“Tatizo la msingi la mgogoro waLoliondo litatatuliwa mezani”- Dkt. Kigwangalla

October 27, 2017


Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla amewataka viongozi wa Serikali na wale wenye upande wa mgogoro wa pori tengefu la Loliondo kukaa chini ili kupata ufumbuzi wa suala hilo lililochukua karibu miaka zaidi ya 20 sasa huku akitoa tamko la kusitisha operesheni zote zilizokuwa zikiendelea katika suala hilo.
Waziri Dkt. Kigwangalla ameyasema hayo kwenye mkutano wa wazi jioni ya jana Oktoba 26,2017 wakati akizungumza mamia ya wananchi wa Loliondo wakiwemo wale wenye mgogoro na pori hilo.
“Kuanzia leo, mimi kama Waziri wa Maliasili na Utalii, nina waahidi kufanya uhifadhi endelevu, kukaa na wananchi kuhifadhi. Hivyo nawaomba viongozi wa Serikali na wananchi kwenye mgogoro huu sasa kufikia mwisho na kukaa meza moja.
Mgogoro utatatuliwa kwa kukaa mezani. Kwa pande zote mbili sasa kuja na jibu moja juu ya kusitisha mgogoro huu. Hatutaki tumuone Mkuu wa Wilaya mbaya ama Mkurugenzi wake ama wahifadhi wabaya au Waziri wa Maliasili  bali, sote tuwe kitu kimoja katika meza ya majadiliano na kufikia mwisho” alieleza Dk.Kigwangalla.
Ameongeza kuwa:
“Tutasimamia kushirikiana na nyie. Lakini hatutokubalana na watu miongoni mwetu wa watu ambao wataivunja sheria kwa makusudi. Kwa msingi huo, napenda kutamka kuwa, nasitisha operesheni iliyokuwa ikiendelea Loliondo ile ya kukamata wafugaji na kuwatesa ama vitendo vingine vibaya.
Pili naagiza watalaam wa maji, wakae na watalaam wa hifadhi washirikiane na serikali ya kijiji wawaruhusu wafugaji kunywesha mifugo yao.
Pia naagiza kwa Wahifadhi na Kamati ya Ulinzi na Usalama, mifugo yote ambayo imekamatwa na mamlaka ambayo ipo chini ya Wizara ambayo nasimamia mimi ile yote ambayo haijahukumiwa na mamlaka za kisheria iachiwe huru kwa wenyewe  kwa  mifugo ambayo itabaki chini ya idara iliyopo kwenye wizara yangu ni ile yenye migogoro ya usuluhishi tu” alieleza Dkt.Kigwangalla.
Waziri Dkt.Kigwangalla yupo Mkoani Arusha kwa ziara ya siku sita ambapo awali alianza kutembelea Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA)mjini Arusha, na baadae Mamlaa ya Hifadhi ya Ngorongoro ambapo pia aliweza kukutana na jamii ya wafugaji wanaoishi kwenye hifadhi ya Ngorongoro kwa namna ya kitatua migogoro kati yao na wahifadhi wa Ngorongoro.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »