Serikali yafurahishwa kuanzishwa kwa kampuni ya bima ya ‘CRDB Insurance Company’

June 28, 2024

 

Mkurugenzi wa Jinsia wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Badru Abdunuru aliyekuwa mgeni rasmi katika hafla ya mafunzo ya ujasiriamali na elimu ya fedha akimkabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 150 Mkurugenzi Mtendaji wa Asasi ya Data Sustainable Development Organization, Sihaba Madenge ambazo ni mtaji wezeshi kwa baadhi ya wanachama wa asasi hiyo waliokidhi vigezo vya Programu ya Imbeju inayotekelezwa na Taasisi ya CRDB Bank Foundation. Wanaoshuhudia ni Mkurugenzi Mtendaji wa BUTA Vicoba, Semeni Gama (wa kwanza kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Mwambapa (wa pili kushoto, Meneja wa Kanda ya Mashariki wa Benki ya CRDB, Badru Iddi (wa nne kulia), Mkuu wa Kitengo cha Kuendeleza Biashara Changa wa CRDB Bank Foundation, Fadhil Bushagama (wa kwanza kulia) pamoja na wanachama wa Asasi ya Data Sustainable Development Organization.

========     =========      ==========

Dar es Salaam: Serikali imeipongeza Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kutoa mafunzo ya ujasiariamali na elimu ya fedha pamoja na mitaji wezeshi zaidi ya shilingi bilioni 10 kwa vijana na wanawake wajasiriamali nchini.

Pongezi hizo zimetolewa na Mkurugenzi wa Jinsia wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu, Badru Abdunuru wakati wa hafla ya mafunzo ya ujasiriamali na elimu ya fedha pamoja na kukabidhi mitaji wezeshi ya jumla ya kiasi cha shilingi milioni 150 kwa wanachama wa Asasi ya Data Sustainable Development ya Dar es Salaam. Katika mafunzo hayo, ilibainishwa kuwa kati ya shilingi bilioni 10 za mtaji wezeshi zilizotolewa mpaka sasa, wakazi wa Dar es Salaam wamepokea zaidi ya shilingi bilioni 3.6.
Abdunuru amesema ni ukweli wa dhahiri kuwa wanawake na vijana ndio injini ya uchumi kwani wana uwezo mkubwa wa kuliinua taifa kiuchumi. Kwa kuzingatia Ripoti ya Sensa na Makazi ya mwaka 2022, amesema asilimia 51 ya watu wote nchini ni wanawake na asilimia 75 ni vijana hali inayodhihirisha umuhimu wa kundi hili kwa nguvukazi ya taifa.

“Hata hivyo, wanawake na vijana wanakabiliwa na changamoto nyingi zikiwamo mila na desturi kandamizi, elimu duni, ukosefu wa mitaji na stadi za ujasiriamali. Tukizitambua changamoto hizi, serikali imechukua hatua mbalimbali zinazolenga kujenga uchumi jumuishi na shirikishi ili kuwakomboa kiuchumi,” amesema Abdunuru.

Aliongezea kuwa, “Tunaendelea kufanya kazi kwa bidii kufikia malengo ya Jukwaa la Kimataifa ya Kukuza usawa wa Kijinsia hususan katika haki na usawa wa kiuchumi. Nawapongeza Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa kuja na ubunifu huu unaounga mkono jitihada za serikali kuwakomboa kiuchumi vijana na wanawake.”
Ili kuwawezesha zaidi wajasiriamali wanawake na vijana, Mkurugenzi huyo amesema ni muhimu kwa wadau wote wa maendeleo wakashiriki mkakati huu kwani serikali pekee haitoweza kutatua changamoto zote zilizopo. 

“Niipongeze CRDB Bank Foundation kwa kuja na programu hii ambayo inalenga kuboresha maisha na kuimarisha biashara za vijana na wanawake kwa kuwapa mafunzo na ushauri wa namna bora ya kusimamia na kuendesha biashara zao, pamoja na kuwapa mitaji wezeshi. Naamini mmefungua milango kwa taasisi nyingine kubuni namna zinavyoweza kuyashirikisha makundi haya katika mipango yao,” amesema Abdunuru.
Akizungumza kwenye mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Mawasiliano na Uhusiano kwa Umma wa Benki ya CRDB na Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB Bank Foundation, Tully Mwambapa  amesema mpaka mwishoni mwa Mei wameshatoa mafunzo kwa zaidi ya wanawake na vijana 400,000 ambao baadhi yao wamenufaika na mitaji wezeshi yenye thamani ya shilingi bilioni 10.

“Uwezeshaji huu umefanyika kupitia madirisha mbalimbali yaliyo chini ya programu yetu ya Imbeju ikiwamo Imbeju Ng’ara ambalo limejielekeza kuwawezesha wanawake, Imbeju Buni kwa ajili ya vijana wenye biashara changa, na Imbeju Kilimo linalowasaidia wakulima wadogo pembejeo na zana za kilimo pamoja na kuwalinda kupitia bima ya maisha na mazao. Vilevile, tuna Imbeju Nishati Safi, dirisha linalotoa elimu na kuhamasisha matumizi ya nishati safi kwa mama lishe,” amesema Tully. 

Mafanikio hayo, Tully amesema yasingeweza kufikiwa bila kuwashirikisha  wabia wao wa kimkakati kama ilivyo Asasi ya Data Sustainable Development yenye zaidi ya wanachama 1,800 na wengine wengi kuanzia mashirika ya kimataifa, taasisi za serikali na vikundi vya wanawake wajasiriamali.
“Katika zaidi ya shilingi bilioni 10 tulizozitoa nchini kote kama mtaji wezeshi kwa wajasiriamali, shilingi bilioni 3.6 tumezitoa kwa wakazi wa Mkoa wa Dar es Salaam na leo tunajivunia kutanua wigo wa wanufaika kwa kutoa mitaji wezeshi kwa wanachama wa Asasi ya Data Sustainable Development ambao tumeingia nao mkataba wa ushirikiano hivi karibuni,” amesema Tully wakati wa kuakikabidhi mfano wa hundi ya shilingi milioni 150 kwa Mkurugenzi Mtendaji wa asasi hiyo, Sihaba Madenge.

Akipokea mfano wa hundi hiyo kwa ajili ya wanachama wake, Sihaba amesema ubunifu wa CRDB Bank Foundation ni wa kipekee kwani umeliona kundi kubwa ambalo ni muhimu ila lenye vikwazo vingi kupata huduma za fedha hasa mikopo ya kukuza biashara zao.

“Wanawake wengi wanapambana na maisha kuhakikisha wanazihudumia familia zao kwa kufanya biashara ndogondogo. Kikwazo kikubwa kwao ni mtaji kwani wengi hawana dhamana zinazohitajika katika benki nyingi hivyo kujikuta wakikwama kwa muda mrefu. Fursa hizi za kupata mtaji wezeshi kupitia Programu ya Imbeju bila masharti yoyote hakika ni ukombozi wa kiuchumi kwa wanawake wengi tunaipongeza na kuishukuru sana Taasisi ya CRDB Bank Foundation kwa ubunifu huu,” amesema Sihaba.
 
Mkurugenzi huyo pia ameiomba CRDB Bank Foundation kupeleka fursa za Programu ya Imbeju mpaka vijijini waliko wanawake wengi kwani kuna mwamko mkubwa wa wanawake kujishughulisha kiuchumi japo suala la upatikanaji wa mitaji linawakwamisha wengi. 





Benki ya CRDB yaadhimisha Siku ya Wajasiriamali Duniani ikitooa Shilingi Bilioni 995 mpaka Mei 2024

June 28, 2024

 

Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Benki ya CRDB, Bruce Mwile (kulia) akiwa pamoja na Mkurugenzi wa Wateja wa Awali na Kati wa Benki ya CRDB,  Bonaventure Paul wakizindua rasmi Akaunti ya Biashara  'CRDB Biashara Account' kwenye hafla ya maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani iliyofanyika kwenye makao makuu ya benki hiyo, jijini Dar es salaam Juni 27, 2024.
Dar es Salaam. Tarehe 27 Juni 2024: Benki ya CRDB imeungana na wadau wengine kuadhimisha Siku ya Wajasiriamali Duniani (International MSME Day) kwa kuendesha semina kwa wateja wake na baadhi ya wabia wa kimkakati.

Sherehe za maadhimisho hayo zimefanyika makao makuu ya Benki ya CRDB zikifunguliwa na Afisa Mkuu wake wa Uendeshaji, Bruce Mwile aliyesema kuwa kipaumbele chao siku zote ni kumhudumia Mtanzania na kuhakikisha anaboresha maisha yake kwa kumpa huduma zinazoendana na kukidhi mahitaji yake.
Ili kukuza ujasiriamali, Mwile amesema Benki ya CRDB inatambua kuwa shughuli zake zikichangia asilimia 27 ya Pato la Taifa na ili itoe mchango wake ipasavyo kunahitajika huduma na mifumo shirikishi itakayowasaidia wajasiriamali kuyafikia malengo waliyojiwekea.

“Kutokana mikakati tuliyojiwekea, Benki yetu imekuwa kinara katika uwezeshaji wajasiriamali kwani hadi Mei 2024 tulikuwa tumetoa zaidi ya shilingi bilioni 995.346 kwa zaidi ya wajasiriamali 21,470 katika sekta mbalimbali ikiwamo sekta ya kilimo, ujenzi na makazi, miundombinu, usafirishaji, afya, elimu, nishati, madini, biashara na viwanda, pamoja na uchumi wa buluu ili kuimarisha shughuli zao,” amesema Mwile.

Mwile amesema sekta ya ujasiriamali imekuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi wa mataifa mengi duniani kwa kuchochea ubunifu na uanzishaji biashara mpya ambazo huongeza ajira na kuimarisha kipato cha watu binafsi na jamii kwa ujumla. 
“Kwa kuanzisha biashara ndogo na za kati, wajasiriamali huchangia moja kwa moja kwenye ukuaji wa pato la Taifa na kuongeza mapato ya serikali kupitia kodi. Sekta hii pia ina mchango mkubwa katika kuboresha teknolojia na kuongeza ufanisi katika uzalishaji wa bidhaa na huduma, hivyo kufanya uchumi kuwa na ushindani zaidi kimataifa,” amesema Mwile.

Taarifa za Umoja wa Mataifa (UN) zinasema wajasiriamali ni injini muhimu ya kufanikisha utekelezaji wa Maendeleo Endelevu (SDG) kwani kundi hili linachangia asilimia 90 ya biashara zote zilizopo duniani ambazo hutoa kati ya asilimia 60 mpaka 70 ya ajira zenye staha na kuchangia zaidi ya nusu ya pato la dunia. Tanzania kuna zaidi ya biashara ndogo za ujasiriamali milioni 3 zinazowapa uhakika wa kipato wamiliki wake.
Ili kumkuza mjasiriamali kuanzia ngazi ya chini kabisa, Mwile amesema Taasisi ya CRDB Bank Foundation ambayo ni kampuni tanzu ya Benki ya CRDB inatekeleza programu ya Imbeju inayotoa  elimu ya ujasiriamali na fedha kwa wanawake na vijana pamoja na kuwapa mitaji wezeshi inayoanzia shilingi 100,000. Hadi sasa tayari programu hiyo imewafikia wajasiriamali zaidi ya 400,000 na kutoa mitaji wezeshi zaidi ya shilingi bilioni 10.

Sambamba na maadhimisho hayo, Benki ya CRDB imezindua ‘CRDB Biashara Account’ ambayo ni mahsusi kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo wenye malengo ya kukuza miradi yao ili kuongeza idadi ya wateja wanaowahudumia, kukuza mapato yao ili wakue zaidi na kuanzisha kampuni kubwa zitakazohudumia nchi nzima hata nje ya mipaka pia.
Akizungumza kwenye mjadala uliofanyika katika maadhimisho hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Royal Mark, Johnson Kapira amesema kwa Mtanzania kuwa masikini kunatokana na kutokuwa na ujasiri wa kufanya uamuzi binafsi wa kuzichangamkia fursa zilizopo.

Akieleza jinsi alivyoanza mwanzoni mwa miaka ya 1990 baada ya kuhitimu chuo kikuu, amesema kutokana na changamoto za kupata ajira zilizokuwapo alianzisha kampuni yake na akawa anaomba mikopo ya kufanikisha kazi alizokuwa anazipata na mpaka sasa anakopesheka kiasi kikubwa zaidi.

“Nilianza nikiwa mfanyabiashara mdogo sana. Nilianza biashara mwaka 1995 nikiomba zabuni serikalini na kampuni binafsi. Mtaji ulikuwa changamoto lakini Benki ya CRDB imenikuza hasa huduma yake ya Purchase Order Agreement. Leo hii naweza kukopa mpaka shilingi bilioni nne,” amesema Kapira.
Naye Josephat Kibwanga ambaye naye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Qualitas amesema: “Mimi ni mteja mkubwa wa Benki ya CRDB. Mikopo yao imeniwezesha kuimarisha huduma katika hospitali yangu na kwa sasa utakuwa muujiza iwapo mgonjwa atakuja hospitalini kwetu na akaambiwa hakuna dawa. Haya yote yamewezekana kutokana na mikopo inayopatikana kwa wakati kutoka Benki ya CRDB.”

Maneno ya wajasiriamali hao yana akisi kile alichokisema Mwile wakati akifungua maadhimisho hayo aliposema: “Leo hii tukiwa tunaadhimisha Siku ya Wajasiriamali Duniani niwahakikishie kuwa Benki yetu ya CRDB itaendelea kuweka mikakati madhubuti ya kuwawezesha wajasiriamali na biashara changa, ndogo na za kati nchini tukiamini kwa kufanya hivyo tunachochea ongezeko la ajira, kuimarisha kipato binafsi na kukuza uchumi wa Taifa letu kwa ujumla wake. Ahadi yetu ni kwamba tupo tayari kuwahudumia na kutembea nanyi katika safari yenu ya mafanikio.”
Mkurugenzi wa Wateja wa Awali na Kati wa Benki ya CRDB,  Bonaventure Paul akizungumza katika hafla ya uzinduzi rasmi wa Akaunti ya Biashara  'CRDB Biashara Account' iliyoenda sambamba na maadhimisho ya Siku ya Wajasiriamali Duniani iliyofanyika kwenye makao makuu ya benki hiyo, jijini Dar es salaam Juni 27, 2024.



RAIS WA ZANZIBAR MHE.DK.HUSSEIN MWINYI AZUNGUMZA NA UJUMBE WA WATAALAMU KUTOKA NCHI BRAZIL IKULU ZANZIBAR

June 26, 2024

 


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na Kiongozi wa Ujumbe wa Wataalamu kutoka Nchini Brazil wa Mradi wa kupunguza Vifo vya Mama na Mtoto Bi. Camila Guedes Ariza, baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 26-6-2024.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe wa Wataalamu kutoka Nchini Brazil Wanaojishughulisha na Mradi wa kupunguza Vifo vya Mama na Mtoto, ulioambatana na Mwakilishi wa Heshima wa Brazil Zanzibar Mhe. Abdulsamad Abdulrahim (kulia kwa Rais) na Kiongozi wa Ujumbe huo Bi.Camila Guedes Ariza, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 26-6-2024.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe wa Wataalamu Maalumu kutoka Nchini Brazil Wanaojishughulisha na Mradi wa kupunguza Vifo vya Mama na Mtoto (kulia kwa Rais) ukiongozwa na Bi.Camila Guedes Ariza na (kushoto kwa Rais) Uongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar ukiongozwa na Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Nassor Ahmed Mazrui, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 26-6-2024.(Picha na Ikulu)

RAIS DKT. SAMIA ATOA MHADHARA WENYE MADA YA FARSAFA R4 AMBAYO ANAITUMIA KUONGOZA SERIKALI

June 26, 2024

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi mbalimbali kwenye picha ya pamoja na Wanadhimu Wakuu wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi- Tanzania kilichopo Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26 Juni, 2024.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akitoa Mhadhara wenye mada ya Falsafa R4 ambayo anaitumia katika kuongoza Serikali ya Awamu ya Sita . Mhadhara huo umefanyika katika Chuo cha Taifa cha Ulinzi- Tanzania kilichopo Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26 Juni, 2024. Falsafa ya R4 ya Mhe. Rais Samia ni Reconciliation (Maridhiano), Resilience (Ustahimilivu), Reforms (Mageuzi) pamoja na Rebuilding (Kujenga upya)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akipokelewa kwa heshima na Mkuu wa Chuo cha Ulinzi wa Taifa (NDC) Meja Jenerali Wilbert Augustin Ibuge mara baada ya kuwasili katika Chuo cha Taifa cha Ulinzi (NDC), Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26, Juni 2024.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na Wanadhimu Waandamizi Waelekezi wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi  mara baada ya kuwasili  katika Chuo Cha Taifa Cha Ulinzi (NDC), Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26, Juni 2024.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akitoa Mhadhara wenye Mada ya Falsafa ya R Nne (4Rs) ambayo anaitumia katika kuongoza Serikali ya Awamu ya Sita. Mhadhara huo umefanyika  katika Chuo Cha Taifa Cha Ulinzi (NDC), Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26, Juni 2024. Falsafa yake ya R4 ni: Reconciliation (Maridhiano), Resilience (Ustahimilivu), Reforms (Mageuzi) and Rebuilding (Kujenga upya).
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akisaini kitabu cha Wageni mara baada ya kuwasili katika Chuo Cha Taifa Cha Ulinzi (NDC), Kunduchi Jijini Dar es Salaam tarehe 26, Juni 2024.

RAIS MSTAAFU DKT . KIKWETE AONGOZA JOPO WAZEE WA JUMUIYA YA SADC NCHINI

June 26, 2024
Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, leo tarehe 26 Juni, 2024, yuko katika Ufalme wa Lesotho kwa nafasi yake kama Mwenyekiti wa Jopo la Wazee wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

Jopo hili la Wazee wa SADC ambalo Makamu Mwenyekiti wake Mheshimiwa Paramasivum Pillay B. Vyapoory, Makamu wa Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Mauritius, limekutana na Serikali na wadau mbalimbali ndani ya Ufalme wa Lesotho, kama mwendelezo wa juhudi ya kusaidia upatitanaji wa utulivu wa kisiasa katika Ufalme huo.

Jopo limekutana na Mhe. Ntsokoane Samuel Matekane, Waziri Mkuu wa Ufalme wa Lesotho; Mhe. Nthomeng Justina Majara, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Sheria na Masuala ya Bunge; Mhe. Mamonaheng Mokitimi, Mwenyekiti wa Seneti; Viongozi wa Vyama vya Upinzani; Mhe. Constance Seoposengwe, Balozi wa Afrika Kusini nchini Lesotho; na wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanianna jopo la Wazee wa Jumuiya ya SADC wamekutana na Mhe. Ntsokoane Samuel Matekane, Waziri Mkuu wa Ufalme wa Lesotho mjini Maseru leo June 26, 2024


Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanianna jopo la Wazee wa Jumuiya ya SADC wamekutana na Mhe. Constance Seoposengwe, Balozi wa Afrika Kusini nchini Lesotho na wadau mbalimbali mjini Maseru leo June 26, 2024



Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzanianna jopo la Wazee wa Jumuiya ya SADC wamekutana na Mhe. Nthomeng Justina Majara, Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Sheria na Masuala ya Bunge pamoja na Mhe. Mamonaheng Mokitimi, Mwenyekiti wa Seneti; Viongozi wa Vyama vya Upinzani;mjini Maseru leo June 26, 2024.

PICHA NA OFISI YA RAIS MSTAAFU

NAIBU WAZIRI RIDHIWANI KIKWETE ATEMBELEA BANDA LA TIB MAADHIMISHO YA WIKI YA UTUMISHI WA UMMA

June 24, 2024

 Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete ametembelea Banda la Benki ya Maendeleo TIB katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kwenye Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.


Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yalianza rasmi tarehe 16 Juni, 2024 na yanatarjiwa kukamilika tarehe 23 Juni, 2024.

Kaulimbiu ya Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwa mwaka 2024 ni: Kuwezesha kwa Utumishi wa Umma Uliojikita kwa Umma wa Afrika ya Karne ya 21 Iliyojumuishi na Inayostawi; Ni Safari ya Mafunzo na Mabadiliko ya Kiteknolojia.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akipokea zawadi kutoka kwa Meneja Uhusiano na Masoko wa Benki ya Maendeleo TIB mara baada ya kutembelea banda la TIB wakati Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kwenye Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akisaini kitabu cha wageni wakati alipotembelea Banda la Benki ya Maendeleo TIB katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kwenye Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Benki ya Maendeleo TIB wanaoshiriki Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma kwenye Viwanja vya Chinangali Jijini Dodoma.
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete akiagana na watumishi wa Benki ya Maendeleo TIB mara baada ya kutembelea banda la TIB.

RAIS SAMIA NA MGENI WAKE RAIS WA JAMHURI YA GUINEA-BISSAU MHE. EMBALÓ, WASHUHUDIA UTIAJI SAINI WA MKATABA WA MUONGOZO WA USHIRIKIANO

June 22, 2024

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Guinea-Bissau Mhe. Umaro Sissoco Embaló, wakati wakishuhudia utiaji saini wa Mkataba wa Muongozo wa Ushirikiano baina ya Nchi mbili, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 22 Juni, 2024. Kulia ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akitia saini kwa upande wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa na Jamii wa Jamhuri ya Guinea-Bissau Mhe. Carlos Pinto Pereira akitia saini kwa upande wa nchi yake.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba akiwa pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa na Jamii wa Jamhuri ya Guinea-Bissau Mhe. Carlos Pinto Pereira wakati wakionesha Hati ya Mkataba wa Muongozo wa Ushirikiano baina ya Nchi mbili, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 22 Juni, 2024.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu ziara ya Mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Guinea-Bissau Mhe. Umaro Sissoco Embaló Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 22 Juni, 2024. 
Rais wa Jamhuri ya Guinea-Bissau Mhe. Umaro Sissoco Embaló akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu ziara yake, Ikulu Jijini Dar es Salaam tarehe 22 Juni, 2024.

(PICHA ZOTE NA EMMANUEL MBATILO)