UMITASHUMTA mkoa wa Tanga kutimua vumbi leo

June 12, 2013
Na Oscar Assenga, Tanga.
MASHINDANO ya Umoja wa shule za Msingi nchini (Umitashumta) ngazi ya Mkoa wa Tanga yanatarajiwa kuanza kutimua leo katika viwanja vitatu vilivyopo mkoani hapa.

Akizungumza na blog hii, Mratibu wa Mashindano hayo, Rajabu Dimoso alisema maandalizi ya mashindano hayo yanaendelea vizuri na yatashirikisha wanamichezo kutoka shule za wilaya tisa zilizopo mkoani hapa na baadae kupatikana timu ambayo itashiriki ngazi ya Taifa.

Dimoso alizitaja wilaya hizo kuwa ni Kilindi,Handeni,Pangani, Lushoto,Korogwe mjini na Korogwe vijijini,Muheza,Mkinga na Tanga na kueleza mashindano hayo msimu huu yanatarajiwa kuwa ya aina yake kutokana na ushindani uliokuwepo kwa timu hizo ngazi ya wilaya zao.

Aidha aliitaja michezo itakayokuwa ikichezwa kwenye mashindano hayo kuwa ni mpira wa miguu,Pete, mpira wa mikono ,wavu na riadha ambapo washindi watakabidhiwa zawadi zao baada ya kumalizika michezo hiyo.

Alivitaja viwanja ambavyo michezo hiyo itachezwa kuwa ni Mkwakwani, Popatlaly Sekondari na Shule ya Sekondari Tanga Ufundi (Tanga School) ambapo michuano hiyo itashirikisha wanamichezo wapatao 1098 na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Afisa elimu Taaluma Mkoa wa Tanga.

Mwisho.

“Bosnia kuzichapa na Ally Baba”

Na Oscar Assenga, Tanga.

BONDIA Chipukizi Ally Bosnia wa Tanga anatarajiwa kupanda ulingoni kuzichapa na Ally Baba wa Kilimanjaro katika pambano la nane lenye uzito wa kg71 lisilokuwa na ubingwa litakalifanyika Julai 7 mwaka huu kwenye uwanja wa Mkwakwani mjini hapa.

Akizungumza jana, Muandaaji wa Pambano hilo, Promota Abbasi Mwazoa alisema maandalizi ya pambano hilo yanaendelea vizuri na kueleza kuwa siku hiyo pia kutakuwa na mabondia ambao watacheza michezo kadhaa ya utangulizi.

Mwanzoa aliwataja mabondia hao kuwa ni Khamisi Mwakinyo atachuana na Said Mundi katika pambano la raundi nane lenye uzito wa kg61 ambalo linatarajiwa kuwa la aina yake kabla ya Haji Juma kupanda ulingoni kuzichapa na J.J.Ngotiko kwenye pambano litakalo kuwa la kg 55 raundi sita.

Promota Mwanzoa aliyataja mapambano mengine kuwa ni Athumani Boxers atakuwa na kibarua kizito dhidi ya mpinzani wake Saimoni Zabron litakalouwa na raundi sita lenye uzito wa kg 61 huku Rajabu Mahoja nae akipanda jukwaani kuzichapa na Jumanne Mohamed pambano la raundi sita lenye uzito wa kg 59.

Pambano lengine litakalofanyika siku hiyo kuwa ni bondia Zuberi Kitandula atazichapa na Hemed Kangeta litakalo kuwa la raundi 4 lenye uzito wa kg 55 wakati Abdalla Mapoka naye atapambana na Ibrahimu Habibu pambano lenye uzito na raundi sawa na mabondia hao.

Mwanzoa aliwataka wadau wa mchezo masumbwi mkoani Tanga kujitokeza kwa wingi kushuhudia mapambano hayo ambayo yatakuwa na upinzani mkubwa kutokana na uwezo walionao mabondia hao.

Mwisho.

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »