COASTAL Union yawatimua wajumbe wawili wa Kamati ya Utendaji.

July 01, 2013

 Na Oscar Assenga, Tanga.
UONGOZI wa Klabu ya Coastal Union ya Tanga umetimua rasmi wajumbe wa kamati ya utendaji wa timu hiyo ambao walichaguliwa katika uchaguzi mkuu mwaka uliopita kutokana na kushindwa kutimiza majukumu yao ipasavyo.

Akitangaza uamuzi wa kuwafukuza katika mkutano mkuu wa wanachama mwishoni mwa wiki, Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Hemed Aurora alisema hatua hiyo inatokana na wajumbe hao kuwa mzigo katika nafasi zao ikiwemo kushindwa kuhudhuria vikao vya kamati tendaji tokea walipochaguliwa.


Kauli ya Aurora inafuatia na swali aliliulizwa na Mwanachama wa Klabu hiyo, Miraji Wandi aliyetaka kujua uongozi wa timu hiyo umewachukuliwa hatua gani viongozi ambao wanashindwa kutimiza wajibu wao hali ambayo inapelekea kuwa mzigo kwa klabu hiyo?

Aurora alisema tayari wameandaa utaratibu wa kuandika barua kwa ajili ya kuwatimua rasmi katika nafasi zao hizo pamoja na kutangaza nafasi za hizo katika uchaguzi mdogo ambao utafanyika hivi karibuni kuziba mapengo hayo.

Aidha mwenyekiti huyo aliwataka viongozi waliopo katika klabu hiyo na wanachama kila mmoja kutimiza majukumu yake ili kuweza kusukuma gurudumu la maendeleo ya timu hiyo ambayo imedhamiria msimu ujao kuchukua ubingwa.

Mwenyekiti huyo aliwataja wajumbe wa kamati ya utendaji ambao wamewatimuliwa ni Julius Benjamini na Nashoni Kweli ambao tokea wachaguliwe katika nafasi zao wamekuwa wakishindwa kutekeleza majukumu yao.

Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »