Na Oscar Assenga, Lushoto.
WANANCHI wa wilaya ya Lushoto wameunga mkono Agizo la Mkuu wa Mkoa wa
Tanga,Luteni Mstaafu Chiku Gallawa la kufanya usafi katika maeneo yao kila
Jumammosi ya kwanza ya mwezi kwa kuchagua maeneo korofi kwa kufanya usafi wa
pamoja.
Mwishoni mwa mwezi uliopita Mwandishi wa blog hiii aliweza kupita maeneo
mbalimbali wilayani humo nyakati za asubuhi na kujionea maduka yakiwa
yamefungwa huku umati mkubwa wa wananchi wakiwa katika maeneo yao kwa ajili ya kushiriki katika zoezi la
usafi.
Akizungumza mara baada ya kumalizika kwa zoezi hilo,Mkazi wa Lushoto
mjini,Philipo Katemba alisema zoezi hilo la usafi wamelipokea kwa mikono miwili
na kueleza kuwa endapo wananchi watashirikiana kwa pamoja kila wakati basi upo
uwezekano mkubwa wilaya yao kushika nafasi ya kwanza katika usafi mkoani hapa
kutokana na mwamko wa wananchi kijitokeza kushiriki.
Katemba ambaye pia ni mfanyabishara wilayani humo, aliongeza kuwa zoezi la
usafi lilianza muda mrefu lakini wakati huu ndio limetiliwa mkazi zaidi ambapo
wananchi wameweza kuhamasika zaidi kwa kujitokeza kwa wingi kuliko ilivyokuwa
huku nyuma.
Naye Katibu wa Baraza la Biashara wilayani Lushoto (BBW) David Mkami
alisema mchakati huo wa usafi ni mzuri kwa kuwa unaufanya mji wao katika hali
ya usafi na kuwa na muonekano mzuri zaidi na kuwataka wafanyabishara kuendelea
kuunga mkono agizo hilo katika maeneo yao ya kazi.
Mwisho.
DC Mwanga "awataka Vijana kupenda soka"
Na Oscar Assenga, Lushoto.
MKUU wa wilaya ya Lushoto,Alhaji Majid Mwanga amewataka vijana kupenda
michezo na kuithamini kwa kuwa michezo ni ajira ambayo inaweza kuwainua
kimaisha endapo wataithamini na kuipa kipaumbele kwa kucheza kwa kujituma
pamoja na kuonyesha nidhamu wakati wa michezo.
Alhaji Mwanga alitoa wito huo mwishoni mwa wiki wakati fainali ya
Mashindano ya Kombe la Shambalai Cup yaliyofanyika kwenye uwanja wa soka Moa
Mwangoi wilayani humo na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali wa soka wilayani humo
akiwemo mdhamini wake Abasi Shambalai.
Alisema michezo mara nyingi huwakinga vijana kujiingiza katika makundi
mabaya katika jamii zinazowazunguka pamoja na kuwaepusha kutumia madawa ya
kulevya ikiwemo bangi hivyo kuwata vijana kupenda kushiriki katika michezo na
kuacha utumiaji wa madawa ya kulevya.
“Wilaya yetu haipo salama kutokana
na kuwepo watu ambao wanaendesha kilimo cha bangi hivyo kupitia mashindano
mbalimbali ya mpira miguu wilayani tuwe tunapiga vita matumizi ya madawa ya
kulevya “Alisema Mwanga.
Aidha DC Mwanga alisema mashindano hayo yawe chachu kubwa ya wafadhili
wengine kujitokeza ili kuweza kuinua kiwango cha soka wilayani humo pamoja na
kuhamasisha michezo wilayani humo.
Alieleza endapo suala hilo
litatiliwa mkazo mkubwa upo uwezekano wa wilaya hiyo kuwa na timu ambayo
itaweza kuja kushiriki ligi daraja la kwanza ikiwemo ligi kuu siku zijazo.
Pamoja na hayo Mkuu huyo wa wilaya alisifu jitihada za waandaaji wa
mashindano hayo na kueleza malengo hasa kombe hili yaliyokusudiwa yamefanikiwa
kwa asilimia kubwa kutokana na vijana wengi kuhamasika kushiriki.
Katika fainali hiyo,Timu ya Mlalo City waliweza kuibuka kuwa mabingwa wapya
wa mashindano hayo na kukabidhiwa Kombe la Mashindano hayo pamoja na kitita cha
sh.500,000 jezi na mpira kutoka kwa mdhamini wa mashindano hayo,mshindi wa pili
,alipata kitita cha sh.200,000 na jezi,mshindi wa tatu,Kwemshasha alipewa
kitita cha sh.200,000 na mpira na mshindi wa nne,Manyigu Fc alipata 100,000.
Lakini pia washindi wengine waliozawadiwa ni katika awamu ya nane bora
ambapo mshindi wa kwanza alipewa kitita cha sh.100, 000 jezi na mpira mmoja,
mshindi wa pili alipewa kitita cha sh.50, 000 jezi na mpira na mshindi wa tatu
alipewa jezi seti na mpira na kitita cha sh.25,000.
Aidha Mratibu wa Kombe hilo, Fineas Gabriel
Mashombela alisema mashindano hayo yalishirikisha timu zaidi ya 50 kutoka
maeneo mbalimbali wilayani humo na lengo lake lilikuwa
ni kuinua vipaji vya wachezaji wachanga.
Mwisho.
EmoticonEmoticon