MKONGE CUP KUANZA LEO

October 12, 2013
Na Oscar Assenga, Tanga.
MICHUANO ya Kombe la Mkonge Cup inatarajiwa kuanza kutimua vumbi leo kwenye mashamba ya mkonge yaliyopo sehemu mbalimbali hapa nchini.

Akizungumza jana na waandishi wa habari,Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano hayo,Lai Mpuma alisema mashindano hayo msimu huu yanatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na maandalizi yaliyofanywa na timu shiriki.

Mpuma alisema timu shiriki katika michuano hiyo zimepangwa katika makundi manne ambapo katika kundi A kutakuwa na timu za China State ambao watafugua pazia la mashindano hiyo kwa kucheza na New Msowero katika uwanja wa soka Rudewa.

Alisema katika kundi B timu ya Toronto na Magoma hizo ndio zitafungua pazia la michuano hiyo katika uwanja wa Toronto wakati Mkumbara na Mazinde wao watacheza pia katika uwanja wa soka Mkumbara.

Aidha aliongeza kuwa katika kundi C timu zitakazofungua pazia la mashindano hayo ni Kauzeni na Amboni Sp Mill katika uwanja wa soka Kauzeni wakati Lugongo na Muheza Estate nao wakicheza kwenye dimba la Lugongo.

Mwenyekiti huyo alisema michezo mengine itakayochezwa siku hiyo ni Sakura ambao watacheza na Tancord kwenye dimba la soka Sakura huku Mwera na Kumburu wakihitimisha mechi hizo katika uwanja wa soka Mwera.