WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI WAOMBWA KUZIPA KUPAUMBELE HABARI ZA UNYANYASAJI NA UKATILI.

January 08, 2014
Khadija Baragasha,Tanga.
WAMILIKI wa vyombo vya habari na Wahariri Nchini  wameombwa kuzipa kipaumbele  habari zinazohusu unyanyasaji na ukatili kwenye vyombo vyao  ili  jamii iweze kuelimika na kutambua athari  na kuepuka matendo hayo mabaya
Aidha waandishi  wa habari nchini wameshauriwa kutotangaza  habari za taasisi ama vikundi ambavyo shughuli zake zinamuelekeo wa  kuifanya jamii iende  kinyume na  maadili ya mtanzania.
Hayo yalielezwa na  mwanaharakati maarufu Jijini hapa  wa haki za binaadamu, Nuru Rajab  wakati akitoa maoni yake kuhusu matukio ya kinyama yanayotokea ndani ya jamii yanayokiuka mpaka  haki za binaadamu.
Akizungumzia  unyanyasaji huo aliyouelekeza hasa  kwa mtoto na wanawake, Rajab  alisema kuwa unyanyasaji ni kitendo  kisichokubalika ndani ya jamii na taifa kwa ujumla na kwamba elimu ya ubaya na athari zake ni vema ikatangazwa kwa upana zaidi na kupewa kipaumbele katika vyombo vya habari.

Mwanaharakati huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa vijana wa Chadema Wilaya ya Tanga alieleza kuwa hali na mapambano ilivyo  katika suala la unyanyasaji, kunatakiwa elimu ya kutosha ndani ya jamii na kwamba njia pekee ya kusambaza uelewa kwa watu ni kupitia vyombo vya  habari  pamoja na waandishi kuacha kuripoti taarifa za baadhi ya taasisi ama vikundi zinazokinzana na maadili ya mtanzania.
Rajab pia  alieleza umuhimu wa viongozi wa dini kuimarisha suala la  maadili na uadilifu kwa waumini wao pamoja na kuweka bayana ubora wa muumini ni uchamungu wenye uadilifu. 
Hata hivyo alieleza maana ya unyanyasaji, athari zake na jinsi ya kukabiliana na tatizo hilo ndani ya jamii ambapo  alisema  kuwa maana ya unyanyasaji ni kumtoa mtu kwenye hali yake ya kawaida na kuonekana dhariri asiye na thamani mbele ya jamii.
Athari nyingine  za unyanyasaji kwa mujibu wa Rajab ni mtu kutoishi kwa uhuru,kukosa haki ya kufikilia elimu ya juu au zote,kumkatisha mtu kushiriki katika shughuli za kisiasa na kiutamaduni,ongezeko la watoto wa mitaani, kupoteza maisha kwa maradhi au kujiua, mtoto kukosa malezi bora na hata kupunguza nguvukazi.
Aliwataka  wananchi kwa ujumla kuacha woga  katika kudai haki zao za msingi na kwamba mtu mwenye hofu na hata kukidai kilichochake atakuwa anajinyanyasa mwenyewe na  kusema  ili kupambana na unyanyasaji ndani ya jamii ni lazima kila mmoja awe shujaa wa kusimamia haki na kuondoa hofu ya kuifuatilia pale anapoona inaporwa na mtu aidha kwa kutumia nafasi yake,nguvu au uwezo kifedha.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »