Chadema chawataka wafanyabiashara kutopandisha bei vyakula

July 15, 2013

Na Oscar Assenga, Tanga

MKURUGENZI wa haki za binadamu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Mkoa wa Tanga, Jonathan Bahweje amewataka wafanyabiashara kuacha kupandisha bei vyakula kipindi hiki cha mwezi mtukufu wa Ramadhani kwa Waislamu.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kuhamasisha chama hivi karibuni katika viwanja vya  Mwembe Mawazo, Bahweje amewataka wafanyabiashara hao kumkumbuka Mungu kwani mwezi huo ni waheri na baraka.

Amesema kuna baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakivitumia vipindi vya mwezi wa ramadhani kwa kupandisha bei vyakula na kujisahau kuwa ni mwezi wa Baraka na hivyo kuwataka kumkumbuka Mungu na  kuwapa wepesi wafungaji.

Amesema imekuwa kawaida kwa wafanyabiashara kuufanya mwezi wa Ramadhani kuwa ni kipindi cha kujitajirisha na kuwataka kuacha kufanya hivyo kwani kutasababisha kuwapa ugumu wafungaji.

Bahweje amewataka wafanyabiashara hao kuufanya mwezi huo kuwa ni wakutafuta Baraka na kupata malipo kutoka  kwa Mungu lengo likiwa ni kutoa nafasi kwa waumini kufunga mwezi huo na kutouona mgumu.

Akizungumza katika mkutano huo, Mwenyekiti wa Chadema Wilaya, Khalid Rashid, aliwataka wakazi wa Chumbageni kukiunga mkono chama hicho ili kiweze kuwaondoshea kero ambazo zinawakabili likiwemo wimbi la wizi wa madirishani usiku.
 
Amesema kero hiyo ambayo imeshindwa kupatiwa ufumbuzi na chama chenye Udiwani na hivyo kuadhimia kikifanikiwa kuchukua nafasi ya kuongoza kero hiyo itakuwa ya kwanza kuikomesha.

Amesema chama hicho kimeshindwa kuleta umoja na mshikamano na kuunda ulinzi shirikishi na badala yake matumaini ya kusogeza maendeleo yameshindikana na hivyo kuwataka wakazi hao kukiunga mkono chama hicho katika chaguzi zijazo.

Rashid amewataka wakazi hao kuacha kufanya makosa kwa kutokichagua Chadema kwani chama hicho kiko na sera za kumkomboa Mtanzania kutoka katika dimbwi la umasikini na kumuingiza katika maisha ya utajiri kwani nchi iko na rasilimali nyingi.

Mwisho.

Coastal Union yamalizana na Odula

July 15, 2013


Na Oscar Assenga,Tanga.
UONGOZI wa Klabu ya Coastal Union ya Tanga umesema tayari umeshamalizana na aliyekuwa mshambulizi wa timu ya Bandari ya Kenya,Christian Odula kwa mkataba wa miaka miwili kwa ajili ya kuichezea timu kwenye msimu mpya ambao utaanza Agosti mwaka huu.

Akizungumza na Blog hii,Katibu Mkuu wa timu ya Coastal Union ya Tanga,Kassim El Siagi alisema baada ya kumalizina na mchezaji huyo anatarajiwa kutua mkoani Tanga wiki ya leo akiwa na mchezaji mwengine wa timu hiyo Jerry Santos.

Siagi alisema msimu huu wamedhamiri kufanya usajili wa nguvu ambao utaifanya timu hiyo kuwa tishio kwenye mechi zao za Ligi kuu ya Tanzania bara kwani malengo yao ni kuchukua ubingwa wa mashindano hayo makubwa hapa nchini.

Aidha alisema timu hiyo itacheza mechi mbalimbali za majaribio nchini Kenya na timu za Sofapaka,Bandari na Goromahia lengo likiwa ni kukipa makali kikosi hicho ambacho kinatarajiwa kuwa tishio.

Katibu huyo aliwataka wapenzi na mashabiki wa timu hiyo kuendelea kujitokeza kuisapoti timu hiyo ili iweze kutimiza azma yao waliyojiwekea kwenye michuano hiyo.

Mwisho.

TENGA AWASHUKURU WAJUMBE WA MKUTANO MKUU TFF

July 15, 2013
Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amewashukuru wajumbe wa Mkutano Mkuu kwa michango yao, na utulivu waliouonesha katika kupitisha marekebisho ya Katiba ya TFF ya 2013.

Tenga amesema marekebisho hayo yatawasilishwa kesho  kwa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo kwa ajili ya kupitishwa ili mchakato wa uchaguzi uweze kuanza mara moja.

“Tutamuomba Msajili atusaidie kusajili haraka Katiba yetu ya 2013 ili tuingie katika mchakato wa uchaguzi. 


Kama tulivyotangaza awali tumepanga kufanya uchaguzi Septemba 29 mwaka huu, na tusingependa tarehe hiyo ipite,” amesema Rais Tenga wakati akizungumza na Waandishi wa Habari mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji.

Katika kikao chake, Kamati ya Utendaji  imepitisha Kanuni za Maadili, Kanuni za Nidhamu, na marekebisho kwenye Kanuni za Uchaguzi yanayotokana na kuundwa kwa Kamati ya Maadili.

TAIFA STARS KAMBINI TENA JULAI 4

July 15, 2013

Na Boniface Wambura,Dar es Salaam.

Timu ya Taifa (Taifa Stars) imeondoka leo asubuhi kwenda Mwanza ambapo itapiga kambi ya siku kumi kujiandaa kwa mechi ya marudiano dhidi ya Uganda (The Cranes) kutafuta tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imeondoka kwa ndege ya PrecisionAir na itafikia hoteli ya La Kairo wakati mazoezi yatafanyika Uwanja wa CCM Kirumba kulingana na programu ya Kocha Mkuu Kim Poulsen.

Wachezaji walioko katika kikosi hicho ni Juma Kaseja, Aggrey Morris, Mwadini Ally, Ally Mustafa, Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Erasto Nyoni, Haroub Nadir, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba, Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vincent Barnabas, Mudathiri Yahya, Athuman Idd na Haruni Chanongo.

Mechi ya marudiano itachezwa kati ya Julai 26 na 28 mwaka huu kwenye Uwanja wa Nelson Mandela ulioko Namboole nje kidogo ya Jiji la Kampala. Tarehe rasmi itapangwa na Shirikisho la Vyama vya Mpira wa Miguu vya Uganda (FUFA) siku kumi kabla ya mechi.

MECHI YA TAIFA STARS, UGANDA YAINGIZA MIL 113/-

July 15, 2013
Na Mwandishi Wetu,Dar es Salaam.

Mechi ya kwanza mchujo ya kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) iliyochezwa jana (Julai 13 mwaka huu) imeingiza sh. 113,268,000 kutokana na watazamaji 17,121.
 

Akizungumza na waandishi wa habari mapema leo,Ofisa Habari wa shirikisho la soka nchini TFF,Boniface Wambura amesema tiketi za kushuhudia mechi hiyo ziliuzwa kwa sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Wambura alisema mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 17,278,169.49 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh. 7,809,104.

Aidha alisema asilimia 15 ya uwanja sh. 13,227,108.98, asilimia 20 ya gharama za mechi sh. 17,636,145.30 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 4,409,036.33.

Hata hivyo alieleza kuwa asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh. 52,908,435.91 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 2,645,421.80 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.


Mwisho.

Uhuru,Boban wajaza mashabiki mazoezini

July 15, 2013
Na Oscar Assenga,Tanga.
WACHEZAJI waliosajili na timu ya Coastal Union ya Tanga,Uhuru Seleman na Haruna Moshi "Boban"jana walikuwa kivutio kikubwa kwenye mazoezi ya timu hiyo yaliyofanyika katika uwanja wa Mkwakwani mjini hapa.
 
Baada ya wachezaji hao kutua uwanjani hapo mashabiki wa soka mkoani hapa walianza kuingia kwa wingi huku wakiwa makini kuangalia aina ya uchezaji wao huku wengine wakiwashangilia mara kwa mara waliokuwa wakigusa mipira.
 
Akizungumza mara baada ya kumalizika mazoezi hayo,Uhuru alisema lengo la kuichezea klabu hiyo ni kuipa ushindi timu hiyo na  pamoja na kuisapoti timu hizo ifikie malengo yake iliyojiwekea kwa siku zijazo.
 
Uhuru alisema endapo wachezaji wanzie wataunganisha nguvu ya pamoja itasaidia timu hiyo kufikia malengo yake ya kuuutwaa ubingwa wa ligi kuu kwani hilo linawezekana iwapo mshikamano baina ya wachezaji utakuwepo.
 
"Ninaamini Coastal Union ni sehemu nzuri ya kuirudisha nafasi yangu kwenye timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars)kwa sababu niliwahi kuchaguliwa kuichezea timu ya Taifa nikitokea Coastal Union "Alisema Uhuru.

Kwa upande wake,Kocha Mkuu wa timu hiyo,Hemed Morroco aliwataka wachezaji ambao hawajawasili kwenye mazoezi kuwasili ili kuweza kuunganisha nguvu za pamoja kufanya maandalizi kabla ya kuanza msimu mpya wa Ligi kuu Tanzania bara.
 
Mwisho.

"RC Gallawa amuunga mkono DC Gambo sasa kuanzisha Gallawa Cup"

July 15, 2013
Na Oscar Assenga,Korogwe.

MKUU wa Mkoa wa Tanga,Chiku Gallawa ameunga mkono Mashindano ya Gambo Cup ambapo amehaidi kuanzisha Mashindano ya Gallawa Cup ambayo yatachezwa mkoa mzima wa Tanga lengo likiwa ni kukuza na kuinua kiwango vya soka mkoani hapa

Kauli ya Mkuu huyo wa Mkoa aliitoa wakati wa fainali ya Mashindano ya Vijana ya Gambo Cup yaliyofanyika katika viwanja vya chuo cha ualimu wilayani hapa ambapo alisema mashindano hayo yalikuwa na msisimuko na dhahiri kufika lengo lililokusudiwa la kuinua viwango vya soka wilayani humo.

Gallawa alisema michezo hivi sasa ni ajira ambayo inaweza kuwainua vijana kutoka katika maisha ya chini hadi juu hivyo hawapa budi kuzingatia na kujifunza kwa moyo mmoja ili kuweza kupata mafanikio yatokanayo na soka ambayo ni makubwa sana.

Aidha mkuu huyo wa mkoa alimpongeza Mkuu wa wilaya ya Korogwe,Mrisho Gambo kwa kuanzisha mashindano hayo ambayo faida zake ni nyingi kwa vijana ikiwemo ajira,huleta undugu na kuwaepusha vijana kufanya vitendo viovu badala yake kwenda uwanjani kucheza au kuangalia mpira.

Mkuu huyo wa Mkoa alisema Mashindano ya Gallawa Cup yataanza hivi karibuni na kila wilaya itapata fuksa ya kushiriki katika michuano hiyo ambayo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kwani kila timu itahitaji kujipanga vema kwa ajili ya kuchukua ubingwa huo.

Mwisho.

Odula atua Coastal Union.

July 15, 2013
(Picha juu ni Katibu Mkuu wa Klabu ya Coastal Union ya Tanga,Kassim El Siagi aliyevaa shati jeupe na mistari meusi akizungumza na mmiliki wa Blog hii kuhusu ujio wa mchezaji huyo ambao utaleta ushindani mkubwa sana)

Na Oscar Assenga,Tanga.
UONGOZI wa Klabu ya Coastal Union ya Tanga umesema tayari umeshamalizana na aliyekuwa mshambulizi wa timu ya Bandari ya Kenya,Christian Odula kwa mkataba wa miaka miwili kwa ajili ya kuichezea timu kwenye msimu mpya ambao utaanza Agosti mwaka huu.

Akizungumza na Blog hii,Katibu Mkuu wa timu ya Coastal Union ya Tanga,Kassim El Siagi alisema baada ya kumalizina na mchezaji huyo anatarajiwa kutua mkoani Tanga wiki ya leo akiwa na mchezaji mwengine wa timu hiyo Jerry Santos.

Siagi alisema msimu huu wamedhamiri kufanya usajili wa nguvu ambao utaifanya timu hiyo kuwa tishio kwenye mechi zao za Ligi kuu ya Tanzania bara kwani malengo yao ni kuchukua ubingwa wa mashindano hayo makubwa hapa nchini.

Aidha alisema timu hiyo itacheza mechi mbalimbali za majaribio nchini Kenya na timu za Sofapaka,Bandari na Goromahia lengo likiwa ni kukipa makali kikosi hicho ambacho kinatarajiwa kuwa tishio.

Katibu huyo aliwataka wapenzi na mashabiki wa timu hiyo kuendelea kujitokeza kuisapoti timu hiyo ili iweze kutimiza azma yao waliyojiwekea kwenye michuano hiyo.

Mwisho.