February 18, 2014

KOCHA AHLY AGOMA KUJIUZULU ,AISUBIRI YANGA.

Wachezaji wa timu ya Yanga wakiwa mazoezini kujiandaa kwa ajili ya mzunguko wa pili wa ligi kuu
KOCHA Mkuu wa Al Ahly ya Misri, Mohammed Youssef, ameziba masikio na kutupilia mbali kelele za mashabiki wanaomshinikiza ajiuzulu kutokana na matokeo mabaya na kesho Jumatano anaiingiza timu kambini.
Ahly inajiandaa na msimu mpya wa Ligi ya Mabingwa ambapo itaanza na Yanga mwishoni mwa mwezi huu jijini Dar es Salaam, lakini kesho kutwa Alhamisi itacheza mechi ya ‘Super Cup’ dhidi ya Safaxien ya Tunisia nchini Misri kwenye Uwanja wa Cairo.
Mechi hiyo ni kuashiria mwanzo wa msimu mpya wa mashindano ya kimataifa na hukutanisha bingwa wa Kombe la Shirikisho na wa Ligi ya Mabingwa Afrika msimu uliopita.
Mashabiki wa Al Ahly wanahofia kwamba mwenendo wa timu hiyo katika ligi yao ya ndani usije ukaiathiri na kukumbana na kipigo cha aibu kutoka kwa Yanga na wakaondoshwa mapema na kuwa timu ya pili ya Misri kuondoshwa mashindanoni na timu ya Tanzania ikiwa bingwa mtetezi. Simba iliitoa Zamalek mwaka 2003 wakati Wamisri hao wakiwa mabingwa watetezi.
Kocha huyo alisema kwamba kujiuzulu siyo hoja ya msingi kwa sasa kwa vile timu hiyo inayumba kutokana na majeruhi waliomo, ingawa kocha wa Yanga, Hans Pluijm, amedai hiyo ni danganya toto tu ili wajisahau.
Akizungumza baada ya mchezo wao wa mwisho uliopigwa wikiendi iliyopita dhidi ya vibonde katika kundi lao El Gounah  ambapo Al Ahly ilipokea kipigo cha bao 1-0, Youssef alisema licha ya kikosi chake kupokea kipigo cha tatu tangu kuanza kwa ligi hiyo, matokeo ambayo yaliwashusha mpaka nafasi ya tatu, hana mpango wa kuachia ngazi.
Youssef alisema kwa sasa kikosi chake kinapita katika wakati mgumu na wanasumbuliwa na tatizo la majeruhi ambao ni  kiungo mshambuliaji, Walid Soliman na mabeki wao wa pembeni; Ahmed Fathi na Sayed Moawad.
Alisema bado timu yake ina nafasi ya kurudisha makali yao ambapo amewataka wachezaji wake kusahau matokeo ya mchezo huo haraka na kujikita katika kuangalia michezo ya Ligi ya Mabingwa.
“Sina mpango wa kujiuzulu kwa sasa, nitabaki kuondoa changamoto tunazokutana nazo kwa sasa, nataka wachezaji wangu kusahau kila kitu kuhusu kufungwa kwetu katika mchezo uliopita, nawaamini wachezaji wangu wanao uwezo mkubwa wa kuirudisha timu katika mwendo mzuri,” alisema Youssef.
“Najua kwamba kuna presha kubwa kwa wachezaji wangu hasa katika hiki kipindi kigumu ambacho tunachopitia, tuhahitaji kupewa muda kuwa sawa, huu ni mchezo wa soka lolote linaweza kutokea wakati wowote.”
Yanga itamtuma kocha msaidizi wake, Boniface Mkwasa, kwenda Cairo kuiangalia mechi hiyo ya Super Cup.
-mwanaspoti

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »