TASAC YATOA WITO KWA WASAFIRI WANAOTUMIA VYOMBO VYA MAJINI

May 31, 2023


Afisa Mfawidhi wa Shirika la TASAC Mkoani Tanga Kapten Christopher Shalua  (kushoto) akitoa maelezo kwa Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji,Viwanda na Biashara Conrad Millinga wa kwanza kulia ambaye alimwakilisha Waziri wa Viwanda wakati alipotembelea banda lao katika maoanyesho ya 10 ya biashara na Utalii yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwahako Jijini Tanga
Afisa Mfawidhi wa Shirika la TASAC Mkoani Tanga Kapten Christopher Shalua  akizungumza na vyombo vya habari katika Banda lao kwenye  maoanyesha ya 10 ya biashara na utalii yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwahako Jijini Tanga
Afisa Masoko Mwandamizi wa Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) Martha Kelvin (kushoto) akimkabidhi zawadi Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji,Viwanda na Biashara Conrad Millinga kulia wakati alipotembelea Banda lao


Na Oscar Assenga,TANGA

SHIRIKA la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa wito kwa wasafiri wanaotumia vyombo vya Usafiri majini kuhakikisha wanatumia vyombo vilivyo ruhusiwa kisheria kubeba abiria na sio kupanda vyombo vya kusafirisha mizigo ikiwemo majahazi.

Wito huo ulitolewa leo na Afisa Mfawidhi wa Shirika hilo Mkoani Tanga Kapten Christopher Shalua wakati akizungumza na waandishi wa habari katika maonyesho ya 10 ya biashara na utalii yanayoendelea katika viwanja vya Mwahako Jijini Tanga

Aidha, alisema kwa sababu viwango vya vyombo vipo kwenye madaraja tofauti ni vema kila chombo kikatumika kulingana na matumizi huzika yaliyothibitishwa na amewataka  wananchi wa Tanga kwa ujumla kutembelea Banda lao ili kupata elimu zaidi.

Alisema TASAC imeshiriki maonesho hayo kwa ajili ya kuwafikia wananchi hususani wanaoishi maeneo ya fukwe na kuwaelimisha kuhusu Usalama, Ulinzi na Utunzaji wa Mazingira Majini pamoja na majukumu yanayotekelezwa na Shirika hilo kwa Mujibu wa Sheria. 

Hata hivyo alisema kwamba jukumu lao pia ni kuhakikisha wanasimamia Bandari kuhakikisha wanatoa huduma katika viwango vinavyokubalika kimataifa ili kuweza kuchochea ukuaji wa uchumi nchini .

Mwisho.

DKT. NCHEMBA AWAAGIZA WATAALAM WA UCHUMI WA KITAIFA NA KIMATAIFA KUTAFUTA SULUHU YA UPUNGUFU WA DOLA ZA MAREKANI KATIKA SOKO LA FEDHA

May 31, 2023
Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) akifungua kikao cha wataalamu wa Wizara hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) kuhusu tathmini ya Program ya Huduma za Mikopo (EFC), jijini Dodoma.

 

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) akimsikiliza Kiongozi wa ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Harris Tsangaride wakati wa kikao cha wataalamu wa Wizara hiyo na IMF, waliokuja nchini kufanya tathmini ya Program ya Huduma za Mikopo (EFC), jijini Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) akiwa katika picha ya pamoja na Kiongozi wa ujumbe kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF), Bw. Harris Tsangaride baada ya kufungua kikao cha wataalamu wa Wizara hiyo na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), waliofika nchini kwa ajili ya kufanya tathmini ya Program ya Huduma za Mikopo (EFC), jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-WFM-Dodoma)





Na Farida Ramadhani-Dodoma


Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amewaagiza wataalamu wa Wizara ya Fedha na Mipango na ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), kujadili namna ya kushughulikia athari za upungufu wa dola za Kimarekani katika mzunguko wa fedha ili kunusuru uchumi wa nchi zinazoendelea.

Mhe. Dkt. Nchemba (Mb) ametoa maagizo hayo wakati wa kufungua kikao kilichowashirikisha wataalam kutoka Shirika la Fedha na Kimataifa (IMF) waliowasili nchini kwa ajili ya kufanya tathimini ya Program ya Huduma za Mikopo (EFC), kwa kushirikiana na wataalam wa ndani wa Serikali.

Alisema mabadiliko ya Sera za Fedha nchini Marekani ya kubana matumzi na kupunguza dola kwenye mzunguko wa fedha, yameleta athari zinazoonekana mpaka kwenye nchi zinazoendelea, ikiwemo Tanzania.
“Tumekuwa tukirejea Uviko na vita baina ya Urusi na Ukraini kama moja ya vitu vinavyoathiri uchumi wa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania lakini upungufu wa dola unaathiri uchumi kwa kiwango kikubwa ikiwemo uagizaji wa mafuta na uagizwaji wa bidhaa mbalimbali zinazotumika katika shughuli za Sekta Binafsi”, alisema Dkt. Nchemba.

Alisema ni vema kutafuta namna ya kushughulikia jambo hilo kisera ili kunusuru nchi zinazoendelea kwa kuwa sekta ya nje ni muhimu katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa ndani.

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe kutoka Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF), Bw. Harris Tsangaride, alisema Shirika hilo litaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuhakikisha nchi inaendelea kupiga hatua kiuchumi na kijamii.
Aliipongeza Serikali kwa Sera zake nzuri ambazo zinaendelea kutekelezwa katika kukabiliana na athari za vita ya Ukraine na kuongeza kuwa ni matarajio yao kuwa zitaendelea kuchokea ukuaji wa uchumi na maisha ya wananchi.

Bw. Tsangaride alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi chache katika kanda ambazo zinafanya vizuri katika kutekeleza programu mbalimbali kwa kushirikiana na Shirika hilo na hivyo katika kikao hicho watajadiliana namna bora ya kuendelea kuiona nchi ikifanya vizuri zaidi. 

Mwisho.

BWAWA LA KIDUNDA KULETA AHUENI DAR NA PWANI KIPINDI CHA KIANGAZI

May 31, 2023

 Serikali kupitia Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) imeanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi Bwawa la Kidunda litakalojengwa Mkoani Morogoro na kugharimu Tsh Bilioni 335 na litakalokuwa na uwezo wa kuhifadhi maji kwa yatakayotumika kwa miaka mitatu mfululizo.


Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya ya Morogoro, Kaimu Afisa Mtendaji DAWASA, Ndugu Kiula Kingu amesema lengo la utekelezaji mradi huo ni kuwezesha mitambo ya maji ya Ruvu juu na Ruvu chini kuwa na maji ya kutosha ili kuzalisha maji kipindi cha kiangazi.

Aidha Kingu amebainisha kuwa bwawa hilo litakapokamilika litakuwa lina hifadhi maji kipindi cha masika ili maji hayo yaweze kutumika nyakati za kiangazi.

Mbali na upatikanaji wa maji kwa uhakika, Ndugu Kiula ameeleza faida za mradi huo na namna utakavyotoa fursa mbalimbali kwa Taifa ikiwemo Ujenzi wa barabara yenye urefu wa Kilomita 101, uzalishaji wa umeme megawatt 20, uvuvi na utalii ambavyo kwa pamoja vitawanufaisha Wananchi kwa maeneo husika kwa kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi.

“Ujenzi wa mradi wa bwawa la Kidunda utaenda kuleta Uhakika wa upatikanaji wa maji kwa muda wote kwa mwaka mzima lakini pia Kuzalisha umeme katika bwawa la kidunda wa Megawati 20 zitakazoenda kuingia katika Gridi ya taifa pamoja na Kutunza hali ya mazingira kwa viumbe hai.” Aliongeza

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Isalama ya Wilaya ya Morogoro Mjini ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya, Mheshimiwa Rebeca Msemwa ameipongeza Serikali kwa udhubutu wa utekelezaji wa mradi na kutoa wito kwa DAWASA kuusimamia na kuutekeleza mradi kwa ukamilifu ili ulete manufaa kwa Watanzania.

“Tunajivunia utekelezaji wa mradi huu katika Mkoa wetu wa Morogoro, Serikali ya awamu ya sita imedhamiria kuhakikisha upatikanaji wa maji kwa kipindi chote cha kiangazi hivyo hatuna budi kuunga juhudi hizi kwa kuhakikisha DAWASA wanatekeleza mradi huu kwa ukamilifu kama ilivyo matarajio ya Watanzania “. Alisisitiza

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bonde la Wami Ruvu, Mhandisi Elibariki Mmasi ameeleza mikakati ya uhifadhi wa vyanzo vya maji kwa kuhakikisha vyanzo vyote vinavyoingia katika bwawa la Kidunda linakuwa na maji ya kutosha kwa kuzuia shughuli zote za uharibifu zinazosababishwa na binadamu au mabadiliko ya tabia ya nchi.

"Tumejipanga kufanya uthamini na tathmini katika maeneo yote yanayozunguka chanzo cha mto Ruvu na kutangazwa kuwa maeneo ya uhifadhi kwa kutenga shilingi Bilioni Nne ili kuhakikisha bwawa la Kidunda linatoa suluhu ya upatikanaji wa maji kwa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani". Alisema Mhandisi Mmasi

Mradi wa Bwawa la Kidunda unaotekelezwa na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Dar es salaam (DAWASA) unatarajia kuanza rasmi Juni 18, 2023 kwa kipindi cha miaka mitatu huku likitarajiwa kupunguza changamoto za huduma za maji kwa Wakazi wa Mikoa ya Dar es salaam na Pwani.

PSSSF YAPEWA TUZO YA KIMATAIFA

May 30, 2023

 

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, DAR ES SALAAM

MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Umepewa tuzo na Taasisi ya Kimataifa ya Hifadhi ya Jamii (International Social Security Association-ISSA)kutokana na mafanikio iliyoyapata katika kipindi kifupi baada ya kuunganishwa (Merge) kwa mifuko minne ya Hifadhi ya Jamii ya PSPF, PPF, GEPF NA LAPF na kuwa PSSSF.

Akizungumzia tuzo hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba alisema sababu nyingine iliyoifanya ISSA kutoa tuzo kwa Mfuko huo ni pamoja na jinsi Mfuko ulivyoweza kupunguza gharama za uendeshaji na ulipaji wa mafao kwa wakati.

“Kwenye suala la kuunganisha mifuko yapo mambo manne ambayo ISSA imeyaona na kuona ni mafanikio ambayo ni pamoja na kupunguza gharama za uendeshaji, kutoa mafao yanayofanana kwa wanachama wa Mfuko licha ya kutoka kwenye mifuko tofauti, kukabiliana na madeni kabla ya mifuko kuunganishwa na pia suala la uwekezaji hususan katika viwanda.” Alisema

CPA Kashimba aliishukuru Bodi ya Wadhamini kwa usimamizi mzuri na hivyo kuufanya Mfuko huo kufanya vizuri.

“Kazi kubwa ya kusimamia zoezi hili la kuunganisha mifuko mmeifanya ninyi Bodi kwa maelekezo ya serikali, sehemu nyingi duniani wanasema karibu asilimia 85 ya kampuni zilizoungana huwa zinashindwa lakini muunganiko wetu sisi umeendelea kufanya vizuri hadi kuivutia taasisi hii kubwa kuifanya PSSSF kuwa mfano wa kuigwa.” Alisema CPA Kashimba.

Alisema tayari Mfuko umeanza kupokea wageni KUTOKA sehemu mbalimbali wakihitaji kujifunza kutoka PSSSF.

“Juzi kamati ya bunge ya Uganda wao wanaanzisha Mfuko wa Watumishi wa Umma na walikuja kujifunza na wameridhishwa na elimu tuliyowapatia.” Alifafanua.

Alisema tuzo hiyo ni zawadi kwa Bodi na sio Menejimenti pekee na mfuko uko kwenye mikakati ya kuhakikisha unaendelea kutoa huduma bora kwa Wanachama na Wastaafu kwa ujumla.

Awali Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Bw. Mbarouk Magawa alidokeza kuwa eneo lingine ambalo liliwavutia watoa tuzo ni jinsi mfukoulivyofanya maboresho makubwa katika utoaji wa huduma kwa wastaafu na wanachama. 

"Suala la Huduma kwa wananchama, jinsi tunavyokusanya michango, tunavyolipa mafao, kutoka kwenye matumizi ya hundi kulipa mafao, lakini jinsi tunavyohakiki wastaafu wetu, haya yote yaliwavutia." Alifafanua Bw. Magawa.

Aidha Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma (PSSSF) Bw. James Mlowe alisema PSSSF ilikabidhiwa tuzo hiyo jijini Abidjan Ivory Coast Mei 17, 2023 na kwamba ifikapo Agosti Mosi, 2023 PSSSF itafikisha miaka mitano tangu kuundwa kwake baada ya kuunganishwa kwa mifuko (merge), Agosti Mosi, 2018.

“Majukumu ya mfuko yanatekelezwa vizuri, uwezo wa mfuko unazidi kuimarika, watumishi wanazidi kuwa kitu kimoja na kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kwakweli mafanikio haya ndiyo yamewavutia ISSA kuweza kutoa tuzo hii” Alisema

“Tunajisikia faraja kwa tuzo hii na hii imekuwa chachu ya  kuendelea kutekeleza majukumu yetu sawasawa kuendelea kuwahudumia wanachama wetu na wastaafu kikamilifu.” Alitoa hakikisho.

Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF),  Dkt. Aggrey Mlimuka (kulia) akipokea tuzo ya Kimataifa inayotolewa na Taasisi ya Kimataifa ya Hifadhi ya Jamii (International Social Security Association-ISSA) kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, CPA. Hosea Kashimba katika hafla fupi iliyofanyika Makao Makuu ndogo ya PSSSF jijini Dar es Salaam Mei 30, 2023. PSSSF ilipewa tuzo hiyo na ISSA kwa kutambua mafanikio iliyopata PSSSF katika kipindi kifupi ndani ya muundo mpya wa mifuko kuunganishwa (merging).

Mkurugenzi wa Uendeshaji PSSSF, Bw. Mbarouk Magawa, akielezea mchakato uliopelekea PSSSF kupewa tuzo hiyo.

Meneja Uhusiano na Elimu kwa Umma PSSSF, Bw. James Mlowe, akionesha tuzo hiyo.


KLABU YA KWANZA YA MKONGE YAZINDULIWA

May 30, 2023


Bodi ya Mkonge Tanzania (TSB) kwa kushirikiana na Shule ya Sekondari ya Coastal ya jijini Tanga, zimezindua Klabu ya Mkonge kwa wanafunzi wa shule hiyo ambayo imelenga kuwafundisha vijana kuhusu kilimo cha Mkonge na Sekta ya Mkonge kwa ujumla hatua itakayowawezesha kujiajiri baada ya kumaliza masomo.

Akizindua klabu hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TSB, Saddy Kambona amesema wazo la kuanzisha klabu hiyo lilizaliwa kwenye Mahafali ya kidato ya shule hiyo Machi mwaka huu, lakini baadaye ikaonekana isiwe klabu kwa ajili ya Shule ya Coastal pekee bali ianzishwe klabu itakayoshirikisha shule zote za Tanga na vizazi vinavyokuja kushiriki kwenye uchumi huu wa mkonge.

Amesema kwa muda mrefu imezoelekea kwamba elimu yetu haimuandai mwanafunzi kwenda kujitegemea anapomaliza shule, wengi wamekuwa na mtazamo kuwa kazi ya kuajiririwa ndiyo inafaa.

“Kwa hiyo sisi tulitazama wazo la kuwa na klabu za Mkonge kwa maana kama tunasema Mkonge ni Tanga na Tanga ni Mkonge, basi tunataka mtu akifika Tanga aone kweli kama Mkonge ni Tanga, tunategemea aone kwamba Mkonge ndiyo zao kuu la kibiashara.

“Yaani kuanzia anatua uwanja wa ndege anapotua anaona bidhaa za Mkonge barabarani hadi anapofika hotelini anakutana na mazuria ya Mkonge na bidhaa nyingine. Sasa sehemu ya kuanzia ni kuwa na klabu za kuhamasisha si tu kilimo cha Mkonge bali  pia kuhamasisha matumizi ya bidhaa za Mkonge lakini pia kushiriki kwenye kuzalisha hizo bidhaa.

“Baada ya hayo sasa Bodi inakuwezesha kupata elimu, utaalamu kuanzia shambani kulima Mkonge na uongezaji wa thamani, wataalamu wetu watatoa ujuzi huo kwa vijana wa Tanga na nje ya Tanga ili wanapomaliza shule huko wanakokwenda wakawafundishe na wengine,” amesema.

Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Zao la Mkonge na Masoko, Olivo Mtung’e akizungumzia faida za Mkonge na somo la kuhamasisha wanachama wa klabu hiyo alisema mahitaji ya Mkonge kwa sasa yameongezeka ndiyo maana wanahamasisha wakulima kulima zao hilo.

“Nchi nyingi sasa zinahitaji Mkonge lakini kiasi ambacho tunakilima kwa sasa ni kidogo ndiyo maana baada ya kuingia kwenye kilimo cha wakulima wadogo sasa tunahamasisha na sisi kwenye familia zetu wenye mashamba ya eka moja hadi tatu walime Mkonge kwa sababu kwa sasa hali ya hewa inatusukuma kuelekea huko kwani zao la Mkonge linahimili hali za hew azote ili kuimarisha uchumi wa familia,” amesema.

Mkurugenzi Mtung’e anasema kutokana na hali hiyo, wahitimu hawana haja ya kutafuta ajira kwa sababu Mkonge wenyewe ni ajira kwani ukishapanda baada ya miaka mitatu unaanza kuvuna hadi kwa muda wa miaka 18.

Kwa upande wake mwanafunzi wa shule hiyo na mmoja wa wanachama wa klabu hiyo, Fatuma Mshashi amesema klabu hiyo yenye wanachama 50 ambao kati yao wavulana ni 23 na wasichana 27, inatekeleza malengo mbalimbali ikiwamo kufanya tafiti kuhusu kilimo cha zao la Mkonge ili kuona faida zake, kutoa elimu kwa wanafunzi, walimu, wadau wa elimu kuhusu umuhimu wa zao hilo, kuhamasisha jamii kutumia bidhaa za mkonge, kuwaandaa wanafunzi ili kuja kuwa wataalamu wazuri na wabobevu katika zao la Mkonge na nyingine nyingi.

“Ili kufanikisha malengo katika Klabu ya Mkonge katika shule yetu, tunaomba ofisi yako kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwalimu Mkuu itusaidie kukutanishwa na wataalamu wa zao la Mkonge ili kupata elimu na ujuzi wa zao hili, kuwezeshwa klabu kuwa na shamba darasa ambalo litakuwa la kujifunzia hatua zote za uandaaji hadi uvunaji ambapo shamba hilo mlitakuwa mradi wa klabu,” amesema.

TETE FOUNDATION YAADHIMISHA SIKU YA HEDHI DUNIANI KATIKA KITUO NA SHULE YA AMANI, MVOMERO MOROGORO

May 29, 2023







Tarehe 28/5/2023 TETE FOUNDATION  imeungana na jamii kuadhimisha Siku ya Hedhi Duniani, ambapo Taasisi hiyo imefanya maadhimisho hayo katika kituo na shule Amani iliyopo Mvomero - Mkoa wa Morogoro 

Shule/ kituo cha Amani, ni kituo kinachojumuisha malezi ya kitaalam na kijamii Kwa Watoto Wanaoishi kwenye mazingira magumu, Uhitaji na wenye Ulemavu.

Ndani ya kituo hicho kuna Shule ya Msingi kuanzia darasa la awali Hadi darasa la saba na Shule ya Sekondari kuanzia kidato Cha kwanza hadi Cha Pili

Takwimu zinaonyesha kwamba mtoto wa kike anaeishi kwenye mazingira magumu, uhitaji na wenye ulemavu hukosa darasani siku 5 - 7 darasani kwa kukosa taulo za kike. 

Katika maadhimisho hayo Mkurungezi wa TETE FOUNDATION, Bi. Suzana Senso amesema kutokana na takwimu hiyo, mwaka huu tumekuja  na dhima "Sitakosa Shule Campaign" ambapo mwaka huu tumegawa taulo za kike za kutumia kwa muda wa miezi 6  kwa kila binti zaidi ya 50 waliopo kwenye  shule ya Amani 

Shukurani za kipekee kwa wadau walioshirikiana na TETE FOUNDATION kufanikisha hili zoezi ikiwemo UAP INSURANCE TANZANIA kwa kuwa sehemu ya kufanikisha zoezi hili bila kusahau wazalishaji wa taulo za kike za HQ PAD na Ministry ya “love of Christ Ministry” kwa kuwa sehemu ya kuhakikisha kila mtoto wa kike wa Shule ya Amani hakosi darasani kwa muda wa miezi 6 kutokana na kuwa kwenye hedhi

Asante kwa kuwa sehemu ya kurudisha tabasamu kwa mtoto wa kike 🙏🏾🙏🏾🙏🏾

@tete_foundation

TASAC YATOA ELIMU YA USALAMA, ULINZI NA UTUNZAJI WA MAZINGIRA MKOANI PWANI, KIBITI

May 29, 2023

 



Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limetoa elimu ya Usafiri Salama Majini kwa wadau mbalimbali wa Wilaya ya Kibiti katika mialo ya Nyamisati Mkoani Pwani tarehe 25 Mei, 2023.


Elimu hiyo iliyotolewa katika mialo iliyozunguka Nyamasati iliwajumuisha wavuvi, manahodha wa vyombo, wamiliki wa vyombo, wafanyabiashara na watumiaji wa vyombo vidogo vya usafiri majini.


Watoa mada mbalimbali kutoka TASAC, TPA na BMU walitoa elimu ya jinsi ya kutumia vifaa vya uokoaji pindi inapotokea dharura au ajali majini;  utumiaji vifaa vya uokoaji pamoja na matumizi ya kizimia moto (fire extinguisher) na umuhimu wa kuwa na kifaa hicho kwenye vyombo vidogo vya majini.


TASAC imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri majini kutoa elimu katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kuwahamasisha wamiliki wa vyombo kuweka vifaa vya kujiokolea lakini pia manahodha na wavuvi kuvaa jaketi okozi wakati wote wawapo safarini au kuendesha shughuli za uvuvi.

MCHENGERWA, WANANCHI WA VIJIJI VYENYE MIGOGORO YA MIPAKA HIFADHI YA SERENGETI WAYAJENGA, WAIPONGEZA SERIKALI, WATAKA USHIRIKISHWAJI.

May 29, 2023

 



Na John Mapepele

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mohamed Mchengerwa amekutana na kufanya vikao na wananchi wa vijiji vyenye migogoro ya mipaka na Hifadhi ya Serengeti na kuutaka uongozi wa Hifadhi ya Taifa (TANAPA) kuimarisha program za ujirani mwema na kuwashirikisha wananchi wanaozunguka hifadhi wakati wa kupanga mipango yao ili wananchi waweze kushiriki kikamilifu kwenye uhifadhi wa raslimali hizo na kupunguza migogoro isiyo ya lazima.

Waziri Mchengerwa ametoa kauli hiyo Mei 28, 2023 wakati alipofanya ziara katika Wilaya ya Tarime na kufanya mikutano kwenye vijiji vyote vinavyozunguka Hifadhi ya Serengeti vilivyokuwa na migogoro na mipaka katika zoezi la uwekaji wa vigingi vya mipaka ambapo wananchi wa maeneo hao wamepongeza kwa hatua hiyo ya Serikali ya kuja na kuwasikiliza na kuahidi kushirikiana na Serikali kwenye uhifadhi.

Mhe. Mchengerwa aliambatana Naibu Katibu Mkuu wa Wizara yake Anderson Mutatembwa na Kamishna wa TANAPA, Afande William Mwakilema na kupokewa na uongozi wa Mkoa wa Mara, uongozi wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Tarime na Mbunge wa Tarime vijijini Mhe. Mwita Waitara ambapo katika mikutano hiyo yote Mhe. Mchengerwa aliongoza vikao hivyo kwa kuwapa wasaa wa wananchi kutoa maoni na mawazo yao na mwisho alitolea ufafanuzi wa hoja hizo na nyingine kuzichukua kwa hatua zaidi.

Wananchi wamepongeza hatua hiyo ya Waziri Mchengerwa kwenda na kuwasikiliza huku wakieleza kuwa kumekuwa na ushirikishwaji mdogo na kuiomba Serikali kupanga kwa pamoja ili kuondoa migogoro isiyo ya lazima.

Diwani wa kata ya Nyanungu Tiboche Richard amesema kuwa wananchi wa Kata yake wapo tayari kushirikiana na Serikali kwenye kila jambo endapo watashirikishwa na hifadhi.

“Mhe. Waziri napenda kukuhakikishia kuwa leo unatufanya tulale usingizi maana umetumwa na Mhe. Rais wetu kuja kutujengea mahusiano mazuri, na sisi hiki ndicho tulichokuwa tunakikosa.” Amesisitiza diwani Richard

Akiwa kwenye mkutano katika Kijiji cha Karakatonga wilayani Tarime, Mhe. Mchengerwa ameutaka uongozi wa TANAPA kushuka chini kwa wananchi na kwenda kuzungumza nao kwa kuwa hifadhi hizo ni za wananchi na wananchi ndiyo wahifadhi namba moja.
Aidha, amesema wazo la uhifadhi wa raslimali katika taifa la Tanzania limeasisiwa miaka mingi ambapo uongozi katika awamu zote toka enzi za baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere hadi Rais Samia Suluhu Hassan limezingatiwa kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Akiwa kwenye Kijiji cha Kegonga, Mhe. Mchengerwa ametoa wito kwa wananchi hao kushirikiana na uongozi wa Serikali wakati wote na kuacha tabia za kugomea kwa kuwa kwa kufanya hivyo wanachochea migogoro.
“Kwa hiyo wanapokuja viongozi wa Serikali kuja kujadili mpango wa matumizi bora ya ardhi wasikilizeni msikatae kusikiliza, shaurini tufanye nini.” Amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Amewataka kutambua kuwa wahifadhi ni sehemu ya jamii yao kwa kuwa baadhi ya watumishi hao ni sehemu ya familia zao na watoto wao.

ALIYOYASEMA DC JOKATE BAADA YA KUFANYIKA MAMATHON KOROGWE

May 29, 2023

 


Na Mwandishi Wetu Korogwe

MKUU wa Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga Jokate Mwegelo amesema kuwa kazi kubwa inayofanywa na Serikali katika kuboresha miundombinu za huduma mbalimbali ya afya lengo lake ni kumsogea huduma karibu na mwananchi.

Jokate ametoa kauli hiyo baada ya kufanyika kwa mbio ambazo zilikuwa zimeaandaliwa kwa wanawake wajawazito wilayani humo na kupewa jina la Mamathon ambapo zaidi ya wajawazito 2000 wameshiriki sambamba na kupatiwa vifaa kwa ajili ya kujifungulia.

"Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anaguswa na changamoto mbalimbali husani huduma za akina mama na watoto na wao, hivyo kupitia Mamathon tunaenzi yale mema na mazuri ambayo Rais wetu amekuwa akiyafanya kupitia Serikali yake ya Awamu ya sita kwa watanzania na zaidi kwenye kundi la akina mama na watoto."

"Sisi akina mama ndio walezi wa jamii zetu, ndio wajenzi wa Taifa kwa maana ukizungumzia watoto wanatoka tumboni mwetu ndio kwa namna moja ama nyingine na wanaume wao wamekuwa wakitusaidia katika malezi lakini kubwa zaidi , akina mama ndio wanatunza hawa watoto."

Jokate amesema Korogwe waliandaa Mamathon ni mahususi kwa ajili ya kumsemea Rais Dk.Samia Suluhu Hassan Samia ambaye ameweika mbele ajenda za mwana mama na mtoto"Kwa hiyo hili tukio sio tukio tu la kutembea lakini kubwa kwenda kuwa mabalozi wa Rais wetu kwani mwendo ameuaza vizuri ,mwendo atauendeleza na sisi wote tunatakiwa kuungana naye."

Aidha amewaeleza akina mama wajawazito kuwa Serikali ya Awamu ya Sita lengo lake nikupeleka huduma za afya kwenye maeneo yao na kwa Wilaya ya Korogwe hakuna kata ambayo haina huduma ya afya.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Pangani Zainab Abdallah na Meya wa Temeke mkoani Dar es Salaam Abdallah Mtimika wametumia nafasi hiyo kumpongeza Jokate kwa kufanya tukio la kuleta hamasa kwa wamama wajawazito kujenga utamaduni wa kufanya mazoezi na kuzingatia lishe bora.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Pangani Zainab Abdallah amesema jambo ambalo amelifanya Mkuu ws Wilaya Jokate ni kubwa na ni jambo la mama."Nimekuja hapa kwa niaba ya wakuu wa Wilaya wote Mkoa wa Tanga, tunampongeza kwani anaupiga mwingitangu ameingia wilayani Korogwe."

Amesema wananchi wa Wilaya ya Korogwe wamelamba dume na kama ni madini basi ya Tanzanite ambayo yanazalishwa Tanzania peke yake.

Amefafanua Jokate ameupiga mwingi akiwa katika Wilaya ya Kisarawe,Temeke na Meya wa Temeke ametoa ushuhuda lakini kubwa zaidi amewaeleza wananchi wa Korogwe kwamba Rais Dkt Samia Suluhu Hassan amewapendelea kwani amewapelekea jembe na sasa wanashuhudia Mamathon.

Amesema kupitia Mamathon , Jokate amefanya jambo kubwa kubwa linalowagusa maisha ya wanawake.


MHE UMMY AFANYA MKUTANO WA HADHARA WA JIMBO LA TANGA

May 28, 2023





MBUNGE wa Jimbo la Tanga (CCM) Ummy Mwalimu ambaye pia ni Waziri wa Afya akizungumza na wananchi wa Kata ya Makorora katika Jimbo hilo mwishoni mwa wiki wakati wa mkutano wake wa hadhara akielezea utekelezaji wa Ilani kwa miaka miwili

Mstahiki Meya wa Jiji la Tanga Abdurhaman Shillow akizungumza wakati wa mkutano huo









*Aanza na matembezi kuhimiza utunzaji wa mazingira na kufungua shina la vijana wa bodaboda Mikanjuni.
*Aelezea utekelezaji wa Ilani kwa miaka miwili.
*Amshukuru Mhe.Rais Dkt. Samia kwa kuendelea kumwaga mabilioni Tanga Mjini.


Mbunge wa Jimbo la Tanga Mjini Mhe Ummy Mwalimu ambae pia ni Waziri wa Afya tarehe 27/5/2023 amefanya mkutano wa hadhara kwa ajili ya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kipindi cha miaka miwili. Mkutano huo umefanyika katika viwanja vya Makorora Sokoni, Kata ya Makorora Jijini Tanga.


Katika mkutano huo uliofunguliwa na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Tanga Meja Mstaafu Hamisi Mkoba, Mhe Ummy ameelezea utekelezaji wa yale yote yalioahidiwa na Mgombea uRais, ubunge na madiwani katika mikutano ya kuomba kura Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020.


Mhe Ummy ameeleza mafanikio yaliyopatikana katika sekta za Elimu, Afya, Miundombinu ya Barabara, upatikanaji wa Maji na umeme hususani katika kata za pembezoni mwa jiji, maboresho ya Bandari ya Tanga, Masoko, Ongezeko la viwanda vya kati vitatu (3) na viwanda vidogo 21 na utoaji wa Mikopo yenye thamani ya shilingi bilioni 3,032,030,000 kwa vikundi 176 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.


Katika mkutano huo uliohudhuriwa na Mjumbe wa Kamati ya siasa Mkoa wa Tanga Ndugu Omari Ayoub, Mkuu wa Wilaya ya Tanga Mhe. Hashim Mgandilwa, Katibu wa CCM Wilaya ya Tanga, ndugu Selemani Sankwa, Katibu Itikadi na Uenezi ndugu Joel Mulenga, wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Wilaya na sekretariet wilaya ya Tanga, Viongozi wa CCM Kata ya Makorora, wanaCCM na wananchi wa Jiji la Tanga, Mhe Ummy alirudia tena kuwashukuru wanatanga kwa kuendelea kumuamini na kuwaahidi hatawaangusha katika utekelezaji wa majukumu yake ya kibunge. Aidha alieleza kufurahishwa kwa jinsi wananchi walivyojitokeza kwa wingi kuhudhuria mkutano huo.


Imetolewa na;
Ofisi ya Mbunge, Jimbo la Tanga Mjini
28/5/2023

JIOPAKI PEKEE KUSINI MWA JANGWA LA SAHARA KUANZISHWA NGORONGORO - MHE MCHENGERWA

May 26, 2023

 


Na John Mapepele

Waziri wa Maliasili na Utalii - Mhe. Mohammed Mchengerwa amepokea timu ya wataalam saba kutoka nchini China ambao wamewasili nchini kwa ajili ya kuanza maandalizi ya utekelezaji wa mradi wa uendelezaji wa jiopaki ya Ngorongoro- Lengai, ambayo ndio jipaki pekee kusini kwa Jangwa la Sahara .

Pamoja na uimarishaji wa uhifadhi wa rasilimali za kijiolojia, mradi huu utaongeza vivutio vya utalii, ujenzi wa makumbusho ya kijiolojia, kuweka mitambo ya kufuatilia hatari za kijiolojia na kuwajengea uwezo wataalam wa kitanzania kuwezesha ukuaji utalii wa miamba na sura za nchi ( Geotourism and landscape tourism)


Mradi huu ambao utagharimu jumla ya dolla za kimarekani millioni 9.5 na kutarajiwa kukamilika baada ya miaka miwili na nusu, umefadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China.  

Makubaliano ya msaada huu yalisainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipofanya ziara ya kitaifa nchini China Novemba, 2022.

Mhe. Mchengerwa amefafanua kuwa dhamira ya Serikali kwa sasa ni kuimarisha uhifadhi wa raslimali na kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii kimataifa na kutoa wito kwa wananchi kushirikiana kikamili kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.


TAKUKURU DODOMA YAFUATILIA UTEKELEZAJI MIRADI 36 YA MAENDELEO

May 26, 2023
Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma John Joseph.

Na Dotto Kwilasa,DODOMA.

Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa nchini (TAKUKURU)Mkoa wa Dodoma katika utekelezaji wa majukumu yake imepokea jumla ya malalamiko 138 ambapo kati yake, malalamiko 81 yalihusu rushwa na mengine 7 taarifa zake kuhamishiwa Idara nyingine kwa hatua zaidi. 

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Dodoma John Joseph amesema hayo leo Mei 26,2023 wakati akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu ufuatiliaji utekelezaji wa miradi 36 ya maendeleo ya zaidi ya bilioni 16.8 ikiwa ni sehemu ya  Utaratibu wake wa kutoa taarifa kwa kila kipindi cha miezi mitatu.

Amesema malalamiko 57 yalihusu rushwa ambapo yalipelekwa kufunguliwa majalada ya uchunguzi na kati ya hayo uchunguzi wa majalada 17 umekamilika ,mashauri mawili yamefunguliwa mahakamani na mengine 15 hatua mbalimbali za kisheria zinatarajiwa kuchukuliwa dhidi ya watuhumiwa.

Mkuu huyo wa TAKUKURU amefafanua kuwa Idara zinazo lalamikiwa Kutokana na taarifa 57 ni pamoja na Elimu (11), TAMISEMI (9),Sekta binafsi (9), Ardhi (7),Afya (7),Polisi(5),Kilimo(3),Manunuzi (2), Mahakama (1), Maji (1), Mazingira (1)na fedha (1).

"Mashauri mapya manne yametolewa maamuzi ambapo hadi sasa mawili tumeshinda na mawili tumeshindwa ,aidha jumla ya mashauri 31 yanaendelea kusikilizwa mkoani Dodoma na yako katika hatua mbalimbali,"amesema

Pamoja na hayo amesema katika kipindi cha miezi mitatu TAKUKURU Mkoa wa Dodoma wamefanya kazi za uzuiaji rushwa,uelimishaji wa jamii na uchunguzi.

Amefafanua kuwa katika jukumu la uzuiaji rushwa wamefanya tafiti 10 katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dodoma kwa Wilaya za Dodoma, Chamwino na Chemba na kufanya tafiti moja moja kwa kila Wilaya.

"Kwa Wilaya ya Bahi zilifanyika tafiti mbili na katika Wilaya ya Kongwa zilifanyika tafiti tano,tumeweza kufanya warsha tano ambazo zilitumika kuwasilisha matokeo ya chambuzi za mifumo zilizofanyika Kwa lengo la kushirikisha jamii kutafuta ufumbuzi dhidi ya mianya ya rushwa,"amefafanua.

Katika ufuatiliaji wa utejekezwaji miradi ya maendeleo, TAKUKURU Mkoa wa Dodoma imefuatilia miradi 36 yenye thamani ya zaidi ya bilioni 16 ambayo inatoka sekta mbalimbali ikiwemo elimu, afya, Ardhi, Kilimo, ujenzi, barabara na fedha .  

Kwa mujibu wa Mkuu wa TAKUKURU Dodoma jumla ya miradi 22 ya elimu imefanyiwa ufuatiliaji, Kilimo miradi 5,fedha 3 na afya miradi 4 hali iliyosaidia  kufikia fedha kiasi cha shilingi 1,050,000 katika Wilaya ya Chamwino.

"Miradi 21 imetolewa ushauri na elimu pia ufuatiliaji unaendelea, miradi 7 imekamilika ,miwili imetolewa maelekezo, chambuzi za mifumo ya warsha miradi miwili,miradi miwili inaendelea na ufuatiliaji nyaraka katika Wilaya ya Chamwino,"ameeleza