MHE. UMMY A. MWALIMU ATOA TAMKO KUHUSU KUNAJISIWA KWA WATOTO KATIKA MANISPAA YA MOSHI, MKOANI KILIMANJARO

March 21, 2016

Ummy Mwalimu 
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imepokea kwa masikitiko makubwa tukio la kunajisiwa kwa watoto watatu wa kike wenye umri kati ya miaka minane hadi tisa, wanafunzi wa darasa la tatu wa Shule ya Msingi Msaranga manispaa ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, ambao limeripotiwa na vyombo vya habari.
Tukio hili la kunajisi watoto ni ukiukwaji mkubwa wa haki za mtoto ambao Serikali imekuwa ikihimiza wazazi, walezi, na jamii kuhakikisha kuwa mtoto analelezwa na kuendelezwa katika mazingira salama na rafiki kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Na. 21 ya mwaka 2009.
Wizara imesikitishwa na taarifa kuwa, kuna baadhi ya wanajamii wanaowafanyia ukatili watoto wa kike kwa kuwashurutisha kuwa na mahusiano na watoto hao katika umri mdogo, kitendo ambacho kwa kiasi kikubwa kinarudisha nyuma jitihada za Serikali kuhakikisha kuwa jamii zetu zinakuwa mahala salama kwa watoto kuishi. 
Wizara inalaani vikali unyanyasaji waliofanyiwa watoto hao kwani katika umri huo mdogo hawakustahili kufanyiwa ukatili huo. Aidha, wazazi na walezi tutambue kuwa tunaowajibu mkubwa wa kufuatilia mienendo ya watoto wetu mara kwa mara ili kuwanusuru na matukio ya ukatili. 
Wizara inatoa pongezi ya dhati kwa wananchi, Jeshi la Polisi, wanahabari na wadau wote ambao wameonesha ushirikiano kuripoti na matukio ya ukatili dhidi ya watoto hapa nchini.  Aidha, Wizara inapongeza Jeshi la Polisi katika Mkoa wa Kilimanjaro kwa kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja anayehusishwa tukio la kunajisi watoto hao. Tunahimiza Polisi katika mkoa wa Kilimanjaro kumsaka mtuhumiwa wa pili na kumjumuisha katika shauri hili.
Maagizo yanatolewa kwa Mganga Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro kuhakikisha anatoa huduma stahiki ya vipimo na tiba kuokoa afya za watoto hao. Aidha, Afisa Ustawi wa Jamii na Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mkoa wa Kilimanjaro wahakikishe wanafuatilia shauri la watoto hawa kwa karibu, ikiwa ni pamoja na maendeleo ya afya za watoto hao; na kutoa ushauri nasaha kwa watoto, wazazi na walezi wa familia za watoto hao na kutoa taarifa mara kwa mara.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »