NA RAMADHANI ALI/MAELEZO
…………………………………..
CHUO cha Uongozi wa Fedha Zanzibar
(ZIFA) kitaanzisha Tawi lake Kisiwani Pemba kuanzia mwaka huu wa
masomo na kitaanza kufundisha masomo ya uongozi wa fedha ngazi ya
cheti.
Akizungumza na waandishi wa Habari
Makao Makauu ya ZIFA Chwaka, Kaimu Mkuu wa Taaluma Dkt. Iddi Salum Haji
amesema wameamua kufungua Tawi Pemba ili kuzipunguzia gharama familia
zenye kipato cha chini.
Amesema utafiti uliofanywa na Chuo
umegundua kuna vijana wengi Kisiwani Pemba waliomaliza kidato cha nne
na wanazo sifa za kujiunga na chuo kwa masomo ya cheti lakini
wanashindwa kutokana na familia zao kukosa uwezo wa kuwasomesha.
Ameongeza kuwa chuo kimejipanga
na kukamilisha taratibu zote za kutoa mafunzo hayo katika Mji wa Wete
na wanafikiria kuanzisha Tawi Mjini Dar es salaam hapo baadae.
Dkt. Iddi amesema lengo la Chuo
hicho ni kujipanua zaidi hasa kufuatia matokeo mazuri ya mitihani ambapo
mwaka huu asilimia 98.3 ya wanafunzi 870 waliofanya mitihani kuanzia
ngazi ya cheti mpaka shahada ya kwanza wamefaulu vizuri.
“Wanafunzi waliohitimu fani ya
Uhasibu wamepasi asilimia mia, IT asilimia 97 na fani ya Ugavi na
Ununuzi wamefaulu kwa asilimia 98,” amesema Kaimu Mkuu wa Taaluma.
Amesema mafanikio hayo
yamepatikana kutokana na wanafunzi kujituma zaidi na walimu
kujitolea kwa uwezo wao wote na kuwa wabunifu katika kufundisha.
Ameeleza kuwa baadhi ya fani
zinzofundishwa na chuo cha Uongozi wa Fedha yanaelekeza zaidi kwa
vitendo na yanawasaidia wahitimu kuweza kujiajiri wenyewe.
Dkt. Iddi amewashauri wazazi
kuwa waangalifu wakati vijana wao wanapotafuta nafasi za kujiunga na
Taasisi za elimu ya juu na kuwataka wahakikishe wanawapeleka kwenye
vyuo vyenye sifa na vilivyosajiliwa na kutambuliwa na Bodi za elimu ya
juu NACTE na TCU.
“Hivi sasa kumeibuka msururu wa
vyuo vinavyojitangaza vinatoa mafunzo ya Elimu ya juu lakini wanafunzi
wanapomaliza na kutafuta ajira ama masomo ya juu inakuwa vigumu kupata
kutokana na kuwa havitambuliki,” alisema Dkt. Iddi
Kaimu Mkuu wa Idara ya Masomo ya
jumla ZIFA Maalim Said Mohd amesema chuo hivi sasa kimejipanga
kuteremka ndani ya jamii kwa kutoa elimu kwa wajasiriamali ili waweze
kujiendesha wenyewe.
“Kwa kuanzia chuo tayari
kimeendesha mafunzo ya ujasiriamali kwa vikundi vya Wilaya ya
Kaskazini A, Wilaya ya Kati na Wilaya Kusini kwa Unguja na Chake chake
na Micheweni Pemba na lengo ni kumaliza Wilaya zote za Zanzibar,”
alisisitiza Maalim Said.
Mmoja wa wanafunzi waliomaliza
masomo mwaka huu Bakar Omar Hamad ameishauri Wizara ya elimu kufanya
mapitio ya Taasisi zinazotoa elimu ya juu nchini ili kuhakikisha
uhalali wa usajili wao, mitaala inayotumika inalingana na masomo na
kuhakikisha walimu wanazo sifa zinazokubalika.
Amesema wazazi wamekuwa wakiwekeza
fedha nyingi kuwasomesha watoto wao lakini baadhi ambao mwamko wa
kielimu ni mdogo wanawapeleka vijana wao katika vyuo ambavyo pamoja na
kupata usajili lakini masomo yanayotolewa yanakosa ithibati ya
kufundishwa.