DR.MVUNGI AFARIKI DUNIA

November 12, 2013
DAR ES SALAAM, Tanzania

MJUMBE wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama cha NCCR-Mageuzi, Dk. Sengondo Mvungi (61), amefariki dunia leo majira ya mchana katika hospitali ya Milpark, nchini Afrika Kusini alipopelekwa kwa ajili ya matibabu zaidi.

Dk, Mvungi alivamiwa Novemba 3 mwaka huu na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi saa 6:30 usiku nyumbani kwake Kibamba, Kata ya Mpiji Majohe nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam na kujeruhiwa kwa mapanga sehemu za kichwani na usoni.

Akithibitisha kutokea kwa kifo hicho, Mwenyekiti wa Taifa wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema kuwa wamepokea kwa masikitiko taarifa hizo na kuwa chama hicho kimepoteza kiongozi makini na pengo lake haliwezi kuzibika.

“Ni kweli tumepata taarifa hizo mwenzetu hatunaye tena ni huzuni kwa chama na Watanzania tutamkumbuka kwa mambo mengi ndani ya chama hata taifa,” alisema.

Alisema kuwa Dk Mvungi alifariki dunia jana saa 9:30 katika hospitali hiyo ambapo alihamishiwa Novemba 8 mwaka huu akitokea katika Taasisi ya Mifupa ya Muhimbili (MOI).

Naye Mwenyekiti Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) alisema kuwa wamepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo Dk Mvungi.


Mbowe alisema kuwa Chadema kinatoa pole kwa familia, chama cha NCCR-Mageuzi, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba pamoja na Watanzania wote kwa kupoteza mtu makini na muhimu katika mustakabari wa taifa letu.

“Nimepokea taarifa hizo kwa masikitiko kwa kuwa Dk Mvungi ni mmojawapo ya waasisi wa mageuzi nchini, ambaye hakukata tamaa kutumia taaluma yake Mungu ana mipango yake, huyu ndugu alijitahidi kupigania suala la Katiba mpya kwa miaka 20, na akateuliwa aiandae, tunasikitika kwa kuwa hataona katiba mpya yenye mawazo yake,” alisema.


Alisema kuwa Tume inapaswa kuendeleza mawazo na michango aliyokuwa akisaidia katika kuandaliwa kwa katiba mpya.


Aidha taarifa za kifo cha mwanasheria huyo ilisambaa kwa kasi katika mitandao mbalimbali ya kijamii, huku wadau wa mitandao hiyo wakionekana kushitushwa na kifo hicho na kuwataka Watanzania kuwa na subira kwa wakati huu mgumu.

Aidha Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Hussein Bashe katika ukurasa wake aliandika kuwa wahalifu wamekatisha uhai wa kiongozi huyo wakati akitekeleza jukumu zito la kwa ajili ya maslai ya Taifa letu. Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema peponi,” alisema Bashe.


Source:Habarimsetoblog

ASHIKILIWA NA JESHI LA POLISI KWA KUOA BINTI WA MIAKA 18

November 12, 2013
Na Oscar Assenga,Tanga.
MZEE wa Miaka sabini anashikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kuoa binti mwenye umri chini ya miaka kumi na nane Mosa Hamisi kinyume cha sheria zilizopo hapa nchini.

Mkasa huo ulitokea Novemba 10 mwaka huu majira ya saa kumi na moja jioni ambapo mzee huyo tayari alishafunga ndoa na binti huyo lengo likiwa ni kuishi naye kama mke na mume.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga,Constatine Massawe alithibitisha kutokea tukio hilo na kueleza tayari jeshi linamshikilia mtuhumiwa huyo pamoja na mama mzazi wa binti huyo.

Massawe alimtaja mzee huyo kwa jina la Abdallah Tuppa (70)mkazi wa barabara kumi mbili na mama mzazi binti huyo Batuli Tupa (35)ambaye anaishi barabara kumi na nne jijini Tanga.

Alisema tukio hilo liligunduliwa na wasamaria wema baada ya kuona binti huyo anaozeshwa ndipo walipoamua kutoa taarifa kwa jeshi la polisi ambapo wakati polisi walipofika eneo hilo walimkuta mzee huyo akidai mke wake ndipo walipomkamata.

Kamanda Massawe alisema askari walifanikiwa kumuhoji binti huyo ambapo alisema umri wake ni zaidi ya miaka kumi na saba hali ambayo ilipelekea kumuambia alete cheti chake cha kuzaliwa ili kuthibiti umri huo.

Wakati huo huo,mtu mmoja amekufa baada ya kugongwa na gari akiwa anaendesha baiskeli katika barabara ya Segera –Chalinze.

Kamanda Massawe alisema tukio hilo lilitokea juzi majira ya saa 3 za usiku na kumtaja dereva aliyesababisha ajali hiyo kuwa ni Abdallah Msangi (30) wa gari hilo aina ya fuso lenye namba T390 DCB.

Massawe alimtaja aliyefariki katika ajali hiyo kuwa ni Hamisi Saidi mkazi wa Michungwani ambapo alisema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva.

DIWANI ATAKA SOKA LA DEEPSEA LIVUNJWE

November 12, 2013


NA OSCAR ASSENGA,TANGA.
DIWANI wa Viti Maalumu Kata ya Chumbageni jijini Tanga kupitia chama  cha Mapinduzi (CCM)Saida Gadafi amelishauri baraza la madiwani kuridhia soko la kuuzia samaki la deepsea livunjwe kuliko kila mwaka litengewe sh.milioni 50 kwa ajili ya ukarabati wake.

Gadafi alitoa kauli hiyo  wakati wa kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa mipango miji jijini Tanga ambapo alisema fedha hizo zinazotengwa hazionekani zinafanyia kazi gani kwa sababu ukarabati wenyewe hauonekani kama umefanyika.

Alisema kitendo hicho kinapelekea kurudisha nyuma kasi ya maendeleo ya halmashauri hiyo na kueleza kwa maslahi yake inabidi soko hilo livunjwe lakini mchakato huo uendane na kuwashirikisha wataalamu ili waweze kuamua nini kifanyike.

Diwani huyo alisema lazima madiwani wahakikishe wanakuwa mstari wa mbele kusimamia maslahi ya wananchi wanaowaongoza ili kuondoa kero zao lengo likiwa ni kuwapa maendeleo.

  “Kila mwaka zilikuwa zikitengwa milioni 50 kwa ajili ya ukarabati wa soko hilo lakini watu walikuwa hawazisema ila hizo milioni 11 kwa ajili ya kupewa mtathimini zimekuwa zikileta maneno naamini wataalamu tunao kwenye halmashauri waamue nini cha kufanya pale lakini hilo soko bora livunjwe “Alisema Gadafi.

Akizungumza suala hilo,Mjumbe wa Kamati wa Fedha,Shehe Fadhili Bwanga alisema masuala ya kuvunjwa soko hilo ni kutokana na kuona kuwa halikidhi haja ya kuendana na hadhi ya jiji na wao kupitia kamati ya fedha wameona zifuatwe sheria za nchi ikiwemo kuthaminiwa na kampuni zinazotambulika kiserikali ili ziweze kutoa idhini ya uvunjwaji wa jengo hilo.

Bwanga aliongeza kuwa uamuzi wa kuvunja soko hilo pia utatokana na gharama zake za sh.milioni 11 lakini sheria za uvunjwaji zilizowekwa inabidi zifuatwe kabla ya kuachukua maamuzi wa uvunjwaje wake.

BODI YA LIGI YAFUNGIA VIWANJA SABA

November 12, 2013
Release No. 194
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Novemba 12, 2013
NA BONIFACE WAMBURA,DAR ES SALAAM.
Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPL Board) imefungia viwanja saba vilivyokuwa vikitumiwa na timu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) hadi vitakapofanyiwa marekebisho ili kukidhi mahitaji ya mechi za mpira wa miguu.

Uamuzi huo umefikiwa na TPL Board katika kikao chake cha kwanza kilichofanyika juzi (Novemba 10 mwaka huu) jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine kilipitia ripoti za mechi za VPL na FDL katika mzunguko wa kwanza.
 
Viwanja vilivyofungiwa na marekebisho yanayotakiwa kufanyika kwanza ili viruhusiwe kutumika tena ni Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba (majukwaa yake yamechakaa, hivyo kuhatarisha usalama wa watazamaji), na Uwanja wa CCM Mkwakwani jijini Tanga (vyumba vya wachezaji kubadilishia nguo (dressing rooms) havina hadhi).

Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya (sehemu ya kuchezea- pitch ni mbovu), Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha (pitch ni mbovu), Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi (vyumba vya kubadilishia kutumika kwa ajili ya shule ya awali), Uwanja wa Majimaji mjini Songea (pitch ni mbovu) na Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro (pitch ni mbovu).

Klabu ambazo timu zake zinatumia viwanja hivyo zimeshaarifiwa rasmi juu ya uamuzi huo ambapo ama vinatakiwa kuwasiliana na wamiliki wa viwanja hivyo ili wafanye marekebisho au kutafuta viwanja vingine vya kuchezea mechi zao.

Kwa upande wa ripoti za mechi za VPL; Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 na kupewa onyo kali kwa timu yake ya U20 kutocheza mechi ya utangulizi walipocheza na Yanga. 

Pia wanatakiwa kulipa gharama za uharibifu baada ya washabiki wao kuvunja kioo cha basi la Yanga baada ya gharama hizo kuthibitishwa na Bodi ya Ligi.

Pia Mbeya City imepigwa faini ya sh. 500,000 kwa washabiki wake kushambulia basi la wachezaji wa Tanzania Prisons baada ya mechi dhidi yao, na kulipa gharama za uharibifu baada ya kuthibitisha na Bodi ya Ligi.

Coastal Union imepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake ilipocheza na Azam kwenye Uwanja wa Mkwakwani ambapo mwamuzi msaidizi Hassan Zani alishambuliwa kwa mawe na kujeruhiwa mkononi na kichwa, tukio lililosababisha mchezo kusimama kwa dakika tatu.

Beki wa Coastal Union, Hamad Khamis wa Coastal Union amepigwa faini ya sh. 500,000 kwa kumpiga kichwa kwa makusudi Kipre Tchetche wa Azam. Kitendo hicho kilisababisha refa amtoe nje kwa kadi nyekundu, hivyo atakosa mechi tatu zinazofuata za timu yake.

Mchezaji Cosmas Lewis wa Ruvu Shooting alifanya kitendo cha utovu wa nidhamu kwa kupiga kelele wakati mgeni rasmi akisalimia timu na kukataa kupeana mkono na kamishna kwenye mechi dhidi ya Rhino Rangers, hivyo amefungiwa mechi tatu na kupigwa faini ya sh. 500,000.

Mtunza vifaa (Kit Man) wa JKT Ruvu, Selemani Oga aliondolewa kwenye benchi la ufundi wakati wa mechi yao dhidi ya Mbeya City kwa kosa la kutoa lugha chafu kwa refa, hivyo suala lake litapelekwa katika Kamati ya Maadili.

Kocha Msaidizi wa Oljoro JKT, Fikiri Elias amepigwa faini ya sh. 500,000 na kufungiwa mechi tatu kwa kumshambulia kwa matusi refa wakati wa mechi yao dhidi ya Ashanti United. Naye mtunza vifaa wa timu hiyo Elas Justin amepelekwa Kamati ya Maadili kwa kumshambulia refa kwa matusi ya nguoni.

Simba wamepigwa faini ya sh. 500,000 kutokana na vurugu za washabiki wake wakati wa mechi dhidi ya Kagera Sugar.

Katika FDL, mchezaji Ally Mtoni wa Villa Squad amepigwa faini y ash. 200,000 na kufungiwa mechi tano. Kosa lake ni kujisaidia haja ndogo golini wakti wa mechi dhidi ya Ndanda FC iliyochezwa mjini Mtwara.

Kamishna Paul Opiyo wa mechi ya FDL kati ya Villa Squad na Transit Camp kwa kutokuwa makini. Katika ripoti yake ameeleza kuwa Transit Camp ilichelewa kufika uwanjani, lakini hakusema ilichelewa kwa muda gani.

Kocha wa Polisi Dar es Salaam, Ngelo Nyanjabha na Meneja wa timu hiyo Mrimi Masi wamepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi tatu kila mmoja kwa kuongoza kundi la washabiki kumvamia refa wa mechi yao dhidi ya Villa Squad iliyochezwa Dar es Salaam.

Pia Bodi ya Ligi imeagiza Polisi waandikiwe barua ya onyo kwa vile wakati waamuzi wanapigwa walikuwepo lakini hawakutoa msaada kwa wakati.

Kocha wa Friends Rangers, Kheri Mzozo amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi sita kwa kosa la kumtukana refa na kutishia kuhamamisha washabiki waingie uwanjani kufanya fujo kwenye mechi dhidi ya Villa Squad.

Naye Kocha msaidizi wa timu ya Transit Camp, Haji Amiri amepigwa faini ya sh. 200,000 na kufungiwa mechi sita kwa kutoa lugha ya matusi kwa mwamuzi wa akida wakati wa mechi dhidi ya Friends Rangers.

Adhabu zote zimetolewa kwa mujibu wa kanuni. Pia Bodi ya Ligi imeahirisha kufanya uamuzi wa mechi kati ya Stand United na Kanembwa JKT iliyochezwa Uwanja wa Kambarage ili kukusanya taarifa zaidi. Mechi hiyo haikumalizika. Bodi ya Ligi itakutana tena Jumapili (Novemba 17 mwaka huu).

FUTURE TAIFA STARS vs TAIFA STARS UWANJANI KARUME

November 12, 2013
Timu za Taifa za Future Taifa Stars na Taifa Stars zinacheza kesho (Novemba 13 mwaka huu). Mechi hiyo ya kirafiki itafanyika Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume jijini Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.

Mechi hiyo ni maalumu kwa Benchi la Ufundi la Taifa Stars linaloongozwa na Kim Poulsen kuangalia wachezaji kumi kutoka Future Taifa Stars watakaoongezwa katika Taifa Stars tayari kwa mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayochezwa Novemba 19 mwaka huu jijini Arusha.

Watazamaji 300 tu wataruhusiwa kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imeingia kambini leo (Novemba 12 mwaka huu). Miongoni mwa wachezaji wanaotarajia kuripoti ni kipa Ivo Mapunda wa Gor Mahia.
Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

UVCCM WILAYA YA TANGA WAIPIGA TAFU AFRICAN SPORTS.

November 12, 2013
MWENYEKITI WA UVCCM WILAYA YA TANGA,SALIM PEREMBO KUSHOTO AKIKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA MJUMBE WA KAMATI YA UTENDAJI YA KLABU YA AFRICAN SPORTS SALIM OMARI LEO

MWENYEKITI WA UVCCM WILAYA YA TANGA SALIM PEREMBE WA KWANZA KUSHOTO ,MJUMBE WA KAMATI YA SIASA NA UCHUMI WILAYA YA TANGA,MBARUKU OMARI ASILIA,MJUMBE WA KAMATI YA UTENDAJI AFRICAN SPORTS SALIM OMARI PAMOJA NA MENEJA WA TIMU HIYO ABDUL AHMED WAKIWA KATIKA PICHA YA PAMOJA MARA BAADA YA KUKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO KWA TIMU HIYO LEO.


MWENYEKITI WA UVCCM WILAYA YA TANGA,SALIM PEREMBO AKISISITIZA JAMBO KWA WACHEZAJI WA TIMU YA AFRICAN SPORTS MARA BAADA YA KUWAKABIDHI VIFAA VYA MICHEZO VYENYE THAMANI YA SH.500,000