DC Mwanga apiga marufuku Lambalamba”

DC Mwanga apiga marufuku Lambalamba”

April 23, 2013

 


Na Oscar Assenga,Lushoto.
 
MKUU wa wilayani Lushoto Mkoani Tanga,Alhaj Majid Mwanga imepiga marufuku vikundi vya waganga wanaofanya shughuli za kufichua wachawi maarufu kama “Lambalamba” wilayani humo pamoja na kutoa tahadhari kwa wanannchi watakaobainika kushirikiana nao watachukuliwa hatua kali.

Agizo hilo la Mwanga alilitoa jana kutokana na kutokea uharibifu mkubwa katika kituo cha polisi Bumbuli pamoja na Ofisi ya Afisa Mtendaji tarafa hiyo uliofanywa na wafuasi wa lambalamba waliovamia kituo hicho na kuvunja kila kitu kilichokuwemo ndani ikiwemo nyaraka zote muhimu za serikali na kumchomoa mhalifu mmoja aliyekuwa amewekwa kituoni hapo.

Mwanga alisema baada ya wafuasi hao kumaliza wakaamia ofisi ya afisa tarafa ambapo walifanya uharibifu mkubwa ikiwemo kuchana nyaraka ,thamani za ofisi zilizokuwemo ndani yake.
Alisema baada ya kufanyika matukio hayo hatua ya kwanza walihakikisha usalama katika eneo hilo unakuwepo kwa asilimia kubwa na baadae kuanza kuwasaka waliohusika na tukio hilo ambalo lilikwisha kupigwa marufuku muda mrefu.

Mkuu huyo wa wilaya alisema baada ya hapo walifanikiwa kuwakamata watu 32 ambao wanadhaniwa kuhusika na tukio hilo ambapo wanashikiliwa na jeshi la polisi wilayani humo na tayari walikwisha kufikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.
   
“Napenda kuwaasa wananchi na madiwani kuacha kushirikiana na lambalamba au kuwafadhili katika maeneo yao kwani kufanya hivyo ni kinyume cha sheria na hatutawavumilia lazima wachukuliwe hatua stahiki ikiwemo kuwekwa ndani “Alisema DC Mwanga akisisitiza upigaji marufuku suala hilo wilayani humo.

Alisema baada ya tukio hilo jana walifanya kikao na viongozi wote wa jimbo la bumbuli ikiwemo madiwani ,viongozi wa vyama vya siasa na serikali ambapo kikao hicho kilitoa maelekezo ya serikali kupinga marufuku lambalamba.

Mwisho.
DC Mgaza awahimiza wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao kwenye vituo vya afya.

DC Mgaza awahimiza wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao kwenye vituo vya afya.

April 23, 2013
 Na Oscar Assenga,Mkinga. 
MKUU wa wilaya ya Mkinga, Mboni Mgaza amewataka wazazi na walezi wilayani humo kuhakikisha wapeleka watoto wanaostahili chanjo katika vituo vya huduma za afya ili kuwazuia wasipatwe na magonjwa mbalimbali yakiwemo ya milipuko
Wito huo aliutoa leo wakati wa uzunduzi wa wiki ya chanjo iliyofanyika katika kituo cha Afya Gombero ambapo alisema kila mzazi anapaswa kuhakikisha mtoto wake na wa jirani yake ambayo hajapata chanjo anapewa haki yake ya msingi ya kupatiwa huduma hiyo
Mgaza alisema baada ya kuzindua huduma hiyo anaimani kuwa wazazi watawapeleka watoto wao katika vituo vya kutolea huduma hiyo ambayo itatolewa wilayani humo kuanzia leo (jana) mpaka mwishoni mwa wiki.
Aidha alitumia nafasi aliyopata wakati akiwahutubia wananchi waliojitokeza kwwenye uzinduzi huo kwa kuwakumbusha kuhusu chanjo mpya za kuwakinga watoto na ugonjwa wa nimonia, kuhara na homa ya uti wa mgongo zilizoanza kutolewa tokea mwazoni mwa mwaka huu.
Alisema kuwa chanjo hizo ni haki ya kila mtoto mwenye umri chini ya mwaka mmoja hivyo zitaongeza kasi ya kupunguza vifo kwa walengwa na kusisitiza wazazi na walezi kuhakikisha watoto wanapata chanjo zote kwa kufuata ratiba.
Aidha alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana lakini bado zipo changamoto ya kuwepo kwa watoto ambao hawajapata chanjo au hawajakamilisha chanjo kutokana na umri wao.
Alieleza watoto hao wako katika hatari kubwa kupata maambukizo ya magonjwa na kuweza kuhatarisha jamii nzima na kueleza ni muhimu sana kwa kila mzazi na mlezi kuhakikisha wanawapatia watoto wao chanjo zote kila wakati,ili kuwadhibiti na magonja mfano polio na surua hasa ukizingatia kumekuwepo na mlipuko wa polio katika nchi jirani.
Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa huduma ya chanjo katika wilaya hiyo, Mratibu wa Chanjo wilaya ya Mkinga, Aisibo Maimu alisema huduma ya chanjo wilayani humo inatolewa kwenye vituo vya afya 26 vikiwemo vituo vya afya vitatu, zahanati 23 za serikali na zahanati moja ya Mtimbwani ambayo ni ya faith Based Organization (FBO) ambapo pia huduma za chanjo zimekuwa zikitolewa kwa njia chanjo wima katika vijiji 35 na chanjo mkoba katika vijiji 5 wilayani humo.
Aidha amesema pamoja na mafanikio yaliyopo lakini pia zipo changamoto katika utoaji wa huduma hiyo kwa baadhi ya watoto wanaozaliwa, kucheleweshwa na wazazi wao kupata chanjo 0 kutokana na mama zao kujifungulia nyumbani.
Ameongeza kuwa changamoto nyengine ni miundo mbinu ya barabara kuwa tatizo hasa maeneo ya Mkota na Ronjo katika kata ya Mwakijembe ambapo idadi kubwa ya jamii ya wafugaji wanaishi humo.
Hata hivyo amesema idara ya afya wilayani humo haijakaa kimya, bado inaendelea kuhamasisha kina mama kujifungulia katika vituo vya afya ili wapate huduma pamoja na haki zao za msingi ikiwemo chanjo ya polio.
Mwisho.

POKEA mh.DC

April 23, 2013
MRATIBU wa Chanjo wilaya ya Mkinga,Aisibo Maimu akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Mkinga,Mboni Mgaza risala ya chanjo wakati wa uzinduzi wa chanjo wilayani humo iliyofanyika kata ya Gombero.

UZINDUZI WA CHANJO WILAYA MKINGA.

April 23, 2013
 
MKUU wa wilaya ya Mkinga,Mboni Mgaza akifuatilia hotuba ya maadhimisho ya wiki ya Chanjo kiwilaya ambapo ilifanyikia Kata ya Gombero na yeye alikuwa mgeni rasmi.