Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF),
Mwesigwa Selestine ameanza taratibu za kulifikisha mahakamani gazeti la
kila siku la Tanzania Daima ikiwa ni pamoja na wamiliki na wachapaji
wake kwa kumhusisha na njama za upangaji matokeo ya michezo ya Ligi
Daraja la Kwanza.
Mwesigwa ametoa msimamo huo leo baada ya gazeti hilo kuchapisha
habari inayodai alikuwa miongoni mwa waliohudhuria kikao cha upangaji
matokeo ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL).
"Nimeshtushwa na kusikitishwa sana na habari hiyo juu yangu ambayo ni
ya kutunga, yenye nia mbaya isiyokuwa ukweli wowote, kwani sijawahi
kukaa na watu wowote kupanga njama yoyote iliyo kinyume na maadili ya
mchezo wa mpira wa miguu " alisema Mwesigwa.
Gazeti la Tanzania Daima toleo nambari 4143 la leo tarehe 7 Aprili
2016 lilichapisha habari katika ukurasa wake wa 24 chini ya kichwa cha
habari " Vigogo TFF wajikaanga" likisema katika ibara ya 7 kuwa kwenye
mazungumzo yaliyochukua zaidi ya dakika 10 yalihusisha pia Katibu Mkuu
wa TFF, Mwesigwa.