Megawati 150 kuongezeka katika Gridi ya Taifa
Naibu
Mkurugenzi Mtendaji, Uwekezaji Mhandisi Decklan Mhaiki (katikati)
akimweleza Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo
(kushoto) pamoja na Waandishi wa habari moja ya mashine za kufua Umeme
zitakazofungwa katika eneo la Kinyerezi I jijini, Dar es Salaam. Kulia
ni Mkurugenzi Mkazi wa Mradi wa ujenzi huo, Bw. Shaun Moore.
Mmoja
wa mitambo ya kufua umeme ambao utafungwa katika eneo la Kinyerezi I
mara baada ya ujenzi kukamilika. Mitambo hiyo, inatarajiwa kuzalisha
kiasi cha megawati za umeme 150 ambazo zitaunganishwa katika gridi ya
Taifa.
Waziri
wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo katika picha ya pamoja na
baadhi ya watendaji kutoka TANESCO, Wizara ya Nishati na Madini na
watumishi wa kampuni inayojenga kituo hicho ya Jacobsen Elektro.
Waziri
wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo akimsikiliza Mkurugenzi
Mkazi wa Mradi wa ujenzi wa kituo cha Kinyerezi I, Bw. Shaun Moore,
wakati akimweleza maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho.
……………………………………………………………………………………..
Na Asteria Muhozya na Jema Marko, Dar es Salaam
Megawati 150 zinatarajiwa
kuongezeka katika gridi ya Taifa mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa
mitambo ya kufua umeme eneo la Kinyerezi I pamoja na kukamilika kwa
ufungaji wa mitambo hiyo, ambapo shughuli zima inatarajiwa kukamilika
kabla ya mwezi Disemba mwaka 2014.
Waziri wa Nishati na Madini
Sospeter Muhongo wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho
alieleza kuwa kukamilika kwa ujenzi wa kituo hicho ni hatua
mojawapo ya kutimiza azma ya Serikali ya kuongeza umeme katika gridi
ya Taifa.
Aidha, aliwataka watanzania na
wateja wa umeme kujenga imani na Shirika la Umeme Tanzania kutokana na
mabadiliko ambayo tayari yamefanyika katika shirika hilo ikiwemo
utekelezaji wa mipango mbalimbali ya kuhakikisha kunakuwa na umeme wa
uhakika.
“Nataka Watanzania muelewe kuwa,
Tanesco ya sasa sio kama ya zamani. Umeme utapatikana. Kampuni ya
Jacobsen Elektro ambao wanafanya kazi ya ujenzi ni wazoefu katika
shughuli hizi, tuna imani kazi itakwenda vizuri kama tulivyopanga.
Tanesco itatatua tatizo la umeme”. Alisema Waziri Muhongo.
Katika hatua nyingine, Profesa
Muhongo alieleza kuwa, asilimia 98 ya kampuni za kitanzania kupata
kandarasi katika ujenzi huo ni fursa mojawapo ambazo watanzania
wanatakiwa kuzitumia katika kipindi hiki ambacho nchi inaingia katika
uchumi wa gesi.
Akizungumzia kuhusu fedha za
ujenzi wa kituo cha kinyerezi I na ujenzi wa vituo vingine vya kinyerezi
II, III na IV, Waziri Sospter Muhongo alieleza kuwa, fedha za ujenzi
wa kituo cha Kinyerezi I zimetolewa na Serikali kupitia TANESCO. Ujenzi
wa kituo cha kinyerezi II fedha itatokana na ubia kati ya Serikali ya
Tanzania na Japani , wakati ujenzi wa kinyerezi III na IV fedha
zitatokana na kuingia ubia kati ya Serikali na kampuni ya Kichina.
Wakati huo huo, Naibu Mkurugenzi
Mtendaji, Uwekezaji, wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mhandisi
Decklan Mhaiki, aliongeza kuwa, katika kituo hicho zitafungwa jenereta
nne ambapo kila moja itakuwa na uwezo wa kuzalisha kiasi cha megawati
37.5, hivyo kufanya jumla ya megawati 150 kutoka kituo hicho.
Vilevile, alieleza kuwa, katika
jitihada za kuhakikisha kwamba Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco)
linatatua tatizo la Umeme nchini, tayari shirika hilo na mkandarasi
anayejenga kituo hicho, kampuni ya Jacobsen Elektro wameanza mazungumzo
ili kuongeza kiasi kingine cha megawati 200 ili kituo cha kinyerezi I
kiweze kuzalisha umeme wa kiasi cha megawati 350.
Akielezea kuhusu ubora wa jenereta
zitakazofungwa kituoni hapo, Mhaiki alieleza kuwa, generator hizo ni za
kisasa na hazina athari za kimazingira ikiwemo kelele.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkazi
wa Mradi huo kutoka kampuni ya Jacobsen Elektro, Bw. Shaun Moore,
akielezea maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho, alieleza kuwa, ujenzi wa
kituo hicho unaendelea vizuri kutokana na kampuni hiyo kufanya kazi kwa
ushirikiano mzuri na kampuni za kitanzania zilizochukua kandarasi
tofauti tofauti za ujenzi wa kituo hicho, ambapo takriban asilimia 98 ya
kandarasi na wafanyakazi ni kutoka kampuni za kitanzania.