Na Oscar Assenga,Muheza, Tanga
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Maendeleo ya Vijana, Joel
Nanauka amesema serikali itaendelea kuvipa kipaumbele vikundi vya vijana
vinavyoonyesha uwajibikaji kwa kurejesha mikopo wanayopewa ili viweze kukuza
shughuli zao za kiuchumi.
Nanauka aliyasema hayo leo wakati wa ziara ya
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii iliyotembelea kikundi
cha Vijana cha Mali Hai kilichopo wilayani Muheza mkoani Tanga kwa lengo la kukagua
shughuli zao za uzalishaji pamoja na miradi iliyopata fedha kupitia mikopo ya
halmashauri.
Akiwa kwenye kikundi hicho alionyesha
kuridhishwa na juhudi na nidhamu ya kikundio hicho kurejesha mikopo baada ya
kufanikiwa kukuza mtaji wake kutoka shilingi milioni 20 hadi kufikia zaidi ya
shilingi milioni 50, hatua inayotajwa kuwa mfano bora kwa vikundi vingine vya
vijana nchini.
Nanauka alisema kikundi cha Mali Hali ni
miongoni mwa vikundi vichache nchini vilivyofanikiwa kurejesha mikopo kwa
wakati, jambo ambalo limekifanya kupata nafasi ya kuangaliwa kwa karibu zaidi
katika mipango ya kusaidiwa kuongeza mtaji na kupanua shughuli zake.
Alisema katika mchakato unaoendelea wa
kusaidia wajasiriamali wadogo na kurasimisha shughuli zao, serikali itaangalia
namna ya kukiweka kikundi hicho kwenye orodha ya vikundi vitakavyosaidiwa ili
kuimarisha shughuli zao za uzalishaji.
Aidha, alieleza kuwa serikali inatekeleza
maelekezo ya Rais ya kuhakikisha vijana wanaochukua hatua ya kufanya kazi na
kuonyesha juhudi wanapatiwa mikopo na serikali ili waweze kujikwamua kiuchumi
na pia kutoa ajira kwa wengine.
“Vijana hawa wameonyesha mfano mzuri kwa watanzania
wengine wameanza na mtaji mdogo mwaka 2008,wakapata msaada wa shilingi milioni
tano mwaka 2018 na baadaye mkopo wa shilingi milioni 20 mwaka wa fedha
2020/2021. Leo hii wameongeza mtaji wao hadi kufikia zaidi ya milioni 50. Huu
ni ushahidi kwamba ndoto kubwa zinaweza kuanza na mwanzo mdogo,” alisema
Nanauka.
Aliongeza kuwa serikali itahakikisha vijana
wenye juhudi kama hao wanapata fursa zaidi, ikiwemo mikopo mingine, pamoja na
kushirikishwa katika zabuni za serikali ili waweze kukuza biashara zao.
Nanauka pia aliwashauri vijana nchini
kutokudharau mwanzo mdogo na kuwa na uvumilivu wanapotekeleza ndoto zao za
kimaendeleo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, Hawa Mchafu, alisema kamati
hiyo ipo katika ziara ya kawaida ya kukagua miradi ya maendeleo kabla ya kuanza
kwa Bunge la Bajeti, ambapo wamepita katika maeneo mbalimbali kutathmini miradi
iliyopata fedha za serikali.
Alisema kamati hiyo imevutiwa na kazi nzuri
inayofanywa na kikundi hicho cha vijana, lakini imebaini changamoto ya eneo la
uzalishaji kuwa dogo na huenda lisiweze kukidhi mahitaji yao iwapo wataongeza
mtaji zaidi.
Kutokana na hali hiyo, kamati imeitaka wizara
husika kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga kuhakikisha vijana
hao wanapatiwa eneo kubwa zaidi la kufanyia shughuli zao za uzalishaji ili
waweze kupanua biashara zao.
“Eneo walilonalo sasa ni dogo ukilinganisha na
malengo yao ya kupanua uzalishaji hivyo tunashauri wapatiwe eneo kubwa zaidi na
lililopo sasa likibaki kama sehemu ya maonesho ya bidhaa wanazozalisha,”
alisema Mchafu.
Pia aliishauri serikali kuangalia uwezekano wa
kukipa kikundi hicho mkopo mwingine wa kifedha ili kiweze kukabiliana na
changamoto mbalimbali zinazokikabili, ikiwemo kununua gari kwa ajili ya
shughuli za uzalishaji na usafirishaji wa bidhaa.
Aidha, alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha
vijana nchini kutumia fursa zilizotolewa na serikali kupitia mifuko mbalimbali
ya maendeleo ya vijana badala ya kujikita kwenye mfuko mmoja pekee.
Mchafu alisema kuwa Rais ametoa zaidi ya
shilingi bilioni 200 kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vijana kupitia wizara
na taasisi mbalimbali, hivyo vijana wanapaswa kuzitumia fursa hizo kujikwamua
kiuchumi.
Kamati hiyo pia imeishauri serikali
kuhakikisha sheria ya manunuzi ya umma inayotaka asilimia 30 ya zabuni za
serikali zitolewe kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu inatekelezwa
kikamilifu ili kuwapatia vijana nafasi ya kukua kiuchumi.
Kwa sasa kikundi cha Mali Hali kinadaiwa
kuajiri vijana zaidi ya 20 katika shughuli zake za uzalishaji, jambo ambalo
limeelezwa kuwa linaunga mkono dhamira ya serikali ya kukuza ajira kwa vijana
na kuimarisha uchumi wa wananchi.
Vijana wa kikundi hicho pia wamemshukuru Rais
kwa kuendelea kutoa fursa na kuahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii ili
kufikia ndoto zao za kuanzisha kampuni kubwa inayoweza kutoa ajira kwa vijana
wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga na maeneo mengine nchini.
Mwisho.