MKUTANO WA WADAU WA MADAWA ZANZIBAR WAFANYAIKA ZANZIBAR BEACH RESORT

September 29, 2015

???????????????????????????????????? 
NA RAMADHANI ALI/MAELEZO ZANZIBAR
………………………………
Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi Zanzibar (ZFDB) imeandaa miongozo ya utoaji huduma bora katika kufanikisha  Mpango wa uwiano wa Itifaki ya pamoja kwa Nchi wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki.
Mkurugenzi wa ZFDB  Dkt. Burhani Othman Simai ameeleza hayo katika Mkutano wa wadau wa Madawa Zanzibar ulioandaliwa na Mpango wa Udhibiti wa bidhaa za Chakula na Dawa wa Jumuia ya Afrika Mashariki katika Hoteli ya Zanzibar Beach Resort Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Alisema kuanzia sasa bidhaa zote za chakula na madawa za  Zanzibar na zinazotoka nje  zitasajiliwa na Bodi yake na Viwanda vinavyotengeneza bidhaa hizo vitafanyiwa ukaguzi wa mara kwa mara ili kuhakikisha usalama wa  bidhaa hizo.
Aliongeza kuwa katika kufanikisha mpango huo,  Zanzibar inategemea kupata ithibati ya Kimataifa (ISO Certification) mwezi Disemba na kuanzia Januari 2016 maombi na kazi zote za udhibiti wa bidhaa za chakula na madawa zitafanywa kwa njia ya mtandao kupitia tovuti ya ZFDB.
Dkt. Burhani  aliwataka wadau wa bidhaa za chakula na madawa kutoa ushirikiano kwa  Bodi kwa kujisajili  katika Ofisi  yao  iliyopo Mombasa kwa Mchina na kuandaa utaratibu mzuri wa kurahisisha ukaguzi wa  bidhaa na viwanda vyao.
Alisema taratibu hizo zinazochukuliwa na ZFDB zinalengo la kulinda afya za wananchi wa Zanzibar na Nchi wa wananchama wa Jumuia ya Afrika Mashariki.
Mwakilishi kutoka Sekriteriati ya Jumuia ya Afrika Mashariki Mjini Arusha Mwesige John Patrick aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuwa mstari wa mbele kufanikisha Mpango wa uwiano wa Nchi wanachama wa Jumuia hiyo.
Alikumbusha  kuwa Mpango huo ulioanza mwaka 2012 kwa awamu ya kwanza ya miaka mitatu, ukizishirikisha Nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi na Ruwanda  umeanza kuleta mafanikio makubwa kwa nchi zote  wanachama na mwaka huu umeanza awamu ya pili ya miaka miwili.
Akifungua Mkutano huo Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Zanzibar Bibi Halima Maulid ameitaka ZFDB kuendelea kusimamia mpango wa uwiano wa Udhibiti wa Bidhaa za chakula na dawa  na kuhakikisha zinakuwa salama kwa matumizi ya binadamu.
Mkutano huo uliokuwa na lengo la kuwafahamisha wadau wa Zanzibar miongozo mipya iliyoandaliwa kwa pamoja na wataalamu wa Mamlaka za udhibiti wa Chakula na Dawa wa Wanachama wa Jumuia ya Afrika Mashariki.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »