kuanza upya kwa kuwaunga mkono wagombea waliojitokeza.

Mwajuma alisema kwa sababu kuzuia makundi kwenye chama ni kazi ngumu lakini wakishapatikana wagombea kuyavunje na kueleza makundi hayo zaidi yanakuwa na wapambe na kuwataka wapambe kuwa wagombea wao wanaposhindwa basi wakubaliane na matokeo.

MKUTANO WA RAIS, KLABU ZA VPL

May 13, 2014
NA BONIFACE WAMBURA,DAR ES SALAAM.
Mkutano wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi na wenyeviti wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kupata maoni yao juu ya changamoto zilizojitokeza katika ligi hiyo umefanyika juzi (Mei 11 mwaka huu).

Klabu za VPL zilizohudhuria mkutano huo ni Azam, Coastal Union, JKT Ruvu, Mbeya City, Mgambo Shooting, Mtibwa Sugar, Polisi Morogoro, Ndanda FC, Ruvu Shooting, Stand United na Tanzania Prisons.

Simba na Yanga hazikuhudhuria mkutano huo, na wala klabu hizo hazikutoa udhuru wowote wa kutokuwepo.

Maazimio ya mkutano huo ni kuwa kwa misimu mitatu ijayo kuanzia msimu wa 2014/2015 klabu zimekubaliana ziruhusiwe kusajili wachezaji watano wa kigeni. Kamati ya Utendaji ya TFF itatoa uamuzi wa mwisho juu ya suala hilo katika kikao chake kijacho.

Pia klabu hizo zimekubali timu zao za U20 kuanzia msimu ujao zicheze ligi ya mkondo mmoja. Hata hivyo, utekelezaji wa hilo utategemea na upatikanaji wa mdhamini wa ligi hiyo ambapo TFF inafanya jitihada za kumpata mdhamini huyo.

Vilevile Mwenyekiti wa Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake, Lina Kessy amezishauri klabu za VPL kuanzisha timu za wanawake, ambapo klabu hizo zimesema zitaufanyia kazi ushauri huo.

KIINGILIO MECHI YA TAIFA STARS 5,000/-
Kiingilio cha chini cha mechi ya kwanza ya raundi ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika 2015 nchini Morocco kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Zimbabwe (Mighty Warriors) itakayochezwa Jumapili (Mei 18 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ni sh. 5,000.

Washabiki watakaolipa kiingilio hicho ni kwa wale watakaokaa kwenye viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa upande wa VIP B na C kiingilio kitakuwa sh. 10,000 wakati kwa VIP A itakuwa ni sh. 20,000.

Tiketi zinatarajiwa kuanza kuuzwa siku moja kabla ya mechi hiyo katika vituo mbalimbali jijini Dar es Salaam, na uwanja siku ya mchezo huo utakaoanza saa 10 kamili jioni.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ikiwa chini ya Kocha Mart Nooij inatarajia kurejea jijini Dar es Slaam kesho (Mei 14 mwaka huu) kutoka Mbeya kuendelea na maandalizi ya kuikabili Zimbabwe.

RAMBIRAMBI MSIBA WA MKUFUNZI KASINDE
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha Mkufunzi wa waamuzi nchini, Omari Kasinde kilichotokea jana (Mei 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Mbali ya kuwa Mkufunzi, Kasinde ambaye anazikwa leo (Mei 13 mwaka huu) mchana katika Makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam pia alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati iliyopita ya Waamuzi ya TFF iliyokuwa chini ya uenyekiti wa Kapteni mstaafu Stanley Lugenge.

Msiba huo ni mkubwa katika fani ya mpira wa miguu nchini kwani, Kasinde enzi za uhai wake alitoa mchango mkubwa katika mchezo huu tangu akiwa mwamuzi na baadaye mkufunzi na kiongozi..

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Kasinde, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), na Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Bwana alitoa, Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe. Amina.


BONIFACE WAMBURA
OFISA HABARI NA MAWASILIANO
SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)