TAIFA STARS YAKALISHWA 2-0 NA BURUNDI, SAMATTA, ULIMWENGU NJE!

September 07, 2014


TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, chini ya kocha mkuu Mholanzi, Mart Nooij imetandikwa kwa mara nyingine tena mabao 2-0 dhidi ya timu ya taifa ya Burundi katika mchezo wa kimataifa wa kirafiki uliomalizika muda mfupi uliopita mjini Bujumbura.
Mabao ya Burundi yamefungwa na nahodha Said Ntibanzikiza katika sekundi ya 40 tu na la pili lilifungwa na Yussuf Ndikumana katika dakika ya 24.
Stars iliingia katika mchezo wa leo ikiwa na kumbukumbu ya kufungwa mabao 3-0 na Burundi katika mechi maalumu ya kuadhamisha miaka 50 ya Muungano, iliyopigwa April 26 mwaka huu uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam.
Katika mechi ya leo, Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta hawakuwepo katika kikosi cha Stars kwasababu walikosa usafiri wa kuunganisha ndege kutoka Zambia ilipo kambi ya TP Mazembe kwenda Lubumbashi na hatimaye Bujumbura.
Stars itarejea kesho baada ya kuumizwa kwa mara nyingine tena na kuwapa huzuni Watanzania walioshuhudia timu yao iakitolewa katika michuano ya kuwania kufuzu hatua ya makundi kusaka tiketi za kucheza fainali za mataifa ya Afrika, AFCON mwakani nchini Morocco dhidi ya Msumbiji.
Nooij aliwaanzisha Deo Munish ‘Dida;, Said Mourad, Shomari Kapombe, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Joram Mgeveke, Erasto Nyoni, Mrisho Ngasa, Mwinyi Kazimoto, Mwagane Yeya, Amri Kiemba na Khamis Mcha ‘Vialli’.

Wachezaji wa Burundi walioanza walikuwa ni: Mbonihankuy Innocent, Ntibanzonkiza Said, Kiza Fataki, Hakizimana Issa, Rachid Leo, Ndikumana Yussuf, Pierre Kwizera, Steve Ndikumasabo, Hussein Shaaban, Didier Kavumbangu na David Nshirimana.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »