March 07, 2014

SERIKALI KUENDELEA KUSIMAMIA USAWA WA KIJINSIA NCHINI

Na Jovina Bujulu ,MAELEZO DODOMA
Serikali itaendelea kuchukuwa hatua za utekelezaji katika maeneo ya kijamii ili kuhakikisha kunakuwepo na usawa wa kijinsia nchini.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Mh. Dkt. Pindi Chana hivi karibuni Mjini Dodoma.
Akizataja hatua hizo hizo Dkt. Pindi alisema kuwa serikali imemekuwa ikiwajengea wanawake uwezo wa kisheria ili kuweza kukabiliana na changamoto mbalimbali katika maisha na jamii kwa ujumla.
“Sheria kadhaa zimekuwa zikitungwa na nyingine zikifanyiwa marekebisho, ikiwemo sheria ya makosa ya kujamiiana ya Mwaka 1998, sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini namba 6 ya mwaka 2004 na sheria ya mtoto ya mwaka 2009 na hii yote ni kuhakikisha tunawajengea wanawake mazingira bora” Alisema Dkt. Pindi.
Aidha, Dkt. Pindi aliongeza kuwa kumekuwepo na ongezeko la ushiriki wa wanawake katika ngazi mbalimbali za maamuzi, Ongezeko hilo linatokana na marekebisho ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1995 ambapo viti maalum viliongezwa na kuwa asilimia 15 kwa Tanzania bara na asilimia 20 kwa upande wa Zanzibar.
Pia Dkt. Pindi alisema kuwa Serikali imeanzisha mfuko wa maendeleo ya wanawake unaotoa mikopo ya uanzishwaji wa biashara na shughuli nyingine za kiuchumi ili kuwawezesha wanawake nchini.
Aliongeza kuwa serikali imeandaa sera ya mitaji midogo midogo ya mwaka 2000 ambayo imeweka mazingira mazuri kwa taasisi binafsi za fedha  kama PRIDE, FINCA, BENKI YA WANAWAKE NA CATSBY kutoa mikopo kwa wanawake.
Madhumuni ya kuazimisha siku ya Wanawake duniani ni kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kutambua na kuthamini uwezo na mchango mkubwa unaofanywa na wanawake katika kuleta maendeleo na jitihada zinazofanywa na Serikali katika kuwawezesha wanawake kiuchumi na kijamii.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »