Meneja Mawasiliano wa Shirika la
Hifadhi za Taifa (TANAPA) Pascal Shelutete (kati) akiongea na wanahabari
jijini Arusha jana kuhusiana na Kampeni ya siku Kumi ya Usafi wa Mlima
Kilimanjaro inayotarajiwa kuanza leo. Wengine pichani ni Katibu
Mtendaji wa Chama cha Mawakala wa Utalii Tanzania Bw. Cyril Ako (kulia)
na Mwakilishi kutoka Hoteli ya Kibo Palace BI. Jenipher Swai.
…………………………………………………………………………………………………..
Shirika la Hifadhi za Taifa
(TANAPA) kesho tarehe 21.04.2016 litazindua Kampeni Maalum ya siku 10 ya
usafi wa Mlima Kilimanjaro. Uzinduzi huo Utafanywa na Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro Mhe. Said Mecky Sadik.
Kazi hii ya kusafisha Mlima
Kilimanjaro itafanywa na watumishi wa hifadhi kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali wa utalii zaidi ya 200, wakiwemo mawakala wa utalii (tour
operators), waongoza wageni (guides), wapagazi (porters) na wapishi
(cooks) wanaowahudumia watalii katika Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro.
Usafi huu utahusisha maeneo
mbalimbali ya hifadhi kama vile njia za kupandia mlimani, maeneo ya
kupiga kambi, maeneo ya mabanda, na maeneo ya kupumzikia wageni (picnic
sites).
Kampeni hii ni muendelezo wa
utaratibu wa kawaida wa hifadhi unaofanyika kila wakati kuhakikisha
maeneo ya hifadhi hasa yanayotumika na wageni yanakuwa katika viwango
vya kimataifa vya utoaji huduma kwa wageni. Huu ni utaratibu wenye lengo
la kuwahamasisha wadau mbalimbali kuhakikisha kuwa wanauweka Mlima
Kilimanjaro katika hali ya usafi muda wote.
Mlima Kilimanjaro unachangia
zaidi ya Shilingi Bilioni 60 ambazo ni sawa na asilimia 34 kwa mwaka
katika mapato ya TANAPA. Aidha, Mlima Kilimanjaro hutoa ajira zaidi ya
laki tatu(300,000) kwa mwaka kwa Watanzania wanaofanya shughuli za
utalii mlimani.
Imetolewa na Idara ya Mawasiliano
Hifadhi za Taifa Tanzania
20.04.2016